Msikiti mkubwa unaojengwa Dodoma kwa hisani na ufadhili wa rais wa Libya kanali Muhammar Gaddaf uliopo karibu kabisa na uwanja wa mpira wa Jamhuri jana ulishika moto na kusababisha umati mkubwa wa watu kukusanyika karibu na msikiti huo.Tukio hilo lilitokea majira ya saa moja usiku mara baada ya watu waliokuwa wakipita karibu na eneo hilo kuona moshi mkubwa uliotanda katika moja ya kilele cha msikiti huo.Moto huo ulidhibitiwa na kikosi cha zimamoto kilichowasili hapo mnamo saa moja na robo na kufanikiwa kuuzima kabisa majira ya saa mbili na nusu usiku.Kwa mujibu wa watu waliokuwepo hapo,chanzo cha moto huo ni baadhi ya mafundi kuwafukuza nyuki waliokuwa wameweka kambi hapo kileleni majira ya saa nane mchana kwa kutumia majani yaliyowashwa moto na baada ya kufanikiwa kuwatimua hao nyuki walisahau baadhi ya cheche za moto hapo kileleni.Kutokana na hali ya upepo unaovuma kwa kasi Dodoma,cheche hizo zilijikusanya taratibu kuanzia majira ya mchana hadi usiku na kuwa moto kamili.Kwakweli pongezi kubwa zinawaendea wafanyakazi wa kikosi cha zimamoto kwa jinsi walivyojitolea kukabiliana na janga hilo.