Mwamtafuta Mchungaji? Ni Mimi...

Nimekuwa napokea subliminal messages kwa muda mrefu, makombora kwa muda mrefu watu wakihoji huyu Mchungaji ni nani, anajua nini, anapata wapi habari zake, lengo lake ni nini, anakaa wapi, anamipango gani ya baadaye kugombea na mengine mengi.

Basi nawarahisishia msiendelee kupasuka mishipa na kukosa usingizi, iwe ni nyie Mafisadi na Vibaraka wao, UWT, Vyama vya Siasa au wengine wachangiaji humu jukwaani.

Mimi ni Raia, Mzalendo, Mwananchi wa Tanzania. Nawasilisha nafasi ya Mtanzania aliyeko Kasulu, Mpanda, Geita, Micheweni, Mbinga, Mafia, Arusha Mjini, London, Washington, Dubai, Pretoria na sehemu nyingine nyingi.

Kama mwakilishi wa Wananchi hawa, nafanya kazi yangu kwa mapenzi ya nchi yangu, ni wajibu wangu, ni kiapo changu kulitumikia Taifa langu, kwa manufaa ya Taifa na Wananchi wake.

Mwaniogopea nini, wakati mimi ni mtu wa kawaida tuu?

Ni mwiba katika ngozi zenu, nondo inayokomaza zege la Taifa, Kungwi kwa chipukizi kama Jmushi, Swahiba kwa wazee kama Kibunango.

Makao yangu ni mtaani, kijiweni, magazetini, sehemu ambako mwananchi anakaa, mahali ambako mwananchi hulia kilio cha Uzazi, kwenye Rubisi, Chipsi Dume, Msokoto, Slipuwei, hata kwenye vikao vyenu vya Siri!

Sasa najiuliza mwanitafuta kwa shauri gani ikiwa in Raia wa Kawaida? NImefanya nini kilichozua shauku lenu kujua Mchungaji ni nani?

Upevu na Upeo wa mawazo asili na msingi wake ni Kifimbo, kisha machungu ya maisha na kuwa mkweli kwa nafsi yakafuatia. Wepesi wa kuunganisha nukta kwa kutazama kile kile tunachotazama wote, ni Baraka za Mungu, sina Dataz wala kianzio cha Dataz kama Mzee mwenzangu Kamanda Mkuu.

Je mwataka niwafundishe kazi haswa nyie wa Umoja wa Waangalizi? Niwafundisheni kipi ambacho hamkujifunza Malindi, Kurasini, Monduli au Ngerengere?

Nyinyi mmesomea fani, kwa jasho la Taifa, wengine ni vipawa tuu, na baraka za Mola ndio maana maoni na uchambuzi wetu, huwachuna ngozi na kuwafanya vihiyo.

Kwa mlio mafisi wagombea nyama, mwaeza endelea angamiza zizi, lakini hata ujanja wenu kupangusa midomo ardhini kufuta damu, hakusaidii. Mchungaji na wenzake wapembuzi hung'amua ulafi wenu na kuuanika.

Ombi langu kwenu wote mnaonitafuta, fanyeni kazi zenu kwa viapo ili Mchungaji na Kondoo waishi kwa Amani, wakila Asali na Maziwa manono ambayo ni halali na haki yao.

Kuendelea kutupuuza, kutawafanya muendelee kujichanganya mkimtafuta ni nani Mchungaji, ni rafiki wa nani, amejuaje, ana nia gani na maswali mengine kemkem ambayo mngejijibu kama msingekuwa Wazembe na Walafi na kutuumiza siye Wakulima na Wafanyakazi wa Tanzania. Fanyeni kazi zenu kwa Bidii, Juhudi na Maarifa kwa Manufaa ya Mchungaji na Kondoo, nanhyi mtaishi kwa Amani bila wasiwasi au woga.

La mwisho, Uchungaji wangu ni wito, binafsi si wa kuombwa na mtu. Mawazo yenu wengine kuwa kama nitakuja sarandia Miliki na Himaya zenu sahauni, ishini kwa amani kwenye viti vyenu, mimi kazi ya Uchungaji naipenda, nitaendelea kuchambua mchicha na kutoa makapi kwenye nafaka mpaka tupate zao bora na nono kutushibisha.
[HASHTAG]#freemaxdemello[/HASHTAG]
 
Back
Top Bottom