Swahilian
JF-Expert Member
- Apr 28, 2009
- 591
- 66
NYERERE BABA
Alotabiri ya kesho, hatunaye nikwambie.
Mwalimu wetu kumbusho, habarize uzijue.
Nyerere namlilia, natamani anisikie.
Alimtoa mkoloni, bendera yetu angani.
Umoja nayo amani,katutoa ujingani.
Kabila kwetu utani, tukasifika barani.
Nyerere katupa lugha, nalonga bara na pwani.
Uongoziwe nchini, tawala bora nadhifu.
Nahodha huyu makini, mpingaji uhalifu.
Alojali masikini, kila kona wamsifu.
Nyerere Baba U wapi, itika nikusikie.
Ujamaa ulileta, azimio la Arusha.
Wote tujitegemee, mali wote kututosha.
Kwa pamoja twendelee, hakuna wa kukatisha.
Nyerere nifungulie, yapo mengi nikwambie.
Nimeona niandike,barua hii ifike.
Maisha yangu upweke. Nchi yote ni ya kwake.
Nakula yalo mapeke, nyama nzima ala peke.
Nyerere baba mwambie, wewe ndo akusikie.
Misingi ulotufunza, wachache wamegeuza.
Kunguni wanatufyonza, vitini wamejibanza.
Nchi yazidi kuoza, yatoka nayo mafunza.
Baba ulo taa yetu, nuru ya wanyonge wote.
Nyumbayo sasa kificho,wala bila wasiwasi.
Wajichana pochopocho, wapatiana nafasi.
Watuzika hali macho, kupunguza zetu gasi.
Nyerere Baba wa kweli, hukutenga waso mali.
Tamati yangu sikia, ni mengi ya kwongeya.
Kwanza msitari pigia, majibuyo nangojeya.
Suluhu pa kuanzia, kwani nazidi umiya.
Nyerere kwa nguvu zako, Taifa tukawa sawa.