Simulizi: Mzimu wa waufi

Simulizi: Mzimu wa waufi

Abdallahking

JF-Expert Member
Joined
Mar 19, 2018
Posts
3,985
Reaction score
10,843
0.jpg



SIMULIZI HII IMEKAMILIKA
IMEANDIKWA NA : MAUNDU MWINGIZI
CHANZO : BURE SERIES


SEHEMU YA KWANZA

“Naitwa Hunudu, ni shefa mkuu katika Dini hii tukufu ya WAUFI, Dini hii inaongozwa na Wafalme wa Bahari, Wafalme wa Pande kuu za dunia, Dini yetu kama zilivyo dini zingine tunaongozwa kwa kuzingatia misingi ya Nidhamu, Adabu na Utii iliyoweka katika kitabu chetu ambacho ndio muongozo wetu wa Kiibada na shughuli zinginezo, Kitabu chetu kinaitwa HADHALUFI“ Maneno haya yalikua yakitamkwa na Kijana mmoja Mweupe, ana mwili wa wastani, alionekana ana jicho bovu(Chongo) kitu kilichofanya wajihi wake uzidi kuonekana ni wa kikatili sana, wakati huo akiyaongea maneno hayo Masumbuko alikua amesimama katikati ya Chumba hicho, huku kwa mbele akiwa amesimama kijana huyo mwenye jicho bovu aliejitambulisha kwa jina la Hunudu, pembeni mwa chumba hicho walikuwepo wazee kama watano hivi, wazee hawa walikua kimya muda wote wakati hunudu akiendelea kuoa maelezo
“Taratibu zetu ziko kama ifuatavyo, Hua tunakutana mara tatu kwa wiki. Siku ya Jumamosi ni siku yetu ya kufanya Ibada maalumu huku huku chini ya mapango ya Bahari, siku ya jumatatu ni siku maalum ya kutoa Kafara ya damu na Adhabu kwa yeyote atakaekiuka miongozo yetu ikiwemo kutunza siri, kutohudhuria ibada, kukataa kutoa kafara, nk, na siku ya alhamisi ni siku ya kutoa hukumu za makosa, na kusikiliza Shida, mashitaka mapya.” Maneno hayo yalizidi kumuogopesha Masumbuko na sasa alianza kuelewa kua yupo chini ya mapango ya baharini, hakujua ni kwa nini yuko pale, kwanini anapewa maelezo hayo ya siri, alikua akitetemeka mwili mzima. Kisha kijana huyu Hunudu mwenye jicho bovu akamshika mkono Almas na kumpeleka chumba kingine huko alikuta watu wakipewa adhabu kali za ajabu ajabu, alioneshwa watu wakikatwa Ulimi, wengine wakiokwa kama mikate, wengine wakipigiliwa misumari katikati ya vichwa vyao, Masumbuko akawa anatokwa na Machozi,
“Acha kulia we mtoto wa kiume, kua makini usije ukakiuka mashart yetu” alimkanya Hunudu
“Kwani nani kaniingiza kwenye hii Dini bila ya Idhini yangu?”
“Si umetaka mwenyewe hakuna aliekulazimisha” akafikishwa sehemu akashuhudia kijana mmoja akichinjwa kama kuku na damu yake watu wanainywa, akamuona Hunudu nae anachuku kibuyu maalum kisha anakinga damu ile nae anakunywa, kisha akakinga tena damu nyingine akampa Masumbuko nae anywe lakini Masu akakataa kunywa ikabidi hunudu amshike mikono yake na kuwaamuru vijana fulani wawili wamnyweshe damu ile ya binaadamu, Masu akajikuta anapiga kelele “NOOOOO..” Ghafla akashtuka, akageuka huku na kule, akajiona kumbe yuko chumbani kwake, alikiua naota, Ni Ndota ya ajabu sana ambayo hajawahi kuota hata siku moja, akiwa anahema kwa hofu kubwa mara mkewe nae akashtuka kutoka usingizi ikabidi amuulize mumewe kulikoni?
“Kulikoni, mbona hivyo”
“We acha tu mke wangu”
“Nini tatizo?”
“Nimeota Ndoto ya ajabu sana”
“Mmmh Ndoto gani tena?” akaanza kumuhadithia mkewe jinsi alivyoota, ilikua ni Ndoto ya kutisha sana mpaka mkewe nae akaanza kuogopa, ikabidi wakubaliane kua walale tu wataongea kesho lakini kila walipojaribu kulala ilishindikana, Usingizi haukupita kabisa mpaka asubuhi
“Pole mume wangu, ni Ndoto tu wala usiwaze sana”
“Mmmh haya mke wangu..”
“Na kama itakusumbua nitaenda kwa Mchungaji kumuambia aje kukufanyia maombi” walijaribu kufarijiana mtu na mkewe japo Masumbuko hakupenda kusikia masuala ya Kuombewa na Mchungaji kwakua yeye Imani yake ni ya Dini ya Kiislam ila mkewe huyu yeye ni Mkristo, na wamekua wakiishi pamoja kwa ndoa ya Bomani, basi wakaendelea kuutafuta usingizi mpaka asubuhi bila ya mafanikio na kulipopambazuka tu Masu aliamka na kwenda bafuni kuoga kwa ajili ya kujiandaa kwenda kazini, japo siku hiyo hakua na amani kabisa kila saa Ndoto ile ilijirudia kichwani mwake Lakini alijitahidi kujisahaulisha akaenda kazini na huko akaendelea na shughuli zake za kila siku pale ofisini kwao, Maisha yaliendelea vizuri bila ya kuota tena ndoto za ajabu kwa takribani wiki nzima na sasa alikua meshaanza kuisahau Ndoto ile ya kutisha
*****

WIKI MOJA BAADAE
“Tulikuambia kua wewe sasa ni mfuasi wa dini ya Waufi, haupaswi kuvunja kanuni zetu Lakini umeamua kwa jeuri kabisa kuvunja taratibu za wakuu wa Bahari na sasa utaadhibiwa” Hunudu alikua akimuambia Masu, wakati huo Masu alikua kidali wazi amesimama mbele ya kiti kirefu cheusi alichokalia mzee mmoja hivi mweusi ananywele nyingi kichwa, Nywele zikiwa zina mvi za mbali mbali, baada ya Hunudu kusema maneno yale, ikawa sasa ni zamu ya Mzee huyu nae kuongea, kaanza kwa kumuuliza swali Masu
“Una watoto?”
“Ndio Mkuu”
“Watoto wangapi na wa Jinsi gani?”
“Mapacha wawili, wa kiume na wa kike”
”majina yao?”
”Wakiume anaitwa Fani na wa kike anaitwa Zani” “Safi, sasa kwakua umevunja taratibu zetu kwa kosa la kutoa siri zetu za WAUFI kwa mkeo sasa tunakupa adhabu” Baada ya Mzee huyu kuongea kwa sauti yake Nzito nay a kukwaruza, akachukua kitabu kikubwa akampa Hunudu kisha Hunudu akakisoma kimya kimya na baada ya kukisoma akaniangalia Usoni na Kisha akasema
“Utatoa kafara ya damu ya mwanao wa kiume siku ya Jumamosi na kama utathubutu kufuata ushauri wa huyo mkeo wa kwenda kuombewa kwa huyo mchungaji tutakuongezea adhabu nyingine”
”Bora mniue mimi ila mwanangu simtoi, nasema simtoiiiii!!!” Kumbe Masu alikua tena usingizini, ndoto ile ilikua imejirudia tena, alipokua akiweweseka kwa kusema kua hamtoi mwanae ndipo Judith(Mkewe) akaamka
“Jamani nini tena mume wangu?”
“Waufi, waufiiiii”
“Umekuaje lakini, Waufi ndo nini?” Kabla hajajibu chochote alishtuka kutoka usingizini ndipo sasa kama fahamu zikawa zimekaa vizuri
“Ile Ndoto imejirudia tena, wanataka kafara ya damu kwakua nilitoa siri yao kwako”
“Nini?? Kafara?wamejuaje kama uliniambia chochote?”
“Ndio, yaani watu walewale niliowaota wiki iliyopita ndo wamenitokea tena, Haiwezekani, hebu nipe simu yangu nimpigie baba”
“Lakini saa hizi ni usiku mkubwa, angalia ni saa Tisa kasoro hii utawashtua sana nyumbani”
“Hapana siwezi kuendelea kuvumilia nipe tu niongee nao sasa hivi” Masu alikua amechanganyikiwa sana akainuka na kwenda chumbani kwa wanae kuwaangalia akawakuta wamelala, akarudi mpaka chumbani kwake na kuchukua simu yake, akaiwasha na kuanza kutafuta namba ya baba yake, akaiona kisha akabonyeza kitufe cha kupigia halafu akaweka simu sikioni
*****

WIMBO mashuhuri ulioimbwa miaka kadhaa iliyopita na Jabari la muziki marehemu Marijani Rajabu, wimbo uitwao ‘Mwanameka’ ulisikika ukivuma kwa sauti kubwa kutoka katika simu ya Mzee Kikoko ambao ameu Set kama wimbo wa kupokelea kwenye simu yake, muda huo ndo kwanza alikua akivuta shuka na kujigeuza upande wa pili, alikua katikati ya usingizi mzito, Laikini kutokana na usiku kua tulivu sana aliweza kuisikia simu yake na akaamka haraka kuangalia ni nani aliekua akipiga simu usiku ule, akaichukua simu yake na kuiangalia kwenye kioo haraka haraka alimtambua kua ni Mwanae Masumbuko “Hallow” ilikua ni sauti ya Mzee Kikoko, sauti iliyojaa mchoko wa usingizi na hofu
”Shikamoo Mzee”
“Marahaba, mbona usiku sana kuna nini tena?”
“Babanina matatizo”
“Matatizo, matatizo gani?”
“Yaani hata sijui nianzie wapi kukueleza,”
“Anzia hapo hapo, huko mbele nitakuelewa”
“Baba basi we lala tu mie kesho asubuhi nitapanda Buss nakuja huko nyumbani”
“Sasa ulinipigia simu ya nini?, niambie hata kidogo ni matatizo gani..” “nahisi kuchanganyikiwa Baba, Ni habari ndefu sana, nikija kesho tutaongea” Baada ya maelezo hayo akakata simu, mzee Kikoko akabaki na butwaa, alama ya mshangao ikajiandika moyoni mwake, Hakua na la kufanya,
Maana Angefanye nini hasa!!
Basi akaamua tu kulala lakini chango la uzazi liliunguruma hata usingizi ukakata alitaka kujua mwanae amekumbwa na jambo gani mpaka ampigie simu usiku mkubwa vile
*****

SIKU ILIYOFUATA
Katika stand ya Ibinzamata, Stand ya mabasi ya mkoa wa Shinyanga, majira ya saa kumi na mbili jioni alikua amesimama Mzee Kikoko na Mwanae mdogo wa kiume, akiwa ameenda kumpokea mwanae Masumbuko akitokea jijini Dar es Salaam. Mzee kikoko alionekana kutawaliwa na hofu kubwa na shauku ya kujua kinachomsibu mwanae huyo anaefanya kazi jijini Dar es Salaam katika kampuni ya Birimuye Holdings Ltd inayojishughulisha na huduma za kifedha katika mitandao ya simu, Kila akikumbuka jinsi alivyoongea nae kwenye simu alipokua akimtaarifu juu ya ujio wake huo wa ghafla alizidi kuamini kua kuna zaidi ya tatizo katika ujio huo wa Almas.. Baada ya kama saa moja hivi tayari Buss la Super Sonic Safar lilikua limeingia katika viunga vya stand hiyo maarufu mkoani hapo, Mzee kikoko akajisogeza taratibu mpaka karibu ya mlango wa Buss kwa ajili ya kumpokea Mwanae, haikuchukua muda mrefu akamuona Masumbuko akiteremka kutoka ndani ya Buss, akamsogelea na kumpokea Begi lake Jekundu
na kisha wakasogea pembeni kidogo ili wasalimiane
“Shikamoo mzee”
“Marahaba, mzima?”
“Mie mzima namshukuru Mungu”
“Enhee mmetembea salama?”
“Salama kabisa baba”
“Haya tukaangalie Tax sasa tuondoke” baada ya kujuliana hali wakatoka mpaka nje ya eneo hilo la Stand kisha Mzee Kikoko akamuita Dereva Tax akaanza kupatana nae Bei na baada ya mapatano wakaingia ndani ya gari, Masumbuko na mdogo wake wakiwa wameketi seat za nyuma na Mzee Kikoko akiwa ameweka kishoka katika seat ya mbele, Kama mjuavyo tena wazee wa mjini kwa mbwembwe, safari ya kwenda Mwasele nyumbani kwa Mzee Kikoko ikaanza, Haikua mbali sana kutoka Stand mpaka Mwasele japo ni ka hatua kidogo, na baada ya mwendo wa kama dakika arobaini dereva alikua tayari kaishapiga break mbele ya Nyumba ya matofari ya kuchoma iliyopigwa ‘plasta’ upande wa mbele tu, hapo ndipo nyumbani kwa mke mkubwa wa Mzee Kikoko ambae pia ndie mama yake Mzazi na Masumbuko. Mzee Kikoko ana wake wawili Bi Mkubwa anaitwa Kapemba Masanja, na mke mdogo ambae yeye anaishi maeneo ya Shaikom anaitwa Bi Mwajabu Fundikira. Baada ya kuwasili nyumbani hapo walitoka nje familia nzima
kuja kumpokea Masumbuko.dada zake na wadogo zake walionekana kufurahi zaidi kumuona tena kaka yao, hawakujua kama ujio huu ni wa matatizo. Ilikua ni furaha kubwa kwao kuonana na ndugu yao aishie jijini Dar es Salaam, nyumba ilikua imefurika ndugu mpaka watoto wa mke mdogo wa mzee Kikoko aishie Shaikom nao walikuja kumpokea kaka yao, ki ukweli Mzee Kikoko alijitahidi sana kuwaweka pamoja na kiupendo wanae wote na wake zake japo changamoto za wake wawili hazikosi ndani ya nyumba Haraka haraka Jogoo akakamatwa kwa ajili ya mgeni japo na family nayo ‘Itasafiria nyota” kama ilivyo kawaida ya uswahilini, na baada ya salamu mazungumzo yakaanza kwa swalila Kikoko ambae alionekana kua hana raha tangu jana yake “Enhee mwanangu, hebu tutoe jaka la moyo maana hatujalala tangu jana tunawaza tu umepatwa na nini”swali hilo la Mzee Kikoko lilimtoa machozi Masumbuko ikabidi atoe kitambaa chake laini aanze kufuta machozi, kitu kilichozidi kuacha maswali kwa
wazazi wake
“Sasa ukishaanza kulia badala ya kusema tatizo nini ndo tutakuelewaje?” alidakia mama yake
“Baba ni matatizo ya ajabu sana, sielewi ni nini hasa”
“Matatizo gani hasa?” Ndipo sasa Masumbuko akaanza kuwasimulia wazazi wake kuhusiana na kadhia inayoendelea kutalii na kutanabahi katika falme za ubongo wake kupia Ndoto, Ndoto ya ajabu!
“Yaani Ndoto tu ndo ikufanye Ulie, Ushindwe kulala, ufunge safari kutoka huko kote mpaka Shinyanga kuja kushitaki, we ni mwanaume wa aina gani?” Baada ya maelezo marefu kutoka Masu sasa ikawa zamu ya Mzee Kikoko ambae hakuonesha dalili za kuguswa na jambo hilo, aliongea kwa ukali na katika hali ya kumshangaa mwanae, ikabidi sasa mama yake na Almas nae aingilie kumtetea mwanae
“Hii sio hali ya kawaida mume wangu, hakuna haja ya kumlaumu Masu, hata mimi nimeshangaa sana tu”
“Ulichoshangaa wewe ni kipi hasa”
“Haiwezekani mtu aote Ndoto halafu iwe na muendelezo kama Tamthiliya tena huku akipewa tahadhari ya kile alichokifanya, Haiwezekani”

“Nyote mmekutana, Mama na Mwana sawa na Pipa na mfuniko tu, Ndoto ni ndoto tu hata uiote mara kumi, kwa hiyo we ukiota umepata pesa halafu baada ya kuamka usizione hizo pesa utaanza kuzitafuta chini ya Mto?” aliuliza Mzee Kikoko huku akisamama na kuashiria kua anaondoka zake, ikabidi Masu ajaribu kujielezea vizuri lakini Mzee Kikoko hakumuelewa na hatimae akatoka zake nje na kuwaacha mtu na mama yake wakifarijiana.
*****

Nje ya nyumba ya Mzee Kagomba, majira ya saa mbili za usiku walikua wamekusanyika watu wengi wakiwa wameketi huku wameizunguka meza ndogo ya mbao, wengi wa watu hawa walikua ni wazee mashuhuri kutoka maeneo tofauti tofauti ya mkoani Shinyanga, kama ilivyo Ada kila siku hukusanyika mahala hapo kwa ajili ya kupata kahawa ambayo ni sehemu ya Biashara zinazo msaidia Mzee Kagomba kujipatia Rizki, mbali ya kahawa Kikubwa zaidi kinachowafanya watu wengi kukusanyika pale na kuacha vijiwe vingine vingi vya kahawa si tu Ubora, usafi, na umahiri wa Mzee Kagomba katika kuiandaa kahawa hii Laa hasha Bali pia ni Mvuto wa Story za kila aina zipatikanazo maeno hayo, Kijiwe hiki cha kahawa kinafahamika zaidi kwa jina la BBC Kutokana na ukweli kwamba habari yoyote itakayotokea mjini hapo au hata nje ya mji huo iwe ya Kimichezo, kisiasa, kidini, nk basi lazima itaanza kufika hapo kabla hijazagaa kwingineko na wasimuliaji wa hapo ni mahiri kwa porojo sijapata kuona. Kila
mtu ni mjuaji kijiweni hapo na hakuna anaekubali kushindwa katika hoja yake, hata kama ukiwa hauna pesa ya kununu kahawa unaruhusiwa tu kwenda kupiga Soga na kama ukija na habari tamu na ya kusisimua basi utanunuliwa kahawa mpaka umalize kutoa habari hiyo.. Ilikua ni siku ya pili sasa Mzee Kikoko hajaonekana kijiweni hapo kitu ambacho si kawaida yake kupitisha japo siku moja bila ya kukanyaga ardhi ile ya Waswahili wa mjini, Wazee wenzie walikua wakiulizana kama mzee mwenzao amekutwa na jambo au imekuaje mpaka hajakanyaga pale!! Walikua wakimkubali sana kwa Story zake za Tambo na Porojo, Ikawa kama bahati wakati wanaendelea kumjadili nae huyo akawasili, kila mtu akafurahi, akapatiwa kiti na baada ya kuketi Mzee Kagomba akaanza kumtania
“We bwana haufi mapema hakyamungu..”
“Kwanini tena, au Izraeli kamchumbia mwanao?”
“Tulikua tukiulizana hapa hivi Mzee Kikoko amekufa na kuzikwa kimya kimya?”
“Utaanza kufa wewe, mimi utaniacha..”
“Haya hebu tujaalie hali ya Maungo yako..”
“Kwakweli mpaka tunaingia mitamboni hali yangu ni murua, naendelea tu kuvuta pumzi mwanana bila ya malipo” watu wote wakaangua kicheko kutokana na majibizano ya wazee hawa watundu wa maneno “Enhee mwenzetu ukapotelea wapi?”
“Ya kuacha tu, matatizo ya kila aina duniani hapa”
“Hebu tujuze, hii ndo BBC Lete maneno upate ushauri kutoka kwa mabingwa wa saikolojia waliosomea miembeni”
“Juzi alikua mwanangu Masu, lakini ujio wake haukua wa Kheri”..” “Enhee..”
“Kwanza kabla hajaja, alinipigia simu usiku mkubwa akiwa ametaharuki vibaya, nilijaribu kumtuliza anieleze tatizo lakini hakusema akaniambia kesho yake angepanda buss ili aje huku Shinyanga tuyaongee vizuri” Wazee wote pale kwenye Kahawa walikua kimya wakimsikiliza Mzee Kikoko
“Kesho yake sasa ambayo ni juzi ndo akaja na Buss nikaenda kumpokea stand kisha tukarudi mpaka nyumbani tulipofika nyumbani baada ya salamu na mazungumzo kidogo, nikamuuliza sasa anijuze tatizo lilikua ni nini hasa, cha ajabu mwenzangu akaanza kulia” Story ilionesha kuwatuliza masikio wadau wote pale, kisha baada ya kupiga funda moja la kahawa Mzee Kikoko akaendelea kutiririka na nyuzi
“Baada ya kumbembeleza aniambie tatizo, nikabaki mdomo wazi akaniambia kua Anasumbuliwa na Ndoto, anaota vitu vya ajabu vinamnyima usingizi na kumkosesha raha” Alipofikia hapo kijiwe kizima kilizizima kwa vicheko vya hali ya juu ikawa sasa ni kelele tu bila ya msikilizano…
“Amaa kweli ukiyastaajabu ya Mussa utayaona ya Firauni, yaani badala umrithishe mtoto mali we umemrithisha huo uoga wako na uzezeta..” maneno hayo yalikua ni ya Mzee Kagomba akimtani mzee mwenzie kisha wakacheka sanaa akadakia Mzee mwingine nae akasema
“Yaani mimi sijatulia ila Kikoko na mwane mmeshinda tuzo..“ Mzee Kagomba akadakia tena
“Waswahili wanasema Bata hata ale kokoto haachi kuharisha, mie nilijua una tatizo kubwa kumbe hujaacha tu maigizo yako“ wakati wakiendelea kucheka na kushangaa tukio hilo Mzee Kikoko hakumjibu mtu zaidi ya kuendelea kunywa kahawa yake, wengi walidhani ni mashara tu ya mzee huyu, na hapo ndipo ilisikika sauti ya Mzee Kapela aliekua muda wote kimya akivuta sigara yake taratibu, yeye akaja na Mpya
“Mie nadhani ni utoto unawasumbua tu, badala tumsikilize amalizie hiyo ndoto ninyi mnataka kutuharibia mjadala huu, Hebu Kikoko Endelea..” Bila ya ajizi Kikoko akaendelea kuwasimulia jinsi Ndoto ilivyomuanza mwanae ikiwa ni pamoja na vitisho alivyopewa, kilichowashtua wengi ni pale sasa Kikoko alipoanza kuwaelezea jinsi ile Ndoto ilivyoendelea pale ilipoishia siku ya kwanza ikiwa na wahusika wale wale, kila mmoja alistaajabu na sasa hali ya kijiwe ikatulia tena na kila mtu akaonekana sasa kuguswa na mkasa huu, na baada ya Kikoko kuhitimisha uwasilishaji wa hoja yake wadau wakaanza kutoa ushauri. Wengi waliendelea kusisitiza kua japo ni Ndoto ya Kushangaza lakini itakua ni Ndoto tu na haitakua na athari yoyote, Lakini Kagomba alikua tofauti na baadhi ya vijana pale, ye aliwaambia kua ile si Ndoto ya Kawaida na kawashauri waende wakamuone Mzee Maguno kwakua yeye ni mtaalamu wa kutafsiri Ndoto. Hali ile ya malumbano pale kijiweni iliendelea bila ya
kupata muafaka wa pamoja
*****

Baada ya siku mbili za kuwa pale Shinyanga, Sasa Masu alikua tena ndani ya Buss la SABENA Akirejea jijini Dar, Kichwani alikua bado anazungukwa na hofu, hafu ya kutokewa tena na Hunudu wa Waufi, mbaya zaidi alitegea kupata ushauri wa kitaalamu kutoka kwa baba yake lakini hali ikawa tofauti aliambulia maneno makali ya dhihaka tu akiambiwa kua ni majiamizi tu hayo yanamsumbua Hatimae jioni majira ya saa moja tayari Buss lilikua limeegesha ndani ya Stand ya mkoa Ubungo Buss Terminal, alipoteremka tu alienda moja kwa moja mpaa nje akavuka upande wa pili wa bara bara kule zinapopaki daladala za Ubungo to Gongo la Mboto akadandia hiyo ili ashuke Buguruni, alifanya hivyo na bahati nzuri hapakua na foleni ndefu hivyo hakuchelewa sana kwani ndani ya Dk kama 30 tu alikua ameshashuka katika kituo cha Buguruni Shelly na hapo akaanza kutembea tu kwa miguu kutokea hapo Shelly kwenda kwake maeneo ya kwa mnyamani anakoishi hivi sasa, haikua mbali kutokea hapo kituoni
Alipofika kwake alipokelewa na Mkewe Judith kwa shangwe na Furaha
“Karibu mume wangu..”
“Ahsante, habari za hapa?”
“Nzuri tu nyumbani hawajambo wote?”
“Hawajambo tu, vipi hawa(wanawe) hawajambo?”
“Nao wazima wako ndani wanaanda madaftari yao ya kesho shule” “Enhee nipe habari za huko, Baba uliongea nae? Na kasemaje?” Swali hili lilimuumiza sana Masu na alijisikia vibaya kumuambia mkewe kua baba yake hajampa ushirikiano wowote zaidi ya maneno ya karaha tu, lakini haina jinsi ilibidi amueleze ukweli tu!

*****
JIRANI na msikiti mkongwe wa Idrisa uliopo Kariakoo mtaa wa Tandamti Jijini Dar es Salaam kuna duka kubwa la vitabu vya dini linalomilikiwa na Sheikh Jabu ambae mbali ya kuishi Dar es Salaam pia ana mke mwingine Tabora hivyo kufanya makazi yake kua sehemu mbili, Lakini pia Sheikh Jabu mzawa wa mkoani Kigoma, watu mbalimbali kutoka mikoa ya Kigoma na Tabora hufanya duka hilo kama vile sehemu ya kukutania na jamaa zao wa huko mikoani kirahisi kwa kua wengi wanapafahamu dukani hapo, pia Dukani hapo ni sehemu iliyozoeleka hata kwa wenyeji wa hapa jijini Dar es Salaam kama ni sehemu maarufu ambayo kila siku watu hukusanyika mida ya jioni kwa ajili ya kubadilishana mawazo, hua kuna mijadala mizito na malumbano ya hoja katika Nyanja tofauti toauti hasa Siasa, dini, michezo na uchumi Masumbuko nae hupendelea sana kwenda dukani hapo kupiga stori, Alipazoea dukani hapo kwakua mara kwa mara Baba yake Mzee Kikoko akija Dar hupendelea kwenda pale kupiga story na
wazee wenzie hasa wa Kigoma pia Mzee Kikoko ni rafiki kipenzi wa mmiliki wa duka hilo Sheikh Jabu, Hivyo basi kutokana na umaarufu na usemaji wa Mzee Kikoko ikamfanya Masu nae akajikuta anafahamika sana Dukani hapo, Siku moja baada ya kutoka kazini kwake aliamua kwenda pale dukani kusikiliza habari za mjini lakini pia alikua ameweka nia kua kama atapata fursa ajaribu kuwadokezea kuhusu ile Ndoto yake maana hakika pale dukani ilikua ni uwanja wa wajuvi wa mambo, Lakini siku hiyo pale dukani hapakua na watu wengi, alikuapo muuzaji wa vitabu na Mzee mmoja kutoka kigoma ila nae kwa sasa anaishi pale Dar, anaitwa Mzee Kishindo, mzee huyu nae hua ni mtu wa maneno sana na hua ni rafiki pia wa Mzee Kikoko mara nyingi kikoko akija Dar hua karibu sana na Mzee huyu, ndipo Masumbuko akaona sasa acha achokoze kuhusu lile tatizo lake na ile Ndoto ya Ajabu
“Mzee Kishindo samahani”
“Bila samahani mwanangu”
“Mie nina swali,,”
“Kaswalie msikitini, hapa hakuna udhu” wakajikuta wamecheka wote “Hapana sio swala, nina jambo nataka kukuuliza”
“Anhaa kumbe una suala, haya uliza”
“Suala hilo linahusu Ndoto” baada tu ya Masu kusema hayo maneno mzee Kishindo akatabasamu kisha akanena
“Unanikumbusha taaluma yangu niliyosoma miaka karibu thelathini iliyopita, taaluma waliyopewa Mitume na manabii”
“Kumbe tatizo langu litakua limepata ufumbuzi”
“Ndoto sio tatizo mwanangu, ni ishara muhimu na dalili zilizojificha za jambo Fulani ambalo ujumbe wake unaupata kupitia Ndoto, na kama utazifanyia kazi hautopata tabu ila ukizipuuza utajuta, utajikuta unahangaika kila siku, utayalaumu Maji machungu kumbe mdomo wako ndo una homa” Masu alikua akicheka kwa vionjo vya maneno kutoka kwa Mzee huyu,
“lakini ziwe Ndoto kweli isiwe njozi zenu umelala haujaoga wala haujala sasa jinamizi linakukaba mpaka ufizi halafu unataka tukutafsirie ndoto yako tutawezea wapi!!!” Mzee alikua na maneno sana huyu mpaka sasa Masu akajikuta anaishiwa cha kuongea ikabidi tu ajitahidi kumrudisha kwenye mada
“Mie kuna ndoto hua inanijia, ndoto ya kutisha sana, cha ajabu hua inajirudia kwa kuendelea pale ilipoishia”
“Mmh,Hiyo kweli Ndot, enhee uliotaje?” Masu akaanza kumuhadithia mzee Kishindo kuanzia siku ya kwanza alivyoota kuhusu Dini ya WAUFI na jinsi anavyosumbuliwa na Hunudu, akaendelea kumsimulia mpaka ilipojirudia tena ndoto ile, ilikua ni hadithi ya kusisimua na kutisha, wakati Masu anaendelea kuongea wakaingia tena watu wawili nao wakawa wanasikiliza habari ile iliyoonekana kuwaingia sana lakini cha ajabu Masu akiwa anaendelea kuongea Mzee Kishindo alikua anacheka mpaka machozi ikabadi sasa Masu aache kwanza kusimulia, na alipoacha tu ndipo Mzee Kishindo akadakia
“Dini ya Waufi?”
“Ndio inaitwa dini ya Waufi, mbona unacheka sasa?”
“Hakuna dini ya Waufi mwanagu hapa duniani”
“Mzee usibishe, Mimi ndie nilieota, na wameniambia mambo yahusuyo dini yao hiyo karibu mara nne usingizini”
“Hata wangekuambia mara mia lakini ujue hakuna Dini inayoitwa waufi”
“Kwahiyo ni nini sasa?”
“Ulishamueleza baba yako juu ya kadhia hii?”
“Ndio nilienda mpaka Shinyanga kwa suala hili lakini kama unavyomjua Mzee Mwenzio, hakuna alichonishauri cha maana zaidi ya kuniambia kua naweweseka na majinamizi tu, akaniambia niwe nasali kabla ya kulala tu basi”
“Ha ha ha aha, baba yako anajaribuKuficha moto sasa moshi utamuumbua”
“Kivipi tena Mzee Kishindo?”
“Nina uhakika kua Kikoko anajua kila kitu juu ya tatizo lako, au pengine amesahau, na kama amesahau basi amesahau kitu muhimu sana, na asipokua makini tatizo hili litakutesa na hata kukuua kabisa”
“Mbona unanitisha Mzee, Kitu gani tena?”
“Unajua sababu ya wewe kuitwa Masumbuko baada ya kuzaliwa? Maana kwenu hakuna babu yako hata mmoja aliwahi kuitwa jina hilo”
“Hapana siijui” Mzee Kishindo akacheka tena kisha akaendelea
“Tatizo lako ni kubwa sana, na pia ni dogo sana kama litawahiwa, kama litawekwa wazi bila ya kuogopa athari zitakazotokea, najua baba yako anaogopa athari za kuliweka wazi tatizo hili, ila kama utakua na ‘kifua’ nitakueleza na kukusaidia nini cha kufanya japo itahitaji muda, pesa na subra”
“Nisaidie mzee, niko tayari kwa lolote”

**MNH! Haya...Atasaidika???
ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA PILI

“Tatizo lako ni kubwa sana, na pia ni dogo sana kama litawahiwa, kama litawekwa wazi bila ya kuogopa athari zitakazotokea, najua baba yako anaogopa athari za kuliweka wazi tatizo hili, ila kama utakua na ‘kifua’ nitakueleza na kukusaidia nini cha kufanya japo itahitaji muda, pesa na subra”
“Nisaidie mzee, niko tayari kwa lolote”
“Una kifua??, sio hicho kidali kama bao la kuchezea kamari, Kifua cha kutunza kila aina ya maumivu?”
“Ndio, ninacho”
“Lakini sio leo, uje nyumbani kwangu siku ya ijumaa, kwanza nitakupa historia yaw ewe kuitwa Masumbuko kisha nitakupa maana ya Waufi, na kisha tutaanza safari ya kukupeleka Umamani kwenu milima ya Unyanyembe huko” Mzee Kishindo alikua anaongea huku akicheka sana, Masu alibaki njia panda, hakujua ni nini alichokielewa mzee huyu, ni nini ambacho mzee kikoko anakificha, Waufi ni nini kama sio Dini? nk lakini ikabidi tu sasa akubaliane na mzee Kishindo kua wataonana Siku ya ijumaa Baada ya mazungumzo yale, tayari Masu alikua ameshaingia hofu hivyo hata hakukaa sana na kwakua tayari duka lilikua limeshaanza kujaa wapiga porojo, ikabidi aage na kuondoka zake mpaka barabarani ili akapande daladala ya kumrudisha nyumbani kwake, akiwa amesimama kituoni anasubiri gari ghafla kuna gari ilikuja na kusimama kwa mbele, ilikua ni gari aina ya Verosa, kioo kikashushwa mpaka chini na kumfanya aonekane vema mrembo aliekua akiendesha gari hiyo, dada huyo alikua amevaa
Tshirt nyeusi na kofia ya kufuma ikiwa na rangi kama za wale Marasta, baada ya Masu kukutanisha macho na dada huyu akatoa mkono na kumuita kwa Ishara, lakini masu kila alipomuangalia dada Yule hakumtambua ila sura kama ilikua ikimuijia, ikabidi asogee tu kumsikiliza
“Mambo” alianza Dada Yule kwa kumsalimia Masu
“Poa, mzima?”
“Mzima tu hujanijua?”
“Hebu nikumbushe kidogo” Masu akajifanya kutabasamu kama kamjua kidogo
“We si ni Masu wa pale Mtaa wa Nyamwezi kwa wale ma Agrigator wa Mpesa”
“Naam ndio mimi, ofisi yetu inaitwa Birimuye”
“Sasa hunijui mimi kweli au unajifanyisha tu nawe!? “
“Sura inaniijia lakini sina kumbukumbuku za uhakika”
“Mie hua ni wakala wenu hua mnaniuzia Float”
“Aaah, nimekujua si unajua tena hua tunawahudumia watu wengi mpaka tunasahau, samahani wangu” Masu alijifanya kumjua lakini ukweli ni kwamba hakua akimkumbuka kabisa
“wala usijali, unasubiri gari za wapi?”
“Za buguruni”
“Haya ingia nikusogeze mpaka ilala, mie hua ndo nakaa pale”
“Ok ahsante nashukuru” Masu akaingia ndani ya gari kisha gari ikaondoka, ndani ya gari kulikua na kijana mwingine aliekua amekaa seat ya nyuma, ikabidi Masu ageuke ili amsalimie, Alipogeuka tu moyo wake ukalia ‘Paa!’ alishtuka mno, mara mapigo ya moyo yakabadilika, hofu ikazidi kutanda, alitamani ardhi ipasuke aingie, hapo hapo akatamani amwambie Yule dada amshushe haraka lakini akashindikana akahisi kama vile Mdomo ujeaa maji, jasho likawa linamfumka mwili mzima. Kijana huyo alikua ni kijana mweupe alievaa Tshirt nyeupe na kofia nyekundu, Masu alijitahidi kuvuta picha kua amemuona wapi kijana huyu, naam Kumbukumbu zake hazikimdanganya, ni kweli alimjua haraka kijana Yule.. Alikua ni Hunudu wa dini ya Waufi, na alimjua zaidi kutokana na ‘Chongo’ jicho buvu, Masu alichanganyikiwa sana kuona sasa yule kijana ambae hua anamsumbua usingizini kwenye ndoto kwa kujisifia kua nikiongozi wa dini ya Waufi leo amemuona ana kwa ana, Sasa alianza kuamini
kua ile si Ndoto ya kawaida, akaanza kukumbuka maneno ya Mzee Kishindo, akiwa bado anatafakari nini cha kufanya mara gari ikawa imefika maeneo ya Ilala bungoni ikakatiza upande wa kulia kwenye kile kibarabara kidogo kinachochepuka kule kilipo chuo cha habari kisha ikasimama pembeni halafu Hunudu akamshika mkono Masu na kumsalimia, Masu alikua akivuja jasho la woga na hofu
“Hali yako kaka Masu”
“HUNUDU!!!!?” Masu aliuliza swali kwa wahka wa hali ya juu sana
“Ndio mimi, kumbe una kumbukumbu sana!!,”
“Yaani umeamua kunifuata mpaka huku duniani?”
“Kwani hua tunaonanie mbinguni?” baada Hunudu kujibu vile wakacheka wote Hunudu na yule dada aliekua akiendesha Gari , ikabidi Masu amuangalie vizuri dada Yule maana aligundua kua nae ni lazima atakua ni mfuasi wa Waufu tu, wakati Masu anamuangali dada Yule huku Hunudu akaendelea kuongea
“Punguza hofu na woga”
“Shida yako nini hasa kwangu?”
“Mimi sina shida yoyote kutoka kwako zaidi ya kuja kukukumbusha mambo kadhaa”
“Mambo gani?!!” “Kwanza tambua popote uendapo na sie tupo, hauwezi kutukimbia, pili tulikukanya usitoe siri zetu hukusikia ukaenda kumuambia mkeo ukapewa adhabu ya kutoa kafara, ukakataa kumtoa mwanao, tukakuacha lakini sasa umeenda kutoa siri mpaka kwa watu baki tena huna hata woga, hivi haujipendi kijana?” Masumbuko alikua akitetemeka, mwili wake kama umeganda jinsi alivyokua katulia,
“Sasa sikiliza Masu leo usiku nitakuijia ukanywe Damu na pia uingizwe rasmi katika kitabu cha kumbukumbu ya wafuasi wa Waufi pia utamtoa Mwanao mmoja kama kafara yako, ukileta tena upuuzi sasa tutakua kinyama, naomba usiniangushe” Baada ya Hunudu kuongea maneno yake yaliyojaa vitisho vikali dhidi ya Masu, haraka Dereva ambae ni Yule dada akafungua mlango wa mbele na kumuambia Masu ateremke ili wao waondoke, Masu akateremka kwenye gari kama aliemwagiwa maji ya jinsi alivyoroana kwa jasho lake mwenyewe, aliposhuka tu mlango ukafungwa halafu Yule dada akamchombeza kwa kimombo
“Tutaonana usiku” halafu gari akatembea Masu alikua amechanganiyikiwa akaenda mpaka mbele huku kwenye Bara bara ya Uhuru akaiita bodaboda ikamchukua mpaka kwake
“Tsh ngapi unanidai”
“Elfu tatu tu kaka mkubwa” Masu akaingiza mkono mfukoni hata hakuhoji kwanini iwe pesa yote ile kutokea ilala tu hadi buguruni kisha huyo akaanza kuingia zake kwake
“Kaka mbona haujachukua chenchi?” Dereva wa boda boda alimkumbusha Masu lakini naona hata hakusikia yeye akawa anawahi tu kwake alipoingia ndani akamkuta mkewe yuko pale uwani akifuafua ngua za watoto, akapita bila hata ya salamu mpaka chumbani, ile hali ikamshangaza sana Judith nae ikabidi amfuate Chumbani
“Kuna nini mume wangu?”
“Ni bora nife tu sasa?”
“Ufe kwanini tena jamani?Hebu niambie kuna nini?”
“Ile ndoto kumbe sio ya kawaida kabisa”
“Imekuaje sasa?” Judith alijaribu kumshawishi sana Masu ili amuambie kilichotokea lakini Masu akawa anaogopa kumuambia akijua kua Waufi wanamuona, baada ya Judith kumsumbua sana ikabidi sasa amuambie tu ukweli wa mambo kuanzia yale maelezo ya kutatanisha aliyoambiwa na Mzee Kishindo halafu akamsimulia jinsi alivyomuona Hunudu uso kwa macho. Judith alipigwa na Butwaa na sasa badala amfariji mumewe yeye ndo akawa amechanganyikiwa mara mbili ya Masu mpaka Masu akawa sasa almanusura awe chizi,
“Mume wangu haiwezekani, hili jambo zito mie naenda kwa Mchungaji Jofrey kumueleza jambo hili”
“Hapana, acha tu”
“Siwezi kuacha, ni bora ukaombewa maana wamesema usiku wanakuja tena” Masu alikua akikataa kuombewa na Mchungaji kwakua yeye ni muislam japo Judith yeye ni mkristo na hata ndoa yao walifungia Bomani tu, Masu alijua kua endapo Baba yake atasikia kua ameombea na Mchungaji itakua kasheshe lakini kwa ushawishi aliopewa na Judith akajikuta amelainika, na Judith akaenda mpaka kwa mchungaji na kumueleza kila kitu, baada ya mchungaji kumsikiliza vya kutosha akakubali kua wafuatane mpaka nyumbani kwake na Judith ili mchungaji akamuhudumie Masu pale pale Nyumbani.. Walipowasili walimkuta Masu akiwa ameketi chini kabisa kwenye kapeti, Mchungaji akamshika mkono na kumuinua kisha akamkalisha kwenye Sofa lake dogo halafu akaanza kusema nae, lakini kabla hajaanza kuongea nae chochote Mchungaji akamuomba Judith awapishe wazungumze, Judith akatoka kasha Mchungaji akaanza..
“Pole sana Bw Masu”
“Ahsante Baba Mchungaji” Masu alikua akijibu kwa utiifu, kwakua maji yalikua yameshamfika shingoni ikabidi tu amtii Mchungaji japo sio dini yake hiyo “Kuna jambo nataka kukushauri kijana”
“Ndio Mchungaji..”
“Najua Hunudu anakusumbua sana mpaka unakosa raha” Maneno haya ya Mchungaji yalimshtua kidogo Masu akawa anajiuliza kua huyu mchungaji kamjuajea Hunudu? Lakini akajipa moyo kua huenda Judith kamsimulia kila kitu, akaendelea kumsikiliza bila ya kumjibu chochote “Lakini usimlaumu sana, hata yeye pia ametumwa na Viongozi wakuu wa Waufi hivyo inabidi atekeleze maalekezo aliyopewa, hata lile jicho lake Bovu alitobolewa na viongozi hao zamani kabisa alipokua akiambiwa atoe kafara ya damu akawa hataki, hata yeye nilimshauri kua akubaliane nao tu japo alinipinga sana hatimae akatobolewa jicho na kafara akatoa, sasa nawewe nakushauri mapema kabla hujaumia, Toa kafara hiyo wanayoitaka na utakua salama vinginevyo utaumia na kafara utatoa tu utake usitake” Masu alisimama ghafla kwa uoga baada ya kusikia maneno mazito kutoka kwa Mchungaji akawa hajitambui sasa, akaanza kusikia kizunguzungu akajikuta ameropoka
“Mchungaji sikuelewi kabisa”
“Utanielewa tu, hata mimi pia ni Mfuasi wa Waufi na ukiendelea kujidanganya kutukwepa utaangamia, Acha kabisa kutoa siri zetu kwa Mkeo na kwenye vijiwe vya kipuuzi, hakuna atakae kusaidia huko” Masu hakuamini maneno yale aliyokua akiyasikia kutoka katika kinywa cha Mchungaji, Mtumishi wa Mungu anaeaminiwa sana, akaona sasa hana ujanja, ni kweli anaangamia, akaanza kusikia anaishiwa nguvu, kizunguzungu kikamzidia na ghafla akaanguka chini kama kifurushi na kupoteza fahamu pale pale
*****

BAADA ya Masu kuanguka chini na kupoteza fahamu, mkewe alishtushwa na mlio wa kishindo kizito uliotokea pale seating room ikabidi haraka akimbilie ndani kuangalia kuna kitu gani, alipofika pale ukumbini alipigwa na butwaa, akabaki kama Msukule au mwintunge kwa lugha ya kwetu baada ya kukuta Mchungaji akiwa amesimama anaendelea na maombi wakati huo Masu yuko chini amepoteza fahamu, Judith hakumuuliza kitu mchungaji akaenda mpaka pale chini huku akitetemeka akaanza kumtingisha na kujaribu kumuamsha lakini haikuwezekana, Judith akaanza kulia huku akimuuliza Mchungaji
“Imekuaje tena jamani Mchungaji”
“Mumeo ana mapepo, nimeyakemea sana yakamzidi nguvu na kumuangusha chini akapoteza fahamu” Mchungaji alikua akijibu kwa utulivu huku akijiamni sana lakini Judith alikua amechanganyikiwa sana akawa anaendelea kulia mpaka wapangaji wenzake wakasikia nao wakaja chumbani na kumkuta Judith akiwa amemuinamia Masu huku akilia wakati huo Mchungaji alikua amefumba macho akionekana yuko katikati ya Maombi, Kilichowashangaza wapangaji wenzao ni kile kitendo cha mchungaji kumuombea Masu wakati wanajua kua Masu ni muislamu, Lakini kwa hali ilivyokua wakashindwa kuhoji sana zaidi ya kujadili tatizo na kutafuta ufumbuzi mapema..

Baada ya majadiliano ya muda mrefu kati ya Judith, Mchungaji, na wapangaji wenzao wakakubaliana kumpeleka Masu hospitali haraka, hivyo mmoja kati ya wapangaji wale akaenda kutafuta Tax kisha akarudi nayo mpaka pale nyumbani wakambeba Masu mpaka kwenye Tax na safari ya kuelekea Hospitali ikaanza, Ndani ya Gari seat ya nyuma alikua amekaa Judith na Mchungaji wakiwa wamembeba Masu, na Seat ya mbelea alikua amekaa mpangaji mwenzie na Masu walikwenda mpaka Amana Hospital iliyopo Ilala na walipofika haraka mchungaji akaenda ndani kuongea na Dokta na baada ya muda wakaja manesi wakiwa na Machela zao, wakasaidizana kumtoa Masu kwenye Tax akiwa hajitambua na kumuweka juu ya machela kisha akapelekwa mpaka ndani kwa Dokta..

Baada ya kutoa maelezo Dokta akaanza kumpa huduma ya kwanza, na kisha akapelekwa Wodini kulazwa, wakiwa Wodini Judith akakumbuka suala muhimu kua alikua hajamuambia mtu yoyote juu ya tatizo lile, akafungua mkoba wake akatoa simu ya Masu kisha akaiangalia namba ya Mzee kikoko na kumpigia alipoweka simu sikioni alisikia ujumbe huu “Asante kwa kutumia mtandao wa Vodacom, simu yako haiwezi kukamilishwa kwa sasa tafadhali ongeza salio na upige tena” Simu haikua na salio, Akainuka na kutoka nje kwenda kutafuta vocha..
Baada ya kununua vocha na kuijaza katika simu ya Masu akampigia Mzee Kikoko
*****

Akiwa nje ya nyumba yake kwa mke mdogo maeneo ya Shaikom akiendelea na shughuli zake za kupalilia majani huku akifagia fagia ndipo Mzee Kikoko akasikia kwambali kutokea chumbani kwake wimbo wa Jabari la Muziki Marijani Rajabu ukivuma na upepo akajua kua ni simu yake inaita, akatupa jembe na kwenda kuchukua simu, alipofika na kuiangalia aliona kua ni namba ya Masu akapokea kwa uchovu
“Hallo”
“Baba shikamoo” Kikoko akashtuka kusikia sauti ya mwanamke kutoka kwenye simu ya mwanae, haijawahi kuokea hata siku moja Masu akampa simu mkewe ampigie baba yake, japo tayari Kikoko alikua amekwisha ing’amua sauti ya Juddy lakini bado alishangaa tu maana hakua na mazoea ya kuiwasiliana na Mkwe wake huyo kwakua kwanza hampendi kuliko maelezo kutokana na suala la utofauti wa Dini kati ya Masu na mwanamke wake huyo, lakini akaitikia na kujiulizisha kama vile hajamjua..
“Marahaba, we nani?”
“Mie mama zani?”
“Mhuu kuna nini?”
“Baba, hali ya Masu ni mbaya sana, Masu anaumwa sana, amezidiwa na amepoteza fahamu hapa tumemleta Amana hospital”
“Amepoteza fahamu? Ilikuaje kwani?” Maneno haya ya Mzee Kikoko yalipenya sawia katika ngoma za masikio ya Mkewe mdogo aliekua Uani nae akaenda mpaka chumbani kusikiliza kinachoendelea, Mzee Kikoko alikua akimsikiliza Judith kwa makini sana kupitia simu yake nyeusi aina ya Nokia
“Leo Masu alikuja nyumbani akiwa anatetemeka sana huku akiwa kama amechanganyikiwa”
“Nikamuuliza kulikoni?, akaanza kunisimulia yaliyomkuta akaniambia kua alienda kule dukani kwa shekhe jabu akakutana na mzee mmoja ni rafiki yako wewe…”
“Anaitwa nani huyo mzee?”
“Anaitwa Mzee Kishindo..”Mzee kikoko kusikia jina la mzee kishindo sasa hofu ikamvaa lakini akajikaza
“Enhee ikawaje?”
“Masu akamuelezea huyo mzee kuhusu hii ndoto yake inayomsumbua, ndipo huyo mzee akampa maelezo mengi kuhusu hiyo ndoto yake na akamuambia kua yeye anakijua kinachomsumbua na akamuahidi kua atamsaidia, baaada ya Masu kuondoka pale dukani akiwa njiani ghafla akatokewa na yule kijana ambae hua anaemuta kila siku na kuanza kupewa vitisho..”
“Nini?Yaani huyo anaemtokeaga kwenye Ndoto akamuona njiani?”
“Ndio baba”
“Haya makubwa sasa..Ikawaje sasa?”
“Baada ya kupewa vitisho vingi wakamuacha, ndipo Masu akaja nyumbani akiwa amechanganyikiwa ndo mie nikaenda hapo jirani kwa Mchungaji Jofrey akaja kumuombea lakini wakati anamuombea mapepo yakapanda akapoteza fahamu ndio mpaka sasa tupo hospitali” Maelezo hayo yalimtoa jasho mzee Kikoko, hakuamini kila anachoambiwa..
“Hivi we mtoto ni Shetani?” Judith akapatwa na mshangao kusikia maneno hayo, ikabdi akae kimya kidogo
“Naongea na wewe, we ni Shetani? Aliekuambia ulete wachungaji kwa mwanangu ni nani? ”
“Lakini baba mie kosa langu ni nini wakati mtu alikua amepatwa na matatizo?”
“Aliekuambia kua Masu anatibiwaga na Wachungaji ni nani?”
“Lakini baba mie sikufanya kwa nia mbaya”
“Amaa kweli nimeamini Mchawi ni binadamu, Paka anatumwa tu, Kumbe wewe na Mzee Kishindo ndio mnanirogea mwanangu halafu mnajifanya kuwaleta hao wachungaji, sasa nakwambia hivi nataka Masumbuko apone Laa sivyo utakiona kilichomfanya kuku aanze kuota manyoa mkiani, Mie ndio Alwatan Kikoko” Baada ya mkwara huo mzito Mzee Kikoko akakata simu halafu akageuka nyuma ili aondoke ghafla akakutanisha macho na mkewe mdogo ambae alikua nyuma yake muda wote aliokua akiongea na simu
“Kwani kimetokea nini Baba Masu?”
“Naenda kwa Mama Masu..”
“Lakini hujaniambia kuna nini?”
“Tutaongea nikirudi” Kikoko akatoka ndani mule akamuacha mkewe huyu akiwa amesimama, cha ajabu huyu mwanamke akacheka kisha akasema kwa sauti ya chini
“Kama ni haki yangu Mungu atanilipia hapa hapa duniani”

Haraka haraka Kikoko akadandia baiskeli yake almaarufu kama Mkulima na kuanza kupiga pedeli kuelekea Mwasele kwa mkewe mkubwa mama Masu, Njia nzima alikua akimfikiria Judith kwa nini anampelekea mwanae wachungaji wakati anajua fika kua Masu ni muislamu, pia alikua akimuwazia Mzee Kishindo basi kwa kweli kichwa chake kilikua kimevurugika haswaa.. Baada ya kutembea umbali wa haja tu hatimae alikua amefika nyumbani kwake akateremka juu ya baiskeli na kisha akapita wima pale uani bila hata ya kusalimia
“Baba Masu kuna usalama kweli?” aliuliza mama Masu huku nae akisimama na kumfuata mumewe ndani
“Hakuna Usalama..”
“Kuna nini tena mbona hivyo?” wakati huo tayari baba Masu alikua ameshaingia chumbani na mama Masu nae alimfuata huko huko ndipo sasa Mzee Kikoko alipoanza kumsimulia Mama Masu kila kilichotokea mpaka mama Masu nae akabaki mdomo wazi
“Si nilikuambia Baba Masu, ile sio ndoto ya kawaida we ukawa unanipuuza?”
“Huu si wakati wa kulaumiana tena Mama Masu”
“Mguu umeshaota Tende ndo unakua muungwana sio, kwahiyo na huyo Mzee Kishindo na kamwambia nini sasa Masu?”
“Tena ngoja, umenikumbusha” Mzee kikoko akatoa simu yake na kumpigia Mzee Kishindo
“Asalamu alaykum Bwana Kikoko”
“Hakuna cha Salama leko hapa, hivi unanitaka nini na maisha yangu we Kishindo?”
“Hebu punguza spidi kwanza kaka, kuna nini hasa”
“Nipunguze spidi ya nini? Reli haina bamzi mie nakuja moja kwa moja nieleza ni kiherehere gani kilichokutuma kwenda kumueleza upuuzi wako Masu mpaka umesababisha amezidiwa na kulazwa?!”
“Masu amelazwa?”
“Usiniulize hilo swali mimi, nakwambia hivi kama umemroga mwanangu kesho nakuja kupambana na wewe nataka nikute amepona”
“Hivi Kikoko uko timamu kichwani wewe? Mie nimroge mwanao wa nini? Au unajifanya humjui anaemsumbua mwanao, sasa kama we ni jemedari na una nguvu sana kwanini usimdhibiti huyo aliesababisha yote hayo? Yaani unahangaika kukinyoosha kivuli wakati uliopinda ni mti?”
“Nitolee maneno yako ya kibaradhuli mie Afirit minal Jinni wewe, nakwambia nitaanza na wewe hayo majungu uliyoyapika utayapakua uyale mwenyewe kesho nikifika”
“Bwana Kikoko utamaliza kuni kwa kuchemsha mawe, huna utakalonifanya mie” Kikoko alikata simu kwa hasira, mkewe alijaribu kumliwaza lakini Kikoko alikua tayari ameshajaa jazba
“Jiandae Kesho asubuhi tunakwenda Dar”
“Mmh, Sawa”
****

AMANA HOSPITAL
Katika WOD No 5 kitanda kama cha nne hivi kutokea mlango wa kuingia alikua amelazwa Masu, kitandani alikuwa amezungukwa na watu kadhaa akiwemo mkewe Judith, wanae wawili wadogo Zani na Fani, pia alikuapo Mr Johaiven Kitale ambae ndie Boss wake na Masu katika kampuni yao ya Birimuye, Matibabu yalikua yakiendelea vizuri tu, na sasa Masu alikua ameshapata fahamu lakini hakua na uwezo wa kuongea sana, pia alikua akilalamika kua anasikia kizunguzungu na mwili hauna nguvu kabisa, lakini pamoja na matatizo yake hayo yote alikua akifarijika kwa ukarimu na upendo unaoupata kutoka kwa Mkewe, japo Judith alikua akimuhudumia Masu kwa moyo mmoja na kwa upendo lakini alikua na hofu kubwa kufuatia vitisho alivyopokea kutoka kwa baba yake Masu, hasa kila akiufikiria ujio wa Baba mkwe wake huyo alizidi kuingiwa na baridi ya hofu mwili,
*****

Majira ya saa kumi na mbili na nusu asubuhi, tayari Mzee Kikoko na mkewe Mama Masu tayari walikua ndani ya Buss la Raha Leo ambalo tayari lilikua limeshaanza kuuacha mji wa Shinyanga kuelekea Dar es Salaam, Kikoko alikua ametinga Kaunda suti ya rangi ya udhurungi na mkewe nae alikua amevaa baibui la ukaya la rangi nyeusi na mtandio wa kahawia, kama ungebahatika kuiona sura ya Mzee Kikoko lazima ungeangua ucheko maana alikua anaonesha dalili za ushari na alikua akitamani hata gari lifike Dar muda ule ili akapambane na Juddy na Mzee Kishindo ambao ndio anaamini kua ni wabaya wake..

Baada ya safari ya masaa takribani kumi, tayari gari lilikua limeshaegesha ndani ya STAND YA MABUSS YA Dar es Salaam, UBUNGO. Kikoko na mkewe walikua wakiteremka kutoka ndani ya gari, hawakua na mizigo mingi isipokua ni begi moja tu waliloweka nguo zao, kwakua kikoko hakua mgeni Dar mara kwa mara alikua akija Dar alikua akifikia nyumbani kwa Sheikh Jabu na kijiwe chake kikuu akiwa ni Dar ni pale Dukani mtaa wa Tandamti, wakatoka mpaka nje ya stand kisha wakapanda daladala mpaka Kariakoo, wakateremkia kituo cha Msimbazi karibu na Shelly kubwa ya mafuta ya Big Bon, haikua mbali sana kutoka Hapo kituoni mpaka Mtaa wa Tandamti ambako ndipo lilipo duka la sheikh Jabu, Lengo lake apite kwanza pale ili kama atamkuta Mzee Kishindo aanze nae kabla ya kwenda Hospital

Bahati haikua yake baada ya kufika Dukani alimkuta kijana mmoja, ambae ndie hua muuzaji wa vitabu na Mtu mmoja aliekua amevaa kanzu nyeupe na kilemba chekundu
“Mzee Kikoko karibu” Muuza duka alimpokea kwa furaha Kikoko kwa kua alikua akimfahamu
“Ahsante haujambo?”
“Sijambo, Shikamoo” kijana Yule akampokea begin a kuliingiza dukani
“Marahaba, habari za hapa?”
“Aaah nzuri, poleni na safari”
“Aaah hatujapoa, hivi kabla ya yote huyumzee Mshindo leo hajafika leo hapa?”
“Sasa hivi ametoka hapa ameenda Hospital kuona Masu”
“Anhaa, Saafi, ngoja nimkute huko huko, hilo begi utaenda nalo nyumbani kwa Sheikh Jabu mie nikitoka Hospital niatenda moja kwa moja nyumbani”
“Haina tabu, lakini Mzee Kikoko kuna jambo nataka kukushauri”
“Jambo gani tena”
“Huyu mzee hapa ni Sheikh wetu na hua anajua sana kuwasomea wenye matatizo kama ya Masu sasa kwanini usiende nae huenda Mungu akasaidia”
“Sawa tu ni wazo zuri, maana tayari nasikia wameshampelekea Eti Mchungaji akamuombee, nakwambia leo huyo mwanamke atanitambua” Baada ya maelekezo hayo ikabidi Kikoko amsogelee Sheikh Mwinyigoha na kumsalimu, na baada ya mazungumzo mafupi walikubaliana kwenda wote hospitali, waondoka wote, Sheikh Mwinyigoha, Kikoko na mkewe wakaongozana barabarani kwenda kupanda daladala ya kuelekea Ilala(Amana Hospital)

Haikua kazi kubwa kwa alwatan Kikoko kupata sehemu ya kupandia Daladala, alikua akiijua vema mitaa hii ya mjini utadhani yuko Shinyanga, wakaenda mpaka barabara ya Uhuru na kupanda Daladala zinazokwenda Tabata Segerea na kwaku hapakua na foleni kubwa siku hiyo basi ndani ya dakika kadhaa kikokoko alisikika akimuambia konda
“Shusha Amana hapo” ni kweli ilikua tayari gari imefika kituo cha amana, Kikoko alionekana kuyajua vema maeneo ya mjini, konda akagonga Bodi na gari ikazua upande wa kushoto mwa barabara, Kikoko na mkewe pamoja na Sheikh Mwinyigoha wakateremka huku kwa mkwara Kikoko akawa amemshika mkono mkewe ili amvushe barabara upande wa pili ambako ndiko iliko hospital, Kweli Wazee wa mjini wana mambo. Kwakua tayari Kikoko alikua ameshapewa maelekezo ya Wodi alikolazwa mwanae wala hakupata shida akaenda mpaka kwenye korido kuu ya kushoto na kisha akaanza kuianga WODI No 5, muda mfupi akawa ameiona akajielekeza huko, mkewe akiwa nyuma akimfuata, muda wote huo walikua hawaongi kitu chochote, Naam wakaingia WODINI
*****
ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TATU

Kwakua tayari Kikoko alikua ameshapewa maelekezo ya Wodi alikolazwa mwanae wala hakupata shida akaenda mpaka kwenye korido kuu ya kushoto na kisha akaanza kuianga WODI No 5, muda mfupi akawa ameiona akajielekeza huko, mkewe akiwa nyuma akimfuata, muda wote huo walikua hawaongi kitu chochote, Naam wakaingia WODINI
*****

Akiwa anamnywesha uji Masu ghafla moyo wa Judith ulifanya ‘PAAA’ Baada ya kukutanisha macho na Mzee Kikoko akiwa na mkewe pamoja na Sheikh Mwinyigoha, miguu ilianza kumtetemeka kwa hofu masikini dada wa watu, Kikoko alipomuangalia Judith alijisikia kama anataka kupasuka kwa hasira, akaenda mpaka pale kitandani alipofika wala hakuuliza akamnyanyua Juddy na kumsukumia pembeni mpaka uji ukamwagika
“We mchawi nilikuambiaje? Nataka mwanangu apone haraka Nguruwe we”
“Baba mbona hivyo lakini, mbaona mnaninyanyasa sana?” Juddy alilalama na hapo hapo mama Masu sasa akamdaka nae
“Hivi umeona kumroga mwanangu haitoshi mpaka umletee hao wachungaji wako si ndio?” wakati hayo yanaendelea Masu alikua anajisikia vibaya sana kuona Judith anadhalilishwa kwa kosa ambalo si lake akashindwa kujizuia akataka kuinuka pale kitandani ili akamzuie Mama yake ambae tayari alikua amemkwida Juddy, ndani ya Wodi pakawa na kelele na zogo mpaka wagonjwa wengine wakawa wapatwa na mfadhaiko, lakini alipotaka kuinuka tu akazuiliwa na Sheikh Mwinyigoha ambae alikua ameshamsogelea pale kitandani na kuanza kutaka kumsomea dua
“Tuli kijana, unataka kufanya nini sasa?”
“Sheikh, wanamuonea bure tu huyo mwanamke”
“Yote umeyataka wewe”
“Kivipi Sheikh?”
“Kama ungetunza siri za waufu unadhani yangefika huku? Na hata hivyo unabahati umemkuta Hunudu hiki kipindi ametulia vinginevyo saa hizi angeshakutia kilema wewe” Masu alishtuka sana akaanza kutetemeka, hakuamini kabisa maneno ya Sheikh Yule, inaonesha Sheikh huyu anajua kila kitu kuhusu Dini ya Waufi, Masu alitamani baba yasogee karibu ili amsikie huyu shekhe aliekuja nae lakini ilikua ngumu maana muda huo Kikoko na Mkewe walikua wakimshambulia Juddy
“Sasa we na Shekhe au ni mfuasi wa Waufi? Masu alipouliza swali hilo Shekhe Mwinyigoha alicheka sana kisha akamjibu
“Mimi ni mfuasi wa huyo hapo..” Mwinyigoha alisonta kwa kidole chake uswa wa mlango wa kuingia kwa Dokta, Ikabidi Masu ainuke ili amuangalie ni nani, ile kuinua macho yake hivi akamuona mtu akiwa amevaa mavazi ya kidaktari amesimama kule mlangoni, ikabidi Masu amuulize Shekhe Mwinyigoha
“Kwani ni nani huyo?”
“Acha mzaha Masu inamaana we hujamjua huyo? Hebu muangalie vizuri” Masumbuko akajiinua tena na kuangali vizuri TOBAA! Macho ya Masu yakakutana na HUNUDU akiwa katika mavazi ya kitabibu
“Nooooooooo..” Masu alipiga kelele huku akisimama pale kitandani, Hamad!! Mzee Kikoko akarudi mbio mpaka kitandani na kumshika mwanae
“We una nini hasa?”
“Baba, ni Hunudu huyo kaja mpaka huku, tuondokeni haraka” alijibu Masu huku akilia
“Yuko wapi?” Masu akageuka ili amuoneshe baba yake lakini ghafla hakumuona tena hunudu
“Baba hata huyu Shekhe wako nae ni Mfuasi wao” baada ya kusema hivyo tu Masu akatoka mbio na kumponyoka baba yake, akatoka mpaka nje ya Wodi na kutokomea kusikojulikana

“Sheikh imekuaje tena na wewe?”
“Mmh Mzee inaonekana mwanao ana matatizo makubwa, sasa kila mtu yeye anamtuhumu tu” Mzee Kikoko na mkewe wakachanganyikiwa wakamuacha Sheikh Mwinyigoha akiwa amesimama Wodini wao wakatoka kumtafuta Masu
*****
*****

KUFUATIA taharuki ile pale hospital iliyoletwa na Mzee Kikoko na mkewe, hakuna aliebaki mule wodini baada ya Masu kutoka mbio. Judith alitoka na kukimbia, Mzee Kikoko na Mkewe mama Masu nao waliondoka bila hata ya kusemeshana na yule Shekhe waliokwenda nae pale Hospital, haikujulikana Masu amekwenda wapi walijaribu kumtafuta bila mafanikio mpaka usiku ikabidi tu sasa Mzee Kikoko na Mama suma warudi tu mwananyamala kwa Seikh Jabu ambako ndiko walikofikia na kulala ili kesho yake waendelee kumtafuta tena Masu, Sheikh Jabu hakuwapo pale nyumbani alikua safarini Tabora lakini siku hiyo alikua ndio yuko njiani anarejea Dar hivyo Mzee Kikoko hakua na mtu wa kuongea nae sana juu ya kadhia iliyomkumba mwanae Lakini kwakua familia nzima wanamfahamu na wanamchukulia kama mwanafamilia pia hivyo haikua tatizo kwake, ikawa ni yeye na mkewe tu chumbani
“Baba Masu nakuambia hivi hata huyo shekh Mwinyigoha mimi simuamini kabisa”
“Hapana, sidhani kama atakua ni mtu mbaya itakua tu ni kweli Masu amechanganyikiwa sasa”
“Mie najiuliza muda wote ule alikua anaongea nae nini pale kitandani mpaka akapiga kelele?”
“Masu Atakua tu amechanganyikiwa maana haiwezekani kila mtu kwake awe ni sijui Waufi ila kesho itabidi niende pale dukani nikamuulize yule kijana juu ya huyu shekh”
“Mmh ananitia hofu sana, haya”

Huku Buguruni nako Judith alikua peke yake Chumbani analia tu kama mwehu, alikua akiuumizwa sana na matatizo yanayoendelea kutokea ndani ya familia yake na Masu, alikua hata hajui Masu atakua wapi muda ule wa usiku, kama atakua mzima au Laa, na zaidi kila alipowafikiria wazazi wa Masu walivyomzushia kua kamroga mtoto wao ndio kabisa alihisi kuchizi lakini hakua na Jinsi zaidi ya kumuomba Mungu amuoneshe njia, nae alilala tu bila matumaini huku akitia nia kesho yake kwenda kumtafuta hovyo hovyo mumewe
*****

Saa kumi na moja alfajir Mzee Kikoko aliamka kwa ajili ya kusali kama ilivyo kawaida yake, akatoka nje kwa ajili ya kuoga na kujiandaa na swala, hakutaka kwenda msikitini aliamua tu kua ataswali pale pale nyumbani, Alipomaliza kuoga akatoka mpaka pale uani ndipo akamuonaSheikh Jabu akipigwa mswaki akamsogelea na kumsabahi
“Assalamu alaykum”
“Owhoo bwana Kikoko waalaykum salaam, habari za Shinyanga?”
“Nzuri tu Sheikh, nawe za Tabora huko?”
“Huko hawajambo, poleni tu na matatizo?”
“Aaah bwana hivyo hivyo tupo nayo”
“Nasikia umekuja na mama Masu..”
“Ndio, yuko ndani humo bado amelala”
“Vizuri nitamsalimia kukipambazuka, Enhee nasikia tena ikawa mambo ya aibu huko Amana hospital… kunani tena mzee mwenzangu?”
“Unajua Yule mwanamke wake na huyo Masu ni mpuuzi sana, pamoja na Kishindo nae ndo wale wale, hapa hata mwanangu sijui yuko wapi” Kikoko alianza kufunguka sasa, Sheikh Jabu akaona yatakua makubwa ikabidi amkatishe
“Sasa mi nadhani tukaswali kwanza halafu we ukapumzike tu kasha tutaonana kule Dukani ndo tutaongea vizuri”
“Haya hakuna tabu” Kikoko akaingiachumbanikwake, huku nyuma Sheikh Jabu alikua amechia tabasamu la mamba huku akimuangali alwatan Kikoko akiingia chumbani kwake

Baada ya swala tu Shekhe Jabu hakukaa tena akaondoka zake nakuelekea mjini alikua na miadi na mtu maeneo ya dukani kwake Kariakoo, lakini Kikoko yeye alirudi kulala akivuta muda kupambazuke vizuri ili baada ya kupata ‘Istiftahi’ yaani kifungua kinywa ndipo nae aende kwanza dukani akaongee na Sheikh Jabu halafu zoezi la kumsaka Masu lianze
*****

Majira ya saa nne asubuhi tu tayari duka la Sheikh Jabu lilikua limefurika, wengi walikua wameenda kuzungumza juu ya balaa liliotokea jana yake kule Amana hospital maana tayari taarifa zilkua zimeshafika pale, na kwakua Jabu hakuwepo Dar hivyo kila mmoja alifurahi kuonana na kuzungumza na Sheikh Jabu, muda si mrefu Mzee Kishindo nae aliwasili pale dukani akapokelewa vizuri na Sheikh Jabu na baada ya kuketi tu nae akaanza kuwapa mchapo kuhusu mikwara aliyopigwa na Mzee Kikoko juzi yake kupitia simu, Sheikh Jabu alikua akicheka mpaka machozi
“Unajua Yule Bwana Kikoko hua simuelewi kabisa yaani anazeeka na upuuzi wake ha ha ha..” alichombeza sheikh jabu
“Nakwambia jana ungemuona alivyoingia hapa na ule mustache wake kama AmrishPul ungepasuka mbavu” wakati wadau wakiendelea kupashana habari za udaku na ufyetere ghafla kwa mbaali akaonekana Alwatan Kikoko akivuka barabara na kuja usawa wa dukani
“Jamani Kikoko huyo anakuja..”
“Hebu badilisheni mada msije kutuletea songombingo hapa” wadau wakajifanya wanajadili suala la Katiba mpya anayoendelea kuandikwa huko Bungeni, Naam Kikoko akawasili

“Karibu Alwatan Kikoko..” Sheikh Jabu alimpokea
“Shukrani.. Assalamu alaykum”
“Waaleykum salaam, karibu uketi hapo kwenye kiti chako cha uvivu” wakati anasogea kwenye kiti akakutanisha macho na Mzee Kishindo
“Hapana nimeghairi, wala sikai tena kuna Mchawi humu ndani”
“Acha mambo yako bwana Kikoko mchawi gani tena?”
“Si huyu Kishindo, ninyi hamjamjua tu kua ndie anaemroga mwanangu huyu?”hapohapo Mzee Kishindo uzalendo ukamshinda akajibu
“Tafadhali bwana Kikoko naomba heshma iendelee kujizungusha katika mhimili wake”
“Kwahiyo we ni kidume sana? Haya inuke tupambane”
“Naam mie ni Kidume tena Rijali haswaa, na ni baba wa Watoto watato”
“Mpuuzi mkubwa wewe mwanaume mzima unajisifia kua na watoto watano, njoo kwangu uone timu ya mpira, na leo bora nimekukuta hapa unieleze sababu za kumroga mwanangu halafu wewe huyo huyo unajifanya eti utamsaidia”
“Mie nimroge mwanao kwa lipi? Leo unajifanya humjui mchawiwako eeeh?Au nimwage mchele kwenye kuku wengi?”
“Mwaga huo mchele, Kuku wakiula basi nawao usiku tutawala kwa wali, mzandiki mkubwa wewe”
“Sikia bwana Kikoko, mie ni mtu mzima sasa hizo hila na shari unazonitafuta nimeshazijua kitambo kirefu tu ila kaa utambue kua Chiriku mzee hakamatwi kwa makapi..”
“Unajifanya muungwana sasa baada ya kulikoroga, kwahiyo ulizikaanga Bisi halafu unataka kuwaachia wenye meno watafune si ndio? Sasa nakwambia hivi utanionesha alipokwenda mwanangu mwanga mkubwa wewe, Laa sivyo humu leo hatoki mtu kama Airtel money”
“Tafadhali bwana mkubwa chunga ulimi wako, Kumbuka kua Cheche huchoma msitu na ulimi uliponzakichwa, jambo dogo sana unalolidharau lizaweza kukuletea madhara makubwa katikamaishayako..”
“Utanifanya nini wewe? Mie ndio Alwatan Kikoko nitakuhamisha mji huu”
“Debe tupu halichikutika, najua siku zote debe likiwa halina kitu ndani yake basi hata likidondokewa nakitu kidogo kamap punje ya haradani litapiga kelele tu ila debe lililojaa hata unga laini wa azam halitotoa kelele hata ulipige teke, sasa we Debe tupu endelea kupiga kelele tu”
“Unaleta dharau sio? Ngoja nikuoneshe..” Kikoko akavua mfuko mdogo aliokua ameuning’iniza begani ili amvae sasa Mzee Kishindo, yaani Kikoko alikua amejawa shari mwili mzima, watu wote dukani walikua kimya ikabidi sasa Sheikh Jabu aingile kati
Jamani wazee wenzangu hebu muogopeni mungu, angalieni sasa mnajenga picha gani kwa vijana wadogo hawa mbele yenu!!” Kwakua Kikoko hua anamuheshimu sana Sheikh Jabu akashusha pumzi kidogo kasha Seikh Jabu akaendelea
“Wahenga wanasema Chungu kidogo huwahi kuchemka wakati chungukikubwa huchelewa kuchemka wakiwa na maana kua Kichwa kidogo kwa maana ya uchachewa hekma , busara, na maarifa huwahi kuchemka hata kwa mambo madogo tu, sasa wazee wenzangu mnashindwa kutumia hekma zenu kulimaliza jambo hili bila tafrani ukizingatia umri wenu umekwenda sana na wanasemakua ukimuona NyaniMzee ujue kakwepa mishale mingi sana”
“Kwahiyo Sheikh Jabu unamaanisha haya mambo ni madogo wakati mie mwanangu amerogwa na tayari nimeshambamba mchawi wangu ukizingatia mpaka sasa sijui mwanangu amepotelea wapi” alidakia tena Kikoko
“Hapana sina maana hiyo, nina maana ya kwamba kwa tatizo hili ilikua vema mkakaa kama watu wazima nakulimaliza, naamini katika maisha mmeshakutana na changamoto nyingi kuliko hii”
“Mie siwezi Kukaa na huyu fatani na hasidiwa maisha yangu”
“Usiseme hivyo bwana Kikoko kumbuka kua Dhoruba iliko ndiko shwari iliko bimaana kua wagombanao ndio wapatanao, lazima tuliongee na limalizike kwa salama jambo hili”
wakati Sheikh Jabu akiendelea kuwanasihi wazee wenzie kwa mbali wakasikia wimbo wa Mwanameka ukitokea katika Mfukowa Koti wa Mzee Kikoko, ilikua ni simu yake ikiita alipoitoa akaona ni namba ya Masu, mojakwa moja akajua ni Mke wa Masu tu huyo
“Enheee hongea upese na wewe mchawi namba mbili”
“Baba shikamoo” Ilikua ni sauti ya Masu
“Marahaba, we Masu uko wapi?”
“Niko kwangu”
“Ulikua wapi tangu jana sie tunakutafuta”
“Nililala nyumbani kwa Boss wangu”
“Nakuja huko sasa hivi” Mzee Kikoko akakata simu kasha akatoka bila hata ya kumuuaga mtu yeyote na kuanza kuelekea kwa Masu,
Huku nyuma aliacha gumzo kubwa na vicheko vya hali ya juu kwa wadau pale dukani japo Mzee Kishindo alionekana kutokuana furaha kutoka na majibizano yale
****

BUGURUNI KWA MNYAMANI

Masu alikua amejilaza kitandani akionekana ni mwenye mchoko wa hali ya juu huku kichwa chake akiwa amekilaza juu ya miguu Mkewe Judith, halafu kwa pembeni walikua wamekaa watoto wao wawili mapacha Zani na Fani ambao hawakuelewa chochote kinachoendelea kutokana na udogo wa umri wao,
“Yaanimimi nahangaika hivi na wewe halafu wazazi wako wananitukana na kunidhalilisha mbele za watu kiasi kile..”
“Nisamehe mimi mke wangu, wala usiwalaumu wale, uzee umeshawaingia”
“Hapana ni bora nikakuacha uendelee kuishi na wazazi wako kwa amani kuliko haya mateso nayoanza kuyapata, yaani wananiita mimi mchawi”
“Judith yaani uondoke kisa Baba yangu? Kama mimi na wewe tumependana hakuna wakututenganisha zaidi ya Mungu, kumbuka mwanzo wakati tunataka kufunga ndoa ya kiserekali alinikataza na kunitishia kunitolea radhi lakini niliongea nae na yakaisha sembuse hili”
“Haya kwanini na jana ukakimbia hovyo a ukenda kulala kusikojulikana? Una jua mie nilibaki katika hali gani?..” wakati wanaendelea na mazunngumzo wakasikia sauti ya mlango ukigongwa

“Ngo! Ngo! Ngo!..”
“Ngo! Ngo! Ngo!..”

Judith akainuka kitandani na kwenda kufungua mlango, alipofungua tu akakutana na Sura ya Alwatan Kikoko akiwa amenuna vibaya
“Karibu baba” Kikoko hakujibu kitu akaingia mpaka ndani na kumkuta Masu akiwa amejilaza pale kitandani
“Karibu mzee”
“Ahsante” Kikoko akavuta kistuli karibu na kitanda alichojilaza Masu halafu akakaa nae, hapo hapo Zani na Fani wakamsogelea Babu yao na kumkalia miguuni. Mazungumzo yakaendelea
“Enhee unajisikiaje?
‘Naendelea vizuri kiasi”
“Mwanangu umeamini kinywa cha mzazi hakitoi harufu mbaya bali kinatoa maneno ya Baraka?”
“kivipi Baba?”
“Wakati unataka kumuoa huyu mwanamke mie na mama yako si tulikukataza wewe hukusikia sasa si unaona mabalaa hayo?”
“Sasa baba lakini haya matatizo yanahusiana nini Judith?”
“We umesharogwa huwezi kujitambua, tuulize sisi tulioko pembeni, sasa sikiliza mimi sitaki tena kukuona ukiwa na huyu mwanamke, hawa wanao nitaondoka nao nitaenda kuwalea Shinyanga..”
“Lakini baba…”
“Lakini nini? Nimeshamaliza, kwanza Hebu amka ukaoge tuondoke mara moja nikupeleke kwa sheikh Jabu”

Masu akainuka akatoka mpaka nje akamuambia Mkewe ampelekee maji bafuni akaoge, Judith akachukua ndoo ya maji mpaka bafuni kisha Masu akafuata, Masu akaanza kuoga kama kawaida,
Wakati huo huku chumbani Mzee Kikoko akiendelea kucheza cheza na wajukuu zake, lakini Judith akaamua tu kukaa zake nje maana aliona sasa tayari bwawa limeshaingia Ruba. Akiwa Bafuni Masu akijipaka sabuni, tayari alikiwa na mapovu mwili mzima ghafla alisikia mlango akigongwa, akajiuliza huyu nani tena?! Ikabidi ajimwagie haraka maji usoni ili atoe mapovu, alipomaliza akafumbua macho HAMAD!! Alipigwa na butwaa, alijiona yuko katika Bafu, zuri na la kisasa tofauti na kule alikokua akioga, akawa hajitambui kua yuko wapi, akaanza kutetemeka, alipojiangalia vizuri akajigunduakua alikua sio Masu tena, alikua amebadilika kabisa maumbile yake na sasa alionekana kama mwanamke mzuri na mrembo hasa, Masu alizidi kuchanganyikiwa, akajiangalia zaidi ya mara mbili, vile vile akiwa ni mwanamke kabisa tena alieumbika kike, akiwa bado hajaelewa ni nini kimemtokea akasikia tena mlango ukigongwa kwa mara ya pili, ikabidi ajikaze aulize
“Nani?” heee! cha ajabu hata sauti yake ilikua imeshabadilika na kua sauti laini na nyororo kabisa
“Hebu fungua haraka we Shamsa, kuoga gani masaa sita? Tayari wageni wameshafika huku?” Masu alizidi kupata hofu alijiuliza sauti ile ni ya nani? Na kwanini amebadilika vile? Na je huyo Shamsa ndio yeye au ni nani hasa? Na ni wageni gani waliokuja? Na pale yupo wapi? Lakini hakupata jibu, akaanza kupepesa macho huku na kule akijaribu kuangaza nguo zake lakini hakuona nguo zake zaidi ya Khanga moja ya laini pamoja na nguo ya ndani, ikabidi tu avae nguo ile ya ndani kisha ajifunge khanga ile nusu bega, nahivi alikua na maji maji mwilini ndio kanga ikayashika vema maungo yake na kumfanya azidi kuvutia, Akafungua mlango sasa ili atoke nje akukutana uso kwa suo na huyo Bi Mkubwa aliekua akimgongea mlango, Bi mkubwa huyu alionekana kupata jazba sana akaanza kumpokea huku akimtokomeza kwa maneno
“Hivi we unaakili kweli wewe? Naomba usinisumbue mie nakuona siku hizi kama umekua jeuri sana, kama ulikua hautaki kuolewa si ungesema mapema kuliko kutusumbua hivi”
“Mama mbona sikuelewi?” Masu alijibu kwa mshangao sana japo kwa wakati huo sio Masu tena ni Shamsa
“Leo nimekua mama yako? Muone mpaka unayachanganya maneno, hebu pita huko ndani ukavae haraka, tayari mshenga ameshakuja yuko huko seating room” Masu alizidi kuduwaa ikabiditu sasa akubali kuingia ndani, ilikuani chumba kizuri na cha kisasa, inaonekana wanaoishi mule wako vizuri kiuchumi, Baadaya Masu kuingia akaanza kuvaa sasa baada ya kumaliza kupaka mafuta japo nguo za kike zilimchanganya zaidi, muda akaingia tena Yule Bi mkubwa akaanza kumtengeneza na kumremba vizuri Masu mpaka Masu akaonekana kua sasa amependeza na kuvutia mno
“Inatakiwa hata huyo Shemeji yako alietumwa tu nae akutamani mtoto wakike” Masu akazidi kupata picha sasa kua pale anatambulika kama SHAMSA na anatakiwa kuolewa japo hakujua anaolewa na nani, pia alielewa kua kuna mtu ametumwa na baba harusi mtarajiwa kuja kuongea nae, Roho ilikua ikimuuma sana kwakua alishangaa ataolewaje wakati yeye ni mwanaume?, Masu akainua macho na kumuangali usoni huyuBi mkubwa ambae alikua Busy akimpodoa Masu a.k,a Shamsa
“Unaniangalia nini hunijui? Shemeji anatakiwa mpaka mwenyewe ajilambe, na akikaa vibaya pita nae tu kwani kitu gani mwali wangu Hehee Haloo” Masu alizidi kupigwa na butwaakusikia maneno ya mama Yule ambae sasa alianza kumuelewa kua yuko pale kama Somo wake,
“Naona umeshapendeza mtoto wa kike, haya naenda kumuita Shemejio ila sasa utulize kichwa uongee vizuri, sawa?”
“Sawa..” Masu alikubali kishingo upande, kisha Somo akatoka nje

Baada ya kama dakika mbili mlango ukagongwa, Masu akaa kimya tu mpaka ulipogongwa tena kwa mara ya pili ndipo akaitika
“Karibu”
“Ahsante” baada ya Masu kumkaribisha mgeni wake akaanza kuingia ndani mgeni Yule wakati huo Masu ameinamisha kichwa chini kwa hofu, mgeniyule ampaka alipokaa Masu na kumsalimia
“Habari yako Shamsa” Masu akainua kichwa ili amjibu ndipo moyo wake ukafanya PAA!!! Hakuamini kilichokua mbele yake, Alikua Ni HUNUDU kutoka katika Dini ya Waufi
“Hunudu???”
“Ndio mimi Shem”
“Hivi kwanini lakini umeamua kunitesa hivi?”
“Hakuna anaekutesa, ila unajitesa mwenyewe, kama ungekubali kujiunga na Waufi na ukamtoa kafara mwanao mmoja wala tusingefika huku”
“Kwahiyo mmeona suluhisho ni kunidhalilisha kiasi hiki?”
“Hakuna anekudhalilisha, tumeamua kukugeuza jinsia na kukuleta huku katika ulimwengu mwingine ili uolewe kisha utuzalie mtoto ambae tutakuja kumtoa kafara, kisha kama Mumeo atakubali ukishajifungua akuache tukurejeshe katika maumbile yako ya awali sawa tutafanya hivyo japo sina uhakika kama atakubali maana jinsi mtoto ulivyoumbika ni balaa” Hunudu alikua akiongea maneno yake ya dhihaka huku akicheka kichinichini, Hakika Masu alikua amepatikana
*****

ILICHUKUA muda mrefu sana bila ya Masu kutoka bafuni, mzee Kikoko akapatwa na wasiwasi, ikabidi atoke mpaka nje, pale nje akamkuta Judith akiwa amekaa kwenye mkeka , kwakua Kikoko alikua hataki kuongea chochote na mkwe wake huyo akaenda moja kwa moja mpaka bafuni, alipofika bafuni akaanza kugonga mlango
“Ngo! Ngo! Ngo!”
Aligonga karibu mara tatu bila ya kusikia sauti ikimuitikia, akazidi kuingiwa na hofu, akawaza pengine Masu hakupendezewa na maamuzi yake ya kwamba aachane na mkewe na kwamba yeye(Kikoko) atawachukua wajukuu zake akina Zani na Fani kwa ajili ya kuwalea, Mzee Kikoko akaanza kuita kwa sauti
“Masumbuko..”
“We Masu!!”
Hakuna sauti iliyomjibu, alipoangalia juu ya mlango wa bafuni kwa juu aliziona nguo alizokua amezivaa Masu zikiwa zimetundikwa hivyo inaonekana Masu yuko bafuni, sasa kwanini haitiki? Ni swali alilojiuliza mzee Kikoko bila ya majibu, ikabidi sasa amuite tu Mkwewe
“We Mama Zani..”
“Abee Baba..”
“Hebu njoo” Judith akainuka pale alipokua amekaa na kuelekea kule lilipo bafu, hakujua anaitiwa nini ila tu alijua kua tayari kuna tatizo,
“Huyu Masu ameshatoka bafuni?”
“Hapana sijamuona kutoka”
“Sasa mbona haitiki naona nguo zake tu?”
“Mmmh labda amepatwa na tatizo” Hali ile pia ilimshtua sana Juddy, hofu ikamvaa, ikabidi amuite Mama Jay, ambae ndie mama mwenye nyumba ili wamueleze suala hilo, Baada ya mama Mwenye nyumba kutoka walimuelezea kila kitu, nae hofu ikamtinga, ikabidi sasa wakubaliane kuvunja mlango ili wamuangalie maana kila mtu sasa aliamini kua atakua ameanguka tu kutokana na kuzidiwa na hayo matatizo yanayomsibu maana watu wengi tu sasa mpaka majirani tayari walikua wameshaanza kujua kua Masu anasumbuliwa na vitu visivyoeleweka
Mama mwenye nyumba akumuita kijana wake anaeitwa Jay ili ashirikiane na Mzee Kikoko kuuvunja mlango wa bafuni, muda wote huo mzee Kikoko alikua haoengei kitu, alionekana ni mwenye hofu kubwa, haikua kazi kubwa sana kuuvunja mlango ule kwakua ulikua umefungwa kwa ndani na kitasa kidogo tu hivyo Jay peke yake alitosha kuufungua mlango ule, Baada ya kuufungua tu wakaingia haraka Mzee Kikoko na Jay, Laa haula hapakua na mtu, Masu hakuwemo bafuni, Kikoko alichanganyikiwa maana nguo zote za Masu mpaka ile ya ndani kabisa zilikuwepo palepale kwa juu ya mlango lakini mwenye nguo haonekani, ingekua Choo na bafu viko kwa pamoja pengine wangeanza kuhisi kua huenda akawa ametumbukia kwenye shimo la choo, Mzee Kikoko akazichukua nguo za mwanae kasha akatoka nazo nje
“Vipi Baba..?” Juddy aliuliza kwa hofu na woga huku mama Jay akiwa kasimama kwa pembeni
“Kuhusu nini?” alijibu Kikoko kwa jeuri na hasira
“Imekuaje?”
“We usinifanyie mie mtoto wala mpuuzi mwenzio, umesikia?”
“Jamani, sasa kukuuliza ni makosa?”
“Unaniuliza nini?Wewe unajua vizuri Masu alipoenda utanieleza mpuuzi mkubwa wewe”
“Lakini Baba mbona unaninyanyasa sana?”
“Nakwambia hivi leo utanijua vizuri maana naona unataka kunizoea wewe, haiwezekani mtu ameingia bafuni halafu ghafla katoka bila wewe kujua wakati ulikua umekaa hapa hapa uani, inamaana kuna njia gani nyingine ya kutokea zaidi ya hii?” Mzee kikoko tayari alikua ameshachemka kwa jazba akatoa simu na kumpigia swahiba yake Sheikh Jabu akamueleza kila kilichojitokeza pale, Jabu akamuambia amsubiri huko hook Buguruni, baada ya Mzee Kikoko kukata simu tu akahamia kwa Judith akamfuta Juddy mpaka pale alipokua amesimama, akamkwida na kuanza kumpiga makofi huku akimtaka Juddy aseme Masu yuko wapi…
“Baba mie unanionea bure, wala sijui Masu alikoenda”
“Utanieleza tu nakwambia nitakuu mimi” Hali ile ilimtia sana uchungu mama Jay kuona mwanamke mwenzie ananyanyaswa kiasi kile bila ya sababu za msingi, akaingia ndani na kumpigia simu mume wake ambae ni askari polisi kituo cha polisi Buguruni na kumueleza juu ya tukio zima, kasha baada ya kumsikia Kikoko anaendelea kutoa kichapo kwa Juddy ikabidi atoke tena pale uani na kumvulia uvivu

ITAENDELEA


CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA NNE

“Baba mie unanionea bure, wala sijui Masu alikoenda”
“Utanieleza tu nakwambia nitakuu mimi” Hali ile ilimtia sana uchungu mama Jay kuona mwanamke mwenzie ananyanyaswa kiasi kile bila ya sababu za msingi, akaingia ndani na kumpigia simu mume wake ambae ni askari polisi kituo cha polisi Buguruni na kumueleza juu ya tukio zima, kasha baada ya kumsikia Kikoko anaendelea kutoa kichapo kwa Juddy ikabidi atoke tena pale uani na kumvulia uvivu
“Hivi we Mzee una matatizo ya akili?” Mama Masu aliongea kwa taharuki
“Unanitusi mimi we mwanamke?”
“Nakutusi ndio huna akili, mtu mzima hovyo kazi kuonea tu wanawake”
“Naomba uwe na adabu nitakufata na wewe nikharibu sasa hivi huo mdomo wake”
“Njoo uniharibu, nakwambia njoo, usinitishe nipo kwangu”
“Huna hata haya wakiitwa wenye nyumba na wewe utatoka na hiki kibanda chako cha kuoshea maiti”
“Wewe unayo? Ungekua nayo si ungempa mwanao akakaa kulioko kuja kupanga. Muone kwanza kwanzia zile sharubu zilivyomchachamaa” Kikoko akapata jazba akahamia kwa Mama Jay akamvaa ili aanze kumshushia kipigo lakini kabla hajafanya hivyo akazuiliwa na Jay ambae alikua akiangalia malumbano yale yakiendelea,
Wakati hayo yakiendelea gari ya Polisi ikawa imepiga breki nje ya nyumba kisha wakashuka askari watatu, wawili wakiwa wamevaa kiraia na mmoja akiwa amevaa kikazi, wotw wakiwa na Bunduki wamezibeba mikononi, kisha wakaingia ndani na kukuta hali ile ya utata mule ndani kati ya mama Jay na Mzee Kikoko, huku Judith akiwa amesimama pembeni analia kwa uchungu
“Habarini za saa hizi..” alisalimia mmoja kati ya wale maaskari polisi aliekua amevaa kiraia
“Salama tu karibuni” alijibu Mzee Kikoko
“Kuna nini tena mbona mmekwidana na huyu nae analia?”
“Huyu mzee kampiga sana huyo mwanamke hapo halafu akawa anataka kunipiga na mimi?” alidakia mama Jay, ikabidi Yule askari amsogelee karibu Mzee Kikoko
“Mzee imekuaje tena unapiga watu tena wanawake haogopi kupatwa na matatizo?”
“We unaniuliza kama nani kwanza..”
“Mimi ni ofisa wa Polisi kutoka kituo cha Buguruni”
“Kwa ushahidi gani kwamba wewe ni askari?” alihoji mzee Kikoko bila ya kuonesha hata chembe ya Soni, Askari Yule nae akajaa hasira na kuanza kumbadilikia mzee Kikoko
“Mzee naomba uwe na nidhamu, nitakunasa vibao sasa hivi, nikakuweke na ndani”
“We unasemaje? Unipige vibao mimi? We unanijua mimi?
“Nikujue ili inisaidie nini?”
“Kama haikusaidii kitu umekuja kuingilia mambo yasiyokuhusu ili ikusaidie nini? Haya hebu thubutu kunipiga hata kibao kimoja uone nitakachokufanya, Hutopata hata kazi ya kupalilia hapa Dar” Kila mtu alibaki kashangaa jinsi Kikoko alivyokua akijibizana na maaskari bila ya hofu hata kidogo,
“Nyie ni askari gani msiojua hata kujitambulisha kisheria? Taja jina lako, namba yako ya kazi, kitabulisho chako, nk” Yule afande akamuangalia sana mzee Kikoko kisha ikabidi Yule askari atoe Kitambulisho chake cha kazi akamuonesha Mzee Kikoko
“Umeridhika eeh?”
“Sio nimeridhika lazima utambue majukumu yako na ufuate taratibu za kazi yako, sasa usipojitambulisha nitakujuaje kama wewe ni askari? Kama ni hizo bunduki na sare hata majambazi wanazo, mie sio wa kijijini, mimi ni mtoto wa mjini”
“Sawa mzee utaenda kutuonesha na hao majambazi wanaomiliki bunduki na sare zetu” Askari Yule alikua amekasirika sana,

Wakati Mzee Kikoko anaendelea kujibizanana maafande hawa Sheikh Jabu nae akawa tayari ameshawasili na pikipiki yake akiwa amembeba Sheikh Mwinyigoha, Kikoko alipomuona Sheikh Jabu ndo akazidikupata kiburi lakini hakupata furaha kumuona Sheikh Mwinyigoha kutokana na malalamiko ya mwanae kua Mwinyigoha nae alikua ni mmoja wa wafuasi wa Dini ya Waufi
“Habari zenu..” alisalimia Sheikh Jabu baada ya kuingia uani
“Nzuri..” waliitikia kwa pamoja, wengine wakamuamkia
“Poleni na matatizo jamani”
“Matatizo ya kujitakia tu haya, huyu mwanamke anajua Masu alipo ila anataka kutuchezea tu vichwa” Mzee kikoko alijibu kwa hamaki ya hali yajuu
“Hebu Bw Kikoko njoo faragha kidogo” Wakasogea pembeni Sheikh Jabu, Mwinyigoha, na Kikoko
“Imekuaje tena mzee mwenzangu naona kuna polisi huku namuona mkweo analia, kuna nini hasa?”
Kikoko akaanza kusimulia kila kitu kuanzia alipofikapale mpaka Masu alivyotoweka katika mazingira ya kutatanisha
“Umefanya makosa makubwa Bw Kikoko” alijibu Sheikh Jabu baada ya kusikiliza maelezo ya Kikoko
“Kivipi?”
“Kwanza haukupaswa kuanza kuongea na Masu masuala ya kumuacha huyu mwanamke wake kwakua akili ya Masu bado haijatulia kabisa, Pili umefanya makosa kumpiga makofi huyo binti hiyo ni kesi kubwa ikifikishwa mahakamani inaweza kukuletea dhahama kubwa sana” Maneno yale yalimuingia sana Kikoko sasa akawa anaanza kujuta lakinitayari ameshatenda kosa na waswahili wanasema majuto ni mjukuu..
“Mzee tunaomba tuelekee kituoni tafadhali..” Afande mmoja alimuita Kikoko ili waondoke nae
*****

Baada ya Masu(Shamsa) kuongea na Hunudu kwa muda mrefu Hunudu akatoka na kuaga kisha akaondoka zake, Shamsa alizidi kuumia sana kwa ndani. Alitamani wale kina mama wajue kua yeye ni mwanamke na wala haitwi Shamsa kama wanavyomuita, yeye ni Mwanaume na anaitwa Masu lakini hakuweza kufanya hivyo, alitamani hata ikiwezekana Baba yake na mkewe wangejua mahala alipo ili wamsaidie kumuokoa lakini haikuwezekana, alitamani angepata walau dakika moja tu kuonana na Mzee Kishindo ambae ndie alionekana kua mkombozi wake lakini haikua rahisi tena, Kikubwa zaidi kila akivuta picha kua sasa anatakiwa kuolewa wiki inayofuata ndio alitamani kupasuka lakini kila alipojaribu kujiangalia vizuri alikubali kua sio Mwanaume tena lakini aliendelea kupingana na ukweli huo!
Alikaa mule ndani kwa takribani wiki mbili mpaka akayazoea Mazingira na kuwaelewa wenyeji wake, Yule Somo yake alikua ni Shangazi yake anaitwa Bi Habiba, pia alimjua Bi mkubwa mwingine kua ndie anaejulikana kama mama yake Mzazi anaitwa Bi Shammy. Maisha yaliendelea kusonga mbele kila siku alikua akifundishwa namna ya kwenda kuishi kwa mume, namna ya kumlea na kumtunza mumewe, nk.
Siku moja zikiwa zimebaki siku mbili tu kufika siku ya harusi Masu(Shamsa) akiwa chumbani kwake waliingia watu watatu, Somo yake Bi Habiba na wadada wengine wawili ambao ukiwaangalia tu utajua kua ni magwiji wa unyago na ni watoto wa mjini haswa, mmoja anaitwa Nunuu alikua aemevaa kikuku mguu wa kushoto ile kiMombasa, na huyu mwingine anaitwa Shumbana, kama kawaida yao huja kumfunda mwali wao ambae ni Shamsa(Masu),
Wakiwa wanaendelea na mafunzo yao yaliyojaa mambo ya ajabu ajabu kama muwajuavyo tena Makungwi walikua wakimpa somo Masu(Shamsa) huku wakifanya vitendo kabisa, Masu aliumia sana na mambo yale ghafla
“Jamani lakini mnanifanyia hivi mjue kua mimi si mwanamke, mimi ni Mwanaume kabisa”
“Unasemaje wewe?” aliuliza kwa ukali Bi Habiba huku wake madada wengine wakionesha mshangao mkubwa kutokana na maneno aliyoyatoa mwali wao
“Ndi hivyo, mie Siwezi kuolewa, mimi ni mwanaume” Basi kwa hasira Bi Habiba akainuka kwa jazba mpaka pale alipokua amesimama Masu kasha akamvua kwa nguvu ile kanga aliyokua amejifunga, Masu akabaki kama alivyozaliwa kasha Bi Habiba akamuuliza
“Haya jiangalie una uanamume gani?” baada ya Bi Habiba kusema hivyo wale wapambe wakacheka kwa sauti za kishangingi, kasha Nunuu akadakia
“Dada Habiba kua makini, makungwi wenzio watakua wameshafanya yao hapo haiwezekani ghafla mtoto wakike aseme ahataki kuolewa eti ni mwanaume…”
“Hakuna cha kuchezewa wala nini ni huyu huyu mpuuzi tu anataka kutuharibia shughuli, na hii si mara yake ya kwanza alishakataa kuolewa zaidi ya mara mbili huyu, ngoja tu nimuite Mama yake Bi shammy aje amalizane nae mie nimeshachoka na vioja hivi” Bi Habiba akatoka nje kumuendea Bi Shammy, hawa wadada nao wakatoka nje wakamuacha Masu(Shamsa) akiwa amesimama chumbani kama alivyozaliwa, walipotoka tu nae akainama akachukua kanga yake na kujifunga upya akijua sasa kua mambo yameshavurugika,
Baada ya muda mfupi mlango ukafunguliwa, Masu akajua sasa balaa tayari limeshamfika, lakini aliponyanyua macho yake akakutanisha na macho yako na HUNUDU, Akataka kutaharuki Ila Hunudu akamsogelea na kumuuliza Masu
“Ndo umefanya nini sasa?”
“Kivipi?”
“Kwanini umewaambia kua wewe ni mwanaume?”
“Kwakua kweli mimi ni mwanaume, siwezi kuolewa”
“Sasa hiyo ni hatari kwako, huyu Mama atakufanyia kitu kibaya sana”
“Basi kama mmeamua kunimaliza nyie nimalizeni mmenitesa vya kutosha”
“Khaa, yaani na wewe unajiona umeteswa? Tutakapoanza kukutesa si hautoamini”
“Lakini Hunudu kwanini mnanifanyia hivi?”
“Kwa sababu ya dharau na kiburi chako, na utateswa zaidi muda ukifika, taka usitake utaolewa tu na utazaa tu na kisha ndo mateso yataanza rasmi” Masu alijaribu kumuomba Hunudu amsaidie, Hunudu hakua na shida hata ya kumuangalia Masu usoni lakini baada ya Masu kulalamika sana Hunudu alimuahidi kumsaidia asipate tabu endapo tu kama atakubali kuolewa au Laa sivyo akubali kumtoa mwanae mmoja ndipo atarejeshewa maumbile yake ya kiume na kua huru huku akiwa ni mwanachama wa dini yao ya WAUFI, Kutokana na matatizo kumfika shingoni Masu akakubali kutekeleza matakwa ya Hunudu
“Hii ni nafasi ya mwisho kwako, ukitoa siri na kuvuruga utaratibu sitakuvumilia tena, sawa Masu?”
“Sawa mkuu”
“Ninakurejesha katika maumbile yako ya kiume na kisha nitakuchukua mpaka kwa Mkuu wetu ili ukaungame uovu wako.. halafu nitakurejesha duniani” Baada ya makubaliano hayo, Hunudu akatoa Pete katika mfuko wa suruali yake na kumvisha Masu katika kidole chake cha kati
Baada tu ya kumvisha ile Pete Masu akajishanga ghafla anaanza kubadilika na kurudi katika maumbile yake ya awali, lakini ghafla akaanza kujisikia vibaya mwili mzima, mara kichefuchefu, mara kizunguzungu, yaani akawa taabani kama mtu anaekaribia kukata roho, Masu akajikua anaishiwa nguvu mwishowe akaanguka chini kama mzigo, wakati huo Hunudu alikua akiendelea kumtazama tu bila ya kumsaidia chochote bila shaka alikua akijua alichokifanya ndani ya Pete ile, Masu aljaribu kutaka kumuomba msaada Hunudu lakini mdomo ulikua mzito kutamka maneno huku akitokwa na udenda, ikabidi amuoneshe kwa Ishara kua anamuomba msaada Lakini Hunudu alionekana kutabasamu kwa dharau tu, Masu aliendelea kutapatapa bila msaada wowote mpaka akaanza kuhisi kupoteza fahamu, na kweli baada ya kama dakika mbili Masu akapoteza fahamu..
Akawa kama alietoka usingizini bila ya kujua yuko wapi, Masu alijikuta akiwa Juu ya maji, katika kati ya bahari akiwa peke yake, Hofu ilimuingi sana mwilini, alijaribu kuangaza huku na kule lakini hakuona mtu yoyote, alikua amevaa nguo nyeupe tupu, nguo zake zilikua ni nyepesi mno kiasi cha kumfanya ahisi baridi kali lililotokana na upepo mkali wa baharini, Hakika Masu alikua kama chizi vile maana hakuna alichokielewa, ghafla kwa mbali aliwaona watu kama watano hivi nao wakiwa wamevaa nguo nyeupe, dalili zao zilionyesha wanakwenda usawa ule aliokuwepo yeye, Masu akachanganyikiwa akaamua kuondoka eneo lile huku akikimbia ghafla alipogeuka aliwaona vijana wale nao wakimkimbiza kwa kasi ya ajabu, alijitahidi kuongeza kasi ya kukimbia lakini vijanawale nao walizidi kumkaribia, alipoangalia mbelea aliona mnyama mkubwa mithili ya Kiboko lakini hakua kiboko, nae mnyama huyo alikua akikutana sasa uso kwa uso na Masu, Mnyama huyo alikua akiunguruma kwa sauti kali
kama Radi vile, Masu alipomuona mnyama Yule akajikuta anapiga kelele hovyo kama mwendawazimu
“Uwiiiiiiiiiiiiiiii, Nakufaaaaaaaaa”
Ghafla akajikuta ametokea tena kule Bafuni kwake alikokua anaoga mara ya kwanza, Masu hakuamini kama amerudi huku tena, alikua anahema kwa nguvu sana,
*****

Mzee Kikoko na Sheikh Jabu walikua wakijadiliana nini cha kufanya ili ile kesi isifikishwe Polisi ndipo ghafla wakasikiahiyo Sauti kali ya Masukutoka Bafuni, wote wakashtuka, hawakutegemea kusikia sauti ile, haraka wakakimbilia kule bafuni wakiwa pamoja na wale maaskari, na kweli wakamkuta Masu akiwa amesimama, kila mtu aliogopa kumsogelea, maana ilikua ni kama mazingaombwe vile, hata maafande wale walioonekana kua ni majasiri nao walipigwa na butwaa, hakuelewa kabisa kinachoendelea,
Safari hii Masu alikua amevaa nguo nyeupe alizotoka nazo kule baharini, kidoleni alikua na ile Pete aliyovishwa na Hunudu, Sheikh Jabu alijikaza na kumshika mkono kisha akamtoa nje ya bafu, Masu bado alikua hajielewielewi wala haelewi amefikaje tena huku ghafla kiasi kile
“We Uliku wapi?” aliuliza Mzee Kikoko lakini swali lake lilikatizwa na Sheikh Jabu
“Bwana Kikoko huu sio muda wa kuongea mambo hayo” Jabu akamshika mkono Msu mpaka ndani huku nyuma akifuatwa na Mzee Kikoko na sheikh Mwinyigoha, baada ya kufika ndani na kuketi ndipo Sheikh Jabu akamuuliza Masu
“Vipi umeshakula?” Masu alijibu tu kwa kutikisa kichwa kua ameshakula
“Ehnhee imekuaje tena?” Jabu alikua akimuuliza Masu maswali kwa mitego ya hali ya juu, lakinikabla Masu hajajibu kitu macho yake yakapiga kwenye kidole cha sheikh Mwinyigoha, Naam akaona Pete kubwa nyekundu, alipojiangalia kwenye kidole chake akagundua ni pete kama aliyoivaa yeye, ni PETE ya waufi
“Noooooo” Masu alipiga kelele huko akmsonta sheikh Mwinyigoha, watu wote walitahayari, viti vikawa vichungu wakasimama juu, lakini Sheikh jabu alikua ni jasiri sana aliendelea kumshika tu masu huku akimuhoji
“We una tatizo gani?”
“Huyu mzee hafai, si shekh huyu, ni mfuasi wa Waufi”

BAADA ya Masu kumtuhumu sheikh Mwinyigoha kua nae ni mmoja wa wafuasi wa Dini ya Waufi kila mmoja akapigwa na butwaa, lakini kabla hawajamjibu chochote Masu akendelea kusema
“Hiyo Pete aliyoivaa ni kama hii yangu, zote ni za Waufi” Mzee Kikoko akashtuka, akamuangalia usoni Sheikh Jabu, kasha kwa pamoja wakamuangalia kidoleni Sheikh Mwinyigoha lakini cha ajabu hawakuiona hiyo Pete
“Pete gani tena Masu? Mbona hana Pete yoyote” Sheikh Jabu aliongea kwa utulivu kiasi,
“Jamani pete si hii hapo tena ni kubwa tu inaonekana vizuri” Masu alipomuangalia Mwinyigoha akaiona pete ile kidoleni, sasa ikawa ni kama muujiza yaani Masu anaiona ile pete lakini wazee wake hawaioni, Mzee Kikoko akawa anatikisa kichwa kwa unyonge kabisa akiamini kua sasa mwanae amaeanza kuchanganyikiwa, wakati wote wakiwa wamepatwa na mfadhaiko Masu akawaponyoka na kutoka nje
“Sasa unaenda wapi wewe Masu” alihoji Mzee Kikoko lakini masu hakujibu kitu akaondoka kwa kasi.. Hali ya simanzi ikazidi kutamalaki pale nyumbani kila mtu sasa aliamini kua Masu amechanganyikiwa
“Itakua Masu amechanganyikiwa tu” alisema Sheikh Mwinyigoha
“Hapana, Masu ni mzima kabisa ila hapa kuna jambo tu, tena kubwa sana” alidakia Sheikh Jabu
“Ni jambo gani sasa lisilojulikana?”
“Cha kujiuliza ilikuaje Masu akapotelea Bafuni, kisha akarudi ghafla akiwa amevaa nguo zingine?”
Kabla Mwinyigoha hajajibu ghafla akadakia Yule Askari polisi huku akimuangalia usono Judith mke wa Masu “Tena akiwa na Pete kubwa, au hua anayo siku zote?”
“No, sijawahi kumuona nayo hata sikumoja” alijibu Judith huku akitokwa na Machozi
“No ndio nini sasa? Ongea Kiswahili ueleweke, unataka kuleta nyodo za kizungu hapa wakati mmeshamroga mwanangu, na wewe ndo chanzo” Kikoko alimkaripia Juddy mpaka kila mtu akashangaa maana hapakua na haja ya kuleta mada mpya
*****

‘Ngo! Ngo! Ngo’

Mlango wa mbele uligongwa kwa nguvu sana, ni maeneo ya Tabata Matumbi, nyumbani kwa mzee Kishindo, wakati huo Mzee Kishindo alikua chumbani akimalizia kuswali hivyo hakuweza kujibu hodi ile, akaendelea tu kuswali lakini kelele za kugongwa kwa mlango zilimshtua sana maana mlango ulikua ukigongwa kwa nguvu bila shaka palikua na mtu aliekua na shida ya haraka sana au mtu aliekuja kiushari vilivyo,

“Mzee Kishindo! Mzee Kishindo!”

Japo Mzee Kishindo hakumjibu kitu kwa kuhofia kuharibu swala yake kwani kwa mujibu wa dini yake hakupaswa kuacha kusali na kumjibu mtu lakini tayari alikua ameishaing’amua sauti inayomuita, Naam ilikua ni sauti ilyojaa mchoko na hofu, ni sauti ya MASUMBUKO. Baada ya kumaliza kuswali Mzee Kishindo akaenda mpaka kwenye mlango wake akaufungua taratibu ili achungulie nje ndipo ghafla Masu akaingia kwa kasi ndani huku akitweta, Mzee Kishindo alijikaza japo alikua nae ameshtuka kwa hali aliyokua nayo Masu ikabidi tu aurudishe mlango akihofia kujifungia nae ndani, alipomgeukia Masu alikua akilia sana kwa uchungu
“Unalia nini Masu?” alianza Mzee Kishindo kwa kumtupia swali Masu
“Mzee Kishindo, ninateseka sana, napitia kila aina ya taabu, Waufi wataniua” Baada ya Masu kujibu vile Mzee kishindo alikua amesimama wima, akamsogelea mpaka pale alipokua ameketi nae akaketi pamoja nae
“Pole sana mwanangu”
“Sijapoa hata kidogo”
“Nadhani unakumbuka nilishakudokeza kua tatizo lako ni kubwa sana..”
“Ndio nakumbuka, na ndio maana nimekimbilia kwako unisaidie”
“Natamani sana kukusaidia ila baba yako mzee Kikoko anasumbua sana, ananitusi mbele za watu na kusema kua mimi ndie ninaekuroga na ananipa kila aina ya vitisho kwa ajili yako, unakumbuka nilikuuliza kua una kifua? Ukasema ndio, sasa ikawaje tena hata kabla sijakuelezea ukaanza kuvujisha habari mpaka zikamfikia baba yako na sasa unanileyea tabu mie?”
“Mzee Kishindo huu sio muda wa kulaumiana kabisa, kwa sasa nahitaji tu msaada wako, pia mimi sijamueleza chochote baba ila nadhani ni mke wangu tu huyo kwakua walimbana sana baada ya mimi kuanguka” Baada ya maelezo hayo ya Masu Mzee Kishindo akainuka na kutoka uani kwake akamuacha Masu peke yake pale Sebuleni, Kisha baada ya muda mfupi Mzee Kishindo akarudi akiwa amebeba sahani mbili ya chakula, moja akampa Masu alionekana kua na njaa sana na nyigine akawa nayo yeye mwenyewe mkononi..
“Kula kwanza upate nguvu mpya” aliongea Mzee kishindo
“Ahsante lakini mie nimeshiba”
“Hujashiba chochote zaidi ya kuvimbiwa na hofu tu, kula ukimaliza tufanye mazungumzo” Basi Masu japo alijisikia kushiba ikabidi tu aanze kula hivyo hivyo ili kumridhisha Mzee Kishindo aweze kumpa msaada maana Mzee hyu ndie anaeonekana kujua kila kitu kuhusiana na tatizo la Masu kulazimishwa kujiunga na Dini ya Waufi, Iliwachukua takribani dakika karibi ishirini wakawa wamemaliza kula na tayari mke wa Mzee Kishindo alikua ameshawasogezea maji ya kunywa na kunawa. Baada ya kumaliza kunywa maji na kunawa ndipo mazungumzo yakaanza tena

“Hebu nihabarishe kwa mukhtasari mambo yako yakoje” alianza mzee Kishindo
“Mkasa wangu ulianzia kwenye ndoto, kuna siku nilikua nimelala…”
“Hapana huko unaanzia mbali ulishanihadithia tukiwa kule dukani, sasa anzia tangu baada ya pale” Kishindo alimkatisha Masu, maana Masu alikua ameshamsimulia jinsi tatizo lake lilivyomuanza, ikabidi sasa Masu aanzie pale alipokutana na Hunudu kwa mara ya kwanza ikiwa ni nje ya Ndito, ilikua ni stori ndefu nay a kuogofya sana, Masu alikua akiihadithia kwa uchungu mpaka anadondosha machozi, Mzee Kishindo alikua akimbembeleza huku akimfuta machozi mpaka akamalizia tukio la mwisho kule bafuni
“We ni motto wa kiume hivyo achana na mambo ya kulia hovyo, jikaze hii sasa ni vita umeivaa”
“Sawa Mzee”
“Pili nakupongeza kwa ushujaa wako na ujasiri wa kua kila jambo unalisema wazi japo huyo Hunudu anakutishia kua usitoe siri maana ungemtii tu masharti yake ndio ingekua mwanzo wa kukutawala” Masu sasa akawa anamsikiliza kwa makini Mzee Kishindo akiamini kua huenda akapata ukombozi
“Ulishajiuliza kwa nini uliitwa Masumbuko wakati kwenu hakuna hata mmoja katika babu zako aliewahi kuitwa jina hilo?”
“Hapana”
*****

TABORA

Mwaka 19970 ndipo bwana Rashid Kikoko alipohamia rasmi mkoani Tabora akitokea kwao Kigoma, na alipofika tabora alikua akijishughulisha na biashara ya kuuza samaki na dagaa aliokua akiwatoa Kigoma na kuwaleta Tabora, biashara yake ilikua nzuri mno, ilimpa faida nzuri na kubwa, ndani ya muda mfupi tu maisha yake yakawa mazuri nay a kuridhisha, akiwa Tabora alikutana na wazee na vijana wenzie kutoka kigoma ambao wanaishi hapo Tabora huku wakijishughulisha na masuala ya kiutafutaji… Kikoko nae alifanya Biashara zake kwa takribani miaka minne mpaka mwaka 1974 alipokwenda kwao Kigoma kufuatia wito alioitwa na Baba yake mzazi..

Baada ya Kikoko kurudi Kigoma kuitika wito wa baba yake alikutana na baba yake huyo Mzee Hassan Kikoko, kikubwa alichoitiwa alitakiwa sasa Aoe maana umri wake ulikua ni mkubwa na pia uwezo wa kifedha alikua nao, japo alijaribu kutaka kuleta vipingamizi lakini alizidiwa na hoja za baba yake mzazi hivyo ikabidi tu akubali kuoa, Bw Kikoko alirudi mjini Tabora kujipanga kwa ajili ya kutafuta mchumba ndipo akakutana na Bi Kapemba Masanja kutokea Shinyanga nae alikua ni mfanyabiashara akiendea vitenge vya wax huko Bujumbura na kuja kuviuza Kigoma, Tabora, na Shinyanga kwao, Kikoko hakua na pingamizi kua amezama katika huba kwa dada huyo.

Mwaka 1975 Bw Kikoko na Bi Kapemba wakafunga ndoa huko Shinyanga na kisha harusi ikaenda kumaliziwa Kigoma kwa baba yake na Kikoko, ilikua ni sherehe kubwa na ya kifahari, kila mtu aliburudika na kufurahikia harusi hiyo, baada ya sherehe za harusi Kikoko akarudi tabora alikokua ameweka makazi yake ili kuendelea sasa na utafutaji wa Riziki, Maisha ya ndoa yalikua mazuri kwao na miaka alikatika wakiwa na furaha. Tatizo Kubwa lilianza kuchomoza kama uyoga kwenye Kichuguu kutokana na Bi Kapemba kutopata ujauzito. Naam mpaka mwaka 1977 takribani mitatu baada ya ndoa bi mkubwa huyo hakupata ujauzito. Hivyo sasa ndugu zake na Mzee Kikoko wakaanza kuleta ghasia za chini kwa chini na hatimae ghasia zikaota mbawa na kutanda katika anga la huba kati ya Mzee Kikoko na Bi Kapemba. Wenyewe walijitahidi kuyapuuza malalamiko ya ndugu huku wakipambana kutafuta tiba kwa kila mganga mashuhuri waliesikia habari zake, lakini jitihada hazikuzaa matunda, ndipo sasa baba yake na Kikoko
akamuamuru Kikoko aoe mke mwingine ili ampatie watoto kwa kua Bi Kapemba ni Mgumba

Mwaka 1979 kwenye mwezi wa kumi na moja hivi, nakumbuka ilikua ni karibu na mfungo wa Mwezi wa Ramadhani hivi Bw Kikoko ilibidi tu sasa Aoe mke mwingine baada ya mikwara ya haja kutoka kwa familia yake, Alimuoa msichana fulani ambae huyu alikua ni mzawa na mwenyeji wa mkoani Tabora, aliitwa Bi Mwajabu Fundikira, ukoo wa Bi mdogo huyu ni ukoo wa kitemi hivyo ulikua ni ukoo ulioheshimika sana pale mkoani Tabora, akatekeleza suala hilo la kuoa lakini hakumuacha mkewe mkubwa Bi Kapemba Masanja, akawa sasa ana wake wawili, wote akiishi nao tabora. Maisha yakasonga mbele bila ajizi, Kikoko alijitahidi sana kuwaunganisha wakeze hao ili waishi kwa kupendana na kufurahiana, alijitahidi kwa kiasi Fulani kukawa na amani japo matatizo ya chichini hayaepukiki ila yalipojitokeza alijitahidi kuyatatua kwa ustadi wa hali ya juu

Naam mwaka 1980 ndoa ikajibu, Bi Mwajabu alipata ujauzito ilikua ni kwenye mwezi wa kwanza hivi yaani miezi mitatu hivi baada ya kuolewa kwake, kila mmoja alifurahia suala hilo, habari zikafika mpaka Kigoma nyumbani kwao na Kikoko nao wakafurahi sana, Lakini hali ikawa tofauti kwa Bi Kapemba kwa kua yeye hakujaaliwa kupata ujauzito hivyo alijiona kama mzigo, lakini Mzee Kikoko aliendelea kumfariji mkewe huyo bila ya kumtenga, ilipofika kwenye mwezi wa tano na ujauzio wa Bi Mwajabu ukiwa nao na miezi mitano, ghafla Bi Kapemba akaomba ruhusa kwa mumewe ambae ni Mzee Kikoko ili akapumzishe akili kidogo nyumbani kwao Shinyanga ikiwa ni pamoja na kwenda kuwasalimu wazazi wake, Mzee Kikoko alimkubalia, akamuandalia safari na kasha wiki moja baadae akaondoka na kwenda Shinyanga..

CHA AJABU, Ilipofika kwenye mwezi wa sita ghafla hali ya Bi Mwajabu ikaanza kubadilika, kila siku lile tumbolake la ujauzito likaanza kuyeyuka mithili ya pulizo lililotoboka na hatimae ujauzito ukatoweka kabisa, ilikua ni tukio la ajabu sana sit u kwa familia ya Bw Kikoko bali hata kwa baadhi ya majirani na wakazi wa mkoani pale, habari zilizagaa mji mzima, kila mtu alisema lake. Walipomuhoji Bi mkubwa huyo akasema aliondoka akiwa mjamzito ila tyeye alikua na tumbo dogo lisiloonekana kiurahisi, Ikabidi sasa Kikoko ampeleke mkewe Hospitali lakini nako vipimo vikaonesha kua hana ujauzito kabisa.. wiki mbili baada ya tukio hilo Bi mkubwa(Bi Kapemba) karejea tabora, kilichowashangaza wengi mpaka mzee Kikoko mwenyewe ni kwamba Bi Kapemba alirudi na Ujauzito mkubwa wa miezi kama sita hivi, hakuna alieaminikua tukio lile linatokea dhahiri lakini huo ndio ulikua ukweli wa mambo, yaani Ujauzito umetoweka kwa Kwa Bi mdogo na ghafla umehamia kwa Bi Mkubwa, Sulahilo
lilizua zogo kubwa na hatimae wakaanza kushikana uchawi

Ndugu zake na Bi Mwajabu walienda kwa waganga wakaambiwa kua Bi Kapemba aliinyakua kichwawi mimba ya mwenzie na kuihamishia kwake kwa kua hakua na uwezo wa kushika ujauzito na hapo ndipo ikafahamika kua Bi Kapemba amefanyiwa hivyo na mizimu ya kwao Shinyanga, unaitwa MZIMU WA WAUFI, Ni mzimu mkali sana na wenye nguvu hivyo sasa yakaanza mapambano ya kimizimu kati ya Mzimu wa Waufi wa kwao na Bi kapemba na Mzimu wa WASWEZI wakwao na Bi Mwajabu Fundikira, mpambano ulikua ni mkali sana kila siku ndani mauzauza, ushirikina, vurugu, nk lakini hatimae mwaka 1980 Bi Kapemba akajifungua motto wa kiume, na kutokana na tabu, shida, na mkasa ho ndipo wakampa jina la MASUMBUKO, Japo Bi Kapemba ndie aliejifungua lakini Bi Mwajabu alisema hakika Yule ni mwanae na ni damu yake hivyo hatokubali kamwe..

Familia zilijaribu kukaa na kufanya suluhu ili kwakua mambo haya yanautata mkubwa waweze kuiyamaliza, ilikua ni suala gumu sana lakini hatimae waliridhiana kishingo upande huku kila mmoja akibaki na lake moyoni, inasemekana wakati Bi Kapemba alipokwenda Shinyanga Mizimu ya kwao iliinyakua kichwawi mimba ya Bi Mwajabu na kuihamishia kwake kisha wakampa sharti kua ni lazima atoe kafara ya damu haraka iwezekanavyo Laa sivyo watamchukua Masu wao na Pia walimtaka Bi kapemba kua Masu akifikisha miaka kumi ampeleke ili akaingizwe rasmi kwenye Ukoo wao chini ya Mizimu ya Waufi kwakua hakua damu yao lakini hakufanya hivyo….

***Mnh! Mambo hayo!

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TANO

Familia zilijaribu kukaa na kufanya suluhu ili kwakua mambo haya yanautata mkubwa waweze kuiyamaliza, ilikua ni suala gumu sana lakini hatimae waliridhiana kishingo upande huku kila mmoja akibaki na lake moyoni, inasemekana wakati Bi Kapemba alipokwenda Shinyanga Mizimu ya kwao iliinyakua kichwawi mimba ya Bi Mwajabu na kuihamishia kwake kisha wakampa sharti kua ni lazima atoe kafara ya damu haraka iwezekanavyo Laa sivyo watamchukua Masu wao na Pia walimtaka Bi kapemba kuwa Masu akifikisha miaka kumi ampeleke ili akaingizwe rasmi kwenye Ukoo wao chini ya Mizimu ya Waufi kwakua hakua damu yao lakini hakufanya hivyo….

*****

Masu alikua amemtolea macho Mzee Kishindo aliekua akimpa mkasa mzima wa kuzaliwa kwake, ilikua ni stori ya ajabu na kustaajabisha sana
“Kwahiyo hakuna Dini ya Waufi mwanagu hiyo ni mizimu ya Waufi na kila wanachokufanyia ni kiini macho tu, hata Yule mchungaji na huyo sheikh wote si WAUFI bali unapokua unaongea na mtu yeyote anaonesha kutaka kukusaidia anakuja huyo hunudu na kujivisha umbile la huyo mtu kisha anajifanya nae ni Waufi”
“Mbona kwako wewe hua hatokei?”
“Nitakupa siri ya mizimu ya kwetu mimi”
“Sasa Baba nae aliamuaje?”
“Kikoko aliyakubali matokeo tu na anajua kila kitu sema anajaribu kujisahaulisha wakati wewe unaangamia” Masu akawa analia baada ya kuusikia Mkasa wake ule, Ikabidi sasa Mzee Kishindo akamkataze kulia
“Nilikuambia uwe na kifua, sasa unalia nini?”
“Mzee Kishindo mie nitakufa tu, sasa nitafanyaje mimi? Yaani kumbe Mama Masu hakua mama yangu halali??!”
“Hauwezi kufa japo huu mpambano ni mkali, unachotakiwa kufanya kwenda kwao na mama yako wa damu Bi Mwajabu Huko kipalapala tabora ili ukafanyiwe tambiko la kwenu, tambiko la Waswezi Laa sivyo utapotea kijana, ukiwa tayari nitakusindikiza”
“Kwahiyo tanafanyaje Mzee wangu?”
“Nitakusaidia, andaa nauli nitakupeleka mpaka Tabora kwenu, kwa mama yako”

Wakiwa katikati ya maongezi mazito ghafla walisikia sauti ya pikipiki ikija maeneo ya pale kwa Mzee Kishindo kisha mlio ukazima na baada ya muda kidogo mlango ukagongwa

Ngo! Ngo! Ngo!

Kabla hawajafanya lolote mlango ukafunguliwa akaingia Mzee Kikoko akiwa na Sheikh Jabu, baada ya Sheikh Jabu kugonganisha Macho na Mzee Kishindo hapo hapo Kikoko akamgeukia Sheikh Jabu
“Si nilikuambia kua huyu mshenzi ndie anaeleta fitna kwenye familia yangu?!!!”

******

MZEE Kikoko hakusubiri kugongewa kengere kama ishara ya kupata kibali cha kumvaa Mzee Kishindo na kuanza kumtembezea kichapo, ilikua ni kitendo cha kunusa na kutoa chafya, balaa kubwa kati ya wazee hawa ikaanza, tayari Kikoko alikua ameshasogelea na ameshamkunja shati Mzee Kishindo,
“Tafadhali Bw Kikoko niachie, hapa ni nyumbani kwangu utajiletea dhahma kubwa” alibwata Mzee Kishindo
“Sikuachii nataka nikuadabishe kidogo maana nilishakukanya kwa maneno ukaweka Nta masikioni” bada ya maneno yale hapo hapo Kikoko akamrukia kichwa mzee mwenzie, akamrushia ngumi, mara akamza ba kelbu la uso, Hakika Kikoko ni mzee mtata mwenye kila chembe ya ukorofi na shari, wakati huo kichapo kinaendelea Masu alikua ameshafika mlangoni kwa ajili ya kukimbia lile varangati lilikua likiendelea kuzizima mule ndani..
“Kikoko acha tafadhali” Sheikh Jabu alikua akijaribu kumuhami Mzee Kishindo asiendelee kupokea kichapo kutoka kwa Alwatani Kikoko ambae alikua ameshamgaragaza chini Mzee Kishindo, Kikoko aliendelea kumvugumizia makonde ya nguvu Mzee Kishindo, hakika ilikua ni hali ya hatari sana, baada ya purukushani kubwa pale chini hatimae Mzee Kishindo alifanikiwa kuinuka na kuponyoka kutoka katika mikono ya Kikoko, akatoka mbio akielekea Chumbani kwake
“Nitakuua mimi, unaleta ubwege wako hapa..” Kikoko aliendelea kutamba pale sebuleni kabla Kishindo hajatoka chumbani kwake kwa kasi ya ajabu, Alionekana kama Ng’ombe aliechanganyikiwa, hakika alikua amepandwa na ghadhabu, Mkononi akiwa ameshika kitu cha hatari sana, kitu chenye madhara, Naam ilikua ni mkia wa taa, Mkia wa taa ni hatari sana kwa mwenye kuujua hata ikiwa katika ugomvi mkubwa kiasi gani mtu akiutoa tu ule kila mwenye kuujua atakimbia kabisa, Ukichapwa na mkia ule kwanza utapata maumivu makali yasiyo ya kawaida na pia baada ya siku kadhaa utajishanga ukiugua tu hovyo
“Kishindo achaa tafadhali hiyo ni hatari” alipayuka Sheikh Jabu” Lakini Kishindo hakusikia ‘La Imam wala la mnadi swala’ Alikua amekasirika haswa! dakika chache tu akawa kaishamkaribia Mzee Kikoko na hapo hapo alianza kumcharaza kwa nguvu zote Mzee Kikoko, alimtandika mwilini hovyo hovyo, Kikoko alikua ameshahamaki hivyo kila alipojaribu kutaka kujihami ilikua ni sawa na kazi bure maana tayari Kishindo alikua ameshamtaiti vilivyo, Kipigo kilipozidi Kikoko Akaamua kutoka nduki kali lakini kutokana na Simenti laini iliyopo sebulaeni kwa Mzee Kishindo akaanguka chini ndipo sasa Mzee Kishindo akapata upenyo mzuri wa kumuadhibu Alwatan, Kikoko akawa anagaa gaa pale chini huku akipiga kelele lakini Kishindo hakua na hata chembe ya huruma aliendelea kutoa kiminyo utadhani anaua Nyoka,

Wakati hayo yakiendelea tayari Masu alishatoweka mule ndani, pia Sheikh Jabu alikua amekimbilia upande wa pili wa sebuleni akihofia kukaa karibu maana alijua bila shaka Mzee Kishindo atamgeukia na yeye na kumuadhibu pia, na kwa jinsi alivyoijua sumu iliyomo kwenye mkia wa taa hakutaka dhahma ile imkumbe,

Ghafla Kikoko akapata upenyo akachomoka na kutoka mbio mpaka nje ya nyumba ile, nae Sheikh Jabu akafuata mbio mpaka nje, Mzee Kikoko alikua kavimba mwili kwa kichapo cha mkia wa Taa
“Kama mwanaume kwanini ukimbilie mkia wa Taa?” Alipayuka kwa sauti Mzee Kikoko huku akiwa anatweta
“Pole Swahib wangu ila nilikukanya wewe, kua tukifika usifanye fujo hata kama tutamkuta Masu”
“Yule asingekua na ule mkia ningemdhibiti tu mimi ni mtoto wa mjini, we hukuona nilivyomuanzishia mpaka akahuma, halafu ananishambulia na silaha na wewe umekaa tu pembeni na kanzu yako mchinjo hiyo kama mtoto anaesubiri kutahiriwa..”
“Hilo ndo tatizo lako Bw Kikoko”
“Na hakyamungu usingekua swahiba wangu leo ningekutandika na wewe maana huna maana”
Baada ya malumbano na majibizano ya muda mrefu yale, Sheikh Jabu na Kikoko wakapanda pikipiki yao aina ya ‘Bata vuz’ kisha wakaondoka kwa kasi kuelekea nyumbani

*****

Nje ya Ofisi ya Birimuye Holding Ltd alikua amesimama Masumbuko Kikoko akiongea na kijana mmoja mfanyakazi mwenzie pale ofisini aliezoeleka kwa jina Shamsi, lengo la Masu ni kwenda kuongea na Boss wake Mr Kitale aweze kupatiwa kiasi kidogo cha fedha kwa kama mkopo ili akitumie haraka kwenda Tabora akisindikizwa na Mzee Kishindo ili akafanyiwe Tambiko na Zindiko kutoka katika Mizimu ya damu ya mama yake huko Kipalapala, Mizmu ya WASWEZI, Lakini Masu alishangazwa na taarifa alizopewa na Shamsi..
“Mbona sikuelewi Shamsi?” Alishangaa Masu
“Ndio hivyo Kaka, unajua mimi nimekulia uswahilini kama wewe, hayo mambo ya kishirikina ninayaelewa vema lakini hapa Ofisini kuna watoto wa Kishua tu hawayaelewi kabisa, wanachoamini wao kua wewe umechanganyikiwa hivyo wameamua kukusimamisha kazi kwa muda usiojulikana mpaka Boss atakapojiridhisha kua sasa umepona, na pia kama utaonekana hapo ofisini kwa kipindi hiki utaitiwa askari’
“Shamsi mbona nazidi kuchanganyikiwa ndugu yangu, sasa nitakimbilia wapi mie hapa nilikua nimekuja kuomba kukopa pesa kwa ajili ya nauli”
“Nauli ya kwenda wapi tena?”
“Si nimekudokeza kuhusu hilo suala la kwenda kufanyiwa tambiko huko Tabora”
“Sasa na wewe huna hata akiba nyumbani? Kwani inatakiwa kiasi gani?”
“Sio kama sikua na akiba, nilikua nayo kidogo lakini sasa nasikia Mzee Kikoko kamnyang’anya mke wangu kila kitu muhimu ikwemo na kadi za Benki na kwakua nitaenda na Mzee Kishindo hivyo nahitaji kama Tsh laki tatu tu zingenitosha kabisa” Masu alikua akitikisa kichwa kwa uchungu huku akiwa ameinamisha paji lake la uso chini kwa huzuni, kasha akamtupia swali Masu
“Sasa mwanzo uliniambia kua Mzee wako amewavamia pale kwa huyo Mzee Kishindo halafu akawaanzishia vurugu sasa huoni kua huyo mzee hatokua tena na nia ya kukusaidia?”
“Hayo nitaenda kuyajua hukohuko lakin kwanza niwe na pesa mkononi ili hata kama nitamshawishi na kumuomba radhi basi kazi itafanyika si unajua tena mkono mtupu haulambwi, Kwani humo ofisini yumo nani?”
“Aaah wamo tu kina Leylah, Hindu, nadhani na Yule dada mtata kutoka tabora”
“Ritha..??”
“Yeah Ritha, ila hao wote ndo wale wale wanamjaza Sumu Boss na kama wakikuona tu watampigia simu sasa hapo itakua shida kwako” Kikapita kimya cha muda mrefu kidogo kila mmoja akionakana kuzama katika dimbwi la mawazo, ndipo tena Shamsi akavunja ukimya
“Sikia ndugu yangu, mimi na wewe tumetoka mbali sana siwezi kukuacha ukiangamia, nitakuusaidia mpaka pumzi yangu ya mwisho”
“Nitashukuru kaka.. nifae ndugu yangu”
“Nitakupa hiyo pesa na utakapo rudi utanirejeshea, sawa?”
“Sawa kaka yaani nikirudi tu nitafanya mpango wa kukulipa”
“Ok usijali, ila sasa kwakua baba yako anaonekana kutaka kuvuruga kila kitu kwako sasa mie ninakushauru uje ulale kwangu na usimuambie mtu yoyote kua uko kwangu, au we unaonaje?”
“Yeah ni wazo zuri tu ila sasa kwakua umenipa uhakika acha sasa nikaongee kwanza na Mzee Kishindo”
“Poa, take care”
“Ok” Baada ya makubaliano hayo sasa Masu alipata nguvu hivyo akaanza tena kupuyanga kuelekea nyumbani kwa Mzee Kishindo huku kichwani akiwaza itakuaje kama atamkuta bado Mzee wake yuko kule

*****

Haikuchukua muda mrefu tayari Sheikh Jabu alikua ameshafunga breki za pikipiki yake mbele nyumba yake akiwa amembeba Mzee Kishindo, wakateremka na kuingia ndani, walipofika tu ndani wakakutana Mama Salman(Mke wa Sheikh Jabu) pale uani akiwa amefura kwa hasira
“Haya wenzetu mmeanza lini ubondia huko?” Mke wa Sheikh Jabu aliwauliza kwa kejeli
“Ubondia gani?” akajibu haraka haraka Sheikh Jabu
“Hamjui eeh”
“Hebu we fanya shughuli zako achana na mambo yasiyokuhusu..”
“Hayanihusu eeh.. ok sasa mtaenda kumtafuta Mama Masu kila kituo cha Polisi mpaka mtakapo mpata”
“Hee Mama Masu kakamatwa? Na nani? Na kwa nini?”
“Heheee, mie si hayanihusu haya kaeni na ujuaji wenu..” Baada ya kashda zile haraka Bi mkubwa Yule akachepuka zake ndani akiwaacha wazee wale wakitazamana bila ya majibu, Mzee Kikoko alipepesa macho huku na kule lakini hakumuona Mkewe, alizidi kuhamanika, ikabidi wamfuate kwa utaratibu huko huko sebuleni
“Mama Salma hebu kua makini kidogo mke wangu, imekuaje tena?”
“Wamekuja hapa maaskari utadhani kuna mtu ameua, wanamtaka Kikoko, wanadai alimpiga mkwewe na kumjeruhi vibaya na mbaya zaidi kaingia ndani kachukua pesa pamoja na kadi za benki walipomkosa ndo wamemchukua Mama Masu ili akaisaidie Polisi mpaka Kikoko atakapopatikana”
“Mungu wangu” Kikoko alijisemea huku akishusha pumzi nzito” Sheikh Jabu akamgeukia swahiba yake Kikoko
“Sasa na wewe kwanini umechukua hivyo vitu?”
“Jabu, vile vitu ni mali ya mwanangu sasa kulikua na ubaya gani mimi kuvichukua?”
“Sasa ukizushiwa umeiba vitu vingine vingi au pesa nyingi uatakatalia wapi na kweli uliingia chumbani?” Kikoko alibakia ameduwaa asijue cha kufanya

*****

Baada ya muda mrefu wa kutembea hatimae Masu alikua nje ya nyumba ya Mzee Kishindo, nyumba ilikua kimya, hapakua na dalili hata ya mtu ndani. Akasogea mpaka mlango halafu akategesha sikio lake mlangoni ili asikie kama kuna dalili za watu kule ndani, GHAFLA
“Toka hapo we mwanaharamu, naona sasa mnataka kuniulia mume wangu Toka kabisa kabla sijafika hapo” ilikua ni sauti ya mke wa mzee Kishindo ikitokea chumbani, Kumbe muda wote huo Bi mkubwa Yule alikua akimuangalia kupitia dirisha la mbele ya nyumba hiyo, Masu alihamanika akajua sasa tayari bwawa limeshaingia ruba, akajifanya kama hajaelewa alichoambiwa, akabaki amesimama kama mtoto ya yatima.
“Nakwambia TOKAA Hausikii wewe mpaka nije nikumwagie maji ya moto hapo?”
“Mama ungenisikiliza japo kidogo tu”
“Sina hata hamu ya kuyaona hayo magwambala yako hapo” Masu akabaki kimya akiwa amehuzunika, maswali kibao yakizunguuka kichwani mwake, alijiuliza kama mke tu amekasirika vile Je Huyo Kishindi mwenyewe yuko katika hali gani?, wakati anaendelea kufikiria ghafla akasikia sauti ikitokea kwa ndani zaidi, ilikua ni chumba cha uani, ni sauti ya Mzee Kishindo mwenyewe
“Mwache aingie kama ni Masu”
“Ili aje alete sekeseke lake humu au sio?, ukiumizwa au ukipelekwa Polisi atakaehangaika ni nani”
“Hapana huyo hana kosa lolote anahitaji kusaidiwa tu” Mke wa Kikoko akasonya kwa sauti mpaka kule nje akasikika , Masu kimoyo moyo alikua akimshukuru Mungu alianza kupata matumaini mapya kutoka kwa Mzee Kishindo ambae ndie aliekua kimbilio lake kwa muda ule, ghafla mlango ukafunguliwa akakutanisha macho na mke wa Mzee Kishindo akiwa amenuna vibaya

“Shikamoo mama”
“Hivi kwanini ninyi hamna huruma? Mpaka mumuue huyu mwanaume?” kabla Masu hajajibu lolote akasikika tena Mzee Kishindo
“We hausikii? Nimekuambia umuache huyo aingie” Yule mama akarudi ndani huku akiwa na jazba, Masu akaingia sebule na hapo hapo akakutana na Mzee Kishindo akitokea chumbani kwake, akamkaribisha kwa furaha tu kitu ambacho Masu hakukitegemea, alijiuliza mara mbili mbili juu ya ukarimu wa mzee Yule licha ya tabu anazomsababishia, Masu akenda mpka katika makochi akaketi kisha Mzee Kishindo nae akafuata, akaketi
“Masu uko salama mwanangu?”
“Niko salama mzee wangu, ila kwanza naomba kwa yote yaliyotokea unisamehe mimi, usinichoke mzee wangu tafadhali”
“Ahhh Masu achana na hayo, Yule baba yako kaishachanganyikiwa, sasa chamsingi tulishaongea mengi na sasa inatakiwa ufanye kila uwezalo tuanze utekelezaji wa mpango huu haraka iwezekanavyo” Masu akashusha pumzi, akafurahia kusikia kua mzee Yule hajabadili maamuzi hata kidogo, Basi kwa kua Masu alikua na uhakika wa kupata pesa akaongea mambo mengi na Mzee Kishindo wakakubaliana kua kesho yake asubuhi wakapande Basi waelekee Tabora, baada ya makubaliano hayo wakaagana na Masu akatoka na kuondoka zake

*****

Usiku majira ya saa mbili Masu alikua nyumbani kwa Shamsi wakijadiliana juu ya tatizo lake huku wakipeana ushauri wa hapa na pale
“…Zaidi ya yote Mungu ndie mjuzi ya yote atakusimamia,”
“Amiin, nashukuru sana kaka kwa ushirikiano wako”
“Sasa utachukua hiko ki begi kidogo maana hauna haja ya kwenda na nguo nyingi pia utachukua na nguo zangu kidogo tu” Baada ya mazungumzo yao, Shamsi akaingia chumbani halafu punde akatoka na bahasha ya kaki, alipofika pale seating room akaifungua na kutuoa pesa kisha akampa Masu ahesabu, Masu akahesabu na kuthibitisha Tsh Laki tatu taslim
“Nashukuru sana Shamsi, sina cha kukulipa ila Mungu ndie anajua cha kukulipa kwa wema wako”
“Ahh usijali kaka, sisi sasa hivi ni ndugu, sasa we ingia tu chumba hicho ukajipumzishe ili asubuhi usipate tena tabu ya usingizi”
“Ok poa, Mungu akipenda kesho” Masu akainuka akimuacha Shamsi akimuangalia kwa jicho la huruma sana, akingia chumbani kwa ajili ya kulala!!

Japo usingizi ulikua wa Mang’amng’am kutokana na kiwewe cha safari pia na hofu ya kutokewa na Hunudu, lakini hatimae akalala….

****

Ndani ya Basi la NBS kutoka Dar es Salaam kwenda Tabora, seat namber tisa na kumi walikua wameketi Mzee Kishindo na Masumbuko, walibahatika kupata seat zilizokaribu karibu hiyo ikawa ni nzuri kwao wakaweza kupata wasaa wa kupanga kila hatua wanayopaswa kiuifanya, hakika Kishindo alikua amejitoa kumsaidia Masu..
“Mama yako huko nimeacha tumenuniana, alikua hataki niondoke”
“Nik kweli unajua wanawake wana roho ndogo sana pia usikute anahofia kama Kikoko atatokea pale ghafla itakua shida”
“Hawezi kufanya lolote tena kwanza anatafutwa na Askari huko”
“Bora tu wameweke ndani ili sisi tukamilishe zoezi letu”
“.. haya ila sasa inabidi tuwe makini kwa kila nukta maana hii ni vita ya mizimu”
“Ni kweli mzee ila mimi naomba Mungu tu tufike salama kwani sidhani kama umakini wetu utaweza kuzuia nguvu zao kama watatuvamia hapa hao waufi”
“Ondoa shaka, kwanza kaa ukijua hauko peke yako, ile mizimu ya kwenu huko Tabora iko pamoja na wewe ndo maana kila walipokua wakikuijia usiku kwa njia ya ndoto kila walipotaka kukulazimisha kutoa kafara ulikua unashtuka usingizini, sasa ile na nguvu ya Waswezi ilikua inakuokoa”
“Kwa hiyo kumbe hiyo Mizimu inanitambua nayo?”
“Ndio, we ni damu yao kabisa hawaezi kukutelekeza, pia hata ule ujasiri wa kutoa siri zao unadhani uliupata wapi?”
“Mmmh”
“Ndio hivyo, hebu lete huo mfuko wangu hapo chini nikuoneshe kitu” Masu akautoa mfuko na kumkabidhi mzee Kishindo ambae alifungua na kutoa kitu falani hivi kama mkia wa Ng’ombe
“Unajua hii kitu?”
“Hapana, ni nini hasa?”
“huu unaitwa USINGE, nilipewa na wazee wa kwetu kigoma, kazi yake ni kupambana na nguvu za kichawi na ki mzimu kama zinazokusumbua wewe, hivyo kama litatokea tatizo kubwa tutatumia huo kutatua”
Safari ilikua ndefu sana, kutoka Dar kwenda Tabora ni hatua ndefu tena kama kipindi hiki cha mvua nyingi barabara nyingi hua mbovu sana, Hatimae Basi likafika porini sehemu na Konda akanadi
“Haya Abiria tuna dakika tano tu za ‘kuchimba dawa’..” haraka abiria wakaanza kuteremka na kwenda kwenye vichaka kwenda ‘Kuchimba dawa’, Mzee Kishindo nae akashuka lakini Masu hakushuka akaendelea kukaa pale pale kwenye seat yake, na kabla ya dakika zile kuisha mvua ikawa inaanza kunyesha kwa mbali, musa si mrefu abiria wote wakawa ndani ya Basi kuendelea na safari lakini Madsu akashtuka kuona gari inaanza kuondoka bila ya kumuona Mzee Kishindo
“We Konda hebu zuia mzee wangu hajapanda” Masu alimwambia Konda
“Sasa nae amekula nini? Tangu muda ule aah, Oyaa Suka zuia kuna mtu hajapanda” Dereva akazuia lakini mzee Kishindo hakuonekana, waliposubiri kwa takribani dakika kadhaa bila kumuona ikabidi Masu ateremke ili afuate kule kichakani akaangalie kuna nini? Wakati hua Masu anateremka ile mvua ilikua ikiendelea kwa mbaali, Masu aliingia mpaka kichakani lakini hakumuona mzee Kishindo
“Mzee Kishindo!!!, MZEE KISHINDOOO!!” Masu alikua akiita kwa sauti lakini hakujibiwa na mtu, ghafla mvua ikaanza kuongeza kasi na dakika chache tu mbele ikarindima mvua ya adabu, ilikua ni mvua kubwa sana kiasi kwamba hata mbelea hauoni, ikabidi sasa Masu ajaribu kukimbia tu kurudi kwenye kule alipoliacha Basi, lakini kila alipozidi kuongeza kasi alizidi kuhisi kupoteza muelekeo maana hakuliona Basi wala hata dalili ya Basi
“Hivi wameniacha au?” alijisemea peke yake Masu “Huu sio uungwana, sasa watatuachaje porini peke yetu? Halafu na mifuko yetu imo humohumo dah” Masu aliendelea kuulaumu upepo maana hakukua na mtu aliemsikiliza, Mvua alikua kubwa mithili ya enzi zile za Elnino, takribani nusu saa ilinyesha mvua kubwa ya mawe iliyofanya hali ya pale porini kuwa ya kutisha na kuogofya sana

Baada ya nusu saa ya kunyesha mvua ya kishindo sasa hali ikaanza kua shwari, mvua ilianza kupungua na hatimae kukatika kabisa, ilipokatika sasa Masu akiwa almelowana chepechepe akaanza kuangaza huku na kule kama atamuona mzee Kishindo lakini hakumuona ila kilichomshangaza zaidi hakuliona Basi walilokua wamepanda haikuchukua muda mrefu akasikia sauti ikimuita kwa kasi
“Masuuuuuu, njoooo” Masu akageuka haraka aliifahamu vema ile sauti, ilikua ni ya Mzee Kishindo, sauti ile ilikua ikitokea kwenye kichaka kikubwa tu upande wa mashariki mwa pori lile, Masu akakimbia mpaka maeneo yale na punde akamuona Mzee Kishindo akiwa amekaa chini, cha ajabu licha ya Mvua kubwa iliyonyesha lakini mzee Kishindo hakua amelowana hata kidogo
“Mzee vipi? Ulikua wapi?”
“Lete haraka ule USINGE wangu, tumeshavamiwa na Waufi “
“heee, Mzee usinge umo kwenye Basi na Basi lenyewe hata silioni itakua limeshaondoka”
“Kwanini sasa ulishuka jamani? Tumekwisha sasa”
“Sasa ningefanyaje maana uliposhuka wewe kwenye Basi ukachelewa kurudi ndo maana ikabidi nishuke kukuangalia”
“Halafu mbona umelowana hivyo?”
“Mzee inamaana wewe hukuiona mvua hii yote? Mvua kubwa yam awe mpaka mie nikawa sioni mbele”
“Mvua gani? Mbona mie sijalowana?” Masu alipigwa na butwaa, akaendelea kumuhoji Mzee Kishindo
“Kwani imekuaje mpaka ukasema kua Waufi wameshatuvamia?”
“Wakati nikiwa najisaidia hapo kichakani ametokea kijana mmoja mweupe kiasi ana Jicho bovu…” Kabla Mzee Kishindo hajamaliziakuongoa wakasikia mlio mkali sana kama wa Simba aliyejeruhiwa na ghafla akatokezea mnyama mmoja mweusi, mnyama wa ajabu haelewekua ni aina gani ya mnyama, akaanza kuja kwa kasi ya ajabu usawa ule waliokua wamesimama Masu na Mzee Kishindo
“TOBAA.. Masu kimbiaa” Mzee Kishindo alipayuko kwa hofu, wakatimua mbio za hatari, wao mbele yule mnyama nyuma, walikimbia kwa muda mrefu na kwa umbali mrefu mpaka wakabaki hio bin taaban bila ya kujua hatima yao ni nini na ghafla walipogeuka nyuma hawakumuona tena yule myama,

*****

“Khaa!! amepotelea wapi?” aliuliza Masu
“Mungu wangu hii sasa ni hatari kabisa”
“Sasa tutafanyaje hapa Mzee?”
“Tusubiri kufa tu, maana Usinge nao umeutelekeza kwenye Basi” wakiwa wamesimama wako hoi kwa zile mbio za bila kutarajia ndipo tena mvua ikaanza kunyesha ikabidi sasa wakimbile kwenye mti mkubwa uliokua pembeni ili wajisitiri, walipofika tu chini ya mti ule yaani kitendo bila kuchelewa Ikapiga RADI kubwa na yanguvu ikamrarua hapo hapo mzee Kishindo, akakauka na kua mweusi kama mkaaPia Radiu hiyo ikaunguza na ule mtiwaliokua wamesimama ukawa sasa unawaka moto tu! ilikua ni Radi ya hatari kisha mvua ikazidi kuchukua kasi yake, hakika Masu alikua amechanganyikiwa kisawasawa , akaanza kulia huku akiukimbia mwili wa Mzee Kishindo uliokauka kama vile ulio chomwa kwenye tanuri la mkaa, wakati masu akiwa ametaharuki ndipo tena alipomuona Yule mnyama mkali asieleweka akija tena kwa kasi inaonekana kama aliekua amewapoteza machoni pake akina Masu na Mzee Kishindo ambae tayari bila shaka ameaga dunia kwa Radi ya ajabu iliyomtandika vilivyo, Yule Mnyama
alionekana ana ghadhabu ya hali ya juu..

Masu akaanza kukimbia kwa kasi ya nguvu, sasa yule mnyama alikua amedhamiria kabisa kummaliza Masu, na sasa alikua akizidi kumkaribia, Masu alikua ameulenga mti mmoja mkubwa ili akifika ajaribu kukwea japo hakua na uwezo mkubwa wa kukwea miti, ila alijipa moyo kua angeweza tu bila ya kujali hata kama Mnyama huyo nae anaweza kukwea mti pia. Mnyama Yule alikua anakimbia kwa kasi kubwa kiasi sasa cha kumkaribia Masu, sasa Masu akajua kua mwisho wake umefika akaanza kulia kwa sauti kubwa sana lakini haikusaidia kitu, ilipobakia hatua kadhaa mnyama Yule amkamate Masu Masu akaongeza Speed kwa nguvu zake zote, Laa Haula!! Kumbe mbele kulikua na Shimo kubwa sana Masu hakulitambua hilo masikini! akatumbukia, lilikua ni Shimo refu kupita kiasi, Masu aliendelea kwenda chini bila kufika mwisho huku akijipigiza hovyo pembeni mwa shimo hilo bila ya kufika mwisho, hakujua kama lilikua ni Korongo au ni shimo la aina gani maana aliendelea kwenda chni bila ya kujua
atafikia wapi na muda gani.. hatimae alianza kusikia kizunguzungu kutoka na na kasi kubwa iliyokua ikimpeleka chini na hapo ndipo sasa akaanza kujua kua halikua shimo la kawaida bali itakua ni nguvu tu ya Waufi maana sasa ilichukua takribani masaa matatu akiwa anaenda tu bila kufika mwisho wa shimo hilo na hajui yataongezeka masaa mangapi kabla ya kufika chini, Pumzi ikawa inamuishia kutokana na upepo mkali aliokua akikutana nao wakati anazidi kwenda chini

DAR ES SALAAM

Nyumbani kwa Mzee Kishindo kilio kilikua kimetawala, watu wengi walikua wamejumuika, wake kwa waume, ndugu na majirani wote walikua wakilia kwa uchungu mkubwa, ni baada ya kupokea taarifa kuwa Mzee Kishindo amefariki kule Porini aliposhuka kujisaidia akapigwa na Radi kali, taarifa hizo zililetwa na Polisi baada ya kuthibitisha kutokea kwa tukio hilo…
“Jamani samahani, kwani ilikuaje?” aliuliza mzee Jfari jirani yake na Bw Kishindo, alimtupia swali hilo Sheikh Jabu aliekua tayari ameshawasili hapo msibani
“Kwa maelezo tuliyoyapata kutoka kwa mkwewe ni kwamba Kishindo na Masumbuko yule kijana wa Mzee Kikoko walikua safarini wakielekea Tabora lakini masaa mawili yaliopita amepokea simu kutoka Polisi kua mumewe amefariki kwa kupigwa na Radi ndipo akanipigia mimi haraka nikaenda Mochwari kuutambua mwili”
“Duh jamani mbona kama siamini vile!! Kishindo huyu huyu nilikua nae jana hapa?”
“Ndio huyo hivyo hakuna cha ajabu hapo, kwa Mungu ni madogo hayo, ila mwili umeharibika hivyo tunasubiri tu Ruhusa ya daktari tukauchukue mwili tuje tuusitiri, cha ajabu huyo Masu aliekua nae hajulikani alipo, wanadai amepotelea hukohuko Porini, yaani hizi taarifa zinachanganya sana”
“Hajulikani? Kivipi?”
“Inasemekana kua Mzee Kishindo alishuka kweny Basi kwenda kujisaidia lakini akachelewa sana kurudi ndani ya Basi hivyo sasa Masu akaenda kumuangalia lakini nae hakurudi wakati huo mvua kubwa ikawa inanyesha, na kabla ya mvua kukatika ndo ikapiga Radi kubwa, mvua ilipotulia ikabidi abiria washuke kwa ajili ya kujaribu kuwatafuta, ndipo walipomkuta Mzee Kishindo akiwa amefariki kwa KUPIGWA NA Radi hiyo mpaka kakauka, Lakini Masu hawakumpata kabisa”
“Mmh, haya sasa Maajabu’

***Tena si madogo!

ITAENDELEA


CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA SITA

“Inasemekana kua Mzee Kishindo alishuka kweny Buss kwenda kujisaidia lakini akachelewa sana kurudi ndani ya Buss hivyo sasa Masu akaenda kumuangalia lakini nae hakurudi wakati huo mvua kubwa ikawa inanyesha, na kabla ya mvua kukatika ndo ikapiga Radi kubwa, mvua ilipotulia ikabidi abiria washuke kwa ajili ya kujaribu kuwatafuta, ndipo walipomkuta Mzee Kishindo akiwa amefariki kwa KUPIGWA NA Radi hiyo mpaka kakauka, Lakini Masu hawakumpata kabisa”
“Mmh, haya sasa Maajabu’
*****

Masu aliendelea kwenda chini na hatimae akajikuta ameanguka kama mzigo au kifurushi, Naam Maajbu na mauzauza yameanza tena kwa Masu, kajikuta ameangukia katikati ya Zizi la Ng’ombe, cha Ajabu na yeye ni Ng’ombe pia, japo ameumia kwa jinsi alivyoanguka vibaya lakini sasa anastaajabu kujiona katika hali ile, akaanza kuhata hata, inaonekana hata wale Ngo’ombe wenzie wameshangaa kumuona pale bila shaka hawamjui kabisa, kulikua na Ng’ombe wakubwa sana, wana pembe mpaka zimejikunja kwa juu ya vichwa vyao, Masu akaanza kulia kwa woga lakini haikua sauti yake ile ya mwanzo, ilikua ni sauti mujaribu ya Ng’ombe, Ghafla akaanza kupokea kichapo cha haja kutoka kwa Ngo’ombe wenzie, Masu akawa anavuja damu kichwani baada ya kuchomwa na pembe la mmoja kati ya wale Ng’ombe waliokua waimuadhibu,,

Masu akiendelea kujaribu kujinusuru na kichapo kutoka kwa Ngo’ombe wenzie ndipo akawaona watu watatu wakija mpaka pale kwenye zizi, akawa anasikiliza mazungumzo yao, anatamani kuwajibu lakini kila akitaka kuwasemesha sauti inatoka kama ya Ng’ombe wengine tu, hali hiyo ilimtia sana uchungu sasa ikabidi tu atulie asubiri hatma yake, huku mazungumzo ya wale mabwana yakiendelea
“Mzee Songoro sisi ni ndugu zako na tumepatwa na msiba hivyo tunataka Ng’ombe kwa ajili ya pale msibani hivyo tufanyie tahfuf kidogo” aliongea mmoja kati ya wale vijana wawili
“Ni kweli, hata mimi na marehem Kishindo tulikua na ujamaa pia ila hiyo be nimewatajia ni ya chini kabisa kwakua tu nawafahamu na nimeangalia uzito wa jambo lenyewe” Masu alizidi kushangaa kusikia zile taarifa kua hawa jamaa wamekuja kununua Ngo’ombe kwa ajili ya kwenda kuandaa chakula msibani kwa Mzee Kishindo, alianza kulia baada ya kuamni sasa kua Kishindo amekufa, laiki alizidi kushangaa kua yaani pamoja na kuzama kwenye lile shimo kule kumbe ametokezea tena sehemu uliko msiba, hakika alijua kua amepatikana

Baada ya makubaliano ya muda mrefu sana hatimae wakaafikiana bei, wakalipana pesa, kisha Mzee Songoro akaingia zizini na kumkamata Masu(Ambae kwa sasa kawa Ngo’ombe) halafu akaanza kumfunga kamba, na baada ya muda ikaja gari na kumbeba Ng’ombe huyo na kumchukua mpaka msibani, Walipokua njiani Masu alishangaa kuiona mitaa ya jiji la Dar es Salaam, akajua kua kumbe amerudishwa kule kule mjini na sasa anakwenda kuchinjwa, Roho ilimuuma lakini hakua na ujanja tena na Baada ya muda akawa amefikishwa nyumbani kwa Mzee Kishindo, akateremshwa kwenye gari na akafungwa kwenye mti kwa kamba ngumu ya manila, Hali ya pale nyumbani ilithibitisha kua Kishindo hayupo tena duniani watu walikua wakilia kwa uchungu sana, Masu alimuona Sheikh Jabu, pamoja na vijana kadhaa kutoka kule dukani wanakokwenda kupiga stori, nao walikua katika majonzi na simanzi ya hali ya juu, kilichomuuma zaidi aliwaona kwa pembeni wanawe wadogo wale mapacha wakiwa wamesimama pale uani japo
hakumuona mkewe yaani Masu alipatwa na uchungu wa aina yake aisee

“Sasa jamani tugawane majukumu hapa haraka haraka kwakua wenzetu wameenda kufuatilia mwili, sasa sisi tungeanza majukumu mengine ya kupanga mazingira wakati wengine mkamchinje kabisa huyo Ng’ombe na mumchune kabisa” alikua ni Sheikh Jabu akijaribu kugawa majukumu pale msibani
“Sawa ila hapa hakuna mtaalam wa kuchnja Ng’ombe, Labda mumuite Mzee Kikoko ndio hua anachinja Ng’ombe” alijibu kijana mmoja pale msibani lakini alikatishwa na Jabu
“Mzee Kikoko hayupo ameenda kule ilipotokea hii kadhia, si mnajua mwanae kapotea ghafla huko ndio ameenda Polisi kujaribu kumtafuta”
“Aaah sasa nani ataweza kuchinja?”
“Ngoja nijaribu kuuliza hapo nje kwa hao waliokaa kwenye jamvi kama kuna mtu wa kuchinja” Sheikh Jabu akatoka, Masu alikua akiyasikia mazungumzo yote yale, alikua akilia kwa uchungu lakini haikusaidia kitu, alionekana kua ni Ng’ombe tu

Baada ya Muda Sheikh Jabu alirudi akiwa na kijana mmoja amevaa kofia ya kibaraghashia, bila shaka ndie Mchinjaji mwenyewe maana tayari ailiakua na kisu kikubwa mkononi, Masu alivyoinua macho AFANALEKI!! Alikua ni Hunudu Bin Waufi, Hunudu alisogea mpaka pale kwa Ng’ombe kisha akawaita wale vijana
“Njooni basi mumfungue kamba halafu mje tusaidiane kumshika tumalize harakaharaka” Masu alikua akilia kwa uchungu kila alipojaribu kujitetea kwa Hunudu hakuweza kusikika kwa kua sauti iliyokua ikitokani ni ya Ng’ombe. Wakati vijana wale wakija Hunudu akamsogelea Yule Masu halafu akamuambia kwa manenoya chinichini
“Kiburi na ujuaji ndivyo vinavyokuua leo, mwenzio kaisha kufa na kabla ya kwenda kumzika kwanza Ndugu, jamaa na marafiki watakula wewe nyama yako ndio tukamfukie huyo mwenzio, Pole Masu” Hunudu masikini akawa analia, cha ajabu mtoto wa Masu wa kike akawa nae amesogea pale halafu kama akaropoka
“Huyu Ng’ombe mbona analia mpaka anatoa machozi kama mtu?”
“Hebu toka hapa, kacheze huko” alifoka Hunudu
*****


UMATI wa watu ulifurika nje ya nyumba ya hayati mzee Kishindo, wanaume walikaa mbele nyumba hiyo kama ilivyo desturi ya misiba mingi ya kiislam, na wanawake walikaa uani, Sura za waombolezaji zilisawajika vilivyo kutokana na vilio vilivyotawala muda mrefu tangu kupatikana kwa taarifa za msiba huo, Msiba huu uliwagusa wengi, wake kwa waume, na hii ni kutokana na tabia njema alizokua nazo mzee huyu, Mzee Kishindo alikua ni msemaji, mchangamfu, na mcheshi sana, alikua na moyo wa upendo, wengi amewasaidia pale mtaani si kwa pesa basi hata kwa ushauri wake wenye busara, Wengi walihuzunika sana na kubaki na maswali kichwani juu ya utata ulio kigubika kifo cha mpendwa wao, Kifo chenye utata, Kifo cha kutisha, Kifo cha kuhuzunisha..

Vijana wengi walikua wamekaa katika vikundi vidogo vidogo wakijaribu kupeana mkasa mzima ulivyokua maana kama ilivyo desturi ya jamii nyingi ‘Apatwae na mkasa hupatwa na visa’, Tayari habari zilishajulikana kua marehemu alikua akienda Tabora kwa ajili ya kumpeleka Masu kufanyiwa matambiko kwenye Mizimu ya mama yake (japo hilo nalo liliwaumiza vichwa wengi tu kwakua mama yake Masumbuko wamjuao wao ni mwenyeji na mzawa wa hapohapo Shinyanga) kutokana na kusumbuliwa sana na mizimu, pia walikua wameshapata taarifa za tukio la kifo hicho kule Porini, pia habari kwamba Masu ametoweka kabisa hukohuko porini zilizidi kuwaacha vinywa wazi. Kila mtu alikua akisema lake, kila mtu alikua ni msimuliaji, hakika msiba huu ulizigusa hisia za wengi
*****

Pembezoni mwa nyumba ya Mzee Kishindo walikua wamesogea vijana kadhaa wakimfunga kamba Yule Ng’ombe kwa ajili ya kumchinja, hakuna aliejua kua Ngo’ombe Yule hakua Ngo’ombe wa kawaida bali ni binaadamu, tena wengine ni swahiba wao wa karibu, ila kutokana na kiini macho kilichofanywa na Mzimu wa Waufi alionekana kama ni Ng’ombe tu kumbe ni Masumbuko, Baaada ya kumfunga kamba vizuri Hunudu akajongea na kisu chake kikali kwa ajili ya kumaliza zoezi la kumchinja Masu/Ng’ombe lakini kutokana na nguvu za mnyama huyu ikabidi na vijana hawa waendelee kumshika ili achinjwe vizuri, wakati zoezi hili la kinyama na kuhuzunisha likiendelea Mtoto Fani, mtoto wa Masu aliekwenda msibani hapo na mama yake alionekana kuvutiwa na tukio lile kila mara alisogea japo alifukuzwa akacheze pembeni lakini aliendelea kung’ang’ania kukaa eneo lile, na kabla hajachinjwa Masu mwanae huyu akalopoka
“Kwanini mnamchinja Baba yangu?” Swali hili kutoka kwa mtoto huyu liliwashangaza wale vijana wakajikuta wanamuangalia wote kwa pamoja kila mmoja akiwa kama ameshangazwa na swali lile
“Baba yako yuko wapi?” aliuliza kijana mmoja akiwa katika hali kama ya mzaha maana aliamini kua yale maneno yalikua ni ya kitoto tu, ndipo mtoto akaendelea
“Basa si huyo mmemfunga kamba” baada ya jibu hilo, Masu alijisikia uchungu kupita kiasi kuona mwanae amemjua, Masu akashindwa kujizuia kaanza kulia kwa sauti akiamini labda angesikilizwa lakini sauti iliyotoka kinywani mwake ilikua ni mlio tu kama wa Ng’ombe wengine, Masu alihuzunika sana. Haraka Hunudu akamfukuza Yule mtoto
“Hebu nenda ukacheze huko pembeni”
“Namtaka baba yangu” Fani alipojibu tu kua anamtaka baba yake hapohapo akajipenyeza na kumng’angania Yule Ngo’ombe asichinjwe
“Hebu mtoeni huyu mtoto jamani tufanye kazi” Hunudu aliwaambia wale viajana waliokua wamemshika Yule Ng’ombe lakini vijana hawa walionekana kama kutomsikiliza sana Hunudu, tukio lile japo lilifanywa na mtoto mdogo lakini lilizivuta hisia za vijana wale, ndipo mmoja kati ya vijana wale akauliza
“Kwani huyu ni mtoto wa nani??”
“Ni mtoto wa Masu” alijibu kijana mwingine
“Mmh jamani hapa kuna kitu”
“Kuna kitu gani sasa? Yaani mambo ya watoto ndio yatukwamishe hebu acheni ujuha nyie” Hunudu alijikuta anashindwa kuzificha hisia zake na kuanza kuongea kwa ghadhabu

Wakati hayo yakiendelea, upande wa mbele ya nyumba uliingia msafara wa gari kama kama tatu hivi zikiwa zimeandamana huku zimewasha taa, kila mtu akageuka kuangalia, ilikua ni Maiti ya Mzee Kishindo ikiingia ndani kutokea Hospitali ilikofikishwa kwa ajili ya taratibu za kitabibu, watu wote walisimama kuupokea mwili huo, ikabidi sasa hata zoezi hili la kuchinja Ngo’ombe/Masu lisitishwe kidogo kwa muda ili vijana hawa wakaungane na wenzao kwenda kuupeleka mwili ndani , vijana wakajumuika pamoja na vijana wenzao waliokwenda kuuchukua mwili hospitali, wakafika pale kwenye zile gari, wakaupokea mwili wa hayati Bw Kishindo ukiwa umelazwa juu ya Machela huku umefunikwa na shuka za hospital, wakaushusha kwenye gari, wakaubeba vizuri kwa pamoja kisha wakaanza kuingia nao ndani, Wanawake walikua wamejaa pale sebuleni, wote wakasimama kuonesha ishara ya utii na nidham wakati maiti inaingizwa ndani, wanaume waliokua wameubeba mwili ule wakakatiza mpaka upande wa
kushoto ndipo kilipokua chumba cha marehemu wakaingia na mwili mpaka mule ndani. Chumba kilikua tayari kimeshasafishwa na vitu vyote vilikua vimeshatolewa nje, kulikua na kabati moja tu kubwa liligeuzwa ukutani, na kitanda cha kamba kwa ajili ya kuoshea maiti

Wakati wanaume wakiendelea kuuweka mwili vizuru kule chumbani, huku Sebuleni sasa wanawake wakaanza kulia kwa sauti huku wakiomboleza kwa maneno yaliyozidisha hisia kali za kuondokewa na mtu muhimu sana, Mke wa hayati Kishindo nae alishindwa kabisa kujizuia, alikua analia kwa sauti mpaka anaishiwa nguvu kabisa, kina mama wenzie wakawa wanajaribu kumbembeleza huku wakimpepea nakanga zaokutokana na joto la mule ndani ambalo lilimfanya atokwe na jasho sana, Ghafla Mama huyo akapandisha majini kichwani, akawa sasa ana nguvu za ajabu, nguvu zinazowazidia wanawake wenzie, alikua akitaka wamuachie, aingie chumbani
“Niachieniiii, nasema niachieni, Mume wa kiti wangu hajafa kabisa, Waufu manataka kumchukua Kishindo, nasema tutapambana mpaka mwisho” Maneno hayo ya Bi mkubwa Yule yalizidisha taharuki mule sebuleni, ikawa ni mkanyagano tu, wengine waoga wakaanza kutoka uani kabisa, lakinikina mama majasiri waliendelea kumzuia huku wakiomba msaada kwa wanaume maana sasa alianza kuwazidi nguvu,
“Tulia basi kwanza utueleze tatizo ni nini” aliongea bi mkubwa mmoja aliekua amejitahidi kumzuia mjane wa mzee Kishindo
“Huyo ndani sio Kishindo, ni mzoga tu huo, utoeni njeeee, nakuja kusaidia mume wa kiti, Kiti wangu hawezi kudhalilishwa mbele yangu” Watu walihamaki kusikia maneno haya, sasa Msiba ukazidi kunoga kwa taarifa za ajabu kila abaada ya muda mfupi, Wanaume wakaja mpaka pale sebuleni kusaidiana na kina mama ili kumtuliza mke wa Kishindo, pia ikabidi waingie ndani mashehe wataalamu wa masuala ya majini, wakaanza kumsomea dua mbalimbali ili atulie lakini wapi ikasindikana, Dua ziliendelea kwa muda mrefu bila kukata tamaa mpaka hatimae Mama yule akatulia sasa, Bila shaka jinni lilikua limeruka, Sebule nzima ikawa kimya, Bi mkubwa huyo akaanza kupepesa macho huku na huko alionesha kua ahakua akijua chochote kilichokuakikiendelea pale, akajikuta tu anauliza
“Kuna nini?”
“Hakuna tatizo shemeji, Presha ilitaka kukuzidia” Sheikh Jabu kwa hekma sana, baada ya Bi Mkubwa kutulia, watu wakatoka nje ili kuendelea na majukumu mengine pale msibani huku hofu ikizidi kutawala zaidi

Nje ya nyumba kila mtu alikua ameingiwa na baridi ya uoga na hofu, vikazuka vikundi vya majadiliano
“Hiki kifo kina utata wa hali ya juu sana kila kitu kama sinema vile” Mzee mmoja jirani wa karibu wa marehemu, aitwae Kabango alikua akiongea na wanaume wenzie nje ya nyumba ya Kishindo
“Mie hata huyo ng’ombe nimeshamtilia mashaka, hata mkimchinja mie sitokula” alijibu mmoja katika wale vijana waliokua wanajiandaa kwenda kumchinja Ngo’ombe
“Kwanini tena?”
“Sisi tunaona ni Ng’ombe halafu mtoto anamuona baba yake, halafu baba yake mwenyewe nasikia ndio aliepotelea huko porini”

“Mbona sijakuelewa kijana, hebu nieleweshe kwa kituo..” wakati stori zikizidi kutamalaki wakakatizwa na Sheikh Jabu aliesogea pale na kuongea harakaharaka huku akijiandaa kuondoka
“Sasa Bw Kabango mimi ninaondoka sasa hivi naenda Kituo cha polisi kumtoa Mama Masu mke wa Bw Kikoko si unajua yuko ndani?”
“Hapana sina habari, amefanya nini tena?”
“Kuna matatizo yaliotokea sasa askari wakawa wanamtafuta mumewe hivyo walivyomkosa ndo wakamkamata yeye, hivyo naenda kumtoa huko”
“Mhh haya sawa Kaka yangu, kwahiyo Kikoko yuko wapi?”
“Kikoko alikua ameenda huko ilipotoke ajail hii ya radi, maana mwanae nae ametoweka hukohuko, lakini taarifa mbaya zaidi nilizozipata ni kwamba hali ya Bw Kikoko imekua mbaya, na hivi sasa amepumzishwa katika hospitali moja pale Dodoma Sijajua ni Presha au ni nini! hivyo nikashamtoa mkewe tu huenda nikaondoka nikamuangile huko Dodoma hata maziko nadhani sitashiriki”
“Sasa Sheikh Jabu wewe ndio kinara hapa utakapoondoka itakuaje?”
“Hakuna kitakachoharibika, utabaki wewe kwa niaba yangu” Hapo hapo Sheikh Jabu akaondoka akiwa anaonekana kuzidiwa na majukumu kichwani, kapanda pikipiki yake na kisha akaondoka..

Hunudu alikua amesimama karibu na Ng’ombe/Masu kwa ajili ya kutekeleza zoezi la uchinjaji, hakika Hunudu alikua amemshupalia hasa kijana mwenzake, na kama alikua ametumwa na hao waufi basi alieetendea haki mizimu yao, vijana walisogea kushirikiana kumshika Yule Nng’ombe, Masu/Ng’ombe alilia kwa sauti kubwa ya uchungu ambayo iliotoka kama ilivyo kwa Ng’ombe wengine wanaokua machinjioni, Hunudu akasogea na kisu chake kisha akamshika kichwa na kuibinua shingo kwa juu, Koromeo likawa liko mbele likisubiri kisu
Wakati Hunudu ndo ananyanyua kisu achinje ghafla kikazuka kimbunga kikubwa sana, Kimbuka kilichoambatana na upepo mkali kupita kiasi, vumbi likatinga vilivyo eneo lile, watu wakainuka na kujificha sura zao kuhofia mchanga kuwaingia machoni, wengine walijigeuzia kwenye kuta za nyumba ili kuupisha upepo huo mkali upite, Kimbuka hiki hakikua cha kawaida kabisa maana kilichukua muda mrefu eneo moja tu pale pale msibani, mpaka baada ya dakika kama tano kimbunga kikaisha na kutoweka kabisa, vumbi likapungua, watu wakawa wanajifuta mchanga machoni, Vijana waliokua wameinama kumshika Ngo’ombe nao walikua wamesambaratika kwa Kimbunga kile kilichoacha gumzo pale msibani, baada ya hali kutulia watu wakarudi kukaa kwenye majamvi na wachinjaji nao wakarudi kuchinja, Hunudu alionekana kubadilika sura yake kwa jazba, ni kama vile ameshagundua kua hali haikua ya kawaida kabisa, Vijana wakasogea na kumshika Ng’ombe tena kwa mara nyingine ili achinjwe, sasa awamu hii
hata kabla Hunudu hajainama na kisu chake Kikazuka tena Kimbunga kikali kuliko kile cha awali, watu wakataharuki tena, kama ilivyo kawaida ya Vimbunga hua vinazunguka kwa mtindo wa duara huku kikihama sehemu moja kwenda nyingine, basi Kimbunga hiki kikahama na kusogea mpaka kule anapotaka kuchinjwa Ng’ombe/Masu kikazunguka eneo lile mpaka wachinjaji wakasambaana kisha Kikafuatiwa na Tetemeko kubwa sana la ardhi, baada ya sekunde kadhaa kimbunga kikasambaa kwa kuelekea juu!!!

TOBAA!!

Kimbunga kikampita Ng’ombe na kupeperuka nae juu ya anga, baadhi ya watu waliokua wamefumbua macho yao walishuhudia tukio lilela ajabu na la kuogofya sana, wakajaribu kuoneshana juu kabisa jinsi Kimbunga kinavyoondoka na Ng’ombe mzima, watu wakaanza kukimbia kwa woga, hakuna alieamini tukio lile la kustaajabisha, na baada ya sekunde chache hali ikatulia na upepo ukapoa na kurudi kama ilivyokua mwanzo, Kina mama wengi walitoka uani mpaka barabarani kuja kushuhudia kilichotokea kufuatia kelele zilizokua zikiendelea huku Barabarani
“Imetokea nini?” Aliuliza Bi mkbwa mmoja wa makamo hivi
“Tangu nizaliwe mpaka natoka mvi zote hizi sijawahi kushuhudia muujiza kama huu” alijibu mzee Kabango huku akiwa bado anaangalia juu ambako Kimbunga kimepotelea huko
“Nini hasa kimetokea sasa?”
“Ng’ombe amebebwa na kimbunga kimemchukua na kupotelea nae juu”
“Maajabu haya jamani” kila mtu alieshuhudia tukio lile alikua akiwasimulia vijana wenzie alichokiona
“Hapa kuna kitu tu sio bure, haiwezekani kila tukianza tu kumchinja Yule Ng’ombe kinazuka kimbunga, mara kimeibuka na kumpitia kabisa ng’ombe” alisema mmoja kati ya wale viajana waliokua wameinama kwa ajili ya kumshika vizuri Yule ng’ombe
“Halafu jamani si mnakumbuka Yule mtoto aliekua analia anasema tusimchinje baba yake, sasa ndo naanza kupata picha kamili”
“Halafu baba yake na huyo mtoto ni Masu huyu aliekua na marehemu huko porini na amepotea hukohuko”
“Jamani hapana, hili sio jambo la kufumbia macho”

Judith, mke wa Masu alikuwepo pale nje akisikiliza mkasa mzima hivyo akawa analia kwa uchungu mkubwa baada ya kuanza kupata picha kuwa inawezekana ni Mume wake huyo aliekua anataka kuchinjwa
“Kwani huyo Ng’ombe mlimnunua wapi?”
“Mimi hata sijui alinunuliwa wapi, itakua ni machinjioni tu” Watu walizidi kumiminika pale msibani, wengine walikua wanatokea maeneo ya mbali sana, nao walifika kufuatia kusambaa kwa taarifa hiyo ya ajabu kua Ng’ombe amebebwa na Kimbunga, Wazee wenye hekma walijitahidi kuwatuliza watu na kujaribu kuwafanya walichukulie lile jambo ni la kawaida tu ukizingatia pale ni msibani na hata maiti angali hajahifadhiwa bado, japo ilikua ngumu kueleweka ila kwa kiwango kidogo walijitahidi kuituliza hali ile na watu wakarudi kwenye utulivu uliokuwepo, japo stori zilizoendelea kutawala ni hizo tu
*****

Nje ya kituo cha Polisi cha Msimbazi alikua amesimama Sheikh Jabu akiwa amefanikiwa kumuwekea dhamana mke wa Mzee Kikoko, na sasa alikua akimpa habari zote za Mkasa wa Masu na kifo cha Mzee Kishindo, Japo mama huyu hakuonesha kushtuka kabisa kutokana na habari hizo, zaidi mama huyu alikua akiulizia hali ya mumewe tu
“Kwahiyo huko Ddodoma unaenda na nani?”
“Ninaenda peke yangu, we nakuchukulia bodaboda uende nyumbani ukaoge halafu uwahi msibani”
“Hapana mimi sitakwenda huko msibani kabisa”
“Shemeji kwanini usiende, hivi hauoni utaleta picha mbaya sana kwa jamii?”
“Hapana Sheikh Jabu, kumbuka kwamba ni majuzi tu marehemu aligombana na mume wangu nasikia mpaka wakapigana na mikia ya taa, halafu Mzee Kishindo ameng’ang’ania kumlaghai Masu, na sasa amefariki katika mazingira ya utata hivyo naweza kufika pale nikaonekana mimi ndio muhusika”
“Kwanini ujishuku kua umehusika, Shemeji jaribu kujifikiria mara mbili” Baada ya majibizano hayo wakaagana Sheikh Jabu akaenda kutafuta gari ya kumpeleka Dodoma kumuangalia swahiba wake na huku mke wa Kikoko akachukua bodaboda iliyompeleka moja kwa moja mpaka nyumbani kwa Sheikh Jabu ambako ndiko alikofikia
*****

AKIWA njiani kuelekea stand ya mabasi ya UBUNGO kwa ajili ya kuangalia kama ataweza kupata usafiri wa gari ndogo inayokwenda Dodoma, simu yake ikaita, kwakua alikua barabarani na anaendesha pikipiki hivyo hakujishughulisha kuipokea wala kuingalia, lakini mtetemesho aliouweka kwenye simu yake hiyo wakati wa muito ulimtoa katika umakini wa uendeshaji akajikuta anakosa utulivu kabisa, na kwakuhofia kusababisha ajali ikabidi apaki pembezoni mwa barabara ili aiangalia simu yake apate kumtambua huyo anaempigia simu, alipoitoa simu yake na kuiangalia ilikua ni namba mpya, akabonyezo kitufe cha kupokelea kishaakai lengesha spika ya simu hiyo katikati ya sikio lake la kushoto
“Hallo..”
“Sheikh Jabu?...” ilikua sauti ngeni kidogo kwake, hakuweza kuitambua vema
“Naam, ni mimi, we nani?”
“Mzee Kabango hapa naongea”
“Ndio Bwana mkubwa, kuna usalama?”
“Hakuna usalama, uko wapi sasa hivi?”
“Mie niko njiani naelekea Stand ya mkoa, mbona unanitisha?”
“Fanya hima urudi kaka, mambo yameharibika huku”
“Bwana Kabango, nilikuambia tangu mwanzo kua jukumu la hapo nyumbani ni la kwako sasa mimi nije kufanya nini tena! Hapa najitahidi kumuwahi Bwana Kikoko hali yake ni mbaya huko”
“Najua hilo, lakini mpaka nimekupigia ujue maji ya yametufika shingoni, Chondechonde fanya hima uje kila mtu anakusubiri wewe hapa” Simu ikakatwa ghafla na kumuacha Sheikh Jabu akibaki njiapanda asiejua pa kwenda, Hali ya Kikoko ilizidi kumtia hofu, huku msibani nako kuna umuhimu sana, alitafakari kwa kina mwishowe akaamua kurudi tu kule msibani ili akapate taarifa ya kilichotokea
*****

Huko msibani watu sasa walikua wametulia kidogo, utulivu ulirudi katika hali yake, na sasa watu wote waiofurika kuja kuangalia ule muujiza wa Ng’ombe kubebwa na Kimbunga walianza kusambaa na kuifanya idadi ile ya mwanzo ya wafiwa kurudi kama ilivyokua awali, Hunudu alitoweka katika mazingira ya ajabu sana kiasi cha kuacha maswali kwa watu wengi pale msibani maana kila walipomuangaza hawakumuona tena, na hata hivyo hakuna aliekua akimjua pale msibani. Pikipiki ya Sheikh Jabu iliingia pale msibani na haraka haraka akaigesha chini ya uga uliosukwa vizuri kwa nyasi kisha akajongea mpaka pale kwenye Jamvi kubwa la rangi ya kijivu, Baada ya kuwasalimu aliketi chini na kumfanya sasa Mzee Kabango aliekua amejilaza kama mtu aliekimbia kilometa kadhaa ainuke na kuketi huku wakiwa wametazamana
“Naam bwana mkubwa nimetika wito..” Baada ya Sheikh Jabu kufungua mazungumzo mzee Kabango alikohoa kidogo nae akaanza kushusha mtiririko wa kisa kizima kilivyokua mpaka mwisho, Kisa hiki kilimuacha mdomo wazi Sheikh Jabu, licha ya ujasiri ambao hua ndio vazi lake kuu lakini kwa hili aliingiwa na baridi ya hofu, watu kadhaa walijisogeza karibu pale kujaribu kuchangia mada
“Huyo aliyekua mchinjaji yuko wapi?”
“Ametoweka tu na hakuna aliemuona wakati anaondoka”
“Mnajua kweli huyo?”
“Hapana ila cha ajabu wakati tunataja wajih wake kuna Binti mmoja alishutuka sana akasema kua anahisi kumjua huyo mtu”
“Ni nani huyo binti?”
“Wanamuita Mama Zani..”
“Mmh Judith? Mke wa Masu?, Amemjuaje?”
“Anadai kua mumewe alikua akisumbuliwa sana kwenye Ndoto ya ajabu, na katika sifa za huyo mtu aliekua akimuota kila siku ndo huyo kijana mwenye Jicho bovu, sasa ukijumlisha na utata wa hili tukio la leo ndo kabisa ameamini” Kisa hiki hakika kilizidi kuacha maswali mengi yasiyo na majibu, Lakini kwa Hekma na Busara ikabidi Sheikh Jabu awatulize watu pale msibani kwa kuwanasihi kwa maneno ya busara sana mpaka wakatulia, akawaomba kwanza washirikiane kulimaliza suala la mazishi halafu hayo mengine yatapata muda wa kutosha wa kuyajadili, watu walimuelewa na sasa Shughuli za kuandaa mazishi zikaendelea kama kawaida, Ikabidi sasa bila ya kupenda Sheikh Jabu asisafiri tena na badala yake abaki pale nyumbani ili kukabiliana na matatizo yatakayojitokeza

Ilipotimu saa tisa alasiri watu walikusanyika nje ya nyumba ya Mzee Kishindo kwa ajili ya kufanya Ibada ya visomo maalum kama dua ya mwisho kwa marehemu wao, hakika watu walikua wengi kuliko kawaida, bila shaka wapo waliohudhuria kutokana na uvumi tu uliojitokeza wakati wa tukio lile, Naam Dua zilifanyika kwa ukimya na utulivu mkubwa tofauti na misiba mingine, Hatimae Mwili wa marehemu ukawekwa ndani ya Jeneza tayari kwa ajili ya kuswaliwa kisha kwenda malaloni kumuhifadhi.. Ikafanyika Sala ya Maiti iliyoongozwa na Sheikh Jabu mwenyewe, mbali ya ukaribu wake na marehemu pia Sheikh jabu alikua ni msomi mzuri tu na mjuvi wa masuala dini, Baada ya kumaliza swala hapakua na cha ziada tena maana hata chakula hakukuandaliwa tena tangu Ngo’mbe apotee ghafla, hivyo wanaume wakanyanyua Jeneza na kuliweka katikati ya mabega na shingo zao kama ilivyo kanuni na taratibu za ubebaji wa Jeneza, na safari ya mwisho ya hayati Kishindo ikawa inakaribia kufikia tamati

Makaburini hapakua mbali sana na nyumbani hivyo safari ya mwendo wa miguu tu ilitosha kuwafikisha katika viwanja hivyo vya makaburi ndani ya muda wa kama nusu saa hivi, na taratibu zote za mazishi zikafanyika na hatimae Kishindo akazikwa, ilikua ni huzuni na vilio kila kona, vijana kwa wazee walishindwa kuzificha huzuni zao na kuangua vilio hukohuko makaburini, hapakua na Jinsi tena maana neon la Mungu limetimia, Wafiwa na ahali zao wakarejea nyumbani baada ya kumalizia dua ya mwisho katika kaburi la Marehemu Kishindo

ITAENDELEA

CHANZO BURE SERIES
 
SEHEMU YA SABA

Makaburini hapakua mbali sana na nyumbani hivyo safari ya mwendo wa miguu tu ilitosha kuwafikisha katika viwanja hivyo vya makaburi ndani ya muda wa kama nusu saa hivi, na taratibu zote za mazishi zikafanyika na hatimae Kishindo akazikwa, ilikua ni huzuni na vilio kila kona, vijana kwa wazee walishindwa kuzificha huzuni zao na kuangua vilio hukohuko makaburini, hapakua na Jinsi tena maana neon la Mungu limetimia, Wafiwa na ahali zao wakarejea nyumbani baada ya kumalizia dua ya mwisho katika kaburi la Marehemu Kishindo
*****

MKOANI SHINYANGA, Kama ilivyo ada nje ya nyumba ya Mzee Kagomba hukusanyika watu wa rika tofauti kwa ajili si tu ya kununua kahawa bali pia kupashana habari zinazojiri ndani na nje ya mkoa wao, na kwa siku hiyo habari iliyochukua ‘Ukurasa wa mbele’ katika kijiwe hicho cha kahawa maarufu kama BBC ni taarifa za matukio yanayoendelea huko jijini Dar katika familia ya swahiba wao Mzee Kikoko, walikua wakizipata habari za matukio yote kupitia kwa wenzao kadhaa walioko huko, na kwakua Kikoko mwenyewe alishapata kuwaeleza kila kilichokua kikimsibu mwanae kupitia Ndoto ya ajabu,
“Unajua tangu mwanzo sisi tulimuhadhari Bw Kikoko kua hiyo Ndoto ya mwanae si kitu chepesi kiasi hicho na tukamnasihi kua aende kwa Mzee Maguno huenda akasaidiwa ushauri na tafsiri ya Ndoto hiyo ya mwanae lakini Mjuaji Yule akatupuuza..” Mzee Kagomba alikua akizungumza na hadhira ile iliyojikusanya kuizunguka meza yake ndogo ya kahawa, Bahati nzuri siku hiyo mzee Maguno nae alikuwepo kijiweni hapo, akamuwahi kumdakia neno Mzee Kagomba
“Kwangu asingeweza kuja kwakua mimi naijua vema kesi yao hiyo ya Mizimu ya Waufi”
“Ni mizimu ya waufi au Dini ya waufi? Maana sisi tulisikia kua ni dini”
“Hakuna dini ya hivyo hiyo ni mizimu ya huyo mkewe mkubwa, ila katu hawatomuweza Masu japo ni kijana wao wenyewe, mwenzao anasaidiwa na Mizimu kutoka Kigoma kwa babu yake mzaa baba na pia anasaidiwa na mizimu ya umamani kwake Tabora” Maneno haya yalionesha kuwaingia sana watu wote pale, ikawa kimya kimetanda mpaka Mzee Kagoma alipovugumiza swali kwa Mzee Maguno
“Sasa mnatuchanganya, huko Tabora kwa mama yake gani wakati mama yake ni huyuhuyu Mama Masu wa hapo kwa hayati bwana Masanja, na inakuaje unasema kua hiyo mizimu ya Waufi ni ya mke mkubwa wa Kikoko wakati huyo mke mkubwa ndie mama yake mzazi na huyo Masu?” Mzee Kishindo akacheka kidogo, kisha akajiweka sawa katika kiti chake kirefu cha uvivu kilichofungwa kwa kitambaa cha rangi ya maziwa ili aanze kuwapa somo wadau wa BBC KAHAWA. Lakini kabla hajasema chochote aliwasili motto mkubwa wa Mzee Kangomba anaefanya kazi ofisi za Tanesco, anaitwa Abuu, alipofika akawasilimu
“Wakubwa Shikamooni”
“Marahaba..”
“Jamani mna habari za mjini huko au mmekaa tu?” Swali hili liliwashtua wanywa kahawa wote na kufanya Mzee Kagoma amjibu manae huyo
“Habari gani tena mwenzetu?”
“Mzee Kasimba amefariki huko”
“We motto!! Kasimba Amefariki?.. Innalillah..”
“Kasimba ndo nani huyo?” aliuliza Mzee Maguno aliekua ameunika kidogo kwa mshituko kutoka pale katika kiti cha uvivu alichokua amejiegesha
“Aaah yaani we humjui Kasimba? Sema tu mtu kidole unamjua ukimuona ni shemeji yake na Bwana Kikoko”
“Aaah nimeshamjua si ni Yule bwana mrefu anapenda kunyoa kipara muda wote pia hua kama mgangamganga hivi?”
“Naam huyo huyo, na huo uganga ni wa urithi kutoka kwa marehemu babu yao” Watu wote walisikitishwa na taarifa zile, ndipo sasa Mzee Maguno alipomgeukia tena aliezileta habari hizo ambae ni Abuu
“Enhee, alikua anaumwa? Na amefariki saa ngapi?”
“Sasa ninyi ndo mnajifanya eti BBC halafu hamna habari nyeti kama hizo, hamna u BBC wowote” Abuu alijibu kwa mzaha huku akimuangalia usoni mzee Maguno ambae alikua kama hamuoni vizuri kutoka na mwanga hafifu wa chemli ndogo iliyopo juu ya meza ya kuuzia kahawa
“Embu acha upuuzi wako bana, hii ni BBC ndo maana hata wewe umetoka na habari zako huko na kuja kuripoti hapa kitu kikuu cha habari Shinyanga mjini” Watu wote wakacheka kwa pamoja kabla ya Abuu kuanza kuwapa habari zilizozidi kuwaacha vinywa wazi
“Yule bwana amekufa ghafla, amekutwa katika vile vijumba vyake vya kufanyia mambo yao ya uganga mnaviita ‘Nzu’ Akiwa na jeraha dogo kifuani upande wa kushoto lililotengeneza tobo, Baadae imegundulika kua alinyofolewa moyo kwenye jeraha hilo, na pia amekutwa na alama za vidole na michubuko kama vile alikabwa sana kooni na kukwaruriwa kwa kucha maeneo ya Shingoni” watu walizidi kupigwa na mshangao huku wakimkodolea macho Abuu ili aendelee kuwapa habari,
“Ebwana eeh, mbaona mauji ya kinyama sana!! Sasa kama hizo alama za kucha na vidole ni za muuaji basi lazima atapatikana kama hakuzitifuta kwa kitambaa, siku hizi teknolojia imekua sana” alisema kijana mmoja aliekua ameketi tu bila ya kinyaji maridhawa cha kahawa
“Agundulike mara ngapi?” alijibu Abuu na kuwafanya watu wote wamgeukie kumsikiliza nae kwa maringo akajifanya kama hana hamu ya kuwapa habari hizo akaanza kuondoka kuelekea ndani kwao
“We mtoto kuja hapa, na ukiondoka nitakutolea radhi” Aliongea Mzee Maguno kwa sauti kali lakini ya Mzaha ili kumfanya Abuu arudi, nae karejea
“Mie siwezi kusimama hapa naongea tu hata kiti hamnipi, wala kahawa hamninunulii wakati nawapa habari nyeti ambazo pamoja na uBBC hamjazipata licha ya kua zimetokea tangu saa sita mchana”
“Hee tangu saa sita? Kweli dunia sio kijiji tena, hebu kaa kiti hicho hapo kipo wazi”
“Mninunulie na kahawa kwanza”
“Hilo tu? Sema jingine, kama kahawa inalewesha basi leo utaema kushoto kasha utafukia kulia, utakunya TANI yako” Alijibu tena Mzee Magunokwa mshawasha wa hali ya juu, hakika zilikua ni habari tamu na za majonzi kwa upande wa pili,
“Hizi habari bado ni siri, mie ninawadokeza tu kwakua nilizipata kutokea kwa chanzo changu cha habari ndani ya kitengo muhimu na nyeti sana, hivyo muwe makini kuzisemasema kwa sasa, mkikamatwa mie simo”
“Tupe ufyetere huo kaka mkubwa” alijibu kijana mwininge aliekua ametulia akisikiliza kwa usongo
“Baada ya maiti kufikishwa hapo katika Hospitali ya ‘Gavumenti’ vipimo vikafanyika ambapo walizichunguzo hizo alama za vidole mnaziita sijui fingaprint” Watu wote walikua kimya wakimsikiliza, akachukua kikombe kidogo cha kahawa alichokua tayari ameshamiminiwa na baba yake Mzee Kagomba ambae muda wote alikua kimya akisikiliza kisa hicho kipya
“Alama za vidole zilizopo katika mwili wa marehemu zimegundulika kua na za mtu mmoja anaitwa Kishindo Rehani”
“NINI?? Kishindo rehani huyu wa Dar?” aliliza kwa mshangao Mzee Kagomba
“Huyo huyo aliekufa majuzi kwa kupigwa na Radi na kuzikwa juzi”
“Mtoto acha maskhara tafadhali”
“Sio wewe tu, hata uongozi wa usalama na jopo la madaktari wote hawaamini kilichoonekana kwenye vipimo vyao wenyewe na ndomaana wameamua kuifanya siri kwanza”
“Sasa nimepata majibu kamili, vita ya mizimu imeanza” alidakia tena mzee Maguno ambae ni gwiji wa Nujumi(Masuala ya Nyota) na Tafsiri za Ndoto, Kauli hiyo sasa ikawafanya watu wote pale wapate kiu ya kusikiliza hiyo vita, nae Mzee Maguno hakusubiri kuambiwa aendelee ‘kumwaga mchele’
“Iko hivi siku yoyote ukikuta mtu ameuawa kisha ametobolewa sehemu ya kifuani wakaunyofoa Moyo wake ujue huyo mtu ni Mchawi au anahusishwa na Uchawi…” Akavuta kikombe chake cha kahawa kisha akaendelea “..Iko hivi wachawi wote duniani hua wana kitu mfano wa Fitra kinakua ndani ya moyo wa kila mmoja wao na hicho ndo uchawi wenyewe hasa, na kinamtambulisha kwa wachawi wenzie popote atakapokwenda hata kama ni nje ya nchi, pia kazi ya kijidubwasha hicho ni kumuamsha huyo mchawi kila ifikapo usiku wa manane kwa ajili ya kujumuika na wenzake katika shughuli zao za kichawi, ndomaana mchawi yoyote hata kama awe amechoka vipi ikifika muda wa kwenda kuwanga usiku lazima atashituka tu, sasa huyo Bw Kasimba anahusika kikamilifu katika hii kadhia ya huo mzmu wa Waufi akisaidiana na dada yake ambae ni mke wa Kikoko, sasa itakua nguvu ya Mizimu ya WASWEZI ya huko Tabora umamani kwa Masu na nguvu nyingine ya mzimu ya WALUWA kutoka Kigoma na Kongo kwenye asili ya
ubabani kwa Masu imeanza kumsaidia mtumishi wan a kijana wao ndomaana katolewa moyo ila ngoja tuvute subra tutayasikia mengi tu..” Maneno hayo ya Mzee Maguno yaliwaogopesha wengi pale kijiweni na pia yalizidi kuacha maswali mengi hata kwa mtu mzima Kagomba pia ambae alishindwa kujizuia na kuendelea na maswali yake ya kidadisi na kichokonozi
“Sasa kwani mama yake na Masu sio huyu tumjuaye sisi? Na ni yeye anaemroga Masu? Na kwanini sasa vipimo vioneshe kua muuaji alikua ni marehem Kishindo ambae sio Masu anaeteswa kama ni kweli” Baada ya swali hilo kila mmoja alimgeukia Mzee Maguno kusikia jibu ambalo bila shaka lilikua likimkwaza kila mmoja pale
“.. Jibu ni jepesi sana, Ni hivi Ya Ngoswe mwachie Ngoswe, nay a Kaisari..??” alijibu kimkatao tu Mzee Maguno
*****
*****


NDANI ya Nbs, Basi lifanyalo safari zake toka Dar es Salaam kwenda Shinyanga, seat za katikati walikua wameketi Sheikh Jabu na Mama Masu, na safari yao hii ilikua ni kuelekea Shinyanga msibani, tayari taarifa za kushtua za msiba huo ziliwafikia tangu jana yake hivyo ikabidi tu sasa wapange safari ya kurudi Shinyanga ili wajaribu kuwahi mazishi, ndani ya gari sura zao zilikua zimesawajika kwa matatizo makubwa yanayoendelea kujitokeza, Matatizo ambayo hakika ni mitihani mikubwa kwa familia yoyote ikikubwa, Raha na amani ilianza kufifia tangu ilipoanza ile Ndoto ya ajabu aliyokua akiiota Masu, Ndoto hiyo ikapelekea Mzee Kikoko akapigana na marehem Kishindo akimtuhumu kumfitinisha na mwanae, Ndipo Mzee Kikoko akacharazwa na mkia wa taa, Mara Kikoko akazidi kugombana na Mkwe wake kwa Masu akimtuhumu kumroga mwanae na kumtorosha pale nyumbani, Kesi ya Kikoko ikiwa tayari chini ya mikono ya Polisi mara Kishindo akafa kwa kupigwa na radi akiwa safarini,
ikagundulika kwamba katika Safari hiyo iliyomtunukia kifo Mzee Kishindo kumbe alikua na Masu, Cha ajabu baada ya tukio hilo la ajali ya Radi ane akapotea ghafla huko msituni, mara msibani mke wa marehemu kapandisha majini akidai kua mumewe katekwa na Waufi, mara mtoto wa Masu anasema Yule Ng’ombe aliebebwa na Kimbunga ndie alikua baba yake, Basi ni songombingo kila kukicha, na sasa Bw Kasimba kaka yake na Mama Masu nae ameuawa kinyama sana kwa kunyofolewa moyo, mawazo yalionekana kumzidia mama Masu aliekua akitiririsha machozi mashavuni mwake kila nukta.. Maziko yalikua yamepangwa kufanyika siku hiyohiyo kutokana na hali ya mwili wa marehemu lakini ikabidi muda waupeleke mbele kidogo mpaka saa kumi alasiri ili kujaribu kuwavutia muda Mama Masu na Sheikh jabu ambao walikua wameshatoa taarifa kua wapo njiani wanakwenda,, Na kwa taarifa za kimawasiliano kutoka kwa Mzee Kikoko alieko hospitalini Dodoma na swahiba wake wa karibu sana Sheikh Jabu
zilidhihirisha kua hali yake haikua mbaya sana hivyo aliahidi kua yeye angelihudhurua huko msibani keshokutwa baada ya kupata ruhusa pale Hospital kwahiyo akawa amemridhia Sheikh jabu akamuwakilishe huko msibani kwa Shemeji yake
*****
Koplo Sebastian Bangirana kutoka kituo cha polisi cha wilaya ya Shinyanga kilichopo jirani na mahakama alishawasili pale msibani kwa ajili ya mahojiano na wanafamilia kama mpelelezi wa kesi ile, aliingia pale msibani akiwa amevalia sare zake za kazi zilizomkaa vizuri maungoni ukijumlisha na ule mwili wake uliojengeka kimazoezi basi alionekana ni kamanda kwelikweli, alienda mpaka pale jamvi walipokaa wafiwa, akavua viatu kiustaarabu na utulivu kisha akajisogeza karibu nao, alipofika pale kila mtu alikua makini kumpokea afande huyo, akavua miwani yake ya macho halafu akawasalimia salam kwa lafudhi iliyodhihirisha kua hakua muumini wa dini husika
“Saramaleku”
“Waaleykum salam..” Walimuitikia wazee hao huku wakimkaribisha “Karibu sana Afande..”
“Ok ahsanteni jamani, Poleni sana na matatizo”
“Aaah bado hatujapoa, ila ndo kazi ya Mungu haina makosa”
“Mimi ni Ofisa wa Polisi kutoka kituo cha kati, naitwa Sebastian Bangirana unaweza kuokoa nguvu na muda kwa kuniita ‘BANGI’..” Wazee wote waliangaliana halafu wakaachia tabasam hafifu kusikia mtu najiita Bangi japokua ilikua ni kifupi cha jina lake, baada ya utambulisho huo Sajent BANGI akaendelea
“Naweza kumpata kiongozi wa familia kwa ajili ya mazungumzo kidogo?” Mzee Maguno na Mzee Kagomba nao walikua wamejilaza hapo jamvini wakisikiliza mazungumzo hayo
“Kiongozi wa familia ndo huyo aliefariki, ila mimi nipo kwa niaba yake”
“Ok hata wewe utanifaa tu, tunaweza kusogea pembeni kidogo kwa mazungumzo kiasi?”
“Haina shaka Afande” alijibu Bwana huyo aliejitambulisha kua ni kwa niaba ya familia, wakainuka na kusogea mbele kidogo ya nyumba ili wawe huru kuzungumza kuhusiana na tukio hilo la mauaji, inaonekana Mzee Kagomba hakupenda jambo lile la Afande kutaka mazungumzo yake yawe faragha, bila shaka alitaka ‘kunyonya’ umbea wa kwenda kuuongea jioni maeneo ya ‘BBC’
“Poleni sana kwa msiba mzito sana kwenu” alianza Afande Bangi baada ya kusogea pembeni
“Ahsante Afande”
“Umesema wewe ni nani hapa?”
“Mimi ni Katembo Masanja, mdogowake na marehem Kasimba Masinja”
“Ohh kumbe we ni mdogo wa marehem, mmh mbona majina yenu ni ya aina moja? Katembo. Kasima?” Swali la Inspekta Bangi lilimfanya Bw Katembo akaachia tabasamu la mbali kisha akajibu
“Marehemu baba yetu alikua ni kiongozi mkubwa sana katika kabila lao, na pia alikua ni mganga mashuhuri sana hivyo maisha yake ikiwa pamoja na hili la kutoa majina kwa baadhi ya wanae lilijikita kiimani na kimila zaidi”
“Safi sana wazee wetu walikua wakizienzi sana tamaduni zetu, sasa hebu niambie ilikuaje wakati marehemu anafariki?”
“Mimi binafsi sikuwepo hapa nyumbani, mimi hua naishi sehemu nyingine huko nimepanga hivyo nilipigiwa simu na mama Salum kua kaka amefariki ndipo nikaja haraka nyumbani”
“Huyo mama Salum ni nani?”
“Ni Mke wa Marehemu”
“Unamjua Mzee Kishindo?”
“Sijawahi kumuona ila namfahamu tu kwa jina kwa kua ni rafiki wa Shemeji yetu, mume wa dada yetu, nae nilisikia kua amefariki kwa kupigwa na Radi na muda huo alikua na mtoto wa dada yetu huyo anaeitwa Masu ambae nae tangu tukio hilo alitoweka ghafla”
“Huyo shemeji yako ndo Mzee Kikoko?”
“Ndio huyo”
“Kikoko amekua Bidhaa adimu sana mikononi mwa Polisi”
“Kwanini Afande?”
“Ahh tuacheni nae, kwa ukaribu wako na marehemu Je kuna mtu yoyote alikua anadaina nae au alikua na ugomvi nae?”
“Hapana sijawahi kusikia maana watu wengi walikua wakimuheshimu sana kutokana na uganga wake, amewasaidia wengi sana”
“Kwahiyo Kikoko yuko wapi?”
“Nasikia alikua anaumwa ila yuko njiani anakuja msibani” Baada ya mahojiano ya muda mfupi, Sajent Bangi alitaka kuonana na mke wa marehemu lakini ilishindikana kwa wakati ule maana hali ya mke huyo ilikua mbaya sana kutokana na kifo cha mumewe basi Sajent Bangi akamuaga Bw Katembo na kumuahidi kua takuja mazishini, ila akamsisitiza kua asimuambie Mzee Kikoko kua aliuliziwa na Polisi, kisha Sajent akaondoka zake
*****

Ndani ya chumba kidogo, walikuwemo watu kama watano hivi wamesimama huku wakiwa wameizunguka maiti iliyomo ndani ya Sanda, walikua wakijadili kuhusu utaratibu wa kumzika maiti huyu, kulikua na mabishano ya namna bora ya kuyafanya maziko hayo
“Hapana, hiyo ni hatari zaidi, kwasasa hatuna muda wa kupoteza ni kumzika tu kama hajafa vizuri basi atamalizikia humu humu kaburini” alisema mzee mmoja wa makamo
“Tutakua hatujafanya kitu, mie nadhani huyu kijana atakua ameshajifunza kua nguvu yetu ni kubwa kiasi gani na atakubali tu kujiunga na kutoa kafara ya mwanae mmoja” alijibu mmoja kati ya wale watu mule ndani
“Acheni mawazo yasiyowezekana, huyu azikwe tu tena sasa hivi tumalize huu udhia vinginevyo tutazidiwa nguvu halafu tutaangamia wote, kaeni mkijua kua mizimu ya kwao huko Tabora imeanza mapambano nasi huku ikisaidiwa na mizmu ya Kigoma kwa Mzee Kikoko kwahiyo nguvu yao ni kubwa sana, hebu fikirieni kua wameweza kumuua Kiongozi mkubwa wa ‘Nzu’ ya Waufi bwana Kasimba, hivyo kama tutamkosa huyu kijana basi mjue Mizimu hiyo itatumalizia na sisi pia mkumbuke tuna deni la damu yakara kutoka kwa wakuu wetu wa Waufi, Mizimu inataka damu ya kafara hivyo tutaambiwa tumtoe mama yake mzazi ambae ni mtiifu kwa mzimu itakua ngumu sana,” alijibu kijana mmoja aliekua amejifunga kitambaa Chekundu kichwani, alikua ni kijana mrefu kiasi, ana sura ya kikatili sana inayosababishwa na Jicho lake bovu, huyu ni Hunudu

Katikati ya Sanda hiyo alikua maevingirishwa na kufungwa kama Pipi kijana Masumbuko Kikoko tayari kwa ajili ya kwenda kuzikwa akiwa hai, japo alikua hai lakini alikua ni nusu mfu maana hakua na uwezo wa kusema lolote wala hata kutikisika mithili ya mtu aliechomwa sindano ya nusu kaputi, alichokua anaweza kufanya ni kufumbua macho na kusilia tu, bali vingine vyote havikua tena kwenye mamlaka yake, alijitahidi kuwajibu wale mabwana kutoka katika Mizimu ya Waufi lakini mdomo ulikua mzito kama mtu aliyechomwa sindano ya ganzi wakati wa kung’oa jino, alipojirabu kujitikisa japo kidogo ilikua ni zoezi gumu sana kwake ikabidi atulie tu aendelee kusikilia majadiliano ya kikatili sana dhidi yake, kilichomshtua zaidi pale aliposikia kua mama yake ni mtiifi sana kwa Mizimu yao hivyo hapaswi kuuawa zaidi yake yeye ndipo akaanza kukumbuka maneno ya Marehemu Kishindo kua mama yake alisaidiwa na Mizimu kuinyakua mimba ya mke mwenzie na kuiamishia kwake kwa njia ya
nguvu za giza, akiwa anavuta picha aliwasikia watu wale waliosimama huku wakiwa wamemzunguka wakiafikiana kua akazikwe tu kufuatia Ushauri uliotolewa na Hunudu, Masu alipata uchungu sana kuona sasa anaenda kuzikwa akiwa hai, kajikaza na kutoa sauti kali ya kuashiria kua wasimuue lakini sauti haikutoka hata kidogo..
“Kaburi mlichimbia wapi?” akauliza Hunudu
“Hapo kwenye shamba la midizi”
“Mna uhakika ni refu?”
“Ndio, zaidi ya futi tisa”
“Vizuri, haya mnyanyueni huko twende haraka haraka kabla hakujapambazuka” Masu alikua katika wakati mgumu akijaribu kuipigania nafsi yake bila ya uwezo wowote, akaona ananyanyuliwa juu kutokea pale chini alipokua amelazwa, GHAFLA Masu akajishangaa anapata nguvu na ujasiri wa ajabu akapiga KELELE Kali sana, akaijikua anafumbua macho na kujigundua kumbe alikua usingizini anaota, alijitikisa kichwa ili aone kama yuko sawa, taarifa kutoka katika ubongo wake ikazidi kumthibitishia kua alikua akiota tu, lakini kumbukumbu zake za mwisho anakumbuka alivyosombwa na Kimbunga kikali sana kikampeleka masafa marefu kwenda juu na hakujua mwisho wake, akainuka pale juu ya kitanda kidogo cha chuma, akasimama na kuanza kuangaza huku na kule ndipo akamuona Mzee mmoja akiwa amesimama karibu ya kitanda hicho, alijaribu kumuangalia vizuri na baadae sura ikaanza kumuijia japo hakuweza kwa haraka kutambua alimuona wapi mzee huyu
“Pole sana Masu, hila za Hunudu sasa zinafikia tamati, hawezi kukuzika mshenzi huyo, Sisi tunapambana na waliomtuma, acha yeye ajidanganye tu” Maneno haya yalizidi kumpa maswali zaidi Masu kua hapa yupo wapi na huyu ni nani hasa, lakini baada ya Masu kumtazama Mzee huyu kwa utulivu alimkumbuka aliwahi kumuona siku moja Shinyanga, tena ilikua ni nyumbani kwa Kikoko, na alipozidi kuvuta fikra vizueri alipata jibu kua ni Babu yake na mke mdogo wa Kikoko ambae yeye anamuita Ma’mdogo japo kwa sasa ameshaanza kugundua kua ndie aliekua mama yake stahiki kabisa, pia Masu anajua kua mzee huyu hua anishi Kipalapala, Tabora, sasa hapa ni wapi? Na kama ni kipalapala amefikaje? Maswali hayo alikua akijuliza mwenyewe kichwani lakini cha ajabu Mzee huyu alianza kuyajibu utadhani alikua akiyaona yakipita kichwani mwake
“Ni kweli mimi na Babu yake na mama yako mdogo ambae ndio mama yako hasa, na hapa ni Kipala pala Tabora, umeletwa kwa nguvu za mizimu ya WASWEZI iliyokuijia huko Dar ulipokua umegeuzwa Ng’ombe na Hunudu akawa amejiandaa kukuchinja, kile Kimbunga ilikua ni Waswezi na Walua wamekuijia, uje nyumbani kwenu uitambue asili yako na mizimu ya kwenu, pia ufanyiwe Tambiko la zindo kubwa kwa Mshenzi yoyote atakae jaribu kukusumbua tena, Kisha sasa ndo tutaanza kazi ya kuwamaliza hao Waufi”
*****

MUDA wa mazishi ukawadia, tayari nyumba ilikua imezungukwa na waombolezaji, wake kwa waume, lakini mpaka muda huo unatimu Basi lililowabeba Sheikh Jabu na na Mama Masu lilikua halijawasili Shinyanga mjini hivyo suala la kwenda kuzika likawa halina budi kutendeka bila ya kuwasubiri walioko njiani, Baada ya kukamilika kwa Ibada maalum ya dua kwa marehemu na swala ya MAITI sasa wanaume walikua wamelinyanyua Jeneza tayari kwenda makabuburini kuitimiza faradhi ya kuuhifadhi mwili, wakati kundi la wanaume likizidi kutokomea makaburini Tax ikasimama mbele ya nyumba ya marehemu kisha akashuka Sheikh Jabu huku akifuatiwa na kilio cha hamaki kutoka kwa Mama Masu ikabidi Ndugu waliobaki wasimame kusaidiana kuwapokea na kumtoa ndani ya Tax Mama Masu ambae hakua na nguvu kabisa, Kwa kuzingatia taratibu za misiba ya kiislam ni kwamba wanawake hawaruhusiwi kwenda makaburini kuzika hivyo hapo ndio ikawa mwisho wa mama Masu lakini Sheikh jabu akaongea na dereva wa Tax
ile iliyowapeleka hapo nyumbani ili imuwahishe huko malaloni, cha ajabu Mama Masu alikua kama aliechanganyikiwa baada ya kukuta tayari maiti haipo tena, akawa analia sana huku nae aking’ang’ania nae aende makaburini, jambo hilo liliwashangaza wengi na kuacha maswali yasiyo na majibu juu ya taharuki hiyo ya bi mkubwa huyu,. Kina mama watu wazima ambao walikua wamesogea kuwapokea wakamzuia na kumuingiza ndani huku wakimuacha Sheikh Jabu akiingia ndani ya Tax tayari kwenda makaburini, kwakua Sheikh Jabu hakua mwenyeji sana wa Shinyanga hivyo ikabidi aondoke na kijana mmoja pale nyumbani ambae hakwenda makaburini ili awe kama muongazaji wake.

Haikuchukua muda mrefu kwa mbali Sheikh Jabu aliuona msafara wa watu wakiwa wamebeba jeneza, walipowakaribia akamuamuru dereva asimamishe gari, akamlipa pesa zake kisha yeye na kijana aliekwenda nae wakateremka na kuungana na wenzao kwenda mazikoni. Haikua kitambo kikubwa tokea pale walipowakuta mpaka yalipo makaburi hivyo waliwasili katika viwanja vya makaburi, na baada ya dua kadhaa za mwisho zoezi likaanza la kumuhifadhi mzee Kasimba, na hapo ndo ukawa mwisho wake wa safari hii ya Dunia
*****

Nje ya nyumba waliyomtoa marehemu kulikua kimya kabisa kwakua wanaume walikua bado hawajarudi kutokea makaburini, na wanawake wengi walikua wamekaa uani, Sebuleni walikua wameketi watu wawili waliokua katikati ya mazungumzo mazito, alikua ni dada wa marehemu ambae ni Mama Masu alieketi katika kochi dogo la kukaa mtu mmoja, huku upande wake wa kushoto alikua ameketi Koplo Bangi huku shingo yake akiwa ameilaza kiupande hivi ili apate kumuangalia vizuri bi Mkubwa aliekua akimsaili, wakiwa katikati ya Mazungumzo ndipo wanaume nao walikua wakirejea kutokea huko malaloni, ikabidi Inspekta asitishe kidogo mazungumzo kutokana na watu kuzidi kuwasili mahala pale,
“Huyo Sheikh Jabu ndo yuko wapi hapo?” alisaili Koplo Bangi huku akimuelekea Mama Masu ambae muda huo alikua akijaribu kuinua kichwa chake huku akiangalie kwa nje ya nyumba ile kama atamuona anaetafutwa,
“Huyo hapo alievaa kofia ya kufumwa kwa mkono”
“Naona wenye kofia hizo kama watatu hapo.. ni yupi sasa hapo?”
“Huyo mwenye ndevu kama nyekundu hivi,, hua anazipaka hina” Baada ya maelekezo hayo sasa Inspekta aliweza kumtambua vilivyo mtu mzima Yule na hapo hapo akamuagizia kijana amuite ndani, na baada ya kuwasili sebuleni pale alijumuika nao katika amzungumzo yale
“Karibu sana Mzee..” alianza Koplo Bangi kumkaribisha sheikh jabu
“Ahsante sana”
“Poleni na msiba”
“Aah kazi ya mola haina makosa”
“Vipi mbona mlichelewa sana kuingia Shinyanga?” Koplo alitupia swali la kwanza la mtego
“Nadhani tungewahi kufika kama kama isingekua hitilafu za lile basi njiani..”
“Oooh poleni kumbe basi liliwapa tabu, na vipi Mzee Kikoko mmemuacha wapi?” Sasa swali hili lilimshtua kidogo Sheikh Jabu, hakutegea kuulizwa vile maana bila shaka kama huyu anae muuliza ni mwanafamilia pale au ni jirani wa karibu atakua anajua tu kua Kikoko anaumwa nab ado yuko Dodoma
“Kwanza samahani, umeanza tu kunisaili bila ya kujitambulisha..”
“Ooh bila ya samahani mzee, mimi naitwa Koplo Sebastian Bangilana, unaweza kuniita Koplo Bangi,”
“Sasa kwani Bi Mkubwa hapo hajakueleza juu ya alipo mumewe mpaka ukanihoji mimi?”
“Sio vibaya nikisikia pia kutoka kwako”
“Mwenye Jukumu la kujibu wapi alipo Bwana Kikoko ni mkewe na si mimi”
“Iko hivi Mzee, mimi hapa niko kazini na nimechagua kuhojiana nanyi mahala hapa kwa wema wangu tu kutokana na hali yenyewe ya msiba ila kwa sasa mlipaswa nyote muwe chni ya ulinzi huku mkinijibia maswali yangu katika viti vya mbao ofisini kwangu, hivyo naomba Ihsani yangu isiwe Nuksani, nitabadili mfumo wa mahojiano sasa hivi, umenieelewa?” Koplo Bangi alibadilika mara moja na kua kama pilipili, Macho ya Sheikh Jabu yakagongana nay a Mama Masu, kisha akarudi kumtazama tena Inspekta halafu akakohoa kidogo ndipo akaendelea
“Kuna kitu sijakuelewa, yaani sisi tulipaswa kua chini ya ulinzi? Kwa kosa gani hasa?”
“Kwa kumficha Mzee Kikoko ambae ni mtuhumiwa namba moja wa mauaji haya yote yanayoendelea”

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA NANE

MWANAUME Mrefu aliejazia mwili wake kimazoezi alikua akirandaranda kwa kwenda mbele hatua kadhaa na kurudi nyuma huku kichwa chake akiwa amekiinamisha chini, mikono yake miwili akiwa ameipa hifadhi katika mifuko ya suruali yake ya kijivu, akiwa anendelea na zoezi hilo la hiari ndipo ghafla alisitisha zoezi lake hilo baada ya kumuona Dokta Nyango ambae ni mganga mkuu katika Hospitali hiyo ya Kitete ambapo mwanaume huyo alikua akirandaranda katika korido zake,
“Habari yako..” Dk alimsabahi mwanaume huyo
“Salama tu Dk, pole na majukumu”
“Aah ahsante, najua u-mgeni wangu karibu ofisini”
“Ahsante sana Dk” Baada ya salamu waliongozana mpaka katika Ofisi ya dokta huyo ambayo haikua mbali na hapo alipokua akitalii mwanaume huyo, kisha wakaingia ndani
“Karibu uketi hapo..“
“Ahsante.. Naitwa Sajent James Marumbo kutoka kituo cha polisi kati, tumepokea taarifa za wito wako hivyo ikanibidi nije haraka haraka” Sajenti Marumbo alianza kwa kujitambulisha baada ya kuketi huku akihangaika kuingiza mkono katika mfuko wa suruali yake ambako alitoa kitambulisho chake cha kazi kwa lengo la kumuonesha Dk
“Oooh No, hakuna haja ya kitambulisho, ninakufahamu vizuri tu” Dk Nyango alivua miwani yake ya macho akaiweka juu ya meza yake kisha akaanza kujipikicha macho kabla hajainua tena uso wake na kumtulizia macho yake Sajent Marumbo kwa sekunde kadhaa kabla ya kumtupia swali la uchokonozi
“Mlileta maiti hapa, Sio?”
“Yeah”
“Mliitoa wapi maiti hiyo?”
“Aahh tulikua na operesheni yetu maalum maeneo ya kipalala, kuna mtuhumiwa wa mauaji tulienda kumkamata, sasa tukiwa eneo la tukio ndipo tukamkuta huyo dada akiwa amelala katika Dimbwi la damu lililotokana na kupigwa na upanga kichwani, na bahati nzuri tukamkuta Mwanaume mmoja akiwa na Panga hilo mkononi na tulipomuhoji..” Kabla hajamalizia hadithi yake akatizwa na sauti ya utulivu kutoka kwa Tabibu huyu
“Sina haja ya kufika huko kote. Nilitaka tu kufahamu mlijuaje kua amekufa wakati hamkua na mtaalamu yeyote huko”
“Dk kuna vitu vingine vinaonekana hata kwa macho tu, Dada alikua amepoteza maisha” Wakati mtaalamu huyu wa upelelezi akibwabwaja maneno yake huku akitupa mikono yale huku na kule kama ishara ya kuonesha msisitizo kwa hicho anachokiongea lakini hiyo ilizidi kumfanya sasa huyu Mtaalmu wa Afya atikise kichwa chake kabla hajaaendelea kuzungumza
‘”Ok, Ok, nimekuelewa.. Sasa iko hivi naomba nikushauri kijana wangu jambo moja la msingi sana..” akaweka nukta ndogo ili aruhusu mwayo uliokua jirani na koromeo lake kisha akaendelea “..Ninyi ni wataalamu wa masuala ya upelelezi, walinzi wa raia na mali zake, sasa haipenzi kabisa kwa namna yoyote ile kuingilia taaluma zisizokua zenu..” Akaweka tena nukta ndogo huku akiupikicha uso wake katikati ya viganja vyake vipana vya mikono, Sajenti Marumbo akataka kuongea lakini hapohapo akakatishwa na Sauti ya Dokta iliyoendelea tena kutoa maelezo amabyo afande huyu alihisi kutokuyaelewa “..Mmemleta Yule dada hapa huku mkishinikiza kua awekwe mochwari, bila ya kujali taratibu za kitabibu zilizopo hapa, na hata pale mlipopewa taratibu zeti mlizidi kuelekeza kwa kukaripia wataalamu, Sasa iko hivi huyo dada wala hakupoteza maisha kama unavyosema bali alipoteza kitu kingine kabisa, Fahamu tu”
“Ama!” Sajent Marumbo ambae alikua na uhakika kabisa kua dada Yule alikua amefariki alishituka wazi wazi huku akipepesa macho yake kwa kauli ile ya Dokta
“Ndo hivyo, na mpaka sasa tunaendelea na jitihada zetu za kupambana na hali hiyo mbaya ya mgonjwa maana mpaka sasa hajarejewa na fahamu, sasa Je vipi kama tungemuweka kwenye barafu si ndo tungekua tumemmalizia kabisa?? Na Je vipi kama tutawashitaki kwa kutaka kummalizia mgonjwa aliekua mahututi kwa kuwashinikiza wataalamu wetu wamuhifadhi mochwari?” Sajent alizidi kupagaishwa na majibu haya maana kwa jinsi alivyomuona Yule dada pale kituoni wakati anafikishwa alikua ameshakufa, sasa ghafla vipimo vinadai kua Yule dada ni Mgonjwa tu, hakua na jinsi tena ya kuyakataa majibu ya Dokta, bali ni kuyapokea na kuomba radhi kwa niaba ya wenzake
“Ok dokta nimekuelewa, naomba tu radhi kwa kilichotokea kwakua ni kutokujua kwetu lakini hapakua na nia mbaya yoyote, sasa Je tunaweza kwenda kumuona japo kidogo?”
“Ooh yes, why not?(Kwanini ishindikane, tunaweza tu) ila tu muwe makini muda mwingine” waliinuka na kuongozana mpaka wodini ambako Nyamizi alikua amelazwa, hali yake haikua mbaya sana ukllinganisha na jinsi alivyokua hapo awali, japo hata kufikia muda huo alikua bado hajarejewa na fahamu zake..

Baada ya Sajent kujiridhisha na hali hiyo ya mgonjwa akabidi kumuaga Dk na kisha akarejea mpaka kituoni ambako alifanya mazungumzo na mkuu wa kituo kwa kina juu ya tukio hilo na taratibu za kawaida zikaendelea kama kawaida huku wakisubiria hali ya mgonjwa itakavyokua, Lakini kutokana na kesi hiyo kua na mlolongo mrefu ambao umepelekea mpaka hata Masu kutokuwepo pale ikabidi sasa wampigie simu mpelezi wa kesi ya kule Shinyanga Koplo Bangirana ili nae wampe taarifa za mabadiliko ya habari za mwanzo kua dada aliekutwa amekatwa na Panga kichwani amefariki, na kwakua Sajenti Marumbo alipata kuwasiliana na Koplo Bangi mwanzoni mwa kesi hiyo hivyo alikua na kumbukumbu ya namba za Koplo Bangi hivyo ilikua ni kazi rahisi tu kumpata kwa namba yake binafsi
*****

TAARIFA za hali ya Nyamizi huko kitete zilizidi kumpa hamasa na matumaini Koplo Seba ya kujaribu kuifuatilia vizuri kesi hiyo, ikabidi sasa azidishe ukaribu na Sajent Marumbo kwa ajili ya kua anapata habari zote muhimu kutoka huko, akili yake alikua imeshagoma kuamini kua kina Masu ni wauaji kweli kutoka na utata unaoendelea kuigubika kesi hiyo, Lakini hakumuambia chochote mkuu wake wa kazi akihofia kuzidi kujichanganya kutokana na vitisho anavozidi kupewa, na kwakua jioni ilikua imeshaanza kutanda akaamua kuiacha kipolo kesi hiyo mpaka kesho yake ndipo ajue la kufanya
*****

USIKU WA MANANE,

Usiku wenye kiza kinene,
Chini ya Mbuyu mkubwa ulipo katika moja ya Shamba kubwa laukoo wa marehemu kasimba walikua wamekusanyika watu zaidi ya Hamsini hivi, wote wakiwa wamevaa nguo nyeupe vichwani wamejifunga vitambaa vyeusi kiasi kwamba kama ungetokea ghafla ungeweza kuwajua tu maana nguo nyeupe katika giza huonekana kiurahisi sana, wote walikua wamekaa chini huku wakionekana kua katika kina cha mazungumzo mazito, Kila aliekua akipata fursa ya kuongea alisimama juu na kuongea kwa hisia kali, Ulikua ni mkutano wa dharurawa wafuasi wa Mzimu wa Waufi..
Aliekua akiongea wakati huo alikua ni Bazazi asiekua na huruma, kijana mwenye jicho moja, Hunudu!
“Jamani binafsi nataka kusema jambo moja tu, naomba mniskilize vizuri..” akaweka kituo kidogo, akakohoa kisha akendelea “..Hii vita imeshakua kubwa sana japo mnaweza kudhani kama vile imekwisha Laa hasha iVita ndo kwanza inaanza, Japokua tumewatengenezea kesi ya mauaji lakini bado tunakibarua kigumu kulitimiza hilo, ukweli ni kwamba Yule Dada hakufa bali alipoteza tu fahamu na nilishindwa kummalizia kwa kua hali ilikwishavurugika pale..”
“NINI??” Hunudu alikatizwa na sauti ya mshangao iliyotokea usawa wa chini kwa hawa waliokaa ikionesha kushangazwa na taarifa ile ya Hunudu, huyu aliyeshangaa alikua ni Afande Ngulinzila, mfuasi mwingine wa Waufi Lakini alikatishwa kuongea na sauti kavu ya mzee mmoja alieonekana kua kama kiongozi wao pale
“Kaa kimya binti,hujui taratibu zetu wewe? huu muda anongea mtu mwingine..” Baada ya Mzee Yule kumkaripia Afande Ngulinzila sasa Hunudu hakusubiri kuambiwe aendelee
“Zimebaki siku saba tu za kuhakikisha Masu anajiunga na waufi au tunamuondoa duniani, vinginevyo zikipita siku saba kama hatujaitekeleza amri hiyo basi mkumbuke kua Mzimu unataka tumtoe kafara mama Masu mwenyewe kwakua ndie alieingia makubaliano na Mzimu tangu hajamzaa huyo Masu kua atatoa kafara ya Damu ya mjukuu wake atakaekujakumpata kwa Masu, japoyeyealidhani itakua mbali sana ila kwa mizimu hilo ni jambo la muda mfupi..” Hunudu akaweka kituo, akajikohoza kidogo halafu akaendelea
“..Kesho inabidi sasa dada Joyce Ngulinzila kwakua Masu yuko mikononi mwako huko kituoni utafute nafasi ya faragha ili ukae nae umpe vitisho ili akubali kujiunga nasi na akubali kutoa kafara ya mwanae mmoja ili tumnusuru huyu Bi mkubwa, na hiyo itakua ni mara ya mwisho, wakati huo mimi nitasafiri kwa upepo mpaka tabora ili nikammalizie Yule dada ili tuzidi kuwaweka katika mazingira magumu ya kesi ya mauaji, watakapokua wakihangaika kupambana na kesi yao ndipo sisi tutakapozidi kuchanja mbuga kuwamaliza wote” Baada ya Hunudu kutoa ripoti yake akapigiwa makofi kisha akasimama Mzee mmoja hivi baada ya kupewa ruhusa, nae akaanza Kuwasalimia kwa ari zao za kimizimu
“WAUFIIII..”
“Mzimu wa watemi wa bahari” wakaitika wote kisha akaendelea kuongea
“Jamani tatizo kubwa ni huyuhuyu mama Masu, sisi tulimshauri tangu mwanzo kua tummalize tu huyo Masu maana anataka kutuzidi nguvu lakini akakataa sasa leo tunasumbuana hapa kutaka kumuokoa kwa jambo alilojitakia, kwanini hasa? Kwani ni wangapi tulishawatoa kafara kwa kuzembea maelekezo ya Waufi? Mie nadhani tungeacha hii kesi aimalize mwenyewe na kama atashindwa ndani ya siku saba hizo zilizosalia basi awe asusa ya Mzimu” kauli ya Mzee huyu alipekea sauti ya kilio cha uchungu kutoka kwa Bi mkubwa mmoja aliekua ameinamisha sura yak echini muda wote wa majadaliano haya, na aliponyanyua uso wake akadhihirika kua ni Mama Masu, Baada ya Mzee huyo kuwasilisha hoja yake nae akaketi ndipo sasa kilio cha Mama Masu kikakatizwa na faraja kutoka kwa mwanamke mwenzake ambae ni Afande Ngulinzila aliesimama na kuanza kuongea kwa jazba kama ilivyo kawaida yake
“Tumeitana hapa kwa ajili ya kutatua jambo la dharura, na hatupo hapa kwa ajili ya kulaumiana, hata hao mnaosema walitolewa kafara kwa makosa yao ilibidi kufanya hivyo baada ya kuwasaidia kwa muda mrefu sasa kwanini leo kwa Mama Masui we tofauti? Tangu tulipoanza kupambana na nguvu za Mzimu wa KASOMANGILA uliopo chini ya Waswezi tumekumbana na vikwazo vingi sana lakini hatujalalamika cha ajabu leo analalamika mtu ambae wala hajafanya lolote.. Mjinga mjinga tu na tumbo lake” Ghafla Ngulinzila alikatishwa na mkuu wao ambae ni Mwanamama mmoja hivi mweupe aliekua amejifunga kitambaa cheupe kilichokatiza juu ya kifua chake, akasimama na kumuamuru Joyce Ngulinzila aketi chini halafu akawasalimu salamu yao ya hamasa
“WAUFIIII”
“Mzimu wa watemi wa bahari”
“Sasa naongea kama Kiongozi, Mimi ndo mtemi Kalovya, naomba sana msitutie aibu na fedheha mbele ya Mzimu, kumbukeni Mzimu wetu ni mzimu mkubwa sana, ni mzimu wa baharini, mzimu ambao matambiko yake ni ya baharini ndio maana wengi hushindwa kupambana nao, sasa itakua ni kituko eti tushindwe na wapuuzi wachache kutoka bara tu, hivyo sioni haja ya kuendelea kutupiana lawama hapa badala ya kupanga mipango ya kuwamaliza hawa waswezi, Hunudu ameongea vizuri sana kwa kutuonesha dira na mbinu ya kuwamaliza na hicho ndio kitu pekee kinachopelekea kila siku tumpe vyeo Hunudu, sasa hakuna malumbano tena zaidi ya kuutekeleza mpango kazi uliowasilishwa na Hunudu hapa, ila cha kuwasihi ni kua makini katika kila hatua maana tuna upinzani mkubwa, kumbukeni tayari tumeshampoteza kiongozi wetu wa mazindiko marehemu Kasimba aliuawa na Mizimu ya Kigoma huko kwao na marehemu Kishindo, Mizimu hiyo inatumia kivuli cha marehemu Kishindo kupambana na sisi huku wakishirikiana
kwa karibu na Mzimu wa Waufi, na hilo ni kosa tulilolifanya baada ya kumsambaratisha Kishindo kwa Radi ilipaswa tuisambaze na nguvu yake ya asili ya mzimu ambayo ndio hicho kivuli chake. mizimu yote hii imeungana kumsaidia Masu, kumbukeni kua Masu ni wa Kigoma kwa upande wa Baba yake bwana Kikoko, sasa hapa tunapambana na nguvu za aina mbili tofauti, sio padogo hapo..”
*****

SIKU Iliyofuata ilikua ni Siku ya majuku mazito,
Majukumu mazito kwa Afande Bangi wa kituocha Polisi cha Shinyanga kuanza kuifuatilia kesi hii kwa ukaribu zaidi,
Majuku mazito kwa Afande Malumbo wa kituo cha Polisi Tabora kufuatilia kesi hiyo kwa kuanzia na kuifuatilia hali ya mgonjwa alie taabani hospitalini,
Majuku mazito kwa Afande Ngulinzila aliepewa jukumula kumtisha Masu mpaka akubali kumtoa kafara mwanae na ajiunge na Waufi,
Majukumu mazito kwa Hunudu kuhakikisha anasafiri kwa nguvu ya upepo na anafanikiwa kummaliza mgonjwa alie Mahututi huko katika Hospitali ya rufaa ya Kitete mkoani tabora..

Wakati kila mmoja akiwa akiwa ameshaamka katika siku hiyo mpya akiwa tayari kutekeleza majukumu yake huku kituoni nako nyuma ya Nondo za Selo ndogo hapo kituoni walikua wameketi chini Sheikh Jabu na Masu wakiwa katikati ya Mazungumzo marefu sana, Masu alikua akimsimulia swahiba huyo wa baba yake kuhusu hali ile iliyojitokeza jana yake mule ofisini alipoingia yule askari wakike. Alielezea kwa ufasaha mkubwa jinsi alivyomkumbuka dada huyo siku ile alipomtokea akiwa na Masu, ilikua ni muda mfupi tu baada ya kuongea na marehemu Kishindo, suala hilo lilimtisha sana Sheikh Jabu kwani aliamini kua kumbe hawakua wakipambana na washabiki wa Waufi bali ni wafuasi hatari wa Mzimu huo, lakini kwa mtu mwenye hekma kama yeye hakupaswa kuonesha hofu yake mbele ya Masu, na badala yake alijifanya kua hajatishwa kabisa na matukio yanayoendelea
“Nimekuelewa sana mwanangu, ila nataka kukuambia jambo moja na ulishike sana, kaa ukijua hii ni vita ya Mizimu, vita ya nguvu za giza, wote wanapambana kwa ajili yako,kila mmoja anakuhitaji kwa maslahi ya mzimu wake, japo tunajua kuahawa Waufi ndo washenzi kabisa lakini uje kila muwamba ngoma huvutia kwake hivyo hata hao Waswezi wa huko Tabora nao hata kama wana mapungufu yao lakini watavutia kwao tu hivyo uwe makini sana..” Sheikh Jabu akavuta pumzi kidogo kisha akaendelea kutoa somo kwa mwanae “..katika vita hii utakaeumia ni wewe kwa kua huoni mbele, huna taaluma ya nguvu wanazozitumia wao, hakuna sehemu mbaya kama pale ulipogeuzwa Ng’ombe maana kama hao watu wa kwenu kipalapala wangechelewa kidogo tu saa hizi tungeshakula nyama yako zamani sana, pia ukae ukijua kwamba japo Mama yako aliiba mimba lakini nae alikuzaa kwa uchungu, pia alieibiwa mimba nae alipata tabu kubwa ya kuilea mimba yako kwa miezi ya awali hivyo hao wote ni mama zako..”
Kabla Jabu hajaendelea Masu akamdakia
“Mama zangu?? Yaani niwe na mama wawili?” Kabla Sheikh Jabu hajaendelea kuongea wakasikia sauti ya OC CID Ngulinzila akiingia kituoni kwa mikwara kama ilivyo kawaida yake, na baada ya kusalimiana na askari wake alisikika akitoa amri
“Hebu nileteeni huyo Masumbuko Kikoko Ofisini kwangu, Haraka” Masu na Sheikh Jabu walitazamana baada ya kusikia kua sasa Masu anaitwa ndani na kabla hawajapeana cha kuongea tayari mlango palikua na sura kavu ya askari mmoja akliemwita Masu huku akifungua makufuli, ikawa Hakuna ujanja tena, ni kwenda tu kumsikiliza mfuasi huyu mahiri wa Waufi anaefanya kazi za serikali huku akichanganya na Waufi,

Baada ya Mlango kufunguliwa Masu akawa ameshasogea mlangoni kwa ajili ya kutoka na kuelekea ofisini kwa Afande Ngulinzila ndipo ghafla ukasikika ukelele wa nguvu kutoka ofisini kwa OC CID, kelele za hamaniko na maumivu makali kutoka kwa apigae kelele hiyo, ilikua ni sauti ya Afande Ngulinzila, Askari wote walioisikia sauti ile walihamanika vilivyo, wote wakatoka mbio huku wakipamiana kuelekea ofisini kwa mkuu wao huyo, kwa kua hawakua mbali na ofisi hiyo hivyo haikuwachukua muda mrefu kuwasili ndani ya ofisi hiyo na kumkuta akiwa amelala chali juu ya Dimbwi la damu, ikawa ni kelele za hofu kutoka kwa baadhi ya askari wa kike walioshindwa kujizuia, Askari wakazidi kujaa ndani ya Ofisi hiyo kushuhudia tukio hilo la ajabu ambalo liligonga kichwa cha kila mmoja wao, ikabidi haraka baadhi ya askari watoke nje ya Ofisini hiyo ili kuangalia kama kuna dalili ya mtu aliefanya unyama huo!!
*****

Nje ya Ofisi ya muuguzi wa zamu katika Hospitali yaKitete mkoani Tabora alikua amesimama kijana mmoja akisubiri ruhusa ya kuingia ndani kuonana na muuguzi huyo, alisimama kwa muda karibu wa dakika mbili baada ya kugonga mlango ndipo akaruhusiwa kuingia, alipoingia ndani ya ofisi hiyo ndogo yenye kabati moja kubwa lililowekwa shuka nyeupe katika baadhi ya droo zilizozungukwa na vioo, pia kulikua baadhi ya mafaili yaliyojipanga ubavuni mwa meza hiyo, pia kulikua na meza ndogo ambayo juu yake kulikua na Trei ndogo iliyokua na Glove pamoja na mabomba ya sindano, katika kiti kilichokua kimetazamana na mlango wa kuingilia alikua ameketi muuguzi mmoja aliejitambulisha kupitia mavazi yake ya kitabibu, macho mawili ya muuguzi huyu yaligongana na jicho moja la kijana huyu alieingia ndani humu, Hunudu!
“Karibu..”
“Ahsante sana, habari za hapa?”
“Nzuri tu, naweza kukusaidia..”
“Oooh yeah, naitwa Hunudu nimekuja kumuangalia ndugu yangu”
“Kaka huu si muda wa kuona wagonjwa, uje kwenye saa nane mchana”
“Samahani Dokta, mimi nimetokea safari baada ya kupata habari za hali mbaya ya mgonjwa wangu, hivyo naomba tu unisaidie hata kwa dakika kumi nimuone tu”
“Kaka huo sio utaratibu wa kazi, naomba uzingatie hilo,” Hunudu alibaki akimkodolea muuguzi huyo kwa jicho lake moja ndipo alipogundua kua dada huyu alikua akimaanisha akisemacho, akaona isiwe tabu, akaingiza mkono mfukoni kisha akatoa noti mbili nyekundu akamuwekea muuguzi yule juu meza, nae bila ajizi akazichukua na kuzisunda mfukoni kabla ya kumtupia macho yake bazazi huyu kutoka waufi
“Mgonjwa wako anaitwa nani?”
“Nyamizi Fundikira..”
“Ohh yule aliepigwa panga kichwani?”
“Ndio huyu huyo”
“Ok nitakupeleka ila usikae muda mrefu maana wakitokea wakuu utaniletea kizaazaa, sawa?”
“Haina shida dada, ni kama dakika kumi tu” Baada ya maridhiano hayo wakatoka ofisini huku wakielekea wodini kwa mtindo wa watoto wa bata
*****

Huku Shinyanga hali ilizidi kua tete kufuatia tukio hilo la kustaajabisha, Askari walikua wamechanganyikiwa kisawasawa, kila mmoja alikua akisema lake huku mwili wa Afande ukiwa badoumelala pale chini, muda huu sasa Afande Ngulinzila alikua kimya!!
“Hakuna haja ya kuendelea kuduwaa hapa, tungemuwahisha kwanza hospitali” aliongea askari mmoja wa kike aliekua amesimama ndani kidogo kwa mlangoni
“Hospitali kufanyaje? Afande hatunae tena, ameshakufa huyu, ametobolewa kifuani na inaonekana kama aliemtoboa alikua akinyofoa kitu ndani yake kama Moyo vile maana kuna nyamanyama nyekundu katika tundu” Kauli hiyo ilizidi kuzua taharuki ofisini pale na hapo ndipo sasa akili ya Koplo Bangi ilipogonga kengere baada ya kusikia kua huenda Afande Ngulinzila amenyofolewa moyo, akakumbuka tukiolilivyokua kwa marehemu Kasimba, wakati huo Koplo Bangi alikua amesimama katika mlango wa kuingilia ndani ya Ofisi hiyo, ikabidi sasa asogee ili aone hicho alichokisika cha kunyofolewa Moyo, aliposogea akashuhudia zaidi ya kilichompeleka, akashuhudia alama za kucha zilizokwaruza sehemu ya shingo ya afande huyu,

‘Taswira ya tukio la mauaji ya namna hiyo yaliyomkuta hayati Mzee Kasimba sasa yamemdhihirikia Afande Ngulinzila ambae amekua akionesha dalili ya kumtetea mama Masu ambae ni dada wa marehemu Kasimba’ Mawazo yalifanya utalii wa ndani katika kichwa cha Koplo Bangi
*****
Wakati Hunudu akiwa tayari ameshaingia ndani ya wodi kwa ajili ya kutekeleza azma yake ya kummaliza yule mgonjwa aliemkata na panga kichwani ndipo alipopokea ishara ya hatari ikimuarifu juu ya hali ya tukio la kuuawa mfuasi mwenzie wa Waufi ambae ni afande Ngulinzila, taarifa hiyo ya kiishara ilimfikia kwa nguvu zao za giza, Sasa tayari Hunudu alishahamaki kwa kiwango cha juu sana, akawa njia panda asijue cha kufanya, alitamani ammalize yule dada haraka lakini pia alihisi labda ajaribu kumuwahi Afande Ngulinzila labda angeweza kumnusuru, Ilimchukua kama dakika tano ndani ya wodi ile akiendelea kupambana na mawazo yake mwenyewe kabla hajapitisha maamuzi ya kuondoka ili akamuwahi afande Ngulinzila huku akitia nia ya kurudi tena pale wodini

Haraka kwa mwendo wa upepo Hunudu alitoka hospitalini hapo bila ya kuaga huku akijaribu kuwahi Shinyanga kama atafanikiwa kuokoa uhai wa mfuasi mwenzie wa Waufi, alijaribu kupingana na taarifa zinazoendelea kupita kichwani mwake kua Ngulinzila ameshatokwa na uhai..
*****

Katika kituo cha polisi mkoani Shinyanga tayari maiti ya afande Ngulinzila ilikua imeshatolewa na kupelekwa hospitalini kwa ajili ya uchunguzi wa kifo hicho cha kutatanisha, hali ya simanzi, hofu na mashaka vilizidi kutamalaki katika mioyo na askari kadhaa waliokua pale kituoni, Gumzo la vuguvugu kufuatia tukio hilo la aina yake vilizidi kutiririka kutoka katika vinywa vya askari waliopo kituoni wakiungana na askari wengine waliozidi kuwasili kituoni hapo baada ya kutapakaa kwa taarifa za kifo cha afande Ngulinzila, Wahenga wanasema ‘Apatikane na mkasa hupatwa na vingi visa’ msemo huo ulidhihiri sasa maana kila mmoja alikua akisema yake anayoyajua, mazuri na mabaya ya Marehemu Ngulinzila huku wakiyanasibisha na tukio lenyewe lililotokea, hakuna aliekubali kutoa mtazamo wake ukizingatia askari hawa ni weledi wa upelelezi..

Wakati hayo yakiendelea kufukuta hapo kituoni, katika ofisi ndogo ya upelelezi alikuwa ameketi peke yake Koplo Bangi akiwa ‘busy’ akipekua makaratasi katika mafaili kadhaa yaliyozagaa juu ya meza yake, wakati huo akiandika baadhi ya vitu katika faili lake maalum, Kazi kubwa iliyokua ikimmakinisha Koplo Bangi ni agizo maalum alilopewa na Mkuu wa kituo OCD Amosi Nkeli la kuandika maelezo ya kina juu ya kadhia iliyotokea kuanzia mwanzo wa kesi mpaka mwisho, Taarifa za utata wa kesi ya kina Masu ilizidi kumpa wakati mgumu Ocd Nkeli na tayari alikua ameshapata fununu na ‘udambudambu’ kuhusiana na Waufi, hivyo basi kwa kua Koplo Bangi alionekana kua na taarifa za kina hivyo akaachiwa aandae taarifa ya kiuchunguzi na kiuchokonozi ili aikabidhi kwa wakubwa wake wa kazi kwa ajili ya hatua endelevu..

Baada ya takribani saa tatu na ushee tayari Koplo Bangi alikua ameshapanga mafaili yake vizuri ndipo akainuka kutoka kitini alipokua ameketi kisha moja kwa moja akatoka mpaka nje ya ofisi hiyo huku akielekea kaunta kwa ajili ya kuwachukua watuhumiwa wake kwa ajili ya mahojiano maalum, safari hii akiwa huru zaidi kuhoji atakalo kwa watuhumiwa hawa, sio tu kwa kua aliekua akimzuia amefariki bali kufuatia agiza maalum kutoka kwa mkuu wa kituo. Alipofika kaunta akaanza kutaniana na askari waliokua zamu pale
“Haya sasa majukumu ya Afande Ngulinzila umeachiwa mzee wa kazi, bila shaka hata kifo kitakachofuatia ni cha kwako..” alidhihaki mmoja wa askari aliekuwa pale kaunta
“Acha kuniombea dua baya hilo kaka, hii ishu sio ya kitoto bana”
“Lakini afande Bangi hebu tupe ufyetere kidogo, kuna nini hasa hapa katikati”
“Na wewe kwa udadisi mambo unajiweza!!..” Wote wakacheka kwa pamoja kisha Afande Bangi akamalizia kuongea
“…Hebu nawaomba kwanza hao watuhumiwa halafu baadae tutaongea tu”
“Lakini afande Ngulinzila si alikukemea wewe kujihusisha na kesi hii?”
“Hah ha ha yake yamekwisha, hi indo dunia bhanaa” wakacheka tena kwa pamoja kisha afande alieklua zamu akawafungulia Akina Masu, Jabu, na mke wa mdogo wa Mzee Kikoko

Walipotoka tu Koplo Bangi aliwachukua bila kupoteza muda na kuondoka nao wakielekea ofisini kwake huku nyuma waliacha gumzo likizidi kutia nanga, japo muda wote wa tukio la kifo cha ngulinzila watuhumiwa hawa walikua ndani tu lakini tayari walikwishajua kinachoendelea baada ya zogo la taharuki kua kubwa kufuatia kifo cha Ngulinzila, hivyo wote walikua kimya, wakielekea ofisini kwa Afande Bangi huku kila mmoja akiwaza yake, walipofika ofisini waliketi katika viti vitatu vilivyopangwa maalum kwa ajili yao huku kiti kingine cha nne kikiwa kitupu kikiangaliana na vile vya kwao huku wakifarakinishwa na meza iliyo katikati, na muda wa sekunde kadhaa baada ya wao kuketi ndipo Koplo Bangi nae akaketi katika kiti kile huku akiwatembezea macho yake kila mmoja wao kisha akaanza
“Najua nyote mnajua kadhia inayoendelea kuighubika kesi yenu, na hicho ndicho kitu pekee kinachowafanya muendelee kukaa ndani muda wote huu..” Koplo Bangi akajikohoza kidogo kabla ya kuendelea
“Sasa nataka tuyamalize humu ndani mimi na nanyi ila endapo tu mtanieleza kila kinachoendelea kwa ukweli na uhakika” Baada ya afande Bangi kuweka nukta ndogo akaangaliana na watuhumiwa wale halafu akaanza na Masu
“Masu kwakua wewe ni muhusika mkuu wa kesi hii, hebu nipe kila kitu ukijuacho kuanzia mgogoro wa baba yako na marehemu Mzee Kishindo na mpaka kifo cha kishindo kule porini ukiwa nae wewe na ikawaje mpaka ukatokomea porini huko kabla ya kukamatwa kule kipalapala Tabora… Nasisitiza ukweli utawale mahala hapa” Baada ya Koplo Bangi kumaliza kusema yake ndipo sasa ikawa zamu ya Masu ambae alianza kuielezea kadhia ile mwanzo mpaka mwisho huku Sheikh Jabu na mke wa Mzee Kikoko wakisikiliza kwa makini, wakati huo Koplo Bangi alikua akiandika baadhi ya vitu muhimu kutoka katika maelezo ya Masu kilichozidi kumshtua na kumpa udadisi zaidi koplo Bangi ni pale Masu alipoelezea alivyokua akimjua marehemu Ngulinzila na kumuhisisha na Waufi siku ile alipotokewa na Hunudu kwa mara ya kwanza..

Kama ilivyo taaluma hii ya upelelezi kila unapotoa maelezo basi maswali huzalika zaidi, ndivyo ilivyokua kwa Koplo Bangi
“Sasa Je unajuaje kama afande Ngulinzila alikua ni mfuasi wa Waufi? Je kama huyo Hunudu alipewa lifti tu kama ulivyopewa wewe?” lilikua ni swali la kipuuzi tu kuoka kwa afande huyu lakini lenye utafiti mkubwa ndani yake
“Bila shaka walikua wakijuana kwa kua maongezi yetu yote yalikua yakua yakifanyikia ndani ya gari hiyo hiyo na wala dada huyo hakushtuka, pia zaidi ya hayo alikua akisapoti kinachosemwa na Hunudu huku akitabasamu mara zote, na ndo maana hata aliponiona hapa tulitazamana kwa dakika kadhaa kabla hajaendelea kukaripia” Baada ya majibu ya Masu sasa Koplo akamgeukia Mke wa Mzee Kikoko
“Mama haya umesikia habari yote kutoka kwa Masu inawezekana kua ni mwanao kweli? Na je unaijua na kuikumbuka hii habari?”
“Ni kweli naijua hili tukio, lilinitokea mimi mwenyewe, na kila alichokisema Masu kuhusu upande wangu ni kweli kabisa”
“Mimi nataka unielezee wewe kwa maelezo yako” Mke wa Kikoko sasa alianza kuelezea hatua kwa hatua tangu kuibiwa ujauzito wake kishirikina, hatua zote za usuluhishi zilizopitiwa, mpaka kufikia hapo walipofikia, lakini alikataa kujua chochote kuhusiana na kifo cha marehemu Kishindo,
“Sasa ilikuaje ukawa unataka kutoroka ukiwa tayari na begi lako mkononi kama hauhusiki?”
“Mimi sikuwa nikikimbia, bali nilikua naelekea stendi kwa ajili ya kuangalia usafiri wa kwenda Dodoma kumuangalia mume wangu baada ya kuambiwa kua anaumwa na amelazwa huko” baada ya maelezo yake nae alikumbana na maswali ya papo kwa papo ambayo aliyajibu kwa kadri ya uwezo wake.. Baada ya kumaliza sasa koplo Bangi akamgeukia Sheikh Jabu ili amalizie Ngwe yake
“Sheikh wewe ni swahiba wa karibu sana wa Mzee Kikoko na marehemu Mzee Kishindo, najua una mengi unayajua, hebu nahitaji hekma zako ambazo mwanzo ulizificha mpaka ukjikuta upo hapa leo hii” Swali lile lilikua kama la dhihaka kidogo kwa Sheikh Jabu lakini halikumfanya ashindwe kutumia hekma na fasaha yake katika uzungumzaji, alieleza mambo mengi sana japo yakiwa hayana tofauti sana na wenzie waliomaliza kuhojiwa punde, sema tu Jabu aliyaongea kwa balagha ya hali ya juu kiasi cha kuyafanya yazidi kueleweka na kumuingia vema afande Bangi
“Sasa Mzee wangu hauoni kua huu ni utata? Yaani Ndoto tu ndo imezua yote haya? Tazama sasa Kishindo ameshakufa na kuzikwa lakini vipimo vinaonesha Marehemu Mzee Kasimba amekutwa na alama za mikono ya marehemu Kishindo, we haudhani kua huyu Masu anajua mahala alipo Kishindo?”
“Hata mimi najua mahala alipo Kishindo” jabu alimkatisha Afande Bangi
“Mnh.. yuko wapi?”
“Kishindo yuko Kaburini sasa hivi, tumeshamzika! Kifo cha kishindo na kuendelea kuhusishwa na tukio la mauaji ya hayati Kasimba ndio litakua jibu la swali lako la kwanza”
“Swali lipi?”
“Umesahau ulichoniuliza? Umenuiliza hivi ‘Mzee hauoni kua huu ni utata?’, Naam huu ni Utata”

Wakati Koplo Bangi akizidiwa na hasira ndani ya moyo wake zilizosambamba na udadisi uliomjaa kufuatia maelezo ya laini kutoka kwa Sheikh jabu ndipo ghafla mlango wake ukasukumwa kwa nguvu na hapo hapo akaingia Ocd Nkeli, mkuu wa kituo cha Polisi, akionekana ni mwenye taharuki kubwa. Kitendo bila kuchelewa Koplo Bangi akasimama na kutoa saluti kwa Bosi wake huyo kisha akampa kiti aketi huku akimuhoji
“Mzee kuna usalama kweli?”
“Hakuna usalama Koplo..” wote mule ndani wakawa wanamuangalia Mkuu huyo akiongea kwa hali ya hofu na wazo mengi kichwani, hakuna alieingiza neon mpaka alipoendelea mwenyewe kutiririka
“Nimetokea hapo Hospitali ya mkoa kuonana na Dr Shamsi, amenipa majibu ya vipimo vya Mareh.. ahh Afande Ngulinzila”
“Majibu gani hayo kayatoa?” Koplo Bangi alijaribu kuchombeza swali
“Muuaji wa Mzee Kasimba ndie aliemuua Afande Ngulinzila…” akaweka nukta kidogo kuipa nafasi pumzi nzito iliyoambatana na mwayo kisha akaendelea
“… Alama za vidole zilizoonekana katika mwili wa marehemu kasimba ndizo zilizoonekana tena maeneo ya kifuani na kooni mwa Afande Ngulinzila” hapo hapo Ocd Nkeli akaitupia juu ya meza ya Koplo Bangi bahasha ya kaki yenye nakala ya vipimo kutoka hospitali kasha akamalizia kwa kuhoji
“Hawa ni akina nani?” huku akiwatazama Masu na wenzie
“Si ndio wale watuhumiwa wa kesi hii”
“Oooh sorry…” alijua amefanya kosa kuongea mambo nyeti kama yale mbele ya watuhumiwa, halafu akamalizia kusema
“..Ok ingiza na taarifa za vipimo hivyo katika Report yako kabla hujaiwasilisha mezani kwangu” hapo hapo Mkuu Akatoka

Kichwa cha Koplo Bangi sasa kikahama kwenye majibu yaliyomghadhibisha kutoka kwa Sheikh Jabu na sasa mawazo yakahamia kwenye taarifa mpya aliyoipokea kutoka kw mkuu wake wa kazi, sasa kazi ilikua ndio kwanza inaanza, akafunika mafaili kisha akanyanyuka kwenye kiti na kuwaamuru watuhumiwa wake wasimame na baada ya hapo akawarejesha tena selo ili aweze kuandika kwa utulivu taarifa yote baada ya kupata picha ya kila kinachoendelea kuzunguka ndani ya kichwa chake
*****
ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TISA

Katika hospitali ya mkoa wa Shinyanga shughuli za kila siku zilikua zikiendelea, pilikapilika za matabibu na wauguzi ziliendelea kama ilivyo ada, Hali ya ukimya ilitawala kidogo katika mabenchi maalum waliyokua wameketi baadhi ya wagonjwa waliokua wakisubiria huduma wakati mwili wa Marehemu Ngulinzila ukitolewa katika chumba maalum cha vipimo na kurejeshwa katika chumba cha kuhifadhia maiti, Hakika maiti hazoeleki maana watu wote waliingiwa na ubaridi, bila shaka wangejua aina ya kifo cha huyo anaetolewa ndani humo wangezidi kuzizima kwa hofu na upweke wa nafsi. Wakati Zoezi hilo likiendelea nae Koplo Bangi alikua amewasili eneo husika akiwa ametinga koti jeusi la suti na suruali ya kaki vijana wa mjini wanaita Mchuzi juu, cha ajabu Koplo Bangi hakua akijishughulisha kabisa kuangalia machela maalum iliyokua umeubeba mwili wa Ngulizila bali macho yake yaliyokua yamejificha ndani ya miwani ya jua yalikua yakiangaliana kwa tahadhari ya hali ya juu na Jicho moja la kijana mmoja mtanashati aliekua amesimama huku akiiangalia machela ile kwa umakini wa hali ya juu, Jicho hilo lilikua ni la Hunudu

Takribani dakika nzima macho mawili ya koplo Bangi yaliendelea kumtazama kijana huyu katili kutoka Waufi, tayari Koplo Bangi alianza kuhisi hali ya hatari eneo lile, alijaribu kuvuta kumbukumbu ya maelezo ya Masu kuhusu mtu mwenye ‘Chongo’ ambae ameukua akishirikiana na marehemu Ngulinzila katika kutaka kumuangamiza Masu. Wakati huo tayari kengere ya hatari ilikwishaanza kugonga ndani ya kichwa cha Hunudu baada ya kugundua kua alikua akiangaliwa sana na Afisa huyu wa jeshi la Polisi
“Hunudu..” Koplo Bangi aliita kwa sauti ya utulivu na ya uhakika kwamba alikua habahatishi, Sauti ya Koplo Bangilana ilipenya sawia katika masikio ya Hunudu lakini akajikausha kama mtu ambae hakusikia chochote
“Hunudu” Koplo Bangi aliita tena bila kuitikiwa na kijana huyu aliemkusudia, ndipo sasa akaamua kumsogelea na kushika Begani
“We Kijana si ninakuita wewe?”
“Nani? Mimi?” Hunudu alijibu kama mtu asiejua lolote kama kuna mtu alikua akimuita
“Sasa kumbe naongea na nani hapa?”
“Mbona Kibabe sana Mzee? Sikukusikia si unajua tena tunatembea na mawazo mengi, pengine ungeniita kwa jina langu ningesikia”
“Nimekuita mara mbili nzima, Hunudu, Hunudu, uko kimya tu”
“Hunudu? Mie siitwi Hunudu”
“Acha maskhara kijana au ulitaka nikuite Hunudu wa WAUFI?...” Baada ya swali hilo la kichokonozi Jicho moja la hunudu lilianza kuzunguka kama saa mbovu, hakika Hunudu alihamanika dhahir, mdomo ukajaa maji kabla ya Koplo Bangi kuendelea …
“..Pole kwa msiba wa mwenzenu, najua jinsi gani unavyoumia”
“Oya mbona unanizingua mzee? Hebu endelea na Shughuli zako, me sio Hunudu wala sijafiwa na mtu yoyote hapa”
“Haha ha ha..” Koplo Bangi alicheka kwa dharau ya hali ya juu aliyokua akimuoneshea Hunudu kua amemjua vizuri kasha akaendelea “Hunuduuu, Shefa Mkuu kutoka katika Dini ya Waufi, haya niambie umekuja kumuuguza nani hapa hospitali kama sio kuhakikisha umauti uliomfika mwenzio? Mimi najua kupambana na wachawi mnaotumiwa na mizimu, leo nitakudhibiti” Hunudu akainuka kwa jazba na wahka wa hali ya juu sana huku akianza kuondoka eneo lile kabla kiganja kipana cha Koplo Bangi hakijatua juu ya paji la uso la Hunudu na kumuachia maumivu makali Hunudu hali iliyopelekea taharuki kubwa kwa baadhi ya wagonjwa na ndugu zao waliokua wameketi katika mabenchi,

Masu hakukubali kudhalilika nae akarusha ngumi iliyotua katika kimpuma cha Koplo Bangi mpaka miwani ikaruka hewani na hapo sasa watu walishuhudia Sinema ya Bure kati ya miamba hii miwili, zilpigwa ngumi zenye viwango vya kimataifa, kila mmoja alionekana kupambana kwa kuzingatia kanuni sahihi za ngumi, Japo Hunudu alikua na Jicho bovu lakini alikua akizikwepa ngumi na mateke ya Koplo Bangi mithili ya Twiga anavyokwepesha shingo yake katikati ya miti mirefu awapo anakimbia, Baada ya kivumbi hicho cha dakika kama tano hivi Hunudu alikua akifuta damu iliyokua ikichuruzika kutoka katika tundu moja ya pua yake, Ngumi ya Koplo Bangi ilipenya na kutua alipokusudia..

Mpambano wa vidume hawa ulipelekea hali ya Sintofahamu hospitalini hapo kiasi cha wagonjwa na wauguzi kuanza kuparaganyika hovyo kila mmoja akijaribu kuiokoa nafsi yake,
“BANGIIIIIII” Sauti kali ilitokea nyuma ya ofisi ya Mganga mkuu, Koplo Bangi akageuka ndipo alipokutanisha macho na Ocd Nkeli , kabla jajafanya chochote huku nako kwa wepesi wa ajabu Hunudu alirukia upande wa pili ambako kuna Korido ndefu isiyokua na kona akakatiza ili akimbie, hapo hapo kitendo bila kuchelewa Koplo Bangi nae akaruka mpka upande wa pili cha ajabu alipofika katika Korido hiyo aliokatisha Hunudu alikuta ‘PATUPU’ Hunudu hakuonekana kabisa, alikua amepotea ghafla. Wakati Koplo Bangi akiendelea kustaajabu tukio lile kama la mazingaombwe tayari OCD Alikua ameshafika eneo lile huku Pistol yake ikiwa mkononi pia akiwa na kijana mwingine alievalia sare zake za jeshi la Polisi bila shaka ni dereva au mlinzi wa OCD
“Kuna nini Koplo?” Alisaili Amos Nkeli
“Afande dah, haya maajabu ya mwaka”
“Kivipi?”
“Amepotea ghafla tu kama maigizo”
“Ni nani kwani Yule?”
“Hunudu wa WAUFI”
“HUNUDU??”
“Ndio afande, huyo huyo niliemuelezea kwenye maelezo ya kesi ile ya kishirikina”
“We umemjuaje?”
“Ni story ndefu Afande”
“Twende haraka Ofisini” OCD Amos Nkeli na Koplo Bangi wakaanza kuondoka huku kundi kubwa la watu likiwashangaa, nao hawakugeuka nyuma wakaanza kutoka kabisa katika eneo lile la hospitali, walipofika nje ya Hospital wakakuta gari ya OCD ikiwa inawasubiri na ndani yake kuna askari mwingine akiwa ameketi vizuri katika uskani , wakaingia wote na safari ya kurudi kituoni ikaanza
*****

Ndani ya Ofisi ya Amos Nkeli, mkuu wa kituo cha Polisi Shinyanga alikua ameketi juu ya kiti Koplo Bangi, wakati huo Afande Nkeli Akiwa amesimama huku amechegama kidogo katika nondo za dirisha, Saa ya ukutani ilikua ikionesha kua ilikua imetimu saa Kumi kamili Alasiri, Ocd Nkeli alikua amechanganyikiwa sana baada ya kusikiliza maelezo yote ya Koplo Bangi kuanzia alivyomtambua Hunudu kutokana na maelezo ya Masu, mpka alipoanza kumuhoji na kumgundua na hatimae mapambano yalipoanza, hakika Amos Nkeli alikua katika lindi la mawazo yasiyo na majibu
“We ulienda pale Hospitalini kufanyaje?”
“Afande ni wewe ndie ulienipigia simu kua tukutane pale, kuna taratibu za kufanya” Majibu ya Koplo Bangi yalizidi kumfanya sasa Ocd azidi kujiona kua amechanganyikiwa maana ni kwli yeye ndie aliemuagiza Koplo Bangi kua wakutane kule..
“Ooh.. Ok Ok, nimekuelewa Koplo, sasa naungana na wewe kua Afande Ngulinzila alikua akijihusisha na mambo ya kishirikina,Maelezo ya kina Masu ni sawa kabisa hivyo sasa tunaweza kuwapa dhamana hawa watuhumiwa wote kasoro Masu tu…” Kabla hajamalizia kuongea akakohoa kidogo halafu akarudi akaketi katika kiti chake akawa anaangaliana na Koplo Bangi ndipo akaendelea “Masu kwakua bado anapaswa kutusaidia ukweli kuhusu Mzee Kishindo hivyo inabidi aendelea kua hapa, wakati huo huo pia Masu anakabiliwa na ile kesi kule Tabora mpaka mgonjwa atakapokua na hali nzuri ili tujue ukweli wa mambo”
“Sawa afande..”
“Wakati huo jitihada za kumtafuta Yule Mzee Kikoko nazo ni za muhimu sana maana nae anaonesha anajua mengi sana katika kesi hii,,” wakati Amos Nkeli anajaribu kumpa maelezo Mpelezi wa kesi hiyo Koplo Bangi mlango ukagongwa kasha akaingia askari mmoja wa kike, akapiga saluti kasha akatoa taarifa ya muhimu kwa Mkuu wake huyo
“Afande kuna mzee hapo Nje amekuja amesema amepata taarifa kua anatafutwa na Jeshi la Polisi na pia watu wake wamekamatwa wako hapa, nadhani ndo Yule Mzee afande Bangi ulitupa taarifa zake”
“Mzee gani huyo?” Koplo Bangi aliuliza kwa haraka na hamu ya kutaka kumjua
“Amesema yeye ni Alwatan Kikoko” wakati askari huyu anamaliza tu kuweka nukta katika sentesi yake tayari Koplo Bangi alikua ameshainuka huku akienda huko kaunta kumuangalia mtu waliekua wakimuhitaji muda mrefu wakiamni amekimbia, sasa anaambiwa amejileta mwenyewe, amejisalimisha

Koplo Bangi alipofika pale Kaunta alikutanisha macho na Mzee Kikoko, Mzee mtata, Mzee wa mjini, Mzee anaeonesha dalili zote za kujiamini ikiwa ni pamoja shari inayomtembea mwili mzima, Koplo Bangi hakua akimjua vizuri mzee huyu ila baada ya kumuona aliweza kuitambua sura ile kwa kua ni ya Mtu wa palepale Mkoani Shinyanga na pia alikua akifanana sana na mwanae ambae amekua akihojiwa na Koplo Bangilana mara kwa mara, Koplo akamuashiria Mzee Kikoko azunguke nyuma ya Kaunta hiyo nae Mzee Kikoko bila ajizi akiwa na Begi lake dogo la nguo lililoashiria kua alikua ndo amefika kutoka huko Dodoma alizunguka kule alipoitwa na kukutana na Koplo Bangi ambae alimchukua mpaka Ofisini kwa Ocd Nkeli, na baada ya kuketi katika kiti chake alianza kusailiwa mfululizo
“Mzee Kikoko?” alianza kuongea Afande Nkeli
“Naam ndo mimi, Alwatan Bin town”
“Umekua wapi siku zote hizo wakati unatafutwa?”
“Mie nilikua Dodoma, ambako nilikua nimelazwa hospitalini, ndipo nilipopata taarifa kua mnanitafuta na mmewakamata watu wangu kwa ajili yangu, haya sasa nimekuja mwenyewe na muwaachie huru”
“Sio kwamba ulikua umekimbia?”
“We unaona kuna sura ya kukimbia hapa?”
“Ulipata wapi taarifa kua unatafutwa?”
“Kutoka kwa vyanzo vyangu vya khabari, na mashushushu wangu wa kujitegemea” Kikoko alikua akijibu kama vile anaongea na wahuni tu wa mtaani, kitu ambacho kilizidi kumjaza hasira Afande Nkeli japo alijitahidi kuzificha hisia zake, baada ya afande Nkeli kutulia kwa muda muda akaendelea
“Koplo”
“Afande” Koplo Bangi aliitika kwa nidhamu
“Wapigie simu wale wazee waliokuja kuwawekea dhamana hao watuhumiwa, waje wawadhamini ndugu zao, ila Masu asitoke na huyu Mzee muweke ndani mpaka atakapokua tayari ku..” kabla hajamalizioa sentesi yake akakatizwa na Mzee Kikoko
“Hivi kosa langu ni nini hasa mbaona kama siwaelewi? Na kwanini mnapanga nani adhaminiwe na nani asidhaminiwe?”
“Kaa kimya mzee” Bangilana alimjibu kwa mkato kabisa
“Siwezi kukaa kimya, ni haki ya kila mtuhumiwa kujua kwanini anashikiliwa, na ni haki pia kwa mtuhumiwa kupewa dhamana, kijana haujui kazi yako inataka nini?” Kabla Koplo Bangi hajajibu lolote Afande Nkeli kadakia
“Ulipigana na marehemu Kishindo siku moja kabla ya kifo chake hivyo una kila sababu za kujibu juu ya hilo”
“Vipimo vya matabibu vinaonesha kua Kishindo alikufa kwa kupigwa na radi, kwahiyo unataka kuniambia kua zile ngumi zangu zilikua kama shoti ya umeme iliyojilimbikiza mwilini mwake ikaenda kugeuka radi huko porini?”
*****

Nje ya wodi ya wagonjwa mahututi katika Hospitali ya rufani ya Kitete mkoani Tabora kulikua na hali tete, baada ya wauguzi kugundua kua mmoja wa wagonwa waliokua mahututi ametoweka katika mazingira ya kutatanisha, Mgonjwa huyu Nyamizi Fundikira alikua katika uangalizi maalum kufuatia kesi liyopo kituoni inayohusisha tukio lake la kupigwa mapanga mpaka kupoteza fahamu huko Kipalapala na kufanya watuhumiwa wa tukio hilo ambao ni akina Ngaliba Kayoka na Babu yake Masu washikiliwe na Polisi kituoni hapo Tabora mpaka hali ya mgonjwa itakapoimarika kwa ajili ya kupata uhakika wa taarifa za maajabu kua aliempiga na mapanga alitoweka katika mazingira ya ajabu

Wauguzi walikua wamechanganyikiwa vilivyo, hofu ilizidi kutamalaki hospitalini hapo, hakuna aliejua mahala alipokwenda mgonjwa Yule, kama ametekwa au Laa, kama amerudiwa na Fahamu akaamua kutoweka au Laa, ilikua ni hali ya fadhaa kubwa, tayari taarifa zilikua zimepelekwa Polisi na muda huo Sajent Malumbo alikua njiani akielekea hospitalini hapo kufuatilia ukweli wa kadhia hiyo
*****
Baada ya majibizano ya muda mrefu hatimae Koplo Bangi alimchukua Mzee Kikoko na kuandika maelezo yake yote na kisha ‘akamsweka’ ndani, baada ya zoezi hilo kukamilika ndipo akachukua simu na kuwapigia wazee waliokuja kuwadhamni Sheikh Jabu na Masu hapo mwanzo, wazee hao ni akina Mzee Kagomba ambao ni watu wa karibu sana na Mzee Kikoko. Na haikuchukua muda akina Kagomba wakawasili pale kituoni na walipokamilisha taratibu zote za dhamana walifanikiwa kuwatoa watu wawili tu Sheikh Jabu na Mama Almasi ambae ni mke mdogo wa Mzee Kikoko
*****

Kijiwe mashuhuri cha kahawa kinachomilikiwa na Mzee Kagomba swahiba wake wa karibu na Mzee Kikokoo Kilichopachikwa jina la BBC kutoka na kupatikana wa kila habari zote zinazojiri kila pembe ya mji siku hiyo kilikua kimesheheni wadau wengi zaidi kutoka na kupatikana kwa habari mpya kua Mzee Kikoko amejipeleka Kituoni na hatimae amewekwa ndani, pia katika Kijiwe hicho siku hiyo alikuwepo na Sheikh Jabu ambae baada ya kuachiwa na Polisi ilibidi aende akafike nyumbani kwa Mzee Kagomba ili kuepusha hali ya utata baina ya familia hizi mbili za Mzee Kikoko, alijua fika endapo ataenda kukaa kwa Mama Masu basi angetafsirika vibaya kwa Upande wa familia ya Mama almas ambae ni mke mdogo wa Mzee Kikoko halikadhalika kama angeenda kufikia kwa Mama Almasi, na kwakua msiba ulikua umekwisha kule nyumbani kwa marehemu Kasimba hivyo hakua na sababu ya kufikia kwa yeyote kati ya wake wa rafiki yake, akaamua kufikia nyumbani kwa Mzee Kagomba ambae ndie alieenda kumdhamini akishirikiana na mke wa Sheikh Jabu ambae yuko pale Shinyanga tangu kwa takribani siku tatu hivi akiwa na watoto wadogo wa Masu ambao walitakiwa kutolewa kafara na Mzimu wa Waufi, Judith ambae ni mke wa Masu muda wote huo alikua Arusha baada ya kuchukuliwa sasa na kaka yake mkubwa ambae anafanya kazi huko

Siku hiyo mjadala mkubwa ulikua ni juu ya kadhia nzima inavyoendelea katika family ya Kikoko
“Sasa ilikuaje bwana Kikoko akajitokeza?” aliuliza mzee Maguno
“Yule bwana ni mwingi wa khabari, mie wakati ndo nimechukuliwa na askari siku ile ya kwanza nilipata Wasa’a wa kuteta nae kwa njia ya simu nimpa hadhari kua asijitokeze kabisa, Khaa ghafla leo namuona mwenzangu huyu hapa kituoni na sharubu zake”
“Kweli alwatani Kikoko kidume, nasikia kamkaripia mpaka mkuu wa kituo”
“Unajua hakuna mkate mgumu mbele ya chai, atalainika tu ile ni dola inataka heshima yake”
“Naam, na Wahenga walisema ‘Akikalia kigoda mtii’, mwenye mamlaka ni mwenye mamlaka tu”
“Hivi jamani mie naomba kuuliza, hivi pamoja na ukaribu wenu na Alwatan Kikoko mmeshindwa kabisa kumuweka chini wazee wenzie mkamkanya na kumpa ushauri ili sasa suala hili lifikie mwisho? Maana kwa hali nayoiona mimi ni kwamba Mzee Kikoko anazidisha tatizo kila kukicha” alidakia mazungumzo bwana mmoja mmoja hivi anaeonekana kua si kijana sana lakini pia si Mzee wa rika la kina Mzee Kagomba, swali lake liliwafanya wengi wakae kimya huku wakionesha kumuunga mkono kwa hoja yake aliyoiwasilisha kwa mtindo wa swali, ndipo Jabu sasa akaanza kutiririka
“Binafsi leo niliongea kwa kirefu sana na Bwana Kikoko kuhusiana na kisanga hiki, hasa hasa tatizo lake la jazba na mihemko isiyokua na maana, na ameonesha kujutia kila nukta aliyoisababisha, na akaniagiza kua sasa ni wakati wa kumpeleka Masu huko Kipalapala akafanyiwe matambiko yao, na pia amekiri kua sasa ni wakati wake yeye kwenda kuwataka radhi ukweni kwake huko Tabora kwa kuyapuuza na kuyazembea matatizo haya, pia akanitaka nikishatoka ndani mule niende kwa Mama Masu nikajaribu kumsihi kua nae akawatake radhi huko Tabora ili tusafiane nia sote kwa pamoja..” Baada ya maelezo hayo Sheikh Jabu akachukua kikombe chake cha kahawa na kuanza kuinywa taratibu huku hadhira nzima ikiwa imetulia kuskiliza maelezo ya Sheikh Jabu, ndipo tena Mzee Kagomba alipoongeza neno
“Kikoko anakuja kukunja ngumi ugomvi umekwisha”
“Hapana, ni hatua kubwa sana hiyo kwa mtu mtata kama Kikoko kuonesha kukiri, unajua Dhambi ikikaririwa ni nusu ya marekebisho na kulijua tatizo ni nusu ya tiba” alidakia Mzee Kagomba
“Nimesema hivyo kwa maana kua hayo maamuzi angeyakubali tangu mwanzo pengine saa hizi wala tusingekua tunajadili jambo hili hapa, lakini upuuzi wake kidogo tu umezua yote haya, ndio maana Wahenga wakasema ‘Cheche ya moto huteketeza msitu’ Sasa umesikia habari za Tabora huko?..”
“Zipi tena?”
“Si yule Mgonjwa aliekua akisubiriwa apone ili atoe ufumbuzi wa tukio la kupigwa kwake Panga ili walau akina Masu na babu yake wapate tumaini la kutoka..”
“Amefariki?”
“Bora angefariki tukajua moja, Mgonjwa ametoweka tu ghafla”
“Afanaleik..” Wadau wote walipigwa na butwaa kusikia habari hizo mpya sasa, na mjada wa kina ukachukua nafasi, kila mtu alikua ameingiwa na hofu na kuamini kua sasa akina Masu wataozea ndani, lakini Sheikh jabu akawapa moyo kidogo
“Unawajua Waswezi wewe? Wale ni hatari usije ukawachezea, bila shaka hilo tukio ni lao”
“Sasa kwanini wamteke mgonjwa wao?, Itakua ni Waufi hao Baba, wababe wa vita” Kijana mmoja aliongea kwa sauti ya kebehi,
“Sasa nimeongea na Mama Masu, ananiomba nimsaidie haraka iwezekanavyo ili kesho aende huko Kipalapala Tabora ili akaombe msamaha na pia akaombe hifadhi huko maana amesema zimebaki siku tatu ili afanyiwe kitu kibaya na hao Waufi, nimejaribu kumdodosa lakini hajaniambia siku tatu hizo ni za nini hasa! Na kitu hicho kibaya afanyiwe kivipi tena!, Basi ni utata juu ya utata”
“Mama Masu anawajua vizuri waufi, ana makubaliano nao ambayo amaeyakiuka, na sasa watammaliza yeye pamoja na Masu kama hatokua makini” Mzee Maguno ambae ni mtaalam wa tafsiri za ndoto aljibu kwa kujiamini sana kitu ambacho kilisababisha Mzee Kagomba atie neno
“Sasa wewe unazipata wapi hizi habari na kila siku unajifanyaga haujui chochote?”
“Ajuaye mengi, hasemi mengi, lakini pindi mwaka ila kuna siku mtanikubalia maneno yangu”
“Mnh haya, tuyaache hayo, sasa Sheikh Jabu utaenda na shemejiyo huko Tabora?”
“Hapana, nimemwambia kua kesho inabidi nirudi mara moja Dar kuongea na bwana mmoja hivi mkubwa serikalini pengine atatusaidia katika kesi hii hivyo huenda yeye kesho kaondoka peke yake na kwenda Tabora, ila anaonekana kuchanganyikiwa sana hasa baada ya ile habari ya mpambano wa nguvu hopitalini kati ya afande Bangi na huyo Hunudu wa Waufi”
“Hunudu wa Waufi?” Kagomba aliuliza kwa mshangao, bila shaka hakua na taarifa zozote za kilichojiri kule Hospitali. Ndipo sasa Sheikh Jabu akaanza kuwapa mkasa mzima ulivyo kuanzia kwa Marehemu afande Ngulinzila mpaka tukio hilo la hospitalini, kila mmoja alibaki mdomo wazi…
*****

USIKU WA MANANE
Chini ya mti mkubwa kama ilivyo ada wafuasi wa Mzimu wa waufi walikua wamekusanyika kwa wingi, hoja zilikua nzito, walikua wakijibizana mpaka kutishia hali ya utengamano wao, inaonesha walikua katika malumbano makali sana
“Mimi nataka kujua kwanza kwa nini yeye Mama Masu mwenyewe hajaja leo?” aliuliza mama mmoja wa makamo aliekua amejifunika shuka nyeusi ambapo akajibiwa na mkuu wao aliekua amekaa juu ya Kigoda cheusi
“Mama Masu hatukumpa taarifa ya kuja hapa leo kwa sababu mjadala huu unamuhusu yeye hivyo hapaswi kuwepo hapa”
“Sawa, sasa mimi nasema hivi hakuna muda wa kupoteza hapa, Mizimu imeshakasirika huko na tusipokua makini tutatahamaki tumeangamizwa wote hapa, cha msingi bado siku tatu tu za kupambana na Masu na bila shaka siku hizo hazitoshi tena kwetu hivyo huu ni muda muafaka wa kumtoa kafara Mama Masu mwenyewe ili tuendelee na mambo mengine” Mama yule alihitimisha hoja yake kabla ya kijana Hunudu kusimama na kuanza kutoa taarifa yake
“WAUFIIIIIII”
“Mzimu wa watemi wa Bahari”
“Jamani mimi sioni haja ya kulumbana hapa, muda umeshatutupa mkono, kwa sasa tunapambana na watu wengi sana, hata yule askari niliepambana nae kule hospitali leo ana nguvu za ziada, anasaidiwa na Waswezi bila ya kujijua mwenyewe ndomaana alikua akinizidia maarifa mara kwa mara, wakati huo mfahamu kua yule Mgonjwa sitaweza kumpata tena kirahisi maana Waswezi wameshamtorosha hivyo baada ya siku tatu hizi kukamilika inabidi sasa tummalize Mama Masu mwenyewe na kuachana na Waswezi mapema” Baada ya maelezo hayo ya Hunudu kukamilika aliketi chini, ndipo sasa mkuu wao anaefahamika kama Mtemi Kalovya aliposimama na kuanza kuongea
“Najua inauma kumtoa mwenzetu lakini hayo ndio makubaliano yake na Waufi, hatuna jinsi, tumejitahidi kwa kadri ya uwezo wetu lakini imeshindikana, inabidi maamuzi yapitike tu vinginevyo tutaangamizwa sote hapa, Mzimu umetuasa kwamba zikipita hizo siku zilizosalia bila ya kua tumemmaliza mmoja kati ya Masu au Mama yake basi sote hapa tutaangamizwa kila mmoja kwa namna yake, pia mkumbuke kwamba kitengo chetu cha mapambano kimepwaya baada ya Ngulinzila kuuawa hivyo amebaki Hunudu peke yake, nae akizidiwa tu basi tumekwisha, hivyo sasa mwenye mapenzi mema na Mama Masu kwa sasa anaweza kumsaidia tu kwa kumuangamiza Masu ila ikifika siku ya tatu kutokea leo endapo Masu akiwa bado salama nimetoa Ruhusa kwa Hunudu kufanya kazi yako ya kutuletea damu na kiwiliwili cha Mama Masu…, kama atatokea mwenye mawazo yoyote anifuate mapema nyumbani kwangu, kwa sasa hakuna jipya kila mmoja arudi nyumbani kwake” alihitimisha Mtemi Kalovya na kundi lote kutawanyika japo wengine wakiwa na kinyongo kwa mpango wa kummaliza Mama Masu
*****
Siku iliyofuata asubuhi na mapema zikiwa zimesalia siku mbili tu ili aangamizwe na Waufi kama kafara Mama Masu alikua ndani ya Basi akielekea Kipalapala mkoani Tabora akiwa na malengo makuu mawili, Mosi, ni kwenda kuwaangukia ama kuwataka radhi wazazi na familia ya mke mwenzie ambae ni Mama almasi kwa kitendo alichokifanya miaka mingi iliyopita cha kuuiba ujauzito wa mke mwenzie kishirikina, pia aliamini kua nguvu za mizimu ya Kasomangila chini ya Waswezi ni kubwa kuliko Waufi hivyo aliona kwa sasa muda wake wa kutolewa kafara umeshasogea hivyo ni bora akawaombe radhi huko ili apate hifadhi kwa nguvu ya mizimu hiyo ya Kasomangila chini ya Waswezi.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA KUMI ................. MWISHO

Siku iliyofuata asubuhi na mapema zikiwa zimesalia siku mbili tu ili aangamizwe na Waufi kama kafara Mama Masu alikua ndani ya Basi akielekea Kipalapala mkoani Tabora akiwa na malengo makuu mawili, Mosi, ni kwenda kuwaangukia ama kuwataka radhi wazazi na familia ya mke mwenzie ambae ni Mama almasi kwa kitendo alichokifanya miaka mingi iliyopita cha kuuiba ujauzito wa mke mwenzie kishirikina, pia aliamini kua nguvu za mizimu ya Kasomangila chini ya Waswezi ni kubwa kuliko Waufi hivyo aliona kwa sasa muda wake wa kutolewa kafara umeshasogea hivyo ni bora akawaombe radhi huko ili apate hifadhi kwa nguvu ya mizimu hiyo ya Kasomangila chini ya Waswezi.

Wakati Mama Masu akiwa ndani ya basi kuelekea mkoani Tabora kisanga kingine kinatokea katika kituo cha Polisi mkoani Tabora ambako Sajent Malumbo alikua katika ofisi yake ya upelelezi, alikua ameketi juu ya kiti chake huku akiwahoji watuhumiwa wake wa kesi ya kule Kipalapala mkoani Tabora ambao walikua wameketi chini sakafuni, japokua kesi haikua ni ya mauaji tena kama ilivyotafsiriwa mwanzoni lakini ilikua ni kesi ngumu sana baada ya mtuhumiwa aliekua mahututi hospitalini kutoweka ghafla, wakati Sajent Malumbo akiendelea kuwahoji watuhumiwa wale ili japo kupata kujua japo labda pa kuanzia kufuatia kutoweka kwa Nyamizi ndipo alisikia sauti ya askari mwenzie nje ya ofisi hiyo ikitokea usawa wa dirishani
“Mr Malumbo”
“Ndi afande”
“Kuna mgeni wako hapa”
“Ok, nina mazungumzo kidogo anaweza kunisubiri?”
“Lakini ingekua vema kama angekuja tu humo humo ndani maana anweza kusaidia kazi yako”
“Ok Mlete” Sajent Malumbo alishtushwa na maneno ya afande mwenzie kua mgeni huyo anaweza kusaidia kazi aliyonayo, hakujua ni nani, akahisi labda ni daktari amekuja kutoa taarifa mpya kuhusu mgonjwa alietoweka, kwakua ofisi ya Sajent Malumbo ilikua ndani kabisa na ukizingatia kuna kona nyingi sana mpaka kuifikia hivyo ilichukua kama dakika tano hivi kabla ya Afande Salma kuingia ndani ya ofisi hiyo akifuatiwa na mgeni alitajwa, Macho ya Sajent Malumbo yalipiga usoni kwa sasa huyo alieambiwa klua ni mgeni wake lakini hakumtambua kwa haraka, alijaribu kuvuta kumbukumbuku sura ikawa iamuijia lakini haikumbuki vizuri lakini sauti kali kutoka kwa Ngaliba Kayoka, mmoja kati ya wale watuhumiwa wake wawili waliokua wamekaa katika sakafu ya zege ya ofisi hiyo iliweza kumpa jibu la swali lake
“NYAMIZI?” Ngaliba Kayoka alishtuka sana kumuona Nyamizi akiwa mzima kabisa japo amefunika kilemba kichwani hivyo hakuweza kuona jeraha lililosababishwa na upanga wa Hunudu
“Ndio mimi Mjomba”
“Mungu ashukuriwe” Ngaliba Kayoka akainuka kwa furaha ili akamkumbatie mpwa wake huyo aliesemekana kua amekufa na baadae ikadhihirika kua ni mzima japo mahututi, na baadae akatoweka kabisa hospitalini. lakini alakemewa na sauti kali kutoka kwa Sajent Malumbo
“Kaa chini mzee, unataka kufanya nini? Unataka kutoroka? Au unataka kutunyang’anya silaha?”
“Hapana afande nilitaka kumpokea binti yangu, ndie huyu uliesema ametoweka hospitalini”
“Kaa chini Mzee” Ikabidi Ngaliba Kayoka arudi aketi tena chni kwa upole, wakati huo babu yake Masu nae alikua ameketi pale chni akiangalia kila kinachotokea kwa macho ya mshangao
“Afande Salma umemtoa wapi huyu dada?” Malumbo aliuliza
“Amekuja mwenyewe akajieleza sasa kwa kua nilikua naijua hii kesi ndipo nikamuelewa na kumleta huku” baada ya majibu ya afande Salme sasa Sajent Malumbo akamgeukia Nyamizi
“haya dada hebu keti hapo kwenye kiti” tayari sasa sura ya Nyamizi ilikita katika ubongo wa Sajent Malumbo, alimkumbuka haswa kwa alikwisha muona mara kadhaa alipokua hospitalini
“Ahsante” Nyamizi akaenda mpaka kwenye kiti alichoelekezwa na kuketi kwa nidhamu
“Enhee Nyamizi hujambo?” alianza Sajent Malumbo kumuhoji Nyamizi sasa
“Mie sijambo afande”
“Pole na maumivu”
“Ahsante ninaendelea vizuri tu kwa sasa”
“safi, haya, hawa wazee unawafahamu?”
“Ndio, wote ni wajomba zangu”
“Ilikuaje wakakukata mapanga? Uliwafanya nini?”
“Hwakunikata hata na kiwembe, ila ni Yule Hunudu mshenzi ndie alienifanyia unyama ule”
“Hunudu? Ndo nani?” Sajent Malumbo alijifanya kutokufahamu kilichotokea japo alikua na habari zote za tukio zima la Hunudu kuvamia kule kipalapala na kumdhuru dada huyu
“Hunudu Yule kijana mwenye Chongo kutoka kwa wachawi wa Waufi”
“Mnh, haya hebu tuelezee ilikuaje tukio zima” Sajent Malumbo alimpa swali la mtego dada huyu ili atakapoelezea ndipo aoanishe na maelezo ya hawa babu zake Masu, Nyamizi alianza mwanzo wa tukio mpaka mwisho bila ya kupishana na maelezo ya akina Ngaliba Kayoka.. Maelezo yalikua ni ya kutisha na kuogofya sana, japokua ilikua kama vile filamu lakini ikambidi Sajent Kuamini tu sasa kwakua anaesimulia ndie aliepigwa na amekanusha kuusika kwa wazee wale zaidi ya kumtuhumu huyo Hunudu..
“Kwahiyo hata kama tutawaachia huru hawa wazee wako una uhakika hawakukudhuru hata kidogo?”
“Ndio afande, hawa ndio waliokua wakipigana na Hunudu muda mfupi kabla hajanirukia mimi wakati nilipokua nakimbilia kuwaita ndugu zetu wengine kama nilivyokueleza”

Wakati Nyamizi alipokua akitoa maelezo yake Sajent alikua akiendelea kuandika maelezo hayo kwa utulivu na umakini wa hali ya juu
“Afande acha mie nikaendelee na majukumu ya kujenga Nchi nyie endeleeni kupambana na ushirikina” Sauti hii ilimshtua Sajent Malumbo, ilikua ni sauti ya Afande Salma, Malumbo hakujua kama kumbe afande Salma alikuwepo muda wote mule ndani maana kwa utata wa stori ile alijukuta kama hamuoni vile. Baada ya Sajent kumaliza kufanya mahojianona kuandika aliwasainisha watuhumiwa wote na kisha akamsainisha Nyamizi katika maelezo yake kisha alinyanyua simu na kumpigia Koplo Bangi wa Shinyanga na kumuelezea hali halisi ilivyo ili sasa kama ni dhamana Masu apewe, alipomaliza kufanya kazi hiyo akawatafuta kwa njia ya simu ndugu zao na kina Ngaliba kayoka waliowasili kituoni hapo mara kadhaa kwa ajili ya kuwadhamini ndugu zao ili sasa waweze kufanya hivyo Ndugu waliwasili na kukutana na Nyamizi hapo kituoni walifurahi sana, wakapokeana na kulakiana kabla ya kuanza zoezi la kuwawekea dhama wazee wao lakini kutokana na taratibu baadhi za kipolisi zoezi la udhamini halikukamilika siku hiyo, ikabidi Ndugu waondoke ili kesho yake ndipo wakawatoe akina Ngaliba Kayoka na Babu Masu
*****
Huko Shinyanga nako Baada ya Koplo Bangi kuongea na mkuu wake wa Kituo ambae amekua akimsaidia kwa karibu sana kupambana na kesi hii waliamua kuwapa dhamana watuhumiwa wao wawili Mzee Kikoko na Masu hivyo Mzee Kagomba , Sheikh Jabu na Mzee Maguno waliwasili kituoni hapo kuwadhamini watu wao lakini zoezi halikua rahisi japo waliambiwa dhama iko wazi, walifanikiwa kumdhamini Masu tu ila Mkuu wa kituo aligoma kumuachia Mzee Kikoko bila shaka kutokana na majibu mabaya ya Kikoko tangu awapo pale kituoni, Baada ya akina Mzee Kagomba kuhangaika sana ndipo mkuu huyo akawaambia kua waende kesho yake kumtoa hivyo ikabidi sasa kwa siku hiyo waondoke na Masu tu
*****

Siku ya ijumaa ikawasili ikiwa imebaki siku moja tu ya Kafara kwa Mama Masu, bila shaka sasa Waufi walikua wakisubiri muda ufike ili wammalize Mama Masu ambae muda huo alikua ameshafika Tabora mjini kwa baadhi ya ndugu zake waishio hapo ili jioni yake wamsindikize sasa Kipalapala kwa ajili ya dhamira aliyoikusudia. Jitihada za waufi za kumshambulia Masu zikawa kama zilizofifia sana kitu ambacho kilifanya sasa hali iwe mbaya sana kwa Mama Masu. Asubuhi hiyo tayari Wazee wa mji walikua katika kituo cha Polisi kwa ajili ya kumdhamini Mzee Kikoko japo zoezi lilizidi kua gumu japo Kikoko hakua na makeke tena lakini dharau na majigambo yake yalikua yakimgharimu, Mkuu wa kituo alikua ‘busy’ sana na shughuli zake na alitoa taarifa kituoni kua mtu yeyote asitoe dhamana kwa Mzee Kikoko mpaka atakapoidhinisha yeye. Baada ya kuhangaika sana kwa wazee hawa ndipo saa Nne asubuhi kwa huruma tu ya Ocd Nkeli akapata dhamana na kuachiwa, wakaondoka mpaka nyumbani kwa Mama Masu lakini hawakumkuta
“Vipi huyu nae kisisina kaenda wapi?” Mzee Kikoko alikua akiuliza kuhusu mama masu
“Usimuite kisisina mkeo, sio uungwana” Mzee Kagomba alimjibu
“Huyu mwanamke ni kisisina tu, yeye ndie sababu ya yote haya”
“Wewe ndie kisisina kwakua uliyafumbia macho matatizo uliyoyajua kabisa, na mkeo alikua akijivunia jeuri na ubabe wako”
“Mimi sikua nikijua kuhusu haya mambo ya kishirikina kwa kua nilishapata kuyasahau kitambo kirefu sana, lakini kumbe yeye alikua akielewa kinachomsibu mwanangu halafu akazidi kuchochea tu”
“Usimshushie zigo la lawama, wewe mzee mwenzangu ujuaji umekuzidi sana na ndio maana sasa yamekukumba yote haya”
“Bwa Kagomba tafadhali ntakudandia sasa hivi nikutwange vichwa, ohoo usitake kunikoroga saa hizi”
“Nini? We una ubavu wa kupigana na mimi? Hapo ulipo unawazo kila mia kichwani nikikusukuma tu unaanguka, halafu ukiniletea ujuaji wako nakurudisha polisi mimi ndie mdahamini wako” Maneno ya Mzee Kagomba yalimtisha kidogo Kikoko ikabidi tu sasa apunguze Munkari
“Jamani hapa hakuna haja ya kulumbana, tuongee ki utu uzima sasa, iko hivi Bwana Kikoko mkeo Mama Masu amekwenda Kipala pala Tabora” alianza kuongea Sheikh jabu
“Umeona sasa huyu mwanamke, ameenda kufanya nini wakati huko ndiko alipoyakoroga?!” alidakia Mzee Kikoko alieonekana kujawa na jazba kama kawaida yake, lakini aliwahiwa na Mzee Kagomba ambae licha ya kumdhamini lakini alionekana kukerwa sana na vitendo vya rafiki yake huyo
“Acha akili za uwaluwalu wewe mtu mzima, tulia upewe habari sio unakurupuka tu, hebu Sheikh Jabu endelea
“Haya, Mama Masu amekwenda Kipalapala kutafuta suluhu na kuwaomba radhi wazazi wake na Mama almasi pamoja na mama Almasi mwenyewe ambae nae ameondoka kaenda huko huko Kipalapala ameitwa na wazee wake wamemuambia kua kuna dharura huko… Mwanao Masu nae ameondoka amekwenda huko huko”
Sheikh Jabu akanyamaza kidogo huku akiwaangalia machoni wazee wenzie waliokua wakitupiana macho kama majogoo yanayojiandaa kuvaana, kisha akaendelea “Pia habari kutoka huko kipalapala ukweni kwako zinasema hivi leo baada ya kutachiwa na Polisi na wewe unahitajika huko inaonekana kuja jambo zito na la muhimu hivyo jiandae muda huu tunaenda kutafuta usafiri wa kwenda Tabora,” Maneno ya Sheikh Jabu yalimuingia sana Mzee Kikoko akawa kama aliyepagawa sana
“Jamani kwa jinsi nilivyochoka hapa mpaka mkia sidhani kama nitaweza kusafiri leo” hapo hapo Mzee Kagomba akampigapiga Mzee Kikoko na kiganja chake begani huku akimjibu kwa dharau
“Acha ujuha we mzee, tunaondoka sasa hivi, ingia bafuni uoge kisha tunapitia nyumbani kwangu kumchukua mke wa Sheikh Jabu na wale watoto wa Masu baada ya hapo msafara wa hiari ulio wa lazima utaanza, umeelewa” Kikoko alikua na jazba lakini akajikuta hana cha kufanya, alitamani kuuliza juu ya hao wajukuu zake alioambiwa kua wapo hapo Shinyanga lakini muda haukua rafiki tena ikabidi aingie bafuni kwa upole kabisa kichwa chini mikono nyuma, ambako baada ya kupata maji alipata chakula kasha safari ya kwenda kwa mzee Kagomba kuwachukua watoto wa Masu pamoja na mke wa kikoko ikaanza, Sheikh Jabu alikua na hali nzuri ya kiuchumi hivyo gharama zote zilikua juu yake ikiwa ni pamoja na kukodisha gari ndogo ya kuwapeleka Tabora, Kipalapala

Wakati huo kule Tabora akina Ngaliba Kayoka na Babu yake Masu walikua wameshaachiwa kwa dhamana, na mpaka muda huo walikua nyumbani kwa ndugu zao hapo hapo Tabora mjini katika kata ya Chemchem, japo walikua wamechoka ila walipokea taarifa kutoka kwa mkuu wa waswezi huko Kipalapala kua ni lazima siku hiyo waende huko kuna jambo zito linatakiwa kufanywa hivyo waliamua kupumzika ili mchana waanze safari ya kuelekea huko kipalapala
*****

Safari ya kutoka Shinyanga ilikua ndefu sana lakini ilikua ni lazima Kikoko afikishwe kipalapala siku hiyo, Ndani ya gari alikuwepo Sheikh Jabu alieketi siti ya mbele, Mzee Kikoko, Mzee Kagomba na Mke wa Sheikh Jabu walikua wameketi katika siti tau za nyuma huku wakiwa wamewabeba Zani na Fani watoto wa Masu majira ya saa tisa lasiri tayari akina Kikoko walikua Tabora mjini, hakika dereva waliempata alikua vizuri katika usukani, hawakua na haja ya kupumzika wala kupitia popote ikabidi tu waunganishe kipalapala ili wakapumzike huko huko, saa kumi na moja kasoro walikua tayari wamewasili katika ardhi ya kipalapala, walipofika walipokelea kwa mbwembwe kubwa za kimila, walistaajabu jinsi walivyokuta uwanja umefurika watu, kundi la wakazi wa kipalapala walikua wamejaa wakiwa wote wamevalia mavazi maalum wayavaayo waswezi, walikua wamejifunga Khanga sehe ya juu kifuani na chini, huku wakiwa wamejipaka pemba katika nyuso zao, ngoma za waswezi zilikua zikipigwa huku baadhi ya vijana wakicheza kwa mbwembwe kwa ule mtindo wao wa kutingisha mabega,

Baada ya Akina Kikoko kuwasili wote walifikishwa mpaka mbele ya Mkuu wa Waswezi aliekua amejitanda shuka jeupe huku akiwa amejifunga kilemba chekundu, wote wakainama kumsalimia mkuu huyo ambae alikua ameshika Usinge kama ule ambao Masu alikabidhiwa na Marehemu Kishindo akausahau kwenye basi, Macho ya Kikoko yalikua hayatulii alikua haamini kila anachokiona mahala pale, Aliwaona wake zake wote wawili na watoto zake wadogo waliokua wamekwenda likizo huko kipalapala karibu mwezi sasa, hakujua ni mbinu gani aliyotumia Mama Masu ambae ni adui mkubwa wa ukoo huo mpaka wamekaa nae kwa wema vile hakujua kinachoendelea, pia alimuona Masu akiwa amekaa mbele kabisa karibu na Mkuu huyo wa Waswezi, na baadhi ya watu aliokua akiwafahamu
Ndipo sasa baada ya salamu ile kama vile waliokua wakisubiriwa ni wao tu, watu wote waliketi kwa utulivu ndipo sasa Mkuu wa Waswezi aliposimama na kuanza kuongea baada ya salama yao ya lugha ya Kinyamwezi
“Jamani tumekutana hapa kwa kazi kubwa tatu ama nne tu…” watu wote walikua kimya wakimsikiliza mkuu “..Kwanza ni Zindiko kubwa kwetu sote hapa ili kujiweka salama dhidi ya hila za Waufi na wachawi wote, pili leo tutamtawaza Masu cheo kikubwa sana kutoka na shida na dhahma alizopambana tumeamua kumpa mamlaka na nguvu kubwa sasa, pia Bibie alieuiba ujauzito wa Masu na kujipa u-mama wa lazima nae yupo hapa akiwa amekuja kuomba msamaha na kukiri kosa lake, pia Bwana Kishindo nae yupo hapa, hivyo kwa atakaesamehewa leo itakua ni bahati kwake na kwa atakae adhibiwe itakua ni balaa kwake..” Macho ya Kikoko yalimtoka Pima kusikia habari za kuadhibiwa akajua tu bila shaka kwa upuuzi alioufanya basi hatotoka salama, wakati huo mkuu alikua akiendelea kuongea kwa sauti kali lakini ya utlivu sana “… Lakini kabla ya yote hayo kwanza tutafanya mazishi ya heshima ya kumzika mpendwa wetu Nyamizi ambae aliuawa kwa kupigwa panga la kichwa na kijana mmoja mshenzi anaetumiwa na Waufi..” Maneno hayo sasa yalimshtua sana karibu kila aliekua akijua kua Nyamizi alikua hai, Ngaliba Kayoka alimuangalia Babu yake Masu kwa jicho la mshangao lakini Babu Masu alionekana kua naijua siri hiyo, baada ya ukimya kutawala kwa dakika chache ndipo Mkuu wa waswezi akaendelea
“..Baada ya Nyamizi kupigwa panga alifariki pale pale na mpaka wakati anafikishwa hospitali alikua ameshafariki lakini kwa Nguvu ya Waswezi tulikiinua kivuli chake kilichoendelea kuonekana kua kama yupo hai ili iwe ni sababu ya kuachiwa kwa wazee wenu waliokua wakituhumiwa kumuua, hakika huyo Hunudu alikua ametushinda vikali kama isingekua nguvu ya Waswezi, na baada ya kivuli cha Nyamizi kumaliza kazi husika pale Polisi sasa leo hatuna jinsi ni kumzika tu mpendwa na Shujaa wetu, Maiti yake iko ndani imeshaandaliwa kwa ajili ya amaziko, ila baada ya matukio yote haya kukamilika mwisho nitawatambulisha viongozi wa kilua kutoka Kgoma nao tumekua tukishirikiana nao kwa kariu sana kwenye vita hii, Baada ya maziko tutaanza mkakati wa mwisho wa kummaliza huyo Hunudu kivyovyote kabla jua halijachomoza kesho, Eeeh Mungu tusaidie, na Mizimu itusikie” Mkuu wa Waswezi akahitimisha kuongea na kuwaacha wote wakiwa midomo wazi
*****

Wakati hayo yakiendelea huko Kipala pala, Hunudu alikua njiani kwa kasi ya ajabu akielekea huko kwenda kummaliza Mama Masu na yeyote atakae kaa mbele yake, agizo hilo alipewa na wakuu wake, na akapewa Shart kua kama atashindwa basi Mzimu wao wa WAUFI Utawaangamiza wote

MWISHO.

TOA MAONI YAKO

CHANZO : BURE SERIES
 
Story kali sn mkuu lkn hitimisho lake halijajitosheleza. Hunudu hatujajua amepata adhabu gani na pia hatujajua hatima ya Mama Masu.
 
Habari mambo naitwa Mr Equator Nimeandika ujumbe huu kuku omba swala moja tu!
Mimi nimetengeza website ya ku share story ambayo ni EquatorStory
Je umekuwa ukipata tabu kupost story zako hapa?
Hili ndo suluhisho lako.
Mimi nataka nkupe nafasi ya kuwa mmoja wapo wa kwanza kutumia hii website
unda account yako na uweze kupost story yako mpya.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom