SERIKALI imesema uhakiki wa watumishi wa umma, utakamilika ndani ya mwezi huu, hivyo nafasi zilizoachwa wazi baada ya kuondolewa kwa watumishi hewa, zitaanza kujazwa.
Aidha, imesema kwamba baada ya uhakiki huo ambao utasaidia kuwa na orodha sahihi ya watumishi waliopo katika taasisi za umma kwa lengo la kuboresha hali ya utumishi nchini, itaanza mfumo wa kuhakiki majina mapya.
Akizungumza katika awamu ya pili ya kipindi cha Tunatekeleza kinachorushwa TBC 1 juzi, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dk Laurean Ndumbaro alisema uhakiki wa watumishi hewa, umesaidia kuongeza ufanisi katika taasisi zake.
Dk Ndumbaro alisema baada ya kukamilika kwa uhakiki huo, pia wataanza mfumo mwingine wa kuhakiki majina mapya ambayo yatajitokeza mara mbili na kuyatoa ili kubaki na majina sahihi.
“Kwa mfano, yupo mtu anatumia majina matatu lakini akatokea mmoja akaondoa lile la katikati na kubaki na majina mawili labda Laurean Ndumbaro hivyo mfumo utaona kuwa ni jina jipya kumbe kuna mtu ambaye amejitengenezea jina hilo,” alisema Dk Ndumbaro na kufafanua kuwa ili kuondoa mkanganyiko huo, mfumo utatambua na kuyaondoa majina yasiyohusika.
Chanzo: HabariLeo =>12/10/2016