macho_mdiliko
Platinum Member
- Mar 10, 2008
- 28,336
- 57,214
Mtangaza nia akataa bilioni moja
MMOJA wa waliokuwa mawaziri katika serikali ya Rais Jakaya Kikwete amefuatwa na wafanyabiashara wakimuahidi shilingi bilioni nne endapo atajitosa kuwania urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Wakati huohuo, mmoja wa watangaza nia wa CCM amekataa mchango wa zaidi ya shilingi bilioni moja aliopewa na mmoja wa wafanyabiashara ambao wanahusishwa na ufisadi hapa nchini.
Waziri huyo ambaye jina lake tunalihifadhi kwa sasa, aliliambia Raia Mwema katika mahojiano maalumu wiki hii kwamba hata hivyo amekataa fedha hizo kwa vile ameona itakuwa sawa na kuuza "urais wake".
Gazeti hili lilikuwa limemfuata waziri huyo, ili pamoja na mambo mengine, aeleze kwanini hadi sasa hajachukua fomu ya kuwania urais ingawa jina lake limekuwa likitajwa kwa muda mrefu.
"Nina uwezo wa kuwa Rais wa Tanzania na nchi ikapata maendeleo na ikawa salama, lakini katika mazingira haya siwezi kuingia kwenye kinyang'anyiro.
" Sina fedha za kushindana na wenzangu. Uwezo nilionao ni wa kujaza mafuta kwenye gari langu na kuzunguka kutafuta wadhamini. Lakini hiki kinachoendelea sasa sina uwezo nacho.
"Kuna watu wenye uwezo mkubwa kifedha ambao wamenifuata na kuniambia wako tayari kunichangia shilingi bilioni nne ili niingie kwenye kinyang'anyiro hicho lakini mimi nimekataa.
"Sijakataa kwa sababu siutaki urais, lakini nimekataa kwa sababu kama ningechukua fedha zao na kuupata urais, maana yake ningekuwa nimeununua kwa fedha na nitauuza pia kwa fedha kupitia hao walionipa," alisema.
Awali, waziri huyo alizungumza na Raia Mwema kwa masharti kwamba mazungumzo yalikuwa ni ya binafsi lakini gazeti hili linaandika kwa sababu taarifa hii ina maslahi ya taifa.
Kumekuwapo na hofu hapa nchini kuhusu matumizi makubwa ya fedha kwenye mchakato wa kuwania urais kupitia CCM, ambapo mmoja wa wanasiasa wakongwe nchini, Hamad Rashid Mohamed, aliwahi kuliambia gazeti hili kuwa wako wagombea ambao watatumia zaidi ya shilingi bilioni 20 kupata wadhifa huo.
Kiasi hicho ni kikubwa na si rahisi kwa mwanasiasa asiye mfanyabiashara kuwa nacho na ndiyo maana kuna hofu kwamba wengi wa wanaowania nafasi hiyo wanafadhiliwa na makundi mbalimbali nje ya siasa yenye maslahi na rasilimali za taifa.
Waziri huyo aliliambia Raia Mwema kwamba watu waliomfuata na kutaka kumpa fedha hizo ni watu anaowafahamu vizuri lakini alikataa kwa sababu za "kiuadilifu tu".
Katika hatua nyingine, mmoja wa wana CCM ambao tayari ametangaza nia ya kuwania urais kupitia chama hicho amekataa mchango wa shilingi bilioni moja kutoka kwa mfanyabiashara maarufu jijini Dar es Salaam.
Mwana CCM huyo ambaye wapo wanaompa nafasi ya kuweza kupitishwa na chama chake kuwa mgombea urais anadaiwa kushtushwa na hatua hiyo ya kutaka kuchangiwa na mfanyabiashara huyo.
"Katika mambo ambayo Rais Jakaya Kikwete amehangaika nayo sana ni jinsi ya kujitofautisha na makundi ya wafanyabiashara ambao kwa kiasi kikubwa walimwezesha kupata urais.
"Kikwete angefanya makubwa kuliko aliyoyafanya kwenye vita dhidi ya ufisadi endapo tu asingekuwa ameingizwa kwenye uhusiano wenye shaka na wafanyabiashara wasio wasafi.
"Sasa huyu bwana (mtangaza nia) ameamua kuwa atajiepusha na makundi hayo ili akiwa rais asijikute kwenye mazingira ambayo Jakaya amekumbana nayo," kilisema mojawapo ya vyanzo vya kuaminika vya gazeti hili.
Hadi juzi Jumatatu, wanachama 35 wa CCM tayari walikuwa wametangaza nia ya kutaka kupitishwa na chama chao kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu baada ya Asharose Migiro kuchukua na wawili, Dk. Mohamed Bilal na Samuel Sitta, walikwishakurejsha fomu zao.
Chanzo:raiamwema