BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,792
- 287,994
Na Mbasha Asenga
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa mbele
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa mbele
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, amesema wakati wa watu kutumia fedha kununua uongozi umepita.
Alitoa kauli hiyo kwenye kilele cha maadhimisho ya kitaifa ya miaka 32 ya CCM yaliyofanyika uwanja wa Kambarage, mjini Shinyanga.
Kauli ya rais imeibua hoja nzito. Je, ni viongozi wangapi ndani ya CCM waliopo sasa ambao walitumia fedha kununua uongozi?
Swali hili ni muhimu zaidi hasa tunaposikia kauli ikitoka kwa rais na mwenyekiti wa chama tawala.
Uchaguzi wa CCM ulifanyika Novemba mwaka jana, huku uchaguzi mkuu uliomweka madarakani Kikwete ulifanyika miaka mitatu iliyopita.
Tuelezane vizuri. Manunguniko na lawama za ununuzi wa kura bado zingali vichwani mwa wengi. Kuna wanaoendelea kudai kuwa hata Kikwete mwenyewe alinunua njia nzima hadi ikulu.
Katika baadhi ya chaguzi ukiwamo uchaguzi wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT), kuna watu walikamatwa wakituhumiwa kutumia rushwa ili kufanikisha njia yao ya kuingia madarakani.
Hata katika jumuiya nyingine kama vile Jumuiya ya Vijana (UVCCM), fedha zilitembea sawasawa. Viongozi wake wanakiri hivyo.
Kwa hiyo, Kikwete anajua haya. Je, huu wito wa Shinyanga ameuelekeza kwa nani? Kwa waliomo kwenye uongozi kwamba wasirudie au kwa wanaotaka kugombea ili wasitumie njia hiyo?
Sasa tuna viongozi kuanzia ngazi ya shina, tawi, kata, wilaya, mkoa hadi taifa. hawa ndio watakuwa mihimili ya kupatikana kwa wagombea uenyekiti wa serikali za mitaa, udiwani, ubunge na hata urais.
Ni hawa waliofika kwenye nafasi zao kwa njia ya fedha. Sasa tuseme nini? Kwamba mwakani watakuwa wamesahau jinsi walivyotumia fedha zao au za kupewa ili kutimiza matakwa fulani baadaye?
Kwa maana hiyo basi, ni kwa jinsi gani hawatashiriki kutuwekea madarakani watu wanaochumia matumbo ili kurejesha fedha walizotumia kwenye uchaguzi?
Katika hali hii, linakuja swali gumu zaidi. Hivi baada ya kauli ya Kikwete, kutakuwa na mkakati wa kuwaengua wagombea katika nafasi mbalimbali kama vile udiwani, ubunge na hata urais?
Hivi CCM haiwezi kufikiria njia ya kuwaondoa viongozi walioingia madarakani hivi sasa ili kusafisha njia?
Watanzania wangependa miaka 32 ya uhai wa CCM taifa liingie kwenye kumbukumbu za kuwa mwisho wa dhuluma na badala yake kukaribisha pambazuko jipya na mwanzo wa uongozi adilifu.
Kwa nini iwe mwisho wa dhuluma? Ni dhahiri kwamba uongozi wa kununua umejaa dhuluma ya moja kwa moja. Na kwa CCM ya sasa, uwezekano wa kujinasua kwenye dhuluma ni mdogo.
CCM imedhulumu taifa kwa kushindwa kutoa uongozi madhubuti, chama hiki kimeweka madarakani baadhi ya viongozi wachumia tumbo.
Viongozi wasiokuwa na hata chembe ya huruma katika chembechembe za damu yao, nasaba zao ni dhuluma.
Dhuluma katika ofisi za umma, dhuluma katika kusimamia rasilimali za nchi, dhuluma hata katika vinywa vyao kwa kushindwa tu kushuhudia ukweli.
Dhuluma inawangaa machoni; inawasukuma kudhulumu hata fukara midabwada aliyovaa! Hiki ndicho chama kilichoadhimisha miaka 32 ya kuzaliwa kwake huku kiongozi wake akihubiri mwisho wa kununua uongozi.
Tunashukuru mwenyekiti wake amesema hadharani kwamba sasa fedha haiwezi kuendelea kuwa kigezo cha kujipatia uongozi ndani ya chama na kwa maana hiyo kwenye ofisi za umma.
Hata hivyo, hii si mara ya kwanza kwa Kikwete kuzungumzia uongozi na fedha. Katika hotuba yake ya kwanza baada ya kuchaguliwa kuwa rais, 30 Desemba 2005 bungeni mjini Dodoma, alilitaja hilo.
Leo miaka mitatu akiwa madarakani bado anazungumzia matumizi ya makubwa ya fedha katika kusaka uongozi; wakati akisema haya wapo wasaidizi wake wanamwaga fedha ambazo ni muhali kusema ni safi au chafu.
Wapo wanaotumia hadi ofisi za umma kuchota fedha hizo kwa ajili ya kununua uongozi. Hawa ndio wameididimiza CCM katika tope zito, huku baadhi yao wakiwa wasaidizi wake wa karibu. Je, Kikwete yuko tayari kuwaweka kando?
Mwakani chama hiki kitakuwa tena kwenye mtihani wa kujipima, kama kinakubali kwa dhati au ni kwa nguvu ya fedha. Tusubiri kuona ahadi ya Kikwete; fedha zisizo na mipaka ndani ya chama chake sasa basi.