Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,639
DAMU YA MWANAMWALI KITANDANI
MTUNZI: ALLY KATALAMBULA
UTANGULIZI
“MWANAUME kutokwa na machozi, iwe kwasababu ya maumivu au majonzi, si kitu kinachokubalika katika ukoo na kabila letu.
Ukiona mwanaume analia, ujue ana roho ya kike. Ukilia, huna sababu ya kuvaa kaptula ama suruali. Machozi ya mwanaume yanatakiwa kuwa adimu sana. Mwanaume kutokwa machozi ni udhaifu wa kiwango cha mwisho.”
Ni maneno ya marehemu baba yangu. Niliyakumbuka nikiwa katika madhila makubwa. Donge kavu lilikuwa limenikaba kooni. Uso wangu ulikuwa umesawijika kwa hasira iliyochanganyikana na simanzi kubwa.
Nilikuwa nimejiinamia mkono ukiwa shavuni. Maungo ya mwili wangu yalikuwa yakivuja jasho kama mgonjwa wa homa kali. Macho yalikuwa mekundu kama yaliyoingiliwa na pilipili. Kila wakati nilikuwa nikitoa msonyo mdogo, huku nafsi yangu ikijilaumu ndani kwa ndani.
Kwa mara nyingine, nilinyakua simu yangu ya mkononi iliyokuwa kando na kupiga namba fulani.
Namba niliyokuwa naipiga, nilikwishaipiga kabla zaidi ya mara kumi na moja bila mafanikio. Simu ilipokuwa sikioni, mapigo yangu ya moyo yalikuwa yakinienda kasi kuliko kawaida. Japokuwa haikuwa mara yakwanza kuipiga simu ile, ila safari hii nilikuwa na presha kubwa.
Baada ya muda fulani kupita, majibu kupitia sipka za simu hiyo nikayapata:
“…namba ya simu ya mteja unayempigia haipatikani kwa sasa...”
Nilikata simu bila kusikiliza maneno yote punde baada ya kupokea ujumbe ule.
Donge kavu likaendelea kunikaba kooni, wivu na hasira vikaendelea kutanda moyoni mwangu, kwa mara nyingine nilijikuta nikisaliti ujasiri niliofundwa na baba yangu. Machozi yakanibubujika tena!
“Kwa nini unanifanyia hivi Nasra? Kwanini? Iweje jambo hili lifanywe na wewe? Haya ndiyo malipo ya pendo langu? Kosa langu ni kukupenda si ndivyo? Nini maana yake hii sasa? Eeh!!..” nilinong’ona kwa sauti iliyojaa mfadhaiko huku machozi yakijikusanya machoni.
Kwa mujibu wa saa yangu ya mkononi, ilikuwa ni saa sita na nusu usiku, nilichukua pakiti ya sigara na kutoa mche mmoja na kuupachika mdomoni, nikawasha kwa kiberiti cha gesi ambacho kilitoa mlipuko mdogo wa moto, nikaunguza ile sehemu mbele ya sigara.
Nikavuta kwa mkupuo mmoja na kutoa moshi mwingi kupitia tundu za pua na mdomo.
Nafsi yangu ilikiri wazi kuwa mke wangu Nasra hakuwa mtu sahihi kwangu, hakuwa na sifa hata moja ya kuwa mke nimtakaye, mke niliyekuwa nikimwota usiku na mchana, lakini moyo wangu ulinionya kutofanya kitendo chochote kitakachopelekea kuwa mbali na kiumbe yule.
Haja ya moyo wangu ikazidi nguvu mtazamo wa utashi wangu. hali hiyo ikanifanya nizidi kuangamia nafsini.Nikawa mtu wa kujilaumu.
Ndiyo. pamoja na mgogoro wa ndani kwa ndani uliokuwa ukinivuruga hata afya ya mwili wangu bado nafsi yangu ilijiapiza kufa Kijerumani na tai shingoni!!!!.
SURA YA KWANZA
Jina langu halisi naitwa Faraji Hussein Mpangalala, ni mzaliwa wa Kigoma katika Kijiji cha Nguruka, japo kwa sasa naishi katika Jiji la Dar Es Salam. Ni mtoto mwisho kati ya watatu kutoka kwa mzee Mpangalala, mbele yangu wakiwa ni dada zangu wawili Halima na Shadia.
Dada zangu hao, wote walikwishaolewa miaka mingi iliyopita, baada tu ya kumaliza kidato cha nne na kupata matokeo ambayo hayakuwawezesha kuendelea na masomo.
Naweza nikasema, katika familia yetu, ni mimi pekee ambaye wazazi wangu walikuwa na matumaini makubwa ya kuja kuwa kiongozi wa familia siku za usoni. Hii ni kutokana na kwamba, kwanza nilikuwa mtoto wa kiume lakini pia nilikuwa ndiye mtu msomi kuliko mwingine yeyote.
Nikiwa na umri wa miaka 27 baada ya kumaliza shahada yangu ya kwanza ya ualimu pale Mlimani, niliajiriwa ofisi ya mkurugenzi wa manispaa ya Temeke Jiji Dar, kama mratibu wa elimu wa manispaa hiyo.
Mwaka 2004 rasmi niliyaanza maisha ya kujitegemea, nikiwa kijana mwenye ndoto kubwa za mafanikio mbele yangu, mshahara mzuri pamoja na malupulupu ya hapa na pale yaliniweka katika daraja la juu sana kimaisha, kimsingi nilishi maisha ambayo kijana yeyote anayaota na angapenda awe nayo.
Ni katika kipindi hicho, ndipo nilipoanza kupata shinikizo kubwa kutoka kwa wazazi wangu, ni kuhusu ndoa. Kuoa.
Ni kweli, kwangu mimi wakati huo, ulikuwa ni wakati sahihi kabisa kuoa, hasa ukizingatia nilikuwa na kipato kikubwa, tena cha uhakika. Hata hivyo, tatizo lilikuwa ni moja tu. Sikumwona mwanamke sahihi wa kuwa mke wangu.
Siyo kwamba katika Jiji la Dar nilikuwa sikutani na warembo. Laa!!. Warembo niliwaona utitiri ila wengi wao walikuwa viruka njia. Ndiyo. Baadhi ya wanawake wengi wa mjini wanahitaji mwanaume wa kariba yangu.
Si labda kwakuwa nilikuwa mwanaume mwenye mvuto, Laa! Isipokuwa nilikuwa kijana mwenye fedha na mafanikio makubwa maishani.
Baadhi ya wanawake wa Dar Es Salam kwao fedha ni zaidi ya upendo, hivyo sikupenda kabisa kuoa mwanamke ndani ya jiji hilo ambaye nitamweka ndani huku nikijua mwanamke huyo kapenda fedha na mali zangu.
Kwangu mimi, urembo ilikuwa ni sifa ya pili baada ya uchamungu, heshima, upendo na uvumilivu.
“Mwanangu kama tatizo ni hilo, tupe ruksa sisi tukutafutie mwanamke wa kuoa huku kijijini,” siku moja mama yangu alinieleza, ilikuwa ni baada ya kumpa sababu za kwanini nachelewa kuoa.
“Siyo jambo baya na wala siyo jambo zuri.”
“Kwa nini unasema hivyo baba?”mama aliniuliza.
“Ni jambo zuri kama mwanamke mtakayenichagulia ndiye wife material nimtakaye, na ni jambo baya kama mkinichagulia mwanamke ambaye hatokuwa na sifa nizitakazo.”
“Naamini mimi na baba yako hatuwezi kukuangusha mwanangu Faraji. Chombo nitakachokutafutia utakipenda,” mama aliniambia.
Nawaamini mno wazazi wangu, Sikuwa na pingamizi juu ya ombi hilo, niliwakubalia kwa roho moja wanitafutie mke.
Hazikuzidi wiki mbili, nilipigiwa simu na baba yangu akanieleza kuwa wamekwishampata mchumba na kilichokuwa kimebakia ni kumposa, kulipa mahari, kisha ndoa.
“Jina lake?” niliuliza kwa kiherehere
“Anaitwa Nasra Mfaume.”
“Kabila gani?”
“Unauliza kabila, unataka kutambika mwanangu?” baba yangu alinitania.
“Napenda kujua tu.”
“Hana kabila lakini nadhani ni sahihi kukwambia ni Africast, mchanganyiko wa Kiajemi na Kibantu, mababu zake ambao asili yao walitokea nchini Yemen na kuishi kisiwani Pemba, lakini baada ya kulowea huku na kuzaliana na Waswahili wamekuwa ni hukuhuku kwetu,” baba alinieleza.
Nilishusha pumzi fupi huku taswira ya machotara wa Kipemba ikijengeka kichwani mwangu.
“Atakuwa bomba huyo mchumba. Niliwaza kimoyomoyo simu ikiwa bado sikioni.
“Kwa hiyo mipango iliyobakia ni kulipa mahali kisha ndoa tu mwanangu,” baba akaendelea kuongea zaidi kwenye simu.
“Unaweza kunitumia picha yake huyo mrembo?”
“Nakutumiaje?”
“Kwa njia ya mtandao?”
“Bila shaka mwanangu.”
“Basi nitumie picha yake huyo mchumba sasa hivi,”nilisema nikiwa na wahaka wa kumwona huyo mwanamke wa Kipemba.
Je, nini kitaendelea?
KITABU KIPO MTAANI NICHEKI KWA 0687750295