Kutokana na giza nene lililopo la ucheleweshaji wa ajira mpya Serikalini kutokana na kauli mbiu ya watumishi hewa kushika kasi na kutumika na serikali kama ngao ya kuchelewesha au kutotoa ajira mpya serikalini hadi sasa hasa katika sekta za vipaumbele, leo baada ya kutoka mjini Nzega, nimetembelea wilaya ya Igunga.
Safari yangu ilinifikisha katika kijiji cha *Mwamashiga* kilichopo kata ya Mwamashiga katika wilaya hiyo.
Pamoja na mambo mengine nilikuwa nafanya utafiti mdogo juu ya huduma za afya vijijini pamoja na hali ya elimu nchini nikiwa nimechukua wilaya 5, katika mikoa mitatu kwa ufadhili wangu binafsi.
Pamoja na kutembelea zahanati kadhaa na shule kadhaa wilayani Igunga na kubaini mambo kadhaa kutokana na utafiti wangu mahususi, nimegundua kuwa hali ya upungufu wa walimu katika shule za Msingi na Sekondari ni kubwa sana kiasi kwamba watoto wa Masikini wanahudhuria shuleni na kurudi nyumbani bila kufundishwa.
Walimu waliopo ni Wachache kiasi kwamba wanaelemewa na mzigo na kujikuta wakiacha baadhi ya madarasa kutofundishwa kabisa.
Walimu katika shule za sekondari licha ya kuwa wachache pia, tatizo la walimu wa sayansi ni kubwa zaidi kiasi kwamba mwalimu wa sanaa mfano aliyesoma kiswahili na somo la Jiografia, analazimika kufundisha Biolojia au kemia ili walau watoto wapate msimamizi wa somo.
Baadhi ya mikoa, wanafunzi hawajasoma masomo ya sayansi tangu januari kifasaha kutokana na kukosa mtu wa kuwafundisha.
Shule za Msingi hali ni mbaya zaidi, walimu wachache, wanaishi katika mazingira Magumu huku masomo ya kufundisha yakiwa Mengi zaidi. Mfano katika Shule ya Msingi Mwamashiga wilayani Igunga, walimu waliopo kituoni wakifanya kazi kwasasa ni sita tu (06), huku idadi ya wanafunzi shuleni hapo ikiwa ni zaidi ya wanafunzi 500 ikiwa madarasa kuanzia la kwanza mpaka la saba.
Wakati nafika shuleni hapo nilikuta walimu wawili tu (02) huku wanafunzi wakipiga kelele madarasani bila kufundishwa huku wengine wakizagaa nje. Mkuu wa shule alikuwa safarini, mmoja akiwa ameshiriki mazishi ya mwanakijiji, na wengine wawili hawakutajwa waliko na Mwalimu niliyemkuta kituoni.
Kwa hali hii na kwa mfano huu mmoja utaona kuwa watoto wa Masikini wanateseka, hawana walimu, hawana msaada huku walimu wachache wakifanya kazi nzito iliyo nje ya uwezo wao.
Wakati hayo yakitokea, walimu wapo mtaani hawana ajira tangu mwaka jana huku serikali kupitia mawaziri wake wakiahidi kutekeleza ahadi ya kuajiri walimu bila mafanikio. Rais Magufuli naye aliahidi kuanza kuajiri baada ya miezi miwili lakini miezi miwili imepita bila mafanikio.
Rais wetu Mpendwa, waajiri sasa walimu na watumishi wa idara ya afya ili wawasaidie watanzania Wanyonge
Elizabeth Kapwani
Kapwani24@gmail.com