Wanasiasa wajanja mtanaswa

sulphadoxine

JF-Expert Member
Nov 1, 2010
2,257
644
SIAMINI kama siasa ni mchezo mchafu kama ambavyo watu wengi wanavyodhani, isipokuwa siasa ni njia ya kuwapitisha viongozi waadilifu wanaoweza kujua wapi tulipo toka na wapi tunapokwenda.
Siasa ndio chimbuko la uimara wa nchi na ujenzi wa viongozi wanaotakiwa kuwa mstari wa mbele kupigania haki za nchi zao na kuwa wazalendo zaidi kwa kila njia wapitayo ili kuweza kurutubisha misingi ya uongozi na utawala bora.
Kuwa mwanasiasa hakumaanishi kuwa kunajengwa na kundi la watu wahuni ama kwa kupitia vyama vyao vya siasa au kilio hiki kinachoendelea cha baadhi ya wananchi wanaotaka siasa kujaribu kujenga mfumo wa siasa huru na dhana ya mgombea binafsi bila kuhitaji chama.
Kuwa mwanasiasa kwa kiasi kikubwa kunahitaji kuvuta dhamira na matarajio ya watu wengi kukuona ama kuwaona kuwa kitendo cha kusimama mbele ya watu na kuongoza mapambano ya kisiasa kusiwe chanzo cha uhaini au usaliti wa nguvu ya umma inayoamini kuwa bendera ya wanasiasa ndio dira ya uongozi.
Kama ndio hivyo na wengi wanavyoona kuwa huwezi kuwa kiongozi wan chi au kuwa Mbunge bila kupitia siasa basi tuamini kuwa hiyo ndio njia nyofu ya mwanzo wa ukomavu na uadilifu wa viongozi wanaotakiwa kuwa tegemeo la wananchi wengi.
Lakini kama siasa inafanywa kwa mtego mtego,ujanja ujanja huo ndio unakuwa mwanzo wa hila na njama chafu za kuvuruga amani ya nchi, kurudisha nyuma maendeleo ya nchi na kubaki na kundi la watu wasioweza kuaminiwa na umma ambao dhamira yao sasa inageuka mwiba kwa wale waliowachagua.
Wanasiasa walioamua kuwageuka wananchi na kushindwa kuwapigania kwa dhati kamwe hawawezi kung’ara tena machoni mwa mamilioni ya watu waliokuwa na matumaini makubwa ya kuvuka mto wa umasikini na kwenda kwenye bahari ya neema.
Itakuwa vigumu sana kuongozwa na kundi la wanasiasa wachanja wanadhani kuwa kuupata uongozi ndani ya nchi kwa kupitia siasa ni sehemu ya ufinyu wa mawazo ya wananchi na kwamba lolote linalotokea linatokana na nguvu ya kisiasa na si utashi wa umma.
Haya yanayotokea hivi sasa kwa kiasi kikubwa ni chimbuko la wanasiasa waliosahau wajibu wao na kudhani kuwa kutokuwepo kwa maendeleo makubwa ya kiuchumi kumesababishwa na kundi la watanzania wengi waishio vijijini ambao asilimia kubwa ni wakulima.
Au kutokukua kwa uchumi wa nchi kunatokana na kundi kubwa la vijana waliojazana mijini wakiuza vipodozi na nguo za mitumba huku wengine wakifanya kazi ya kukata kucha na kupaka rangi miguuni kuwa hao ndio wanaosababisha uchumi usikue kwa haraka.
Au hawa wazee wastaafu waliomaliza kazi za utumishi wa umma na kulipwa mafao ya kupunjwa hivi sasa wamegeuka kuwa omba omba mijini wakipita kwenye kila ofisi kuwa hawa nao ni kikwazo cha uchumi na hawahesabiki tena kwa mchango wao walioutoa kwa zaidi ya miaka 35 ya utumishi uliosahaulika.
Au ni kundi la watoto wa mitaani walioshindwa kupata malezi bora kwa sababu mbali mbali za kukosa haki zao za msingi, kufiwa na wazazi wao, jamii kuwatenga na kusababisha kizazi hicho kiwe cha hatari kuwa hawa nao ni kundi linalosababisha uchumi usikue kwa kasi.
Kama hayo yapo na wanasiasa hawa kwa dhamira zao waliamua kujiunga kwenye vyama vyao na kuunda sera za kuondokana na adha mbaya za umasikini ni wapi ambapo hawa wanasiasa wajanja wanapoweza kusimama na kudai kuwa wanaweza na wameweza nini.
Ni kipi ambacho wanasiasa hawa wanaweza kujivunia katioka kipindi cha takribani miaka 50 kuwa wamesaidia kujenga uchumi imara,kulinda vyanzo muhimu vya ajira kwa kupunguza wimbi la wasomi wa kitanzania wanaokimbilia nchi za nje kwenda kufanya kazi.
Sababu za wanasiasa wajanja kutumia turufu ya unyonge wa wananchi kumesababisha wasomi wengi kushindwa kuhimiri mfumo wa kiutawala uliopo kwa kuwa haukidhi mahitaji ya jumla na haubebi dhana ya utaifa isipokuwa kunachochea chuki na matabaka ndani ya jamii.
Siku zote kumekuwa na msemo rahisi unaosema hivi “ Ndege mchanja hunaswa kwenye tundu bovu” huo sio usemi wangu lakini naamini kabisa kuwa wanasiasa wajanja hawatofautiani na msemo huo kwa kuwa huishia kwenye historia mbaya baada ya kushindwa kutimiza matarajio ya umma.
Naamini kabisa kuwa kitendo cha wanasiasa kushindwa kutekeleza wajibu wao kwa dhati na kwa uaminifu mkubwa kumekuwa na dosari kadhaa zinazofanya chombo cha umma kiende mrama na manahodha walioaminiwa kuendesha chombo hicho wamezidiwa na inda iliyojaa uchu wa madaraka.
Wanasiasa kwa nafasi zao ndio waliopata nafasi ya kuingia bungeni na ndio wanaoketi kwenye viti vilivyopambwa na kodi za wananchi lakini shingo zao hazigeuki nyuma ili kuangalia kule walikotoka,walipokuwa wakiomba kura hawakubagui kuyafikia makundi ya wanyonge hoehae.
Wanasiasa hawa kwa nafasi zao za kisiasa na ubunge wengine ndio mawaziri na wakuu wa mikoa ambao sifa njema ya uongozi uliotukuka siamini kama wamefika hapo kiujanja ujanja ili kuweza kuvuruga matarajio ya wengi isipokuwa wameingia siasa ili kuweza kuondoa makovu ya umasikini.
Kwa tafsiri hiyo,ya wapi maisha bora kwa kila Mtanzania ni yupi ambaye anaamini kuwa Watanzania wengi hawaishi gizani,ni mwanasiasa yupi ambaye hajui kuwa gharama za maisha zi juu kiasi cha kuwafanya wengine wengi walale njaa majumbani mwao.
Ni mwanasiasa yupi ambaye hajui kuwa zipo kaya kadhaa ambazo wazazi hawawezi kununua hata kijiko kimoja cha sukari,hawawezi kununua koroboi moja ya mafuta ya taa,hawawezi kununua kipande cha sabuni na wapo ambao hawawezi kununua hata sindano na uzi wa kushonea viraka kwenye nguo zao kuu kuu.
Lazima dhamira za kweli ziwasute wanasiasa hawa na kamwe kama wapo walioingia siasa kiujanja ujanja na kusahau kuwapigania watu masikini watashindwa kuwavusha wananchi kwenye daraja la umasikini na kuwatumbukiza kwenye shimo la ufukara usiweza kukoma.
Ipo haja kila mwanasiasa kwa nafasi yake abaki na kutafakari kwa kina sababu zilizomfanya awe mwanasiasa na ajue kuwa kwa kuamua kuwa hivyo atakumbukwa kwa jambo gain la maana na ameweza kupigania mabadiliko yapi ndani ya chama chake na nje ya wananchi.
Lazima wanasiasa wajiulize nimewezaje kuacha kazi ya kuwatibu wagonjwa nikiwa daktari na kuamua kuingia siasa, nimewezaje kuacha kazi ya kuwafundisha wanafunzi vyuo vikuu nikiwa mhadhiri na kuamua kuwa siasa, nimeachaje kuwa mhandisi wa ujenzi wa barabara na majengo makubwa na kuwa mwanasiasa.
Lazima wataalamu hawa wajiulize nini mchango wao ndani ya siasa na ni nini matokeo ya kuamua kuacha kazi zao za kitaaluma na kuingia siasa, wameongeza nini au wameingia humo kwa ujanja ujanja wakijua kuwa ukitaka kula na kipofu usimshike mkono.
Ili nchi hii iweze kuendelea na kuondoa dhana ya chokochoko za kisiasa kuwa kwa namna fulani zinachangia kuwavuruga wananchi sio kweli, siasa hizo hazikuanzia Tanzania na wenzetu waliopiga hatua kubwa za kiuchumi wamwetoka huko,kikubwa na uadilifu na kupiga vita ufisadi bila hivyo hatutafika. Kama tumedhamiria kufika kule tuendako na kikubwa wanasiasa wanapaswa kuacha kutumia nyadhifa zao kwa itikadi ya vyama vyao bali wageuze msimamo utakaoweza kuwafikisha kwenye nia ya kupata jahazi moja bila kupigana, vinginevyo hatutavuka mto wa umaskini.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom