Wapanga kumburuza Babu wa loliondo kortini

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,322
33,126
BABU KORTINI

Na Makongoro Oging'
Baadhi ya wagonjwa wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi waliokunywa kikombe cha Mchungaji Ambilikile Masapile (pichani) mwaka huu katika Kijiji cha Samunge, Loliondo mkoani Arusha hatimaye wameamua kumburuza mahakamani kiongozi huyo kwa madai kwamba dawa yake haitibu kabisa na wamedanyanywa.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti wiki iliyopita kwa sharti la kutoandikwa majina yao, watu hao ambao wako katika Muungano wa Vyama vya Watu Wanaoishi na Virusi vya Ukimwi Tanzania (TANOPHA) walisema kwamba wao ni kati ya waathirika waliopelekwa na chama chao Samunge kupata tiba lakini cha ajabu ni kwamba tangu wanywe dawa hiyo wamekuwa wakipimwa hospitalini na kuonekana kuwa bado wana virusi vya ugonjwa huo.

Waliendelea kusema kwamba kila wakienda kupima ili waone kama wamepona, wamekuwa wakielezwa na daktari kwamba hakuna mabadiliko na kikombe hakijawasaidia lolote lile, hivyo wameona ni udanganyifu na utapeli mkubwa hivyo wameamua kumfikisha mahakamani wakati wowote.

“Hatuwezi kupoteza muda na fedha zetu kwa kwenda kunywa dawa ambayo haitibu, hii ni kuwarubuni wananchi, wengi wameuza mali zao, wengine kutumia akiba ya fedha walizokuwanazo kwenda Loliondo wakijua kwamba wangepona lakini cha kushangaza ni kwamba baadhi yetu wanakufa.

“Wengine wako mahututi baada ya kupewa kikombe, tulikuwa na matumaini ya kupona hadi tuliacha kutumia vidonge vya kurefucha maisha vya ARV, hatuna mengi zaidi ila tunaomba umtafute mwenyekiti wetu akueleza zaidi,” alisema mmoja wa wanachama hao.

NIA YA MWENYEKITI WA TANOPHA
Mwenyekiti wa TANOPHA, Julius Kaaya alipotafutwa kwa njia ya simu juzi ili kueleza madai hayo ya wanachama wake, alisema kwamba ni kweli walipelekwa watu 14 kwenda kunywa dawa Loliondo lakini hakuna hata mmoja aliyepona kwani kila wanapopimwa hospitalini wanaonekana bado wana virusi.

“Nakumbuka kwamba kipindi tunaenda huko Loliondo Machi, 19 mwaka huu tulifanya mkutano na waandishi wa habari, tulifika Samunge Machi 22, ambapo Machi 24 walikunywa dawa hiyo kila mmoja akiwa na matumaini ya kupona, baada ya siku 20 tangu wanywe dawa hiyo walienda hospitali kuangalia kama wamepona, daktari aliwaambia hakuna hata mmoja aliyepona, “ alisema Kaaya.

Aidha, aliendelea kusema kwamba wanachama hao hawakukata tamaa , baada ya siku 90 walirudi tena hospitalini kuangalia kama kuna hauweni, daktari aliwapima na kuwaambia hakuna mabadiliko hata kwa mtu mmoja.
Aliendelea kusema kwamba wanachama hao baada ya kuelezwa hivyo walikata tamaa na kuamua kuendelea kutumia ARV.

“Wengi ambao tunajua kwamba wana HIV na walikunywa kikombe wanapukutika na hata juzi tulihudhuria mazishi ya mmoja wapo, hii dawa haitibu kwani kuna wagonjwa wa kisukari ambao waliinywa hawajapona .

“TANOPHA ina vyama 230 vilivyosajiliwa na mimi ndiye mwenyekiti wao, nimekuwa nikipokea taarifa za baadhi ya wanachama wetu waliokwenda Samunge ambao waliacha kutumia ARV wakijua kwamba wamepona, wengi wamefariki.

“Babu wa Loliondo amedanganywa na shetani na siyo kwamba alielezwa na Mungu, nashangaa viongozi wa dini wanaompigia debe wakati wao siyo wataalamu wa kujua kama dawa hiyo inaponya au la, ni ushabiki wa kidini usiokuwa na maana, lengo lao ni kuchuma fedha kwa wagonjwa.

Kwa nini wasiwaachie wataalamu kushughulikia suala hilo?
“Wanasiasa waliokunywa dawa hiyo na kupigwa picha na vyombo vya habari walihamasisha wananchi kwenda huko kunywa dawa, hawakupaswa kufanya hivyo, wao kama viongozi wangesubiri kwanza wapate matokeo ya utafiti wa Wizara ya Afya.

“Ni kiongozi gani aliyejitokeza na kuonyesha cheti chake hadharani mbele ya vyombo vya habari kwamba amepona, wanaona aibu, ile siyo dawa ni maji tu.

“Wizara ya Afya nao wameingiliwa na wanasiasa ambao wamekuwa wakidai kwamba inatibu wakati Waziri wa Afya kwa upande wake anasema kwamba dawa ya Ukimwi bado haijapatikana duniani.

“Wizara inasema bado wanaendelea kuifanyia uchunguzi hiyo dawa ya Masapile,mpaka lini? Watutajie wangapi walikunywa maana mpaka sasa hakuna idadi kamili, kwa kweli wengi wamefariki ,wengine wako hoi, nawashauri wasiache kutumia ARV.

“Wanaoishi na virusi wasione aibu wajiamini watumie ARV, watambue kwamba ni tatizo limeshawapata na wakifanya hivyo bila kuwa na hofu wanaweza kuishi miaka mingi,” alisema Kaaya.

Alipoelezwa kuwa kuna watu waliokunywa kikombe wanataka kumfikisha mahakamani Mchungaji Masapile, Kaaya alisema hata yeye yupo tayari endapo atampata mtu wa kumsaidia kufungua kesi.

“Masapile ameharibu taifa, ingekuwa kesi inafunguliwa bure kwa kweli ningeshafanya hivyo na kama wanachama wangu wameamua kumfikisha kortini, nawaunga mkono,” alisema Kaaya.

MCHUNGAJI MTIKILA
Naye Mchungaji wa Kanisa la Full Salvation, Christopher Mtikila kwa upande wake amesema kwamba dawa hiyo haitibu na analishughulikia suala hilo ili kumfikisha mahakamani pamoja na mawaziri, wabunge na viongozi wa juu waliokunywa kikombe.

“Mawaziri hao wamewahamasisha wananchi kwenda Loliondo kunywa dawa, lazima tuwashitaki pamoja na viongozi wa dini waliopiga debe,” alisema Mtikila. Viongozi wa dini waliohamasisha ni Askofu Thomas Laizer na Martine Shayo.

Baadhi ya Mawaziri waliopata kikombe ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Sera na Uratibu wa Bunge), William Lukuvi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira, Waziri wa Ujenzi, John Magufuli.Wabunge ni Augustine Mrema, Edward Lowassa na wakuu wa mikoa ni Yohana Balele na Abbas Kandoro.

MAJIBU YA BABU KWA WASIOPONA
Mwandishi wetu wa Arusha wiki iliyopita alizungumza na msaidizi wa Mchungaji Masapile kwa njia ya simu, Paulina Lucas na kuulizwa kuhusu malalamiko hayo akasema wasiopona ni wale ambao hawana imani.

“Kama hawajapona siyo makosa yetu. Tuliwaambia kabla kuwa katika tiba hii kigezo cha kwanza ni kuwa na imani na hapa tuna uthibitisho wa kutosha wa watu walioponywa na maajabu ya dawa hii wakiwemo wagonjwa wenye Ukimwi,” alisema Paulina.

Alidai kuwa kuna baadhi ya watu wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi si wakweli kwani kuna uwezekano kuwa wamepona lakini wanashindwa kuweka wazi kwa malengo ya kukosa fedha wanazopewa na wafadhili.

Chanzo:BABU KORTINI - Global Publishers
 
Msimlaumu Babu wa watu wala kiongozi yeyote wa dini maana wao ni viongozi wanaohubiri suala la imani na Babu alisema kabisa wazi kwamba ili mtu upone inabidi uwe na imani, sijui kwanini watu walikuwa wagumu kuelewa.
Viongozi wa Serikali walisema pia wazi kwamba hakuna uthibitisho wowote wa kisayansi uliogundua kwamba dawa hio inafanya kazi. Sasa walioenda wametumia uhuru wao wenyewe wa kuamua na wakaamua waende kutibiwa ili wapone kama wataamini. Ni kama kwenda kwenye mkutano wa kiroho vile au mganga...! Kisheria hakuna kosa ila wananchi wenyewe ndo wamejiingiza mkenge kwa sisi wasomi tunasema "volenti non fit injuria"
Hata Yesu alisema aaminiye ataokoka...! Pole kwa wasioamini.
 
Imani yao ndio iliyotakiwa kuwaponya...imani yao ikakataa kuwaponya.

Imani yao ndio inayotakiwa kufikisha kortini..kama kweli wana nia.Wamwache babu wa watu maana yeye hakusema ni daktari wala mtenda miujiza.Kama walichagua kutokumuelewa aliposema imani ya wanywaji ndo itakayowapona ni makosa yao wenyewe!
 
Babu ndio kawambukiza Ukimwi?

Babu nae alikosa Mwanasheria yaani Angewasainisha kuwa usipotumia imani hutopona baada ya hapo No Kesi

But Si Walienda wenyewe kwa hiali yao na hawakuwekeana Mikataba yaani kwa kuwa na imani potofu Ndio ushitaki tatizo DP atawasilisha ushahidi Dhaifu na babu atakuwa huru Wengine walishapona

Endapo hao wenye ukimwi wakishinda kesi Fidia yao babu atambiwa awarejeshee mia tano tano zao.

Mwendo huu Watakuja kumdai hadi Mwenyezi.
 
ashitakiwe kwani lilikuwa ni dili la kujichotea mahela akishiriana na hao viongozi wa dini
 
hii thread imenifurahisha japo ni ya kuhuzunisha! manake in my young days nilikuwa najiuliza iweje mumlipie mgonjwa bill ya hospitali na dawa, washindwe kumtibu akifa mnalipia na mortuary! hebu washtaki tupate mwanga,lol
 
mamabo mengine hadi yanachekesha,

jamani mwacheni babu wa watu apumzike baada ya kazi ngumu, walipokuwa wanajipeleka huko loliondo kama vichaa hawakusikia la muazini wala la mpiga kengele, leo ndo wanajua mahakama iliko? kwani walikuwa na mkataba wowote na babu? je hadi leo wameishakunywa dawa za waganga wangapi na hawajapona? iweje wa kushtakiwa awe ni babu tu? kwa kweli kesi kama hiyo ni upuuzi mtupu!

vikesi vingine kwa kweli vinamaliza stationery za mahakama zetu bure, havina hata hadhi ya kusajiliwa mahakamanini, ni vya kutupilia mbali mara moja!
 
Hii imenikumbusha alichosema TB Joshua! Kwamba wachungaji wengi (healing ministries) wanawaombea watu, wasipopona wanajitetea kuwa imani yako haba! Imagine mtu aliyeuza shamba akapata nauli kusafiiri kwa shida unamwambia imani yake haba! Kipimo cha imani ni nini?

Babu was either smart au huyo mungu wake alimpa tricky hiyo, au kulikuwa na brain nyingine behind Babu yeye akatumika tu!
 
Lakini huyu Babu Ambilikile Mwasapila si kabla ya kupata kikombe si nasikia alikuwa akitoa somo ikijumhisha na ibada na akisisitiza ya kwamba m2 apataye kikombe lazima uwe na Imani. Kwani alikuwa anawalazimisha wa2 kunywa? Mi wakati wa2 wanafurika huko wengi walikuwa wanarudi wakiwa na furaha lakini leo ni mambo ya mahakamani. Na nasikia mpk leo kuna magari ya kwenda huko na ina stendi yao binafsi. Okey! Hebu ngoja 2one mwisho wake.
 
I don't believe kuwa watu hawakuwa na imani ndo waspone mtu atoke iringa mufindi na alipe nauli ya laki na nusu uniambie hana iman.
 
Suala la babu halihusiani na imani bali lilikuwa la kisanii toka mwanzo! We kept on insisting this time and time again lakini watu walikuwa vipofu na hawakuwa na masikio!

Kuna tofauti kubwa kati ya kuombewa ili upone na Mtumishi wa Mungu ambako neno la Mungu linasema inahitajika imani ili uweze kupkea huo muujiza na kitendo cha kupewa kikombe bila kuombewa wala nini!

kikubwa kuliko vyote wakati Mtumishi wa mungu note the use of word Mungu & mungu,alipokuwa akitoa kikombe je? Alikuwa akiwahubiria wagonjwa habari njema ili waokoke? Au nia yake ilikuwa tu kuponya miili yao kutoka kwenye magonjwa? je,si vizuri sana kwa Mungu watu kuponywa roho zao na si mwili maana kinachorudi kwa baba ni roho na si mwili.

Mungu anahitaji roho zetu zirudi kwake na si miili yetu! Remember man is a spirit,he has a soul and he lives in the body! Mungu wa Ibrahim,Isaka na Yakobo anataka roho zetu zisipotee.
 
mamabo mengine hadi yanachekesha,

jamani mwacheni babu wa watu apumzike baada ya kazi ngumu, walipokuwa wanajipeleka huko loliondo kama vichaa hawakusikia la muazini wala la mpiga kengele, leo ndo wanajua mahakama iliko? kwani walikuwa na mkataba wowote na babu? je hadi leo wameishakunywa dawa za waganga wangapi na hawajapona? iweje wa kushtakiwa awe ni babu tu? kwa kweli kesi kama hiyo ni upuuzi mtupu!

vikesi vingine kwa kweli vinamaliza stationery za mahakama zetu bure, havina hata hadhi ya kusajiliwa mahakamanini, ni vya kutupilia mbali mara moja!

Ningeshangaa nisingeona comment yako kwenye hii thread Miss
 
Back
Top Bottom