Ujenzi wa Jengo la Kumbukumbu ya Kawawa: 800 Milioni zadaiwa kutafunwa!

Candid Scope

JF-Expert Member
Nov 8, 2010
11,890
6,898
JINAMIZI la ufisadi limeendelea kuzitesa taasisi za umma na za viongozi wastaafu, ambapo hivi sasa mradi wa ujenzi wa jengo la kumbukumbu la aliyekuwa Waziri Mkuu mstaafu hayati Rashid Mfaume Kawawa ‘Simba wa Vita’, inadaiwa zimetafunwa sh milioni 800 pamoja na vifaa. Fedha na vifaa hivyo vilitokana na harambee iliyoendeshwa mwaka 2008 iliyokuwa na lengo la kukusanya kiasi cha sh bilioni moja ili kujenga jengo la ghorofa tatu katika Kijiji cha Madale, Wilaya ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam.

Tanzania Daima Jumapili limedokezwa kuwa jengo hilo lilitarajiwa kuwa na ofisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM), ofisi za kituo cha kutunzia kumbukumbu za uelimishaji jamii kuhusu ugonjwa wa ukimwi, afya ya kina mama na watoto na kumbi za mikutano. Kwa mujibu wa watu walio karibu na familia ya Kawawa, wamebainisha kuwa iliundwa kamati maalumu kwa ajili ya kuratibu michango hiyo lakini mpaka sasa viongozi wa kamati hiyo wamekuwa wakirushiana mpira kuhusu ubadhirifu wa michango iliyokusanywa.

Diwani wa Kata ya Madale, John Moro, ndiye alikuwa mwenyekiti wa kamati hiyo na anatuhumiwa kuhusika na kashfa hiyo iliyoibuliwa na baadhi ya wananchi waliokuwa wakishangazwa na kusuasua kwa ujenzi husika. Baadhi ya wananchi waliozungumza na Tanzania Daima Jumapili, kwa sharti la kutotaka majina yao yaandikwe, walisema awali wahusika walikwenda kwenye kiwanja kilichotolewa kwa shughuli hiyo na kuchimba mashimo na kuweka saruji pamoja na nondo, ikiwa ni ishara ya ujenzi wa ghorofa. Walidokeza kuwa eneo hilo kwa hivi sasa limegeuka pori kwa kuwa hakuna mwenye kulihudumia tofauti na ilivyokuwa siku za nyuma. Tanzania Daima Jumapili liliwasiliana na Diwani wa Kata ya Madale, John Moro, kumtaka kujibu tuhuma za kutafuna kiasi cha sh milioni 800 pamoja na vifaa vya ujenzi vilivyopatikana kwenye harambee na baada ya harambee.

Moro alikiri kuhusika na uchangishaji wa fedha katika ujenzi huo lakini alikana kutafuna mamilioni ya fedha na vifaa vya ujenzi wa jengo hilo kama baadhi ya watu wanavyomtuhumu. Alibainisha kuwa sababu kubwa ya kukwama kwa ujenzi huo ni mvutano unaoendelea hivi sasa baina ya kamati yake na familia ya Kawawa inayotaka ujenzi huo ufanyike nyumbani kwake na si kwenye eneo lililotengwa. “Msimamo wa familia ndio umetukwamisha, hatuwezi kuhamisha ‘plan’ iliyokuwapo na kwenda kujenga nyumbani kwa marehemu kitega uchumi kama hiki, ni lazima tuangalie eneo sahihi, si vinginevyo,” alisema. Diwani huyo pia alikana kuhusika na uuzaji wa vifaa vya ujenzi yakiwamo matofali 8,000, ambapo alisema aliyekuwa mwenyekiti wa serikali ya mtaa ndiye aliyehusika na uuzwaji huo. “Unajua matofali yalikuwepo lakini aliyekuwa mwenyekiti wangu wa serikali ya mtaa ndiye aliyeuza, mimi sikuwapo wakati biashara husika inafanyika,” alisema Moro.

Tanzania Daima Jumapili lilifanikiwa kuzungumza na mwenyekiti huyo aliyetajwa kuhusika na uuzaji wa vifaa hivyo ambaye alijitambulisha kwa jina moja la Mbelwa, ambaye alisema hahusiki na kashfa hiyo. Mbelwa alimtupia mpira Diwani Moro, kwa madai ndiye anayehusika kuuza tofali, nondo, mifuko ya sarufi pamoja na kutafuna fedha zilizochangwa na wananchi. Alisema Moro aliuza vifaa kwa mkandarasi mmoja aliyekuwa akijenga zahanati iliyopo maeneo ya Madale na fedha zilizopatikana hajazitolea maelezo zilipopelekwa. Alibainisha kuwa tangu ujenzi huo uasisiwe na hayati Kawawa kwa lengo la kuhifadhi kumbukumbu, wengi walifurahia jambo hilo na walitoa michango yao kwa hali na mali. “Kimsingi kitendo cha uuzwaji wa vifaa vya ujenzi na matumizi yasiyojulikana ya fedha zilizochangwa kimetukera wengi wetu, ndugu yetu Moro ameuza vifaa hivyo, asikane tuhuma hizi,” alisema Mbelwa.

Tanzania Daima Jumapili liliwasiliana na familia ya hayati Kawawa, ambapo mmoja wa watoto wake ambaye hakutaka kutajwa jina lake alisema familia yao inatengwa katika maamuzi yakiwamo ya fedha ambazo zilikuwa zimechangwa na vifaa ambavyo wahisani mbalimbali walitoa. Alisema kutengwa huko kulianza baada ya kuonyesha kutoridhishwa na utunzaji wa kumbukumbu wa kile kinachotolewa na wachangiaji wa mradi huo. “Mwenyekiti wa kamati ile ana mambo ya ajabu ajabu sana, kabla ya mzee kufariki dunia alikuwa anaonyesha utu wa kutushirikisha lakini sasa kila akiulizwa juu ya ujenzi, hana majibu yanayoeleweka, zaidi ya kusema utaisha tu,’’ alisema mtoto huyo.

Baadhi ya wananchi waliozungumza na Tanzania Daima Jumapili walibainisha kuwa hivi sasa wanashindwa kuhoji zilipo fedha na vifaa husika kwa sababu ya kuchoshwa na majibu ya diwani huyo pamoja na vitisho vyake. Walibainisha kuwa waliamua kufikisha kilio chao TAKUKURU ili ifanyie uchunguzi sakata hilo, lakini hadi hivi sasa bado hawajaona uwajibishwaji wa wahusika. Tanzania Daima Jumapili lilifika ofisi za TAKUKURU na kuonana na ofisa aliyekataa kuandikwa jina lake kwa madai kuwa si msemaji wa taasisi hiyo, licha ya kukiri kuiona barua ya malalamiko ya wananchi hao. Ofisa huyo alisema anayeshughulikia suala hilo kwa sasa yuko katika likizo ya uzazi na hajui ni nani aliyekabidhiwa jukumu la kuchunguza sakata hilo.

Tanzania Daima
 
Halafu wanacheza ngoma na kufurahisha watu eti wanamuenzi mzee wetu! Ccm imebaki na usanii na unafiki mtupu!
 
Duh kila angle upigaji tu,hamna accountability kwenye hii serikali yetu kabisa! Tuone hili sakata litakapoishia. Ona hata takukuru inaogopa eti
 
No! Hili linatakiwa life na mtu. Ufisadi ni ufisadi na waliohusika waende wakale na kulala bure immediately!
 
Duh kila angle upigaji tu,hamna accountability kwenye hii serikali yetu kabisa! Tuone hili sakata litakapoishia. Ona hata takukuru inaogopa eti

Takukuru inaenda kushika minyoo isiyo na kinga na kuyaacha majoka machatu yaendelee kumeza nchi, hii inatisha jamani
 
Kila kona ufisadi,je tutafika kwa kuishia kupiga kelele bila vitendo?
 
Kila kona ufisadi,je tutafika kwa kuishia kupiga kelele bila vitendo?

Na polisi wanaowalinda maisha yao ni kama ifuatavyo: lwakatare alisema ndani ya ccm kuna makundi matatu; kuna 'ccm tafuta kivuli', 'ccm maslahi' na 'ccm kiherehere'. Alisema miongoni mwa wanaoteseka nchini, ni askari polisi, ambao wengi wao wamekuwa wakiishi katika nyumba za mateso. "kule kwetu kagera askari wamejengewa nyumba, juu bati, pembeni bati. Likija jua mnaokwa kama mikate, ikija baridi utadhani mochwari gani sijui.
sasa haya ni maisha gani?" alihoji lwakatare.
 
kila siku najiuliza hivi taasisi kama pccb na usalama wa taifa kazi yao hasa ni nini? kama hawana manufaa katika maslahi ya taifa kuna haja gani ya kyendelea poteza hela nyingi kwa watu hawa, sikun hizi wao ndio wamekuwa wala rushwa wakuu.
 
kila siku najiuliza hivi taasisi kama pccb na usalama wa taifa kazi yao hasa ni nini? kama hawana manufaa katika maslahi ya taifa kuna haja gani ya kyendelea poteza hela nyingi kwa watu hawa, sikun hizi wao ndio wamekuwa wala rushwa wakuu.

Wapi MWALIMU NYERERE FOUNDATION HOUSE?

mnfhouse.jpg


Wapi Sokoine Foundation?



photo.jpg
 
SAKATA la ufisadi wa sh milioni 800 za ujenzi wa jengo la kumbukumbu ya Waziri Mkuu mstaafu, Hayati Rashid Kawawa, limeingia katika sura mpya baada ya kamanda wa vijana wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Gration Mbelwa, kufichua siri zaidi. Mbelwa amewataka viongozi wa CCM ngazi ya taifa kuingilia kati suala hilo na kujivua gamba kwa kuwaadhibu waliotafuna fedha na kukwamisha ujenzi wa kumbukumbu hiyo muhimu akiwemo Diwani wa Wazo Hill, John Moro.

Akizungumza na Tanzania Daima Dar es Salaam jana kamanda huyo alisema serikali inapaswa kulichukulia kwa uzito suala hilo ambalo limekifedhehesha chama ambacho kiko kwenye zoezi la kujivua gamba. Fedha hizo zilipatikana wakati wa harambee. Alisema mradi huo ulihujumiwa na diwani Moro tangu awamu ya kwanza ya uchangishaji wa fedha; fedha hizo zilitumika kwa ajili ya kampeni za udiwani huku nyingine zikinunulia magari ya biashara.

Alieleza kuwa hata saruji iliyotolewa katika harambee hiyo na kiwanda cha Wazo Hill zaidi ya tani 40 hadi 50 baadhi aliamua kuuza na nyingine akitumia katika ujenzi wa nyumba yake. Alifafanua kuwa jambo la kushangaza bila hata kuwashirikisha wana kamati diwani huyo aliamua kuhamisha vikao vya kamati hiyo kwa makusudi na kuvipeleka katika Hotel za Protea, Ununio Beach na Bagamoyo.
Kamanda huyo alisema kuwa baadhi ya wanakamati saba waliamua kujiengua kutoka katika kamati hiyo baada ya kuwepo dalili za ulaghai. “Diwani Moro aliamua kuhamisha vikao kwa lengo la kutengeneza mtandao wa kuwaibia watu hivyo baadhi ya wanakamati (majina yanahifadhiwa) akiwemo injinia wa mradi huo waliamua kujitoa,” alisema kada huyo. Alisema kuwa baada ya mradi huo kuota mbawa ilifika mahali baadhi ya wanafamilia ya Kawawa walikuwa wakikimbiwa jambo ambalo liliwasikitisha na walishindwa kuchukua hatua kutokana na kuhofia kukiyumbisha chama.
Aliongeza kuwa CCM inapaswa kujisafisha katika hilo kwani ni aibu kwa diwani kufanya kitendo kama hicho huku serikali ikishindwa kumchukulia hatua za kisheria kiongozi huyo.

Aliongeza kuwa suala hilo linafahamika hadi katika ofisi za Taasisi za Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) lakini imeshangazwa kuona limeshindwa kupewa uzito. “Kwa kweli zengwe hilo limeidhalilisha familia ya kiongozi wetu ambayo ni adilifu…huku diwani akiachwa na kuendeleza udhalimu wake,” alisema. Alisema kuwa hata Katibu wa Mkoa wa Dar es Salaam aliongopewa na kutapeliwa pindi alipokwenda kukagua mradi huo na kupelekwa katika eneo ambalo si husika mwaka 2009,” alifafanua.

Mbelwa alisema hatua hiyo inachangiwa kwa kiasi na CCM kutokana na kuwaingiza watu ambao hawana sifa katika masuala ya uongozi ambao wanafikiria jinsi ya kuwaibia wananchi. Alisema gamba hilo linapaswa kuvuliwa kwa haraka kwa kuwa linaweza kukiletea chama hicho kashfa na serikali iliyo madarakani.

Hata hivyo gazeti hili lilipomtafuta diwani Moro alikataa kujibu tuhuma hizo na badala yake alilitishia Tanzania Daima kulifikisha mahakamani. “Sina la kuongea bali nataka kukwambia kuwa nawasiliana na mwanasheria wangu kwa ajili ya kufungua kesi hapo ndipo tutakapojua ukweli ni upi na uwongo uko wapi,” alisema Moro na kukata simu. Juzi iliripotiwa habari kuwa mradi wa ujenzi wa jengo la kumbukumbu ya aliyekuwa Waziri Mkuu mstaafu hayati Rashid Mfaume Kawawa ‘Simba wa Vita’, zinadaiwa kutafunwa kiasi cha sh milioni 800 pamoja na vifaa.

Fedha na vifaa hivyo vilitokana na harambee iliyoendeshwa mwaka 2008 iliyokuwa na lengo la kukusanya kiasi cha sh bilioni moja ili kujenga jengo la ghorofa tatu katika Kijiji cha Madale, Wilaya ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam. Tanzania Daima
 
Hayo magari ya biashara yalinunuliwa kwa ajili ya mtu binafsi au chama? CCM na serikali yake kila kukicha kuna jipya
 
ndio maana Nape kaona ngoma ya 'kujivua gamba' ni sarakasi itamvunja uti wa mgongo na sasa yupo bize na Slaa (PhD) na CDM!!! wenzio waliimba ubeti wa kwanza tu wakaacha yeye akaendelea ubeti wa 2 na wa 3 na wa 4 na wa 5 plus chorus sasa anajuta anabaki kuropoka yasiyo na tija
 
Sasa ajabu iko wapi kwa ccm kufanya jambo kama hili!!!! Milioni 800 tu? We unafikiri hawo unasema wamshuhulikie wahahusiki!! Wao wamo, watamshughulikiaje? Wataanzaje kwanza? We tulia tu, 2015 mtaipata nakwambia! Sasa kama una ushahidi kuwa ametumia saruji kujenga nyumba yake basi hiyo nyumba iwe makumbusho ya huyo bwana, c muitaifishe? Hao takukuru ndiyo wanaongoza kwa rushwa, watamkamata nani, labda uwe umeiba laki 2 ndiyo utafungwa miaka 10.
 
Hivi inakuwaje nchi hii ,viongozi wa serikali na CCM kukosa heshima kabisa na ufinyu wa uzalendo mpaka leo hii Jengo kwa ajili ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere halijasimama na hakuna hata taarifa unamuona Butiku kwenye TV akizungusha zunguhsa ulimi na Viingereza vya Oxford,Mwalimu aliaznisha sera ya ujamaa na Kujitegemea mpka vyuo vikuu sehemu mbalimbali Afrika wakawasomesha watoto wao,leo Nchi wanashindwa hata kuweka kumbukumbu yake
Mzee Mfaume Rashidi Kawawa Mzalendo wa kweli ambaye hakuthubutu kutmia nafasi yake kujitajirisha wala kutajirisha watoto wake,mpiganaji maarufu,mtu safi aliyetumikia nchi hii kwa maisha yake yote,mpigania uhuru huyu pamoja na wenzao hakuna,Jengo linaloweza kuweka kumbukumbu zao hata chama chao cha Magamba hakina hata eneo ambapo wanaweza wakaweka kumbukumbu za hawa wazalendo,Chama cha Magamba hakina aibu kabisa
 
Sasa ajabu iko wapi kwa ccm kufanya jambo kama hili!!!! Milioni 800 tu? We unafikiri hawo unasema wamshuhulikie wahahusiki!! Wao wamo, watamshughulikiaje? Wataanzaje kwanza? We tulia tu, 2015 mtaipata nakwambia! Sasa kama una ushahidi kuwa ametumia saruji kujenga nyumba yake basi hiyo nyumba iwe makumbusho ya huyo bwana, c muitaifishe? Hao takukuru ndiyo wanaongoza kwa rushwa, watamkamata nani, labda uwe umeiba laki 2 ndiyo utafungwa miaka 10.

Umenena iliyo kwali, kwani kila kona wamechafua hakuna kwa kukimbilia
 
Back
Top Bottom