Kamanda wa Zamu.(Mwanajeshi hatishii, hutenda)

Kudo

JF-Expert Member
Nov 2, 2017
1,809
6,081
RIWAYA; KAMANDA WA ZAMU.
NA; BAHATI K MWAMBA.
WHATSAPP; 0658564341.

1.
Alikuwa akitetemeka mwili na roho, jasho lilimmwagika hadi kwenye ncha za vidole vyake vya miguu na mikono, miwani aliyokuwa ameivaa ni kama haikuwa ikimsaidia kwa lolote kwa sababu hakuwa akiona mbali zaidi ya kuliona zulia lenye rangi nyekundu alilokuwa ametandika juu ya sakafu sebuleni kwake. Uvutaji wake wa hewa ulikuwa umebadilika kwa kiasi kikubwa na alikuwa akiivuta harakaharaka na kwa sauti kubwa kiasi kwamba mtu yeyote angelikuwa nje ya mlango wa nyumba yake angelisikia, kwa sababu ya kuvuta kiasi kikubwa cha hewa kuliko uwezo wa mapafu yake, kifua kilijaa na alianza kukohoa mfululizo hadi misuli ya kichwa ikamtutumka na jicho kuwa jekundu mithili ya pilipili hoho iliyovunwa. Kukohoa huko kilimfanya ainue shingo yake kwa mara ya kwanza tangu alipotembelewa na mgeni wa ajabu, mgeni ambae wakati huo alikuwa mbali na hapo alipokuwa. Macho yake yaliangukia pale alipokuwa amekaa mgeni ambae alimfanya akose amani kwa zaidi ya nusu saa nzima, aliuona mfuko uliokunjwa vema ukiwa umetulia palepale alipokuwa amekaa mgeni wake aliyeingia ndani kwake kwa namna ya ajabu ambayo hakuwahi kuitarajia kama itatokea kwenye maisha yake. Aliinuka huku miguu yake ikiwa haina nguvu kabisa na alikuwa akitetemeka, akaufikia mlango wake na kuufunga kwa funguo kisha akazitupa kwenye sofa na kurejea kukitazama kitasa cha mlango wake, alitikisa kichwa kwa kusikitika ni kama hakuwa anaamini kitu kilichokuwa kimetokea muda mfupi uliopita. Akainua macho yake na kutazama ukutani, akaiona saa ambayo mishale yake ilisoma majira ya saa saba na nusu usiku, muda wa wanga kama wasemavyo waswahili na kweli ulikuwa ni muda wa wanga na yeye ni mmoja wa watu waliowangiwa na kiumbe halisi ambae hakuhitaji mazingaombwe kuonekana. Utata kwake namna kiumbe yule alivyoweza kuingia ndani kwake ikiwa alifunga milango yote, kuanzia mageti mawili ya nje na milango miwili, wa kuingilia sebuleni na ule wa kuingia kwenye chumba alichokuwa akilala. Alikaa kwenye sofa huku akizishusha pumzi zake kwa nguvu na ahueni ya kuona ni angalau amebaki peke yake ndani ya nyumba yake aliyoanza kuiogopa. Akili yake ilianza kuchanganua mambo kwa usahihi kidogo baada ya hofu kuanza kutoweka, akakumbuka kuitafuta simu yake na mikono yake ilianza kujipapasa na alijikuta akiangusha tabasamu la chuki baada ya kugundua alikuwa amevaa boksa na hakuwa na nguo nyingine yoyote mwilini mwake, akainuka kivivu na kuelekea chumbani kwake, akaikuta simu ipo kitandani kando ya mto aliokuwa ameegesha kichwa chake wakati alipoenda kulala. Akaichukua na kuanza kuzitafuta namba za simu za watu kadhaa aliiona wanastahili kujua kilichomkuta na ikiwezekana washauriane jambo la kufanya. Majina mengi aliyapita ijapokuwa yote yalikuwa na umuhimu mkubwa kwake, lakini jina moja likapata hadhi ya kuwa nambari moja kupigiwa na lilikuwa ni jina la aliyewahi kuwa bosi wake kwenye benki ambayo alikuwa akiifanyia kazi hadi wakati huo wakati bosi wake huyo akiwa anafanya kazi tawi jingine la benki hiyohiyo aliyokuwa akiifanyia kazi.
“Hujui ni muda wa kutafuta watoto we kijana! Au hujui mi ni mke wa mtu na huu ni wasaa sahihi wa mume kunimiliki?” Sauti ya mwanamke wa makamo ilifoka kimasihara huku mwisho ikimalizia kwa cheko la usichukulie siriuzi mpenzi..
“Kabina!” Jamaa aliita kwa sauti ambayo haikuonekana kulainishwa na utani wa mwanamke aliyetoka katikati ya usingizi mzito. Upande wa pili ulikaa kimya kwa sekunde zipatazo thelathini hivi kabla ya kusikika tena..
“Miaka zaidi ya sita sijawahi kusikia ukiniita kwa jina langu... Kuna tatizo?” Kabina aliuliza akiwa mnyonge wa sauti, hakuwa ametarajia kuitwa hivyo na mwanaume ambae alikuwa ni tulizo la nafsi yake, mwanaume aliyejua kuusindikiza utu uzima wake akiwa mjane wa watoto wawili waliozodiwa na mwanaume wake kwa umri wa miaka sita pekee, kiufupi alikuwa anapapatuliwa na kijana mwenye rika la wanawe wa kuzaa, lakini angeliona vipi ajabu ikiwa moyo hauna soni? Moyo waweza penda pasipofikiriwa seuze kwa kijana barobaro mwenye sifa zote za kuwa mume wa mtu? Mshangaeni lakini mwenzenu hujihisi fahari akiwekwa kwenye kona ya uwanja usio na aibu, uwanja wa fujo za kidunia, kwake ilikuwa ni fahari kupelekwa puta, iwe mashariki ama magharibi ilimradi nafsi yake itasuuzika na mwili utaondolewa uchovu wote na kuachwa salama na barobaro wake.
“Tatizo lipo!” Jamaa alisema kwa sauti ileile isiyotetereshwa na lawama za mpenzi wake, mpenzi ambae alimfaa kwa kila hali; alimtoa mtaani alipokuwa akihangaikia ajira na kumwajiri kwenye benki kubwa aliyokuwa akiisimamia kama meneja, akamtoa kuishi kwenye mitaa yenye waswahili wengi na kumpangishia kwenye mitaa ya watu wastaarabu, ambao waswahili waliwaita washua. Alimtoa kwenye usafiri wa daladala na bodaboda na kumnunulia gari zuri la kutembelea lenye hadhi ya ujana wake. Joseph Mkweche aliamua kuyalipa yote aliyoyendewa na mwanamama huyo kwa suluba ya sita kwa sita, alihakikisha haishiwi mbinu za kumchakaza mwanamama huyo ambae alinogewa haswaa na ufundi wake na kila akifikishwa mlimani iwe kwa kutafunwa au kulambwa kama koni, alihakikisha anatoa zawadi nzuri zaidi ili asije kuzikosa raha hizo na zikahamia kwa mwanamke mwingine.
“Tatizo gani?” Kabina aliuliza kwa sauti yake halisi, sauti ambayo ni wafanyakazi wake pekee huwa wanaelewa ina maana gani wakiisikia, sauti isiyo na chembe ya mzaha.
“Fisi mwekundu!” Joseph alisema huku akimeza mate, lakini hakupewa nafasi ya kuzungumza neno la ziada.
“Usizunguke sana.. sema tatizo!” Kabina Mkwepu alifoka kwa sauti kubwa, Joseph aliisikia vema na alitambua mwenzake alikuwa kwenye mchecheto mkubwa wa kutaka kujua tatizo.
“Nimekwambia ni Fisi mwekundu. Tatizo ni Fisi mwekundu.” Joseph alisisitiza.
“Una maanisha nini unaposema Fisi mwekundu?” Kabina aliuliza akiwa haelewi sawasawa kilichomaanishwa.
“Usitake kunambia jambo la muhimu namna ile ulishalisahau kirahisi hivyo, kuwa makini kidogo kwenye kumbukumbu zako.” Joseph alimwakia.
“Fisi...mmmh Fisi, Fisi.. oh my God! Unamaanisha Mbitiyaza?” Kabina aliuliza kwa wahka huku sauti ya godoro ikisikika kumaanisha alikuwa anashuka kitandani.
“Kumbe hujazeeka, ni huyohuyo Mbitiyaza kwa kisukuma na ulinitafsilia mwenyewe kuwa ni Fisi mwekundu kwa kiswahili.”
“Imekuwaje tena?” Kabina aliuliza huku mapigo yake ya moyo yakianza kuongeza kasi ya usukumaji damu, kwake hilo jina lilimaanisha matatizo na popote likitajwa yeye hukosa amani kabisa.
“Alikuwa hapa kwangu dakika kumi zilizopita.” Joseph alisema.
“Kwako? Aliwezaje kufika hapo? Una uhakika na unachokisema?” Kabina aliuliza akiwa haamini anachoambiwa.
“Unanibishia au huniamini? Unahisi naweza kuweka utani kwa kulitaja jina kama hilo? Usinikosee tafadhali...” Joseph alitupa tuhuma ili maelezo yake yaaminike.
“Labda nikwambie kitu ambacho sikuwahi kukushirikisha, Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu alishakufa na alizikwa kwenye makaburi ya magereza akiwa na pingu mikononi, labda ulikuwa unamuota na ukaamua kuniharibia usingizi wangu.” Kabina alijaribu kumwelewesha.
“Sijawahi kuota nabebwa na mikono yenye joto kutoka kitandani kwangu hadi sebuleni, sijawahi kuota ndoto na nikaamka nikakuta nilichokiota kipo hadi sasa nakitazama. Ukweli mchungu, kama mlidhani Fisi mwekundu kafa mtakuwa mnakosea, jipangeni na anataka pesa zake.” Joseph Mkweche alisema kwa msisitizo.
“Huyo Shija uliyemuota kakwambia nini?” Kabina aliuliza.
“Amenambia kesho anakuja kuchukua milioni kumi na tano benki, anataka azikute hizo pesa kwenye dirisha langu. Amenihakikishia atakuwa benki saa tano na nusu ahsubuhi.” Joseph alisema alichoagizwa na mtu aliyeitwa Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu, mtu ambae walisadiki alishafariki miaka michache nyuma tena akiwa kwenye mikono ya askari magereza.
“Unaona sasa, nimekwambia umemuota Fisi mwekundu, mtu anawezaje kutaka kuingia benki kwa wizi atoe taarifa saa chache kabla ya muda wa uhalifu? Amka bwana, usingizi wa muda huu usitupite kirahisi na kama umenikumbuka ni vema unambie nije usiku huu kukumasaji kidogo mume wangu...” Kabina aliongea kwa kulegeza sauti.
“Kanambia muda huohuo pia atakuwa ofisini kwako kudai pesa yake, amenambia atawadai wote wenye pesa zake.” Joseph Mkweche akaongeza lakini ni kama hakuwa akieleweka kwa Kanika ambae aliishia kucheka kimahaba na kujaribu kumpooza kwa maneno matamu, hakuwa akiamini kama kweli mtu waliyethibitishiwa kifo chake anaweza kuwa hai ikiwa kifo chake kilitokea akiwa chini ya mikono ya taasisi imara ya ulinzi na usalama.
“Sijachanganyikiwa Kabina, nipo timamu na afya yangu na nikwambie ukweli..” Joseph alinyamaza kidogo kisha akaendelea..
“Jamaa haonekani kutania, anaweza kufanya kama alivyosema ila kama unahisi nipo ndotoni, naomba nikutakie usiku mwema na pole kwa usumbufu.” Alikata simu na kuitupa pembeni yake, usingizi haukuwa na faida yoyote kwake na badala, macho kodo bila hata lepe la usingizi na hakuwa tayari kulala, picha ya mwanaume mwenye mikono imara ikimnyanyua kitandani iliutisha ubongo wake, sauti nzito yenye mamlaka kutoka kwa mwanaume huyo aliyeingia ndani kwake kwa kufungua kitasa cha mlango kwa namna aliyojua yeye, ikawa ni tishio lingine la usingizi wake lakini tishio kubwa zaidi ni pale jamaa huyo mwenye nguvu za ajabu alipomkumbusha jambo ambalo alilishiriki miaka kadhaa iliyopita, jambo hilo lilisababisha mtikisiko mkubwa kwenye familia za baadhi ya watu ambao kwa asilimia kubwa hawakuwa na uhusika lakini msalaba ukawaangukia, wao waliohusika waliendelea na maisha yao kwa amani kabisa hadi siku hiyo aliyotembelewa na huyo mgeni ndipo alipoanza kuhisi amani yao ipo mashakani, angelipata vipi usingizi?
Wakati Joseph Mkweche akishindwa kupata hata lepe la usingizi ili kuyatafuta mapambazuko, Kabina Mkwepu nae hakuwa na amani moyoni mwake. Kitendo cha Joseph kumkatia simu na kisha kuacha kupokea alipompigia ni kama kiliamsha hisia zake zilizolala, hisia za ukweli wa alichaombiwa na ili kulithibitisha hilo ilimlazimu kufanya jambo ambalo alishalisahau kwa zaidi ya miezi kumi na sita, hakulisahau bahati mbaya, alilisahau makusudi kabisa na ilikuwa ni kwa lengo zuri la kiusalama baina yake na wenzake wachache ambao walishakubaliana kuwasiliana endapo kutakuwa na shida ya muhimu sana. Aliitafuta namba aliyokuwa ameihifadhi kwa jina la G.Afande. Akaipata na kuipiga, ikaita kwa mara ya kwanza na haikupokelewa, akasonya huku akirejea kuipiga tena ila ikabaki kuwa vilevile, haikupokelewa. Akatukana kimya kimya na kuiweka kando simu yake huku akianza kuwaza kitu cha kufanya kwa usiku huo ili kupata uhakika wa habari aliyoisikia, akakata shauri kwa kutaka kufanya jambo lingine lakini kabla hajaanza utekelezaji, simu yake ikaita na mpigaji alikuwa ni G.Afande.
“Nilikuwa katikati ya ufundi maana sikuwepo nyumbani kwa karibuni miezi mitatu.” Jamaa alisema huku akicheka.
“Ooh, pole sana kwa bugudha..” Kabina alisema huku nae akicheka.
“Kuna nini? Si kawaida simu yako!” Alisema.
“Huyo uliyekuwa unamfinya upo nae karibu?” Aliulizwa.
“Hapana! Simu yako ni ngumu kuisikiliza mbele ya mtu yeyote.” Jamaa alijibu.
“Sawa.. Unataarifa zozote kuhusu Fisi mwekundu?” Kabina aliuliza. Ukapita ukimya mfupi wa mshangao kwa yule bwana aliyeseviwa kwa jina la G.Afande.
“Una maanisha Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu?” G. Aliuliza.
“Kwani yupo mwingine unaemfahamu?”
“Huyo jamaa si tulishazika kila kitu kuhusu yeye? Unaniulizaje taarifa zake tena, au umemuota?”
“Hebu mpigie yule binti atupe uhakika, nahisi kuna kitu hakipo sawa.”
“Yule binti ni mtaalamu anaetumiwa na idara zetu zote za siri kunyamazisha watu, hawezi kufanya kosa lenye kutuchora. Pia shuhuda wetu alihakikisha jamaa anazikwa kwenye futi sita akiwa na pingu mikononi, haiwezi kuwa maajabu kwa lolote.”
“Mpigie akupashe lolote.. Mpigie sasa hivi.” Kabina alisema na kukata simu, akabaki akiwa anaitazama huku akianza kuingiwa na mawazo yaliyomfanya alikumbuke shuka lake, akalivuta na kulizungusha mwilini mwake ili limsaidie kupambana na ubaridi ulioivamia ngozi yake ghafla na asijue ni kwa sababu gani. Aliyakumbuka macho makali ya Shija Mbitiyaza, macho ambayo alipata kuyaona siku moja tu tena siku ambayo ilikuwa ni siku ya mwisho kabla ya tukio alilohusika nalo kutokea, aliyaona macho yenye ukatili wa kutisha na kuogofya na hata alipopewa sifa nzuri za mtu huyo bado hakuwa na imani na kile alichoambiwa, kwa hisia zake za kike alijikuta akimwogopa mtu huyo ambae alikuwa ameshapewa historia yake kwa kifupi sana, historia ambayo ilianzia huko Misungwi alikozaliwa na kukulia kisha ikahamia kwenye kambi ya jeshi la kujenga taifa huko Rwamkoma, wilayani Butiama mkoa wa Mara. Baada ya hapo ikahamia Orujolo, Arusha kwenye kambi ya jeshi la wananchi na haikuishia hapo tu, ikaenda hadi mkoani Morogoro kwenye kambi ya wanajeshi wenye sifa za ziada kuliko wenzao, sifa ya ukakamavu na usugu kiasi wakapachikwa jina la komando. Baada ya hapo wasifu wake uliendelea kutanuka pale alipokuwa miongoni mwa wanajeshi walioenda kujiunga na kundi la walinda amani nchini Sudan, baadae alienda kulinda amani nchini Mali na huko ndiko uanajeshi wake ulipokoma, alivyoenda sivyo alivyorudi. Alienda kwa kivuli cha mlinda amani lakini alirudi kama mzamiaji na aliufanya siri uwepo wake nchini kwake, miaka michache mbele maisha yalimfanya ajitokeze lakini kwa namna nyingine ambayo ni ngumu mtu kuilewa, jina lake aliongezea majina mengine mawili ili apate kazi kwenye moja ya kampuni za ulinzi zenye kuwalipa vizuri wafanyakazi wake, akafanikiwa kuipata na maisha yake yakaanza kusogea kwa namna ambayo hakuwa ameitarajia, maisha magumu ya mshahara usiokidhi mahitaji yake ya mwezi mzima, lakini hakuwa na namna zaidi ya kukubaliana na hali halisi ya maisha hayo mapya, maisha ya taabu na yaliyochangiwa na kujifichaficha kila muda ili kutotambulika na watu aliyoamini ni wabaya wake, watu walioiwinda roho yake usiku na mchana. Kitumbua chake kilichokuwa kinampa shibe kidogokidogo kikatumbukia nyongo, wasifu wake ukakoma akiwa kwenye moja ya magereza magumu kuyaishi na hapo ile hostoria yake asiyopenda kuisimulia kwa watu ikawa imetamatishwa kwa namna ambayo hata yeye hakuwa ameelewa, wakamzika na maisha yake.
“Lakini picha za mwili wake zilipigwa na tukaziona... Inawezekanaje arejee na uhai wake?” Kabina alizidi kujiuliza pasipo na kupata majibu.
“Itakuwa Jose alikuwa kwenye ndoto na hataki kuamini kama ilikuwa bahati ndoto mbaya kwake.” Aliwaza huku akikata shauri arejee kitandani ili asiendelee kuitafuta sonona ya kujilazimisha. Akajilaza chali na kujivuta shuka hadi kifuani, akafumba macho taratibu na kupiga mwayo wa kuita usingizi. Dakika moja haikukatika tangu ajilaze kitandani kabla ya simu yake kuita kwa fujo, akaipuuza ili kupima shida ya mpigaji kwa kuamini kama asingelipigiwa tena ina maana mpigaji hakuwa na shida ya maana sana, akaacha iite hadi ikate. Sekunde chache baadae ilianza kuita tena, akainuka taratibu na kuishika mkononi mwake, akalitazama jina la mpigaji, akajikuta akinywea kwa kuwa hakurajia kusikia habari njema.
“Tuna msiba mzito...” Sauti iliunguruma kwa wasiwasi.
“Msiba! Nani tena?” Kabina aliuliza kwa wahka.
“Yule binti ameaga Dunia, majirani wameiona maiti yake usiku huu baada ya kuona hatoki ndani tangu mchana na milango ipo wazi...”
“Amekufa kwa kuuawa au?”
“Ripoti ya awali inaonekana alikufa kwa kukosa pumzi, shingo yake ina alama za vidole na bado polisi wanafanyia kazi alama hizo.”
“Majirani wanasemaje?”
“Walimuona jamaa mmoja mrefu mwenye mwili wa chuma akiingia na hawakumuona akitoka hadi walipoigundua maiti ya mwenzao.”
“Alivaa nguo gani huyo mtu?”
“Kofia nyeusi, shati la damu ya mzee na suruali ya michezo..”
“Nakurudia sekunde chache...” Kabina alisema na kukata simu, haraka haraka alimpigia Joseph Mkweche aliyekuwa amelihifadhi jina lake kwenye simu kwa jina, Tulizo.
“Ulisema Fisi alikuwa amevaa nguo gani?” Aliuliza kwa sauti yenye kitetemeshi..
“Kofia, shati la damu ya mzee na suruali ya michezo na buti za jeshi...” Joseph alijibu.
“Basi unabahati kuwa hai, kamuua askari magereza wa kike jioni ya leo.. He’s alive..” Kabina alisema na kukata simu yake, akarejea kumpigia G.Afande..
“Fisi Mwekundu anaishi... Anaweza kuwa mzimu au mtu halisi ila yupo hai...” Alisema huku akitupa shuka kando na kushuka kitandani akiwa amejisitiri kwa nguo ya ndani pekee.
“Haiwezekani bwana...!”, Jamaa alikataa.
“Kwa hiyo unahisi nani kamuua dokta?” Aliulizwa.
“Wapo wengi wanaoweza kufanya hivyo, anaweza kuwa hata mpenzi wake.” Jamaa alijibu kinyonge.
“Mpenzi wake anaweza kuvaa nguo zenye ufanano na mgeni aliyemtembelea kijana wangu usiku huu?”
“Una maanisha mtu mwenye mavazi kama yaliyokwenye ripoti ya upelelezi amemtembelea mtu wako? Kasemaje mtu huyo? Huyo kijana anamjua Fisi Mwekundu?”
“Joseph hawezi kunidanganya mimi wala hawezi kukudanganya. Shija Mbitiyaza amemtembea usiku huu na amemwambia kesho anaenda kuzifuata pesa zake benki kuanzia saa tano ahsubuhi.”
“Una imani ya kwamba marehemu anaweza kufufuka?”
“Una maana gani?”
“Namaanisha tayari Fisi alishakufa na tukazika, pengine kuna mtu mwingine mwenye jambo na kijana wako na si Mbitiyaza Lupandagila.”
“Niliwaza kama wewe lakini uliponipasha kifo cha yule binti na ukanipa ripoti ya mshukiwa wa kwanza, nachelea kusema kwamba, mizimu ya kisukuma imeamka.”
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Sikiliza George..” Kabina alisema kisha akanyamaza kidogo kabla ya kuendelea..
“Wewe ni Kamanda wa polisi naomba usiku huu usilale uhakikishe unapata uhakika wa kifo cha mwanamke huyo, wasiliana na askari wenzake ujue wao wanasema nini... Lakini ahsubuhi pia itatulazimu kuongeza ulinzi kwenye benki yetu, kuanzia ninapofanyia kazi hadi kule anakufanyia kazi Joseph, tufanye mambo kwa umakini ili kujua nani anataka kutuchezea akili...” Kabina alitua.
“Hapa sherehe ameingia mmasai, silali tena.” Kamishina wa polisi, George Kilomba alisema na kukata simu huku jasho likiwa limamtoka, alijiuliza swali, inawezekanaje marehemu aonekane hai? Na kama siyo marehemu ni nani mwenye wajihi wa kufanana nae? Kwa nini tabibu wa magereza ameuawa? Kila swali halikuwa na jibu lake na hakuona wa kumjibu zaidi ya kuuacha muda uwe mwamuzi wa mwisho. Usingizi haukuwa miliki yake tena na badala yake akaamua kukimbilia bafuni kujimwagia maji kabla hajachukua kitabu na kuanza kusoma ili kuisubiri ahsubuhi iliyokuwa mbali nae.

Mapambazuko yalikuwa ni neema kwa kila mtu aliyeamka salama bila mawaa kichwani mwake, lakini yalikuwa ni chungu kwa yeyote aliyelala na kiporo cha mazongemazonge na miongoni mwao ni Kamanda wa kanda maalumu Dar es laam, George Kilomba na wenzake. Yeye aliamka akiwa na lengo moja tu la kuhakikisha anaweka usalama nje ya benki ya biashara na ndani ya benki huku vijana wake wakiwa na picha ya mtu waliyehisi anaweza kuingia ndani ya benki kwa wema au kwa ubaya, ndani ya benki waliingizwa watu wawili wenye silaha na walijifanya kama wateja wa kawaida waliowahi kupata huduma lakini hawakuhangaika na kupata huduma zaidi ya kujizungusha pasi na kueleweka, nje ya benki kulikuwa na kundi kubwa la askari polisi wenye silaha waliokwenye sare na wasio na sare. Licha ya kuwa na taarifa za uwezekano wa matawi mawili yaliyokuwa katikati ya jiji kutembelewa na mtu mmoja lakini nguvu kubwa ikawekwa kwenye tawi lililokuwa mitaa ya Kariakoo, kwa nini? Kwa sababu tawi jingine kubwa lilikuwa kando ya kituo kituo kikuu cha polisi Dar es laam, umbali wa mita nne tu na mita moja kutoka kituo cha daladala. Kwa akili za kawaida ingelikuwa ngumu kwa mtu mwenye nia yoyote kufanya hujuma yake hapo ikiwa kuna askari lukuki umbali mfupi kuliko kawaida. Tawi la Kariakoo ndiko alikofanyia kazi mwanamama Kabina Mkwepu na tawi lilikokando ya kituo kikuu kilikuwa ni kituo cha kazi cha bwana Joseph Mkweche. Hadi inafika saa tano na nusu hakukuwa na kitu chochote chenye kuashiria uwepo wa mtu aliyeitwa Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu, hali ilikuwa shwari sehemu zote za kazi na watu waliendelea kuingia na kutoka wakiwa na amani, kwa Joseph hali ilikuwa tofauti kila aliyefika dirishani kwake alikuwa anahakikisha ameiona vema sura yake, moyoni mwake hakuwa na amani kabisa kila alipomkumbuka mgeni wa ajabu aliyefika nyumbani kwake usiku wa maanani, pengine angelikuwa na amani kama asingeliambiwa mtu huyo alikuwa ni marehemu kwa miaka zaidi ya miwili nyuma, pia mtu huyohuyo aliyesadikika kufa kabla ya kumtembelea usiku alikuwa ametoka kufanya mauaji mahali fulani, mauaji ya mmoja wa watu waliokuwa wakidaiwa na huyo jamaa aliyeaminika alishafariki. Hali yake ilizidi kuwa mbaya zaidi alipohisi ni yeye atakaefuata kuuawa. Saa tano ilipotimia aliamua kuondoka kwenye dirisha lake na akaelekea kantini kwa ajili ya kupata kiamsha kinywa. Haikuwa kama alivyotaka iwe, chai kwake ikawa ni dawa chungu mdomoni kiasi kwamba alishindwa kunywa angalau funda mbili za chai wala kutafuna skonzi zilizokuwa kwenye sahani kando ya kikombe cha chai. Kila mara saa yake ilikutana na jicho lake na mishale aliona ni kama haisogei. Dakika alizopaswa kutumia kuamsha kinywa zilimalizika akiwa bado anaangaliana na kikombe kilichojaa chai, kwa kuwa hakutaka watu wengine wajue hali aliyokuwa nayo akaamua kuelekea maliwatoni angalau kupunguza muungurumo wa tumbo lake. Chooni napo hakufanya lolote licha ya tumbo la kukata kumsumbua, wakati anainuka ili kuzipandisha nguo zake ndipo alipogundua alikuwa anatetemeka na mwili wake ulikuwa umeloa jasho licha ya kiyoyozi kupuliza kila mahali ndani ya benki. Ilikuwa bado ni saa tano licha ya kujizungusha mara zote hizo angalau ule muda wa madai upite, wazo moja likampitia kichwani na akaamua kulifanyia kazi, aliona ni vema atoke nje ya jengo kwa kuzuga anaenda kutafuta dawa za kutuliza maumivu ya tumbo. Huko nje aliona ni bora kuitumia nafasi hiyo kumpigi mtu wake wa karibu, Kabina Mkwepu.
“Nambie baba wa kifua changu..” Kabina aliitikia punde baada ya kupokea simu, sauti yake ikawa faraja kwenye moyo wa Joseph Mkweche ambae alijikuta akifumba macho na kuzishusha pumzi zake kwa tuo.
“Siko sawa tangu usiku wa jana...” Alisema kinyonge huku akivuta pua zake kukabiliana na hali ya mafua iliyoanza kumwandama.
“Usijali sana kwa kuwa jambo hili linafanyiwa kazi kwa umakini mkubwa ili kuzijua mbivu na mbichi, ulinzi upo kila mahali kuhakikisha kama kweli huyo mtu yupo na atajitokeza basi aishie mikononi mwa polisi.” Kabina alimtia moyo.
“Mkishamkamata mtu aliyeandikiwa ripoti ya kifo kwa ushahidi usio na chembe ya shaka mtafanya nae nini?” Joseph aliuliza.
“Itafahamika tukishamtia mikononi na atasaidia serikali kuwaibua waliotengeneza kifo chake.” Kabina alimjibu.
“Lakini kwa nini tusimpe mgao hata kidogo? Naiona hatari huko mbele..” Joseph alionesha shaka yake.
“Upo tayari kutoa kiasi gani kwenye mgao wako? Sikia nikwambie, yeyote aliyekuwa kwenye lile gari hatakiwi kupata hata sumni wala hatakiwi kuwepo Duniani... Mgao ni kwa watu makini tu...” Kabina alisema kwa sauti ndogo ambayo hata ungelikuwa karibu yake angalau mita moja ingelikuwia ugumu kumsikia...
“Nilitoka nje kidogo, naomba niwahi kazini..” Joseph alisema na kukata simu yake huku akiinua mkono wake wenye saa na kuyatazama majira yake ambayo yalikuwa ni kuelekea saa sita na dakika mbili mchana, ikiwa imepita saa moja zaidi tangu alipotoka ofisini. Akarejea dirishani kwake ikiwa ni saa sita na dakika kumi, akaita wateja waliokuwa kwenye foleni na kuendelea kuwasikiliza huku akiwa hajaupoteza umakini wake kwa kila mteja wa kiume aliyelikaribia dirisha alilokuwa akifanyia kazi. Hadi inafika saa saba na dakika ishirini, dakika kumi kabla ya wahudumu wa benki kujumuika kwenye chakula cha mchana, hakukuwa na mgeni yeyote wa kutisha aliyezitembelea benki zote na hapo likafanyika kosa pande zote mbili; askari polisi waliokuwa wameweka ulinzi nje na ndani ya tawi la benki Kariakoo walikata shauri la kuondoka kuendelea na majukumu mengine huku kamanda wao ambae alikuwa anajua kinachoendelea akimpigia simu Kabina na kumwambia uamuzi wake wa kuondoa askari lindoni wakaendelee na majukumu mengine.
“Kijana wako alikuwa anaota..” Alisema baada ya simu yake kupokelewa.
“Inawezekana kweli alikuwa anaota, marehemu hawezi fufuka bwana.” Kabina nae alikubaliana na Kamanda George Kilomba na askari wakaondolewa. Upande mwingine Joseph nae umakini ulipungua na alikuwa anawaza mlo wa mchana ambao kwake ungelimpa muda wa kuikimbia ofisi yake angalau kwa muda wa dakika ishirini hadi ishirini na tano. Ziliposalia dakika mbili kabla ya saa saba na nusu mchana kuna mambo mawili yalikuwa yanatokea sehemu mbili tofauti na sehemu zote zilihusiana, tawi la benki ya biashara Kariakoo kulikuwa na mteja akiondoka ndani ya benki akiwa ameusahau mfuko mdogo ambao ulikuwa na mzigo uliofungwa vizuri kwenye karatasi. Wakati huohuo kwenye dirisha namba nne ambalo lilihudumiwa na Joseph Mkweche, mwanamke mmoja aliyejifunga vizuri kichwa chake na mavazi marefu yakifunika sehemu kubwa ya mwili wake, alikuwa analifikia dirisha huku akiwa na karatasi mkononi na haikuwa mhuri wa benki aliyokuwepo bali ilikuwa ni karatasi nyeupe yenye maandishi machache juu yake.
“Naomba huduma tafadhali..” Mwanamke alisema kwa sauti iliyoisaliti jinsia aliyoamua kujivika, aliongea kwa sauti nzito ya kiume kiasi cha kumshitua Joseph Mkweche ambae alikuwa ameinamia kompyuta yake akitaka kufunga mahesabu ya kuanzia ahsubuhi hadi mchana. Kilichomshitua si sauti ya kiume ya mtu ambae hakuwa ameuona ujio wake, bali ni kuisikia sauti ya mtu aliyemnyima amani tangu usiku hadi wakati huo, akainua macho yake kujihakikishia kama kweli aliyekuwa mbele yake alikuwa ni Fisi mwekundu. Hakuwa amekosea, mbele yake alisimama mwanaume aliye kwenye mavazi ya kike na mkononi mwake alikuwa na karatasi yenye maandishi makubwa yaliyokolezwa.
‘UKILETA UJANJA NALIPUA BOMU.’ Joseph Mkweche aliyasoma hayo maneno na akajikuta akitetemeka kwa hofu.
 
‘UKILETA UJANJA NALIPUA BOMU.’ Joseph Mkweche aliyasoma hayo maneno na akajikuta akitetemeka kwa hofu.
“Naouomba mfuko wangu..” Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu aliunguruma kwa kujiamini huku akimtazama usoni kwa namna ya kumaanisha alichokuwa anasema.
“Niweke shilingi ngapi?” Joseph aliuliza huku akikumbuka kuuchukua mfuko aliokuwa ameachiwa usiku uliopita, aliutoa kwenye moja ya mifuko ya suruali yake na kuuweka juu ya meza iliyokuwa na kompyuta.
“Wewe mtoto mjinga sana, umekaa na mfuko wangu kwa zaidi ya nusu siku na hujui kiasi gani nahitaji?” Shija alifoka kwa hasira kiasi cha kuweza kuwashitua watu wengine ambao walibaki wameduwaa baada ya kusikia sauti ya kiume kwenye mavazi ya kike, taharuki ikaanza kuingia ndani ya benki, wenye moyo dhaifu hawakutaka kuambiwa kitu gani kingelifuata, wakakimbilia mlangoni lakini hawakuufikia kabla ya kupata onyo lenye mamlaka.
“Yeyote atakaeugusa mlango ahakikishe urithi upo kwa mwanasheria..” Shija Mbitiyaza alipaza sauti yake huku akizitupa pembeni nguo za kike zilizokuwa mwilini mwake, alibaki na kaptura iliyofikia juu ya magoti, vesti nyeupe na mguuni kulikuwa buti zilivaliwazo mara nyingi na wanajeshi ama Polisi. Ni bora angelibaki kwenye mwonekano huo pekee lakini alikuwa na vazi la ziada ambalo ni wachache wamewahi kuliona hadharani, zaidi waliliona kwenye sinema za uongo na kweli. Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu p.a.k Fisi mwekundu alikuwa amejivika bomu la kutengenezwa kienyeji lakini alilitengeneza kitaalamu sana, si hivyo tu, alitoa mabomu mengine kwenye mifuko ya kaptura yake, mabomu yenye ukubwa wa kipande cha sababuni aina ya jamaa; yalikuwa mawili, moja akijiweka kwenye dirisha alilokuwa amesimama na ndani yake kukiwa na Joseph Mkweche ambae wakati huo alikuwa hajui kama nguo zake zilishalowa kwa mkojo uliomtoka pasipo na habari, bomu lingine alitembea nalo kwa kujiamini kabisa na kwenda kulipachika kwenye mlango wa kioo uliotumiwa na watu kuingia ama kutoka ndani ya benki, akamalizia kwa kugeuza kibao kilichokuwa kikining’inia mlangoni kikiwa kimendikwa pande zote mbili, upande mwingine uliandikwa Closed na mwingine Open, yeye akachagua kuelekeza Closed kwa yeyote ambae angelikuwa anataka kuingia huku Open ikisomwa na waliokuwa ndani.
“Kaeni upande ule wa kona na hakikisheni hakuna mtu anaesimama bila ruhusa yangu.” Aliwambia watu waliokuwa wakihangaika kumkimbia kwa kusukumana.Agizo lake lilifanyiwa kazi nae hakutaka kuwagasi watu ambao wametii bila usumbufu, akaelekea dirisha namba nne alikoacha bomu moja likilindwa Joseph ambae alishindwa kulia wala kucheka, sauti ilimkauka na mwili wake ulibaki ukiwa umeingiwa na ubaridi wa kutisha, machozi yalimtoka na asitoe sauti watu wajue alikuwa analia au alikuwa kwenye kilele cha furaha.
“Haya nimerejea, nataka unipe pesa zangu.” Shija alisema kwa lafudhi yake ya kisukuma ambayo haikuwa kubadilika, mkono wake mmoja ukitoa kitenzambali chenye vibonyezwa vinne kwenye mfuko wa nyuma wa kaptura yake. Akabonyeza kitufe kimoja na kupotezea kama vile hajafanya kitu chochote cha hatari kisha akamtazama tena Joseph.

2.

Kwenye benki benki ya biashara tawi la Kariakoo kulitokea mlipuko wa wastani ambao uliishia kudhuru watu wawili kwa kuwajeruhi, hiyo ilikuwa dakika moja baada ya uongozi kupata taarifa za uvamizi kwenye tawi lingine lililokuwa mita chache kutoka kituo kikuu cha polisi mkoa wa Dar es laam. Hekaheka za watu kunusuru maisha yao zilishika kasi huku watu waliokuwa nje bila kujali hatari ya bomu lingine kulipuka, wao walisogea na karibu na jengo la benki na kuanza kurekodi yaliyokuwa yakiendelea huku wengine wakianza kusambaza taarifa za mlipuko huo kwenye mitandao ya kijamii, dakika chache baadae nchi nzima ikawa kwenye mtanziko wa kutaka kujua kilichokuwa kimetokea ni ugaidi ama ni kitu gani. Wakati bado taarifa hizo zikiwa hazijapoa, taarifa nyingine zikaanza kusambaa kwa kasi zaidi kuliko zile za mlipuko wa bomu, ilisemekana kuna magaidi ndani ya tawi lingine la benki ya biashara na mmoja wa magaidi hao alikuwa amevaa mabomu. Macho na masikio ya watanzani yakahamia Dar es laam, hofu ikatanda zaidi baada ya kusemekana kulikuwa na watu zaidi ya sitini waliokuwa wamezuiliwa ndani ya benki. Wakati watu wakiendelea kusambazia a taarifa hizo, Kamishina George Kilomba yeye alikuwa anampigia simu Kabina Mkwepu ili kujua kama atakuwa salama ndani ya benki ambayo hawakuwa na uhakika kama na yenyewe imevamiwa au ni bomu la kutegwa pekee ndilo lililoacha madhara.
“Uko salama?” George aliuliza
“Niko salama lakini sijatoka ndani ya ofisi, naogopa...” Kabina alisema kwa kitetemeshi.
“Fanya uwezavyo utoke humo ndani kwa sababu hatujui kama magaidi wapo ndani ya benki au watakuwa upande gani na wanapanga nini.” George alimshauri.
“Unakuja huku au?” Kabina aliuliza.
“Huko hadi sasa tunaambiwa kupo shwari na hakuonekani dalili za mtu mwenye kutishia usalama, waliokwisha kufika hapo wataendelea kushughulikia bomu hilo na kuona kama bado yapo mengine au la, mimi naenda kule anakotamba mvamizi na kituo kizima kitahamia hapo.” George alisema kwa wasiwasi.
“Ni kweli aliyeko huko na mabomu ni Shija Mbitiyaza?” Kabina aliuliza.
“Hadi sasa hatujapata picha halisi za mtu huyo anaesemekana yupo ndani ya benki, lakini tulichona na uhakika nacho ni kwamba yupo peke yake na amevaa mabomu na mengine ameyatawanya..” George alijibu.
“Sijui kama Joseph atakuwa salama huko ndani...” Kabina alisema kwa wasiwasi.
“Hakijaripotiwa kifo hadi sasa...” George alijibu.
“Kama kweli Shija ndiye gaidi unahisi ni kwa sababu ya ule mchezo au anazo sababu zake nyingine?” Kabina aliuliza.
“Ni ngumu kujua hadi tukifanikiwa kumpata na kumhoji, lakini kwa sasa tuseme ni yeye na amefuata pesa zake kwa Joseph.”
“Lakini kwa nini asingelikuja kwangu au kwako na akamchagua Joseph?”
“Nae ni mhusika wa mchezo... Kikubwa tujiulize aliwezaje kutoka kaburini? Ni yeye au ni mtu waliyefanana?” George alisema na kukata simu baada ya kuwa gari iliyokuwa imembeba kuwasili mita hamsini mbali na kituo cha polisi na benki yenyewe, askari wengi walikuwa nje na silaha zao huku wakijaribu kuzuia watu wasipite au kuingia kwenye kituo cha daladala, barabara za kuingia na kutoka kituoni zilifungwa na watu walikuwa wakiombwa kufunga biashara zao na waliokuwa wakipita kwa miguu wasiendelee kuwa karibu na mazingira hayo ambayo yalikuwa ni hatari kwa wakati huo. Askari wengine walikuwa wamefanikiwa kuingia kwenye ofisi zingine zilizokuwa kwenye ghorofa hiyohiyo na kuwatoa watu wenye ofisi kwenye jengo hilo na wao kujiwekea himaya Yao huko wakijaribu kuona namna ya kuweza kufika kwenye ofisi za chini ambako kulikuwa na benki yenyewe ambayo wakati huo ilikuwa chini ya mwanaume mmoja aliyekuwa na kaptura na vesti mwilini mwake.

******
Kwenye ofisi moja ndani ya kamandi ya jeshi la ardhini 34 kikosi cha vita, kulikuwa na kikao cha kumwajibisha mmoja wa wanajeshi ambae alikuwa amekwenda mrama kinidhamu na yalikuwa ni makosa ya kujirudia ingawa wakati huu alikuwa ameendw mbali zaidi. Waliokuwa kwenye kikao walikuwa watatu, kiongozi wa nidhamu kikosini ambae alikuwa kwenye umri wake wa kustaafu, karani aliyesimamia hukumu ya mahakama ya kijeshi pamoja na mkuu wa kikosi ambae alikuwa na cheo kikubwa kuliko wenzake wote. Licha ya tofauti yao kivyeo lakini walikuwa ni watu ambao walielewana sana nje ya kazi na walikuwa na wajibu mwingine kabla ya kuwa hapo walipo sasa, ukaribu wao ulianza miaka mitano iliyopita na ulidumu hadi wakati huo waliokuwa kwenye ofisi ya mmoja wao wakijadili jambo kubwa na lenye kuibeba au kuibomoa taswira ya kambi nzima na jeshi kiujumla. Walijadili hukumu iliyokuwa imetolewa na afisa mmoja ambae alikuwa akishughulika na kesi zote za wanajeshi, hukumu ilitaka mwanajeshi mwenye namba 34901 kuondolewa kikosini kwa sababu ya makosa ya kujirudia. Kilichowafanya wakae ofisini kujadili hukumu iliyotolewa ni umuhimu wa mwanajeshi mwenyewe, kwanza alikuwa ni mchapa kazi asiyetetereshwa na mazingira, pili alikuwa ni dereva mzuri sana wa vifaru vya aina mbalimbali na alitegemewa kwa kiasi kikubwa kwenye kuwafundisha waongoza vifaru wapya na hata wazoefu bado walihitaji kupata maelekezo yake pale aina mpya ya vifaru iliponunuliwa. Sifa kubwa kuliko hata udereva wake ni uwezo wake wa kulenga shabaha, alikuwa ni fundi haswaa wa kutumia silaha ya aina yoyote kulenga chochote na akakitungua bila kuhitaji risasi ya ziada baada ya awali kutoka kwenye silaha, ujuzi wake huo hakuwahi kuuendeleza kwa kwenda shule za walengaji shabaha, alitumika kama chaguo la tatu baada ya machaguo mawili yenye taaluma kuwa yameshapitishwa na hiyo ni kwa sababu hakutumiwa zaidi kwenye ulengaji na badala yeka akawa anatumika kwenye kundi la vifaru. Sifa moja mbaya iliyomwondolea heshima kwa wakubwa wake ni ulevi na maamuzi yake yasiyotabirika, hata wakati huo alikuwa akijadiliwa kwa sababu alitoka na kifaru kambini akaenda kuvamia maeneo ya biashara za watu, alivunja maduka mengi na kuacha hasara ambayo hadi wakati huo bado tathimini yake haikuwa imejulikana, alipoulizwa sababu ya kufanya jambo kama hilo aliishia kutoa jibu jepesi kwa waliomuuliza, eti alikuwa anakijaribu kifaru chake baada ya kukitoa gereji. Uchunguzi wa awali uliofanywa na ulibaini alikuwa anawakomoa wenye maduka kwa kuwa walikataa kumkopesha alivyokuwa akivihitaji na kwa kuthibitisha hilo ni pale alipoyaacha maduka matatu pekee ambayo yalikuwa yakimkopesha sigara kila mara.
“Tunaweza kupitisha uamuzi huu uliokwisha kutolewa na tukampa barua ya kuachishwa kazi, lakini ni pengo ambalo linaweza kutuchukua muda mrefu kuliziba.” Bregedia Lutoji Ngoma mkuu wa kamandi ya vita, aliwambia wenzake waliokuwa wamekaa ofisini kwake.
“Tunaweza kuicha adhabu ipite kama ilivyotolewa lakini baadae kidogo tukamuita na kumrejesha kazini.” Sir Meja Bukumbo Mbeki alishauri.
“Nadhani tuaiche adhabu yake, akikaa mtaani kwa miezi kadhaa atatia adabu na kurudi kazini itakuwa ni kama ndege aliyenaswa na urimbo.” Karani ambae alikuwa ni Luteni, alikazia.
“Hamuoni hadi tutakapomrejesha kazini atakuwa ameshakuwa mlevi sugu pengine na afya aliyonayo sasa akawa hana?” Brigedia Lutoji Ngoma alionesha wasiwasi wake.
“Mkuu, upo sahihi lakini atakuwa nje ya kambi kwa kipindi kisichozidi siku sitini, tutazifungia pesa zake ili maisha yawe ya taabu kwake..” Sir Meja Bukumbo Mbeki alisema.
“Hapana! Hiyo inaweza kuzidisha tatizo badala ya kulitatua. Kipindi hicho kifupi anaweza kuugua hata ugonjwa wa akili au akajiua kabisa, yule ni mbilikasoro..” Brigedia alikataa.
“Tufanye nini?” Karani aliuliza. Lakini kabla ya kujibiwa na yeyote ikawa imetoka ishara kwa Brigedia Lutoji, ishara ambayo iliwataka wote wanyamaze wakati simu yake ikiita, hakuzingatia kikao kwa kuwa hakikuwa kwenye kumbukumbu rejea yoyote kwao. Akaipokea simu huku akiwa makini sana...
“Angalia WhatsApp..” Mpiga simu alisema na kukata simu bila kungoja maelezo yoyote kutoka kwa Brigedia. Harakaharaka aliwasha data na kutulia kwa sekunde kadhaa hadi mlio wa kuingia ujumbe mfupi uliposikika, harakaharaka akaruhusu kupakia ujumbe wa picha uliokuwa umetumwa na namba iliyokuwa imempigia.
“I can’t believe!” Alisema kwa mshangao mkubwa huku akiinua uso wake na kuwatazama wenzake ambao nao walikuwa wameangusha vinywa kwa mshangao licha ya kutokujua mwenzao alikuwa anashangaa nini.
“Ni macho yangu ama ni kweli?” Lutoji aliwahoji wenzake ijapokuwa walikuwa hawajui kilichomfanya ahoji.
“Haiwezekani huyu jamaa akaendelea kuwa hai hadi sasa... Haiwezekani!” Alisema kwa sauti iliyojaa wasiwasi na wakati huu akiwapa wenzake simu iliyokuwa imempagawisha.
“Mbitiyaza!!!” Karani aliyekuwa ameipokea simu kutoka kwa Lutoji Ngoma, alishangaa kwa sauti kubwa huku akijaribu kuikuza picha iliyokuwa kwenye simu, akaitazama vema na kwa ukubwa aliyotaka, midomo ikamuanguka, akaisukuma simu kwa Bukumbo Mbeki ambae aliipokea na kwa msisitizo wa mshangao wake akaamua kusimama na simu mkononi.
“Nani kakukutumia picha hii?” Alimuuliza Brigedia Lutoji Ngoma.
“Soma jina la mtumaji..” Lutoji alijibu kinyonge.
“Kanali Lingu, mstaafu.” Bukumbo alisoma jina kwa kirefu na wenzake wote wakasikia.
“Picha ya muda gani hii?” Karani aliuliza.
“Kanali ndiye mwenye majibu...” Lutoji alisema huku akichukua simu yake na kuipiga ile namna iliyokuwa imemtumia picha.
“Bila shaka hii ni picha ya nyuma kidogo...” Brigedia Lutoji Ngoma alisema.
“Hapana... Hii ni ya leo na imesambazwa mtandaoni kutokea benki ya biashara tawi la bandari, mko mbali na Dunia wakati mwenzenu anaisimamisha nchi.” Kanali Lingu alisema.
“Fisi mwekundu hakufa siku ile?” Lutoji alimuuliza Lingu.
“Aulizwe Luteni Gwaza Limbu, alikuwa kwenye operesheni moja kwa moja.” Kanali Lingu alisema kwa msisitizo.
“Kwani ilikuwaje?” Sir Meja Bukumbo alimgeukia Luteni Gwaza.
“Hata sielewi ilikuwaje lakini nilimuona akilamba risasi tatu kavu..” Alijibu.
“Kwani idadi ya waliofariki ilikuwa ni watu wangapi? Je, jina lake lilitajwa.?” Aliulizwa tena.
“Nilihamishwa kambi siku moja kabla ya uhakiki wa wahanga, niwaulize ninyi kama mlilisikia siku mnahudhuria mazishi.” Alirejesha swali.
“Kosa kubwa sana tulifanya... Sasa Fisi yupo mjini na yupo banki wakati huu..” Lutoji alisema.
“Ingieni mitandaoni na muone yanayoendelea kwenye eneo alilojiwekea utawala na mabomu yake, baadae tuwe na kikao.” Kanali msataafu bwana, Lingu Magubo alisema na kukata simu. Haraka haraka simu za watu watatu waliokuwa kwenye ofisi moja zikawa bize, walipakuwa taarifa kwa kadri walivyoweza na taarifa nyingi zilikuwa ni za kumpamba Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu, ambae wakati huo alikuwa amesimama katikati ya benki akiwa anawatazama polisi waliojazana nje ya mlango wa kuingilia ndani ya benki, walishindwa kuingia kwa sababu mlangoni kuliwekwa bomu na kitenza mbali kikiwa mikononi mwa mtu waliyeanza kumtangaza kama gaidi.
“Tunamhitaji huyu mtu kabla hajaingia mikononi mwa polisi, aliyonayo hatuwezi kuyajua.” Lutoji alisema kwa sauti iliyokata tamaa.
“Unahisi anaweza kusema yote yanayotuhusu?” Gwaza Limbu aliuliza.
“Inawezekana kabisa na bila shaka yupo hapo benki kwa sababu maalumu na sababu hiyo ni kutaka sisi tujue yupo hapa mjini.” Lutoji alijibu.
“Inawezekana ikawa ni njaa iliyosababisha avamie benki...” Gwaza alitaka kuongea kitu lakini Bukumbo alimkatisha.
“Mimi ni mwalimu wake, namjua sana huyu jamaa na hata hilo jina la Fisi mwekundu ni mimi nilieanza kumuita na likapita kama jina lake la vita. Kama angelitaka pesa angelizipata popote na bila kuacha alama. Benki na mabomu ni kutaka kutuonesha hana shida na pesa...” Alisema kwa msisitizo.
“Lakini eneo alilolenga ni hatari sana kwa usalama wake, sina hakika kama tunahitaji kutumia nguvu zetu kumtoa humo ndani.” Gwaza alisema lakini aliishia kukutana na jicho kali la Bukumbo ambae wakati huo alishasahau habari za nidhamu ya kijeshi, hakujali wenzake walishamzidi vyeo bali alichojali ni kile alichokijua kwa Mbitiyaza Lupandagila Masalu.
“Huyo mtu ni Komando mwenye sifa zilizokamilika, bila shaka atakuwa hapo si kwa bahati mbaya na si ajabu akaondoka na watu wote wakashangaa...” Bukumbo alisema huku akitikisa kichwa, alimjua vema huyo mtu, aliujua ufundi wake kwenye kutumia silaha, mapigano na hata kujitoa bila kujali matokeo yake. Kiufupi alimjua ni aina ya wanajeshi wachache wanaojua vingi kwa wakati mmoja.
“Nawahakikishieni kama alijua tulimzunguka wakati akiwa nchini Mali, basi atatuwinda mmoja baada ya mwingine na atatupata. Tujiandae kumjibu..” Bukumbo alisema na kukaa kwenye kiti.
“Unatutisha?” Lutoji alimuuliza.
“Subirieni awashangaze kwa namna atakavyoondoka hapo benki..” Alisema.
“Kwa hiyo tunarudi kwenye hoja ya msingi kwamba ni lazima tuingilie kati ili awe mali yetu?” Gwaza aliuliza.
“Linaweza kuwa suluhisho.” Bukumbo alijibu.
“Tujipe muda kidogo tuone polisi watamfanya nini, wakati tujiandae kuingilia hili jambo.” Lutoji alishauri.
“Lakini kumbukeni sisi tupo pwani na yeye yupo Dar. Ni ngumu kupata nafasi kufanya oparesheni mkoa mwingine..” Bukumbo alisema.
“Tutamtumia Kanali Lingu..” Gwaza alisema.
Ukimywa ukatawala ofisini lakini huko nje nchi ilikuwa kwenye taharuki kubwa, kazi za watu zilisimama kwa sababu walitaka kujua kitu gani gaidi angelifanya, mijadala ikawa kila mahali na nchi ikawa ikishuhudia tukio geni kwa kila mmoja.
 
kongole kwa simulizi nzuri Kudo, mpaka nahisi unachelewa kuuweka mwendelezo asee
 
Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu alikuwa amesimama katikati ya benki akiwatizama watu aliokuwa amewakusanya pamoja, aliwaona namna walivyokuwa wamejawa na hofu kubwa na wengine tayari walikuwa wameharibu hali ya hewa, alitabasamu kinafiki huku akipiga hatua kumfuata Joseph ambae bado alikuwa ameganda ofisini kwake pasipo na kujua kama alitakiwa kukaa au kuendelea kusimama kama ambavyo alikuwa amefanya wakati huo, machozi yalikuwa yanamtoka pasi na kukoma na asijue alikuwa analia nini.
“Utanipa namba za simu za huyo kahaba wako au nifanye jambo lingine?” Alimuuliza.
“0793....” Joseph alizitaja haraka haraka bila kukosea namba hata moja, hakutaka kuendelea kuwa matatani ingali bado kile alichotakiwa kukifanya akiwa bado hajakifanya, alikuwa hajatoa pesa kama alivyoagizwa.
“Naona umekuwa mtiifu wakati huu..” Alisema baada ya kuzinakili namba zilizotajwa, akapiga simu.
“Naitwa Mbitiyaza Masalu... Kama utakuwa umeisahau sauti yangu basi jina langu litakukumbusha uwepo wangu.” Alisema kwa sauti nzito isiyo na masihara.
“Unataka nini?” Kabina alisema kwa wasiwasi mkubwa, hakuwa ametarajia kupokea simu ya mtu ambae wakati huo nchi nzima ilikuwa ikimzungumzia.
“Nataka pesa zangu. Nataka pesa zangu na ziada ya usumbufu mlionipa. Nataka pesa zangu zote na faida ya muda wote mliokaa nazo.” Alisema huku akicheka kicheko chenye ukohozi ndani yake, sauti yake ilionekana kuathiriwa na moshi wa sigara ama pombe kali.
“Pesa gani unadai? Tulianza lini kudaiana?” Kabina aliruka kimanga.
“Kama pesa huzijui na mimi ina maana hunijui..” Mbitiyaza alisema.
“Sikujui... Kwanza umepata wapi namba yangu?” Kabina aliuliza.
“Humjui Mbitiyaza kweli? Humjui Fisi mwekundu?” Mbitiyaza aliuliza maswali mafululizo huku kifua chake nacho kikimkaba na kuanza kukohoa kiasi asiweze kumsikia aliyekuwa akizungumza nae.
“Rudia majibu yako kama kweli hunijui...” Mbitiyaza alisema tena baada ya kushindwa kusikia alichokuwa akiambiwa na Kabina wakati yeye akikohoa.
“Nadhani utakuwa umekosea namba.. angalia upya na umpigie uliyemlenga..” Kabina alisema na kukata simu, kitendi hicho kilimkwaza sana bwana Shija Mbitiyaza Lupandagila Masalu, hasira zake zilikuwa tofauti kidogo na hasira za watu wengine. Wakati watu wengi wakiwa na utaratibu wa kukunja sura, wengine hulia, wengine wakijidhuru kwa vitu vyenye ncha kali, wengine hupoteza fahamu na wengine huumwa degedege lakini kwake hasira ni ilikuwa ni kicheko kikubwa hadi machozi. Shija alicheka kwa sauti kubwa kiasi akajikuta kicheko chake kikiingiliwa na kikohozi, akakakohoa hadi akalia machozi halisi ya mtu mwenye maumivu makali kwenye moyo wake, kama machozi yake yangelisindikizwa na kilio halisi basi kilikuwa ni kilio cha msiba wa mwana kuachwa na Mama. Kicheko chake kilikoma baada ya dakika tatu lakini aliendelea kukohoa kikohozi kizito mithili ya mlioa wa ngoma iliyoloa, alikohoa huku akimfuata Joseph ambae bado alikuwa amesimama kama askari aliyekwenye gwaride la ukaguzi wa mavazi. Alifuta machozi yaliyokuwa yakimtoka, macho mekundu kama mlevi wa Cuka.
“Una uhakika nimeongea na Kabina?” Alimuuliza.
“Ndi... ndiyo..” Joseph alijibu kwa hofu.
Shija alitulia akimtazama pasipo kupepesa macho yake, alichokuwa anakiwaza alijua mwenyewe kwa wakati huo lakini sekunde chache baadae aliuliza.
“Utanipa shilingi ngapi?”
“Hapa mezani zimebaki milioni tano tu...” Joseph alisema lakini kabla hajainua mfuko aliokuwa amepewa ili aweke pesa, alishangaa kioo kilichokuwa kikimtenganisha yeye na Shija kikipasuka na kuparanganyika baada ya kupigwa ngumi moja nzito kutoka kwa Mbitiyaza ambae alikuwa kwenye kiwango chake cha mwisho cha hasira. Wakati kioo kikipasuka, bomu lililokuwa limepachikwa kwenye kioo lilidakwa vizuri kwa mkono wa kushoto wa Mbitiyaza.
“Huu uwazi unakutosha kupita..” Alisema huku akimwekeleza apite kwenye uwazi uliopatikana baada ya kuvunja kioo. Joseph hakuwa na ubishi zaidi ya kujitahidi na kufanikiwa kupita bila kudhuriwa na vipande vya vioo.
“Ukiacha hawa watu hapa, huko ndani kuna watu wangapi ambao unauhakika bado hawajatoka na hawataweza kutoka kwa kuwa mimi nipo hapa?” Shija alimuuliza.
“Sina hakika lakini hawazidi kumi...” Joseph alijibu.
“Wapigie simu...” Alisema na kuivuta simu ya mezani iliyokuwa kwenye ofisi aliyokuwa akiitumia Joseph, akaivusha hadi alipokuwa amesimama na kumpa maelekezo. Joseph kwa kutumia simu hiyo aliwapigia watu wote aliyoamini walikuwa kwenye ofisi zingine na walikuwa kwenye hali mbaya sana, aliwataka watu wote watoke na kujumuika na watu wengine. Dakika tano baadae watu saba walijitokeza kwa uoga mkubwa.
“Sitaki mjichanganye na wale wateja wa benki hii, nataka mkae hapa.” Aliwaeleza sehemu ya kukaa.
“Weka kwenye mfuko wa shati lako...” Alimwambia Joseph huku akimpa bomu lililokuwa kwenye mfuko wa kaptura yake.
“Kaa mbele ya wenzako wo...” Alisita kumalizia maelekezo yake baada ya kusikia sauti ya kipaza sauti kutoka kwa mmoja wa maofisa wa jeshi la polisi, sauti ambayo ilimtaka aliyekuwa ameweka watu mateka ndani ya benki ajisalimishe kabla polisi hawajatumia nguvu ya ziada. Baada ya kusikia onyo hilo akapata nafasi ya kutazama mlangoni, aliwaona askari kadhaa waliojihami kwa silaha wakiwa wanasogelea mlango kwa namna ya kukimbia na kujikinga na magari ya wateja wa benki. Akatabasamu kizembe huku akipiga hatua na kuusogelea mlango wa kuingilia benki ambao ulimwezesha mtu aliyekuwa ndani kuwaona waliokuwa nje ila wa nje ni ngumu kuwaona waliokuwa ndani. Kwa kujiamini kabisa aliufikia mlango na kulibandua bomu alilokuwa amelipachika mlangoni, akalishika kwenye mkono wake wa kushoto na mkono wa kulia ukafungua mlango na kabla hajajitokeza nje akakumbuka kushika kitenzambali cha kuweza kuruhusu bomu kulipuka, akajitokeza nje na mabomu yake mwilini huku lingine likiwa mkononi.
“Rudini nyuma hatua kumi...” Alisema kwa sauti kubwa huku akizungusha shingo yake kushoto na kulia ambako alikuwa na uhakika polisi walikuwa wamejificha.
“Namaanisha yeyote aliyejificha kwa lengo la kunivizia arudi nyuma hatua kumi...” Alisema tena kwa msisitizo mkubwa kiasi sauti yake ikaweza kuwafikia baadhi ya waandishi wa habari ambao walikuwa wanajaribu kupata habari wakiwa mbali na eneo la tukio, picha na sauti yake vikarekodiwa na kuwekwa mmbashara kwenye mitandao ya kijamii.
“Nikiwahesabia nina uhakika hatutarudi kwenye majumba yetu tukiwa na sauti.. sutanii ..” Alisema huku akiinua bomu alilokuwa ameshika mkononi na kitenzambali nacho kikipepea hewani kwenye mkono mwingine wa kulia.
Kitu kimoja ambacho kilikuwa akilini kwa Shija ni kuwa isingelikuwa rahisi kwa polisi kumshambulia kwa sababu hawakujua athari za mabomu aliyokuwa amevaa endapo yangeliguswa na risasi, lakini imani yake ikaanza kutumbukia nyongo baada ya kusikia sauti kwenye kipaza sauti ikiamrisha kushambuliwa.
“Shambulia...!” Sauti ya kiongozi mmoja aliyekuwa eneo la tukio iliamrisha kwa ukali, Shija akafumba macho na kujiandaa kubonyeza kitufe cha kuruhusu mlipuko, alitaka afanye hivyo punde baada ya kusikia mlio wa risasi au risasi moja itakayopenya mwilini mwake.
“Askari shambuliaaaa!”Sauti ilipazwa kwa mara nyingine na sauti hiyo aliifahamu vizuri sana na alijua ni kwa nini kiongozi huyo alikuwa anajaribu kuwashawishi askari wa kikosi maalumu cha kupambana na kuzuia ugaidi waweze kushambulia, bahati nzuri baada ya kugundua waliokuwa wakiinyemelea benki ni askari wa kikosi maalumu, akawa na uhakika askari mwingine wa kawaida ni ngumu kuwapa amri na wakaitekeleza labda awe mkuu wa polisi pekee. Kwa nini? Kwa sababu wao huwa wamefundishwa kumdhibiti gaidi mwenye bomu au bomu lililotegwa wakishajiridhisha kuwa ni salama kwa wao wenyewe au watu wengine ambao huwa wamewazunguka, kwa mazingira yaliyokuwapo ni ngumu wao kukurupuka kushambulia kwa amri ya kamanda wa kanda maalumu ambae aliomba usaidizi kutokwa kwao na siku zote hawakuwa wakiwajibika kwake na hadi wanafika pale walikuwa wanaweza kupokea amri kutoka kwa kiongozi wa oparesheni pekee na si vinginevyo.
“Retreat!” Ilisikika sauti ya askari mmoja alikuwa hatua chache kutoka kwa Shija kisha askari wengine wenye silaha wakaanza kutoka kwenye maeneo yao na kurudi nyuma kwa tahadhari kubwa huku wakitoa ishara kwa askari wa kawaida warudi nyuma zaidi. Ukajitokeza mgogoro baina ya askari waliokuwa wakitii amri ya kamanda wa kanda maalumu na askari wa kikosi maalumu ambao wao wanayomafunzo maalumu ya kupambana na kuzuia ugaidi. Huo ukawa mwanya wa Shija kutembea kwa kasi na kuifuata gari moja ya kifahari iliyokuwa kwenye maegesho na kulipachika bomu sehemu aliyoiona ni sahihi, kisha akakimbia kwa kasi na kurejea ndani ya benki akiwa anapumua kwa ahueni. Akatembea taratibu kuwafuata watu aliokuwa amewakusanya pamoja, akawatazama mmoja baada ya mwingine kisha akatabasamu kivivu.
“Sina nia hiyo mnayoniwazia wala msifikirie kama kitatokea kitu kibaya kiasi kwamba mkashindwa kuonana na familia zenu baada ya hapa, labda nilazimishwe na wale mabwana walioko nje na ni wao watakaosababisha ninyi mpoteze maisha, lakini wakiwa waungwana hakuna kitu kibaya nitawafanyia...” Alisema huku akitabasamu, akageuza shingo yake kuwatazama watu saba waliokuwa wamejitokeza kutoka kwenye ofisi nyingine ndani ya benki.
“Mtu mmoja ambae anaweza kukubali kutumwa na mimi ajitokeze..” Aliwaambia huku akiwa ameliua tabasamu lake na kubaki na ile sura yake ya huzuni na hasira. Watu wote walikaa kimya na hakuna aliyethubutu kuinuka au kusema lolote. Akaachana nao kuzisogelea meza za msaada zilizokuwa maalumu kwa wateja waliozitumia wakati wa kuandika, akachana karatasi moja kutoka kwenye kitabu cha hundi kisha akavuta kalamu iliyokuwa imeunganishwa na kamba ya kuvutika, akainama kuandika kitu kwenye karatasi ya hundi kisha akarejea kwa watu waliokuwa wamejikunyata chini.
“Nani?” Aliuliza tena huku akiwatizama mmoja baada ya mwingine, mwisho macho yake yakaangukia kwa mtoto mwenye umri usiozidi miaka kumi na tatu, akammazia macho kisha akampa ishara ya kuinuka.
“Mzazi au mlezi wake ni yupi?” Aliwauliza, Mama mmoja mtu mzima wa kumkadiria miaka zaidi ya arobaini alisimama huku akitetemeka mithili ya mtu aliyekatikati ya milima ya barafu.
“Ni mjukuu ama mwanao?” Alimuuliza.
“Mjukuu wangu...”Alijibiwa.
Shija alikaa kimya akimtazama kisha akageuza macho yake na kuwatazama watu wengine waliokuwa wamekaa chini wakitaka kujua alikuwa anataka kufanya nini. Hakusema lolote na badala yake akaenda tena kwenye kitabu cha hundi na kunyofoa karatasi moja kisha akavuta kalamu na kuandika kitu kwa haraka, akarejea pale alipokuwa amewaacha mtu na mjukuu wake. Akamshika mkono bibi na kusogea nae pembeni, akazungumza nae kwa dakika moja nzima kisha akampa karatasi ambayo ilipokelewa na kuhifadhiwa kwenye sidiria. Akarejea kwa mtoto na kumpa karatasi nyingine na akatoa maelekezo ambayo kila mtu aliyasikia.
“Hii karatasi ukishatoka pale mlangoni iinue juu, mpe yeyote ambae atakuja kuichukua kwako.” Alisema na kuwashika mikono Bibi na mjukuu wake, akatoka akawaongoza hadi mlangoni.
“Bibi... Hakikisha unampa mwandishi wa kituo kidogo ambacho hata wewe hukijui... Askari asione.” Alisema kwa msisitizo na maelekezo yake yakaitikiwa kwa kutikisa kichwa, akawaruhusu watoke nje ya benki.
“Sisi tunaweza kufa kwa sababu tunayo ya kushuhudia, yule mtoto anahitaji maisha mengine ya ziada ili kukamilisha kusudi la Mungu. Acheni aende.” Aliwambia watu waliokuwa wamesalia na hakuhitaji jibu lao, akapiga hatua kumfuata Joseph Mkweche.
“Bado unamahusiano na Kabina?” Alimuuliza.
“Ndiyo..” Joseph alijibu.
“Pesa zangu alimgawia nani?” Alimuuliza.
“Kiukweli sijui maana hata mimi nilikuta mgao kwenye akaunti yangu na sikujua aliyeniwekea ni nani..” Joseph alijibu.
“Kwa nini mlinigeuka? Kwa nini?” Alimuuliza kwa ukali lakini sauti yake haikuweza kuwafikia watu waliokuwa pembeni, ni yeye na Joseph pekee walioweza kuisikia.
“Sijui kitu kuhusu mipango mbali na ile niliyoshiriki, Kabina anajua zaidi.” Joseph alijibu.
“Rudi pale...” Alimruhusu kuungana na wengine.
“Kuna yeyote ananamba za IGP? Rais au Mkuu wa jeshi la wananchi?” Aliwauliza watu waliokuwa wakimtazama na wasijue lengo lake.
“Naona hamna mwenye majibu... Ninazo dakika kumi za kusubiri, baada ya hapo kila mmoja atawajibika kujitafutia hizo namba kwa namna atakayoijua.” Aliwaambia kwa kumaanisha lakini kabla kauli yake haijapoa akaachia kicheko cha mkwaruzo wa kohozi lililotuama kifuani, lakini hakulitema na badala yake akagairi kumalizia cheko lake ili asije kubanja na kuwakera mateka wake, alijua si busara kujiachia kwa kikohozi kizito mbele za watu.
“Kuna yeyote atahitaji kupiga picha na mimi?” Aliwauliza huku akiwauzia tabasamu bandia, watu wakaishia kutazamana na wasimjibu.
“Hii ni historia ambayo pengine hakuna kati yenu atakuja kukutana nayo kwenye maisha yake ya baadae, najua huko nje mimi ni maarufu sana na sasa nusu ya Dunia imeshajua uwepo wangu. Au ngoja...” Alisema na kuifuata runinga ya ukutani ambayo ilikuwa imezimwa, akaiwasha na kurudi nyuma hatua kadhaa.
“Mnaona? Hadi picha yangu imeshapatikana na sasa mimi ni habari kila mahali...” Alisema huku akicheka kwa sauti ndogo ambayo kila mtu aliisikia.
“Ukipiga picha na mimi ni historia nzuri ambayo kamwe hutakuja kuisahau maishani mwako, labda nikwambie...” Alinyamaza kidogo kisha akaendelea.
“Mimi siyo gaidi na sijawahi kufikiria kuwa gaidi. Haya mabomu nimevaa kwa sababu ya kisu kilichokaa moyoni mwangu, kuna watu wamewahi kukizamisha kisu na hawakukitoa, hata pale nikiwa bado naugulia kuna watu wengine wakazamisha panga na kuusambaratisha kabisa moyo wangu, hawakuridhika kabisa, wakahakikisha nakufa kifo walichotaka wao.” Alisema huku akijitahidi kuyazuia machozi yasimtoke, alipofanikiwa akaendelea..
“Walinizika kabisa na kupiga picha za uthibitisho wa kifo changu, nipo hapa kuwaonesha maajabu ya Dunia ya Mungu, nimekuja kuwaonesha hata Yesu alifufuka siku ya tatu baada ya kifo chake cha maumivu na mateso makali kutoka kwa wanadamu.. Binaadamu ni watu wabaya sana tena sana na ubaya wao unaweza usiuone hadi utakapowapa pesa...” Akacheka kidogo huku akigeuka na kumtazama Joseph, hakumsemesha na badala yake akaendelea na hadithi yake kwa mateka wake.
“Si unaona sasa hivi watu wamekimbia mjini kuogopa mlipuko wa mabomu, lakini nakwambia ukweli wa Mungu, kama nikitoka hapo nje na vibunda vya pesa kisha nivitawanye hewani, wapo ambao watakuwa tayari kufa na mimi wakijaribu bahati Yao ya uhai kwa kuzipata pesa. Pesa, pesa ni haramu ambayo hata maandiko yameshindwa kuweka wazi, sijui ni fumbo au hata mitume na manabii walishindwa kuelewa haramu ya pesa inavyoweza kuziteka hisia za mwanadamu..” Akameza mate na kuendelea kuongea kiasi kwamba hata mateka walisahau kama walikuwa na mtu ambae alikuwa amevaa mabomu na mara kwa mara kitenzambali kilikuwa kinacheza kwenye mikono yake kumaanisha wakati wowote angeliweza kufanya chochote kile.
“Najua hapa kuna watu mmfuata pesa kwa nia ya kuhonga, kulipa wauaji, kudhulumu haki za watu na wengine mpo hapa kwa nia moja ya kwenda kununua uhai wa ndugu yako kwa tabibu ambae amegoma kuokoa maisha yake bila pesa ya ziada, yaani unanunua ujuzi wake mbali na mshahara wake ambao bado unaulipa kwa kodi.” Alitulia na kuyatupa macho yake kwenye kituo cha runinga ambayo bado ilikuwa inaendelea na matangazo huku kukiwa na ujumbe na picha yake vikipita chini ya kioo cha runinga.
“Ajabu kabisa ni kwamba, hata mimi nipo hapa kwa sababu nataka pesa..” Alimalizia kwa kucheka kiasi kwamba na watu wengine nao ambao walivutwa na maneno yake nao waliungana nae kucheka.

2
Wakati Shija Mbitiyaza akiendelea kuongea na mateka wake, nje ya benki kulikuwa na mabishano baina ya kamanda wa kanda maalumu na kiongozi wa kikosi maalumu cha kupambana na kuzuia ugaidi.
“Unahatarisha sana kubarua chako.. mimi ndiye kamanda wa kanda ambayo ugaidi unatendeka, wewe kazi yako ni kunisikiliza na kutekeleza bila kuuliza swali la ziada.
“Naomba iwe mara ya kwanza kukubishia mkuu wangu, lakini kwa namna jamaa alivyojiweka na mabomu yake ni ngumu kumshambulia na eneo hili likabaki salama, jamaa kabeba milipuko ya hatari sana ambayo ni ngumu kuelewa kama huna taaluma ya milipuko.” Jamaa ambae alikuwa na cheo cha Inspekta msaidizi, alisema akiwa mbele ya Kamishina George Kilomba.
“Afande!” Jamaa mwingine ambae alikuwa kwenye timu ya kikosi maalumu alimuita Inspekta msaidizi ambae alikuwa akiongoza timu ya watu kumi na tano, timu ambayo ilikuwa imekamilika kwa kila kitengo kuwa na angalau watu wawili hadi watatu, kulikuwa na wataalamu wa kutathimini milipuko, wataalamu wa kutegua mabomu, watalaamu wa michoro ya eneo la tukio pamoja na mdunguaji mmoja ambae hakuwa miongoni mwa maofisa ambao walikuwa wamemzunguka kamanda wa kanda maalumu ambae alikuwa amechukua uongozi wa eneo zima kwa kutoa amri kwa namna aliyoiona inafaa.
Baada ya kuitwa aligeuka kutazama kule ambako askari wake alikuwa anatazama.
“Oh my God! Isiwe kama ninavyowaza.” Inspekta msaidizi alisema huku akiweka sawa silaha yake.
“Unawaza nini?” Kamishina George Kilomba aliuliza kwa mashaka huku nae akiwa amekodoa macho kule walikogeukia wenzake.
“Hakikisha vijana wako wote wanasogea nyuma zaidi ya hapa, hata wewe nakuomba ufanye hivyo kamanda.” Inspekta msaidizi alisema.
“Unahisi nini? Na kwa nini turudi nyuma ikiwa tuko umbali wa zaidi ya mita hamsini kutoka ulipo mlango wa benki? This is my oparation, remember that..” Kamishina George alifoka.
“This is your security area, oparesheni ni juu yangu na timu yangu..” Inspekta msaidizi alisema huku akimkata jicho baya lenye onyo juu yake. Hakusubiri malumbano zaidi, akatoa ishara kwa vijana wake na wakaanza kusonga mbele kwa tahadhari kubwa, macho yao yakiwa kwa mtoto na bibi yake ambao walikuwa wameongozana huku mtoto akiwa ameinua mkono mmoja juu na alitembea taratibu kwa kuwa alikuwa anatetemeka.
Inspekta msaidizi na timu yake walisogea hadi karibu na pale walipokuwa wamesimama mtoto na bibi yake.
“Macho..” Aliita kwa sauti ndogo na aliyeitwa alijua anatakiwa kufanya nini. Jamaa mmoja alisonga mbele hatua nyingi na kuwaacha wenzake wakiutazama mgongo wake.
“Simameni hapohapo...” Macho alipaza sauti kuwaonya wasiendelee kusogea mbele, amri yake ilitekelezwa na alizidi kuwasogelea zaidi huku akiitupa bunduki yake ubavuni mwake na kuiacha mikono huru ili kuondoa taharuki zaidi kwa mtoto ambae alionekana kuogopa zaidi kuliko hata wakati anatoka ndani ya benki.
“Unaitwa nani?” Macho alimuuliza mtoto huku akimshika mkono na kuichukua karatasi, akaiweka mfukoni bila kuisoma kisha akamtazama mama wa makamo akiwa nyuma ya yule mtoto, akamkagua kwa macho harakaharaka kisha akainama na kuanza kumkagua mtoto kwa mikono. Alipohakikisha hana kitu kingine mwilini mwake akahamia kwa mwanamke ambae muda wote alikuwa anatokwa na machozi, akamkagua kwa umakini bila kumgusa maeneo asiyotakiwa kuyagusa kwa sababu ya tofauti ya jinsia zao, lakini alihakikisha hakuna kitu cha ziada mwilini mwa yule mwanamke. Macho alikuwa ni mtaalamu wa ukaguzi na utambuzi na jina Macho lilikuwa ni jina la uficho nyakati za oparesheni.
“Kuna kitu kingine tofauti na hii karatasi mmetoka nacho huko ndani?” Macho alimuuliza.
“Hapana baba...” Alijibiwa.
“Kwa nini kawaruhusu?” Aliuliza tena.
“Karuhusu tulete hiyo karatasi.” Alijibiwa.
“Watu wengine wapo kwenye hali gani?” Aliuliza tena.
“Wapo salama kabisa..” Alijibiwa.
“Nifuateni..” Macho aliwambia na kuwaongoza kuelekea walipokuwa wenzake.
“Hawa si wetu tena, watu wa huduma ya kwanza wanamhitaji huyu na mtoto.” Inspekta msaidizi alimwambia Macho huku akipokea karatasi kutoka kwa Macho, akaipokea. Kabla ya kuisoma akatoa ishara upande wa maofisa wa msalaba mwekundu waliokuwa wamejitenga upande wao wakisubiri kukabiliana na janga lolote lililokuwa chini ya uwezo wao.
“Ofisa... Unawaitaje watu wa huduma ya kwanza ikiwa unajua wanatakiwa kuhojiwa na timu yangu?” Kamishina George alisema huku akipiga hatua ndefu ndefu kuwasogelea, nyuma yake walifuata askari wengine waliokuwa chini yake.
“Shiit!” Inspekta msaidizi alisema kwa jaziba huku akiwa anayakumbuka maneno ya mkuu wake ambae alikuwa na cheo cha Kamishina msaidizi wa jeshi la polisi, ambae alimjumuisha kwenye oparesheni licha ya cheo chake kutoruhusu kuwa msitari wa mbele, alimpa sababu za kumjumuisha na moja wapo ni kuhakikisha mwenye cheo kikubwa zaidi yake haingilii majukumu yake, kwa sababu kama angelipeleka maofisa daraja la pili pekee ingelikuwa ngumu kupinga amri za ofisa daraja la kwanza. Kwa uwepo wake licha ya cheo kuwa chini kwa Kamishina lakini kulikuwa na uzito kiasi chake. Kamishina Msaidizi aliyekuwa mkuu wa kikosi maalumu alifanya hivyo kwa sababu kesi kama hizo zinapokutanisha vitengo tofauti ni rahisi wengine kuharibu kwa sababu ya vyeo vyao, aliyakumbuka ya nchini Kenya wakati wa uvamizi kwenye supermarket. Magaidi walitingisha kwa saa nyingi kwa sababu vikosi vilijikuta kwenye mgogoro mkubwa, kila kiongozi alitaka vijana wake wafanye kazi ili apate sifa mwisho wa oparesheni na badala yake wakajikuta wakiweka mwanya kwa magaidi kutoroka na wengine kuendelea kutesa na kuua raia. Bila mgogoro pengine uthibiti ungelifanikiwa haraka zaidi. Hilo likawa somo kwake na hakutaka lijitokeze kirahisi ndiyo sababu ya kumteua Inspekta msaidizi kuongoza kikosi hicho na alichokuwa akikiwaza Kamishina Msaidizi ndicho kilichokuwa kinajitokeza wakati huo, lakini Inspekta hakutaka kuwa mnyonge, aliendelea kusimamia weledi bila kuathiri ushirikiano na Kamanda wa kanda maalumu ambae alikuwa haongozi kwa weledi bali kwa masilahi yake kiasi kwamba akasahau itifaki na ushirikiano.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom