Mwenye Mawazo ya Kuleta Amani Aje-SMZ

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,319
33,125



30 01 2010 SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imesema kama yupo mtu anahisi anayo njia sahihi zadi ya kuleta amani na umoja visiwani Zanzibar serikali inamkaribisha mtu huyo kufanya hivyo na suala lake litapokewa na kufikiriwa.
Hayo yameelezwa na Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha katika hutuba yake ya kufunga mkutano wa 18 wa baraza la wawakilishi uliochukua takriban wiki mbili Maisara Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Hata hivyo Nahodha alisema wapo baadhi ya watu walitilia shaka maridhiano hayo lakini mwisho wa yote wamekubaliana kwamba jambo la msingi linalotafutwa na kurejesha hali ya amani na utulivu wa wananchi wote bila ya ubaguzi.
“Najua wapo watu watakaotilia shaka jambo hili lakini mwisho wake sote tukubaliane kuwa maridhiano ya kutafuta amani ni jambo jema. Na kama yupo mtu anahisi anayo njia sahihi zaidi ya kuleta amani na umoja basi anaweza kuipendekeza na sisi tutaitafakari safari yetu ni moja lakini njia za kutufikisha tunakokwenda zinaweza kuwa ni nyingi” alisema Nahodha.
Aidha aliwashukuru viongozi wawili walioafikiana katika kuivusha Zanzibar katika hatari ambao ni Rais Amani Karume na Maalim Seif na kuwarejesha wananchi katika matumaini mazuri ya kuweza kuishi kwa amani hivi sasa.
“Hapana shaka yoyote kuwasilishwa kwa hoja hii barazani hapa kunafungua mwanga wa matumaini katika kuijenga Zanzibar mpya, hili ni tukio la kihistoria ambalo hatupaswi kulisahau katika maisha yetu.” alisema Nahodha.
Amewahakikishia wananchi wote kwamba yupo tayari kutoa msaada wowote kuhusiana na suala la kudumisha amani na kama mtendaji mkuu wa serikali atahakikisha mambo ya msingi yote yaliyokubaliwa katika muundo wa serikali ya umoja wa kitaifa yanatekelezwa na kuwa tayari kutoa kila aina ya msaada kufanikisha dhamira hiyo vyema.
Alisema suala la kuleta maridhiano na kuwasilishwa kwa hoja binafsi katika baraza la wawakilishi ni jambo kubwa ambalo linapaswa kuungwa mkono kwa kuwa dhamira yake ni kuwaweka wazanzibari katika hali ya amani na maridhiano.
Nahodha alisema makubaliano yaliyofikiwa na wajumbe wa baraza la wawakilishi ya kupitisha muundo wa mfumo wa serikali ya umoja wa kitaifa yawe ndiyo safari ya moja kwa moja ya kuwafikisha wazanzibari katika amani na sio kurudi nyuma walipotoka kwani wananchi wamechoshwa na matatizo yasiokwisha ambayo mengi yake yanachangiwa na kauli za wanasiasa.
“Mimi Shamsi Vuai Nahodha nikiwa ndani ya serikali au nje ya serikali nitasaidia kiongozi yoyote atakayekuwa na dhamira ya kutuongoza kudumisha amani na utulivu na umoja nitafanya hivyo kwa sababu naamini umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu” alisisitiza Nahodha.
Alisema hivi sasa Zanzibar imo katika amani kutokana na maridhiano yalioafikiwa na viongozi wakuu wa nchi ambao imani na mapenzi yao ya Zanzibar wameamua kukubaliana kuacha siasa zilizopita na kufungua ukurasa mpya wa kuendesha siasa safi na kuendeshwa kwa njia za kistaarabu.
“Hapana shaka hali ya utulivu tunayoishuhudia sasa ni matokeo ya maridhiano yalioafikiwa kati ya rais Karume na Maalim Seif. Namshukuru sana rais Karume kwa kuchukua hatua alizozichukua. Kiongozi yoyote makini anayewapenda na kuwajali watu wake atafanya kama alivyofanya rais Karume” alisema Nahodha.
Nafasi ya kuleta maridhiano Zanzibar ilikuwa ikitafutwa kwa miongo kadhaa lakini sasa kumeleta faraja kubwa baada ya viongozi wawili kukaa pamoja na kutaka kujenga Zanzibar mpya yenye amani na maridhiano.
Nahodha alisema matatizo ya kisiasa Zanzibar ni ya muda mrefu na wapo baadhi ya ya wanafalsafa wa kiafrika waliowahi kutamka kwamba Zanzibar ina matatizo ya kisiasa ingawa kwa wakati huo ulikuwa mgumu mtu kuweza kuthubutu kusema ingawa ndio ukweli wenyewe kwani yapo baadhi ya mambo hata kama yapo lakini mtu anafanya kutokuyaona au kukataa kusema kama kuna tatizo.
Akiwataja wanafasafa hao wa kiafrika ni pamoja na Mwalimu Julisu Nyerere ambaye aliwahi kusema suala hilo mwaka 1995 baada ya uchaguzi na kuthibitishwa kwa matokeo ya uchaguzi huo alithubutu kusema kwamba ipo haja ya Zanzibar kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa.
Mwengine aliyemtaja ni rais Abeid Amani Karume amabye wakati anaingia katika kipindi chake cha kwanza cha urais mwaka 2000 alitamani sana kuijenga Zanzibar mpya ambayo ingewashirikisha wananchi wote wa Unguja na Pemba akiamini wazanzibari wote ni ndugu.
Mwanafalsafa mwengine aliyemtaja Nahodha ni rais Benjamin Mkapa mwaka mnamo mwaka wa 2003 alisema hadharani kwamba ananyimwa usingizi na matatizo yaliopo Zanzibar ambayo kwa miaka kadhaa yamekuwa yakiitafuta Tanzania na kuisababishia matatizo ya kiuchumi na kuiwacha nyuma Zanzibar kimaendeleo.
Aidha alimtaja rais Kikwete ni miongoni mwa watu waliotamka kwamba Zanzibar kuna mpasuko wa kisiasa mwaka 2005 wakati akiingia madarakani kwa mara ya kwanza ambapo alisema atatumia juhudi kubwa katika kushughulikia suala hilo la kisiasa ambalo limeathiri sekta ya uchumi wa Zanzibar.
Nahodha alimtaja mwafalsafa wa mwisho wa kiafrika ni Mwakilishi wa jimbo la Chambani (CUF) Abass Juma Mhunzi ambaye mwaka jana wa 2009 alitamka katika kikao cha baraza la waakilishi kwamba misimamo ya kisiasa inafaa kupunguzwa ili kuinusuru Zanzibar na akasema suala la kutomtambua rais Karume ni mbwembwe za kisiasa tu.
Nahodha alionesha maneno yaliotamkwa na viongozi mbali mbali ni ushahidid tosha kwamba Zanzibar ilikuwa inaelekea pabaya katika mustakabali wa kisiasa, kiuchumina kijamii hivyo alisema suala la kurudi tena nyuma si jambo la usara na kuwataka viongozi na wananchi kusaidia katika kulimaliza suala hili ili wazanzibari waweze kuishi kwa amani zaidi.
Alisema wananchi wa kawaida hawana matatizo yoyote juu ya kuwepo hali ya amani lakini viongozi wa kisiasa ndio wenye matatizo makubwa na wenye kuwachochea kutokana na kauli zao wanazozitoa majukwaani na katika vyama vyao.
Hata hivyo aliwataka viongozi hao wa kisiasa kuachana na lugha mbaya na za uchochezi katika kipindi hiki muhimu cha kuelekea katika maridhiano ya kuijenga upya Zanzibar iliyogawanyika kwa miaka kadhaa kati ya Unguja na Pemba.
“Viongozi wa vyama vya siasa waondokane na kauli za uchochezi ili watu wasirejee kule walipotoka ambapo wananchi waliishi kwa chuki na hasama na kushindwa kusaidiana hali ya kuwa ni ndugu na majirani katika mitaa yao” alisema Nahodha.
Akitoa mfano Nahidha alisema Zanzibar ni kama jahazi kubwa ambalo limejaa mizigo na iwapo litachezewa na ndani yake kuna watu bila ya shaka watu wote watazama baharini na iwapo ikifanywa kinyume chake watu hao watavuka salama ngambo ya pili bla a matatizo yoyote.
Juzi wajumbe wa baraza la wawakilishi wote kwa sauti moja walikubaliana kupitisha hoja binafsi iliyowasilishwa na kiongozi wa kambi ya upinzani Abubakar Khamis Bakari inayotaka kufanyiwa marekebisho ya katiba ili kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa visiwani Zanzibar.
Wajumbe hao wote kwa umoja wao bla ya kujali itikadi za vyama vyao walikubaliana kwamba suala la ridhaa na wananchi kwa kuitishwa kura ya maoni ni muhimu kabla ya kuingia katika uundwaji huo kwa kuwa suala la maoni ni muhimu hasa katika jambo zito kama hilo ambalo litapelekea kuwepo kwa mabadiliko ya katiba ya Zanzibar.
 
Watu wamekula kuku na wakati umefika wa kuachia madaraka wameanzisha maridhiano/muafaka. Upinzani visiwani wamechanganyikiwa?

¬K
 
Back
Top Bottom