Mshipa wa aibu kwa CCM umekatika

Mzalendo80

JF-Expert Member
Oct 30, 2010
2,508
1,338
KUENDELEA kubaki kuwa mwanachama au mpenzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kama ni kwa bahati mbaya inakubalika, kama ni kwa kujua, basi wewe ni wakala wa kutuangamiza sisi Watanzania. Iwapo kama kauli hiyo inakuudhi funika gazeti acha kusoma.Tutafakari machache yaliyojitokeza muda mfupi tangu wakati wa uchaguzi mkuu, na yaliyojirudia katika uchaguzi mdogo wa Igunga unaofanyika leo.


Watanzania katika Uchaguzi Mkuu uliopita tuliahidiwa ahadi nyingi ngumu ambazo hazitekelezeki. Tulidanganywa kweli tukakubali. Imekuwa ni bahati mbaya, tulidanganywa ovyo na CCM, tukachagua viongozi wanaoonekana kuwa ni ovyo wa CCM, na sasa wanatuongoza ovyo hadi muda huu sisi tunalalamika ovyo. Je, nini hatima yake?


Hatuhitaji mwekezaji katika vichwa vyetu kuelewa janga linalofika sasa kwa Watanzania kwa kuongozwa na CCM. Tuliahidiwa ujenzi wa reli mpya kutoka mkoa wa Dar es Salaam hadi Kanda ya Ziwa, Rais Jakaya Kikwete akaahidi tena kujenga barabara za juu kuepusha msongamano, akaahidi kujenga machinga complex mbili katika kila wilaya katika Mkoa wa Dar es Salaam, akatudanganya tena kuwa atajenga hospitali kila jimbo, huku akiahidi kuwa tatizo la maji nchini litakuwa historia.


Bahati mbaya ahadi hizo alitoa hata Geita na Nyamongo ambapo tangu atoe ahadi wananchi wa kule bado wanakunywa maji yenye sumu za migodini. Hapa kulikuwa na aibu katika kudanganya kweli? Aibu haikuwepo ili aweze kutamka vizuri tena kinagaubaga.
CCM na viongozi wake wanaweza kufanya kitu, au wakaahidi kitu ambacho hata kama mtu hujaenda shule sana ukisikia, unatamani kuwatafuta uwakalishe chini uwafundishe. Tutaacha lini kuamini kuwa CCM na viongozi wake ni waongo kupita kiasi ili tujikomboe kwa manufaa ya nchi yetu?


Tunaadhimisha miaka 50 tangu tumepata Uhuru, serikali inaahidi uongo hakuna utekelezaji. Serikali ya CCM imekaa kuhudumia wezi, wasio na tija kwa Taifa. Serikali isiyo na msimamo. Serikali ya CCM inaahidi kujenga reli kutoka Dar hadi Kanda ya Ziwa, au kujenga hospitali kila jimbo, au kujenga Machinga Complex mbili Dar, yatatekelezwaje na hiyo serikali? Ni hii ya CCM ya Tanzania au kuna CCM nyingine nchi jirani? Serikali imeshindwa kudhibiti wafanyabiashara wa sukari, itawezaje kufanyia kazi ahadi kubwa hizi?


Serikali isiyo na aibu, inayowaambia Watanzania tunasherehekea miaka 50, huku haina hata ndege moja, Shirika la Ndege la ATCL lina ndege moja tu tena ya kukodi. Tumepitwa hata na timu ya mpira ya TP Mazembe ambayo ina ndege mbili sisi hatuna ndege, tunajisifu nini? Kuna haja ya kuendelea kuongozwa na serikali ya kisanii hivi hadi lini?


Timu imeshinda Taifa linalokusanya kodi lenye watu zaidi ya milioni 36, timu imenunua ndege tena mbili si moja, sisi tunafanya usanii kuchekacheka na maisha ya Watanzania, bado na sisi tunaochekwa na hawa tunafurahi, kwanini tunajiangamiza maisha yetu kwa kuwaamini CCM na viongozi wake? Serikali ya CCM imeshindwa kudhibiti bei ya sukari, itawezaje kupata fedha ya kununua ndege kwa ajili ya shirika lake? Tulinganishe hapa, TP Mazembe na Serikali ya Tanzania, nani ana mapato zaidi? Kati ya TP Mazembe na Nchi ya Tanzania, nani ana umri mkubwa? Kwanini TP Mazembe ina ndege mbili za kununua sisi tuna ndege moja ya kukodi? Hivi hapa tunahitaji mwekezaji kujua kuwa tunaongozwa na serikali ya wachumia tumbo wasiojali maisha ya Watanzania?


Serikali ya CCM inaweza kudanganya Watanzania kwa lolote, bahati mbaya na viongozi wake, tena wale ambao tunadhani wanajiheshimu bila kujua kuwa sisi tunawaheshimu au hata kama hatuwaheshimu, viongozi hao wa CCM hujitokeza mbele yetu kutetea uovu huo, kwanini CCM wanatudharau hivi? Hivi Viongozi wa CCM mmepoteza wapi mishipa ya aibu?


Tuchukulie mambo mawili ya msingi yaliyotengenezwa na CCM Igunga katika kampeni ambazo uchaguzi wake ni huu wa leo, Tukianzia na Suala la DC. Fatuma Kimario, hivi alienda kufanya nini kwenye mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA)? Kama alienda kufanya mambo mazuri kwanini alienda mwenyewe bila ulinzi wa polisi, kama alienda kuzungumzia mambo ya maendeleo kwanini alienda bila mkurugenzi, kutokana na ajenda alizokutwa nazo eti mambo ya mifugo na mambo ya elimu.


Aliendaje huko bila kuwa na ofisa wa Kilimo na Mifugo au ofisa Elimu? Ilikuwaje vijana wa CCM, Nape Nnauye na Januari Makamba wakaanza kutulelea kichefuchefu kuhadaa Watanzania eti DC alikuwa katika kazi rasmi? Hivi hatujui? Hivi CCM huwa hamuoni aibu? Mnatetea kila kitu bila kufanya utafiti. Mmewaingiza mkenge baadhi ya Waislamu, mkawatengenezea matamko ovyo, yasiyoweza kuvumilika katika taifa, mkawalisha upuuzi sasa mmewaacha hoi.


Kutokana na ghiliba za CCM, sasa baadhi ya wazee wa Kiislamu wakasema uongo. Wakaita ushungi kuwa hijabu, wakatofautiana wao kwa wao katika mkutano. Hivi CCM mnafikiri Watanzania hawajui hijabu? Kama hiyo haikutosha CCM mkatengeneza tamko eti CHADEMA ni adui wa Uislamu, je, CCM mtapata lini aibu ili mseme ukweli muache kupandikiza upuuzi katika jamii?.


Katibu Mkuu wa CCM Wilson Mukama na Umri wote, ambao vijana wa Tanzania tunapaswa kumheshimu, akakurupuka kutengeneza hoja dhaifu ambayo hata chekechea wasingeitengeneza. Anazungumzia nyumba kuungua halafu karatasi iliyobaki imeandikwa ‘CHADEMA wajanja’. Ni wapi aliwahi katika umri wake kuona nyumba inaungua yote na kuku halafu ikabaki karatasi.


CCM hivi kweli tangu vijana hadi wazee hizi ndizo fikra zenu? Na hivi ni kweli uwezo wenu wa kufikiri ndio mwisho hapo? Mukama bila aibu unatembelea banda la kuku unahadaaa Watanzania kuwa ni nyumba imechomwa, nyumba gani huungua hakuna hata jirani anayeenda kuamshwa hadi Katibu Mkuu wa CCM aitwe kuja kupigwa picha hapo? CCM hii ni aibu jamani.


Hivi kweli ilihitajika mwekezaji kujua kuwa hii mbinu ni ya hali ya chini zaidi kuliko zote? Ubunifu gani huu? Kama kweli ubunifu wenu ndio unarudia katika mambo ya hali ya chini hivi, mtalala wapi siku hiyo? Hakika Mungu awabadilishe muanze ubunifu wa mawazo ya kimaendeleo, Unadhani kwa akili hizi tunaweza kumiliki ndege?


Unadhani kwa akili hizi wataacha kutetea mafisadi? Unadhani kwa akili hizi wataacha kutudanganya waibe hela zetu wadanganye wanalipa Dowans? Uamuzi ni wenu Watanzania. Muda uliopo bado unatosha sisi kunyonywa hadi aibu yao iishe. Lakini kwa hali ilivyo, sitegemei mabadiliko. Tujue tumeliwa.


Hali hii inakatisha tamaa kwa wakati ujao na kutoa matumaini wakati uliopita hasa hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alipokuwepo. CCM wamethubutu kutudanganya, wamefanikiwa kutudanganya, na wanasonga mbele kutunyonya na kutuhadaa kwa nguvu. Nini hatima ya Tanzania na uongozi wa CCM? CCM hawana aibu, mshipa huo umepotea, kama upo basi umekatika.

Source: Tanzania Daima - Sauti ya Watu
 
Mkuu mi nimeshaamka...muda mrefu sana...ILAANIWE CCM WALAANIWE VIONGOZI WOTE WA CCM...
Na huko tuendako lazima kieleweke tumechoka kudangwanywa..
 
Mkuu wote tuna uchungu lakini huu uchungu wako unaelekea kufikia the point of no ruturn. Ni kama uchungu wako umefikia escape velocity
 
Wadau matokeo yameshaanza kutangazwa huko Igunga kwa baadhi ya Kata , Chadema kwa mjini tunaongoza ila kwa difference ndogo wasi wasi wangu ni kule Vijijini CCM B QUESTN,

Mungu Ibariki Tanzania na Ibariki Chadema , Magamba wapotelee mbali
 
KUENDELEA kubaki kuwa mwanachama au mpenzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kama ni kwa bahati mbaya inakubalika, kama ni kwa kujua, basi wewe ni wakala wa kutuangamiza sisi Watanzania. Iwapo kama kauli hiyo inakuudhi funika gazeti acha kusoma.Tutafakari machache yaliyojitokeza muda mfupi tangu wakati wa uchaguzi mkuu, na yaliyojirudia katika uchaguzi mdogo wa Igunga

...unaongea sana but mi n tunaona hizo sera za kichichiem tu,swala hilo tunajua.tuambie tufaye nn
 
Mungu haja lala tushikamane kuubadlisha umma wa watanzania hasa kwa elimu ya uraia na jinsi mfumo wa serikali unavyofanya kazi ama unavyoendeshwa,leo hii kuna watu hasa vijijini wanachukua vyama ni kama timu za mpira au kwa kule mikoa ya kanda ya ziwa hasa shinyanga na mwanza wanachukulia ni kama ngoma ambako kuna bagalu na bagika ambao ndio wapinzania wakubwa,hivyo basi ni vigumu kwa mfuasi wa ngoma fulani kuhama na kuacha upande wake,kwani mara nyingi huwa inatokana na generation ya nyuma sanammababu na mabibi wa enzi hizo,basi baadhi ya watanzania wanachukulia usimba na yanga kwenye masuala ya maisha.siasa si entertainment,ngoma na mpira ni entertainment kwa sisi washabiki au wanachama.
Kikubwa ni kuunganisha nguvu zetu na kila mmoja kuwa na wajibu wa kutoa kile alichonacho au elimu aliyo nayo itakayosaidia kuibadli jamii ambayo kwayo iinachukua ushabiki wa mpira au ushabiki wa ngoma katika masuala ya siasa.
Tuyatumie majukwaa kama haya ya JF kuelimishana,kujadili mstakabali wa nchi yetu,na kutoa ushawishi wa msingi katika kuleta mabadiliko chanya,vinginevyo hawa jamaa wa magamba wamesha anzisha mfumo ambao hata miaka 25 ijayo wanaweza wakaendelea kutunyonya wazi tena mchana kweupe,angalia nchi sasa hivi inamilikiwa na watu wachache na ndio wanamiliki resources za nchi hii.
Nisisahau mfumo wa hawa mafisadi na magamba ya CCM ni kurithisha watoto wao katika siasa na hata watoto wao mnawaona,bila aibu wanasimama na kusifia CCM na kuwabeba mafisadi na wengine ni baba zao,mnategemea wataukataa ufisadi?
Aluta continua
 
Wanaojua kuwa ccm inadanganya ni wachache sana na ndio maana walio wengi wanaendelea kuirudisha madatakani kila uchaguzi! Muhimu ni kusaidia kuhamasisha wananchi waamke na kutambua kuwa wanadanganywa na wasiendelee kuendekeza tshirt na kanga ambazo haziwasaidii.
 
Wanaojua kuwa ccm inadanganya ni wachache sana na ndio maana walio wengi wanaendelea kuirudisha madatakani kila uchaguzi! Muhimu ni kusaidia kuhamasisha wananchi waamke na kutambua kuwa wanadanganywa na wasiendelee kuendekeza tshirt na kanga ambazo haziwasaidii.
Unaujua mtindo wa Dance unaoitwa " CHAKACHUA?" kwa taarifa yako umeingizwa kwenye siasa na "effect" yake kwenye matokeo ya uchaguzi ni nzuri kuliko "effect" ya kura za PILAO/T-shirt
 
Mzee umesomeka Sana tena vizuri, tutafute namna namna ambayo Watanzania wengi watasoma habari hii jamani, kama ikiwezekana irudiwe kila wiki.
 
Back
Top Bottom