TAKUKURU Kilimanjaro yabaini ufisadi wa Sh. Bilioni 1.5 katika ujenzi wa Hospitali ya wilaya ya Siha

davimsu

Member
Mar 28, 2019
13
4
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mkoani Kilimanjaro imebaini ufisadi katika ujenzi wa Hospitali ya wilaya ya Siha unaoendelea sasa ambapo ujenzi wake unagharimu shilingi Bilioni 1.5 fedha zilizotolewa na Serikali kuu.

Hayo yalibainishwa jana na Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Kilimanjaro, Holle Makungu alipozungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ambapo alisema kuwa, mradi huo wa ujenzi wa hospitali unagharimu Bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa majengo sita.

Makungu alisema kuwa, katika ufuatiliaji wao ujenzi huo walibaini kuwa nondo na tofali zilizokuwa zimenunuliwa kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo zilikuwa chini ya kiwango na kuelekeza ziondolewe eneo la mradi huku wakita wazabuni kurejesha fedha zilizokuwa zimetumika kununulia vitu hivyo.

“Tumeagiza matofali na nondo zile ziondolewe katika eneo la mradi kutokana na kuwa chini ya kiwango lakini pia kwa kuwa wazabuni walishalipwa fedha za vitu hivyo wazirejeshe mara moja na wasipewe kazi hiyo tena na halmashauri” alisema Makungu.

Mkuu huyo aliendelea kudai kuwa, fedha ambazo zilikuwa zimelipwa kwa wazabuni hao ni 12,037,900/= ambapo kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Halmashuri ya wilaya ya Siha fedha hizo zimekwisharejeshwa na mchakato wa manunuzi ya nondo na tofali zenye ubora unaendelea.

Alisema kuwa, Mhandisi aliyekuwa anasimamia mradi huo wameagiza aondolewe na uchunguzi wa Uhujumu Uchumi dhidi yake na wote waliohusika wakiwemo wazabuni waliowasilisha nondo na tofali zisizo na ubora umeanzishwa na pindi uchunguzi utakapokamilika hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Aidha Makungu alizitaka mamlaka za umma zinazohusika na manunuzi makubwa zikiwemo Halmashauri za majiji, manispaa, wilaya na miji, mamlaka za barabara vijijini na mijini (TARURA), Wakala wa Barabara, Temesa, GPSA na Idara zote za Serikali kutoa taarifa PPRA kuhusu wakandarasi na wazabuni wadanganyifu na wasiotekeleza miradi kwa mujibu wa mikataba ili waweze kuondolewa kwa mujibu wa sheria za manunuzi ya umma.

Katika hatua nyingine Takukuru pia imebaini mapungufu katika ujenzi wa Hospitali ya wilaya ya Rombo unaondelea sasa ambapo gharama ya ujenzi ni Bilioni 1.5 kwa majengo sita fedha ambazo zimetolewa na Serikali.

Alisema kuwa, katika hospitali hiyo ya Rombo wamebaini mapungufu katika ujenzi wa ukuta wa jengo la Dawa na kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kurekebisha mapungufu hayo na kufanya usimamizi wa karibu kupitia mhandisi wa ujenzi mwenye uwezo.
 
Hakuna ajabu hapo,Mchawi utampa vipi mtoto amlee?
 
Back
Top Bottom