Mambo yanayosababisha ajali za meli

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,314
33,108
000000000001acosta.jpg
KUZAMA kwa meli ya Skagit Jumatano iliyopita ni ajali ya tatu ya aina hiyo kutokea hapa nchini na kusababisha vifo vya watu wengi.Mwaka 1996, ilitokea ajali ya MV Bukoba iliyozama Ziwa Victoria, ambayo kwa mujibu wa takwimu za Msajili wa Vizazi na Vifo Wilaya ya Mwanza, ilisababisha vifo vya watu 1,020.

Mwaka jana ikiwa miezi kumi imepita hadi sasa, pia ilitokea ajali nyingine ambapo meli ya MV Spice ilizama katika ukanda wa Bahari eneo la Kisiwa cha Nungwi na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 200.
Matukio mawili ya Mv Spice na Skagit yaliyotokea nchini kweye Bahari ya Hindi, katika kipindi cha miaka miwili mfululizo yameshtua wengi.
Ajali zote tatu zilizotokea kwa vyombo hivyo majini zilitokana na sababu mbalimbali.
Bila shaka Watanzania wengi watapenda kufahamu nini kilisababisha ajali hizo na pengine kitafutiwe ufumbuzi wa haraka.

Ili kuweza kufahamu hayo ni vyema kujua namna meli inavyofanya kazi na kuifanya ielee kwenye maji.

Meli inavyoelea
Utengenezaji wa meli hufuata kanuni ya Mwanasayansi, Newton ambaye katika utafiti wake aligundua kuwa ili kitu chochote kiweze kuelea kwenye maji kunakuwa na nguvu inayokisukuma juu.
Katika hali hiyo kinachofanya kisizame ni kusukuma nje kiwango cha maji kinacholingana na uzito wake.

Watengenezaji wa meli hutumia kanuni hiyo katika kutengeneza meli za aina mbalimbali na kuweka bayana kiwango cha uzito kinachofaa kubebwa na chombo hicho.

Uzito unapoongezeka huwa ni hatari, kwa sababu meli hiyo itakuwa inazama kwenye maji.

Maelezo ya kiufundi yaliyopatikana katika mtandao wa Wakala wa Meli wa Kimataifa yanaeleza kwamba, meli imetengenezwa kwa namna ambayo uzito wake unasukuma nje maji yanayolingana na uzito wake wakati ambapo sehemu yake bado imebakia juu ya uso wa maji.

Licha ya kutumia kanuni hiyo, inaelezwa kuwa watengenezaji wa meli huzingatia vigezo vingine kama vile joto, ambalo linaweza kubadilisha uzito wa maji kulingana na kipimo cha ujazo.

Kwa sababu hiyo, inaelezwa: "Msukumo wa kwenda juu wa kwenye maji ndiyo unaosababisha meli kuelea na injini zake ndizo zinazoiwezesha kutembea.”

Kasi ya kutembea kwa meli hutegemeana na uwezo wa injini pamoja na namna nahodha wake anavyoamua, kulingana na mazingira yanavyomruhusu.

Hata ikiwa injini za meli zitakuwa hazifanyi kazi, meli huelea kwenye maji kwa sababu utengenezaji wake unaifanya isizame.

Aina za meli
Kwa kawaida zipo aina zaidi ya 16,000 za meli. Lakini zinaweza kuwekwa katika makundi makuu sita.

Makundi hayo ni ya meli zinazobeba makontena, malighafi maalumu, mizigo, mafuta, kemikali, meli maalumu za kuvunja barafu, za kusafirishia abiria na zile za kivita.

Hata hivyo, wataalamu hao wanasema kuwa kwa kawada meli zimetengenezwa kwa ajili ya kubeba mizigo, lakini zipo maalumu ambazo hutumika kwa ajili ya kuvusha abiria katika safari fupi.

Ajali za meli
Zipo aina nyingi za ajali za meli, lakini nyingi zimekuwa ni za meli za kubeba mizigo, ambazo mara nyingi ndizo zinazosafiri umbali mrefu.

Mara nyingi mambo yanayoweza kusababisha ajali za meli ni kubeba vitu vinavyozidi uwezo wake, upangaji mbaya wa mizigo, machafuko ya bahari, vyombo kugongana pamoja na kugonga miamba baharini.
Nyingine ni moto wa ghafla unaoweza kusababishwa na hitilafu ya umeme au mizigo iliyobebwa na chombo husika.

Tatizo jingine linaelezwa kuwa ni kuchakaa kwa chombo na matatizo mengine ya kibinadamu kama vile uzembe katika matengenezo na ukarabati.

Uimara wa aina ya chuma kinachotumika kutengeneza meli ni mojawapo ya mambo ambayo wataalamu hao wanaeleza kuwa yanazingatiwa katika kuipa uwezo wa kudumu kwa miaka mingi ikifanya kazi bila kuharibika.

Kwa kawaida vyuma hupata kutu na kusababisha matundu yanayoweza kusababisha meli ipate ajali, hivyo ukarabati na uchunguzi wa mara kwa mara hufanyika.

Ufanyaji kazi wa meli, unaelezewa kitaalamu kwamba huwa na mwisho, ambapo haifai tena kwa ukarabati wa aina yoyote kuirudisha katika hali yake ya kawaida.

Katika hali hiyo ikifanyiwa ukarabati na kulazimishwa kufanya kazi, hapo inaweza kusababisha ajali ya ghafla.

Moja ya mambo yanayosababisha vyuma vya meli kupata kutu haraka hasa inavyokuwa imezama baharini ni uwepo wa chumvi kwenye maji bahari au maziwa.

Hata hivyo, mambo mengine yanayoweza kusababisha ajali ya meli nje ya uwezo wa kawaida wa kibinadamu inaelezwa kuwa ni hali ya hewa kama vile upepo mkali na vimbunga.

Wataalamu hao wanasisistiza kuwa kwa namna meli ilivyoundwa ajali zake nyingi hutokana na matatizo yanayosababishwa zaidi na makosa ya kibinadamu.

Hii ni kwa sababu wataalamu wameweka masharti mbalimbali ya kutumia chombo hicho kama ikiwamo muda wa kutumika, muda wa matengenezo na namna sahihi ya matumizi.

Vilevile inaelezwa kuwa iwapo waongozaji wa chombo hicho watafanya kazi muda mrefu bila kupumzika, wanaweza kupoteza umakini katika kukiongoza.

“Suala la usimamizi ni la msingi na muhimu katika kuepusha chombo cha majini kisipate madhara. Kwa kawaida nahodha huchunguza mazingira ambayo chombo kinapita na kuhakikisha kinasonga mbele kwa usalama," inaeleza ripoti hiyo ya wataalamu wa meli.

Ili kuepusha ajali za vyombo vya majini, inaelezwa kuwa utendaji wake wa kazi umewekewa masharti kadhaa, ambayo husimamiwa kitaifa na kimataifa kwa usalama wa watu na mali zao.

Mmoja wa makapteni wa meli nchini Marekani Cmdr Paolillo, ambaye meli aliyokuwa akiiendesha ilipata ajali, alisema ajali hiyo ilitokana na sehemu ya chombo chake iliyozama ndani ya maji kugota kwenye mwamba ndani ya bahari.

Anasema kosa hilo lilitokana na uzembe wa kutofuata njia salama, hasa ikizingatia meli aliyokuwa anaiendesha ilikuwa ni ya kizamani.

Anasema meli za kisasa zina uwezo wa kuchunguza njia na kufahamu kama kuna hatari ya meli kugota popote.
Habari hii imeandikwa na Leon Bahati kwa msaada wa taarifa mbalimbali

Mambo yanayosababisha ajali za meli
 
Hapa kwetu vyanzo vya ajari za meli ni kuwa meli hizo zinamilikiwa na watu wasioguswa na sheria
 
Hapa kwetu vyanzo vya ajari za meli ni kuwa meli hizo zinamilikiwa na watu wasioguswa na sheria

umeona eehh...

sehemu kubwa ya boti hasa zenye kufanya safari baina ya Znz na Tanganyika zinamilikiwa na aidha ndugu au jamaa wa viongozi katika serikali zote mbili.
 
Back
Top Bottom