' Waliotumia mihadarati wasibezwe,wasaidiwe'

BabuK

JF-Expert Member
Jul 30, 2008
1,845
329
MKE wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, Mama Awena Sanani, ameitaka jamii ya Wazanzibari kuacha kuwanyooshea vidole vijana waliojiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya na badala yake wawasaidie kurekebisha tabia zao pamoja na kuwapatia mahitaji ya kibinadamu.

Amesema vijana hao wana nafasi kubwa ya kujirekebisha na kuwa raia wema watakaoweza kuisaidia nchi katika kukuza maendeleo.

Mama Awena alisema hayo jana baada ya kutembelea vituo vya kurekebisha tabia kwa vijana walioingia katika matumizi ya dawa za kulevya pamoja na kutoa msaada wa vitu mbalimbali vikiwemo unga wa ngano na mafuta ya kupikia, yenye thamani ya Sh milioni tatu.

"Hawa watoto wetu, tuwe nao kwa kuwapa nasaha na misaada na tuwaingize katika kazi za ujasiriamali ili waondokane na fikra mbaya ambazo husababishwa na kukaa muda mwingi bila ya kazi," alisema Mama Awena.

Alisema vijana wanategemewa katika maendeleo ya taifa, lakini wanapokosa afya njema mchango wao katika uchumi unakua mdogo na kusababisha kuwa mzigo katika jamii. Alisema dawa za kulevya na ulevi kwa ujumla ndiyo mama wa maasi na chanzo kikuu cha kuenea kwa maradhi ya Ukimwi.

"Nimefurahishwa sana na juhudi zinazochukuliwa na Serikali pamoja na ninyi jumuiya zisizokuwa za kiserikali kwa kuanzisha vituo hivi vya kuwasaidia vijana kurekebisha tabia na kuwapa ushauri, hili ni jambo zuri na jamii inapaswa kukuungeni mkono," alisema.

Alionya kuwa jamii isiposhirikiana na Serikali kupiga vita dawa za kulevya, vijana wanaweza kuwa chanzo cha kuvurugika kwa maadili mema ya Wazanzibari na utamaduni wao kutokana na kuibuka kwa vijana wengi wanaojihusisha na dawa hizo.

Katika maelezo yao kwa Mama Awena, maofisa wa Jumuiya ya Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar (ZFD), walisema unyanyapaa kwa vijana walioathirika na matumizi ya dawa hizo ni changamoto kubwa katika kuwarejesha vijana hao kwenye maadili mema.

Akisoma risala ya jumuiya hiyo, Joneid Abdulkadir alisema wamefarijika kwa misaada hiyo iliyotolewa na Mama Awena na kuwahimiza wanajamii kufuata nyayo zake kwa kuwasaidia watu wenye mahitaji maalumu.

SOURCE: HABARILEO..


 
Back
Top Bottom