Kwanza kabisa, Mwombe Mungu kwa dhati kutoka moyoni akusamehe, na akupe nguvu za kushinda kishawishi. Ibilisi ni mjanja sana. Kakuingia bila wewe kujua, au kama ulijua umemruhusu aendelee kukutesa. Kumbuka kisa cha mfalme Daudi. Dhambi moja ya kumtamani shemeji yake, iliongoza kwenye madhara MAKUBWA, mpaka alimuua mume wa shemeji yake ili amchukue mkewe jumla!!!! Kama hujakisoma kisa hiki, nakushauri usome 2Samweli 11:2-27 na 2Samweli 12:1-25. Jifunze kutokana na yaliyomkuta mtumishi wa Mungu, na kutoka kwa watu wengine wa nyakati za sasa. Ukisoma NDANI ya BIBLIA, kwa kuwa ina roho takatifu ya Mungu, unaweza kupata nguvu isiyo ya kawaida, kushinda jaribu lako. Amini, utamaliza bucha, nyama ni ile ile.
Mambo muhimu niliyojifunza binafsi kutokana na kisa cha Daudi na Bethsheba ni haya:-
1. Alikuwa mahali pasipofaa kwa wakati ule. Vita ilikuwa ikiendelea. Hivyo kurandaranda bure, kulimfanya asiwe na jambo la maana la kufanya, ndio maana akajikuta anamtizama mwanamke anayeoga. Epuka kukaa kaa bure, unampa Ibilisi mianya ya kukuletea majaribu. Kuwa busy.
2. Daudi alipomwona Bethsheba akioga, aliendelea kumtizama, mpaka hamu ikampanda, kisha akaagiza aletwe kwake. Ukimwona mwanamke ambaye si mkeo, ukajisikia kumtamani au kumpenda, hilo ni jambo la kawaida kwa binadamu aliye kamili. Ila USIENDELEE KUMTAZAMA. Ukiendelea kumtizama, tamaa yako itapanda, akili yako itaigandamiza dhamiri yako na kuanza kuhalalisha kuwa naye, hatimaye utatenda kosa. Ndio maana Yesu Kristo alisema, amtizamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.
3. Daudi alipogundua kuwa Bethsheba amepata mimba kutoka kwake, aliamua kumwita Uria Mhiti, mume wa Bethsheba, arudi kutoka vitani, ili alale na Bethsheba, kabla mimba haijaonekana, baadaye ionekane mimba ni ya Uria. Dhambi moja, inazaa dhambi nyingine. Ibilisi anafanikiwa sana kuendelea kukuzamisha. Nawe unajifanya rafiki na mume wa hawara yako, ili kuficha madhambi yenu, hiyo ni hatari kubwa, na hatimaye itajulikana tu.
4. Uria aliporudi kutoka vitani, hakulala nyumbani kwake, badala yake alilala langoni pa Mfalme Daudi. Asubuhi Daudi alipomkuta alishangaa, akamuuliza kwanini hakwenda kupumzika kwake? Akasema, angelalaje wakati watu wamo vitani? Daudi akaona mbinu yake haijafanikiwa, akampeleka tena Vitani, kisha akaamuru awekwe mstari wa mbele, ili auawe, na ndivyo ilivyokuwa. Uria Mhiti akauawa vitani. Dhambi nyingine hiyo ya KUUA. Yote hii ni ili kuficha dhambi yake ya uzinzi. Hapo alishasahau kuwa Yehova Mungu hafichwi kitu. Kuna hatari ya wewe kuua au kuuawa, endapo utaendeleza mahusiano na huyo mwanamke, na itakapojulikana.
5. Daudi akaamua kumwoa Bethsheba baada ya mumewe kufa vitani. Mtoto waliyemzaa akafa. Uchungu mkubwa huo!!! Mtoto asiye na hatia yoyote akafa. Uzinzi wenu, utaleta madhara fulani, (madogo au makubwa au yote) kwa washiriki wa familia zenu, i.e. watoto, wazazi, ndugu na marafiki wasio na hatia yoyote.
6. Nabii wa Yehova alipomfunulia Daudi dhambi yake, alimwambia matata yasingeisha katika nyumba yake. Unajua nini kilichokuja kutokea baadaye? Watoto wa Daudi wa kiume waliamua kulala na wake za baba yao Daudi. Laana iliendelea kumla Daudi mbele ya macho yake. Nawe usipoacha kabisa uzinzi na mke wa mtu, laana yake itakutafuna kwa njia ambayo kwa sasa huijui. Tena unaweza kuipitisha laana hiyo mpaka kwa watoto wako na wajukuu na vitukuu.
TAFAKARI: JE, UKO TAYARI KWA YOTE HAYO? Naamini jibu ni LA! Na kama ni la, basi acha mara moja.
Kuhusu kufanya biashara na mumewe, kama hutafanya lolote na mkewe tena!!! mnaweza mkaendelea kibiashara, huku ukiishinda nafsi. LAKINI, ushauri wangu bora ukaachana tu na hiyo biashara ili usiendelee kumwona ona yule mke na kumtamani. Fanya kama vile alishakufa, hayupo. Msahau. Ni ngumu kwa binadamu, lakini KWA MUNGU YOTE YANAWEZEKANA.Baada ya kuacha, utapata amani ya akili na moyo, afya njema na dhamiri safi.
Kila la kheri. Bila shaka utarudisha matokeo hapa kwenye mtandao, kwa faida ya wengine.