Miss Zomboko
JF-Expert Member
- May 18, 2014
- 4,500
- 9,279
POLISI Kanda ya Dar es Salaam linawashikilia watu tisa kwa tuhuma za kuharibu miundombinu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na kuiba mafuta kwenye transfoma na kuyauza.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kamanda wa Polisi kanda hiyo, Lazaro Mambosasa aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Shukuru Hamis (39) aliyekamatwa usiku akiwa kwenye ghala la Tanesco lililopo maeneo ya Kigamboni na baadaye aliwataja watuhumiwa wengine walioshirikiana nao.
Kamanda Mambosasa alisema watuhumiwa wengine ni Witness Elimansia (35), Yusuph Salum (38), Shaban Juma (38) na Mwamudu Ramadhani (39).
“Tulifanikiwa kuwakamata watuhumiwa hawa kutokana na ushirikiano uliopo kati ya jeshi na Tanesco na kupitia operesheni mbalimbali za usiku na mchana ambazo tumekuwa tukizifanya maeneo ya jiji hili,” amesema Mambosasa.
Amefafanua kuwa watuhumiwa hao baada ya kuiba mafuta na kuyauza kwenye kampuni zinazohusika na uuzaji wa mafuta na kwamba yalinunuliwa na watu wanaojulikana kama Selemani Mrutu na Praygod Kimaro.
“Polisi walikwenda kwenye ghala linalomilikiwa na Kimario na Mrutu lililopo maeneo ya Tabata Dampo, lakini watuhumiwa hao walikimbilia. Katika msako tulikuta makontena 68 ya lita 20 kila moja na kukuta mapipa ya lita 200 yaliyojaa mafuta ya transfoma,” alisema.
Kwa mujibu wa Mambosasa, watuhumiwa hao walichanganya mafuta ya transfoma na vimiminika vingine kutoka kwenye kampuni nyingine zinazouza mafuta na kuuza kwa wateja wao.
Alisema watuhumiwa watafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi katika kesi hiyo utakapokamilika.