kwamtoro
JF-Expert Member
- Nov 15, 2010
- 4,922
- 3,234
- Kipi kilokukimbiza?, natamani kukijua
mahaba nimetimiza, kadiri nilivyojua
mpenzi umeniponza, moyoni ninaugua
kidonda nakiuguza, sijui lini tapoa.
- Nateseka na giza, mawazo yanisumbua
maswali najiuliza, kipi nilokukosea?
baadae najikaza, kuishukuru kadhia
mola ataniliwaza, naye atanisaidia..
- Mapenzi yalinawiri, raha nikajiskia
leo nini kimejiri?, mbona unanisusia
tuliiweka dhamiri, tutahimili udhia
leo bila tahayuri, mwenzio wanikimbia
- Vingi vimeniponyoka, wala mimi sikujali
wengi wamenitoroka, ikawa kwangu sahali
wewe nikikukumbuka, ninapata idhilali
ahadi uliiweka , leo hii hunijali.?
- usije ukalalama, baadae ukumbuke
nuru yangu umezima, niachie niteseke
rabi tanipa salama, wala nisiadhirike
- Moyo wangu nilikupa, tena nikakuridhia
leo hii wanilipa , unyonge bila hatia
penzi umeshalitupa, kwengine waelekea
mimi waniacha kapa, bila kunihurumia
- Ahsante nashukuru, nami nimeyakubali
madhali sikukudhuru, nenda potelea mbali
mola nitamdhukuru, anipe wangu asali
yaILAHI YA KAHARU, nipe moyo nihimili.
- Nalia ninaumia, leo hii sina hali
wajua nateketea, penzi letu kulijali
mwenzangu wafurahia, umenitwisha jabali
nami nimelipokea, nifanye mie jahili.
- Dunia yazunguka, waswahili wamesema
wewe utanikumbuka, si hiyari ni lazima
kwa wema nilikuweka, kwa maradhi na uzima
leo hii watoweka , kwa mabaya wanisema
- Nenda "usotabirika", iko siku nitapona
kweli nimefadhaika, kwani nilipenda sana
leo umefarijika, mwenzio ninasonona
kuna siku nitacheka, tena sio mbali sana.
- Mola wangu nisitiri, unipe subira njema
unilinde YA QAHARI, unipe kilicho chema
uniepushe athari, ya kupenda aso mwema
uniongoze JALALI , uwe namimi daima.