Elections 2010 Wafungwa watumika kuandaa mkutano wa JK

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,266
33,039




jksiasaaa.jpg
Mgombea Urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete akiwapungia mkono wananchi wa shinyanga waliojitokeza kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika jana kwenye Uwanja wa Kambarage mkoani humo.

Waandishi wetu
HALMASHAURI ya wilaya ya Serengeti mkoani Mara imeingia katika kashfa nzito baada ya kujihusisha na maandalizi ya mkutano wa kampeni za mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete. Halmashauri hiyo ilijihusisha na mkutano huo kwa kuwinda wanyamapori ambao nyama zake zilitumika kama kitoweo cha baadhi ya wageni waliohudhuria mkutano huo, huku mamlaka nyingine zikitumia wafungwa kuandaa eneo hilo la mkutano.

Habari zilizoifikia tovuti hii zimeeleza kuwa halmashauri hiyo iliwinda wanyamapori kwa ajili ya kitoweo cha wana-CCM waliohudhuria mkutano huo wa Septemba 24.

Kitendo hicho kimevifanya vyama vingine vya siasa wilayani humo kutaka halmashauri hiyo igharimie pia kitoweo kwa ajili ya watu wanaohudhuria mikutano ya wagombea wao wengine wa urais wakati watakapokifika wilayani hapo kuendesha mikutano yao ya kampeni.

Halmashauri hiyo imefanya uwindaji huo katika kipindi ambacho mwekezaji wa eneo hilo, Kampuni ya Gurumeti Reserve amelipa Sh200 milioni kuzuia kisheria uwindaji kwenye pori hilo katika msimu unaoanzia Julai hadi Desemba.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, siku moja kabla Kikwete hajafanya mkutano huo, ulibaini kuwa halmashauri hiyo iliamua kufanya uwindaji kwa ajili ya kuwalisha wajumbe na wageni waliohudhuria mkutano huo.

Kwa mujibu wa sheria za uchaguzi, vyombo vya serikali haviruhusiwi kutumika katika kampeni za uchaguzi na kwamba waliotakiwa kugharimia maandalizi ya mkutano huo walikuwa ni CCM.

Uchunguzi umebaini kuwa gari lililotumika kwa uwindaji huo ni aina ya Toyota Landcruiser (pick up) ambalo tumesitiri namba zake za usajili tunazo na ambalo linamilikiwa na halmashauari hiyo.

Majira ya saa 1:00 jioni juzi, gazeti hili lilishuhudia gari hilo la halmashauri likishusha nyama za mnyama aina ya nyamera na pofu katika hoteli ya Giraffe inayomilikiwa na mwenyekiti wa CCM wa wilaya.

Kazi ya kuwinda wanyama hao ilifanywa na askari wa wanyamapori wa halmashauri hiyo, wakitumia bunduki, risasi na gari hilo la umma.

Chanzo cha habari kililidokeza gazeti hili kuwa mbali na kuwinda wanyama hao, viongozi kadhaa wa wilaya hiyo waligawana kitoweo hicho kwa ajili ya matumizi ya familia yao.

Suala hilo limeonekana kuibua mjadala kwa wananchi kwa kuwa baraza la madiwani liliingia mkataba na mwekezaji huyo kuuza mgao wa wanyama kila mwaka ili wananchi wasiwinde kama hitaji la sheria lilivyo.

"Inaonekana wanaozuiwa ni wananchi wa kawaida tu. Lakini sheria gani hii ambayo ina upendeleo wa kuruhusu CCM itumie rasilimali za umma," mmoja wa watu waliozungumza na gazeti hili alihoji.

Katika shughuli hiyo ya mandalizi ya mkutano wa Kikwete, wafungwa wa gereza la mahabusu la Mugumu walifyeka nyasi kwenye uwanja ambao mgombea huyo alifanyia mkutano wake wa kampeni.

Magari mengine ya halmashauri yaliyotumika katika maandalizi ya mkutano wa CCM ni pamoja na lori lililotumiwa kubeba jukwaa kwa kuwatumia wafungwa, tofauti na vyama vingine ambavyo hutumia wanachama wake.

"Hata viti vilivyotumika kwenye mkutano huo wa CCM vilitoka ofisi ya halmashauri hiyo, lakini vyama vingine vikihitaji havipati huduma hiyo. Sasa wamewinda wanyama, kutumia wafungwa kuandaa uwanja na magari ya halmashauri," alilalamika mmoja mmoja wa wakazi wa eneo hilo.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Kimulika Galikunga alikana kuiruhusu CCM kuwinda kwenye pori hilo, akieleza kuwa asingefanya hivyo kwa kuwa taratibu hazimruhusu.

"Mimi sijui hilo limefanyikaje maana uwindaji hauturuhusu. Nashindwa kulisemea suala hilo kwa kuwa hawakupitia kwangu na hata kama wangepita, nisingekubali kwa kuwa hili ni suala la chama," alisema mkurugenzi huyo.
Hata hivyo, mkurugenzi huyo hakusema endapo ana mpango wowote wa kuwachukulia hatua maafisa wa halmashauri hiyo waliotumia rasilimali za umma kwa ajili ya CCM.

Habari zaidi zilieleza kuwa wafungwa hao walifanyishwa kazi hiyo kwa agizo la Mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Edward Ole Lenga.

Lakini alipoulizwa, mkuu huyo wa wilaya alisema hana taarifa kwamba wafungwa walitumika katika maandalizi ya mkutano wa CCM na kwamba akiwa DC, hajawahi kuitisha wafungwa kwa ajili ya mkutano wa chama.

"Nakuhakikishia, mimi sijui sina taarifa hiyo labla wamechanganya na tukio la kulala kwa Mwenge wa Uhuru. Lakini nikiwa DC sijawahi hata siku moja kuomba wafungwa kwa ajili ya chama," alisema.

Mkuu huyo wa wilaya alikiri halmashauri hiyo kuwinda wanyama, lakini akasema walikamata nyamwera wawili tu ambao walikuwa mboga kwa ajili ya wakimbiza mwenge.

"Kwanza hata huyu JK hakula chakula hapa wala kulala. Kama ni wanyama sisi tulikamata wanyama wawili tu kwa ajili ya ugeni wa mwenge na sio Chama cha Mapinduzi," alisema Ole Lenga.

Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Serengeti, Chandi Marwa alikiri na kusema: "Naomba hilo uliache maana litaleta picha mbaya. Liache kama lilivyo."

Kamishna wa uendeshaji wa Magereza nchini, Fidelis Mboya alisema hana habari hiyo, lakini akaweka wazi kwamba wafungwa hawaruhusiwi kutumika kwenye shughuli za kisiasa.

"Si sahihi wafungwa kutumika katika shughuli za kisiasa," alisema Mboya katika mahojiano na Mwananchi jana.
Kutokana na ofisi yake kutokuwa na taarifa hiyo, Mboya aliahidi kwamba atafanyia kazi suala hilo na baadaye ataliweka wazi kwa umma.

Hata hivyo, alisema sheria zinaruhusu wafungwa kufanya shughuli ambazo zimethibitishwa kuwa ni kwa manufaa ya serikali.

Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ameshakemea tabia ya baadhi ya vyama vya siasa kutumia mali na vifaa vya serikali kwenye kampeni akisema kuwa sheria hairuhusu na kuitaka CCM kuondoa baadhi ya mabango ya kumnadi mgombea wake wa urais ambazo zimepigwa Ikulu.

Tendwa matumizi ya picha na vifaa hivyo si sahihi kwa sababu vyama vingine haviwezi kupata nafasi ya kuvitumia.

Chanzo: Wafungwa watumika kuandaa mkutano wa JK
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom