Septemba 29, 2025 Serikali ya Tanzania, Zambia na China walisaini mkataba wenye thamani ya dola bilioni 1.4 ( Takribani Trilioni 3.4 Tshs) kwa ajili ya ukarabati wa reli ya Tanzania-Zambia (TAZARA), ambayo kwa miongo kadhaa imekuwa uti wa mgongo wa Biashara kati ya Afrika Mashariki na Kusini mwa bara la Afrika.
Akizungumza mara baada ya kusaini mkataba huo, Waziri wa Uchukuzi wa Tanzania, Prof. Makame Mbarawa, aliishukuru Serikali zote tatu kwa mshikamano na dhamira ya dhati ya kuhakikisha TAZARA inarejea katika ubora wake
Prof. Mbarawa pia aliwapongeza Marais watatu: Rais Xi Jinping wa China, Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania na Rais Hakainde Hichilema wa Zambia, kwa mchango wao mkubwa katika kufanikisha hatua hiyo muhimu ya uhai mpya wa Shirika hilo la Reli
Waziri huyo alibainisha kuwa kufufuliwa kwa TAZARA kutakuwa na manufaa makubwa, yakiwemo Kuimarisha usafirishaji wa mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia na nchi nyingine wanachama wa SADC,Kupunguza gharama na muda wa usafirishaji, Kuchochea biashara ya kikanda na kuvutia wawekezaji, Kuongeza ajira na kipato kwa Wananchi, Kuimarisha Uhusiano wa Kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania, Zambia na China
Kwa upande wake, Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Zambia, Mhe. Frank Tayali, alisema mkataba huo umesainiwa kwa wakati muafaka, na mara baada ya maboresho kukamilika, Reli hiyo itaimarika zaidi na kupanua wigo wa usafirishaji wa abiria na mizigo kwa nchi zinazotegemea huduma za treni
Reli ya TAZARA, iliyojengwa miaka ya 1970 kwa ushirikiano wa kihistoria kati ya Tanzania, Zambia na China, imekuwa mhimili muhimu wa uchumi wa kikanda. Kufufuliwa kwake kunatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika kukuza Biashara, Ajira na Maendeleo ya kanda nzima ya Afrika Mashariki na Kusini
Soma pia China kuendesha TAZARA kwa miaka 27, Uwekezaji wa dola bilioni 1.4 kuanza