Naibu Katibu Mkuu CUF aongea na Wandishi wa Habari

5525

JF-Expert Member
Apr 6, 2014
5,412
6,273
Naibu Katibu Mkuu wa CUF-Chama Cha Wananchi, Zanzibar, Mhe. Nassor Ahmed Mazrui, atakuwa Live na Mkutano na Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Ofisi ya Makao Makuu, Vuga, Mjini Unguja. Kupitia 102.9 SWAHIBA FM tutakuletea matangazo mubashara ya mkutano huo, kuanzia saa 5 kamili asubuhi, leo Jumatano, Machi 08, 2017.

Mikakati imekwenda sawasawa tumefanikiwa kuwavusha na kumvusha katika daraja kabla ya wakati wake (untimely).

Stay tuned and updated,

Aluta Continue.

Maharagande,



THE CIVIC UNITED FRONT

CUF-CHAMA CHA WANANCHI)





TAREHE: 08/03/2017



MKUTANO NA WAANDISHI WA HABARI

(PRESS CONFERENCE)



TAARIFA KWA WAANDISHI WA HABARI KUHUSU MUENDELEZO WA HUJUMA NA NJAMA ANAZOFANYA IBRAHIMU LIPUMBA NA WASHIRIKA WAKE DHIDI YA CHAMA CHA CUF NA VIONGOZI WAKE KWA KILE ALICHOKIITA KUTENGUA UTEUZI WA WAKURUGENZI NA MANAIBU WAKURUGENZI.



Ndugu Waandishi wa Habari,

(Assalamu aleykum)

Awali ya yote hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kutujaalia uhai na Afya njema tukaweza kukutana wakati huu kwa ajili ya kuzungumza nanyi. Niwashukuru kwa kuitikia wito wetu wa kuja kutusikiliza na kupitia kwenu kuzungumza na watanzania wote waliopo ndani na nje ya nchi yetu. Tuwashukuru kwa ushirikiano munaoendelea kukipa chama chetu cha CUF mara zote kwa kujulisha Wananchi kwa usahihi masuala mbalimbali yanayoendelea na hasa katika kipindi hichi ambacho kwa makusudi na dhamira ovu dhidi ya Chama. Msajili wa vyama vya siasa nchini Jaji Francis Mutungi ametupandikizia mgogoro usiokuwepo hapo kabla wa kulazimisha kutaka kutuchagulia viongozi wa Taasisi yetu kinyume na kazi, wajibu na majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258, iliyoanzisha uwepo wa Ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa nchini.

Ndugu Waandishi wa Habari,

Tarehe 4/3/2017 mimi binafsi na wenzangu ambao ni wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya Taifa tulipokea ujumbe mfupi (SMS) wenye maudhui yanayofanana katika simu zetu unaoeleza kuwa; Mheshimiwa Naibu Katibu Mkuu, Nassor Ahmed Mazrui, Muheshimiwa Salim Bimani- Mkurugenzi wa Habari na Uenezi na Mawasiliano na Umma. Mhe. Abdalla Bakar Hassan - Naibu Mkurugenzi wa fedha na Uchumi. Mhe. Omar Ali Shehe - Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Uchaguzi. Mhe. Pavu Juma Abdallah - Naibu Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu na Mhe. Yussuf Salim Hussein – Naibu Mkurugenzi wa Ulinzi na Mhe. Mahmud Mahinda – Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Vijana Taifa, Ujumbe huoukieleza kuwa na tunanukuu.



“Nimeagizwa na Mkt Taifa kuandaa kikao cha Kamati Tendaji Taifa. Kitakachofanyika tarehe 6/3/2017 ofisi kuu Buguruni saa 3.00 asbh….Katika kikao hicho Mkt atahudhuria ana maswala muhimu ya kuongea na wajumbe….Tafadhali unaombwa kuhudhuria bila ya kukosa….NMKB.. Magdalena Sakaya”mwisho wa kunukuu. Ujumbe huo tumeujibu kwa barua yenye Kumb Na. CUF/HQ/AKM/003/017/03 ya tarehe 5/3/2017 na kusainiwa na sisi sote na kuituma barua hiyo kwa njia ya email yasakayamagdalena@gmail.com Jumapili majira ya saa 4 usiku na nakala halisi za barua hiyo tumeituma Dar es Salaam Jana tarehe 6/3/2017 wakala wa mahakama (Court Broker) ameendelea na taratibu zake za kufikisha barua hiyo rasmi kwake. Nakala ya barua hiyo nimeiambatanisha na taarifa hii.



Jana tarehe 6/3/2017 Magdalena Sakaya na Lipumba wameshindwa kufanya kikao walichokiita cha Kamati ya Utendaji ya Taifa kwa kuwa hakukuwa na wajumbe halali waliohudhuria kikao hicho lakini pia hakukuwa na akidi iliyotimia hata ya hao wajumbe ‘Fake’ waliohudhuria. Badala yake na kwa kuwa alikuwa anajua anguko hilo alishafanya maandalizi ya kuwaita waandishi wa habari na kufanya mkutano ambao alitangaza kwa kile alichokiitaKUTENGUA UTEUZI WA WAKURUGENZI NA MANAIBU WAKURUGENZI WOTE KWA UPANDE WA ZANZIBAR kwa madai ya mamlaka aliyopewa na Katiba ya CUF pamoja na kutoonesha ni Ibara ipi hiyo ya Katiba iliyompa mamlaka hayo ya kutengua uteuzi wa Wakurugenzi na Manaibu Wakurugenzi ambao majina yao nimeyaorodhesha hapo juu.



Akieleza sababu za kufanya hivyo kuwa eti wameshindwa kuhudhuria kikao kilichoitishwa na Magdalena Sakaya kwa agizo lake. Lipumba anadai eti ameamua kufanya hivyo kwa kuwa Katibu Mkuu Maalim Seif Sharif Hamad hafiki Ofisi Kuu Buguruni ili ampe maelekezo ya ujenzi wa Chama na mipango ya kuimarisha Chama na kukabiliana na matatizo na Changamoto za Chama. Na kwamba alitaka kutoa muongozo kwa kikao hicho cha Kamati ya Utendaji ya Taifa juu ya mambo aliyoyaita muhimu ya kuandaa kama ajenda za kufikishwa kwenye Baraza Kuu. Mambo hayo ni pamoja na;



a) Utekelezaji wa Maamuzi ya Baraza Kuu baada ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa tarehe 25 October 2015 kufutwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar;



b) Tathmini ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani; (c) Mkakati wa Chama wa kukabiliana na hali ya kisiasa ya Zanzibar; (d) Tathmini ya Uchaguzi Mdogo wa madiwani katika kata 20 za Tanzania Bara; (e) Mpango Mkakati wa Ujenzi wa Chama Tanzania Bara; (f) Kupitia Bajeti ya Chama ya 2016/17 na maandalizi ya bajeti ya 2017/18.



Ndugu waandishi wa habari,



The Civic United Front (CUF –Chama Cha Wananchi) ikiwa ni Taasisi imara yenye maamuzi na misimamo isiyoyumba wala kuyumbishwa na yeyote awaye, ikiongozwa na Jemedari wa mapambano ya Kudai Mamlaka Kamili, Haki, Usawa na Neema kwa wote Maalim Seif Sharif Hamad, inapenda kutoa ufafanuzi wa masuala hayo na kuweka msimamo wake kama ifuatavyo;



1. Kama tulivyoeleza hapo juu ni kweli tulipokea ujumbe mfupi (SMS) kwenye simu zetu kutoka kwa Magdalena Sakaya tarehe 4/3/2017 majira ya saa 6 za usiku na tumemjibu kwa barua yenye maelezo yanayojitosheleza kwamba; “Hatukuona uhalali wa kikao hicho ulichotutaka tuhudhurie. Kikao hicho si halali kwa mujibu wa Katiba ya CUF Itakuwa ni haramu na makosa makubwa kwetu kuwajibika kwa mamlaka zisizo na mamlaka kisheria na ki Katiba. Kikao hicho ni BATILI Hatuwezi kuwa sehemu ya washiriki wa kutaka kukihujumu Chama chetu cha CUF na kwa mantiki hiyo,HATUTOHUDHURIA kikao hicho”.



2. Kwa mujibu wa Katiba ya CUF Ibara ya 84 (1) ikisomwa pamoja na Ibara ya 93 (1)(d) inaeleza kuwa; “Kutakuwa na Kamati ya Utendaji ya Taifa ambayo itakutana mara moja kwa kila miezi miwili. Isipokuwa kwamba ikitokea dharura Kamati hiyo inaweza kufanya kikao cha dharura wakati wowote ambao Mwenyekiti wa Kamati hiyo ataamuru hivyo.” Mwenye mamlaka ya KUAMURU kuitishwa kwa Kamati ya Utendaji ya Taifa ni Mwenyekiti wa kamati hiyo ambae ni Katibu Mkuu ambaye yupo Ofisini Makao makuu Mtendeni, Zanzibar na anaendelea na anatekeleza majukumu na wajibu wake kama Katiba inavyomtaka kufanya hivyo. Sote ni mashahidi kuwa hivi karibuni tarehe 24/2/2017 amekamilisha ziara ya kikazi ya ukaguzi na Uimarishaji wa Chama aliyoifanya katika wilaya zote za Unguja na Pemba.



3. Maalim Seif amepata mapokezi makubwa yenye hamasa na shauku, imani na mapenzi ya dhati ya wananchi juu yake. Maalim Seif ameweza kufungua ofisi mpya za matawi na majimbo, kumbi za mikutano, amezindua waratibu wa Chama zaidi ya 1600, amepokea wanachama wapya waliojiunga CUF, na kufanya vikao na viongozi wa kada mbalimbali za Chama. Kwa mara ya mwisho ameongoza kikao cha kawaida cha Kamati ya Utendaji ya Taifa kilifanyika tarehe 2/2/2017 katika ofisi ndogo ya Chama Vuga, Mjini Unguja.



4. Magdalena Sakaya amechukuliwa hatua za kinidhamu na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa katika kikao chake kilichofanyika tarehe 28/8/2016 katika Ofisi ya Makao Makuu ya Chama Vuga, Mjini-Unguja. Kikao hicho kilihudhuriwa na wajumbe 46 halali kati ya wajumbe wote 59.



Wajumbe walifikia maamuzi ya kumsimamisha uanachama. Maamuzi hayo ya kusimamishwa uanachama hakuridhika nayo na kwa mujibu wa Katiba ya CUF Ibara ya 108 (5) ameamua kukata Rufaa kwa Mkutano Mkuu wa Taifa kwa barua yake ya tareh 5/9/2016 na kupokelewa Ofisi kuu Buguruni Tarehe 11/9/2017. Ibara hiyo inaeleza “Mwanachama au kiongozi yeyote aliyeamua kukata Rufaa kwa jambo lolote lile, basi atafanya hivyo kwa ngazi iliyo juu ya kikao kilichotoa maamuzi ambayo hakuridhika nayo katika kipindi kisichozidi siku kumi na nne (14) tokea siku ulipotolewa uamuzi huo”. Kwa maamuzi hayo ya Baraza Kuu, Magdalena Sakaya si Naibu Katibu Mkuu wa CUF Tanzania Bara.



5. Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kwa mamlaka yake ya Kikatiba Ibara ya 97 (4) (kuhusu kusimamishwa/kufukuzwa uongozi Naibu Katibu Mkuu) ikisomwa pamoja na Ibara ya 105(1) (kuhusu kukaimu madaraka) imemteua Mheshimiwa Joran Lwehabura Bashange kuwa Kaimu Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara. Ibara hizo zinaeleza kama ifuatavyo; “Endapo Naibu Katibu Mkuu ataachishwa au kufukuzwa uongozi, basi Baraza Kuu la Uongozi la Taifa litamchagua mwanachama mwengine kujaza nafasi hiyo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii” Ibara ya 97(4)

“Pale ambapo mwanachama yeyote wa chama mwenye madaraka kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, kwa sababu yeyote ile, hawezi kutekeleza kazi zake kwa muda au amesimamishwa au kuvuliwa madaraka kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, mamlaka iliyo na uwezo wa uchaguzi au uteuzi wa nafasi hiyo inaweza kumteua mwanachama mwingine mwenye sifa zinazohitajika kukaimu madaraka hayo”. Ibara 105 (1)



6. Ibrahim Lipumba alijiuzulu nafasi ya uenyekiti wa Chama Taifa kwa matakwa yake mwenyewe binafsi. Alikataa katakata ushauri wa kutochukua maamuzi hayo. Baraza Kuu likaandaa ajenda na kuitisha Mkutano Mkuu Maalum/dharura wa Taifa uliofanyika katika Hotel ya Blue Pearl Tarehe 21/8/2016 na wajumbe 476 kati ya wajumbe 700 wa Mkutano huo waliohudhuria walikubali kujiuzulu kwake kama Ibara ya 117 (2) inavyoelekeza.



Kutokana na Lipumba kuvamia Mkutano Mkuu huo bila kualikwa, kusababisha vurugu na uharibifu wa mali, samani za Hotel na kukisababishia Chama hasara ya kiasi cha shilingi milioni 600 Baraza Kuu la Uongozi la Taifa katika kikao chake kilichofanyika tarehe 28/8/2016 kilifikia maamuzi ya kumsimamisha UANACHAMA Lipumba, na baadae Tarehe 24/9/2016 alifanya uvamizi wa Ofisi Kuu ya Chama Buguruni akiwa na kundi la wahuni na kufanya uharibifu wa mali na thamani pamoja na kuwajeruhi wanachama na walinzi wa Ofisi.



Kutokana na vitendo hivyo vya ukiukaji wa Katiba ya Chama, utovu wa nidhamu na kukiharibia chama taswira yake mbele ya jamii, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa katika kikao chake cha tarehe 27/9/2016 lilifikia maamuzi ya KUMFUKUZA UANACHAMA. Lipumba si Mwenyekiti wala mwanachama wa CUF. Hana mamlaka ya kuagiza kufanyika kwa kikao chochote kile cha chama, kuteua na au kutengua watendaji wa Chama.



7. Lipumba amekuwa msahaulifu sana. Katika taarifa yake ameeleza kuwa tangu tarehe 23/9/2016 amekuwa akitoa wito kwa Katibu Mkuu, Maalim Seif aende ofisini Buguruni ili ampe maelekezo ya Mipango ya ujenzi wa Chama. Lipumba amesahau kuwa wakati huo Katibu Mkuu alikuwa anaendelea na majukumu yake katika Ofisi hiyo ya Buguruni.



Lipumba na wahuni wenzake wamefanya uvamizi wa ofisi ya Chama Buguruni siku ya Jumamosi ya Tarehe 24 Septemba, 2016. Na Tangu wakati huo Chama kupitia Bodi ya Wadhamini ya CUF imefungua shauri la madai Namba 23/2016 mbele ya Mahakama Kuu ya Tanzania dhidi ya Msajili wa Vyama vya siasa nchini, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Lipumba na wenzake wengine 10 ili kupata tafsiri ya kisheria juu ya uhalali wa maamuzi ya Msajili wa Vyama vya siasa nchini Jaji Francis Mutungi kuingilia shughuli za utendaji wa Chama na maamuzi halali ya vikao vyake. Shauri bado linaendelea Mahakamani na limepangwa kutajwa tarehe 22/3/2017.



8. Tunashindwa kumuelewa Lipumba anaposema ameagiza eti kufanyika kwa kikao cha Kamati ya Utendaji ya Taifa kwa lengo la kuzungumzia ujenzi wa Chama na mipango ya kuimarisha Chama. Anataka kujua Utekelezaji wa Maamuzi ya Baraza Kuu baada ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa tarehe 25 Oktoba, 2015 kufutwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, Mkakati wa Chama wa kukabiliana na hali ya kisiasa ya Zanzibar, Kupitia Bajeti ya Chama ya 2016/17 na maandalizi ya bajeti ya 2017/18 Hili nalo linastaajabisha kwa sababu Lipumba si Mwanachama wa CUF, ameshafukuzwa UANACHAMA. Uwepo wake CUF mpaka sasa unatokana na njama na hila za Jaji Francis Mutungi, Msajili wa Vyama vya siasa nchini wa kutoheshimu sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa ofisi yake na Vyombo vya dola kumlinda kwa amri ya viongozi wa CCM.



Kiongozi gani wa CUF atakaye kuwa tayari kukaa meza moja na Lipumba kuzungumzia eti mipango ya ujenzi wa Chama hali ya kuwa Lipumba amekuwa swahiba mkubwa wa Viongozi wa CCM na serikali yake? Kila uchao haishi kufanya vikao vya siri na viongozi hao? Viongozi wa CCM Tanzania Bara na Viongozi wa CCM Zanzibar, nani atamwamini kibaraka Lipumba aliyekubali kutumiwa? Mkakati gani wa Chama wa kukabiliana na hali ya kisiasa Zanzibar unaoweza kujadiliana na kupanga na Lipumba hali ya kuwa tarehe 10 februari, 2017 alikuja Zanzibar kwa kificho na kukutana na Viongozi wa CCM kupanga kufanya haya anayoendelea kuyafanya sasa?



9. Tangu ajiuzulu Baraza Kuu la uongozi la Taifa limefanya vikao vyake vya kikatiba na kujadili masuala mbalimbali na limefikia maazimio ya msingi kwa mustakbali mwema wa CUF, Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Hatuna jambo jipya ambalo tunahitaji kuelekezwa kulijadili na au kulipanga kwa maelekezo ya Lipumba. Lipumba anazungumzia eti kupanga bajeti ya chama 2016/2017 na maandalizi ya bajeti ya chama ya mwaka 2017/18. Lipumba amechanganyikiwa? Baraza Kuu la Uongozi la Taifa limepanga Bajeti ya Chama katika vikao vyake vilivyofanyika mwaka jana 2016. Lipumba ameshirikiana na Jaji Francis Mutungi kuiba fedha za ruzuku ya chama kinyume na Katiba ya CUF na taratibu za Chama kiasi cha shilingi milioni 369.



Lipumba amegawana fedha hizo na washirika wake aidha wiki kadhaa zilizopita waliomba kupatiwa tena kiasi cha shilingi milioni 230 fedha za ruzuku za CUF kama walivyofanya awali. Hawakufanikiwa, wamekutana na vikwazo vilivyowekwa na Bodi ya Wadhamini ya CUF kutokana na wizi walioufanya awali kutoka kwa mamlaka za usimamizi wa fedha hizo serikalini. Je wakati huo hakuona umuhimu wa kuitisha Kikao cha kupanga bajeti ya chama kama yeye anadai ni Mwenyekiti Halali wa chama na ana nia njema na chama cha CUF?



10. Hata kama angekuwa ni Mwenyekiti Halali wa Chama Taifa, Lipumba hana mamlaka ya kuwachukulia hatua za kinidhamu watendaji wa Chama. katika dhana ya uwajibikaji na mizania ya utendaji haki, usawa na usimamizi bora(Check and Balance) na mgawanyo wa madaraka (Separation of Power)Mwenyekiti wa Chama amepewa mamlaka ya Kuteua watendaji kwa mujibu wa Ibara ya 90 (1) (f) inayoeleeza kuwa; “Atateua kutoka miongoni mwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa, Wajumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa, au wanachama wajasiri wa Chama, Wakurugenzi na Manaibu wakurugenzi wa Kurugenzi za Chama Kitaifa, Katibu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Taifa na Naibu Katibu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, baada ya kushauriana na Makamu Mwenyekiti, na kufikisha uteuzi wake huo mbele ya Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kwa kuthibitishwa. Ila ijulikane kuwa Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa na wanachama wajasiri wa Chama walioteuliwa kuwa Wakurugenzi/Manaibu Wakurugenzi, Katibu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama na Naibu Katibu wa Ulinzi na Usalama ambao hawakuwa wajumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kabla ya kuteuliwa kushika nyadhifa hizo watasita kuwa Wajumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa mara tu baada ya kusita kushika nyadhifa hizo.”



Hakuna Ibara yeyote ya Katiba ya CUF inayompa mamlaka kuwatengua Wakurugenzi na Manaibu Wakurugenzi na Viongozi wengine wa Chama. Ibara ya 85 (11) (kuhusu Wajibu wa Kamati ya Utendaji ya Taifa) “Kumsimamisha kazi Mkurugenzi na Naibu Mkurugenzi kwa utovu wa nidhamu au kushindwa kazi na kulitaarifu Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kwa uamuzi wa mwisho” Baraza Kuu la CUF ndio muhimili wa usimamizi wa shughuli za Chama



Ibara ya 113 (1) (imeeleza kuhusu masharti ya kuchaguliwa na kipindi cha uongozi)



“Isipokuwa pale ambapo Katiba hii imeeleza vinginevyo masharti ya kuchaguliwa kwa kiongozi na kipindi cha uongozi kitakuwa kama hivi:- “Kipindi cha uongozi wa chama kitakuwa miaka mitano (5) kwa ngazi zote isipokuwa kama kiongozi huyo ameshindwa kazi aliyopewa” Kama kumetokezea suala lolote lile la kinidhamu na maadili lilipaswa kupita katika mkondo huu wa kiKatiba. Lipumba amekurupuka. CUF ni taasisi Imara sio kikundi cha wahuni kama Lipumba na genge lake wanavyojidhihirisha. Lazima utaratibu wa kikatiba ulipaswa kuzingatiwa pale ambapo kama angekuwa na mamlaka halali ya kufanya alivyofanya. Pindi panapotokea utovu wa nidhamu na ukiukwaji wa maadili ya uongozi Katiba ya Chama imeweka kamati maalumu ya kushughulikia Nidhamu na Maadili. Kamati hiyo inaongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Chama. Ibara ya 92 (c), 99 (1) (2) na 100 (1) (2) (3) (4) (Ibara na vifungu hivi vinazungumzia Kamati ya Maadili na Nidhamu, Wajumbe wa Kamati na majukumu yake)



Lengo la kunukuu maelezo haya ya Katiba ni kuonyesha kuwa Wakurugenzi na Manaibu Wakurugenzi na Katibu Mtendaji wa JUVICUF aliodai Lipumba kuwatengua hawajashindwa kutekeleza majukumu yao, Watendaji hao wote wamekuwa mstari wa mbele katika mapambano ya kukiletea ushindi chama chetu katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 Oktoba 25, 2015 na kupelekea kuwagaragaza vibaya CCM kwa kura nyingi na Maalim Seif Sharif Hamad Kushinda nafasi ya Urais wa Zanzibar. Lipumba hana msingi wa uhalali wa maamuzi yake (Basis of Justification) zaidi ya chuki, kutumika, na ukibaraka wa kutaka kurudisha nyuma juhudi za kuwaletea Wazanzibar na Watanzania kwa ujumla Mamlaka Kamili, Haki, Usawa Na Neema kwa Wote. Watendaji hawa wanalindwa na Katiba ya Chama na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.



11. Kutokana na Makamu Mwenyekiti wa CUF Mhe. Juma Duni Haji kujiuzulu mwaka 2015 kwa madhumuni ya kujenga nguvu ya pamoja ndani ya UKAWA na kuchaguliwa kuwa mgombea mwenza wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ikizingatiwa maslahi mapana ya kitaifa, hakika huo ulikuwa mkakati na maamuzi sahihi (Executive and Strategic Decision) ambao mpaka sasa CUF na viongozi wake wote makini wanauheshimu uamuzi huo. CUF inaongozwa na Kamati ya Uongozi Taifa iliyoundwa na Baraza Kuu la Uongozi Taifa kwa mujibu wa Katiba ya CUF Ibara ya 101 (1) (kuhusu Baraza Kuu la uongozi la Taifa Kuanzisha Kamati/ Taasisi za Kitaifa) “Baraza Kuu la Uongozi la Taifa linaweza, pindi likiona inafaa kuanzisha Kamati, Tume au Taasisi yoyote ile ya Kitaifa yenye lengo la kusaidia utekelezaji mzuri wa sera na itikadi za Chama, au kufanya uchunguzi juu ya jambo lolote lile linalohitaji kufanyiwa uchunguzi”.



Kamati hiyo ya Uongozi Taifa inaongozwa wajumbe watatu (3) na Mwenyekiti wake Mhe. Julius Mtatiro, Saverina Mwijage (MB), na Katani Ahmed Katani (MB)



Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya Taifa wanaotambuliwa na kuthibitishwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la Chama ni



1. Maalim Seif Sharif Hamad -Mwenyekiti

2. Joran Lwehabura Bashange -Kaimu Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara na Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi

3. Nassor Ahmed Mazrui -Naibu Katibu Mkuu-Zanzibar Zanzibar

4. Abdallah Khamis - Naibu Mkurugenzi wa fedha na Uchumi

5. Mustafa Wandwi -Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama

6. Yussuf Salim - Naibu Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama.

7. Umar Ali Sheikh - Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Uchaguzi

8. Shaweji Mketo - Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Uchaguzi

9. Ismail Jussa Ladhu -Mkurugenzi wa mambo ya nje na Mahusiano ya Kimataifa.

10. Abdallah Mtolea - Naibu Mkurugenzi wa mambo ya nje na mahusiano ya Kimataifa

11. Salim Bimani - Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma.

12. Mbarala Maharagande - Kaimu Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma.

13. Kulthum Mchuchuri -Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu.

14. Pavu Abdallah - Naibu Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu.

15. Mahmoud Ali Mahinda, Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Vijana Taifa-JUVICUF

16. Fatuma Kalembo- Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Wanawake Taifa-JUKECUF

17. Na Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Wazee wa Taifa -CUF-JUZECUF



Mwisho:



Tunawata wanachama, wapenzi wa CUF na viongozi wetu wote kutokuwa na wasiwasi wowote kwa kadhia hii inayoendelea kufanywa na vibaraka wa CCM. Tembeeni kifua mbele macho mita mia moja kwa kujiamini kabisa. CUF ni taasisi imara yenye viongozi makini. Katiba ya CUF inatambua kuwepo kwa Kamati ya Utendaji ya Taifa Moja pekee na wajumbe wake ni hao tuliowataja hapa. Hakuna na wala hakutakuwa na Kamati ya Utendaji nyingine. Baraza Kuu la Uongozi la Taifa lipo na limeendelea kukutana kama kawaida. Bodi ya Wadhamini ya CUF ipo na imefanya maamuzi mengi muhimu na ya msingi kukilinda Chama chini ya Mwenyekiti wake Mhe.Abdallah Khatau na hivi karibuni ndio imeamuru kufungwa kwa akaunti zote za CUF ili zisiendelee kutumiwa na Lipumba na genge lake kufanya uhalifu wa kuiba fedha za Chama za Ruzuku.



Tunatoa pongezi kubwa kwa wanachama na viongozi wetu wa Mkoani Tanga kwa kumkataa na kumpuuza Lipumba na wenzake waliokwenda mkoani humo kwa ziara ya kutaka kukivuruga Chama. Bodi ya Wadhamini ya CUF imefungua kesi ya madai kuwazuia kutekeleza majukumu ya Chama wale wote waliochukuliwa hatua za kinidhamu na Chama na waliopewa nafasi za uongozi na mtu asiyekuwa na mamlaka hayo katika mahakama ya Kisutu Dar es Salaam na leo baadae tutawajulisha maamuzi ya maombi hayo yaliyowasilishwa mahakamani hapo. Itakumbukwa kuwa CUF imevuka vigingi vizito katika nyakati tofauti kila ilipojaribiwa ikiwa kwa uadui wa ndani au wa nje. Na kwa ithibati, dhati na imani kubwa ni kwamba mwisho wa vitimbi hivi vyote, CUF itaibuka mshindi. Tunatoa wito kwa wanachama, wapenzi wa CUF, na watanzania wote kwa ujumla wapenda mabadiliko, waendelee kuwa na Subira na kila mmoja atekeleze wajibu wake kikamilifu katika eneo lake.



Ahsanteni kwa kunisikiliza.

HAKI SAWA KWA WOTE



NASSOR AHMED MAZRUI

NAIBU KATIBU MKUU-ZANZIBAR



IMETOLEWA LEO TAREHE 8/3/2017
 
SASA HATA. AKIONGEA NA WAANDISHI. WA HABARI SISI ITATUSAIDIA. NINI.

WAO SI WALIJIFANYA KUSUSIA UCHAGUZI WA MARUDIO LEO WANATAKA KUTUAMBIA NINI ????.

HAWA WATU STAKI HATA KUWASIKIA WALA KUWAONA ""CUF WAMEIFANYA KAMA KITEGA UCHUMI. CHAO
 
kwikwikwi naona umeamua kujitoa ufahamu?
we ndiye unayejitoa ufahamu huku ukijua ukweli....hivi unajua chimbuko LA cuf...unajua kwa nini Zanzibar INA nguvu kuliko hapa? Mkiwa hapo Lumumba muwe mnajaribu Mara moja moja kutumia akili zenu si kila kitu uambiwe cha kufanya...
 
we ndiye unayejitoa ufahamu huku ukijua ukweli....hivi unajua chimbuko LA cuf...unajua kwa nini Zanzibar INA nguvu kuliko hapa? Mkiwa hapo Lumumba muwe mnajaribu Mara moja moja kutumia akili zenu si kila kitu uambiwe cha kufanya...
nchi inakustikia kwa ujuha huu
 
Hivi cuf mliomuokota wapi Lipumba , mbona ukimuangalia tu unajua ni mchumia tumbo ?
 
Back
Top Bottom