Mnyika ashtukia Mswada wa mabadiliko ya Katiba

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797






MBUNGE wa Jimbo la Ubungo (CHADEMA), Bw. John Mnyika amedai kushtushwa na maudhui ya muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa
mwaka 2011 uliochapwa katika Gazeti la Serikali toleo No. 1 Vol. 92 la Machi 11, mwaka huu, akidai kuwa hauna nia ya dhati ya kuleta mabadiliko ya katiba.

Bw. Mnyika alisema jana kuwa kilichomshtua zaidi ni mamlaka makubwa aliyonayo rais katika muswada huo, ambapo maudhui yamedhihirisha tahadhari aliyotoa mara kadhaa kwamba serikali haina dhamira ya kweli ya kuhakikisha panakuwepo na mchakato mzuri wa kuwa na katiba mpya.

Alisema kuwa muswada huo umelenga kuhalalisha yote ambayo yalitangazwa kufanywa na rais kuhusu mchakato wa katiba mpya na kupingwa na wadau mbalimbali, ambapo sasa yanataka kupewa uhalali kwa sheria inayotaka kutungwa na bunge kupitia muswada huo.

"Muswada huo unataka kumpa mamlaka rais ya kuunda tume ya kuongoza mchakato mzima wa katiba bila kuhusisha bunge ama wadau wengine wa msingi. Muswada huo pia utaka kumpa rais mamlaka ya kuteua wajumbe wa tume husika bila kushauriana na mtu yoyote isipokuwa Rais wa Zanzibar.

Muswada huo unaelekeza kuwa katika kuteua wajumbe, rais atazingatia uwakilishi wa makundi ya kijamii, lakini makundi husika hayatajwi hata kwa ujumla wake na hivyo kuacha mamlaka yote ya kuamua uwakilishi kubaki kwa rais," aliongeza.

Mambo mengine yaliyomo kwenye muswada huo, Bw. Mnyika aliyataja kuwa ni pamoja na kumpa rais mamlaka ya kutengeneza hadidu rejea za tume jambo ambalo lilipaswa kufanywa na bunge kwa kuwa sehemu ya sheria husika ama kufanywa na Mkutano Mkuu wa Kikatiba.

Aliongeza kuwa kwa kutoa mamlaka ya kuunda hadidu rejea kwa rais mwanya umetolewa kwa mtu mmoja kuweka mipaka ya nini kinastahili kufanywa na tume wakati wa mchakato wa katiba mpya na hivyo kuminya wigo wa mabadiliko.

"Muswada huo unataka tume iwasilishe ripoti yake kwa rais ambaye atampa nakala Rais wa Zanzibar na baadaye kumwelekeza waziri mwenye dhamana kupeleka bungeni yale atayoamua rais. Muswada huu kwa kuwa na kifungu hiki utaendeleza yaliyofanywa na marais waliopita kuhusu ripoti na mapendekezo ya tume zingine na hivyo kukwamisha mabadiliko ya kweli," alisema Bw. Mnyika.

Pamoja na hayo, aliongeza kuwa muswada huo unataka kutoa mamlaka finyu kwa jukwaa linalohusiana na mambo ya katiba tofauti na mkutano mkuu wa kikatiba ambao ungekuwa na mamlaka zaidi katika mchakato husika.

Aidha kwa mujibu wa Bw. Mnyika pia, muswada huo unataka kutoa mamlakama kubwa kwa rais kuteua wawakilishi wa chombo kikuu zaidi katika mchakato wa katiba bila kushauriana na kundi lolote ama wananchi kuhusika katika uteuzi ama kuwa na wawakilishi walioteuliwa na makundi yenyewe, mathalani vyama vya siasa, asasi za kiraia, taasisi za dini, vyama wa wakulima, vyama vya wanafunzi, vyama wa wafanyakazi na wengineo.

Alisema muswada huo unataka Rais ashauriane na Rais wa Zanzibar na Mwanasheria Mkuu wa Serikali pekee ambapo pia unatoa mamlaka makubwa zaidi ya rais kuamua hata kufanya bunge la kawaida kuwa ndilo bunge la katiba, jambo ambalo linaweza kurejesha udhaifu uliofanywa katika mchakato wa katiba inayotumika sasa ambapo umma uliporwa wajibu na mamlaka yake ya kushiriki moja kwa moja katika kupitisha katiba.

"Muswada kwa ujumla haujaeleza muda wa mchakato wa katiba na vipindi vitavyotumiwa na vyombo mbalimbali katika hatua mbalimbali za mchakato wa katiba; ama kutoa mamlaka ya kuwekwa kwa muda huo kwa chombo chenye uwakilishi mpana wa umma kama mkutano wa katiba au bunge na hivyo kutoa mwanya kwa mchakato mzima kucheleweshwa," alisema.

Bw. Mnyika alikumbusha kuwa mnamo Februari 9 mwaka huu, alitoa tamko kuwa alipokea kwa tahadhari uamuzi wa Serikali kupitia kwa Rais Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kubadili misimamo ya awali kuhusu mchakato wa katiba mpya na kuamua kukubaliana na mwito wa kutaka mchakato husika uanzie bungeni kupitia kutungwa kwa sheria ya bunge ya kuratibu na kusimamia mchakato husika kama alivyokuwa akitoa mwito kwa nyakati mbalimbali.
 
Kwa upande wetu Zanzibar tunahisi nibora kuzaliwa upya Tanganyika kwa jina la Tanzania? Chadema kelele tu sio wangombozi wa wa Wtanganyika. Kama kweli Chadema niwagombozi wasingali lilia katiba ambayo inalinda misingi ya ilani za ccm kuendelea kutawala. Wange pigania nchi ambayo wengi wa Tanganyika wanahisi Zanzibar wana nchi wao hawana. Na wangehamasicha kujita Wtanganyika kuliko kujita Wtanzania kwa kurudicha hadhi ya Tanganyika na historia mama.
 
Gazeti la Tanzania Daima la leo 31.3.2011 lina kichwa cha habari: "Chadema yagundua Madudu ya Katiba mpya." Licha ya ugunduzi huo wa kuipiga danadana katiba mpya hadi mwaka 2014 Siri iliyopo hapo ni kwamba, Kundi la mafisadi wana mikakati mizito kwa sasa ya kuwagawa watanzania chini ya mwavuli wa udini dhidi ya wazo la katiba mpya. Sasa wamesema, katiba ipo lakini hadi 2014. Na wala hakuna aliyepinga..

Siri nyingine iliyopo ni kwamba, itakapofika 2014 katiba mpya itapigwa tena tarehe ili kupisha maandalizi ya uchaguzi mkuu 2015. Watanzania wawe tayari kuteseka tena hadi mwaka 2020! Bila maandamano na migomo ya nchi nzima ya kudai katiba kwa nguvu, hakuna jipya Tanzania! Maisha ya maskini ni balaa, huzuni na mahangaiko wakati mafisadi na wapambe wao wanatamalaki kwa shangwe, hoihoi, vifijo na ndelemo.. Mabadiliko ya katiba yafanyike ndani ya mwaka 2011-2013. Hakuna sababu ya kuchelewesha!
 

Nguvu ya Umma isiyoratibiwa imeanza kufanya kazi nchini


Wednesday, 30 March 2011 10:52


nguvu-ya-umma.jpg


Editha Majura

KILA kona nchini Tanzania yanasikika malalamiko ambayo msingi wake ni ugumu wa maisha ambao unasababishwa na mambo kadhaa wa kadhaa. Wanasiasa nao wanahaha kutafuta kuungwa mkono na wananchi kwa lengo la kushika au kuendelea kuwa madarakani.

Harakati hizo za kisiasa zinafanywa kwa kutumia mbinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na semi na mitindo anuai, mathalani kujivua gamba, operesheni sangara, operesheni zinduka na nyinginezo.

Lengo la kila Chama ni kuufikia na kuuhamasisha umma ili ukiunge mkono.Harakati hizo hivi karibuni zimeibua dhana kwamba nchi inaweza kupoteza amani kutokana na baadhi ya mbinu zinazotumiwa na wanasiasa. Inadhaniwa kuwa nguvu ya umma inaweza kuchochewa kwa lengo la kuuondoa uongozi uliopo madarakani.

Hata Rais Jakaya Kikwete, akihutubia taifa mwishoni mwa mwezi wa pili mwaka huu, alikishutumu Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwamba maandamano na mikutano ya hadhara ya nchi nzima kinayofanya ambayo ilianzia mikoa ya Kanda ya Ziwa ina ajenda ya siri ya kutaka kuuondoa uongozi wa nchi madarakani isivyo halali.

Mtaalamu wa siasa ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Bashiru Ally, anabainisha kuwa nguvu ya umma siyo dhana hamasishi bali huleta maana inapohalalisha mapambano dhidi ya mfumo unaothibitika kuumiza umma. Anasema nguvu ya umma hailengi mtu, chama wala kundi fulani la watu.

Ally anasema nguvu ya umma kabla haijafikia hatua ya kuleta mabadiliko, hutafakari na kubaini kuwa madhara yanayoipata kutoka kwa kundi, mtu au chama fulani yanatokana na mfumo, hapo ndipo nguvu ya umma huratibiwa kukabiliana na mfumo huo na kwamba siyo lazima uongozi ulio madarakani uondolewe, ingawa hutokea mabadiliko makubwa ndani yake.

Vuguvugu la nguvu ya umma nchini linaweza kuleta mabadiliko ya kiuongozi?
Ally anasema Tanzania ni sawa na Chuo Kikuu cha nguvu ya umma kwa sababu hata uhuru wake ulipatikana kwa nguvu hiyo, nembo ya chama tawala (CCM) yaani ni jembe na nyundo inamaanisha nguvu ya umma (wakulima na wafanyakazi).

"CCM kipo kwa nguvu ya umma. Asili ya Tanzania ni kuongozwa kwa nguvu ya umma bila shaka unakumbuka enzi za Hayati Mwalimu Nyerere…, matatizo yalianza miaka ya 80 baada ya serikali kuingia kwenye mtego uliovishwa vazi la biashara huria…, ambao unalazimisha serikali kulinda maslahi ya mwekezaji badala ya maslahi ya umma," Ally anaeleza.

Anasema ili nguvu ya umma isababishe mabadiliko yenye kuleta manufaa, lazima iratibiwe ingawa yeyote anayejipa jukumu hilo lazima akumbane na kigingi cha kuitwa mchochezi. Hata hivyo iwe isiwe, pale nguvu ya umma inapohitajika inatokea tu kwa sababu hakuna mwenye uwezo wa kuzuia matakwa ya umma.

" Yeyote anayejitolea kuunganisha umma ili ukabiliane na mfumo kandamizi ni lazima adhibitiwe kwa kuitwa mchochezi lakini nguvu ya umma haidhibitiki, wakati unapowadia umewadia," Ally anabainisha.

Katika hali ya kawaida nguvu ya umma huratibiwa kupitia makundi maalumu katika jamii, kama vile vikundi vya wanawake, vyama vya wafanyakazi, vyama vya wakulima; Ushirika, vyama vya vijana na vile vya kiraia kwa lengo la kupinga mfumo ambao umethibitika kukandamiza jamii.

Awali kila kikundi hufanya mapambano peke yake kwa namna inavyoonekana inafaa, lakini malengo yanaposhindikana kufikiwa, ndipo umuhimu wa kuungana unapoonekana na hatua za makundi hayo kuunganisha nguvu dhidi ya mfumo husika inapotekelezwa.

Hatua hiyo ya kuunganisha nguvu ya vyama na vikundi vyote ndiyo inayoonekana kuwa ngumu hapa nchini na hivyo kuashiria hatari ya kuibuka nguvu ya umma isiyoratibiwa. Hatari hiyo inatokana na makundi hayo ambayo kwa kujua au kutojua, kugawanyika, jambo linaloleta ugumu katika kuwezesha uratibu wa nguvu ya umma.

Kwa mfano vyama vya wafanyazi, vimegawanyika na kila kukicha vinashambuliana kwa namna tofauti. Kadhalika vile vya wakulima, wafanya biashara, wanawake na hata vyama vya vijana.

Ally anasema ili nguvu ya umma ilete matunda bora kwa jamii ni lazima vikundi hivyo viungane kwa nia moja tu ya kukabiliana na mfumo bila tofauti za kisiasa, kidini wala kabila.

Mtazamo wa Ally kuhusu vyama vya siasa kusababisha nguvu ya umma kuleta mabadiliko ya kiuongozi nchini ni kwamba hilo haliwezekani kwa sababu wanasiasa karibu wote hawaumizwi moja kwa moja na ubovu wa mifumo ya huduma kwa jamii.

Aidha jamii ya Watanzania imeng'amua kuwa dhana wakilishi haina uwezo wa kuikomboa dhidi ya mifumo kandamizi hivyo linalotarajiwa ni jamii yenyewe kuondoa tofauti zake na kuungana kwa lengo la kujiletea mabadiliko, kwa maslahi yake yenyewe.

"Jukumu la kuwa na uongozi bora ni la umma wenyewe, umma wenyewe hutekeleza jukumu lake la ama kuuondoa madarakani uongozi uliopo au kushinikiza yafanyike mabadiliko makubwa," Ally anaeleza.

Hata sasa nchi inapitia kipindi cha mabadiliko yanayotokana na nguvu ya umma isiyoratibiwa. Ally anatoa mfano mmoja wapo kuwa ni matibabu yanayotolewa na aliyewahi kuwa Mchungaji wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, (KKKT), Ambikile Mwaisapile, Loliondo mkoani Arusha.

Mwaisapile almaarufu Babu, alianza kutoa tiba ya magonjwa yote sugu ukiwamo UKIMWI siku nyingi lakini tiba hiyo imepata umaarufu mkubwa baada ya vyombo mbalimbali vya habari kutangaza shuhuda za baadhi ya waliokunywa na kuponywa na tiba hiyo ambayo hutolewa kwa kipimo cha kikombe kimoja tu.

Kufuatia shuhuda hizo kutiwa nguvu na baadhi ya madaktari baada ya vipimo kuonyesha maradhi yaliyokuwa yakiwasumbua hayapo tena, idadi ya watu kuelekea kwa babu kunywa kikombe cha dawa iliongezeka kwa kasi kubwa. Katika kinachosadikiwa kuwa ni serikali kutekeleza jukumu lake la kulinda raia dhidi ya hatari au ashirio la hatari, ilitangaza kuzuia tiba hiyo.

Hata hivyo Serikali ya Mkoa wa Arusha ilitamka wazi kuwa ni vigumu kutekeleza uamuzi huo kwa sababu ya wingi wa watu wanaoamini na kufuata tiba hiyo. Baadaye Uamuzi huo ulilegezwa na mpaka leo matibabu yanaendelea. Ingawa tiba inatolewa kwa imani, wanaotibiwa hawabaguliwi kwa imani zao.

Kilichozuia Serikali kushindwa kutekeleza jukumu lake hilo ni umoja wa watu ambao haujali tofauti zao za dini, siasa, umri, jinsia, elimu wala kabila bali unaoashiria kukosa imani na mfumo wa kisayansi duniani katika kutibu magonjwa sugu badala yake kuamini tiba inayotolewa na babu Mwaisapile. Ally anasema huo ni mfano halisi wa jinsi nguvu ya umma inavyofanya kazi.

SOURCE: Nguvu ya Umma isiyoratibiwa imeanza kufanya kazi nchini
 
Jamani hivi katiba mpya ndio itakufanya ufanye kazi kwa bidii, uache wizi na ufisadi japo mdogo?
 
PLEASE DON'T MOVE IT IS NOT APRIL FOOL JOKE PLEASE DON'T


*Fagio kuwapitia Makamba, Membe, Mkuchika
*Lukuvi, Jack Mwambi, Chiligati kurithi mikoba
*UVCCM wamtajia JK mawaziri 9 wanaosaka urais




KUNA siri nzito ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inayofanyiwa kazi kwa uangalifu na unyeti wa aina yake, ambayo ikihitimishwa yatatokea mabadiliko ya kutisha ndani ya chama hicho.

Mwezi Aprili, utakuwa mwezi wa kusuka au kunyoa kwa CCM, ambapo ndani ya mwezi huu, baadhi ya viogozi wa Sekretarieti ya CCM wanapaswa kuwa wamefunga virago vyao tayari kuondoka, kwani litapita fagio la chuma.

Hoja inayojadiliwa kwa sasa, ni pangua pangua ya nafasi za juu za wajumbe wa Sekretarieti, ambapo kuna kila dalili kuwa Mzee Yusufu Makamba, ameomba kupumzika na kuwaachia kazi hiyo damu mpya, hali itakayowalazimu kufanya mabadiliko si zaidi ya Aprili.
Vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya CCM vitakavyofanyika Aprili, mwaka huu, vinaelezwa kuwa vitafanya mabadiliko mazito ndani ya chama, kwa nia ya kurekebisha makosa yaliyotokea katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba, mwaka jana.

Majina yanayotajwa kumrithi Makamba, ambaye ni Katibu Mkuu wa CCM mcheshi na mwenye nahau na semi za kila aina, ni matatu. Mbunge wa Isimani (CCM), William Lukuvi, anapewa nafasi kubwa ya kurithi mikoba ya Makamba.

Yusuph Makamba


Wengine wanaotajwa kwa kiwango ambacho si cha kubezwa ni Balozi wa Tanzania nchini Urusi, Kapteni Jack Mwambi na Katibu wa sasa wa Uenezi na Itikadi, Kapteni John Chiligati. Mweka Hazina wa CCM, Amos Makala, ambaye ni Mbunge wa Mvomero (CCM), ishara zinaonyesha kuwa atarithi mikoba ya Chiligati kwa kupewa kitengo cha Uenezi na Itikadi. Haikujulikana mara moja nafasi anayoishikilia itakwenda kwa nani. Hapa wanalenga kutoa fursa kwa damu ya vijana kukinadi chama mara nyingi kadri iwezekanavyo.

Mawaziri wenye nyadhifa kwenye Sekretarieti ya Halmashauri Kuu; ambao ni Bernard Membe, ambaye anasimamia Idara ya Kimataifa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Kapteni George Mkuchika, hawa wanatajwa kupumzishwa.

Inaelezwa kuwa umefanywa uamuzi wa makusudi kuhakikisha wajumbe wa Sekretarieti wote hawapewi majukumu mengine ya kiserikali, hali itakayowapa muda wa kutosha kufanya shughuli za chama tofauti na hali ilivyo sasa.

Kwa upande mwingine, uongozi wa Jumuiya ya Vijana ya Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umempelekea Rais Jakaya Kikwete waraka wenye siri nzito ambazo zinadaiwa kujadiliwa katika kikao cha Baraza Kuu la jumuiya hiyo kilichomalizika Jumapili iliyopita mjini Dodoma.

Vyanzo vyetu vya habari vinasema pamoja na Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM, Beno Malisa kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu kilichojiri katika Baraza hilo, kuna masuala mengi nyeti yaliyojadiliwa ambayo hakuyatolewa ufafanuzi kwa kuwa hakutaka kuyaanika hadharani kabla ya ujumbe huo kumfikia Rais Kikwete.
Kwa mujibu wa habari zilizoifikia Rai, waraka huo unatokana na sehemu ya maazimio mazito zaidi yaliyofikiwa na Baraza hilo, ambayo wajumbe walikubaliwa yasizungumzwe hadharani kwa kuwa yalilenga kutoa ushauri kwa Rais Kikwete juu ya uendeshaji wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Ingawa haijaweza kufahamika kwa uhakika nini kilichomo ndani ya waraka huo, ambao ulitarajiwa kuwasilishwa kwa Rais Kikwete na uongozi wa UVCCM makao makuu pamoja na Mzee Kingunge Ngombale-Mwiru, habari kutoka vyanzo mbalimbali vya habari zinasema vijana hao wameeleza namna baadhi ya viongozi ndani ya Serikali na katika chama, wanavyochangia kuzorotesha harakati za kukiimarisha chama kwa wananchi.

Kingunge ndiye aliyechaguliwa na Baraza Kuu la UVCCM la Dodoma kuwa Kamanda wa jumuiya hiyo, akichukua nafasi iliyoachwa wazi na marehemu Mzee Rashid Kawawa, aliyefariki dunia jijini Dar es Salaam Desemba 31, 2009.

Hata hivyo, Katibu Mkuu wa UVCCM, Martin Shigela alipoulizwa kuhusu waraka huo wiki hii, alikanusha kuwapo kwake, akisema kila kitu kilichozungumzwa katika mkutano wa Baraza Kuu, kilifafanuliwa kwa waandishi wa habari.
“Hakuna waraka kama huo, kila kitu kilichoamuliwa na Baraza Kuu kilizungumzwa katika mkutano na vyombo vya habari. Hakuna cha kuficha. Hata kama kuna waraka maalum kwa Rais Kikwete tungewaambia upo, lakini tusingewaeleza kilichomo ndani,” alisema Shigela, ambaye pia alikiri kuwa Kingunge sasa ndiye ameshikilia rasmi mikoba ya marehemu Mzee Kawawa.

Inaelezwa kwamba moja ya mambo aliyoambiwa Rais Kikwete katika waraka huo ni namna baadhi ya mawaziri wanavyohangaika katika kampeni za kujenga mitandao yao kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na kusahau kabisa jukumu lao kubwa la kumsaidia Rais kutekeleza ahadi zilizomo katika Ilani ya Uchaguzi wa mwaka 2010.

Vyanzo vyetu vya habari vinasema pamoja na mambo mengine kwamba, UVCCM inamshauri Rais Kikwete katika waraka huo kuwatema mawaziri hao ili waendelee na mipango yao ya kujenga mitandao ya uchaguzi wa 2015 badala ya kuendelea kuikwamisha Serikali katika kutekeleza ahadi zake kwa wananchi.
Inaelezwa kuwa mawaziri hao wametajwa kwa majina kuthibitisha namna mawaziri hao wanavyotumia rasilimali za Serikali kujijengea mitandao yao ya kisiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Rai iliwahi kuandika katika matoleo yake ya nyuma namna baadhi ya mawaziri wanavyohaha katika maeneo mbalimbali mikoani, wakijenga mitandao yao ndani ya CCM nyakati za usiku wanapokuwa katika ziara za kiserikali, badala ya kuumiza vichwa kutatua matatizo mengi yanayowakabili wananchi.

Ilielezwa katika habari hizo kwamba mawaziri tisa wanaofanya ziara mikoani, wamekuwa wakitumia ziara hizo kujenga mitandao yao na marafiki zao kwa kufanya vikao vya kampeni ndani ya chama nyakati za usiku badala ya kufuatilia majukumu mazito yaliyowapeleka katika ziara hizo.

Waraka huo haukuwagusa mawaziri peke yao, bali pia umeeleza namna Kamati Kuu ya CCM inavyoshindwa kumshauri Mwenyekiti katika masuala mbalimbali mazito yanayolikabili taifa, huku wakitaka mabadiliko makubwa yafanyike ndani ya chombo hicho.

Haikuweza kufahamika mara moja iwapo suala la kujiuzulu kwa Sekretarieti ya chama hicho inayoongozwa na Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, limo katika waraka huo, unaoelezwa kuwa ni mkali kuwahi kutolewa na UVCCM kwa kiongozi wa nchi.
Kwa wiki kadhaa sasa, vyombo vya habari vimekuwa vikiandika kuhusu azma ya kujisafisha kwa CCM kutokana na matokeo mabaya katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana uliosababisha chama kipoteze majimbo mengi yaliyokuwa ngome yake, huku vikieleza kwamba moja ya njia za kujisafisha ni pamoja na kuunda upya Sekretarieti ya chama hicho.

Hata UVCCM Mkoa wa Pwani pia walionyesha kuunga mkono hoja hiyo, pale Makamu Mwenyekiti wa jumuiya hiyo Mkoa, Abdallah Ulega, alipoitaka sekretarieti hiyo ijuzulu kwa madai kwamba ndiyo iliyokuwa ikivujisha siri na mikakati ya chama kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) pamoja na kushindwa kumshauri vizuri Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete.

Inaelezwa kuwa Baraza Kuu la UVCCM liliitishwa kutoa mapendekezo yake kwa Mwenyekiti kabla vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa vya chama hicho vinavyotarajiwa kukutana katika siku za karibuni, havijakaa.

Vikao hivyo ndivyo vinavyotarajiwa kufanya maamuzi kadhaa mazito baada ya kupata taarifa ya tathmini ya Uchaguzi Mkuu kutoka katika maeneo mbalimbali ya nchi inayofanyika kutokana na agizo la Rais Kikwete katika kilele cha maadhimisho ya miaka 34 ya CCM yaliyofanyika mjini Dodoma Februari 5, mwaka huu.
Katika mkutano wake na waandishi Jumapili iliyopita, Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM, Malisa, alieleza namna Baraza Kuu pamoja na mambo mengine, lilivyopitisha azimio la kujipanga upya katika nyanja zote, ikiwamo uanachama, uongozi, maadili, uimarishaji kiuchumi na kiitikadi kwa lengo la kuboresha zaidi muundo wa jumuiya hiyo.

Kutokana na uzito wa kazi hiyo, baraza hilo liliteua kamati maalum, itakayokuwa chini ya mjumbe wa Baraza Kuu, Hussein Bashe, ambayo itafanya uchambuzi yakinifu wa namna ya kuifanyia mabadiliko jumuiya hiyo na kisha kuwasilisha mapendekezo yake katika vikao vya maamuzi vya UVCCM.
Mbali na Bashe, wajumbe wengine wa kamati hiyo walitajwa kuwa ni Riziki Pembe, Fadhili Ngajilo, Zuberi Bundala, Rogers Shemelekwa, Daud Ismail, Ashura Seng’ondo na Athony Mavunde.
 
Tatizo ninaloona hapa ni watu kujaribu jaribu kila kitu wala siyo kufanya kabisa. Tunahitaji msimamo wa kweli, serikali haitaki kufanya kwa hiari hadi ishinikizwe vinginevyo kila kitu kiko upande wao, who cares? We need to act more intelligently with good strategy! Hope CDM is what are doing now. Ngoja tuwape muda , tuwaungeni tunaoweza na kuwatia moyo CDM , ikifika 2014 hakuna la maana tuwape warning viongozi wetu wa CDM ili tujue nini kinakwamisha.
 
Ni nani huyo katika Tanzania hii ya leo anayedanganyika na MABADILIKO YA SURA ZA WATU ndani ya vyama bila mfumo mzima, katiba, sera na kanuni mbali mbali kubadilishwa kwa jinsi wanavyotaka WANANCHI na wala si kushinikiza matakwa ya watawala???????????

Acha wapoteze zaidi muda wao kwa kujifurahisha kuchubua gamba la CCM badala ya kulivua kabisa.
 
Same story!......as long as the legislature is dominated by CCM,...nothing really is gonna happen.
 
Back
Top Bottom