Taarifa kwa Umma
Idadi ya Vijana wanaoajiriwa katika Utumishi wa
Umma yaongezeka.
Rasilimaliwatu yenye sifa ni nguzo muhimu katika
utendaji kazi uliobora na wenye kufikia malengo
katika sehemu yeyote iwe ya huduma au
uzalishaji. Rasilimaliwatu hasa katika utumishi
wa umma hutegemea watumishi wenye sifa,
weledi na viwango vya hali ya juu wenye kukidhi
matarajio ya waajiri na utumishi wa umma kwa
ujumla katika kuleta maendeleo kwa wananchi.
Sekretarieti ya ajira Katika utekelezaji wa
majukumu yake takwimu zinaonyesha kuwa idadi
kubwa ya watumishi wanaoajiriwa katika
Utumishi wa umma ni vijana wenye umri kati ya
miaka 25 hadi 35 hali inayonyesha kuwa vijana
wengi wamekuwa na muamko na hamasa ya
kupenda kufanya kazi katika utumishi wa umma
mara baada ya kuhitimu masomo yao kutoka
vyuo mbalimbali hapa nchini.
Sababu zinazoweza kuelezwa na vijana kupenda
kufanya kazi serikalini ni pamoja na zifuatazo;
i. Uboreshaji wa Mishahara,
ii. Kuboresha mazingira ya kufanyia kazi,
iii. Usalama wa kazi unaotokana na
kuwepo kwa taratibu za kazi zinazotabirika,
iv. Mabadiliko ya mara kwa mara ya
kanuni naTaratibu za kazi yanayofanywa
kukidhi mahitaji ya watumishi kwa wakati
unaohusika na
v. kuwepo kwa taratibu maalum
zinazomhakikishia mwajiriwa maslahi/malipo bora
baada ya kuhitimisha ajira yake.
Maombi ya kazi yaliyopokelewa na waliopangiwa
vituo vya kazi.
Tangu sekretarieti ya Ajira kuanza uendeshaji wa
mchakato wa ajira katika Utumishi wa Umma
mwaka 2010 hadi kufikia Septemba mwaka jana
2014 tumepokea jumla ya maombi ya kazi
191,844 katika matangazo ya kazi
yaliyotangazwa ambapo baada ya uchambuzi wa
maombi hayo waliokuwa na sifa na kuitwa kwa
ajili ya usaili (shortlisted candidates) walikuwa
waombaji 71,124.
Katika maombi hayo yote hadi kufikia Novemba
mwaka jana (2014), jumla ya waombaji kazi
12,858 walipangiwa vituo vya kazi kwa waajiri
mbalimbali katika utumishi wa umma. Waombaji
hawa waliopangiwa vituo vya kazi ni kwa wale tu
waliopangiwa kupitia Sekretarieti ya Ajira, kwa
kuwa wapo watumishi wengine wa kada za afya,
walimu na vyombo vya dola ambao wanaajiriwa
moja kwa moja na mamlaka husika.
Uwiano wa Jinsia na Umri.
Katika idadi hiyo (12,858) ya watumishi
waliopangiwa vituo vya kazi Wanaume walikuwa
7,598 sawa na asilimia 59.1 na Wanawake
walikuwa 5,260 sawa na asilimia 40.9.
Hapa ieleweke kuwa idadi ya wanawake
wanaoajiriwa katika utumishi wa umma imekuwa
ikiongezeka mwaka hadi mwaka, Kwa mfano
mwaka 2010/2011 wanaume wanaoajiriwa kupitia
sekretarieti ya ajira walikuwa ni 72.1% na
wanawake walikuwa 27.9% wakati mwaka
2013/2014 wanaume walikuwa 52.9% na
wanawake walikuwa 47.1%.
Aidha, katika ya waajiriwa 12,858
waliopangiwavituo vya kazi vijana wenye umri
kati ya miaka 21-25 ni 1045 sawa na asilimia
8.1, wenye umri kati ya miaka 26 - 30 ni 6,346
sawa na asilimia 49.4. Kwa msingi huo kati ya
mwaka 2010 hadi 2014 utumishi wa umma
umeingiza 57.5% ya vijana wenye umri wa miaka
21-30.
Hii inaonyesha kuwa utumishi wa umma unaajiri
vijana wengi zaidi wenye mtazamo mpya na
wenye uwezo wa kutumia vifaa vya kisasa katika
utendaji kazi. Aidha kwa umri huo vijana hao
wanao uwezo wa kubadilisha na kubuni mbinu za
kisasa za kufanya kazi na kutoa huduma bora
kwa wananchi kadri muda unavyoenda.
Rai yetu ni kuendelea kuwahimiza vijana wengi
walioko mashuleni kujikita katika fani za masomo
ya Sayansi ambako bado kuna uhitaji mkubwa wa
wataalam katika Nyanja mbalimbali za utumishi
wa umma.
Tunatoa wito kwa wale wote ambao
wameshapangiwa katika utumishi wa umma
kujituma na wawe wabunifu katika sehemu zao
za kazi kwa kuwa taifa letu linategemea sana
vijana kusaidia taifa hili kufikia malengo yake
katika mwaka 2015 na kuendelea.
Mwisho Sekretarieti ya Ajira inapenda kuwataarifu
waombaji kazi waliofanya usaili mwezi Decemba,
2014 kuwa waliofaulu na kupangiwa vituo vya
kazi ambao idadi yao ni 572 tangazo la
kuwapangia vituo vya kazi litatolewa kabla ya
mwezi huu kwisha.
Imetolewa na kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi
wa Umma.