Tunatawaliwa na walionunua uongozi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Na Mbasha Asenga
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa mbele​

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, amesema wakati wa watu kutumia fedha kununua uongozi umepita.

Alitoa kauli hiyo kwenye kilele cha maadhimisho ya kitaifa ya miaka 32 ya CCM yaliyofanyika uwanja wa Kambarage, mjini Shinyanga.

Kauli ya rais imeibua hoja nzito. Je, ni viongozi wangapi ndani ya CCM waliopo sasa ambao walitumia fedha kununua uongozi?

Swali hili ni muhimu zaidi hasa tunaposikia kauli ikitoka kwa rais na mwenyekiti wa chama tawala.

Uchaguzi wa CCM ulifanyika Novemba mwaka jana, huku uchaguzi mkuu uliomweka madarakani Kikwete ulifanyika miaka mitatu iliyopita.

Tuelezane vizuri. Manung’uniko na lawama za ununuzi wa kura bado zingali vichwani mwa wengi. Kuna wanaoendelea kudai kuwa hata Kikwete mwenyewe alinunua njia nzima hadi ikulu.


Katika baadhi ya chaguzi ukiwamo uchaguzi wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT), kuna watu walikamatwa wakituhumiwa kutumia rushwa ili kufanikisha njia yao ya kuingia madarakani.

Hata katika jumuiya nyingine kama vile Jumuiya ya Vijana (UVCCM), fedha zilitembea sawasawa. Viongozi wake wanakiri hivyo.

Kwa hiyo, Kikwete anajua haya. Je, huu wito wa Shinyanga ameuelekeza kwa nani? Kwa waliomo kwenye uongozi kwamba wasirudie au kwa wanaotaka kugombea ili wasitumie njia hiyo?


Sasa tuna viongozi kuanzia ngazi ya shina, tawi, kata, wilaya, mkoa hadi taifa. hawa ndio watakuwa mihimili ya kupatikana kwa wagombea uenyekiti wa serikali za mitaa, udiwani, ubunge na hata urais.

Ni hawa waliofika kwenye nafasi zao kwa njia ya fedha. Sasa tuseme nini? Kwamba mwakani watakuwa wamesahau jinsi walivyotumia fedha zao au za kupewa ili kutimiza matakwa fulani baadaye?

Kwa maana hiyo basi, ni kwa jinsi gani hawatashiriki kutuwekea madarakani watu wanaochumia matumbo ili kurejesha fedha walizotumia kwenye uchaguzi?

Katika hali hii, linakuja swali gumu zaidi. Hivi baada ya kauli ya Kikwete, kutakuwa na mkakati wa kuwaengua wagombea katika nafasi mbalimbali kama vile udiwani, ubunge na hata urais?

Hivi CCM haiwezi kufikiria njia ya kuwaondoa viongozi walioingia madarakani hivi sasa ili kusafisha njia?

Watanzania wangependa miaka 32 ya uhai wa CCM taifa liingie kwenye kumbukumbu za kuwa mwisho wa dhuluma na badala yake kukaribisha pambazuko jipya na mwanzo wa uongozi adilifu.

Kwa nini iwe mwisho wa dhuluma? Ni dhahiri kwamba uongozi wa kununua umejaa dhuluma ya moja kwa moja. Na kwa CCM ya sasa, uwezekano wa kujinasua kwenye dhuluma ni mdogo.

CCM imedhulumu taifa kwa kushindwa kutoa uongozi madhubuti, chama hiki kimeweka madarakani baadhi ya viongozi wachumia tumbo.

Viongozi wasiokuwa na hata chembe ya huruma katika chembechembe za damu yao, nasaba zao ni dhuluma.


Dhuluma katika ofisi za umma, dhuluma katika kusimamia rasilimali za nchi, dhuluma hata katika vinywa vyao kwa kushindwa tu kushuhudia ukweli.

Dhuluma inawang’aa machoni; inawasukuma kudhulumu hata fukara midabwada aliyovaa! Hiki ndicho chama kilichoadhimisha miaka 32 ya kuzaliwa kwake huku kiongozi wake akihubiri mwisho wa kununua uongozi.


Tunashukuru mwenyekiti wake amesema hadharani kwamba sasa fedha haiwezi kuendelea kuwa kigezo cha kujipatia uongozi ndani ya chama na kwa maana hiyo kwenye ofisi za umma.

Hata hivyo, hii si mara ya kwanza kwa Kikwete kuzungumzia uongozi na fedha. Katika hotuba yake ya kwanza baada ya kuchaguliwa kuwa rais, 30 Desemba 2005 bungeni mjini Dodoma, alilitaja hilo.

Leo miaka mitatu akiwa madarakani bado anazungumzia matumizi ya makubwa ya fedha katika kusaka uongozi; wakati akisema haya wapo wasaidizi wake wanamwaga fedha ambazo ni muhali kusema ni safi au chafu.

Wapo wanaotumia hadi ofisi za umma kuchota fedha hizo kwa ajili ya kununua uongozi. Hawa ndio wameididimiza CCM katika tope zito, huku baadhi yao wakiwa wasaidizi wake wa karibu. Je, Kikwete yuko tayari kuwaweka kando?


Mwakani chama hiki kitakuwa tena kwenye mtihani wa kujipima, kama kinakubali kwa dhati au ni kwa nguvu ya fedha. Tusubiri kuona ahadi ya Kikwete; fedha zisizo na mipaka ndani ya chama chake sasa basi.
 
Ni lazima Kikwete aseme hivyo na hana au hawezi kukiri kuwa ndani ya Chama chake matumizi ya fedha kununua uongozi yameota mizizi na yanamea na kukua pamoja nakushika kasi na kupata ari mpya kila uchao,ni juzi tu tumesikia mmoja wa wabunge akisema wenzake wanatumia fedha za chama kwa fujo na zaidi wanazitumia kumuangusha na yeye kudai kuwa ana fedha nyingi kuliko chama asije akalaumiwa nae akianza kuusaka na kuulinda ubunge wake wake kwa kutumia fedha na kwa maana hiyo ya kutumia fedha inaonekana wazi kuwa wananchi wa Tanganyika bado wapo nyuma na wanananunulika na wanauza kura zao kwa wenye fedha ,hapa wakulaumiwa sio wanaotumia fedha bali ni wanunuzi wanaolipwa fedha hizo.

Kama wanunuzi ingekuwa wanauza bidhaa hewa kwa maana fedha anayopewa na mnunuzi wa haki yake anaipiga kuni na kura yake anaipeleka anapopaona pana maslahi au kuiepusha kwa mnunuzi basi kwa muda mfupi kusingekuwepo na wanunuzi wa Uongozi.

Wapi CCM wananunua uongozi ,CCM kwa ujumla wananunua uongozi kwa wasimamizi wa uchaguzi,wananunua uongozi kwa polisi kupitia kwa wakuu wa vituo vya polisi ambao ndio wanaowatuma kuruti wao kufanya hujuma za kupenyeza kura za bandia na kuziondoa za uhakika ,pia kuwatisha wapiga kura na kusababisha kutojitokeza siku ya upigaji kura ,hivyo kuwapa mwanya mafisadi kujipangia matokeo, na kujidai wanasimamia uchaguzi na kuulinda CCM wananunua uongozi kupitia tume za uchaguzi hivyo kukamilisha zoezi zima la ununuzi.

Zanzibar CCM wameshindwa kununua uongozi kutoka kwa wananchi kwani hawanunuliki na ukitoa fedha zinaliwa na adabu au adhabu yake hawakupi kura ,hivyo kwa hatua waliyofikia WaZanzibari imewawia vigumu CCM kuwalaghai wananchi inawabidi watumie sehemu ya pili ya kutumia tume na vyombo vya dola ,kinachofanywa na kupiganiwa hivi sasa ni kuvifanya vyombo hivi navyo visikubali kununuliwa ,je wakuu wa tume na wakuu wa polisi wapo tayari kukataa kununuliwa ukiangalia hapa kidogo kuna hitaji mapambano ya nguvu na ndipo nchi inapoweza kuingia katika umwagaji wa damu kama tuonavyo kule Zanzibar kwani wengi wa wakuu wa polisi ni makada wa CCM ambao CCM imefanikiwa kuwachomeka katika utawala wake na ndipo hapo wanapopaita kushika hatamu za nchi ,hivyo unapowagusa katika nyanja hizo huwa wakali na wapo tayari kuuwa na ndipo tulipomsikia Kikwete majuzi akiwatisha wananchi wa Zanzibar na kuwambia wachague wawatakao lakini hawatapewa kuongoza au hawatakabidhiwa madaraka ,huko ni kutangaza vita au mapambano ,Ununuzi wa uongozi upo kwa namna nyingi na Kikwete amejaribu kulificha ili ionekane ni fedha tu zinazotumika lakini bei za kununua uongozi zipo nyingi na moja kuununua uongozi kwa bei itakayouzwa.

CCM inanunua uongozi kwa bei ya hujuma ,kutumia vyombo vya usalama ,kutumia tume ya uchaguzi bei ambayo inahatarisha usalama wa Taifa ,Mheshimiwa Kikwete , itafikia siku Wananchi Hawatokubali MNUNUE uongozi kwa bei hiyo ,itabidi muwaue kama mnavyowaua WaZanzibar ,ili kuutwaa uongozi kwa siku zijazo,ingawa kule Zanzibar huwa mnaua kama mnapiga ndezi na hamna hasara nao ,ni watu ambao hawakuwahusu hivyo hamna hasara nao ila hapa Tanganyika mtakuwa mnauwa ndugu na jamaa zenu ,japo mtatumia polisi wa mkoa mwingine kuhujumu mkoa mwengine ,damu nzito ndugu Kikwete...Kutakuja kufumka risasi ndani ya risasi na hapo patakuwa pachungu sana maana Taifa litakuwa linaingia katika awamu nyengine ya upinzani.
 
Last edited:

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom