Moja ya tafsiri potofu za wanaojiita walimu wa jamii wa siku hizi ni hii dhana ya pesa kumuamulia mtu ni nini cha kufanya.
Ukweli ni kuwa Pesa haina uwezo wa kuamua ni nini cha kufanya bali binadamu na akili zake ndiye mwamuzi wa mwisho wa matumizi ya rasilimali alizo nazo zikiwepo pesa.
Kuhusu mipango na matumizi, nimewaza haraka haraka makundi matatu nitakayoyaelezea kwa ufupi sana kama ifuatavyo.
Wapo watu wanaopanga mapema mipango ya kufikia lengo maalum kwenye maisha yao kabla ya pesa. Malengo yao ndiyo huwachochea kupanga mipango, na ili kuitimiza mipango yao, rasilimali mbalimbali hutafutwa, zikiwepo pesa. Hawa ndiyo wale wanaojipambanua kuwa wanaamua pesa ziwafanyie nini. Hawa wanapanga mipango na wanajua ni nini kitahitaji rasilimali pesa na kisha hutafuta njia ya kuzipata ili watekeleze mipango yao.
Kundi la pili wanasubiri wapate pesa ndipo waamue watafanya nini na hizo pesa. Hawa huishi kwa kuwaza tu namna ya kupata pesa kwanza kisha kuipangilia ni baadae. Kama kuna chanzo chochote cha pesa, ndicho kitaamua mipango yao. Hili kundi, fikra na mipango yao huathiriwa na uwezo wao wa kupata pesa. Labda hili kundi ndilo linalolaumiwa kuwa pesa zinawapangia ni nini wafanye, japo wao ndio huamua ni nini wafanye na kiasi cha pesa walichopata.
Kundi la tatu ni kundi lisilokuwa na mipango ya pesa. Hili kundi hutumia kilichopo kutimiza mahitaji ya lazima tu, inayobaki huelekezwa kwenye anasa au kugawia wengine kwa njia zozote. Hili kundi wengi wao ni wafujaji wa pesa, watoa misaada bila mpangilio, wale watoaji mpaka senti ya mwisho, nk.
Ninaamini kundi la kwanza lina nafasi ya kufanikiwa zaidi kuliko makundi mengine. Hasa hasa endapo wataweza kuwa na malengo sahihi, mipango mizuri na mbinu bora za kutafuta rasilimali za kutekeleza mipango yao.