Rare Sapphire
JF-Expert Member
- Jul 24, 2021
- 576
- 1,626
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
HALI YA UBORA WA MRADI WA JNHPP NA UHIFADHI WA WANYAMA PORI
Jumapili, 10 Septemba 2023.
Kuna taarifa zinasambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu mradi wetu wa Bwawa la Kufua Umeme la Mwalimu Nyerere (JNHPP). Taarifa hizo zinaelezea na kuleta hofu kuhusu Ubora wa Mradi, pamoja na Uhifadhi wa wanyama pori.
Taarifa sahihi kuhusu mradi wetu ni kwamba, mradi huu umesanifiwa kwa kuzingatia ubora wa hali ya juu na ujenzi wake unasimamiwa na wataalam walio bobea kwenye fani ya ujenzi(Civil Engineering) na Usimikaji Mitambo(Electromechanical Engineering) kutoka ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha tunapata mradi ulio bora.
Kila hatua ya mradi hukaguliwa na kuhakikiwa kabla ya kwenda kwenye hatua nyingine, na pale ambapo hatua iliyotekelezwa inashindwa kufuzu ukaguzi na uhakiki basi marekebisho hufanyika kabla ya kuendelea hatua inayo fuata.
Bwawa letu ndani ya kuta zake limesimikwa vifaa vinavyo pima uimara kadri maji yanavyoingia kwenye bwawa, vifaa hivyo vina pima kama kuna hitilafu zozote zitakazo hatarisha ubora wa bwawa. Mpaka mwisho wa mwezi Agosti bwawa letu lina ujazo wa maji yalioingia wa mita za ujazo zaidi ya bilioni 14, na uzito wa maji unahimiliwa vizuri na bwawa letu kwani hakuna tatizo lolote la ubora au uimara linaloonekana kupitia vifaa vilivyosimikwa kwenye bwawa hilo.
Vilevile, uhifadhi wa wanyama pori na utunzaji wa mazingira unazingatiwa kama vile ilivyoainishwa katika mpango uliopitishwa wakati mradi huu unaanza kutekelezwa.
Mpaka mwezi Agosti 2023, Mradi mzima wa ujenzi umefikia asilimia 91.72%, na ni matarajio yetu mitambo yote itakuwa imefika nchini kabla ya mwisho wa mwezi Disemba 2023, na tutaanza kujaribu kupitisha maji kwenye mitambo mitatu ya kwanza mwezi Februari na tunategemea kupata Umeme wa kwanza mwezi Juni 2024 kama tulivyo ahidi.
Tunashukuru wananchi kwa kushirikiana nasi katika safari hii ya kujenga taifa letu, na hususan ufuatiliaji wa maendeleo ya mradi wetu huu mkubwa wenye manufaa makubwa kwa Taifa letu.
Imetolewa Na;
KURUGENZI YA MAWASILIANO NA UHUSIANO KWA UMMA TANESCO- MAKAO MAKUU.
DODOMA
Pia soma: Bwala la kufua umeme la Mwl. Nyerere, limeanza kutoa nyufa