Simulizi ya kifantasia na kijasusi: The darkness of an angel

Simulizi ya kifantasia na kijasusi: The darkness of an angel

FEBIANI BABUYA

JF-Expert Member
Joined
Mar 5, 2022
Posts
2,229
Reaction score
4,345
Kwenye huu ulimwengu wa mabavu kuna mambo mengi yanatokea kiasi kwamba wanadamu tunakimbilia kulaumu bila kujua sababu ya mambo hayo kutokea.

Kwenye IDAIWE MAITI YANGU uliisoma historia na chimbuko la binadamu hatari sana GAVIN LUCA. Bwana huyu historia yake ilianzia huko Tanga ambapo kuna kijana mmoja alishindwa kumuoa mwanamke ambaye alimpenda sana kwa sababu hakuwa na Mali, alikuwa maskini wa kutupwa.

Hilo lilimfanya kufanya maamuzi magumu ya kulikimbilia jiji la Dar es salaam kutafuta maisha. Baada ya kufika huko mambo hayakuwa vile alitarajia ikamlazimu kujiunga na magenge ya uuzaji wa dawa za kulevya.

Kijana huyo akaja kusumbua sana mpaka akafanikiwa kumuua kiongozi wa watu hao kutoka Mexico ambapo akaja kuwa ndiye kiongozi wa mitaa ya PEENUGA STREETS na mwisho wa siku akaja kujenga mji wake wa LUCAS VILLA baada ya kuwa na ukwasi wa kutosha.

Bwana huyo baadae alikuja kumuoa kwa Siri mtoto wa waziri mkuu wa Tanzania na ndipo historia ya GAVIN LUCA ikazaliwa baada ya watu hao wawili kupata watoto mapacha. Bwana huyu alitupatia mambo ya kutisha mno ambapo alikuwa analipa maisha ambayo aliyaishi baba yake tangu siku atoke Tanga kwenda Dar es salaam.

Mambo yalionekana kuisha na GAVIN LUCA akaja kupotea ikidaiwa kwamba amekufa na hapo ndipo tukaipata sehemu ya pili ya IDAIWE MAITI YANGU ambayo inaitwa THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA-LIONELA yaani SAFARI YA GAVIN LUCA. Humu tulimsoma kwa undani LIONELA, mtoto wa damu na wa pekee wa GAVIN LUCA ambaye alianza kutafutwa na watu ambao walikuwa masalia na makosa ya baba yake kuwaacha hai.

LIONELA alipambana na watu hao baada ya kuwa mkatili kupita kiwango cha mwanadamu wa kawaida naye akaamini kwamba alimaliza kazi na ndipo akaamua kuolewa kabisa kwa ajili ya kwenda kuishi maisha ya kawaida na ya amani lakini haikuwa hivyo.

NANI ALIKWAMBIA MWANADAMU WA HIVYO ANAWEZA KUPUMZIKA KIRAHISI? Mwisho wa andiko hilo ilionekana harufu ya usaliti kutoka kwa mwanaume ambaye alimpenda sana kwa maisha yake yote na akampa maisha.

Sasa kulikuwa na sababu zipi za bwana JABARI kufanya hayo mambo? Alikuwa ni nani haswa mpaka amsaliti mwanamke na familia ambayo ilimpa maisha baada ya kukataliwa na kila mtu? JABARI alikuwa na historia ndefu ya maisha yake na aliapa kwamba ni lazima aiteketeze familia hiyo kwa gharama yoyote ambayo ingekuja mbele yake bila kujali kwamba yeye na mwanamke huyo walikuwa na mtoto tayari naye akiwa kama baba wa familia.

Sasa kwenda kuyajua maisha ya JABARI ndipo tunatakiwa kulisoma andiko hili tuweze kuelewa kulikuwa na nini hasa? Walimkosea wapi kwenye maisha ya nyuma! Yeye alikuwa ni nani na kwanini alikuwa anayafanya hayo? .....

LIONELA na familia yake watapona kutafunwa na mtu ambaye ndiye mume wa bosi mwenyewe na anaaminika kuliko watu wengi ndani ya familia? OTHMAN CHUNGA atahusika vipi kuisaidia familia na mtoto ambaye aliachiwa na bosi wake GAVIN LUCA amchunge kwa gharama ya maisha yake?

Ili kupata majibu yote haya ndiyo sababu ya msingi ambayo imenifanyia leo nikuletee andiko hili ambalo ni season 3 na sehemu ya mwisho kabisa ya collection hii...


Simulizi inaitwa THE DARKNESS OF AN ANGEL - SIKU ZA MWISHO waweza kuita GIZA LA MALAIKA.

Waite marafiki, ndugu na wasomaji wote ili tuweze kujua ni MALAIKA yupi huyo ambaye anatuletea hilo Giza?

Nyuma ya kalamu nipo mtaalamu mwenyewe FEBIANI BABUYA ✍️

NIPE MUDA WAKO........ DIVE IN 👇
 

Attachments

  • Darkness-1.jpg
    Darkness-1.jpg
    439.4 KB · Views: 29
Simulizi hii ipo yote mwanzo mpaka mwisho na inapatikana kwa shilingi 5000 tu za kitanzania kwa wale ambao wanataka kuisoma haraka kwa softcopy. Unaweza ukanipata WhatsApp au kawaida kwa namba hizi
+255621567672.

Lakini pia unaweza ukazipata mbili za nyuma yake yaani IDAIWE MAITI YANGU ambayo ni ya kwanza na THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA -LIONELA ambayo ni ya pili ndipo inakuja hii.

Hizi simulizi zote zipo Fasihinet pia. Kwa wale watumiaji wa coins unaweza kwenda kuisoma kule yote kabisa episodes zote 122 bila kelele unafaidi tu.

Nakukumbusha pia kwamba IDAIWE MAITI YANGU na THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA nazo zote zipo full kule Fasihinet hivyo kama ulipitwa unaweza kunicheki WhatsApp ukazipata au kuzisoma kupitia fasihinet.

Hapa chini ni cover zake, nimekuwekea picha ili kama unaenda huko usianze kuhangaika kuzitafuta uangalie tu cover kisha uende nazo taratibu.

Link ya Fasihinet 👇

 

Attachments

  • Screenshot_20250812-080335.png
    Screenshot_20250812-080335.png
    504.5 KB · Views: 32
  • Screenshot_20250812-080433.png
    Screenshot_20250812-080433.png
    326.6 KB · Views: 29
  • Screenshot_20250812-080416.png
    Screenshot_20250812-080416.png
    409.6 KB · Views: 24
Mpangilio wake 👇

1. IDAIWE MAITI YANGU
2. THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA
3. THE DARKNESS OF AN ANGEL -SIKU ZA MWISHO

Kwa softcopy kila moja ni shilingi 5000 za kitanzania kwa ujumla wake zote tatu ni shilingi 15000 tu ambazo unaweza kulipia kwa namba hizi hapa 👇

0621567672 (HALOPESA).... WhatsApp

0745982347 (M-PESA)

0714581046 (TIGO-PESA)

0689440143 (AIRTEL MONEY)

36316279 (LIPA NAMBA (M-PESA) inapokea mitandao yote)

FEBIANI BABUYA
 

Attachments

  • Darkness-1.jpg
    Darkness-1.jpg
    439.4 KB · Views: 32
  • Lionela-4.jpg
    Lionela-4.jpg
    339.8 KB · Views: 29
  • Lionela2.jpg
    Lionela2.jpg
    496.3 KB · Views: 25
  • idaiwe Maiti3.jpg
    idaiwe Maiti3.jpg
    558.3 KB · Views: 25
Leo kwa sababu ndo kwanza tunaanza, naweka episodes 3.

Ungana na mimi haraka usipitwe.

Wasalaam,

FEBIANI BABUYA
 

Attachments

  • Darkness-1.jpg
    Darkness-1.jpg
    439.4 KB · Views: 25
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+


SEHEMU YA KWANZA

*******************
THE DARKNESS OF AN ANGEL
SIKU ZA MWISHO


JAMHURI YA AFRIKA YA KATI
BANGUI

Saa mbili na dakika hamsini na tano za usiku kwa saa za Jamhuri ya Afrika ya kati, kwenye jengo moja refu la ghorofa kumi na tano alionekana mwanaume mmoja. Ni ndani ya mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya kati uitwao Bangui.

Taifa hilo ambalo linapatikana katikati kabisa mwa bara la Afrika lilikumbwa na balaa zito nyakati hizo za usiku wa mapema katikati kabisa ya mji. Kwenye lile jengo la ghorofa ile ndani ya floo ya tisa, mwanaume mmoja alikuwa kwenye haraka kubwa akionekana kwamba alikuwa anawahi mahali. Alikuwa anayabadilisha mavazi yake akiingia kwenye mavazi ya kawaida. Mezani palikuwa na silaya ya masaafa marefu aina ya SVD Dragunov ambazo huwa zinatumiwa na wadunguaji mashuhuri duniani.

Pembezoni mwa hiyo silaha kulikuwa na bastola mbili, kisu kimoja, ramani pamoja na begi la mgongoni. Bwana huyo alikuwa anajitahidi kwenda na muda na wakati ambao haukuwa rafiki kabisa kwake, aliifungua ile silaha haraka haraka kisha akaipulizia spray ikaanza kusinyaa kisha akairushia kwenye kapu la taka. Alibeba passport zake za kusafiria na kuziweka mfukoni, bastola alizipachika kiunoni pamoja na kile kisu, alibeba vitu vyake na kuiweka kofia usoni kiasi kwamba akawa haonekani vizuri.
Alisogea dirishani na kuchungulia nje ambako aliona kuna kashikashi kubwa ikiendelea huku watu wakiwa wanakimbizana kuelekea kila upande kila mtu akionekana kabisa kwamba alikuwa anayapambania maisha yake. Polisi walitapakaa kila sehemu, walikuwa wanabadilishana kupigiana simu kila mahali huku gari za wagonjwa zikiwa za kutosha eneo hilo, halikuonekana kuwa salama kwa nyakati hizo. Bwana huyo baada ya kuridhika na alichokuwa akikiangalia kwa wakati ule, alivuta droo na kubeba pesa zote akazifukia kwenye begi lake na kulirudishia mgongoni mpaka alipo hakikisha kwamba kila kitu kimemridhisha basi akafungua mlango na kutoka nje.

Nje ya floo yake hapo hapakuwa na mtu, palikuwa na utulivu wa kutosha hivyo hakuna mtu hata mmoja ambaye alikuwa anamuona ikawa rahisi kwake kufanya ayatakayo. Alisogea kwenye kifaa cha alarm akakibonyeza, kilipiga kwa sauti kuwapa tahadhari watu kwamba eneo hilo halikuwa salama kwa wakati huo na kama wangeweza basi kila mtu alitakiwa kuyapigania maisha yake. Japo eneo hilo halikuonekana kuwa na watu wengi kwa wakati ule ila waliokuwepo walitoka nje kwa hofu wakitaka kujua ni kitu gani kilikuwa kinaendelea.

“Bomb! Bomb! Bomb!” bwana yule alitamka maneno hayo kwa sauti kubwa kiasi kwamba kila ambaye alikuwa karibu alisikia, kila mtu alianza kuropoka huku watu wakiwa wanakimbia kwenda chini kuyaokoa maisha yako kwakuwa hali haikuonekana kuwa sawa. Hali ile ilifanya msongamano wa kushuka kwenye ngazi wakati watu wakiwa wanajitahidi kuyaokoa maisha yao kuwa mkubwa hivyo naye akajumuika pamoja na watu hao tena akionyesha kuwa na hofu kubwa. Wakati wamefika floor ya kwanza walipishana na polisi wengi wakiwa wanapandisha kwenye hilo eneo ila alijifanya naye ni mhanga kama walivyokuwa wengine. Kuna polisi mmoja wakati anapandisha alimshtukia bwana huyo ikabidi asimame na kugeuka kuweza kumwangalia, alionekana kuwa tofauti kidogo na watu wengine kwani wenzake walionekana kukimbia wakiwa nusu utupu ila yeye alikuwa amejipanga kama mtu ambaye anasafiri. Hakufanikiwa kurudi kwa sababu wenzake walimuita ili wakaone tatizo.

Mwanaume huyo alihema baada ya kufanikiwa kutoka salama eneo hilo ambapo alikatisha kwenye vichochoro kadhaa mpaka alipofanikiwa kufika kwenye barabara kubwa akaita usafiri ambao alihitaji umpeleke moja kwa moja kwenye uwanja wa ndege ambao upo umbali wa kilomita nane tu kutoka ndani ya mji mkuu wa taifa hilo. Zilitumika dakika kumi na tano tu wakawa wamefika kwenye uwanja huo wa ndege wa Bangui M’poko International Airport, alilipa pesa na hakutaka chenji hata pale ambapo dereva huyo wa gari alipo jaribu kumuita, hakuonekana kama ni mtu ambaye alimjali bwana huyo zaidi ya kutokomea ndani ya uwanja huo wa ndege ambao ndio mkubwa zaidi ndani ya Bangui.

Tiketi alikuwa nayo tayari kwenye mkono wake hivyo alipitia kwenye ukaguzi tu ambapo muda mfupi baadae aliingia kwenye usafiri na baada ya dakika kumi na tano ndege ikaanza kukata anga kuiacha ardhi ya Bangui nyuma huku akionekana kuhema na kushukuru kwa kila ambalo lilitokea kue nyuma, silaha zote ambazo alikuwa nazo mwilini alizitelekeza uwanja wa ndege upande wa vyooni ili zisije kutumika kwenye muunganiko wa jambo ambalo bila shaka alikuwa amelifanya usiku huo wa mapema ikamletea shida ya kuweza kutoka ndani ya eneo hilo.


SAA MOJA NYUMA
Katikati kabisa ya mitaa ya Bangui lilitokea jambo la kutisha, jambo ambalo halikuwa la kawaida na wala halikutarajiwa kuweza kutokea. Ndani ya jengo la soko kubwa ambalo ndilo lilikuwa linatumiwa na watu wengi kwa ajili ya shughuli za kila siku za kibiashara, ulitokea mlipuko mkubwa ambao ulilidondosha jengo hilo. Kudondoka tu kwa jengo hilo hakukutosha kuleta simanzi miongoni mwa watu bali jambo ambalo lilitishia amani zaidi ni idadi ya watu ambao walikuwa ndani ya jengo lile.

Kudondoka kwake kulisababisha msiba wa taifa, msiba ambao ulileta simanzi kubwa miongoni mwa watu na wakazi wa Bangui. Jengo lilienda na maisha ya watu mia tatu na hamsini kwa hesabu za haraka haraka lakini wakati huo pia walikuwa wanaendelea na uokoaji na kuendelea kulifukua jengo hilo. Kushuka kwa jengo hilo haikujulikana sababu yake haswa ilikuwa ni nini kwa sababu halikuwa jambo la kawaida lakini dakika kadhaa nyuma kabla ya jengo hilo kushuka, alionekana mwanaume mmoja akiwa ndani yake.

Mwanaume huyo ndiye yule ambaye baadae alionekana kwenye lile ghorofa akiwa na silaha ya udunguaji. Bwana huyo alikuwa na begi dogo tu akiwa anafanya manunuzi ya bidhaa kadhaa ndani ya jengo hilo hivyo hakuna mtu ambaye alikuwa na muda naye. Kila mtu alikuwa anajali kufanya yale ambayo yalimpeleka pale hivyo akaipata nafasi nzuri ya kutimiza lile ambalo alililenga kulifanya. Alishuka mpaka upande wa chini kabisa wa jengo hilo ambako kulikuwa na utulivu, eneo hilo ndilo ambalo lilikuwa na nguzo kubwa ambazo zilikuwa zimelishikilia jengo hilo, alitazama kila upande mpaka pale ambapo alikuwa na uhakika kwamba hakuna mtu hata mmoja ambaye alikuwa anamtazama ndipo akajisogeza kwenye kona moja iliyokuwa na kiza.

Kwenye kona hiyo aliiweka ile begi ambayo alikuwa nayo na kubonyeza rimoti kwenye mkono wake, bila shaka alikuwa amehifadhi bomu ndani ya ile begi yake. Baada ya kuhakikisha kila kitu kinaenda kama ambavyo alikuwa amepanga, hakuhitaji kukaa hilo eneo tena zaidi ya kuondoka haraka kwani alijua jambo ambalo lilikuwa linafuata muda mfupi baadae. Baada ya kutoka kwa dakika kumi mbele alikaa sehemu na kulitazama jengo lile kwa mbali kisha akaitazam rimoti ambayo ilikuwa inasoma sekunde kwa kasi kubwa.
Zilikuwa zimebakia sekunde kumi na tano tu na baada ya kugota kwenye sifuri, ulisikika mlipuko mkubwa ambao ulisambaa kila sehemu na kuzua taharuki. Upande mmoja wa lile jengo ulishuka huku moto ukiwa wa kutosha japo haukudumu kwa kufukiwa na zile kuta nyingi za jengo lile, upande ambao hakukuwa na mlipuko ulianza kutitia taratibu japo watu wengi walifanikiwa kukimbia ambao walikuwa upande ule ila bado kuna ambao walikufa pale pale na majeruhi wengi walipatikana.

Bwana yule alitabasamu akiwa anahakiki saa yake na kutoa bablish kwenye mfuko wake akaanza kutafuna taratibu na kuingia kwenye kona moja. Akiwa anakatiza kwenye hizo kona mbele yake walitokea wanaume wanne na wakati anawasogelea ndipo aligundua kwamba hawakuwa wanaume tu bali walikuwa ni wanajeshi ambao walikuwa ndani ya magwanda yao. Ule mshtuko ambao aliuonyesha kwa kuwaona bila matarajio ndio ambao hata wao uliwashtua, wanaume hao walionekana kabisa kwamba walikuwa wanawahi kutoa msaada kwenye lile jengo kwa sababu walikuwa karibu ndipo wakakutana na mtu ambaye yeye alionekana kutokea kule tena akiwa na furaha kubwa.

Haikuwa kawaida kwa raia wa kawaida nyakati kama hizo kuwa kwenye furaha au kutokuwa na hofu, maana yake alikuwa ni zaidi tu ya raia ndiyo sababu baada ya kumkaribia bwana huyo, walimtaka asimame ili waweze kumalizana naye kwanza kwa kumhoji ama kumkamata ili baadae waweze kumhoji vizuri lakini hata yeye alikuwa nje ya muda kwa sababu kuna kazi ambayo alitakiwa kuifanya muda mfupi ambao ulikuwa unafuata kuanzia wakati huo hivyo watu hao wangempotezea muda na kumuingiza kwenye hatari.
Wanaume hao walimpa ishara ya kusimama hapo alipokuwepo, walimzunguka kila upande huku mmoja akimsogelea ili aweze kumkagua tena kwa sifa ambayo ilijionyesha mbele ya uso wake. Aligusisha mkono wake kiunoni karibu na zilipo sehemu za siri, ule mkono ulidakwa na kuvutwa kwa nguvu, alipigwa ngumi ya kwenye kwapa karibu na bega akatoa ukelele wa maumivu. Ngumi ya pili ilitua kwenye shingo yake ambayo ilipinda akasukumiwa kweye mfereji mdogo wa maji machafu akiwa ni marehemu. Lilikuwa ni suala la sekunde nne tu tukio zima kuweza kukamilika, wenzake walibaki kwenye mshangao wakiwa kama ni watu ambao hawakuwa wakiamini yale ambayo yalitokea pale nyakati kama zile.


Ndo kwanza naufungua ukurasa wa kwanza kabisa wa simulizi hii. Huyu mtu ni nani na anafanya nini ndani ya taifa hilo ambalo anaonekana mgeni nalo na shida nini mpaka anaonekana anakimbia?


Ungana nami mwanzo mpaka mwisho ili tuweze kwenda sawa na simulizi hii mpya.

FEBIANI BABUYA.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA PILI
Aliyekuwa nyuma alijitahidi kwenda baada ya kujitoa kwenye mshangao, kusogea kwake kwa nguvu likawa ni kosa kwake kwa sababu yule mwanaume aligeuka mkono wake ukiwa kiunoni. Alivuta kisu na kukizamisha kwenye moyo wa yule bwana na kukizungusha mara mbili habari yake ikawa imeishia hapo. Alihisi ujio wa mtu nyuma yake, aligeuka na kukutana na ngumi ya uso, yeye alirusha mkono wenye kisu kwenda pembeni kwa yule mwingine ambaye naye alikuwa anashambulia kwa ngumi ili wamuunganishie wote kwa pamoja.

Wakati anapigwa kwenye uso naye kisu kilizama kwenye mkono wa yule mmoja ambaye alikikutanisha na ngumi yake. Zile kelele za miguno zilitulia baada ya kufuatwa kwa kasi na kupigwa ngumi ya kifua, alihema akitaka kurudi nyuma ila alitulia baada ya kisu kuzungushiwa kwenye shingo yake. Alikuwa mmoja ambaye hakuwa bado anaamini yaliyokuwa yanatokea mbele yake, alimkimbilia yule bwana ambaye hakutumia nguvu kubwa zaidi ya kurusha kisu ambacho kilizama kwenye tumbo la yule mwanajeshi kiasi kwamba akakosa hata nguvu ya kuweza kusogea mbele. Alimfuata na kumsogelea yeye mwenyewe kisha akamziba mdomo na kukivuta kila kisu akakita kwenye shingo mpaka alipo hakikisha kwamba amekufa. Hakutaka jambo lile litambulike haraka hivyo ile miili aliisukumizia yote kwenye ule mfereji kisha akaharibu taa zote za umeme ambazo zilikuwa karibu na eneo hilo ambazo zingemfanya mtu yeyote kuiona miili hiyo. Alijifuta vizuri na kutoweka hilo eneo akiwa amekamilisha nusu ya kazi yake na kwa wakati huo ilikuwa imebakia nusu ya kazi ambayo ndiyo ilikuwa mhimu zaidi.

Tukio ambalo lilitokea nyakati zile halikuwa la kawaida kwa nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati, lilikuwa ni tukio baya, gumu na ambalo lilikuwa linaenda kuacha alama mbaya kwenye taifa hilo ndiyo sababu ambayo ilimfanya raisi wa taifa hilo kutangaza safari ya ghafla ya kwenda huko ili akawafariji wananchi wake ambao walikuwa wamemuweka madarakani. Ujio wake eneo hilo ulifanya jitihada za uokoaji kuwa kubwa zaidi na wananchi wake wakaanza kupata matumaini mapya japo hata ulinzi eneo hilo uliongezwa na kuwa mkali.

Raisi baada ya kufika eneo hilo yaliandaliwa mazingira kwa ajili ya yeye kufanyia mkutano wa haraka na vyombo vya habari ili kuweza kutoa angalau neno la pole kwa wananchi wa eneo hilo na taifa lake kwa ujumla. Ilitumika nusu saa helikopita iliyo mbeba raisi kufika eneo hilo na baada ya dakika zingine kumi alikuwa tayari amesimama mbele ya maiki kwa ajili ya kuweza kuongea. Wakati raisi anaanza kuongea mbele ya vyombo vya habari usiku huo huku kazi ya kuwaokoa watu pia ikiwa inaendelea, yule mwanaume ambaye muda mfupi ndiye alionekana kutega bomu hapo alikuwa amefika kwenye jengo ambalo alikuwa amefikia.

Nyakati hizo alikuwa dirishani akiwa anaifunga vizuri silaha yake, ni mtu ambaye alionekana kabisa kwamba alifanya tafiti za kutosha juu ya tukio hilo na kutambua kwamba kama tatizo likitokea basi ni wapi ambapo mtu wake atakuwepo kwa wakati huo. Alimaliza kuifunga vizuri na ndani yake akaweka risasi moja tu huku zingine zikiwa pembeni, hakuwa na shida ya kuweza kutumia risasi nyingi. Alitoa bablishi na kuitupia mdomoni mwake kisha akasogeza jicho lake kwenye silaha akiwa mtulivu, silaha yake ilikuwa inamtafuta raisi alipokuwepo ambapo ni sekunde thelathini tu zilitosha kumfanya raisi huyo kujaa kwenye kioo chake eneo ambalo lilikuwa ni mbali kidogo kutoka eneo la tukio. Alihema kwa nguvu na kufumba jicho moja kisha akafyatua risasi, alipokuja kulifumbua jicho lingine, raisi wa Jamhuri ya Afrika ya kati alikuwa anadondoka chini baada ya risasi kutoboa sikio lake na kuzama ndani ya kichwa.

Ilikuwa ni ghafla, ilizua taharuki kubwa hususani baada ya watu kugundua kwamba ni risasi ilikuwa imemdondosha raisi wao. Hakuna ambaye aliamini tena kwamba eneo hilo lingekuwa salama kwa wakati huo, lilionekana kuwa eneo hatari kwa maisha yao hivyo walianza kukimbia huku na huko kila mtu akihisi kwamba huenda ikafuata zamu yake. Ule mshtuko ulifanya viongozi wa usalama wa raisi pamoja na polisi kuhitaji mhusika apatikane haraka ambapo baada ya kuangalia kwa umakini waligundua kwamba ni wapi ambako risasi ilitokea hivyo mara moja walihitaji askari wazingire jengo lile kuhakikisha mhusika anapatikana huku raisi akiendelea kupata matibabu na kuwahishwa hospitalini kuona kama wangeweza kuokoa maisha yake.

Wakati ambao polisi wengi walikuwa wanalifikia jengo lile ili waweze kumtafuta mtu wao ndio wakati ambao ilisikika alamu ndani ya jengo hilo na kuwafanya watu ambao walitulia nyakati hizo za usiku kuanza kutoka na kukimbia kila sehemu hususani baada ya kusikia kwamba jengo hilo lilikuwa na bomu ndani yake kiasi kwamba nalo lingelipuka na kushuka kama lile la sokoni. Kuchanganyika kwa watu wengi ndiko ambako kulimfanya yule mwanaume kukamilisha kazi yake na kutoroka bila kupatikana. Polisi walianza kujazwa kila sehemu kuhakikisha mhusika haendi mahali, walizuia ndege zisiondoke, hakuna mabasi yaliruhusiwa kutembea ndani ya mji huo. Polisi walizagaa kila kona ila haikuwa kweli kufanikisha jambo lao kwa sababu mhusika hakuwepo tena muda ulikuwa umekwenda mno.


TANZANIA
TANDIKA SOKONI
Eneo hilo huwa lina amsha amsha muda mwingi kwa sababu ya shughuli zake ambazo zinaendelea. Ni eneo ambalo limekaa sehemu nzuri kibishara kwa sababu kuna mzunguko mkubwa wa watu kutoka maeneo mbali mbali hivyo kufanya biashara kuwa nzuri maeneo hayo.

Usiku wa saa tatu palikuwa pamechangamka kama kawaida wakati ambao akina mama ntilie walikuwa wakijitahidi kwenda na kasi ya eneo hilo kuhakikisha kwamba wanatengeneza pesa kwa biashara ya msosi. Wengi hawakuwa na vibanda au fremu kwa sababu zilikuwa ni ghali eneo hilo hali ambayo ilipelekea kuwa na maeneo ya wazi tu ambayo ndiyo yalikuwa yakitumika kufanyia biashara hiyo.

Hali hiyo ilifanya watu kujazana kwenye maeneo ya mama ntilie hao ili kujipatia milo ya jioni kabla ya kuendelea na shughuli zao na wengine wakiwa wanafunga kwa ajili ya kwenda kulala na wengine kustareheka kama ambavyo imezoeleka kwenye jiji kubwa la Dar es salaam. Kwenye viti vya mbao na meza moja ndefu ya mama ntilie mmoja walikuwa wameketi vijana kadhaa wakiwa wanakula huku wanapiga soga kuhusu taifa lao, pembezoni kwa kiti kimoja kirefu kulikuwa na mwanaume ambaye alionekana akiwa amevalia pama kubwa la kahawia kichwani huku mwilini akiwa na mavazi ya suti.

Umri wake ulionekana kabisa kuwa tofauti na vijana wale kwani yeye alikuwa ni mtu mzima kabisa. Hakuwa na maongezi na mtu yeyote yule kwa sababu hakuonekana kuwa sehemu ya utamaduni wa eneo hilo zaidi ya kulizingatia bakuli lake kubwa la supu na chapati tano ambazo alikuwa anaziendea taratibu bila haraka. Alionekana kuvutiwa na mazungumzo ya vijana wale kwa sababu zile habari zilikuwa zimetokea kwenye taifa lao, ni habari ambazo mpaka wakati huo zilikuwa zinayavutia masikio ya wengi kutokana na historia ya taifa ambako lilikuwa limetokaa na chanzo kikubwa zikiwa ni hizo habari ambazo wakati huo walikuwa wanautumia kuzielezea taratibu.

“Mimi naamini kwamba yale mambo yalitokea kwa sababu ya tamaa za wanasiasa, sehemu ambayo siasa inakuwepo kwa kiasi kikubwa na kuna maslahi basi wanasiasa huwa wapo tayari kuvuka ile mipaka ua ubinadamu na kuvaa uhusika wa ngozi za kutisha. Mara nyingi ukiwakuta kwenye hali kama hiyo basi sahau kabisa kuhusu wao kuuzingatia ubinadamu, mara nyingi hapo huwa wanaangalia zaidi kwenye mifuko yao na namna ya kudili na matumbo yao binafsi pamoja na kulimbikiza mali kwa ajili ya watoto wao ambao baadae ndio huwa wanakuja huku uraiani kuweza kututukana sisi kwamba hatufanyi kazi’’ aliongea kijana mmoja ambaye alivuta hisia za vijana wenzake ambao walikuwa pale kwa sababu ni yeye ambaye alionekana kuwa na akili nyingi na weledi kwenye kuelezea mambo yale.

“Unamaanisha kitu gani moja kwa moja ndugu yangu? Wote tunajua hapa kwamba wewe ndiye mwenye akili kutuzidi sisi sote hivyo ukiongea kwa falsafa namna hiyo unaanza kututesa sisi vichwa maji’’ alilalama kijana mwingine ambaye yale maelezo bila shaka yalimtupia habarini.

“Wote si mnakumbuka yale ambayo yalitokea miaka mitatu ambayo imepita?”
“Hilo sio swali la kuuliza, ni mambo ambayo kila mtanzania anayajua kwa maisha yake yote’’

“Una uhakika kila mtanzania anayajua kiundani’’
“Ndiyo kwa sababu hizo simulizi zilitapakaa kila sehemu, ndani na nje ziliongelewa kwa ukubwa, sasa unahisi ni mtu gani mjinga ambaye atakuwa hajazisikia habari maarufu ambazo zitaishi miaka na miaka?”

“Kuna utofauti wa kusikia na kujua kitu kiundani, kusikia ni kwamba unaweza ukapokea lolote ambalo masikio yako yataruhusu wewe ulipokee ndiyo maana kwenye maisha yako unashauriwa kusikiliza zaidi kuliko kusikia lakini kuelewa kiundani maana yake ujue taarifa zilizo nyuma ya hayo mambo na kuzijua taarifa kama hizo ndipo unaweza kuwa na muunganiko wa yale ambayo kweli yalitokea. Usipende kuamini maneno ya wanasiasa, wale huwa wanaongea lolote ili wakufurahishe kwa muda fulani waje kubeba kura yako na baada ya hapo wanakutupa kama hawakujui”

“Kwahiyo unamaanisha kwamba wanasiasa wote ni matapeli tu’’
“Sina maana hiyo lakini jambo la msingi ambalo unatakiwa kulizingatia kwenye maisha yako ni kwamba kumuamini mwanasiasa ni kuamua kujichosha na kupoteza muda wako kwa sababu they are all liars
(wote ni waongo)’’

Unahisi kijana huyu ana yapi ya kutueleza kiundani kuhusu hiyo miaka mitatu ambayo ilikuwa imepita? Sehemu ya pili inafika mwisho, tukutane ndani ya sehemu ya tatu kuweza kujua yale ambayo yalitokea kwenye hizo nyakati.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA TATU

“Mhhh kwenye lugha hapo ndo unaanza kuharibu sasa, turudishe kwenye mjadala wa kwanza tujue ni jambo gani ambalo ulihitaji kulimaanisha na sisi tupate kulielewa kiundani kama wewe’’ kijana mmoja ambaye alionekana kuwa na hamu kubwa ya simulizi ya stori hizo hakutaka maada ihame, alikuwa anataka naye apate mambo kadhaa ya kwenda kutambia mtaani kwake ili wajue kwamba alikuwa na za ndani kuliko wenzake.

“Una haraka sana ndugu yangu ila binafsi huwa naamini kwamba kama zisingekuwa tamaa za wanasiasa basi yale mauaji yasingetokea, ile familia ya Gavin Luca isingeweza kuacha maafa makubwa namna ile. Mimi nilifanikiwa kukisoma kile kitabu kwa rafiki yangu mmoja mtoto wa tajiri ambaye aliweza kukinunua niseme tu kwamba kuna mambo ya kutisha ambayo hii dunia haiyajui na siku ambayo ulimwengu unafanikiwa kuyajua mambo hayo basi nafasi ya wanadamu kuendelea kuishi inakuwa ni ndogo mno” jambo ambalo aliliongea lilionekana kuwa la mhimu kwa wenzake kiasi kwamba wote waliacha kula na kumzingatia yeye, lakini haikuwa hao tu bali hata kwa watu wengine ambao walikuwa pembeni walianza kusogea na kujazana eneo hilo ili kuipata hiyo simulizi ambayo kila mwanadamu wa Tanzania alikuwa akiihusudu na kuipenda lakini ni watu wa kuhesabika walibahatika kuzipata taarifa zote za watu hao.

“Ina maana kwamba muda wote una simulizi ya hawa watu ambayo sisi hatukuipata na umetukaushia kaka? Aaaaah! Sio kweli bwana’’ alilalama kijana mwingine huku akiwa anavua shati yake na ndani akibakiwa na vest nyeupe ambayo mbele yake ilibandkwa picha ya Gavin Luca akiwa ameushika upanga. Yule msimuliaji baada ya kuona vile, alitabasamu na kumuuliza yule kijana mwenzake.
‘Kwanini una picha ya huyo mtu kwenye nguo yako?”

“Kwa sababu ni shujaa wa kweli ambaye hakuhitaji kwenda kulia lia ili asaidiwe, ni mwanaume pekee ambaye aliamua kuinyoosha serikali kwa upumbavu wao ambao huwa wanawafanyia watu wengine. Kama ningefanikiwa kukutana na mtu huyo kabla ya kifo chake basi ningekubali mimi kuuawa kwa niaba yake. Hakuna mtu mwenye akili timamu hapa duniani halafu asiwe shabiki mkubwa wa Gavin Luca na ndiyo maana mpaka leo ndani ya soko la Afrika nguo zake ndizo nguo ambazo zimeuza zaidi kuliko nguo za aina zozote zile kuwahi kutokea” alijinadi kijana huyo na wenzake wakacheka ila walimtaka kijana mwenzao azingatie zaidi ni yapi ambayo yalikuwa ndani ya kile kitabu cha THE DARKNESS OF AN ANGEL.


“Mle ndani yameandikwa maisha yake yeye, maisha ambayo aliyaishi, maisha ambayo yalimfanya yeye kuwa kiumbe hatari zaidi duniani na namna ambavyo alianza kuua watu. Kuna vitu ambavyo wanadamu wengi huwa hawavielewi na hata kama wakivielewa basi huwa wanavielewa muda ukiwa sio rafiki kwao. Mtu yeyote anapo zaliwa huwa anakuwa malaika kabisa kwa sababu hana dhambi yoyote ile ila maisha ya dunia na maisha ambayo yeye anaamua kuyaishi ndiyo ambayo yanaweza kumfanya akawa tofauti na vile ambavyo wengi walikuwa wanamtaka awe au ambavyo asili iliamua awe.

Dunia huwa inaanza kuwabadilisha watu taratibu, ulimwengu huwa unawafanya watu wanakuwa wa tofauti na kipindi wakibadilika ndipo huwa yanaanza kutokea mambo ya kutisha ambayo huwa yanaufanya ulimwengu usiwe sehemu salama kwa ajili ya maisha ya watu. Kitabu kinazungumzia upande wa giza wa malaika, upande ambao wanadamu wengi huwa wanakuwa nao kulingana na maisha ambayo dunia inawachagulia wao kuweza kuyaishi. Bwana yule alizaliwa akiwa kama malaika, alitamani kuwa mtu safi ambaye hakutaka kuwa sehemu ya kuyakatisha maisha ya mtu mwingine lakini angeweza vipi kuyaishi hayo maisha ingali familia yake mwenyewe iliuawa? Tatizo kubwa lilianzia hapo hivyo yule mtu ambaye alitakiwa kuwa malaika aliamua kutuonyesha ule upande wake wa pili wa giza unakuwaje pale ambapo dunia inamlazimisha kuyafanya mambo ambayo huenda hata yeye mwenyewe hakuwa nayo.

Lakini pia kile kitabu kinatoa somo moja kubwa ambalo ndilo huwa linawafanya wanadamu kuonekana wana roho mbaya kupita ile kawaida ya mwanadamu anavyotakiwa kuwa, KISASI. Kisasi huwa ni haki kama kinatakiwa kulipwa lakini ubaya wa kisasi ni kwamba ni ugonjwa wa milele, ni ugonjwa ambao huwa unaishi siku zote za maisha ya mwanadamu. Mwandishi mle ndani kupitia akili ya Gavin Luca anaelezea kwamba unapo lipa kisasi au kutengeneza kisasi unatakiwa kutambua kabisa kwamba umetengeneza tatizo la milele ambalo litaenda kizazi kimoja mpaka kingine. Leo wewe ukilipa kisasi unatakiwa kulazimika kufanya jambo moja kubwa ambalo ndilo limefanya yeye aone kwamba kisasi huwa kinamfanya binadamu kutoka kwenye ubinadamu wake.

Unapolipa kisasi unatakiwa kuhakikisha unaua kizazi kizima cha huyo mtu ambaye alikukosea kwa sababu kama akibaki mtu hata mmoja kwenye kizazi hicho basi ni lazima naye baadae atakuja kurudi kwako na kuhitaji kulipa kisasi cha wapendwa wake na vivyo hivyo na kwako pia nawewe baadae kama ukibaki utatamani kulipa kisasi. Sasa hilo huwa linaenda vizazi na vizazi na ametolea mfano kwamba Gavin mwenyewe aliwahi kufanya kosa kubwa la kumsamehe mtu na baadae akaja kuwa sehemu kubwa ya majuto yake na alijua lazima kuna mtu mwingine ambaye angekuja kurudi baadae.

Sasa hayo maisha ya baadae hayapo kwenye kitabu na ndiyo ambayo hata yeye mwenyewe yalimfanya akaja kufa. Jambo pekee ambalo ni kubwa na halipo ndani ya kitabu ni kuhusu siri za familia yake na familia yake kwa ujumla ambayo kwa baadae ilikuja kujitokeza na wote tunajua kabisa kwamba mwisho wake haukuwa mzuri mpaka hii leo yeye mwenyewe ni marehemu’’ ilikuwa ni simulizi nzuri na ya kuvutia mno. Ndani ya muda mfupi eneo hilo lilikuwa limefurika watu wakiwa makini kusikiliza habari hizo za ndani kabisa watu wakasahau hata kula na hata wauzaji wenyewe walibaki wamesimama wakisikiliza kwa kumakini mkubwa.

“Unasimulia matukio kama ulikuwepo ndugu yangu, nahitaji tuipate simulizi nzima ambayo ipo humo ndani kwa sisi ambao hatuna uwezo wa kukipata kitabu lakini tunatamani kujua kwamba je ile familia mpaka leo bado ipo, na kama ipo iko wapi? Ni muda mrefu umepita na hakuna taarifa zozote kuhusu wao na wala hawajawahi kusikika mahali popote na serikali kwa sasa haijawahi kuzungumzia tena habari hizo” aliuliza kijana mwingine ambaye alikuwa moja ya wale ambao walivutiwa zaidi na yale maelezo.

“Kuhusu familia naweza kukuhakikishia kwamba bado ipo hai lakini kujua kwamba ni wapi ilipo! Nina imani hata raisi wa taifa hili hawezi kukupa jibu la hilo swali lako”
“Mhhhhh umejuaje kama ipo hai?’’ kijana huyo alitabasamu baada ya kuulizwa swali la namna hiyo, alijikohoza kidogo na kumwangalia muulizaji.

“Nina mgonjwa nyumbani hivyo nawahi kwa sasa, kesho nawaahidi kwamba nitawasimulia simulizi nzima na nitawapa taarifa kwamba nilijua vipi kwamba hii familia iko wapi na nitawapa sababu za msingi za familia hii kuweza kupotea mpaka leo’’ kauli yake ilifuatiwa na yeye kunyanyuka hapo na kuanza kuondoka, watu walianza kulalamika na wengine wakiwa wanatukana kwani aliwapa hamu kubwa ya simulizi halafu akaikata njiani, watu walikuwa tayari kumpatia pesa aweze kukaa na kuendelea lakini aliondoka hapo na kuahidi kwamba angerudi kesho yake. Hakuwasikiliza walalamikaji ambao waliondoka wakiwa wanalaani na kushusha matusi mazito ya nguoni kwa kijana huyo’’

Kumaliza kwake mazungumzo kwa ghafla kuliwafanya watu kuanza kutawanyika lakini pia ilikuwa hivyo kwa yule mwanaume ambaye umri wake ulikuwa wa makamo akiwa anayasikiliza yale maelezo kwa umakini. Hakuna ambaye alikuwa amemshtukia hata kidogo huenda kwa sababu ya kunogewa na ile simulizi hali ambayo iliwafanya watu kuwa na mawazo yote upande huo. Alikuwa amemaliza kula, baada ya kuona yule kijana anaondoka alilipa pesa ambayo hakutaka hata kupatiwa chenji yake kisha akatoweka kwa uharaka kwenye eneo hilo. Hakuwa anaenda upande wowote mwingine zaidi ya kumfuatilia yule kijana ambaye alikuwa msimuliaji wa simulizi ile na alionekana kabisa kwamba alikuwa makini kwenye upande wa utulivu wa akili yake, hakuwa sehemu ya wale vijana ambao walikuwa wakikurupuka.

Kijana yule alikuwa anatembea taratibu kwa sababu alikuwa akiifahamu ile mitaa ya Tandika, hakuwa mgeni sana maeneo yale. Kwenye kukatiza mitaa alikutana na watoto wa mjini, watoto ambao huwa wanaamini kwamba mitaa yote ya jiji ni yao na wao ndio ambao wana haki nayo.

“Toa pesa uende zako mtoto wa kike wewe’’ alifoka dogo mmoja ambaye kimtazamo alikuwa mdogo kwake.

“Acheni zenu, yaani mniibie kwenye mitaa yan….” kabla ya kufanikiwa kumalizia sentensi yake alikoswa na upanga ambao ulimpuliza kidogo kwenye paji la uso, hapo alitambua kwamba ameingia kwenye mikono ya panya road hivyo aligeuka ili akimbie ila hakujua kama kuna wengine wawili walikuwa nyuma yake wakiwa wameshika bisibisi kwenye mikono yao. Kijana ambaye mwili wake ulikuwa na mavazi ya hovyo aliirusha bisi bisi moja na kutaka kuitoboa shingo ya kijana huyo ambaye alikubali kwa sababu hakuwa na namna ya kufanya lakini kabla ile bisibisi haijafika kwenye shingo yake ule mkono ulidakwa na kuvunjwa.

Sehemu ya tatu mpaka hapa, sina la kuongeza tena.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA NNE

Alitoa sauti ya majuto na kelele za maumivu ila hazikudumu baada ya kupigwa kwenye shingo mpaka ikazunguka. Wengine ndipo walishtuka na kutambua kwamba walikuwa wamevamiwa hivyo wakahitaji kumshambulia mwanaume yule kwa pamoja ila hawakufua dafu kwa sababu aliivuta bastola yake na kuwatandika wote risasi za vichwa. Yule kijana msimuliaji aliogopa mno kiasi kwamba alibaki amejikunyata akiwa hana hata uwezo wa kukimbia kwakuwa alitambua kwamba naye ni lazima afe kwa namna yoyote ile. Aliinua uso wake kwa wizi ndipo akashangaa baada ya kumuona vizuri yule mtu, ni mtu ambaye alimuona kule kwa mama ntilie ila hakumtambua kwamba alikuwa ni nani, bwana mdogo huyo alikuwa ni mzuri mno kwenye kuyasimulia na kuyapanga maandishi kwenye maelezo ila alikuwa muoga kwenye uhalisia. Maisha ya watu kama ambao alikuwa akiwazungumzia yeye ni marahisi kuyaelezea kwa maelezo mafupi tu ila kuyaleta kwenye maisha ya kweli yanakuwa magumu isivyo kawaida.

“Unaitwa nani bwana mdogo?’’ ilipenya sauti nzito yenye mamlaka kwenye masikio yake.
“Steven” alijibu akiwa anatetemeka.
“Una familia?”
“Ndiyo, naishi na mdogo wangu”
“Unawajua watu ambao ulikuwa unawazungumzia kwenye ile simulizi yako?”
“Hapana, mimi yale niliyasoma kwenye kitabu tu”
“Leo umebahatika kukutana nao kwenye maisha yako” alibaki ameduwaa akiwa kama vile haamini.
“Wewe ni mmoja wao?”
“Ndiyo”

“Kwanini umenifuata mimi?” alianza kutetemeka kwa sababu alikuwa anaijua historia ya watu hao na namna walivyokuwa wanayafanya mambo yao hivyo hapo alitambua ni lazima ufe.

“Hilo swali nitakujibu siku nyingine ila nina maelezo mafupi ya kukupatia na baada ya hapo hautatakiwa kuja kuongelea haya mambo sehemu yoyote ile na ikiwezekana hii mitaa unatakiwa kuhama usiku wa leo”
“Kwanini nifanye hivyo?”
“Kwa sababu kuanzia sasa wewe unaenda kuwa mmoja wetu”
“Whaaaaat?” alibaki ameshangaa lakini bwana huyo aliingiza mkono mfukoni na kutoa bunda mbili za pesa na kadi ndogo.

“Hizo pesa ni milioni hamsini za kitanzania japo zipo kwa mfumo wa dola na hilo bunda dogo ni milioni tano za kitanzania. Hama hii mitaa bila kumuaga mtu yeyote na uende sehemu kubadilisha maisha yako na baada ya wiki piga kwenye hiyo namba kisha jitambulishe kwamba mimi ni Steven” kijana huyo ni kama bado alikuwa haelewi mambo yanavyo enda, alikuwa na maswali mengi mno kwenye ubongo wake lakini wakati huo huo alibaki amepigwa na bumbuwazi, wakati ambao alikuja kushtuka yule bwana hakuwepo sehemu ile, alikuwa ni yeye na anga tu wanatazamana, alizoa zile pesa na kukimbia nazo huku moyoni akiwa na furaha. Ipo hivyo siku zote, maskini akizipata pesa za ghafla jambo la kwanza huwa ni furaha bila hata kuwaza madhara ambayo yanaweza kujitokeza kutokana na zile pesa ambazo amezibeba.

Zile risasi ambazo zilipigwa pale kutokana na makelele hazikueleweka zimetokea wapi hali ambayo iliwafanya watu wengi eneo lile kuzikimbia biashara zao kuhofia usalama wao jambo ambalo lilikuwa ni fursa kubwa kwa wezi wa mtaani pale. Muda mfupi baadae eneo lile lilikuwa limejaa polisi ambapo waliikuta miili ya vijana ambao walitambulika kama vibaka ikiwa haina uhai na mhusika asijulikane ni nani. Mtu ambaye alikuwa amefika lile eneo na kufanya yale yote alikuwa ni mwanaume mmoja ambaye alifahamika kama Mabanzi Mkwambe, alikuwa ni mwalimu wa Jabari huyu mtaalamu na ndiye ambaye alimfanikisha Jabari kujiunga na jamii yao ya the GL’s.




DODOMA
Mji mkuu wa taifa la Tanzania, eneo moja ambalo linazidi kukua kwenye upande wa biashara kila siku kutokana na upanukaji wa mji na uongezekaji wa huduma za kijamii na maendeleo kwa ujumla. Ni moja ya sehemu ambazo taifa linaziangalia kwa jicho pana kuwa kama moja ya sehemu kubwa za kibiashara kwa baadae kitaifa.

Eneo hilo kutokana na umuhimu wake limekuwa likikumbwa na baadhi ya changamoto kadhaa za kihalifu, sababu kubwa ni kwamba kuna watumishi wengi wa serikali hivyo hata mzunguko wa pesa upo. Sababu hiyo imepelekea eneo hilo kujazwa maafisa usalama wengi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba kunakuwa safi kabisa na shughuli hizo za kihalifu zinaweza kupungua kama sio kudhibitiwa kabisa. Licha ya uwepo wa maafisa hao usalama ambao ni wengi lakini bado eneo hilo imekuwa ngumu kuweza kulirejesha kwenye hali ya amani kama mwanzo kwa sababu sio kila ambaye anatambulika kama afisa usalama basi kweli ni afisa usalama.

Imejitokeza jamii ya watu wengi, jamii ambayo inawagawa watu kwenye makundi matatu na ndiyo ambayo inafanya mambo yanakuwa magumu ndani ya eneo hilo. Jamii ya kwanza ni ya watu hao wa serikali ambao ni watu wa usalama, jamii ya pili ni wahalifu ambao nao wanaishi kwenye mgongo kama watu wa usalama pia na jamii ya tatu ni ya raia wa kawaida ambao kwa asilimia kubwa ndio wanategemea mamlaka kuweza kuwalinda nyakati zote. Uwepo wa jamii ya wahalifu ambao wanapora na kuua kwa kivuli cha kudai kwamba ni maafisa usalama kimefanya eneo hilo kutokuwa salama.

Mpaka wakati mambo yanakuja kuharibika zaidi, tayari ndani ya eneo hilo kulikuwa na miili ya watu hamsini ambayo haikuwa na uhai. Thelathini kati yao walikuwa ni watumishi wa serikali, kumi walikuwa ni wafanya biashara wakubwa na kumi ambao wanabaki walikuwa ni raia wa kawaida tu. Kuzuka kwa yale mauaji ndiko ambako kunafanya serikali ifanye maamuzi magumu, wale maafisa wa kule Dodoma kazi ilikuwa inaelekea kuwashinda ndiyo maana mpaka watu wote hao wakawa wanauawa mbele yao na hawana taarifa juu ya wahusika wa matukio hayo na hatua ambazo zilikuwa zinaenda kufuata baada ya hapo.

Timotheo Ganze, ndilo jina ambalo lilijitokeza kwenye ramani ya watu mhimu wa serikali ambao walitakiwa kwenda kuishughulikia hatari hiyo kwa taifa. Ni mauaji ambayo yalianza kukemewa kwenye mitandao ya kijamii, mauaji ambayo yalianza kuchafua taswira ya taifa kwa ujumla kwa sababu ilionekana kama serikali imetoa baraka kwenye mambo hayo ambayo yalikuwa yakifanyika.

Saa sita na dakika kumi na tano ndio muda ambao shababi mmoja ambaye alikuwa na begi lake dogo mkononi alikuwa anaingia ndani ya mji huo mkuu wa Tanzania. Alifika eneo hilo kwa ndege na hakuna hata mtu mmoja ambaye alikuwa ameenda kumpokea, bwana huyo muonekano wake ulikuwa nadhifu lakini usio na utulivu, kwa mwonekano wake alionekana kuwa kama mfanya biashara maarufu ndani ya eneo hilo la Dodoma. Baada tu ya kufika ndani ya eneo hilo alijua kwamba ana kazi moja kubwa, alitaka kuwa maarufu kwanza kwenye midomo ya watu na kazi yake ilikuwa inaanzia hapo.

Kwa watu ambao wanautafuta umaarufu wa haraka maeneo kama hayo, sehemu sahihi huwa ni kuanzia kwenye kumbi kubwa za starehe. Mwanaume huyo aliingia kwenye kumbi moja kubwa ya starehe na kuanza kutamba na kumwaga pesa, alizitumia pesa mpaka wenyeji wakamkoma hilo eneo. Mpaka inafika asubuhi ya kesho yake jina lake lilianza kutajwa kwenye midomo mingi ya wapenda starehe wakiambizana kwamba kuna bosi mpya wa kuangaliwa kwa umakini alikuwa ameingia jijini. Hakuishia pale tu bali hata kesho yake tena alienda sehemu nyingine ghali zaidi na kufanya yaleyale ambayo aliyafanya jana yake, umaarufu wake ndani ya siku mbili tu ukazidi kuwa mkubwa ungehisi kwamba alikuwa ni mtu ambaye alikuwepo hilo eneo kwa miaka kumi nyuma, pesa inaongea bwana.

Lengo lake kubwa alitaka kufahamika kila kona ya jiji kwakuwa aliamini kwamba wale wahalifu walikuwa wakidili na watu wengi wenye mafanikio, walikuwa ni watu ambao kwa mtazamo tu walionekana kuweka maslahi mbele kwanza kisha mwingine ambaye angeingia kwenye mikono yao basi wangemmaliza haraka ili kulinda siri zao. Umaarufu wa ghafla wa bwana yule kwenye kumbi za starehe uliwafanya baadhi ya watu kumuonea huruma kwani alikuwa anaingia kwenye dunia ambayo hakuwa akiitambua ila hawakuwa na taarifa za aina ya mtu ambaye walikuwa wanamuonea huruma.

Siku ya tatu ambayo alikuwa amedhamiria kuanza rasmi kuifanya kazi yake ndani ya hilo jiji, kuna kitu kama kilimshangaza japo hakuwa na uhakika nacho. Kwenye kasino moja kubwa ambalo alikuwa anaingia usiku huo alipishana na mtu wa makamo, ni sura ambayo alikuwa anahisi kuifahamu tangu hapo zamani lakini hakuwa na uhakika kwa sababu ya uharaka ambao ulitumika kuonana na mtu wake na kwa sababu ilikuwa sehemu ya starehe basi hakuona haja ya yeye kuumiza kichwa juu ya jambo hilo hivyo akawa anasogea ndani zaidi ya eneo hilo ambapo alipokelewa na wapambe kwa sababu jina lake walikuwa nalo kwa siku mbili za nyuma hivyo waliamini kwamba uwepo wa huyo mtu hilo eneo usingekuwa bure bali wangepata ulaji na unywaji kwa raha zao.

Sehemu ya nne inafika tamati hapa.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA TANO

Lakini kabla ya utulivu kuchukua nafasi yake, zilisikika kelele kutoka upande wa juu ya eneo hilo. Ni vyumba vya VVIP ndiko ambako kelele zilikuwa zinatokeea. Kelele hizo zilikuwa zimetoka kwa mwanamke mmoja mrembo mno tena akiwa uchi kabisa. Mdada huyo alikuwa anakimbia kana kwamba alikuwa amekutana na mabomu ya boko haramu ana kwa ana jambo ambalo halikuonekana kuwa la kawaida. Timotheo alihisi kuna kitu hakipo sawa hivyo alikimbilia kwenda kwenye ile sehemu kuweza kujua ni kipi kilitokea huku yule mdada ambaye alikuwa anakimbia akishikwa na walinzi ili aweze kusaidia kutoa maelezo kwamba ni jambo gani ambalo lilikuwa limetokea mpaka awe kwenye hali kama ile.

Baada ya kufika kwenye kile chumba, kulikuwa na tukio la kutisha, ni mwanaume mmoja mbavu kidogo alikuwa ameuawa kwa kuzamishiwa kisu kwenye moyo wake. Mwili ulikuwa na majeraha na sehemu kadhaa ambazo zilikuwa zimeiva bila shaka ni kwa nguvu ya ngumi ambazo zilikuwa zinapenya kwenye ule mwili ila haikujulikana kwamba alipigwa na nani na kwa sababu zipi basi hapo ikalazimu yule binti aitwe. Binti yule akiwa analia na kutetemeka alidai kwamba walikuwa wakifanya mapenzi humo ndani mpaka alipo ingia mwanaume mmoja, yeye hakupata nafasi kubwa ya kushuhudia yaliyo tokea kwa sababu yule bwana ambaye aliingia humo ndani alimzimisha na kubaki na huyo mwanaume wake ambaye alikuwa akifanya naye mapenzi. Muda mfupi baadae baada ya yeye kurejewa na fahamu zake ndipo alizinduka na kukutana na hayo mauaji ambayo yalionekana kumtisha na kumnyima raha.

Sasa muuaji alikuwa nani? Timotheo alishtuka na kugundua kwamba haikuwa bahati mbaya kupishana na yule mtu ambaye yeye alihisi kwamba aliwahi kumfahamu kwenye maisha ya huko nyuma. Akiwa sehemu kama ya watu wa kawaida ambao walikuwa kwenye eneo lile muda ambao hata polisi walikuwa wanaingia aliamua kutoka nje haraka, hakukuwa na shida kuweza kutoka kwa wakati huo kwa sababu kila mtu alikuwa kwenye taharuki, mauaji yalileta hofu ndani ya eneo hilo huku watu wengine wakiwa wanaondoka ili wasije kuhusika kwenye hiyo kesi hivyo ilikuwa rahisi kwake. Alifanikiwa kufika mpaka nje lakini hakukuwa na dalili za kuweza kumuona yule mtu wake ambaye alikuwa anahisi alimuona.

Hali hiyo ilimfanya arudi ndani, kurudi ndani alimfuata meneja moja kwa moja na kumvutia pembeni ili apate msaada. Bwana huyo aligoma hivyo alimshawishi meneja na kudai kwamba anafuatilia kesi ya mauaji ndipo alipo amua kukitoa kitambulisho na kumuonyesha, hata meneja mwenyewe alishtuka, alikuwa ni afisa wa ngazi za juu wa usalama wa taifa. Shida yake kwa meneja huyo ilikuwa ni kuhitaji video za marejeo kwa sababu kuna mtu alikuwa anahitaji kumuona ili aweze kujiridhisha kama mawazo yake yalikuwa sahihi na sio kuishi kwa hisia tu. Hakukuwa na namna nyingine kwani alihitaji kuona video ile kabla haijatua kwenye mikono ya polisi ambao mpaka wakati huo ndo kwanza walikuwa wameanza kuukagua ule mwili wa marehemu.

Kwenye video ambayo alikuwa anaiangalia, watu ni wengi ambao walikuwa wanaingia na kutoka kwenye yale maeneo lakini alishtuka kwa mara nyingine baada ya kumuona yule mwanaume ambaye alihisi anamfahamu. Mwanaume yule aliingia ndani ya ile sehemu na kutoka baada ya dakika kumi tu tena mwili wake ukiwa msafi kabisa, hakuna sehemu hata moja ambayo ilikuwa na tone hata la damu. Alitabasamu kwa wakati mmoja lakini moyo wake ni kama ulishikwa na ganzi kwa wakati huo huo kwa mara nyingine tena kwa sababu ya jambo ambalo alilishuhudia. Aliitoa simu yake mfukoni ili kuweza kujiridhisha zaidi asije kuwa anahisi vibaya, hisia zake zilikuwa sahihi kabisa.

OTHMAN CHUNGA, yule mtaalamu wa zamani, moja kati ya viongozi wa familia ya Gavin Luca ndiye ambaye alionekana kwenye hiyo sehemu, umri kidogo ulikuwa unazidi kwenda ila mwonekano wake haukuwa haba kwa sababu ya mazoezi ambayo yalikuwa yanalishwa kwenye mwili wake. Timotheo alijihakikishia kwamba ni kweli yule alikuwa ni Othaman ndiyo maana hata sura yake haikuwa ngeni. Alijikuta akiwa na maswali mengi ambayo hata majibu yake hayakueleweka kwamba yalikuwa ni yapi na angeyapatia kwa nani.

Othman alikuwa na shida gani na huyo mtu mpaka amuue? Othman alikuwa wapi kwa nyakati zote hizo na ni sababu ipi ilimfanya aje kutokea nyakati kama hizo na eneo kama hilo ambalo lilikuwa na kamera na alijua kabisa kwamba sura yake itaonekana? Familia yake nyingine ilikuwa wapi kwa wakati huo na muda wote ambao ulikuwa umepita? Hakuwa na majibu ya maswali yake na aligundua kuendelea kupoteza muda kwenye eneo hilo ilikuwa ni kuendelea kuuweka wazi utambulisho wake kwa watu ambao hawakutakiwa kumjua kwamba yeye ni nani na alikuwa Dodoma kwa sababu ya kufanya jambo gani japo aliondoka kinyonge ndani ya hilo eneo akimtaka meneja huyo asije kumtambulisha yeye kwa mtu yeyote yule hata hao askari wa polisi kwa sababu hawakupaswa kumjua.

Timotheo kuwa na wasiwasi alikuwa sahihi kwa upande wake kwa sababu ya ujio wa hao watu wapya, ni watu ambao walikuwa na historia ndefu mno na ya kutisha ndani ya taifa lao. Ndiyo ilikuwa familia maarufu zaidi kwenye historia nzima ya taifa la Tanzania kwahiyo aliona kuna hatari kubwa ambayo ilikuwa inakuja kwa mara nyingine baada ya miaka kadhaa tu ya amani ndani ya mipaka ya Tanzania. Ilikuwa imepita miaka mitatu, miaka ambayo ilifanya watu wasahau yale maswaibu na shida ambazo walizipata huko nyuma, zile zama za kuhofia kila siku kuokota miili ikiwa haina uhai zilikuwa zimeisha, zile zama hazikuwepo tena kwa wakati huo na ndio muda ambao familia hiyo ilipoteaga moja kwa moja kwenye masikio na macho ya watu.

Ni wakati ambao haikutambulika familia hiyo iliendaga wapi kiasi kwamba hakuna taarifa hata moja ambayo iliwahi kuvuja kutoa utambulisho wa sehemu ya uwepo wa hao watu hivyo kutokea kwa Othman tena eneo ambalo alijua kwamba lilikuwa na kamera nyingi kama hilo, ilikuwa ni ishara mbaya kwa mtu kama yeye ambaye alikuwa anatambua namna mambo kama hayo yanavyokwenda. Alikumbuka kitu kuhusu mtu huyo, sura yake haikutakiwa kufika kwenye mikono ya polisi hivyo alirudi haraka kwa yule meneja na kuudai ule mkanda wote ambapo aliondoka nao kabla hata wale polisi hawaja unasa rasmi naye akatoka eneo hilo.

Timotheo kwenye tafiti yake ambayo ilikuwa inafuata aliyapata majina ya watu wanne, majina ya watu ambao waliaminika kwamba walikuwa ndio wahusika wakuu wa yale matukio ya mauaji ndani ya Dodoma. Kazi yake ya kutamba kwenye kumbi za starehe iliweza kumrahisishia upatikanaji wa taarifa hizo ambazo alizipata kwa malaya mmoja muuza mwili ambaye alidai kwamba alikuwa akitumiwa na watu hao pale ambapo wangehitaji kufanya naye mapenzi au kama kungehitajika kuteka watu hususani wa serikali ambao mbele ya wanawake huwa wanatekwa kirahisi tu.

Taarifa hizo kwake zilikuwa za dhahabu, zilimfanya kuona kazi yake imekuwa nyepesi kuliko hata ambavyo alifikiria hivyo alikuwa anasubiri usiku uende ndipo aweze kuvamia eneo ambalo aliambiwa kwamba watu hao walikuwa wakipatikana. Saa saba na dakika hamsini na tano usiku, kabla ya muda mfupi ambapo aliambiwa kwamba kesho yake watu hao walikuwa wanapanga kumuua mkuu wa mkoa wa Dodoma ndipo aliweza kutua miguu yake kwenye nyumba ambayo walidaiwa kuwepo hao watu.

Timotheo alikuwa ni mtu mmoja ambaye kazi yake ilikuwa zaidi ya uwepo wa watu hata kumi ndiyo maana licha ya kuiona hatari ambayo ilikuwa mbele yake, bado alihitaji hiyo kazi kuifanya mwenyewe bila uwepo wa mtu mwingine yeyote yule. Kwenye apartment moja kubwa ya kifahari ndilo eneo ambalo alipewa taarifa kwamba hao watu wake walikuwepo, alifika akiwa amejiandaa kwa ajili ya kukabiliana na kila hali ambayo angeikuta hapo japo yale ambayo aliyakuta yalikuwa ni tofauti na yale ambayo yeye aliyatarajia. Kwanza geti la eneo hilo lilikuwa wazi kabisa, hakukuwa na dalili zozote za uwepo wa mtu getini hali ambayo haikuwa ya kawaida ukizingatia ulikuwa ni usiku wa manane.

Aliitoa bastola yake na kuingia kwa tahadhari ambapo mlango wa ndani pia ulikuwa wazi kama getini, jambo hilo lilimpatia taarifa na kuelewa kwamba mazingira hayo kwa wakati huo hayakuwa salama, ilikuwa ni hatari kubwa ambayo huenda ilikuwa mbele yake. Alitembea haraka haraka mpaka mlangoni ambapo aliingia kwa sarakasi moja na kuibukia upande wa pili lakini palikuwa patupu. Taa ya ndani ilikuwa imewaka ila hakuona mtu kwa sababu macho yake yalikuwa yakiangaza kila kona kuweza kutambua kama kulikuwa na hatari yoyote aweze kukabiliana nayo vizuri.

Alianza kutembea taratibu mpaka alipohisi kwamba amekanyaga kitu kwa buti lake ikamlazimu kuangalia sehemu hiyo ilikuwa na nini. Alijikuta akishtuka kwa hofu baada ya kutambua kwamba ameukanyaga ni mwili wa mtu. Hata baada ya kuangalia vizuri, aligundua kwamba haukuwa mwili tu bali ilikuwa ni miili. Eneo hilo lilikuwa na miili ya watu wanne ambao waliuawa kikatili sana huku ikiwa imerundikwa sehemu moja, aliangalia kwa umakini na kutambua kwamba miili hiyo bado ilikuwa ya moto maana yake muuaji hakuwa mbali, alikuwa mazingira hayo hayo na hivyo kupelekea hata yeye usalama wake kuwa mashakani japo hakuonekana kulijali hilo zaidi ya kuhitaji kumpata muuaji huyo kabla hajafanikiwa kutoroka.

Alitoka nje haraka akiwa anaonekana kuwahi jambo, aliangaza upande wa mbele na hakuona mtu hivyo akataka kuzunguka upande wa nyuma wa apartment hiyo ili aweze kuona kama mtu wake alikuwa huko ila baada ya kusogeza hatua mbili mbele alisikia sauti ya mguno nyuma yake. Aligeuka kwa kasi kubwa akiwa ameinyoosha bastola yake akafanikiwa kuona jambo la kushangaza ambalo lilimshtua kwenye moyo wake. Othman Chunga ndiye ambaye alikuwa amesimama mbele yake akiwa ameiweka mikono yake nyuma. Alijikuta akiwa na maswali mengi ila hakuelewa ni swali gani lilikuwa sahihi kuanza nalo, hakuona ni jambo lipi alipaswa kuongea na bwana yule ukiacha tu kutokuelewa uwepo wake eneo hilo na kwamba tarifa hizo yeye alikuwa anazipatia wapi.

“Othman upo chini ya ulinzi”
“Wewe hapo ndo unataka kunikamata mimi?”
“Una haki ya kubaki kimya mpaka pale mwanasheria wako atakapofika, unakamatwa kwa kuhusika na mauaji ya watu watano” alitabasamu akiwa anamsogelea Timotheo ambaye alikuwa akirudi nyuma taratibu japo mkononi yeye ndiye alikuwa na bastola.

Sehemu ya tano sina la ziada mpaka wakati ujao.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA SITA

“Timotheo Ganze, sina mpango wa kukuumiza siku ya leo kwa sababu kuna nyakati zitakuja ambazo huenda mimi na wewe tutahitaji kuumizana ila kwa sasa kazi yangu imeisha hivyo tutakuja kukutana kwa wakati mwingine tena na sio sasa’’ aliongea kama anaongea na mfanyakazi wake akiwa hana hata wasiwasi.

“Umelijuaje jina langu?”
“Unahisi nipo hili eneo kwa bahati mbaya Timoth? Hapana”
“Kwanini unawaua hawa watu?”
“Na wewe naweza kukuuliza kwamba ni kwanini unawawinda hawa watu?”

“Kwa sababu ni kazi yangu ila wewe hii sio kazi yako jambo ambalo linafanya uwe raia wa kawaida tu na raia wa kawaida kama wewe hauna sababu ya kuhalalisha wewe kuua watu”

“Kazi yako? Ungekuwa unajua kuifanya kazi yako unahisi kwamba ungeruhusu hawa vibaka kuua watu zaidi ya hamsini?”

“Hilo ni kosa la kiusalama na mambo kama haya sio yote ambayo unaweza kuyazuia na ndiyo sababu kubwa iliyofanya nikatumwa mimi kuja kuifanya hii kazi”
“Muda umeenda sana na umri unanitupa mkono, naenda kupumzika, siku ambayo nitakuwa na kazi na wewe nitakutafuta mwenyewe” Othman aliongea huku akiwa ananza kuondoka hilo eneo ila alisikia mlio wa bastola kukokiwa.

“Hakuna mahali unaenda muuaji mkubwa wewe, hili ni taifa ambalo linaongozwa kwa misingi ya sheria, familia yako si lolote mbele yangu hivyo hizi sio zama ambazo mnaweza kufanya yale ambayo mnayataka tena. Kubali kwamba mwisho wenu ulishafika Othman na ujisalimishe mwenyewe kwa sababu sitaki kuingia kwenye lawama za kumuumiza ama kumuua mzee kama wewe ambaye mpaka sasa kuwa nje ya gereza ni kwa sababu za huruma za viongozi tu ila ulitakiwa uwe umekufa” aliongea mambo mazito ambayo huenda hakuwa akiyajua madhara yake, Othman alikuwa amempa mgongo na kusimama akiwa anamsikiliza kijana huyo wakati anatamba na maneno yake ya kejeli na dhihaka kubwa.

“Bwana mdogo, umenitamkia kauli ambayo hata raisi wa taifa lako hana ujasiri wa kuitamka. Usinilazimishe nikuue ingali bado hata haujayafaidi matunda ya hiyo kazi yako mpya”

“Hahaha mzee unahisi mimi ni wale ambao ulizoea kukutana nao huko kabla si ndiyo? Niamini mimi hakuna mahali unaenda kwa sababu naweza hata kukuua muda huu hapa’’ Timotheo alionekana kuwa moja ya wale wanaume ambao walikuwa wakijiamini kupita kiasi. Othman aligeuka na kusogea kidogo lakini hata Timotheo mwenyewe alikuwa amesogea hatua kadhaa hivyo hawakuwa mbali. Kijana huyo alionekana kuwa na jeuri kubwa ndani yake, jeuri ambayo ilitokana na yeye kuyakosa yale masomo mhimu na makubwa ya ulimwengu ambayo yangempatia elimu ya kutosha.

Alihisi kama kuna kitu kinakuja upande wake, ndipo alitambua kwamba vidole vya Othman vilikirusha kisu kuelekea upande wake kwa nguvu na kasi kubwa. Alirudi nyuma kidogo na kufanikiwa kukikwepa kile kisu lakini wakati yale yanafanyika Othman alikuwa anamjia pale ambapo yeye alikuwepo, aliugeuza ule mkono wake ambao ulikuwa na bastola kuelekea kwa mzee yule ila haukufua dafu. Alipigwa na mguu bastola ikadondokea mbali na pale.

Alijikusanya na kumfuata Othman kwa nguvu na ghadhabu kubwa, miguu yake ambayo ilikomaa iliishia kupiga hewa kwa nguvu na kumfanya asogee mbele zaidi kwa sababu zile hatua zake zilikuwa za nguvu halafu alikosa kitu cha kumzuia mbele yake. Alikutana na ngumi moja ya kifua akahisi ni nyundo imetua pale mpaka akaishia kujishika kwenye eneo hilo, aliinua uso wake akagundua kwamba kuna miguu ilikuwa inakuja upande wake, alifanikiwa kukwepa mmoja ila mmoja ulitua kwenye shingo yake akajibamiza kwenye ukuta, alitaka kugeuka ila alisita, alisita kwa sababu kisu kilikuwa kinatazamana na shingo yake. Ilikuwa na maana kwamba kama angejitikisa vibaya basi alikuwa anakwenda na maji pale pale.

“Kijana wangu subiri nikupe somo moja dogo la haya maisha ambalo vijana wa umri wako huwa bado hawalitambui. Umaarufu ni kitu kibaya sana kwenye haya maisha, ukimuuliza kila kijana huko mtaani atakwambia anataka kuwa maarufu, wengi huwa wanaamini kwamba ukiwa maarufu mambo mengi maishani unayapata kirahisi tu jambo ambalo linaweza kuwa la kweli au lisiwe la kweli pia ila niamini mimi umaarufu unalipwa kwa gharama kubwa.

Wewe unafanya kazi yako ndiyo ila unahitaji umaarufu kazini kwako, unataka kuwaonyesha kwamba unaweza kuifanya kazi hii wewe mwenyewe kwa mkono wako bila msaada wa mtu yeyote yule ili uweze kupata sifa na ikiwezekana upandishwe cheo. Kazi yako ya kupata taarifa juu ya hawa watu uliifanya vyema lakini wakati wa kuja kuwakamata ulitakiwa uwape taarifa wenzako ambao wapo hapa Dodoma ili waje kukusaidia lakini haujafanya hivyo unajua kwanini? Kwa sababu unapenda umaarufu na kupata sifa za kuonekana unafanya kazi kubwa na nzuri kuliko wenzako wote ambao wapo na ambao wamewahi kuwepo.

Kwenye kumbukumbu zangu ni kwamba kwenye nafasi yako waliwahi kuwepo watu ambao walikuwa na uwezo mkubwa zaidi yako wewe, waliwahi kuwepo wazalendo zaidi yako wewe na waliwahi kuwepo wapenda sifa na umashuhuri zaidi yako wewe hapo lakini leo ukiniuliza kwamba wako wapi? Ni watu wa kuhesabika tu ambao walifanikiwa kupona na kuishi mpaka leo hii wanaanza kuzeeka kama mimi ila wengi wao ni marehemu. Moyo wako unapotaka kulifanya jambo kwa msukumo wa kupata sifa basi mara nyingi mboni za macho huwa zinaacha kabisa kuona yanayokuja mbele na hata akili huwa haifanyi kazi kwa sababu inatawaliwa na ile tamaa ya kufanikisha kupata kile ambacho wewe unakitaka.

Sikuwa na mpango wa kukuua ndiyo sababu nakupa nafasi nyingine ya kuishi siku ya leo lakini kama kuna siku nyingine utakuja kuitaja familia yangu kirahisi kwenye mdomo wako huo basi amini kwamba hata mwili wako hautakuja kupatikana wala kutambulika kama uliwahi kuwepo ama kuishi kwenye huu ulimwengu. Leo ukitoka hapa kawaambie wakubwa zako kwamba hawa watu sio kwa bahati mbaya kuwepo hapa Dodoma na kuanza kuua watu na hawapo hapa kwa ajili ya kupora watu mali kama ambavyo huenda tafiti zenu zinawapa majibu hayo bali huu ni mwanzo wa hatari nyingine ya watu ambao hawatambuliki ambao wameamua kulivamia taifa kwenye nyakati kama hizi.

Siku za hapo mbele yanaenda kutokea mambo ya kutisha zaidi ya haya ambayo umeyaona ndani ya hili jiji na mambo haya sio kwa bahati mbaya bali ni matokeo ya ujinga ambao ulifanywa na viongozi kadhaa ambao wamewahi kupita na wengine mpaka sasa wapo madarakani bado. Hawa watu ambao wamefanya haya sio watanzania moja kwa moja japo kuna watanzania wamehusika ndani yake hivyo ni kazi kwako kwenda kujiandaa na hii hatari ambayo inakuja hapo mbele kabla haya mambo hayajawa mabaya zaidi” Othman alimuachia kijana huyo akiwa amemtoboa kidogo kwenye shingo yake na kuanza kuondoka.

“Hao watu ambao unawasema ni akina nani, wametokea kwenye taifa gani na kwanini wanafanya haya ndani ya taifa letu?” Timotheo aliuliza akiwa anahema kwa hofu yenye matumaini baada ya kukoswa koswa kuuawa eneo hilo lakini hakujibiwa, Othman alitoka mpaka nje ambapo ulisikika mlio wa breki za gari ambayo bila shaka ilimfuata ni yeye na baada ya hapo iliondoka kwa spidi kali eneo hilo akibaki Timotheo mwenyewe amekaa akiwa haelewi ni kipi kilikuwa kinamtokea nyakati kama hizo.




TANZANIA INVESTIGATORY GROUP OF INTELLIGENCE
Jumba nene, jumba kubwa, jumba la kutisha kwa raia wengi, nayazungumzia makao makuu ya shirika la kijasusi la Tanzania ambayo yalikuwa yakipatikana Makumbusho Dar es salaam. Hilo ndilo eneo ambalo lilikuwa linahakikisha usalama wa taifa zima kwa masaa ishirini na manne kwa kuhakikisha ukusanyaji na uchakataji wa taarifa za siri zaidi ambazo zinalihusu taifa la Tanzania.

Ndani ya jengo hilo kubwa ndipo alipokuwepo mkurugenzi mkuu wa shirika hilo mzee Kai Aiden. Kiongozi huyo alikuwa sehemu ya historia ya nyuma ya taifa juu ya taarifa za kukanganya na kuleta taharuki kubwa. Kiongozi huyo wa shirika hilo alishuhudia makubaliano ya mwisho ambayo yalifanywa na familia ya Lionela pamoja na raisi wa nchi naye akiwa sehemu hiyo. Sasa ndani ya jengo hilo wakati huo kulikuwa na kikao cha wazito wa shirika hilo, kikao ambacho mtu aliyekuwa akisikilizwa zaidi alikuwa ni mmoja kwa sababu ndiye ambaye alikuwa na taarifa ambazo zilikuwa zikihitajika kwa wakati huo.

Sita inafika mwisho hapa, panapo majaaliwa tukutane wakati ujao.

Febiani Babuya.
 
####JE WEWE NI SHABIKI NA MPENZI WA SIMULIZI ZA KIJASUSI NA KIPELELEZI?

Kama jibu ni ndiyo basi mwandishi FEBIANI BABUYA ni suluhisho la matatizo yako na kiu yako kwenye ulimwengu wa maandishi.

#### JIPATIE SIMULIZI BORA ZA KIPELELEZI KWA BEI AMBAYO NI RAFIKI KABISA LAKINI UNAPATA BURUDANI, ELIMU pamoja na UTAMBUZI wa DUNIA HII YA SIRI, SIASA na MAPIGANO ambavyo vyote vinaelezewa kwa undani kwenye simulizi hizi za KIJASUSI.


########SIMULIZI HUSIKA NA BEI ZAKE👇


1. ULIMWENGU WA WATU WABAYA...4000

2. I WANT TO DIE JUDGE...4000

3. GEREZA LA HAZWA...5000

4. INNOCENT KILLER (THE REVENGE)/ MUUAJI ASIYE NA HATIA (KISASI)...5000

5. NYARAKA NAMBA 72/ DOCUMENT NUMBER 72...4000

6. ELECTION SAGA MONEY IN BLOOD (SAKATA LA UCHAGUZI PESA KWENYE DAMU)....4000

7. JIJI LA KAMARI....4500

8. BADO NINAISHI (ASHRAFU NDILO JINA LANGU)....4500

9. NAFSI ZILIZO TELEKEZWA ....5000

10. IDAIWE MAITI YANGU....4500

11. THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA (SEASON 2 YA IDAIWE MAITI YANGU)....5000

12. JUMBA JEUSI ....4500

13. SIKU ZA MWISHO (SEHEMU YA MWISHO YA IDAIWE MAITI YANGU)- THE DARKNESS OF AN ANGEL .....5000

14. TONE LA DAMU (THE JOURNALIST)...5000

15. KARATA YA MAUAJI.....5000


#UNAWEZA KUZIPATA KWA KULIPIA KWA NAMBA HIZI HAPA AMBAZO NI ZA MWANDISHI MWENYEWE..... FEBIANI BABUYA

0621567672 (HALOPESA)

0745982347 (M-PESA)

0714581046 (TIGO-PESA)

0689440143 (AIRTEL MONEY)

36316279 (LIPA NAMBA (M-PESA) inapokea mitandao yote)

FEBIANI BABUYA


NB
MAANDISHI YANGU NI HAKI YAKO..... 📚 📖✍️
 

Attachments

  • FB_IMG_1755268206502.jpg
    FB_IMG_1755268206502.jpg
    62.2 KB · Views: 22
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA SABA
Timotheo Ganze alikuwa amerejea kutoka Dodoma, kurejea kwake kulitokana na sababu ya kwamba kazi ambayo alitakiwa kwenda kuifanya huko ilikuwa imeisha lakini hakuwa na furaha. Hakuwa na furaha kwa sababu yaliibuka mambo mengine ambayo huenda kwa wakati kama huo bado hakuwa ameyatarajia kama yanaweza kutokea.

“Umesema kwamba umekamilisha kazi lakini hakuna taarifa yoyote wala ushahidi wowote wa maana kuweza kuamini maneno yako ambayo umeyaweka mbele yetu hapa”

“Ndiyo maana nilisema nahitaji muda wa kuwaza kwanza kiongozi”
“Sina muda wa kuendelea kukusubiri wewe uendelee kuwaza kuhusu haya, nipe taarifa muda huu haraka”
“Uhalisia ni kwamba hii kazi imekamilika lakini sio mimi ambaye nimeikamilisha”

“Unataka kuniambia uliajiri watu wa kuifanya hii kazi kwa niaba yako?”
“Siwezi kufanya hilo jambo wakati nayajua madhara yake’
“Kwahiyo unataka kusemaje labda?”
“Historia imejirudia tena”
“Haupo kwenye sehemu ya historia yoyote ya taifa hili, sasa hiyo historia imejirudia vipi?”

“Wale watu wameuawa na familia ya Gavin Luca” wote walibaki wameduwaa kama sio kushangaa. Kila mmoja alitamani kuongea kitu ila wote waliona kama hakuwa muda sahihi kuongea hivyo waliishia kuangaliana na kumwangalia Timoth ambaye ndiye alikuwa na hizo taarifa zote.

“Hii familia ilipotea miaka mitatu ambayo imepita na waliahidi kwamba hawatahitaji kuhusika kwenye jambo lolote lile hivyo hata serikali isije kuwafuatilia tena kwani inaweza kuwa tatizo na kweli tuliwaacha na mpaka leo hatujawahi kupata taarifa yao hata moja, sasa unasemaje kwamba hii ndiyo familia iliyo husika na haya mauaji?”

“Hata mimi mpaka sasa bado sijaweza kujijibu hilo swali ambalo natamani kuyapata majibu yake”
“Ni nani amefanya haya?”
“Othman Chunga”

“Una uhakika na hizi taarifa?” Timoth hakutaka kuongea sana bali alitoa frash ndogo na kuiweka kwenye runinga kubwa ambayo ilikuwa mbele. Kwenye runinga hiyo alionekana mtu akiingia na kutoka kasino ndani ya dakika zisizofika hata kumi na kwenye hiyo video aliyekuwa anaonekana alikuwa ni Othman mwenyewe.

“Hii ndiyo kasino ambayo mtu wa kwanza aliuawa na ndiyo kwa mara ya kwanza nilipo tambua kwamba mhusika alikuwa ni yeye kwa sababu nilihisi kwamba labda nimekutana naye kwa bahati mbaya lakini nilitambua kwamba hakuna bahati mbaya bali ilikuwa ni mipango yake. Baada ya hili tukio nilifanikiwa kupata taarifa kwa malaya mmoja ambaye nilikuwa naye juu ya mahali ambapo wapo watu hao kwa sababu walikuwa wakimtumia yeye kwenye mambo yao na kufanya nao mapenzi.
Baada ya kwenda eneo lile niliwakuta wale watu wakiwa wameuliwa tena miili ikiwa bado ya moto hivyo nilitambua kwamba mhusika hakuwa mbali ndipo nikaamua kutoka ili niweze kumpata na ndipo nilipo kutana na Othman uso kwa uso” Timoth alitulia lakini alilazimika kuendelea kwa sababu kila mtu alikuwa akimuangalia yeye.

“Ni mtu ambaye anatisha, binafsi nilitaka nimkamate la….’’
“Ulitaka umkamate Othman?” ni swali ambalo mkubwa wake alimuuliza kwa mshangao mkubwa.
“Ndiyo”
“Ulikuwa na wenzako wangapi?”
“Nilikuwa mwenyewe”
“Hayakuwa makubaliano yetu”

“Nilishindwa kumuamini hata mmoja kumpa taarifa juu ya uwepo wa watu wale hivyo nikaamua kuwashtukiza mwenyewe’’ mkuu wake alitulia kumpatia nafasi aweze kuendelea.
“Baada ya pale bwana yule aligoma kufanya vile na kutishia kuniua, nimejaribu kupigana naye lakini niwe mkweli ni kwamba ananizidi uwezo parefu hivyo sijaweza kufua dafu kabisa mbele yake”

“Alikwambia nini mpaka ukatoka ukiwa hai?”
“Alisema kwamba haukuwa muda sahihi wa mimi kufa bali kwa wakati mwingine ambao yeye atanihitaji mimi”
“Kuna jambo lolote la maana ambalo amekwambia?”
“Ndiyo”
“Hiyo ndiyo ilitakiwa kuwa habari ya kwanza kabisa ya wewe kunipatia hapa sio maamuzi yako ya kipuuzi ambayo uliamua kuyabeba huku ukijua kabisa kwamba hauna uwezo nayo”

“Ameniambia kwamba nikufikishie ujumbe kuwa nyakati za giza zinakuja tena, kuna matukio mabaya yanaenda kujirudia kama huko nyuma na ndiyo sababu ya hawa watu ambao hawaeleweki kuanza kujitokeza. Amesisitiza kwamba hawa watu sio watanzania japo kuna watanzania pia ndani yake ambao wanahusika kwenye haya hivyo ni wakati wa kuwa makini kwa mara nyingine tena”

“Kwanini awavamie hao watu na kuwaua?”
“Hilo ni swali ambalo hata mimi amegoma kabisa kuweza kunijibu kiongozi”

“Sina wasiwasi kwamba ni wapi kazipata taarifa, sina wasiwasi kwamba alikuwa ana uwezo wa kufika popote na kufanya lolote lakini kwa familia kama ile ambayo iliamua kuanza kuishi maisha ya kawaida mbali na haya majanga isingeweza kujiingiza kwenye jambo la hatari kama hili kama hakuna sababu nyuma. Sasa swali ni kwanini afanye haya? Kuna jambo gani ambalo lipo nyuma?”

“Ndiyo maana nilihitaji nimpate hata mtu mmoja kati ya wale watu ili aweze kusaidia kwenye kujibu maswali kama hayo”
“Hii video uliipata pale kwenye kasino?”
“Ndiyo”

“Kama ni hivyo maana yake alijua kabisa mamlaka zitaipata sura yake, sasa kwanini ahitaji hayo yote? Ni kwamba alikuwa anataka kufahamika, kwa sababu zipi sasa? hawa watu huwa hawajitokezi hovyo na kama hakuna mambo ya msingi za kuweza kufanya au kama hakuna vitu vikubwa nyuma yake. Mara ya mwisho Gavin Luca kuamua kuonyesha sura yake hadharani ilitokea hatari kubwa kwa baadae, huyu naye kama kafanya haya maana yake alitaka tuone na tutambue kwamba kuna hatari kubwa sana ipo hapo mbele na kafanya haya kwa niaba ya kiongozi wake” Mkurugenzi aliongea akiwa kama ni mtu ambaye alikuwa anakumbuka jambo la siku za nyuma huko.

“Mimi nafikiri huyu ndiye kiongozi wa hawa watu kwa sasa baada ya Gavin kuweza kufa?”
“Huyu ni msaidizi, kiongozi wao mkuu ni Lionela”
“Kama ni yule binti kwanini asionekane yeye?”
“Hapa ndipo swali gumu lilipo, na ni bahati katokea Othman kwa sababu kama angetokea yule mwanamke yangetokea mambo mabaya sana mpaka sasa”

“Kwahiyo tunafanyaje kuhusu hili?”
“Hapa hakuna namna tena, inatakiwa nikutane na raisi tuweze kuvunja yale makubaliano”
“Unamaanisha watu hawa watafutwe kwa nguvu?”

“Kwa sasa hakuna namna, kama kuna hatari kubwa inakuja maana yake watakuwa wanajua ama wamepata taarifa za viashiria vyake na kumbuka kwamba amewaua wote na watu hawa huwa hawaui mpaka wapate lile ambalo wanalitaka na kama ni hivyo lazima kuna taarifa alishapewa ambazo tunatakiwa kuzipata. Sasa kuzipata kwake ni mpaka tuweze kumpata na yeye mhusika mwenyewe, na tunampataje? Hatujui walipo hivyo inatakiwa itoke amri kwa raisi kitengenezwe kikosi kuanza kupeleleza kujua hawa watu kwa sasa wako wapi, wanafanya nini na wana mpango upi?”
“Bosi nadhani hili sio wazo zuri kwa sababu wote tunajua yale ambayo yanaweza kutokea’’

Unamshauri nini mkurugenzi na haya maamuzi yake? Ni kweli atawezana na hili jambo ambalo anahitaji kulifanya?
Mimi sina jibu kamili, sehemu ya saba naweka kalamu kando.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA NANE
“Itakuwa haina maana ya uwepo wetu kama matatizo yanaenda kutokea halafu sisi tunachagua kuendelea kukaa kimya kwa sababu tu ya makubaliano na familia ambayo ilifanya uhalifu halafu inajipangia namna ya kuishi. Najua madhara ya jambo hili ila kwa sasa hakuna namna nyingine, tunatakiwa kujua Lionela yuko wapi na familia nzima” mkurugenzi hakutaka ushauri tena japo maamuzi yake yalionekana kabisa kwamba ni mabaya ila hakuona kama kuna namna. Alibeba koti lake la suti na kutoka humo ndani na walinzi wake kwa ajili ya kuianza safari kwenda Ikulu wakati ambao alikuwa anaivuta simu yake mfukoni kutoa taarifa kwa raisi juu ya ujio wake mzito ambao ulikuwa umaishika hatima ya taifa zima na maamuzi yalitakiwa kutoka haraka.



IKULU, DAR ES SALAAM
Ndani ya jumba kubwa ambalo kila mtu huwa anatamani kuingia ama kuwa sehemu ya historia yake, alionekana mheshimiwa raisi akiwa kwenye moja ya bawa la Ikulu. Eneo hilo alikuwa akipenda kutulia hususani akiwa na mambo yake binafsi ambayo anayawaza na ni ya mhimu au pale ambapo alikuwa anahitaji kupata utulivu wake wa akili. Eneo hilo lilikuwa na bwawa la kutengenezwa na sehemu hiyo alikuwa akipenda kuitumia kuweza kuvulia samaki kama ambavyo ilikuwa kawaida yake kwa siku zote.

Alikuwa ameketi akiwa anamsubiri mkurugenzi wake ambaye alikuwa naye kwenye majanga mengi, mkurugenzi ambaye waliwahi kupishana mara kadhaa kiasi kwamba wakaishia mpaka kutishiana lakini mpaka nyakati kama hizo walikuwa wapo pamoja. Mheshimiwa alikuwa anawaza mbali, maisha yalikuwa yanaenda kasi kuliko kawaida na miaka nayo ilikuwa inazidi kukatika bila kusimama.

“Nina muda mfupi wa kuendelea kubakia ndani ya hili jumba, nilitamani niendelee kuwepo hapa zaidi lakini katiba ya taifa hili hainiruhusu kufanya hivyo” alikuwa akiongea na mzee mmoja ambaye alikuwa mshauri wake, mzee huyo alitabasamu na kumwangalia mheshimiwa usoni.

“Uliwahi kusema kwamba hii sehemu inakukera ni bora ukatafute sehemu nyingine ambayo inaweza kukupatia furaha, ni jambo gani linakufanya mpaka uone hapa kwa sasa panakufaa wewe?”

“Maisha yanaenda kwa uharaka nadhani tofauti hata na mimi mwenyewe nilivyokuwa nayafikiria huenda ndiyo sababu lakini muda mwingine maneno ya sisi wanasiasa usiyaamini kwa nyakati zote, huwa tunabadilisha lugha kila wakati kutegemeana na hadhira ambayo inakuwepo mbele yetu kwa wakati huo”

“Unamaanisha nini mheshimiwa?”
“Unahisi kwanini kila mtu akifika kwenye hiki kiti huwa hatamani kuweza kuondoka tena?”

“Kwa sababu ni sehemu pekee ambayo inakufanya unakuwa juu ya kila mtu, sheria ni wewe na wewe ni sheria, hakuna mtu ambaye anaweza kuja na kuongea hovyo mbele yako kwahiyo kiti hicho kinakufanya wewe kuwa ndiye mtu mwenye nguvu zaidi ndani ya taifa lako” jibu la raisi lilimfanya mzee huyo kutabasamu kwa sababu alijua kabisa wanasiasa huwa hawajali lolote kuhusu raia wao bali ni mali na nguvu ambazo zinawafanya wanaogopwa kila pande na kuheshimiwa na watu.

“Upo sahihi kabisa na ndiyo maana unatakiwa uhakikishe unakiachia kiti kwa amani kabisa”
“Unahisi kwamba natamani kubakia hapa kwa nguvu?”
“Hapana kwa sababu hilo haliwezekani”
“Sababu ipi ambayo inafanya isiwezekane?”
“Katiba”
“Hahaha hahaha katiba inaweza kubadilishwa tu”

“Sio kirahisi hivyo mheshimiwa na nadhani mawazo kama hayo unatakiwa kuyap……” alikatisha maelezo yake wakati ambao ugeni ulikuwa unawasili eneo hilo, mkurugenzi mkuu wa shirika la TIGI alikuwa amefika tayari ikiwa ni usiku wa mapema kabisa ndani ya Ikulu.
“Ni muda mrefu bwana Kai tangu mara ya mwisho mimi na wewe tuweze kuonana na kuongea kuhusu mambo ya taifa letu, bila shaka leo mpaka umeamua kuja Ikulu basi kuna jambo kubwa na la maana ambalo unahitaji mimi nilisikie kutoka kwako”

“Ndiyo kiongozi, nimekuja hapa kwa sababu kuna jambo la mhimu”
“Hilo litazungumzwa lakini kwa sasa unaionaje hali ya taifa hili na mwenendo wake kwa ujumla? Naona kama hali ya utulivu imefanya serikali tuendelee kuzizoa sifa mpaka sasa”

“Hilo ni kweli lakini suala la Dodoma mpaka sasa limeleta taswira nyingine”
“Hilo ni jambo la kawaida kwa sababu nina imani mpaka muda huu upo hapa na mimi basi ulisha limaliza”

“Ndiyo limeisha mheshimiwa”
“Sasa tatizo nini mbona kama haupo sawa?”
“Kwa sababu kuna jambo jipya ambalo limeibuka”
“Nenda kwenye hoja ya msingi moja kwa moja”
“Ile kazi ya Dodoma haijafanywa na vijana wangu”
“Umesema imeisha, sasa inakuaje sio vijana wako tena?”

“Kwa sababu kuna mtu ambaye alikuwa anafanya kazi ile kwa kumtangulia yeye na kila alipokuwa anafika kwenye eneo la tukio basi alikuwa anakuta kazi ikiwa imeshafanyika”

“Kama ni hivyo, unahisi ni nani anaweza kufanya jambo kama hilo? Nilijua ungekuja kunipatia taarifa za jina la huyo mtu kumbe unakuja kwangu kushtakia majukumu ya kazi yako?”

“Sipo hapa kukushtakia bali nipo hapa kwa kwa ajili ya kukutaka wewe ufanye maamuzi magumu ambayo ndiyo unaweza kuwa mwanzo wa kubadilisha kila kitu’’
“Unamaanisha nini?”
“Mtu ambaye amewaua wale watu kule ni Othman Chunga”
“Whaaaaaat?”
“Ndiyo mwenyewe ambaye amehusika na hili jambo”
“Nadhani haupo makini na kazi yako kwa sababu haiwezi kuwa kweli na jambo hili haliwezekani”
“Kwani mheshimiwa, wewe unajua kwa sasa ni wapi walipo hawa watu?”

“Sijui na hayakuwa makubaliano yetu mimi kuanza kuwatafuta kwa baadae au kujua lolote kuhusu haya nadhani hata wewe unayakumbuka vizuri mno haya makubaliano kuliko mtu yeyote yule”

“Othman ndiye ameua hawa watu lakini pia amekutana na kijana wangu ambaye ndiye alipaswa kuweza kuifanya kazi hii” kwa yale maelezo raisi alitambua kwamba mzee huyo alikuwa anamaanisha kila neno ambalo lilikuwa linatoka kwenye kinywa chake.

“Kamuua?”
“Hapana, amemuacha”
“Kwahiyo kimetokea nini?”

“Amempa taarifa kwamba kuna hatari kubwa inakuja hivyo kama taifa tujiandae tena amemsisitizia kwamba zinakuja nyakati za giza ambazo huenda zitakuwa mbaya kuliko hata zile ambazo zimepita huko nyuma”

“Nyakati zipi hizo ambazo anazungumzia?”
“Mauaji ya watu, vurugu na ukosefu wa amani kama ilivyokuwa kwenye maisha ya huko nyuma”

“Kwanini warudi kwa ajili ya kuua watu?”
“Hakumaanisha yeye bali alimaanisha hawa watu ambao walikuwa wanafanya mauaji huko Dodoma”

Sehemu ya nane inafika mwisho.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: THE DARKNESS OF AN ANGEL
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
WhatsApp: +255621567672
Email: thomasibabuya@gmail.com
UMRI: 18+

SEHEMU YA TISA
“Taarifa za mwanzo uliniambia kwamba ni watu ambao walikuwa wanapora tu kwa ajili ya njaa, sasa inakuaje kwamba watu hao wasababishe hali kama hiyo kwenye taifa hili?”

“Kwa sababu tangu mwanzo sikuwa sahihi kuamini hilo, wale watu walikuwa ni zaidi ya hilo ambalo nililifikiria”
“Unamaanisha kwamba wale watu hawakuja kwa bahati mbaya?”
“Hilo ndilo jibu lake sahihi”

“Hawa watu ni akina nani, kwanini waje kwenye nyakati kama hizi na wao wanahusika vipi na hawa watu mpaka yeye ndiye ahusike kuweza kuwaua? Na taarifa mahali ambako wanatoka hawa watu yeye alizipatia wapi?”
“Hayo ndiyo maswali ambayo hata mimi najiuliza japo ninahisi baadhi ya vitu kadhaa kwenye hili”
“Nakusikiliza”

“Hii familia tunajua namna inavyofanya mambo yake, hawa watu walipotea kwa miaka zaidi ya ishirini kiasi kwamba walitafutwa mpaka serikali ikakata tamaa ya kuweza kuwatafuta na baadae wakaja kujitokeza wenyewe. Kurudi kwao hakukuwa kwema kwa sababu kulikuja na matatizo mengi ya kutisha ambayo hayakuwa na mwisho mzuri kwa taifa letu lakini baadae tena wakaja kupotea kwa makubaliano ikiwa na maana kwamba kwa wakati huu hawakuwa kwenye rada za kutafutwa na serikali.

Silaha kubwa ya hawa watu juu ya usalama wao ni usiri wa kuto tambulika kwamba wako wapi kwa wakati huo na wanafanya nini. Kama ingekuwa ni mauaji ya kawaida tu na wao hawahusiki basi wasingejisumbua kabisa kujiingiza kwenye hili hivyo wao kuingilia maana yake ni kwamba huenda kuna taarifa ambazo wanazo zinawahusu moja kwa moja na ndiyo maana wameamua kuja hadharani kwa mara nyingine tena jambo ambalo ni la hatari kuweza kutokea’’
‘Subiri kwanza, umesema kwamba wameamua kuja hadharani?”
“Ndiyo kiongozi”
“Kuua watu sio kuja hadharani Kai na wote tunalijua hilo, hizi habari za uwepo wao unazo wewe tu na vijana wako pamoja na mimi ambaye unanipatia muda huu”

“Hapana mheshimiwa haipo hivyo”
“Unamaanisha nini?”
“Othman alifanya mauaji ndani ya kasino ambayo alijua kabisa ina kamera kila kona na baada ya kukamilisha hilo akaondoka bila hata kuhangaika nayo, unahisi ni kwa bahati mbaya?”

“Kwamba alihitaji mamlaka ziitambue sura yake kuweza kuwepo pale?”
“Ndiyo”
“Oooooh shiiiit! Ni kweli wameamua kurudi kwa namna hii?”
“Iko hivyo na kama sio kijana wangu kuwahi pale pale ingekuwa ni tatizo kubwa”
“Kwanini anataka kutambulika hadharani namna hii?”
“Hii ni njia ambayo huwa wanatumia pale ambapo wanamtafuta mtu ambaye hawamjui”

“Unamaanisha kwamba huenda kuna mtu ambaye alisahaulika wakati ule ndo amerudi tena kwa sasa?”
“Sina uhakika na hilo, inawezekana ikawa hivyo lakini pia inawezekana ni mtu mpya amekuja kwa njia yake mwenyewe na huenda naye alikuwa anarusha karata zake gizani ili familia hiyo isije kutambua uwepo wake ili azipige hatua zake kimya kimya”

“Maana yake kama wakijuana kwamba wote wanawindana itatokea vita ya hadharani!”
“Ndiyo mheshimiwa”

“Unahisi ni nani anaweza kuwa anawatafuta na kwa sababu zipi?”
“Hili ndilo jambo ambalo limenifanya mimi kuja hapa usiku huu kuongea na wewe”

“Ukiwa una maana ya kwamba?”
“Inatakiwa hawa watu tuwapate mapema”
“Watu gani hao?”
“Familia ya Gavin Luca”
“Vipi Kai umechanganyikiwa au?”
“Nipo timamu na akili zangu zote hapa”
“Bila shaka ulikuwepo kule Morogoro na ulishuhudia yote ambayo yalitokea si ndiyo?”
“Ndiyo mheshimiwa”

“Unakumbuka kwamba ni wewe ambaye vijana wako wote walikufa ndani ya mitaa ya zamani ya Peenuga siku ile wakati lile eneo linalipuka si ndiyo?”
“Ndiyo mheshimiwa”

“Bila shaka uliona makubaliano ambayo mimi niliingia na ile familia si ndiyo?”
“Ndiyo mheshimiwa”

“Nadhani unaijua vizuri historia ya hii familia kwenye taifa hili si ndiyo?”
“Ndiyo mheshimiwa”

“Kwa hayo yote basi ni mtu asiye na akili pekee ndiye ambaye anaweza kuja kuniambia mimi nifanye jambo kama hilo. Siwezi kuruhusu ufanye jambo la namna hii kwenye taifa langu tena kwenye nyakati kama hizi ambazo wakati wangu unaelekea tamati, hili taifa limepitia mambo mengi ya kutisha mno sitaki kuwa sehemu ya kuliharibu kwa mara nyingine tena, yale ambayo yalitokea kipindi kile sitaki yaje kujirudia tena” raisi hakuwa tayari kabisa kuweza kufanya jambo kama hilo.
“Unaogopa kwamba hawa watu watakuua mheshimiwa?”
“Unahisi kwamba unaweza ukanilinda Kai?”
“Naweza kujaribu”

“Hahahaha hahaha, hivi unahisi kwamba mimi naogopa kufa?”
“Nisamehe kama nimeongea vibaya mheshimiwa”
“Nisikilize vizuri bwana Kai, ni jambo la hatari kuweza kuvunja ahadi ambayo ipo mezani na umeingia na watu wa namna ile, hili taifa wanaweza kulifanya wanavyotaka wao unajua kwanini?”
“Nakusikiliza mheshimiwa”

“Kwa sababu wale wana nguvu ya pesa na nguvu ya kummudu mtu yeyote yule. Wale wana pesa nyingi kumzidi mtu yeyote yule ndani ya hili bara na wanaweza kumfikia yeyote na kwa wakati wowote ambao wanataka wao hivyo kama kuna utofauti ukifanyika na yale makubaliano basi kuna vifo vingi vitatokea. Halafu kuna jambo ambalo nahisi haulifahamu ngoja nikwambie leo” mheshimiwa alivuta pumzi na kuhema kwa nguvu.

“Kwenye yale makubaliano tulikubaliana kwamba hatuji kuyavunja kwa namna yoyote ile na ndiyo maana yalifanyika kwa maandishi na ahadi ya Lionela ya mwisho kwangu ilikuwa ni kwamba kama ikija kutokea nikayavunja yale maandishi basi atakuja kufanya mambo ya kutisha zaidi ya yale ndani ya hili taifa, je huko ndiko ambako wewe unataka tulipeleke taifa?”

“Sina maana hiyo mheshimiwa”
“Sasa maana yako ni ipi hasa kama unataka kulazimisha familia hiyo ipatikane?”
“Bila hao maana yake itakuwa ni ngumu sisi kujua tunaanzia wapi, watu pekee ambao walikuwa wana uwezo wa kutupatia hizo taarifa ndio hao ambao wao wenyewe wamewaua, maana yake ni kwamba Othman hakutaka hizo taarifa zifike kwa mtu mwingine. Huoni kama ni hatari kubwa kwa taifa na tunajua kabisa kuna janga baya linakuja na hakuna kitu tunaenda kufanya mpaka kusubiri maamuzi kutoka kwenye familia moja kwa sababu tu imefanya mambo makubwa ndani ya hili taifa?” raisi alionyesha masikitiko makubwa akiwa anamwangalia bwana huyo ambaye ni kama alikuwa anajisahaulisha yale ambayo yalikuwa yametokea huko nyuma.

“Una uhakika kabisa upo kwenye akili yako?”
“Mpaka nakuja hapa maana yake sijaona jambo lingine la kuweza kufanya zaidi ya hili, tunapaswa kumpata Othman na kufanya hivyo maana yake ni kwamba tutajua hii familia nzima ilipo. Tukimpata huyu tutampa machaguo ya kushirikiana na sisi kwa lazima au tutumie nguvu kama inawezekana”

“Nenda kapumzike Kai nadhani siku ya leo umechoka sana” Raisi alimtaka kiongozi huyo aondoke huku naye akiwa anamshangaa raisi wake, sio kwamba hakuwa akiwatambua watu hao bali kwa nyakati ambazo walikuwepo hakukuwa na namna nyingine ya kuweza kufanya ili kuhakikisha kila kitu kinaenda sawa. Raisi alitembea hatua kadhaa lakini alisimama na kugeuka.

“Kai kama ikitokea ukapuuza amri yangu basi amini kwamba nitakufanyia jambo baya sana kwenye maisha yako” aliongea kwa msisitizo kuonyesha kwamba alikuwa akimaanisha yale ambayo aliyaongea na kutoweka akimuacha mkurugenzi akishangaana na anga.

Hawa watu wameanza kupishana wenyewe, ngoja tuone wanataka kutupeleka kwenye dunia gani.

Sehemu ya 9 sina la ziada tena.

Febiani Babuya.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom