Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,810
- 15,398
Na ukijaribu kunipiga tu, utajua mimi ni mwanamke wa namna gani, hutakuja kunisahau..........!
Uzoefu unaonesha kwamba baadhi ya wanaume au wanawake hutumia kile walichokiona kutoka kwa wazazi wao katika ndoa zao. Tabia za wazazi huakisi sana maisha ya watoto wao hususan katika maisha yao ya ndoa, labda kama watajitambua na kujivua gamba, lakini vinginevyo watakuwa wanatumia kile walichokiona na kujifunza kutoka kwa wazazi wao. Kwa mfano mwanamke anayeishi na mwanaume mnyanyasaji na mpigani, ni dhahiri kama wana mtoto wa kiume anakuwa na uwezekanao mara saba zaidi kuja kuwa mnyanyasaji kwa mkewe atakapokuwa mkubwa. Na kama ni binti ana uwezekanao mara tatu zaidi kuja kuwa mtu wa kupata vipigo atakapokuwa ameolewa. Hapa wa kulaumiwa ni wazazi, kwa sababu wao ndio wamewafanya wawe hivyo. Kwa kuwa wazazi ndio mashujaa wa watoto wao, huakisi tabia halisi za wazazi wao.
Hebu fikiria una miaka sita na unasikia ukiwa kwenye chumba chako baba yako anapompiga mama yako! Mama yako anapiga mayowe na kulia akiomba msaada! Unamsikia baba yako akimpiga mama yako ngumi na mateke na kumwita majina machafu machafu ambayo kimsingi hutakiwi kuyasikia. Utafanya nini ukiwa ni mtoto na uko katika mazingira kama haya? Ukweli ni kwamba huwezi kuondoka! Na unakuwa huna uchaguzi zaidi yakukubali kuishi na wazazi wako ambao kimsingi aina ya maisha wanayoishi sio kama mke na mume bali mume na mtumwa wake ambaye ni mama yako. Unalazimishwa kuishi hivyo, hutaki hata marafiki zako waje nyumbani kwenu. Mama kila siku ana manundu mwilini kwa vipigo kutoka kwa baba yako. Na si hivyo tu, baba kila siku akirudi nyumbani anaaanza kufoka! Na sasa siri zenu zote ziko nje. Pale mtaani familia yenu imekuwa ni gumzo, huna raha kama watoto wengine. Balaa gani hili!
Mie bado nawalaumu wanawake wanaokubali ujinga huu, ingawa kuna watu wananishambulia humu jamvini, lakini kwa hili siwezi kulinyamazia. Ni ujinga tu ndio unaosababisha wakubali kuishi kwenye ndoa za namna hii. Kama wewe ni binadamu kamili ambaye umezaliwa ukiwa na akili zako timamu, kwa nini ukubali kuishi na mwanaume mfuajaji ? Kama unataka kuishi na mwanaume wa aina hii, basi pinga usikubali kufanywa gunia la mazoezi. Simama imara ukiwa umeshika kikaango na umwambie, ‘Njoo unipige uone. Na siku ukijaribu kunipiga tu, utajua mimi ni mwanamke wa namna gani, hutakuja kusahau.' Au kama huwezi hilo basi zuia upigwaji kwa njia nyingine. Lakini uzoefu unaonesha kwamba, njia iliyo bora kabisa ni kuondoka kwenye uhusiano huo.
Kama uko kwenye ndoa ya mateso na unajikuta huwezi kutoka, umekubali kuwa fuko la mazoezi la mumeo, jiulize ni kwa nini. Anzia kwa wazazi waliokulea na kujiuliza kama wewe siyo mama yako ambaye alikubali kupokea vipigo kwa mumewe huku akiendelea kuvumilia na kuishi katika ndoa hiyo ya mateso. Kama ndivyo, basi kataa kuwa mama yako. Anza safari ya kuwa wewe ambaye huko tayari kuwa mtumwa wa mtu kwa kuhofia kusimama mwenyewe kwa miguu yako. Amua sasa na utamudu, kwani wewe ni binadamu kamili na huhitaji kukamilishwa na mtu mwingine.