Dar es Salaam. Shirika la Ndege la Precision limezindua safari mpya ya Kahama, hivyo kufanya idadi ya maeneo yanayofikiwa na huduma za shirika hilo kufikia 11.
Leo, Septemba 5 saa 12:00 asubuhi ndege ya shirika hilo aina ya ATR42-500 yenye uwezo wa kubeba abiria 48 iliruka kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam na kutua Kahama saa mbili asubuhi. Ndege hiyo imerudi Dar es Salaam kupitia Tabora.
Miongoni mwa abiria walioondoka Dar es Salaam ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack na Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkurlu.
Baada ya kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kahama uliopo kwenye Mgodi wa Pangea (Buzwagi), Telack amesema kuanzishwa kwa safari hiyo ni matunda ya jitihada za uongozi wa mkoa na Wilaya ya Kahama waliofanya mazungumzo na shirika hilo tangu Desemba mwaka jana.
"Hatua hii itatusaidia wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kufanya safari kwa haraka na rahisi kwa kuwa, awali wilaya kama ya Bukombe walikuwa wanalazimika kwenda Mwanza ili kupata usafiri wa ndege," amesema Telack.
Meneja mratibu wa bidhaa wa Precision Air, Hillary Mremi amesema kuanzishwa kwa safari hiyo ni mwendelezo wa mpango wa shirika hilo katika kuiunganisha Tanzania.
"Kahama ni mji uliochangamka kibiashara, unahitaji usafiri wa ndege. Ukubwa wa soko letu katika sekta ya usafiri wa anga utaongezeka kwa kuwa Kahama imezungukwa na maeneo mengi ambayo bado hayajafikiwa na huduma za usafiri wa ndege," amesema.