Simulizi: Nisamehe mke wangu

gstar

JF-Expert Member
Jun 19, 2011
759
1,245
KIONJO!
Kweli nimeamini kuwa asali haionjwi, ni lazima utarudia tu kuionja mpaka utakapo imaliza yote na katika harakati za kuisaka asali iliyo bora ujiandae kung’atwa na nyuki.

Hayo ndiyo maswahibu yaliyomkuta Jamal Twaha (JT) kijana aliyepata mafanikio ya haraka ndani ya jiji la Dar es Salaam lakini baadaye akaja kuitelekeza familia yake kwa kutekwa na mchepuko!

Mwisho wa yote alikuja kugundua kuwa nyama ya bata ni nyama na ya kuku pia ni nyama japo kuwa zinaladha tofauti. Ndipo alipojirudi kwa mkewe.

JT alijikuta akijutia sana kukurupukia uji wa mgonjwa kwani aliutamani kwa sura na muonekano wake ila alipounywa akautapika kutokana na limao na chumvi iliyojazwa kupitiliza.

Mariam mkewe JT alivumilia yote bila kikomo japo kuna kipindi alikata tamaa lakini baadaye aliyasamehe yote bila kikomo na sasa anafurahia ndoa yake bila kikomo.

Ndugu msomaji ushauri wangu ni kuwa, unaposoma riwaya hii uache ile tabia ya kuzuia maji kwa kujenga ukuta kwani maji hufuata mkondo wake na hata kama ukijenga ukuta wa zege ama hakika utavunjika tu.

Hivyo penye kucheka cheka, penye kulia lia na penye funzo ujifunze pia. Ahsante na karibu sana.

SEHEMU YA 01 ---> Inaanzia kwenye comments
(Maoni ushauri 0719682352)
 
SEHEMU YA 01: FAMILIA INAKOSA MAELEWANO

FAMILIA ya Bwana na Bibi Jamal Twaha iliyokuwa inaishi katika eneo la Madale jijini Dar es Salaam ni moja kati ya familia chache zilizoonekana kuwa na maisha mazuri katika eneo hilo. Baba alikuwa akifanya kazi ofisi ya mkuu wa mkoa wakati mama akiwa ni mama wa nyumbani.

Mazingira ya nyumba yao yaliyozungukwa na ukuta wenye fensi ya umeme yalikuwa ni tulivu kabisa, pia nyumba yao iliyokuwa imezunguukwa na miti michache ya kupandwa na nyasi zilizokuwa na rangi yakijani ziliifanya hali ya hewa katika eneo lile iwe ni tulivu na ya kuvutia mno.

Hakuna mtu yeyote ambaye angeamini kuwa ndani ya familia ile kulikuwa na ugomvi mkubwa ulio pelekea wakati mwingine mume na mke wakae wakinuniana bila kuongea chochote. Ndoa ya Jamal ndio kwanza ilikuwa inatimiza miaka miwili na alijaaliwa kupata mtoto mmoja lakini kwa muda huo alikuwa akijiona kuwa hana mapenzi kabisa na mkewe na akijihisi kumchoka kabisa.

“Karibu mume wangu,” ndivyo bi Mariam alivyokuwa akimkaribisha mumewe kila alipotoka kazini lakini mumewe safari hii alipitiliza moja kwa moja mpaka chumbani na kujitupa kitandani akiwa na viatu vyake. “Nimekuandalia chakula mume wangu, na nilikuwa nakusubiri tuweze kujumuika kwa pamoja,” alisema Bi Mariam ikiwa inapata majira ya saa 4 na nusu usiku na kuambulia jibu moja tu, “mimi nimeshiba, unaweza kuendelea.”

Hata ilipofika usiku Mariam alijaribu kumpapasa mumewe lakini aliambulia maneno makali na wakati mwingine matusi.“Mume wangu geuka huku basi ujue nimekumisi sana, si unajua hii ni wiki ya pili sasa hujanipa dozi, nimekumiss mwenzio plizz,” Jamal au JT kama watu walivyopenda kumuita alijifanya kama hasikii na ndio kwaanza anakoroma usingizini. Wakati mwingine alimjibu kwa mkato, “nimechoka mkewangu si unajua kazi yangu ilivyokuwa ngumu, kesho nitakuwa sawa my dear, let me sleep just for today because am so tired!”

Asubuhi JT kama kawaida yake aliamka alfajiri sana na baada ya kupata kifungua kinywa aliingia kwenye gari yake aina ya Toyota Harrier na kudrive kuwahi kazini akiwa amemuacha mkewe na upweke mkubwa. Hali ile iliendelea kwa muda mrefu kidogo mpaka Bi Mariam akaanza kukonda kwa mawazo na afya yake ilikuwa dhaifu mno. Amakweli nyumba zinaficha mengi unaweza kuwaona watu wanafuraha sana kumbe moyoni mwao wameficha mambo mazito.
****
ITAENDELEA kwa sehemu ya 02---->
(Maoni ushauri 0719682352)
 
SEHEMU YA 02: HISTORIA YA JAMAL

JAMAL Twaha, alizaliwa huko mkoani Tanga wilayani Muheza katika kijiji cha Lusanga, wazazi wake wote wawili walikuwa ni wakulima. Mzee Twaha Akida baba yake Jamal alikuwa amejaaliwa kuwa na ekari kadhaa za michungwa na minazi, kiujumla maisha yao pale kijijini yalikuwa ni ya wastani.

Wakati Jamal anasoma katika shule ya Msingi hapo hapo kijijini aghalabu aliweza kuwasaidia wazazi wake shughuli mbalimbali za shambani, shughuli hizo zilichukua muda wake mwingi na kumfanya wakati mwingine kukosa masomo shuleni kutokana na kutingwa na shughuli za shambani. Hali hiyo ilimpelekea Jamal kushindwa kufaulu mtihani wake wa darasa la saba na hivyo kukosa nafasi ya kujiunga na elimu ya sekondari.

“Mwanangu kwakuwa umekosa nafasi ya sekondari wewe utakuwa hapa unisaidie katika shughuli za shamba na haswa, kusimamia mauzo ya machungwa na nazi kule shambani,” alisema mzee Twaha Akida. Jamal ilibidi akubali japo kwa shingo upande, lakini hata hivyo baada ya miaka miwili ya kukaa kijijini Jamal alijiunga na chuo cha VETA kilichopo mjini Tanga.

Jamal alipokuwa chuoni alijitahidi kusoma kwa bidii, akichukua masomo ya udereva. Waalimu wengi walivutiwa na juhudi zake katika masomo hata baadhi ya marafiki zake walimsifia kwamba anajituma sana katika masomo ya nadharia na yale ya vitendo mpaka wengine wakawa wanamtania utasikia wakisema “Duh yaani huyu kaka anavyopenda shule utafikiri ametumwa na kijiji!” Nikweli kuwa wapo waliokuwa wanamsema sana pia wapo baadhi ya wasichana ambao walikuwa ni warembo sana pale chuoni ambao walijaribu kujipendekeza kwake lakini waliambuliwa ‘kutolewa nje’ tena kwa maneno makali!

“Sikiliza Jeritha mimi nipo hapa chuoni kwa ajili ya masomo tu hayo mambo mengine yatafuata muda maalum ukifikia,” Jamal alimjibu msichana mmoja aliye shindwa kuvumilia na kumchana live kuwa amezimika kabisa na hajiwezi juu yake. Aliondoka Jeritha akiwa anaangalia chini kwa aibu huku akitafuna kucha zake. Vijana wenzake pale chuoni walimshangaa Jamal, “yaani mzigo unakuja mpaka geto halafu unaamua kuuchomolea sio bure huyu jamaa atakuwa si riziki.” Walisema baadhi ya marafiki zake walipomuona Jeritha akitoka chumbani kwa Jamal huku akiwa analia.

Licha ya Jamal kusikia kashfa za marafiki zake kibao pale VETA Tanga, yeye aliamua kushikilia msimamo wake kwamba hataki kupoteza nafasi yake adimu ya kumaliza chuoni akiwa amefaulu vizuri. Na ndivyo ilivyokuwa baada ya miaka miwili JT alihitimu masomo yake na kutunukiwa leseni ya udereva yenye daraja C. JT alifurahi na kukumbuka wanafunzi wenzake walivyo mcheka kwani wengine waliishia ‘kudisco’ au kubeba mimba zisizo tarajiwa! Huo ndio ulikuwa mwanzo wa mafanikio ya Jamal.
 
SEHEMU YA 03: JIJINI DAR ES SALAAM

JAMAL TWAHA ambaye baadaye alikuja kufahamika kama JT ni kijana ambaye nyota yake iling’aa kwa haraka sana. Ingawa alikulia katika maisha ya kijijini lakini alipoingia jijini Dar es salaam hakuna kilicho msumbua, alijikuta akifanikiwa kwa kila alicho kifanya. Kunawatu walisema kuwa anatumia kizizi au kuhisi kuwa anadawa fulani hivi.

JT alikuwa na sura ya kuvutia wasichana wengi walivutiwa naye ila yeye hakutaka kuharakisha maswala ya mapenzi. Kwake kazi ilikuwa ni muhimu zaidi na alijua tu kuwa ipo siku atampata ampendaye na kufunga naye pingu za maisha. Kwa muonekano wa nje Jamal alifananishwa na mwanamuziki wa kimarekani aliyeitwa Justin Timberlake, na ndio maana watu wengi walikuwa wakimwita JT.

Jamal hakuwa mtu wa kuchagua kazi, alifanya kazi za kila aina ili aweze kujikimu na maisha ya mjini lakini Mungu hamtupi mja wake Jamal alifanikiwa kupata kazi ya udereva wa daladala. Kwakuwa Jamal alisomea kozi ya udereva na kufanikiwa kupata Leseni ya daraja C ilikuwa ni rahisi kwake kupata kazi hiyo.

“Ndugu yangu Jamal wewe utaendesha hili gari mpaka pale utakapoona inatosha,” Jamal hakuamini ukarimu aliopewa na tajiri mmoja wa kihindi aliyeitwa Patel. “Yaani mtu hanifahamu lakini ananiamini kunikabidhi chombo!” alijisemea moyoni Jamal na kujibu kwa kauli moja tu, “ahsante ndugu yangu.” “Naona una wasiwasi usijali kwani nilipewa sifa zako na marafiki zangu uliowahi kufanya nao kazi, wamenipa sifa zako za ucha Mungu na nidhamu ya kazi nami nimekuamini na kukukabidhi gari hili ulitunze,” alimalizia Patel na kumkabidhi Jamal ufunguo wa garihiyo aina ya Eicher.

Walimalizana na Patel na kuanzia siku hiyo Jamal alikuwa dereva maarufu sana wa Daladala ndani ya jiji la Dar es Salaam, hakuna kondakta, dereva au askari wa barabarani ambaye alikuwa hamfahamu JT. Kuanzia vituo vyote vya mabasi kama Makumbusho, Mawasiliano, Mwenge na sehemu nyingi wote walimfahamu na haswa pia ilikuwa ni ule mfanano wake mkubwa na mkuu mpya wa mkoa wa Dar es salaam aliyeitwa David Adam Billy!

Hata siku moja haikusikika Jamal kukosana au kugombana na bosi wake yule mhindi aliyemkabidhi daladala, kama ni hesabu ya siku aliikabidhi inavyo paswa. “Bosi leo hali ilikuwa mbaya kidogo gari lilipata hitilafu kwahiyo… ehh?!” kabla hajamalizia mazungumzo kwenye simu utasikia Patel akimjibu tu kwa haraka,“oohh Jamal pole sana nimekuelewa usijali utapunguza kwenye hesabu gharama ya matengenezo ya gari hivyo usijali.” Kimsingi ni kuwa walielewana sana na bosi wake na hata siku moja hawakuwahi kukwazana. Jamal alitambua alipotoka hivyo alifanya kazi yake kwa uaminifu.

Taarifa za kuwa kuna kijana dereva wa daladala anayefanana na mkuu wa mkoa wa Dar es salaam ndugu David Adam Billy zilimfikia mkuu huyo wa mkoa. Hivyo mkuu wa mkoa alituma watu kufuatilia na kisha kupata mawasiliano ya kijana huyo. Sikumoja mchana JT alipokuwa kwenye harakati zake za barabarani alishangaa simu yake ikiita na namba ngeni kuonekana, ngrii! ngrii! Simu iliita ilimbidi kupokea ijapokuwa sio kawaida yake kupokea namba ngeni kwani mara nyingi huwa ni za wasichana wanaomsumbua wakitaka awenao kimapenzi.

“Hello, habari unaongea na mkuu wa mkoa ndugu David Billy, hivyo nilikuwa nahitaji kesho asubuhi tuonane ofisini kwangu bila kukosa…” “Eeh sawa, nani…?!” wakati JT anajiumauma simu ilikuwa imesha katwa hapo sasa mapigo ya moyo yakawa yanaongezeka.
****​
Jamal aliamka alfajiri mapema na kujiandaa kwakuwa ilikuwa ni siku ya Jumatatu alitaka kuwahi mapema kwa mkuu wa mkoa ili kama akirudi basi aendelee na shughuli zake kama kawaida. Alimjulisha kondakta wake kuwa atachelewa kufika kazini siku hiyo na hivyo amtafute dereva wa muda kwa siku hiyo.

JT alikuwa ni kijana anaye jali muonekano wake, kwa siku hiyo alivaa vizuri sana, suruali nyeusi ya kitambaa na shati jeupe lenye mistari ya bluu na mikono mirefu. Alichomekea vizuri na kwakweli alikuwa anapendeza sana. Alipo ingia pale ofisi ya mkuu wa mkoa maeneo ya Ilala boma jambo la ajabu lilitokea, kuna askari walikuwa wakimpigia saluti wakati wafanyakazi wa kada nyingine wakimpa ukarimu wa hali ya juu.

Ni kweli, Jamal alifanana sana na mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam ndugu David Adam Billy. Wote hawakuamini baada ya kumuona mkuu wa mkoa anakuja kumlaki JT kwa kumbatio, walikumbatiana na wote wakafurahi sana. Ilikuwa ni kama ndugu walio potezana kwa muda mrefu. “Mkuu huyu ni pacha wako? Nilimfananisha kabisa na wewe pale getini,” alisema yule askari aliyempigia saluti JT pale getini. “Ndio huyu ni ndugu yangu kabisa,” alijibu mheshimiwa Billy huku akitabasamu.

Kiukweli Jamal alikuwa na bahati sana, pamoja na kuwa hakusoma sana lakini mafanikio yake yalionekana dhahiri tangu alipo ingia jijini Dar es salaam. Hata pale mkuu wa mkoa alipo mpa ajira katika ofisi yake Jamal alibaki mdomo wazi. “Kuanzia sasa hivi achana na daladala, kazi yako itakuwa ni kumuendesha huyu afisa wa idara ya ardhi,” aliongea RC David Billy alipokuwa anamkabidhi JT kwa afisa ardhi huyo.

Na ndivyo ilivyokuwa JT akawa ameajiriwa, alifanya kazi kama dereva akihama kutoka kitengo kimoja kwenda kingine. Aliendesha magari ya aina tofauti kuanzia Toyota Harrier, VX, Prado na hata Land Cruiser. Mtaani hakuna aliyetambua kwamba magari hayo JT sio yakwake bali ni ya mabosi wake. Watu wengi walipomwona akibadilisha vyombo vya usafiri walijua kwamba yeye ndiye mmiliki halali wa vyombo hivyo, hali hiyo iliongeza yeye kufukuziwa na wasichana wenye urembo wa kila aina!

Baada ya kufanya kazi kwa muda wa mwaka mmoja JT alifanikiwa kujenga nyumba maeneo ya Madale na hivyo kuhamia katika nyumba yake. Alifikiria kuwa huo ndio muda wake muafaka wa yeye kutafuta mwenzi wa kufunga naye pingu za maisha, hata wazazi wake kule kijijini walikuwa wakimsumbua katika hilo pia, kila siku maswali ya utaoa lini yalikuwa hayawaishi midomoni mwao.
 
Naomba maoni yenu kwamba niendeleze hii hadithi ama niiache...
 
Msikopi na kusambaza hii kazi bila ruhusa yangu
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom