BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,013
Uteuzi mpya CCM wavuruga wabunge
Mwandishi Wetu Machi 11, 2009
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
Mwandishi Wetu Machi 11, 2009
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
BAADHI ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wana matumbo joto kutokana na mabadiliko makubwa yaliyofanywa na chama chao katika utaratibu wa kuteua wagombea yanayoweza kuwatupa nje kwa kushindwa kutetea nafasi zao.
Miongoni mwa wabunge hao ni pamoja na baadhi ya mawaziri ambao sasa wanayaona mabadiliko hayo kuwa yanayowachonganisha na wapiga kura wao kwa kuwa wengi wao hawakuwahi kurejea majimboni kushukuru kwa kuchaguliwa.
Mabadiliko hayo yamefuta utaratibu wa zamani wa upigaji kura za maoni katika kuwapata wagombea wa ubunge, uwakilishi na udiwani. Utaratibu wa zamani uliwapa fursa hiyo wanachama wachache, tofauti na sasa ambapo wagombea watapigiwa kura na wanachama wote, kuanzia ngazi ya tawi.
Katika kufanikisha utaratibu huo, wagombea wote wa nafasi husika watafanya ziara ya pamoja na kutumia usafiri ulioandaliwa kwa gharama za chama hicho, lengo likiwa ni kuhakikisha kila mgombea anapata haki sawa.
Taarifa za kichunguzi zinasema baadhi ya wabunge, licha ya kutimiza takriban miaka mitatu ya ubunge katika kipindi hiki cha Serikali ya Awamu ya Nne, hawajahi kutembelea maeneo yote ya majimbo yao na hata katika maeneo waliyokuwa wakitembelea wamekuwa na uhusiano wa karibu zaidi na viongozi wa chama hicho kuliko wanachama wa kawaida.
Kwa sasa CCM ina wabunge wa majimbo 205, lakini taarifa kutoka katika majimbo hayo, zikiwanukuu baadhi ya viongozi wa chama hicho na baadhi ya wananchama, zinaonyesha kuwa hali ni mbaya kwa baadhi ya wabunge wa sasa.
Kwa upande mwingine taarifa hizo zinabainisha kuwa utaratibu huo mpya wa kura za maoni utawasaidia mno baadhi ya wabunge, hususan katika majimbo ambayo viongozi wa chama ngazi ya wilaya (jimbo) walikuwa wakiwapiga vita lakini idadi kubwa ya wanachama wa kawaida wameonyesha mapenzi yao kwao.
Inaelezwa kuwa karibu katika kila mkoa wa Tanzania Bara, baadhi ya wabunge wa CCM wataumizwa na utaratibu huo mpya.
Mwezi uliopita, Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, aliwaonya wabunge kuwa wanarejea majimboni kwao pengine kutokana na kubaini kuwa baadhi yao waliyatupa majimbo yao baada ya kura za nwaka 2005.
Kikwete alitoa onyo hilo wakati anahutubia katika maadhimisho ya miaka 32 ya CCM katika Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.
Ingawa imebaki miaka miwili kabla ya Uchaguzi Mkuu, ni wakati sasa kwa wabunge ambao wametelekeza majimbo yao kuwatembelea wananchi, kabla wananchi hao hawajaamua kutowapigia kura, alisema Kikwete na kuongeza:
Kutembelea jimbo ni jambo muhimu katika kujihakikishia kuwa wewe mbunge unaendelea kubaki madarakani katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Inadaiwa kuwa wabunge wengi wamekuwa hawafiki majimboni wakitoa sababu ya kubanwa na shughuli za Kamati za Kudumu za Bunge.
Lakini hata kwa sababu hiyo Rais Kikwete alisema: Kutumia sababu kuwa umebanwa na shughuli za kamati hakuwezi kukusaidia katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Lakini wakati baadhi ya wabunge wakiwa wamebanwa na utaratibu mpya tofauti na ule wa zamani ambao mbinu kubwa ya ushindi ilikuwa ni kuwa karibu (hata kwa kusaidia shida binafsi) na viongozi na wajumbe wa mkutano husika katika kupiga kura za maoni kumpendekeza mgombea, utaratibu huu mpya pia unatarajiwa kuingiza wanachama wengi katika CCM, hususan wakati wa kusaka wagombea.
Inaelezwa kuwa kutokana na utaratibu huu kutoa nafasi kwa wanachama kupiga kura za kupendekeza mgombea, baadhi ya wagombea wapya au wa zamani watalazimika kuingiza wanachama wapya kwa wingi kwa lengo la kujiongezea idadi ya wapiga kura.
Hatari iliyopo katika hatua hiyo inatajwa kuwa ni pamoja na chama hicho kupata wanachama mamluki, wasio na malengo ya kukitumikia chama hicho, wakiwa na malengo ya kukidhi maslahi binafsi ya mgombea husika na ya kwao.
Inaelezwa pia ya kuwa chini ya utaratibu huu, viongozi watalazimika kupigana vikumbo kufungua matawi mapya ya chama na kununua kadi nyingi ili kuzitoa kwa wanachama wapya matawini. Wachambuzi wengine wa masuala ya siasa wanaeleza kuwa kuna hatari ya wagombea kuhodhi matawi, hali inayoweza kusogeza mpasuko wa kitaifa wa chama hicho hadi ngazi ya matawi.
Faida kubwa ya mabadiliko hayo inatajwa kuwa ni kupunguza kile kinachoweza kuitwa mashindano ya kutoa rushwa, kwamba aliyetoa rushwa kubwa zaidi ndiye mshindi.
Hata hivyo, faida hii inaangaliwa kwa tahadhari kubwa na baadhi ya wachambuzi wa masuala ya siasa, wakisema utaratibu huo hauwezi kuwa na tija au kufikia malengo yanayotarajiwa kama usimamizi wake hautazingatia misingi ya haki na badala yake kutumika kufanikisha malengo binafsi.
Raia Mwema ilizungumza na baadhi ya wanachama wa kawaida wa chama hicho ambao wengi walifurahia utaratibu huo kwa kile walichoeleza kuwa wakati wa viongozi na wajumbe wa iliyokuwa mikutano ya kupendekeza wagombea kutamba kuwa wamepata fedha (rushwa) nono mitaani umefika ukingoni.
Na wengine walikwenda mbali zaidi wakisema wakati wa wagombea kuteka wajumbe wa mkutano na kuwaficha hotelini ili kuwaweka sawa (kwa rushwa) ili wawape kura umekwisha na kwamba wanaamini kuwa hawatapata wakati mgumu kunadi wagombea kwa kuwa wagombea watakaopatikana watakuwa wanakubalika na sehemu kubwa ya wanachama na wananchi wa eneo husika.
CCM ilipitisha utaratibu huo mpya katika mkutano wake wa Halmashauri Kuu Taifa (NEC) uliofanyika mjini Dodoma mwishoni mwa wiki iliyopita.