Je, ni nani wanamtumia mwana JF huyu?

Bi Sent

Tunaomba utusaidie katika kutoa majibu ya maswali yaliyoulizwa katika waraka huu. Mimi naona mwanakijiji amenyabulisha mambo kwa utaalamu wa hali ya juu sana ambapo hata rafiki yako kasungura ataomba wamusomee kwa sauti ndogo.

Haya yaliyoulizwa pia JK alipofika ktk kipengere(Channel 10) hicho alionekana kupata kigugumizi pia, akifikiri bado wananchi tumefungwa minyororo na yeye tu ndiye mwenye kusoma jambo na kuelewa.

Mafisadi ninachojua huwa wanakaa karibu sana na wanasheria hawawezi kwenda mahakamani, hawawezi kwenda kujishitaki.

Mwanakijiji kwa hili anastaili pongezi, tunaomba Bi sent akishindwa aombe msamaha tu!
 
Wakuu naomba niiweke hii makala yenyewe hapa japo sijapata ridhaa ya Mwkjj ili muweze kuiona kama yasemwayo na Bi. Thumini kama yana uzito au la.

M. M. Mwanakijiji



KUNA michezo mingi ya kitoto ambayo ukikaa chini kufikiria inakuwa kama methali yenye maana. Baadhi ya michezo hiyo bado tunawaona watoto wetu wakiicheza leo hii sehemu mbalimbali nchini. Na kuna nyimbo nyingi za michezo ya kitoto ambayo watoto wetu nao huiimba siku hizi wakicheza kila jua lichwapo na giza liingiapo.

Mojawapo ya nyimbo bado ninazozikumbuka za tangu utotoni ni ule wa “Kakuku ka mama Rhoda”. Sijui ni nani alianzisha wimbo au ni kwa nini waliutunga, lakini kwa vyovyote vile huyo mtu alikuwa na lake kwani kuku wa jirani alikuwa anakula mpunga wa mtu huyo na kila akitaka kukafukuza basi mama Rhoda alikuwa “anamkataza.”

Sehemu ya wimbo huo ilisema “Kakuku ka mama Rhoda, kanakula mpunga wangu, nikitaka kukafukuza, mama Rhoda ananikataza,”. Sasa usijisikie vibaya kujikuta ukiuimba wimbo huo kimoyomoyo kwani hata mimi ninavyoandika hapa najikuta nacheka kimya kwa kubania.

Ninapofuatilia mambo yanayoendelea nchini leo hii hasa katika medani za kisiasa ninajikuta kama mtu yule ambaye kuna “kuku” wa jirani anayekula mpunga wake, na inakuwa kazi kumfukuza kwani jirani mwenye nguvu zaidi anakataza.

Lakini leo sitaki kuzungumzia kuku huyu wa jirani, ninachotaka kuzungumzia ni jambo jingine nadhani mtu analoweza kulitungia wimbo na watoto wakaucheza. Jambo hilo linahusu ‘kasungurak ka Mheshimiwa Lowassa kaligowanywa vipande vipande.

Waziri Mkuu, Edward Lowassa, alipokuwa akihutubia mkutano wa wananchi wilayani Sengerema katika ziara yake huko iliyomalizika siku chache zilizopita, aliamua kutumia mfano mwingine wa kuelezea hali ya kiuchumi ya Tanzania na hasa mgawanyo wa fedha katika bajeti iliyopita.

Waziri Mkuu alinukulikuwa na vyombo vya habari akisema: “Tumekaa bungeni kwa siku 67 tukigawana sungura...mnapaswa kujua mlipata mguu, maini au steki, ni haki yenu kujua ili muweze kufuatilia matumizi yake”

Ni haka “kasungura” ka Lowassa ndiko ninakotaka kukazungumzia kwa leo japo kwa kidogo tu. Baada ya kuja na majigambo ya kupaa kwa uchumi wa Tanzania mwanzoni mwa kikao hicho cha bajeti na kurudia tena wakati akitoa hoja ya kuhitimisha Bunge, leo hii amebadilika na kuja na mfano ambao ni kinyume kabisa na mfano wa ndege yenye kupaa. Lowassa ameamua kutumia mfano wa sungura kuelezea mgawanyo wa fedha za taifa katika sekta mbalimbali.

Lengo la mfano huo wa sungura lilikuwa kuonyesha jinsi gani “kile kidogo” tulichonacho au tulichokipata tumegawana kama taifa. Mfano wa sungura una lengo la kuonyesha kuwa tulichonacho ni kidogo na tunagawana kidogo kidogo na hivyo sisi sote tuwe waangalifu.

Kwa watu wengine mfano huo unaweza kuwa umewapita pembeni, lakini kwa mzee wenu kama kawaida ninaweza kusoma maneno ndani ya maneno. Nilipokaa chini kutafakari maneno hayo ya Waziri Mkuu nilijikuta nikikabiliwa na maswala kemkem.

Kwa nini tugawane ‘kasungura’ wakati tuliona wamenunua ng’ombe? Walipokwenda kuwinda (kuomba misaada na kukusanya kodi n.k) walijitamba kuwa wamenunua ‘ng’ombe’, lakini leo sisi wananchi tunaletewa kasungura imekuwaje? Kuna mtu anahitaji kutupa maelezo fedha zetu za ng’ombe zimekwenda wapi? Au ni nani huyo aliyekula ng’ombe wetu wa taifa na kutuachia sisi watu wa Sengerema, Nansio, Bunda, Ndali, Mabokweni, Endabash, Ujiji, na kwingineko ‘kasungura?’

Wakati walipokwenda kununua ndege ya bilioni 50 na rada ya bilioni 50 sawa walitumia kwa ujumla karibi bilioni 100 na ushee na waliponunua magari mawili ya ofisi yake kwa karibu milioni 200 nina uhakika hatuwezi kusema hako ni ‘kasungura’. Leo hii mawaziri na manaibu wao jumla ya watu 60, madereva, na wasaidizi wao wanapita vijijini kutuambia jinsi tulivyogawana sungura huyo.

Hivi kuna mtu amewauliza wanatumia gharama ya kiasi gani kutuuzia habari za sungura aliyekatwakatwa vipande vipande? Makisio ya rafiki yangu mmoja mwenye kujua undani wa ziara ni kuwa waheshimiwa hao watatumia karibu shilingi bilioni mbili, kutunadia gharama ya sungura ‘mjanja’. Tukisema ufisadi tunaambiwa tunawasingizia. Ufisadi si rushwa tu, hata matumizi mabaya ya ofisi yanaingia humo humo.

Rafiki yangu mmoja (mwalimu wa chuo kikuu kimoja Marekani) nilipomwelezea habari hizi mpya za Lowassa ilikuwa kama bahati hivyo. Siku chache zilizopita yeye na wenzake walikwenda kuwinda sungura, na baada ya majaribio ya hapa na pale walijikuta ili kujitosheleza kwa ‘mboga’ walihitaji kujipatia sungura watatu, kwani sungura mmoja hatoshi. Sijui ni nani aliyempa mfano huo Waziri Mkuu maana mifano mingine inatolewa kwa lengo zuri lakini maana yake inakuwa kubwa kuliko ilivyokusudiwa.

Nikiendelea kuzungumzia huyu sungura wa Lowassa yeye aliyemaanisha ni fedha za wananchi wao bungeni walizokaa kuzigawa na akatamba kule Sengerema kuwa mwaka huu serikali imetenga fedha nyingi kabisa ikiweka kipaumbele kwenye sekta kadhaa. Majigambo hayo yanastahili makofi kwa mtu asiyehoji, lakini katika Tanzania hii wananchi walioameanza kuamka, tatizo haliko katika kasungura kenyewe, bali wale wanaotugawia sungura huyo.

Leo hii kashfa mbalimbali zinazungumzwa na karibu shilingi trilioni moja zinadaiwa kupotea katika mikataba mbalimbali mibovu na maamuzi mbalimbali mabovu. Na hizo ni fedha unazoweza kuchunguza kwa kuangalia vitabu. Lowassa mwenyewe huko huko Mwanza aliwaasa kwa mara nyingine tena (ndiyo mara nyingine nikianza kuwahesabia itabidi niandike makala nyingine) wakurugenzi wa halmashauri kuwa “mkurugenzi atakayerudisha fedha kwa kushindwa kuzitumia katika miradi iliyopangwa atachukuliwa hatua.” Vitisho hivi vya Waziri Mkuu ni vitisho tulivyovizoea tangu walipokwenda Ngurdoto wakatuletea ndoto yao.

Rais mwenyewe, makamu wake na hata mawaziri wengine (Dk. Mwinyi karudia tishio hivi karibuni) wamekuwa wakivitoa kama wimbo wenye ubeti mmoja. Ukweli ni kuwa vitisho hivi vimezoewa na watendaji mbalimbali wa serikali.

Rafiki yangu mwingine aliyeko Dar es Salaam ameniambia kuwa siku hizi kwenye klabu za usiku kuna baadhi ya watu wananyanyua glasi zao za mvinyo na kugongeana wakisema kwa kejeli “maisha ya neema yanawezekana, kwa wana-CCM”. Hakuna mtendaji anayeogopa vitisho vyao, kwani wanajua kuwa “nani atamnyonyeshea nani kidole”.

Leo hii Lowassa na viongozi wengine wanasisitiza wananchi wawafichue wanaofuja mahali za umma na wanaokula fedha za umma. Bahati nzuri Mtanzania mwenzao Dk. Slaa na Watanzania wengine kama kina Tundu Lissu wamejitolea kuwaonyesha wananchi kuwa kale kasungura kalikuwa kamezaa na kuna watu wamekula vitoto vya sungura ndio maana tunaendelea kugawana kasungura kamoja! Watawala wetu hawataki kukubali na badala yake wako kwenye jaribio kuu lililoshindwa la kukana.

Na tatizo kubwa ni kuwa hata kukana kwenye hakuna mantiki. Hivi kama watu wamechafuliwa majina na wametuhumiwa vitu vya uongo kwanini wanaitisha vyombo vya habari kuwaambia ni jinsi gani hawakutendewa haki? Hivi kwa watu wasomi kama kina Dk. Mgonja na kina Rutabanzibwa wanaona ugumu gani wa kwenda Mahakamani?

Binafsi kama kuna kitu kimenichekesha ni kitendo cha watu hawa wote kukimbilia kwa waandishi wa habari na kusema ati watakwenda mahakamani. Hivi nani amewaambia kuwa ili kwenda mahakamani hadi waombe kibali toka kwa wahariri na waandishi?

Binafsi ningefurahi kuona ndugu zetu hawa wakikimbilia mahakamani ili kuwaonyesha wananchi kuwa wao ni waadilifu na wanaofuata utawala wa sheria. Na wakati wakienda huko mahakamani nina uhakika kuwa mahakama itapotoa hati za kuita mashahidi watakaoitwa wataheshimu mamlaka hiyo ya mahakama.

Bila ya shaka kama wakienda mahakamani baadhi ya wananchi ambao wanaweza kuitwa mahakamani ni pamoja na Rais Mkapa, Waziri Mkuu Lowassa, na aliyewahi kuwa Waziri wa Maji, Nishati na Madini Jakaya Kikwete. Nina uhakika kama kuna wakati ambapo demokrasia yetu itatiwa moyo na utawala wa sheria kuinuliwa juu ni pale tutakapowaona kina Mkapa, Lowassa na Kikwete wakinyosha mikono juu kula kiapo pale Kisutu kuwa watasema “kweli na kweli tupu”! Waliotishia kwenda mahakamani sidhani kama wamefikiria hilo.

Sasa hivi viongozi wa serikali na CCM wameanza ziara ya kwenda kwa wananchi kuelezea na kujibu hoja za wapinzani. Bila ya shaka watajaribu kutuelezea kale kasungura ketu kalipatikana vipi, ilikuwaje kasizae licha ya kukalisha kwa kila chakula bora na mashudu! Sitashangaa uhakika wananchi watawapokea kwa mabango yenye kuuliza “kasungura sawa, ng'ombe wetu vipi?” Na sitashangaa wananchi wakiuliza “Aliyekula ng’ombe ni nani, mbona mwatupa sungura?” Usalama wao itakuwa ni kwenda kuwaelezea viongozi wenzao wa CCM wa huko vijijini.

Viongozi wa CCM waache kukurupuka na badala yake wakae chini, watafakari uzito wa hoja zinazotolewa na wajibu hoja hizo kwa hoja. Mambo ya kuwafanya Watanzania hawawezi kufikiri au kwamba hatuwezi kusoma alama za nyakati ni kututukana matusi ya rejareja.

Kama CCM na serikali yake wanafikiri kuwa watawaburuza tena Watanzania kwa hoja zisizo na mkia wala kichwa alimradi vimulimuli, bendera na parapanda zinapigwa, basi wao wazinduke katika jinamizi hilo, maana limewakaba.

Hoja ni lazima zijibiwe kwa hoja. Kutuma wapambe, mawaziri, manaibu waziri au vikundi vya nyimbo kuwataka wananchi wapuuzie hoja ni kutaka kuwaweka mtegoni kwani wananchi wamejiandaa kuwazomea na kuwakatalia majibu yasiyoeleweka. Uwingi wa maneno si uzito wa hoja! CCM na serikali yake wanajitahidi kusema mengi pasipo kusema lolote lenye maana huku wakitumia vyombo vyao kuupotosha umma ili kupoteza mwelekeo wa hoja. Safari hii wameshikwa mashati na hawaachiliwi hadi watoe majibu yenye kueleweka.

Watoe majibu ilikuwaje Rais na Waziri wake wawe na hisa kwenye kampuni ambayo wao wenyewe wamehakikisha kuwa inapata mkataba mkubwa wa serikali? Watoe majibu ilikuwa kampuni inayoitwa ni ya serikali iandikishwe nje ya nchi na kwenye vipengele vya uundwaji wa kampuni hiyo hakuna mahali panaposema kuwa ni ya serikali?

Watoe majibu ilikuwaje kwenye kampuni hiyo urithishaji uende kwa watoto wa wakurugenzi wa “serikali” na wajukuu wao? Watoe majibu yanayoeleweka ya maswali hayo na wajibu swali baada ya swali si kama walivyofanya juzi kwa kuchagua maswali mawili matatu kuyajibu.

Mtu unapopewa mtihani unatakiwa kujibu maswali yote hata kama utakuwa umekosea, lakini kuruka maswali ni kujitakia alama za ‘si vyema’ za bure. CCM mmejichimbia shimo na ni nyinyi wenyewe mjitoe humo!!

Wananchi wamechoka kuambiwa maneno matupu alimradi yanatoka kwenye “tamko rasmi la serikali”. Ndugu zangu wananchi haya ni mapambano ya kifikra.

Mapambano haya yalianza rasmi Mei 1995 wakati Mwalimu alipojenga hoja nzito ya “wapi tunatoka, wapi tulipo na wapi tunataka kwenda”. CCM sasa hivi wamebanwa kwenye uwanja wa hoja, na wanatapatapa; fikra zao zinaonekana kuwa ni dhaifu hata kama watazipigia matarumbeta na kuziwashia vimulimuli na kupiga ving’ora! Hoja dhaifu ni hoja dhaifu hata itolewe kwa ngoma na muziki wa jadi!

Ushauri wangu wa bure ni kwa CCM kukaa chini, wapime uzito wa hoja, na watambue wapi makosa yalitokea, wazungumze na wananchi na kuwaambia wananchi ukweli. Wawaambie kuwa kulikuwa na makosa kwenye mkataba wa Buzwagi, kwamba viongozi kadhaa hawakufuata maadili ya uongozi, na ya kuwa kulikuwa na upotevu wa fedha nyingi na hatua zinachukuliwa dhidi ya wahusika (ikiwamo kufilisiwa) na kuwaahidi wananchi kuwa mambo kama hayo hayatotokea tena.

Wakubali kuwa kuna mtu aliboronga na mtu huyo lazima awajibishwe. Kwa wao kuendelea kung’ang’ania kuwa “hakuna tatizo” na ya kuwa “hoja hizi ni za wapinzani waliopoteza uchaguzi 2005” ni kutudharau Watanzania na kutudhania kuwa hatuwezi kupima pumba na mchele.

Kabla sijamaliza naomba nitoe ombi kwa wachora katuni wa vyombo vyetu vya habari. Katika nchi mbalimbali ambako mwamko wa fikra za kimageuzi zimeanza kusambaa, basi kambi zinazopingana zinakuwa na alama zao. Kenya kulikuwa na Machungwa na Ndizi, na kule Uganda walikuwa na majani ya migomba!

Hapa Tanzania bado hatujawa na alama za pande mbili za kisiasa zinazogongana sasa hivi kifikra. Hivyo, napendekeza kuanzia sasa “sungura” awe ndiyo alama ya CCM, kwanza kwa jinsi alivyotumiwa na Lowassa lakini kubwa zaidi kutokana na ujanja wake katika masimulizi ya fasihi yetu.

CCM imeweze kujijenga na kujijengea mazingira ya kutawala kutokana na kuwa na ujanja wa kisiasa. Hivyo sungura atawakilisha wale wote wenye mawazo ya CCM na ambao maisha yao yamenufaika na kufaidishwa na maisha ya kijanja kijanja.

Kwa upande wa upinzani, napendekea alama ya punda. Nimemfirikia punda kwa vile ni mnyama wa kazi huenda anayetaka kwenda na mara nyingi hawezi kwenda mahali pasipo kusindikizwa na punda mwingine. Zaidi ya yote, punda anatabia ya kuchoka anapotwishwa mzigo kuliko uwezo wake hivyo hata achapwe mijeledi kiasi gani akigoma kagoma.

Ni kiburi cha ‘utu’ wake na hadhi yake kuwa kuna mizigo mingine habebi. Hivyo punda basi atawakilisha wale wote ambao kutwa kucha hufanya kazi kwa kujituma ili wajitengenezee maisha mema ya mafanikio. Watu hao wamefikia mahali sasa hawakubali tena kuburuzwa au kulazimishwa kwenda wasikotaka kwenda, kukubali visivyokubaliwa, na kupigia makofi visivyoshangiliwa.

Mwisho kabisa niseme kuwa watawala wetu wanapokuja na maelezo ya sungura wa Lowassa, wakumbuke kuwa wananchi nao wanajua kilichonunuliwa kuwa ni ng’ombe, tena si ng'ombe mmoja. Kwa muda mrefu wananchi wamekaa kimya kwa heshima lakini sasa wanataka kujua iweje wao wapewe sungura wakati wachache watetewe na walindwe walipokula ng'ombe na mbuzi wa kijiji?

Wakati umefika tukatae kuendelea kugawana kasungura ka Lowassa kanakonadiwa na viongozi wa CCM. Tuwaambie kwa heshima kubwa na taadhima, kuwa tumechoka kugombea kasungura! Na sisi tunataka ng’ombe!

Kama kwenye ndege iliyopaa mmepakiana wenyewe, basi angalau kwenye kula ‘ndama’ na sisi mtugawie! Na hilo si ombi ni takwa, kwani tumemlipia huyo ng’ombe na tumemlisha! Iweje wenzetu mle hadi mrithishane mapaja na mbavu, halafu mje kutuuzia habari za sungura!?

Vinginevyo, tutawatungia wimbo kama ule wa “kakuku ka mama Rhoda” Hatutakubali kuendelea kukatazwa kukafukuza kakuku hako kanakokula “mpunga wetu”. Na maneno ya kwanza ya wimbo huo yatasema “kasungura ka Lowassa kamekatwa vipande vipande, nani kala sungura, na nani kala ng’ombe?”

Niandikie: mwanakijiji@jamboforums.com
Sikiliza mahojiano na Tundu Lissu: http://www.mwanakijiji.podomatic.com


Ndugu MM Mwanakijiji,hii makala ni nzuri sijawahi kuona,natanguliza shukrani zangu,na Mungu akubaliki.heshima yako mkuu.
 
Bi fifty cents nakupa pole, haiwezekani unyamazishe mawazo ya wazelendo. hautufai pamoja na waliokutuma. Huyu Ngoyayi anatuletea kasungura, Je ngombe analiwa na nani. Si ndio hayo madini?

Lazima tuseme kwa sauti kuu hata ikibidi kupoteza maisha ujumbe umefika na ni kwa faida ya kizazi kijacho. Ni heri niingie hatarini nikipigania maslahi ya nchi na watu wake kuliko fedheha hii.
 
Hoja ya Mwanakijiji Amei-present vizuri sana, kama ingekuwa kutuoa hoja ndio kuwa kiongozi mzuri,,, ningemwomba arudi mara moja akagombee angalau ubunge, lakini huwezi jua huenda akawa efficient kwa position yake aliyonayo leo!
 
hata Baba yangu kila siku anamsifia Mwanakijiji,na huwa naniambia niwe namprintia artcle yoyote ya Mwanakijiji,hii ni kutokana na kwamba Mwanakijiji huwa anatulia sana kabla ya kuandika chochote..
mie mwenyewe sikuipenda kauli ya Ngoyai kuhusu ngege inayopaa pamoja na hii ya kugawana ka 'sungura',
au hii ni mifano ya kimasai?
Mzee mwanakijiji endelea..
tena wiki ijayo tunaomba uchambue hotuba ya Mwalimu aliyoitoa wakati wa Mei Mosi 1995
 
Naungana na nyie wote kwenye hilo.. Huyu Senti 50, yeye ndie katumwa, kwa nini amzuie mtu kutoa maoni yake? Kipi ambacho sii cha kweli hapo? Ninlitegemea B50 aweke hoja hizo wazi na kusema hiki ni cha kweli na hiki ni uongo, sio kumuogopesha mwandishi.. au anataka kuturudisha nyuma kwenye miaka ile kwamba haturuhusiwi kutoa maoni? Umechoka Sent 50.. Acha wenye mawazo yenye msingi kwa watu wayatoe...

Nimelipenda jina lako kwani wakati nilipokuwa nafanya mkazi mkoa wa kilimanjaro ,huu ni mti wa kutengenezea mbege au nimesahau?

Mwanakiji kaza buti hapa hapendwi mtu wanapendwa wananchi.

Ni kweli kuwa mwanakiji ametumwa ,ila tofauti ni kuwa yeye katumwa na dhamira safi na mapenzi yake kwa nchi yake.

Ametumwa na kuumia juu ya umasikini wa watanzania , ametumwa na mayatima wanaokosa haki zao kila kukicha.

Ametumwa na wananchi wanaonyanganywa madini yao na kupewa wageni halafu wanafukuzwa.

Ametumwa na wanafunzi wa vyuo vikuuu wanaokosa ada ya kulipia na kulazimika kuacha masomo.

Ametumwa na wakaazi wa eneo la jangwani waliobomolewa nyumba zao eti wahindi wakajenge magodown ya bidhaa zao feki kutoka.....

Ametumwa na vijana wasiokuwa na ajira ,na wakionekana mijini wanaitwa wazururaji,

Ametumwa na wanawake wajawazito ambao wanadaiwa nyembe na glovus wakiwa na uchungu mahosipitalini,

Ametumwa na wazee waliofanya kazi jumuiya ya Afrika mashariki walionyimwa mafao yao,
Ametumwa na wazee waliopigana vita ya pili ya dunia na hadi leo fedha zao zinatafunwa na mafisadi,

Ametumwa na wanyonge wa nchi hii ambao hawana mwingine wa kuwasikiliza ila wamemwona yeye anaweza walau kuwafikishia ujumbe wake ,

Mwisho ametuimwa na wale waliokosa ng'ombe wakaambiwa eti wao wagawane kasungura ile hali first eleven wanagawana ng'ombe.

Nina uchungu sana , nami nimemtuma pia kwani anaweza kunisemea.
 
Bi sent 50 kulikoni? Mbona watetea ufisadi wewe, huoni watz wanavyoishi kwa tabu,gharama za maisha zinapanda kila siku sababu ya watu wachache,halafu unasema Kasungura katumwa? Kweli bi sent 50? Au wewe ndo umetumwa?
 
Na wewe binti senti 50 umetumwa na nani? Na umetokomea wapi? Au hukutarajia majibu haya? Unatupa mawe kwenye mzinga wa nyuki ukitaraji nini? Pole binti. Lakini ninaamini umepata jibu la kumpelekea aliyekutuma.
 
rabbitjumpingb10938wd5.jpg

Kasungura ka Lowasa Ngonyani hakooo


Nyani giladi anakomwa hapahapa na si pengine!

Nondo za JF zinawafundisha adabu vibaka na ipo siku watalipa tu hapa hapa pale watakapofikishwa mahakamani ndani ya karandinga la polisi. Si mnaona waliopata nyama ya kasungura wanavyobwata. BRAVO BRAVO BRAVO ..................Mzee Mwanakijiji.
 
naumia sana,hawa mafedhuli mafisadi ni watu waovyo sana,mie now nikimuona EL anapita hata nchi natamani nimnyoe nywele kwa kutumia mikono..tena karamagi mie naweza hata kumtoa macho,hawa ndio wanaotudumbukiza katika umasikini..
Mungu unagoja nini kuwaangamiza mafisadi hawa?
 
vipi tena mbona walia/ cheka kama kifaranga kilichoona mwewe? au ndo mambo ya wikendi hayo....?

Nyani Nyani Nyani, Vifaranga wa nini wanao lia /cheka hivyo?.... mwewe kikiona mwewe mama yake, kifaranga cha bundi, kifaranga cha tausi, kifaranga cha bata, au kifaranga cha mbuni? :)

SteveD.
 
Nyani Nyani Nyani, Vifaranga wa nini wanao lia /cheka hivyo?.... mwewe kikiona mwewe mama yake, kifaranga cha bundi, kifaranga cha tausi, kifaranga cha bata, au kifaranga cha mbuni? :)

SteveD.

hey dawg...i'm already on tha s#!%...you know...
want some....?
 
Duh!! mwenyewe nimeingia humu, got my breakfast on the table.. ready to read huyu mtu anayetumiwa hapa JF!! Nusura nipaliwe! Kumbe yamekuwa hayo... Anyway, nashukuru ndugu zangu kwa support, but I think it is enough. I'm getting really nervous, nadhani tumsamehe dada Bi. Senti, na kama ni ujumbe nadhani umefika au ni jaribio jingine la kutufanya tukwepe kuzungumzia hoja nyingine. Duh.. hii kali.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom