Simulizi ya kipelelezi: THE JOURNALIST

Simulizi ya kipelelezi: THE JOURNALIST

FEBIANI BABUYA

JF-Expert Member
Joined
Mar 5, 2022
Posts
2,229
Reaction score
4,345
THE JOURNALIST (TONE LA DAMU)


AMANI KILONZO!!!!!...

Ni jina ambalo lilikuwa alama ya ushindi, lilikuwa ni jina maarufu ambalo kila mwandishi wa habari pamoja na waandishi wote walikuwa wakilichukulia kama jina la mfano.

Jina maarufu kutoka kwa mwanaume aliyetokea kwenye maisha ya kimasikini haswa, familia ambayo haikuwa na uhakika hata wa kula mlo mmoja tu ndiye ambaye alikuwa shujaa wa habari Tanzania. AMAN KILONZO alizaliwa yeye na dada yake tu EPIPHANIA KILONZO.

Mwanaume huyu alikuwa mwandishi wa habari za kiuchunguzi, mzalendo na mtu aliye lipenda mno taifa lake hivyo hakuwa tayari kuvumilia ushenzi na ukatili wa mamlaka jambo ambalo lilipelekea yeye kuripoti na kudai alikuwa na ushahidi wa mauaji ya watu ishirini na sita ambayo yalifanyika ndani ya hifadhi ya taifa ya Mikumi, Morogoro.

Hiyo ilikuwa safari nzuri ya kufa kwake kwa sababu nyuma ya hayo, kulikuwa na Siri nzito ambazo hakupaswa kuwa nazo ila kwa bahati mbaya alizipata. Alishuhudia mdogo wake akiwa mfu, mwanamke asiye na nguo hata moja kwenye mwili wake baada ya kubakwa. Kama kaka aliapa kuwashughulikia wale wote ambao walihusika na ushenzi huo ila kwa bahati mbaya hata yeye baada ya hapo hakuwahi kuonekana tena mpaka ulipo okotwa mwili wake.

Kupotea kwake kulianzisha safari nyingine ya mwandishi WILLIARD NZITU ambaye aliandika kitabu kiitwacho TONE LA DAMU, kitabu hicho baada ya kutoka tu kilipigwa marufuku na serikali na wale wote ambao walikinunua waliuawa lakini kuna mtu mmoja alifanikiwa kubaki na nakala moja akaificha vizuri kwa siri.

Sababu za kufungiwa kitabu hicho ni Williard kuandika siri za mambo ambayo yalifanya role model wake AMAN KILONZO kuweza kuuliwa hivyo hata yeye hakuwa Salama kwa watu hao. Uhatari ambao aliutengeneza ulikuwa mbaya kwake, jina lake lilikuwa zaidi ya kirusi hivyo hata yeye alitakiwa kupotezwa.

Baada ya waandishi hao wawili nguli kupotea, ilipita miaka mitano ndipo akaibuka mwandishi mwingine, bwana huyu alitafutwa na watu wasio julikana ambao walimpatia siri nzito ambazo zingemfanya kuingia kwenye maisha ya hatari tofauti na yale aliyokuwa anayaishi mwanzo. RASHID MAZINDE ndilo lilikuwa jina lake, alikuwa mwanaume mmoja mstaarabu sana, mtu wa MUNGU sana ambaye aliishi akiitegemea Kalamu yake hivyo hakuwa na makuu na mtu.

Lakini habari mbaya ni kwamba bwana huyo alidaiwa kuwa na kurasa ambazo zilitisha kwenye maisha yake. Kurasa za maisha yake ya nyuma alikuwa amezizika na hakuna binadamu ambaye alikuwa hai alikuwa anazijua kwa imani yake yeye. Rashid Mazinde alidaiwa kuhusika kwenye mauaji ya watu zaidi ya mia-tano wakiwemo matajiri wakubwa duniani mia-moja lakini hakuna mtu alikuwa anazijua kurasa hizo.

Sasa hao ambao walimtafuta walizijulia wapi? Hizo siri kwanini walimpa yeye na walitaka azifanyie nini? Zilihusiana vipi na mwandishi wa habari za kiuchunguzi AMAN KILONZO?

Huyu ndiye binadamu ambaye anaenda kutulia muda wetu kuweza kuzigusa hizi kurasa tujue kuna nini ndani yake....

Simulizi hii inaitwa THE JOURNALIST (TONE LA DAMU)....karibu tuone namna hilo Tone La Damu linavyo husiana na huyo mwandishi.

Simulizi hii ina mengi ya kukufunza kwenye maisha unayo ishi hususani kwenye mazingira ya kisiasa hivyo ISOME kwa utulivu uielewe...

Usiishie tu kufurahia mapigano, storyline kali Wala dialogue kali sana bali elewa na content yake utaenjoy zaidi.

NB
Hii ni simulizi ya kubuni tu na kufikirika, haihusiani na mtu yeyote, mamlaka yoyote Wala taasisi yoyote hivyo ISITAFSIRIWE TOFAUTI.

Majina ya mahali na watu yamewekwa ili kutia uhalisia kwa wasomaji wake.

Unaweza kunicheki WhatsApp kwa namba +255621567672

Au kwa email thomasibabuya@gmail.com

Langu jina FEBIANI BABUYA

Wasalaam.
 

Attachments

  • Journalist.jpg
    Journalist.jpg
    443.8 KB · Views: 13
HADITHI: TONE LA DAMU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

UKURASA WA KWANZA
MIMI NI MWANDISHI TU
Radi ilipiga kwa nguvu na kuzalisha mwanga mkali ambao ulimshtua mwanaume mmoja ambaye alikuwa ameketi kwenye kiti nyakati za usiku. Bwana yule alipatwa na mshtuko kwakuwa alikuwa kwenye utulivu mkubwa na akili yake ilikuwa inafanya kazi kwa amani hivyo ule mshtuko uliharibu kwa kiasi fulani ule utulivu wake.
Alisimama na kwenda kuchungulia dirishani ili atambue kama huenda kulikuwa na mvua kali inashuka kwa sababu nyumba ambayo alikuwepo haikuwa ikiingiza sauti kubwa ndani yake. Eneo hilo lilikuwa kimya, nje ni manyunyu tu ambayo yalikuwa yakishuka taratibu bila taabu, ulikuwa ni usiku bora kwa wale watu ambao wanaupenda utulivu mkubwa na kuutafuta usingizi mtamu wa pono.
Kwenye nyumba ambayo yeye alikuwepo palikuwa kimya tena na kiza kinene, ni yeye alikuwa amezima taa zote kwa sababu alihitaji utulivu hivyo akawa anatumia taa ndogo ya sola ambayo ilikuwa inamulika mezani tu ambapo alikuwepo yeye. Madirisha na milango yalifunikwa kwa mapazia mazito hivyo hata mtu wa nje asingeweza kuuona ule mwanga wa ndani, alionekana kuwa na jambo la mhimu ambalo alikuwa analifanya kwa wakati ule.
Wakati ananyanyuka mezani taa aliizima hivyo alikaa dirishani kwa muda wa dakika mbili akiwa anahema taratibu na kuyasikilizia mapigo yake ya moyo mpaka pale ambapo aligundua kwamba kila kitu kilikuwa sawa. Alipafunika kama mwanzo na kurejea kwenye meza yake huku akionekana kutofurahishwa na mshtuko ule wa radi japo alijua hakuwa na jambo la kufanya kuhusu radi ile.
Aliketi tena kwenye kiti na kuiwasha taa yake vizuri mezani. Kwenye ile meza kulikuwa na vitabu vingi, alionekana kabisa kwamba alikuwa ni mtu ambaye alipenda kusoma vitabu kama haikuwa kazi yake kabisa kuweza kuandika baadhi ya hivyo vitabu. Kuna kitabu kimoja kilikuwa mbele yake na bila shaka wakati ile radi inapiga ndicho ambacho alikuwa anakipitia.
TONE LA DAMU ndilo lilikuwa jina la kitabu, ni kitabu kilicho onekana kuweza kumgusa vilivyo ndiyo maana alikuwa anakisoma kwa umakini usiku mzito tena akiwa amejifungia mwenyewe. Ni kitabu ambacho ndani yake kilionekana kuwa na mambo makubwa na mazito kwa sababu mwandishi wa kitabu hicho mpaka wakati huo hakuwa akitambulika kama amekufa au yupo hai kwa sababu ni hicho kitabu ambacho kilimuingiza matatizoni hivyo bwana huyo alikuwa anahitaji kuweza kujua ni mambo gani ambayo mtu huyo aliyaandika kitabuni mpaka yakamuingiza kwenye hatari kubwa ya maisha.
Alikuwa amekata kurasa za kutosha hivyo kwa namna fulani alikuwa ameshaanza kuelewa kwamba ni jambo gani lilikuwa linaendelea. Aliufunua ukurasa mwingine kwa ajili ya kuanza tena kuusoma lakini alishtuka kwa mara nyingine na kukosa utulivu. Awamu ya pili haikuwa sauti ya radi tena bali mlio wa simu yake ndio ambao ulimshtua, ilikuwa ni simu janja ambayo kwa kumbukumbu zake ilikuwa na zaidi ya masaa manne bila kuigusa jambo ambalo lilimfanya aweze kuisahau kabisa kama ipo mezani hapo ambapo alikuwa anasomea.
Aliangalia saa yake mkononi na kugundua kwamba ilikuwa ni saa nane usiku, alishangaa kupigiwa simu majira kama hayo kwa sababu haikuwahi kutokea kwa nyakati kama hizo. Aliinyanyua na kuiangalia ile namba lakini aligundua kwamba ni namba ambayo hakuwahi kuwa nayo na namba ile ilionekana kabisa kwamba inatoka ndani ya taifa la Wazulu huko kwa Mandela yaani Afrika ya Kusini. Alijishauri mara mbili kuweza kutambua kama aliwahi kuwa na marafiki huko lakini jibu lilikuwa hapana, akawaza kama yeye alikuwa ni mtu mhimu kwa watu kiasi kwamba wamtafute usiku kama huo jibu likawa hapana. Sasa alianza kuwaza kwamba ni nani alikuwa anampigia wakati kama huo?
Kusita kwake kulimfanya aamue kutoipokea simu hiyo kwa sababu aliwahi kusikia kuhusu matapeli wa mitandaoni aliona kabisa kwamba wangempotezea muda wake tu na kusingekuwa na la maana lolote hivyo akaipotezea kwa kuikata. Kuikata kwake ikawa safari nyingine ya kuweza kuiruhusu simu hiyo kuanza kuita kwa mara ya pili kwa fujo ile ile, kishingo upande aliamua kuipokea simu hiyo kisha akawa kimya kuweza kumsikiliza mtu wa upande wa pili.
“Nenda Temeke Mwisho nyuma ya stendi ya Mtwara kuna gereji moja pale, ukifika simama kuna mtu anakuja kukupatia ushahidi wa mauaji wa mwandishi wa habari Amani Kilonzo” ilisikika sauti nzito kutoka upande wa pili ambayo ilimshtua kiasi kwamba alitoa simu sikioni kuhakiki tena ile namba maana mhusika alionekana kwamba anamfahamu yeye vizuri.
“Wewe ni nani?”
“Mpaka nakupigia simu ni kwa sababu nakuamini sana hivyo nina uhakika kwamba wewe ni mtu pekee ambaye unaweza kulifanya suala hili likawa wazi. Ni nafasi moja tu kwenye maisha yako kuweza kufanya jambo ambalo ni sahihi kwa sababu kama ukiukosa huu ushahidi hii leo basi hautakuja kuupata tena na huenda mwenye nao anaenda kufa baada ya leo”
“Ushahidi wa nini?”
“Wa kila kitu kilicho tokea. Nakupa nusu saa tu uwe pale vinginevyo nikutakie maisha mema” haikuwa sauti ya kubembeleza kabisa kwa sababu mhusika alionekana kulazimisha jambo hilo kuweza kufanyika. Alibaki akiwa anausikilizia upande wa pili mpaka pale alipo tambua kwamba simu ilikuwa imekatwa akiwa amebaki kwenye mataa.
Alikuwa anawaza kwamba ni nani ambaye alikuwa amempigia yeye kumpatia taarifa hizo, alikuwa na lengo lipi hasa la kuweza kumlenga yeye na kwanini amuamini kiasi hicho? Njia ya kuweza kuujua ukweli ilikuwa ni moja tu pekee, kuweza kukutana na mtu ambaye alidaiwa kuwepo huko Temeke Mwisho majira hayo ya usiku wa manane. Aliwaza kwa muda kidogo akaamua kutokwenda kwa sababu aliamini kwamba huo unaweza kuwa mtego mbaya kwake na ikala kwake, lakini aliwaza mbona hana maadui kiasi kwamba awekewe mtego kama huo? kama mtu huyo angehitaji kumdhuru si angemtafuta kwa namna nyingine? Alihisi kwamba huenda kulikuwa na umuhimu wa yeye kuweza kwenda hilo eneo ajionee yeye mwenyewe.
Alikuwa amefanya maamuzi ya kwenda huko kuweza kuona yale ambayo yalikuwa yanaendelea na hatima ya hayo mambo ingekuwa vipi. Alinyanyuka na kufunika kila kitu akasogea kwenye dirisha moja, pembezoni mwa lile dirisha palikuwa na switch ya taa ya umeme, aliibonyeza kwa muda mrefu mpaka ikatoa mlio kama wa kitu kufunguka, ukuta ulijigawa kiasi akaivuta droo moja nzito kisha akaweka nywila kadhaa na kuvuta bastola ndani ya hilo eneo. Pembezoni palikuwa na kisu kirefu kiasi na kipana, alikiangalia kwa muda kisha akakipakia kiunoni.
Mwanaume huyo alivuta funguo na kutoka nje eneo hilo likiwa kimya bado, aliingia kwenye gereji yake na kufungua ambapo alienda moja kwa moja na kuingia kwenye gari ambayo aliitoa taratibu mpaka nje ya geti. Alihakikisha amefunga geti kwa rimoti na kutoka hilo eneo kwa kasi kubwa kuweza kuwahi Temeke mwisho kwa sababu kuwaza waza kwake kulimlia muda hivyo alitakiwa kuufidia ili asije akampoteza mtu wake ambaye alimpatia nusu saa tu ya kuweza kumuwahi mhusika wake.
Alitumia dakika ishirini kutembea na kasi ya mwewe, ulikuwa usiku na mvua ilikuwa inazidi kushuka hivyo njia hazikuwa na watu kabisa. Eneo lilikuwa tulivu na kimya, ni maeneo kadhaa tu ambayo yalikuwa yanakesha kwa biashara ndiyo alikuwa anaona watu wa kuhesabu, wale ambao starehe kwao walizipa umuhimu kuliko hata maisha ya kuweza kujitafutia ridhiki mtaani. Maisha ya jiji hayakuwa yakimshangaza kuona vitu kama hivyo kwa sababu alikuwa ameyazoea kwa miaka na miaka, dakika ya ishirini ilimkutia akiwa SUDAN.
Alisogea pembezoni mwa barabara njia ya kuelekea Tandika Sokoni akapaki gari pembezoni na kushuka. Mvua bado ilikuwa inateremka kwa wingi ila hakujali, alivaa hood safi kabisa kisha akaanza kutembea kwenye mvua kuelekea stendi. Aliangalia saa yake na kugundua kwamba alikuwa amebakiwa na dakika tano hivyo alikuwa anaenda sawa na muda, eneo hilo ambalo mchana huwa linatawaliwa na wafanya biashara wengi huku maduka ya vifaa vya magari na pikipiki yakiwa yamesheheni na mafundi wa kutosha lakini kwa usiku ilikuwa tofauti kabisa.
Eneo lilipoa, alikuwa anaielewa vizuri mitaa hiyo kwa sababu ilikuwa ikitawaliwa na vibaka wengi ila hawakumpatia homa kwa sababu hakuwa anawahofia. Ni majira hayo ya mvua alitambua kwamba hata wao walikuwa wamejificha ili wasipatwe na hiyo kadhia ya kuanza kuloa bila sababu za msingi kwa sababu tu ya kutaka kukaba watu ambao nao kwa hali kama hiyo usingeweza kuwapata. Alifika mpaka stendi na kuona gari kadhaa tu zikiwa zimepaki, hakuonekana mtu hata mmoja na hata zile ofisi za kukatishia tiketi za magari zilikuwa zimefunga hapo ndipo akakumbuka kuiangalia saa yake tena na kugundua kwamba ilikuwa saa tisa.
Alikunja kulia na kunyoosha mpaka ndani ya gereji moja ambayo haikuwa mbali na hapo na ndiyo gereji ambayo ilikuwa ikitumika kutengenezea magari mengi ambayo yalikuwa yakienda mikoa ya nyanda za juu kusini. Alipofika sehemu ya kuingilia alisimama kwanza, alisimama kwa sababu usalama ulionekana kuwa sifuri kabisa baada ya kuona walinzi wakiwa wamelala. Haukuwa usingizi wa kawaida walionekana kuzimishwa watu hao, aliivuta bastola yake taratibu akiwa anahema kwa utulivu mkubwa ambao haukuwa unaendeshwa na hofu ndani yake.
Alihisi kuna mtu nyuma yake ila wakati anahitaji kufanya maamuzi ya kugeuka alikuwa amechelewa hususani baada ya kuguswa na kitu cha ubaridi kisogoni. Alikuwa kwenye mikono ya mtu mwingine hali ambayo ilimhitaji yeye kuwa mpole kwanza kwani hatima ya maisha yake ilikuwa kwenye mikono ya huyo mtu na alilielewa hilo vizuri kabisa.
“Nipatie bastola yako” ni sauti nzito upande wa pili ilisikika hivyo hakuwa na namna zaidi ya kumpatia kwa nyuma bwana huyo bastola.
“Tembea” alianza kujongea taratibu mpaka wakafika karibu na gari moja bovu ambalo lilionekana kuendelea na matengenezo’’
‘Simama na ugeuke” alipo geuka tu yule mwanaume aliishusha ile bastola, ni mwanaume mmoja ambaye alionekana kuwa na hofu ndani yake, hakuwa na utulivu.
“Tunajuana kabla mimi na wewe?’’

Ndo kwanza tunaufungua ukurasa wa kwanza kabisa wa simulizi hii. Ungani nami mwanzo mpaka mwisho ili uweze kujua hatima ya hawa waandishi na hawa wanadamu ambao wamekutana hili eneo la Temeke.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: TONE LA DAMU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

UKURASA WA PILI

“Sipo hapa ili kuweza kujibu maswali yako”
“Ila?”

“Sina muda mrefu wa kikaa hapa ila kuna mzigo ambao inabidi ubaki nao na hakikisha hakuna mtu hata mmoja anakuja kujua kwamba unao”
“Ndo wewe ambaye tulikuwa tunaongea kwenye simu?”
“Hiyo haijalishi tena”
“Kwanini mimi?”

“Haya tutayaongea muda mwingine ila kwa sasa unatakiwa kuondoka hili eneo haraka sana”

“Ulikuwa unafuatiliwa?”
“Sina uhakika na hilo” mwanaume huyo alimsogelea mwandishi huyo na kumkabidhi frash moja ndogo na bastola yake.

“Tunaweza tusionane baada ya hii leo hivyo hakikisha unayafanyia kazi ambayo yapo ndani ya hiyo frash. Ni watu wengi wameyaweka maisha yao rehani ili tu wewe uweze kuipata hiyo frash kwakuwa wana imani kubwa na wewe, natumai hautawaangusha watu hawa ambao damu zao zimepotea kwa sababu hiyo”

“Kwanini unaniamini na hatufahamiani?” mwanaume huyo alitabasamu na kuanza kuondoka ambapo alidunda kwenye gari moja na kutua juu ya paa la nyumba kisha akaishia upande wa pili. Mwandishi alibaki ameganda pale pale akiwa kama haamini bado, alikuwa anahisi anaangalia ni sinema na maisha yale yangeweza kufika mwisho mpaka alipo tambua kwamba haikuwa sinema ile bali yalikuwa ni maisha ya kweli kabisa ambayo yeye alitakiwa kuweza kuyapitia.

Kuwaza waza kwa muda kulimfanya apoteze sekunde arobaini akiwa haelewi anatakiwa kufanya nini kwa wakati ule, maamuzi yake yalikuwa ni kumfuatilia yule bwana aweze kujua kwamba alikuwa anaenda wapi kwa wakati ule na alikuwa ni nani haswa mpaka kumuamini kumpatia siri ambazo alidai zilikuwa na majibu yote kuhusu vifo vya watu wawili ambao walipotea kwenye mazingira ya kutatanisha. Alitembea kwa kasi na kudunda kwenye tairi ya gari akatua juu ambapo hakusimama akaudaka ukuta na kurukia upande wa pili.

Mwandishi alianza kushangaza kwa uwezo ambao alikuwa nao mwilini mwake, alikuwa ni mtu wa kuishika kalamu na kompyuta mpakato tu muda wote kwa ajili ya kuandika. Alipotua upande wa pili aliona alama za miguu ya mabuti ambayo aliyavaa mwanaume yule zikiwa zinaelekea kwenye uchochoro mmoja ambapo alilazimika kuweza kuzifuata kwa sababu aliamini kwamba ndiko ambako bwana huyo alielekea kwa wakati huo.

Alianza kuufuata akiwa anatembea kwa umakini kwa sababu mitaa haikuwa salama kwa nyakati kama hizo, alisimama baada ya kusikia vishindo vya watu vikiwa vinasogea kila alipokuwa anapiga hatua. Alisimama na kusikiliza vizuri ndipo akagundua kwamba hazikuwa hatua za kutembea bali ni watu walikuwa wanapigana akatambua kwamba huenda yule mtu ambaye alikuwa amekuta naye alikuwa amevamiwa na ndiyo sababu ambayo ilimfanya yeye kumtaka mwandishi huyo kuweza kuondoka haraka hilo eneo kwa sababu alitambua hata yeye anaweza kuuawa na ile kazi kubwa ambayo alidai kwamba watu wengi waliitolea jasho ingeishia njiani.

Alikimbilia lile eneo na wakati anafika pale alimuona yule mtu ambaye alimpatia frash akiwa anazamishiwa kisu kwenye kifua. Mwanaume yule alijibetua na kukita buti zito kwenye shingo ya yule mwanaume ambaye alimzamishia kisu mpaka akayumbia pembeni. Alikivuta kile kisu na kukirushia pembeni ila kilionekana kumuathiri kwa sehemu kubwa kwa sababu damu nyingi ilikuwa inamvuja. Yule mwanaume ambaye aliyumbia pembeni, alijikusanya na kutembea kama umeme kwenye maji akiwa anayapiga kwa nguvu ambapo ni wazi kabisa yalimchanganya mvamiwaji hivyo akawa hamuoni mwanaume yule wakati anakuja.

Alijua habari yake imeisha na alikuwa tayari kwa ajili ya hilo hivyo aliyafumba macho yake mpaka alipo sikia kishindo kikali kwenye ukuta wa pembeni. Alipofumbua alishangaa kumuona yule mwanaume ambaye alikuwa anamjia akiwa ananyanyuka huku anavuja damu na mguu wake umeteguka ndipo akageukia pembeni yake na kushangaa kumuona yule mwandishi akiwa amesimama. Akiwa anaendelea kujiuliza maswali ambayo hakuwa anapata majibu yake kwa wakati ule alisikia sauti ya mwandishi yule;

‘Run’’ alitakiwa kuondoka eneo lile. Alibaki njiapanda kwa sababu yeye alitakiwa kujitoa sadaka ili mwandishi yule awe hai kwa namna yoyote ile lakini kwa wakati ule yeye ndiye alikuwa anaambiwa akimbie tena? Kwake hakuona kama ni jambo ambalo lilikuwa linawezekana, ile frash ilikuwa na mambo mengi mno mhimu na kwa akili yake alijua lazima wale watu wamuue yule mwandishi lakini wakati akiwa amefanya maamuzi ya kutoondoka eneo hilo alisikia sauti kali tena.

‘Ruuuuuuuuun’’ mpaka akawa anaogopa na kuanza kuondoka kwa kukimbia akiwa anachechemea huku ameshikilia mkono mmoja kifuani kwake. Akiwa anaendelea kukimbia, mwanaume mmoja alikuwa anaelekea ule upande wake kwa spidi kubwa kwa sababu hakutaka kumruhusu yeye kuweza kupotea kirahisi namna ile. Bwana yule alisimama ghafla baada ya kisu kukita kwenye kuta ya nyumba akabaki anahema kwa sauti ya juu, kile kisu kama angetembea kidogo mbele kingetoboa uso wake hivyo kilipita kwa sekunde zaidi kikaikosa pua yake. Aligeuka kuangalia ni nani alikuwa amekirusha, alikuwa ni yule mwandishi basi hakuwa na haja ya kumfukuza yule ambaye alikimbia, walitakiwa kumalizana na yule mwandishi ambao wao hawakuwa wanamjua ni nani kwa sababu ya hood ambayo alikuwa ameivaa.

Walikuwa jumla yao wanne, mmoja alikuwa ameteguliwa mguu wake akiwa anavuja damu lakini hakuwa mnyonge. Walionekana kuwa wanaume mithili ya mashine, miili ilishiba vizuri na bila shaka walikuwa ni watu wa kazi kwelikweli. Mwandishi yule mpole na mstaarabu alikuwa amesimama akiwa anawatazama mabeberu wale lakini kuna jambo hakulishtukia, kuna mwanaume alimpiga picha wakati amekirusha kile kisu hivyo uso wake ulionekana.

Mwanaume ambaye alikuwa mbele alitembea kwa nguvu kubwa kwenye maji, alijipinda na kugeuka kwa miguu yote miwili. Aliirusha kwa nguvu na kudunda kisha akabinuka tena baada ya kumkosa mwandishi. Nguvu ambazo alikuwa anazitumia zilikuwa zinatisha mno, buti moja lilitua begani mwandishi akayumbia upande wa pili, alipokuja kukaa sawa aliona ngumi nzito inakuja upande wake ambapo alijizungusha na kuupishanisha mkono wa yule mwanaume.

Aliuvunja ule mkono na kuipasulia shingo yake ukutani tena ghafla. Nguvu ambayo aliitumia kuishika ile shingo na kuibamizia ukutani haikuwa inaendana na mtu ambaye alikuwa anashinda kwenye kalamu kuandika pamoja na kushika kompyuta muda wote. Watu wale walishangazwa na hali ile hivyo wakamuendea wote ambapo alirudi nyuma kidogo na kukivuta kile kisu ukutani.

Walipo mkaribia aligeuka nyuma na kudunda kwenye ukuta ambapo aliruka sarakasi tano za harakaharaka akiwa hewani. Alimdaka mmoja na kumvutia upande wake ambapo alimtoboa toboa shingoni kisha akageuka na kisu kwenye moyo wa mwingine na kukiharibu kifua vibaya. Yule mmoja ambaye alibakia pale ni yule ambaye alikuwa amemtegua mguu wake, alimpiga risasi zote ambazo zilikuwa kwenye bastola habari yake ikaishia pale pale. Wanaume wanne tena ambao walionekana kuwa hatari waliuliwa na mwandishi ndani ya dakika mbili, mwandishi huyo hakusimama hilo eneo alitoweka haraka bila kujua kama sura yake ilipatikana.

Muda ambao aliutumia kuyatekeleza yale mambo, yule mwanaume ambaye alikuwa amemletea frash, alikuwa amejibanza kwenye paa moja la nyumba akiwa kwenye maumivu kuweza kushuhudia jambo lile. Hata yeye mwenyewe alibaki anaogopa, mwandishi alikuwa zaidi ya yale ambayo wao walikuwa wanayajua, alibaki na maswali mengi kuhusu maisha ya mwandishi yule mpole na mstaarabu tena mtu ambaye hakuwa na umaarufu. Yale mambo aliyajulia wapi na mbona kama kuna mengi wao hawakuyajua kutoka kwake? Alibaki amechanganyikiwa lakini hata hivyo haikuwa sehemu salama ya yeye kuendelea kuwepo hivyo aliondoka haraka iwezekanavyo.

Ukurasa wa pili unafika mwisho.

Febiani.
 
HADITHI: TONE LA DAMU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

UKURASA WA TATU
GENERAL KAGIMU
Generali mkuu wa jeshi la Uganda na mkuu wa majeshi wa Taifa hilo bwana jenerali Kagimu, alikuwa ni moja ya watu ambao walikuwa wanaheshimika na kuogopeka mno kwenye taifa la Uganda. Alikuwa ni moja ya sehemu za mhimu mno za raisi wa taifa hilo ambaye kwake taifa lilikuwa kama lake yeye na familia yake.

Generali huyo alikuwa ni mtu mjivuni na mpenda sifa mbele za watu, alikuwa anaogopwa sio kwa sababu ya kupendwa ama kuheshimika bali kwa sababu alikuwa anamuua kila ambaye alionekana kuwa kinyume na matakwa yake yeye. Alikuwa ni sehemu mhimu ya raisi wa taifa hilo kuhakikisha taifa linakuwa salama lakini kwa wakati huo hawakuwa na mazungumzo mazuri kwa sababu kulikuwa na tetesi kwamba bwana huyo alikuwa mbioni kuweza kumpindua raisi ambaye alikuwa madarakani kwa wakati huo.


NAKASONGOLA AIRFORCE BASE
Kwenye moja kati ya base kubwa zaidi za kijeshi ndani ya Uganda za jeshi la Anga ndiko ambako jenerali Kagimu alionekana, alikuwa ameenda huko kwa ajili ya kuwatunuku nishani majenerali wengine ambao walikuwa wamepanda vyeo pamoja na wanajeshi ambao nao walikuwa wamepandishwa vyeo kutokana na kazi zao tukuta ambazo walikuwa wamezifanya ndani ya taifa hilo kiasi kwamba walikuwa wakihitaji heshima ambayo walistahili.

Zoezi hilo lilifanyika kwa masaa matatu mfululizo ndipo alimaliza kazi hiyo na kisha akakagua gwaride la watu hao na vifaa vya anga na alipohakikisha kwamba kila kitu kipo sawa, alijiandaa kwa ajili ya kuondoka lakini kabla ya kuondoka alihitaji kwanza kukutana na kiongozi wa eneo hilo kwa sababu alikuwa na mambo kadhaa ya kuweza kuongea naye tena kwa usiri mkubwa bila mtu mwingine yeyote kuweza kuyasikiliza hayo mazungumzo yao.

Generali Kato, mwanaume ambaye alikuwa na historia ya kutisha huko nyuma akiwa kijana, historia ambayo ilimfanya kukaa kwenye nafasi yake ndiye ambaye alikuwa anaenda kufanya mazungumzo na mkuu wa majeshi wa taifa hilo. Wote wawili walikuwa ni watu wazito ndani ya taifa la Uganda ambapo mmoja alikuwa ni mkuu wa majeshi yote na mwingine alikuwa ni kiongozi wa jeshi la anga la taifa hilo.

“Mheshimiwa kuna uvumi unasambaa kwa sasa, kuna ukweli wowote kuhusu jambo hilo?”
“Kato unanijua vyema kwamba huwa sipendi kabisa kuongea kwa njia za mikato, unaweza ukaniambia kwamba ni jambo gani ambalo unalizungumzia hapa”

“Nasikia kwamba unataka kuwa raisi wa taifa hili!”
“Mhhhhhh Kato, wewe sio mtu wa kuanza kuamini kila habari ambayo unakuwa unaiokota kwenye mitandao”

“Ndiyo maana nipo hapa kukuuliza wewe mheshimiwa kwa sababu sitaki kabisa kuamini habari ambayo nitaipata kwa mtu mwingine yeyote zaidi yako”

“Wewe baada ya kuzisikia habari hizo ulizipokeaje?”
“Sikuzipokea kwa uzuri kwa sababu zinaenda kuleta mgawanyiko mkubwa kati yetu na unalitambua hilo general”

“Haujaibu swali langu”
“Mimi na wewe tumetoka mbali mno, unahisi kwamba naweza kwenda kinyume na wewe?”
“Kwa mtazamo wako unaona kwamba huyu raisi anafaa kuendelea kuwepo Ikulu baada ya kukaa kwa takribani zaidi ya miaka ishirini na mitano sasa?”

“Inawezekana sio sahihi lakini pia sioni kama ni ustaarabu mkuu wa majeshi kuingilia jambo hili kwa sababu linaweza kuja kuleta madhara makubwa na mpasuko kwa taifa jambo ambalo sina imani kama hata wewe unatamani kuweza kuona likiwa linatokea kwenye taifa letu’’

“Do you think i care that much about this country?”
“Why not sir?”
“Nobody cares anyway”
“Are you serious about this sir?”

“Nilikuwa nimepanga kuweza kumuua raisi lakini kwa sasa sioni kama jambo hilo lina umuhimu hivyo zoezi litasimama mpaka kama kutakuwa na ulazima wa kufanya hivyo”

“Ulipanga kumuua raisi wa Uganda”
“Wanauawa maraisi wa Marekani itakuwa Uganda Kato”
“So it’s true about the rumours”
“Yes”

“Hili jambo ambalo unaliwaza halina afya kwa usalama wa taifa hili mheshimiwa”
“Tusipoteze muda na jambo hilo, nilitaka kuzungumza na wewe kuhusu Tanzania”

“Imefanyaje?”
“Kuna taarifa ambazo nimezipata asubuhi ya leo kwamba kuna watu wamekutwa wamekufa tena kwa kuuawa kikatili’’
“Sasa hao watu wanatuhusu nini sisi?”

“Nadhani punguza kulala na wanawake kwa sababu wanakufanya unasahau baadhi ya mambo ya mhimu. Kwamba umesahau kila kitu?”
“Usiniambie kwamba jambo hili linahusiana na yale matukio ambayo yametokea miaka ya huko nyuma!”

“Hiyo ndiyo maana yake”
“Unajaribu kuniambia nini?”
“Kuna mtu mwingine ambaye ameonekana kuingia kwenye hili jambo hivyo kumeanza kuonyesha ishara mbaya”

“Sijakuelewa bado”
“Wewe ni mtu msomi jeneral hivyo kuna wakati unatakiwa kujitahidi kuweza kwenda na alama za nyakati kila unapokuwa unayafanya mambo yako”

“Ni stori ambayo unanielezea kana kwamba mimi ndiye nilikuwepo eneo la tukio vile”
“Kuna mtu mwingine ambaye ameingia kwenye jambo lile hivyo ni wazi kwamba kuna watu walikuwa na zile taarifa jambo ambalo linaweza kuwa na hatari kubwa kwetu”

“Kwahiyo ile kesi imefufuliwa?”
“Sio moja kwa moja ila inawezekana kwamba ikafufuliwa muda wowote ule kuanzia hivi sasa’’
“Lakini walituahidi kwamba jambo lile lingeshughulikiwa vyema”

“Hilo ni kweli lakini wote tunajua hapa duniani siri inapokuwa kwa watu kuanzia wawili basi kamwe haitaweza kuwa siri tena”
“Wamemjua huyo mtu?”

“Hapana, wanadai kwamba walikuwa na wasiwasi juu ya mambo kadhaa na kuhusu watu kadhaa ambao walihisi wanaweza kuwa na hiyo siri jambo ambalo lilipelekea watu hao kuanza kutafutwa na mmoja alikutwa usiku wa manane akionekana kwenye dalili za kuweza kukutana na mtu mmoja. Inadaiwa kwamba haieleweki kama alikutana naye au hawakukutana na baada ya hapo hao watu ambao walitumwa kufuatilia jambo hilo ndio ambao wamekutwa wakiwa wamauliwa”
Ukurasa wa tatu unafika mwisho.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: TONE LA DAMU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

UKURASA WA NNE
“Ni watu wa namna gani walitumwa kuifanya kazi hiyo”
“Wote wanadaiwa kuwa ni watu wenye uwezo mkubwa kwenye mapigano”
“Na wamekutwa wakiwa wamekufa?”

“Ndiyo”
“Kwa maana hiyo mhusika pia ni mtu ambaye hana uwezo wa kawaida?”
“Hilo sio swali Kato”

“Yule mwandishi wa habari alikuwa na umuhimu gani kwa watu mpaka wakati kama huu aweze kuwa gumzo na watu waonekane kutaka kuzifukua zile habari ambazo zilizikwa kwa gharama kubwa?”

“Kwenye kundi la watu wengi, watu hatari zaidi ni wale ambao huwa wanainamisha vichwa vyao. Mara nyingi watu wa nanma hiyo huwa wanajifanya kama vile hawaoni yanayo totea, jambo ambalo huwa linamfanya adui aweze kujisahau na hapo ndipo huwa wanaibuka kutokea maeneo tofauti na kuweza kushambulia. Wale ambao huwa unawaona ni wapiga kelele kwenye mitanao huwa hawana la maana lolote wala sio hatari ndiyo sababu hata serikali yenyewe ya Tanzania iliwapuuza ila kuna watu wanaonekana kwamba walikuwa wanalifuatilia jambo hili kimya kimya na mpaka wameamua kujitokeza maana yake ni kwamba lazima watakuwa na ushahidi wa jambo hili”

“Kama watakuwa na ushahidi hata sisi tutajulikana kuhusu uhusika wetu kwenye hili. Hii haitaleta sura nzuri kwetu kwani kila kitu kinaweza kuwa wazi”

“Ndiyo maana nataka kutuma watu wangu kule kwa siri, hii ni kama tahadhari kwa sababu mhusika ambaye alikuwa anafuatiliwa ni kwamba kuna mtu alikuwa ameenda kukutana naye na kama hilo ni kweli maana yake huenda kuna vitu alitaka kumkabidhi na kama amesha mkabidhi hatupo salama mpaka sasa”

“Mhhhhh sikutegemea kama nitapokea habari mbaya kwenye nyakati kama hizi ambazo niliona kama ni muda wa kula matunda ya muda mrefu. Wamefanikiwa kumjua mtu ambaye bwana huyo alienda kukutana naye?”

“Hapana, hakuna ambalo wanalijua mpaka sasa”
“Huyu mtu ni nani na kwanini aje kwa wakati kama huu?”
“Hilo ndilo jambo ambalo tunatakiwa kulifanya kwa sasa, tusimtegemee mtu mmoja kuifanya kazi hii. Wakati wao wanaendelea kumtafuta mhusika, na sisi tunapaswa kuwa makini na kulifuatilia kwa njia zetu na kama ikishindikana basi tukate mzizi ambao unaweza kuonyesha uhusika wetu kwenye hili jambo wabaki wao kwa wao”

“Unahisi hilo linawezekana?”
“Kama ndiyo itakuwa njia pekee ya kuweza kuwa salama itatakiwa itafutwe njia ya kufanya hilo lakini kwanza kabisa nataka kuwajua hawa watu ni akina nani, wanafanya kazi na nani na wanafanya haya kwa maslahi yapi ili kama ni watu ambao wanaweza kununulika tumalize hii biashara haraka”

“Unataka nifanye jambo gani mheshimiwa?”
“Kwa sasa nahitaji ulifuatilie jambo hili kwa nguvu zako zote, nitakupatia vijana ambao wewe ndiye utawasimamia kwa sababu unaelewa kabisa kwamba sitakiwi kujulikana kwamba naingia kwenye skendo mbayambaya kama hizi hususani kwa nafasi yangu’’

“Wanatakiwa kwenda lini Tanzania kwa ajili ya hii kazi?”
“Leo usiku”
“Vijana wangapi?”
“Kumi”

“Vijana kumi kwa ajili ya kuhangaikia kesi ya mwandishi wa habari tu?”
“Nikiwa na miaka ishirini na tisa nilipo fanikiwa kupanda cheo, mimi na wenzangu tulienda kukamata majambazi maeneo ya Kampala mimi nikiwa ndiye kiongozi wa kikosi. Kwenye eneo lile tulimkuta mtu mmoja tu ambaye alikuwa jambazi hivyo tulijaa kiburi na sifa tukamdharau kwa sababu tuliona kama sisi ni watu ambao tulikuwa na mafunzo hivyo tungeweza kufanya lolote lile ila mpaka wakati huu naongea na wewe hapo kati yetu sisi saba ambaye alifanikiwa kutoka salama lile eneo ni mimi pekee. Wenzangu wote waliuawa usiku ule na mimi nilipona kwa sababu nilikuwa na mbio kali vinginevyo ningekufa siku ile ile. Kama umenielewa basi utajifunza kuheshimu mipango ya watu ambao hauwajui na hujui kwanini wanafanya yale ambayo wanayafanya’’ Generali Kagimu alimaliza mazungumzo yake ambayo kiuhalisia ni kwamba yalikuwa tata, aliondoka na kumuacha generali Kato akiwa kwenye mawazo kwa sababu alidai kwamba hata wao walikuwa wamehusika kwenye jambo ambalo lilionekana kuanza kushika hatamu kwa siri.



VWAWA, SONGWE.
Mtaa wa Mwenge Vwawa Mbozi, moja kati ya sehemu ambazo zinaaminika kwa kuwa na watu wastaarabu ndani ya mkoa wa Songwe ni Vwawa. Ni eneo tulivu ambalo linajumuisha maisha ya watu wa hali ya juu na hali ya kawaida lakini wengi wa eneo hilo ni wale watu ambao wana maisha ya kati, yale maisha ya mtanzania ya kula milo mitatu na kuendelea na maisha mengine ya kawaida.

Eneo hilo linapatikana kwenye moja ya ukanda ambao unasifika kuwa na utajiri mkubwa wa ardhi, ardhi ambayo ni sehemu mhimu kwa ajili ya shughuli za kilimo. Ni eneo ambalo wanapatikana watu wa makabila tofauti tofauti hususani Wanyiha ambao ni wengi zaidi kwa sababu watu wengi ambao wanaishi eneo hilo wametokea vijijini ambako wengi wao wanaiongea hiyo lugha ya Kibantu.

Kwenye hilo eneo la Mwenge, watu walikuwa wanaendelea na shughuli za maisha kama ilivyokuwa kawaida kwa kila mtu kuendelea kuupambania mkate wake wa kila siku. Kuna baadhi ya watu ambao walikuwa wamejipata kwenye maisha yao ama wale watoto ambao walizaliwa kwenye familia zenye uwezo wa juu walikuwa wakiamini kwamba wengine kuishi kwenye maisha magumu ilikuwa ni kwa sababu ya uvivu ama kuwa wazembe jambo ambalo halikuwa la kweli kwa sababu kuna watu walikuwa wapambanaji wakubwa lakini bahati haikuwa upande wao hivyo wakijikuta bado wanaishia kwenye ufukara mkubwa.

“Kijana wangu haya maisha ni zaidi ya zile tamathali za semi, ni rahisi mno kuzisoma zikiwa ubaoni au kitabuni lakini ukija kwenye maisha ya ukweli zile ni ngumu sana kuzifuata na muda mwingine unaweza usizielewe. Zile zinapatikana ndani ya fasihi, wewe ni msomi nina imani unaelewa kwamba hapa nipo nazungumzia kitu gani. Fasihi ni maisha yako na zile tamathali za semi ni jumla ya mambo yote ambayo wewe unakutana nayo kwenye maisha yako ya utafutaji mpaka ile siku ambayo unakuja kufa na kupuzishwa kaburini.

Nimekufahamu kwa muda, wewe ni kijana mmoja mtiifu, mwenye nidhamu kubwa lakini hauna uoga, hali hii itakufanya wewe uweze kufika mbali tofauti kabisa na vijana wengine wa umri wako ambao mpaka sasa hawajui waweze kufanya nini. Unaweza ukajiuliza kwamba ni kwanini leo nimekaa hapa nikiwa nakwambia mambo yote haya ambayo pengine kutokana na umri wako unaweza usione kama ni ya mhimu kuweza kuambiwa lakini niamini mimi kijana wangu, haya yote yatakutokea wewe kwenye maisha yako na ni lazima tu uyapitie.

Mimi nikiwa na miaka ishirini na mitano nilifanikiwa kumpatia mwanamke mmoja mimba lakini kwa sababu ya tamaa za ujana wangu nilimkataa na kumlazimisha aweze kuitoa ile mimba lakini haikuwa hivyo. Mwanamke yule aligoma kabisa kutoa mimba ile na hatimae baadae akaja kufa yeye na mtoto wakati wa kujifungua, kuna watu kwenye huu ulimwengu huwa hawaamini kweye hatima na laana ila hivyo vitu vipo kwa sababu yamenikuta na vyote hivyo mimi navipitia mpaka leo hii. Ile ilikuwa kama ni laana kubwa na mbaya sana kwangu kwa sababu tangu pale mambo yangu yalianza kuyumba, sio kwa upande wa maendeleo tu bali kwenye kutengeneza familia pia kwa sababu baada ya kumkana yule mwanamke sikuwahi kuja kupata tena mtoto.

Nimejaribu kila njia ambayo umewahi kuisikia wewe hapa duniani lakini nimeshindwa, ilifikia hatua nikawa nimeamua kuyabeba tu maisha yangu lakini napo bado ilishindikana mara mbili ambayo nilijaribu kufanya hivyo. Mungu aliamua kuniadhibu nikiwa hai, alitaka mimi niwe shuhuda kwa watu wengine ndiyo maana nakusihi kuhusu maisha mwanangu ili usije kuyarudia makosa ambayo yanafanywa na wanadamu wengi na mwisho wa siku huwa yanaishia kuwa majuto makubwa na wengi hutamani kama wanaweza kurudisha muda nyuma waweza kuyafanya kwa usahihi zaidi lakini hilo halipo kwenye maisha haya.” Alimeza mate mzee huyo akiwa anaukata mhindi wa kuchoma na kumpatia kijana mdogo ambaye alikuwa pembeni akiwa anamsikiliza kwa umakini huku kwa mbali kukiwa na manyunyu ya mvua. Ni kijana wa miaka kumi na saba ndiye alionekana kuwa karibu yake. Alitulia baada ya kuona wote wapo sawa, aliendelea;

Ukurasa wa nne unafika mwisho.

Febiani Babuya
 
HADITHI: TONE LA DAMU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

UKURASA WA TANO
“Zamani wakati sisi tunakua maisha yalikuwa tofauti na sasa, zamani nilikuwa naweza kwenda kwa jirani yangu shambani kwake nikala mpaka nikashiba kisha nikaondoka kwenda nyumbani kwangu ilimradi niwe mstaarabu tu lakini kwa miaka hii hili jambo haliwezekani. Kwa sasa hata ukiiba maji ya kunywa tu nyumba ya jirani hapo lazima watakuua, maji tu unauawa, angalia dunia inako elekea mwanangu. Maisha ya sasa yanamfundisha mwanadamu namna ya kuwa mtu katili kwenye jamii, dunia haitupatii ile haki ya kujua namna ya kuishi kwa usahihi na wadamu bali inakutaka wewe uwe mkatili zaidi kwa wanadamu wenzako ili uweze kuwa juu yao kwa kila kitu.

Hapo baadae kikaingizwa kitu kinaitwa dini, kwa hili huwa nashindwa kuwalaumu hawa mabepari na wageni ambao waliwahi kuingia kwenye ardhi ya Afrika kwa sababu mpaka sasa sijajua dhumuni halisi la ujio wa hizi dini. Kwa akili yangu nilitamani kama dini ingekuwa sehemu ya kutoa tumaini kwa watu, ingekuwa sehemu ya kukumbushana kwamba sisi ni wanadamu tu na maisha yetu yana mwisho hivyo tunapaswa kuishi kwa amani na upendo kwa sababu siku moja hatutakuwa sehemu ya huu ulimwengu. Ajabu siku hizi ni kwamba dini imekuwa sehemu ya kutishia watu, sehemu ya biashara ya ulaghai ambapo watu wameanza kukata tamaa kuhusu uhalali wa Mungu. Kuna watu hawana imani tena kuhusu uwepo wake kwa sababu ya tamaa za watu kadhaa tu ambao wanautumia mlengo wa dini kukamilisha mambo yao na……” mzee huyo alitaka kuendelea lakini alikatishwa, kijana yule alikuwa na swali ambalo lilimkaba kwenye shingo yake na alitamani kuweza kupata majibu yake kwa wakati huo.

“Mzee kwamba dini ni utapeli na sio jambo la kweli kama linavyo hubiriwa?” mzee alitabasamu kidogo lakini halikuwa tabasamu lile la kuonyesha furaha kubwa kwa sababu ndani yake alikuwa na majuto mengi na mambo ya kutisha ambayo yaliwahi kumkuta siku za huko nyuma.

“Haahaha nafurahi kwamba upo makini pia kwenye kumjua Mungu. Ukweli ni kwamba dini sio utapeli na wala haijawahi kuwa utapeli kijana wangu ila matapeli ndio ambao wamevamia dini siku hizi na kuanza kuifanya dini ionekane kama ni utapeli na uhuni jambo ambalo sio kweli. Kuna namna unaweza ukawa na uwalakini kuhusu baadhi ya vitu ambavyo walituletea hawa wenzetu wakati wanakuja kwenye bara letu hili lililo barikiwa lakini sio kuwa na shaka kwamba dini ni utapeli.

Dini ni misingi ya maisha ya watu, dini ni misingi ya imani, dini imekuwepo hata kabla ya hawa watawala kuweza kufika. Dini ilikuwa ni imani ya kuweza kuifikia nguvu kubwa ambayo ni msaada mkubwa kwa maisha ya mwanadamu na mwenye hiyo nguvu ndiye tunamuita Mungu ila walipokuja wageni kidogo namna ya hizo imani ilianza kubadilika. Kwenye imani ambazo wao walizileta ndizo ambazo zimefanya mpaka baadhi ya watu kuwa na wasiwasi na kuhisi kwamba dini ni jambo la kitapeli na ulaghai. Unajua wanadamu tupo tofauti kwenye kuzaliwa, uumbaji na namna watu wanavyo yaishi maisha yao.

Kuna watu ambao wanaishi wakiwa wanazitafuta fursa kila sehemu, kwao kila kitu kinakuja na fursa mpya za maisha hivyo hata kwenye dini watu waliona mlango wa upigaji na ndipo hapo masela wakaanza kuingia kila sehemu kuhakikisha tu kwamba wananufaika na zile hofu za watu kupitia dini. Watu wengi leo hii ukiwajaza hofu kupitia Mungu basi wapo radhi kufanya lolote lile ili kuweza kuiondoa hofu yao na ndipo ulimwengu ulipokea uwepo wa manabii wasio isha kila kukicha mwanangu, utapeli na uwizi kwenye dini ulizaliwa hapo”

“Kwahiyo manabii wote wa siku hizi ni matapeli na wafanya biashara?”
“Nikisema ni wote basi nitakuwa nawakosea wale wote ambao wamekuja kwa nia nzuri na ni kweli ni mitume wa Mungu ila naweza kukuhakikishia kwamba asilimia zaidi ya sabini ni wafanya biashara na wengine ni matapeli. Siku hizi dini inauzwa kijana wangu, ogopa sana mtu anakuuzia neno la Mungu au kukuahidi kukusaidia baada ya wewe kumlipa, neno la Mungu ni la bure, sasa kwanini ulipie? Jitahidi kwenye maisha yako kichwa kisiwe mzigo kwa shingo yako”

“Sawa mzee” alijibu kinyonge huku akianza kuzivuta hatua zake kutaka kuondoka mahali hapo lakini mzee huyo aliyavuta mahindi kadhaa kwenye mfuko na kumpatia.

“Mdogo wako anaendeleaje kwa sasa?”
“Bado hali yake sio nzuri sana mzee”
“Mungu amekupatia mtihani mzito kwenye maisha yako ila hakikisha kwamba unapambana nao na unauvuka. Kwa umri wako huo kupata majukumu mapema namna hiyo ni jambo ambalo litakukomaza haraka lakini utapitia mateso mengi. Fanya kila namna kuhakikisha dada yako anakuwa salama na usiruhusu yeye ndiye aje kusimama kwenye nafasi yako kwa sababu huu ulimwengu hauna huruma kabisa kwa mtoto wa kike ambaye ana maisha magumu.

Usiruhusu mdogo wako kuwa daraja la wanaume ambao wamezoea kuharibu ulimwengu kulipitia, pigana, soma sana na upambanie maisha yako kuhakikisha siku moja mdogo wako anaishi maisha mazuri. Wewe ni mtoto wa kimaskini, familia ambayo umetokea haitakiwi kwa namna yoyote uweze kupoteza lolote na hauna msaada wa mtu hata mmoja hivyo msaada wako mkubwa ni kalamu na daftari lako. Inaweza isikuhakikishie maisha mazuri kwa baadae lakini usiitupe elimu, ifanye elimu kuwa sehemu ya maisha yako, ipambanie elimu tena na tena. Jiamini wewe mwenyewe, amini kwenye kila jambo ambalo unalifanya, usiwaogope wanadamu kwa sababu wengi hawana muda na wewe ila watajaribu tu kukutoa kwenye reli na kwenye msingi wa maisha yeko. Siku moja natamani uje unibebe na gari yako hapa hata kama nitakuwa na miaka tisini mwanangu. Nikutakie usiku mwema, wahi ukamuuguze mdogo wako” yalikuwa maneno ya uchungu na nasaha kubwa za maisha kutoka kwa mzee ambaye alikuwa anauza mahindi barabarani kwenye mitaa hiyo ya Mwenge.

Mzee huyo umri wake ulikuwa umeenda lakini kutokana na ugumu wa maisha ambao alikuwa nao, alilazimika kujitafutia ridhiki zake pembezoni mwa barabara ambapo alitegemea kuishi kwa kuuza mahindi ya shilingi miatano miatano. Kijana ambaye alikuwa anaongea naye alikuwa anaitwa Amani, alikuwa ni kijana mpole mwenye akili, hakuwa kijana yule wa mtaani kama walivyo vijana wengine kwa sababu kubwa mbili. Sababu ya kwanza ilikuwa ni kwamba alikuwa akiijua hasara ya kujichanganya na vijana wa mtaani lakini sababu ya pili ni kwamba alikuwa na jukumu zito mbele yake, jukumu la kumtunza mdogo wake ambaye alikuwa na miaka kumi kwa wakati huo.

Alionekana kuwa kijana ambaye alikuwa sehemu ya maisha yale ya umaskini wa kutupwa, alikuwa mwanafunzi wakati huo wa kidato cha nne ambaye alikuwa akijisomesha kwa shida kubwa. Mzee huyo alionekana kumjua vyema kijana huyo na huenda alikuwa anatamani kuweza kumsaidia lakini hali yake haikumpatia hiyo nafasi ambayo yeye alikuwa anaitamani kuwa nayo. Kijana yule yale maneno yalimfanya aondoke pale huku akiwa anatokwa na machozi, ni mengi ambayo yalionekana kujificha kwenye mtima wake ambayo alihitaji iwe siri yake mwenyewe kwani hakukuwa na umuhimu wa dunia kuweza kutambua na hata kama dunia ingetambua basi haikuwa na jambo lolote la kuweza kumsaidia.

Amani, jina lake lilikuwa tofauti kabisa na uhalisia wa maisha yake, kijana huyo ambaye alikuwa anajishughulisha na shughuli ngumu mtaani ili aweze kuishi na kumlisha mdogo wake ambaye pia alikuwa anasoma hakuwa na tafsiri sahihi ya lile jina lake ambalo alipewa akiwa anazaliwa. Maisha yake yalijaa misukosuko ya kutisha kiasi kwamba alikuwa anatamani kukata tamaa ila uwepo wa mdogo wake ndio ambao kila siku ulimfanya aendelee kuiona sababu ya yeye kuwa hai ila vinginevyo basi asingeona umuhimu wa kuishi kwake.

Alifika kwenye kijumba kimoja kidogo, kijumba ambacho kilionekana kuwa cha zamani na maskani ya watu ambao walikuwa na maisha magumu ila yeye ndipo ambapo alikuwa anapaita nyumbani. Alikuwa anamtazama mdogo wake kwa hasira na uchungu, hakuona kama malaika yule alikuwa anastahili kuweza kuishi maisha ya namna ile, aliona kabisa kwamba mdogo wake alistahili kuishi maisha mazuri na yenye furaha kama ilivyo kwa watoto wengine wa kike lakini kwa bahati mbaya alikuwa amepigwa buti na fuko la hela, ufukara ukawa rafiki kwake.

Kijana yule ambaye uso wake ulikuwa unafifia kwa sababu haukuwa na nuru, uso ambao uliongea mengi kwa hisia kali kiasi kwamba mpaka mdogo wake aliweza kumuona kaka yake na kumuonea huruma kwa hali ambayo alikuwa nayo.

“Kaka usijali mimi nitakuwa salama na nakuahidi siku za hivi karibuni nitanyanyuka tena na kuendelea na masomo yangu. Namshukuru Mungu kunipatia ndugu kama wewe, wewe ndiye kaka bora zaidi kuwahi kuwepo hapa duniani, kama kungekuwa na maisha ya mara ya pili huko ambako huwa inaaminika kwamba tunaenda baada ya kifo basi ningekuchagua uwe kaka yangu kwa mara nyingine tena” alimsogelea mdogo wake na kumkumbatia kwa furaha ile ya kulazimisha lakini ambayo ilikuwa na matumaini ndani yake kwa sababu alikuwa anaona ishara ya ushindi kuungwa mkono na mdogo wake.

Ukurasa wa 5 unafika mwisho.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom