CCM walianza kumpiga vita Lowassa tangu alipokuwa ndani ya CCM na baadaye alipojiunga na CHADEMA ili kuwa mgombea wa UKAWA kwa kutumia sababu ya Ufisadi.
Lakini karata hii ikajibiwa kiufundi na Lowassa mara baada ya kutoka CCM na hivyo kuwafanya wananchi waone kwamba anaonewa bure kwani kama ni kweli basi kwa nini Serikali ya CCM isimpeleke mahakamani ili ajibu tuhuma za kuiba mabilioni ya pesa za kodi za wananchi?
Wakabakiza karata tatu - Ugonjwa, matusi na Ukanda.
Karata ya ugonjwa ni moja ya karata ya kijinga kabisa ambayo CCM imewahi kuitumia na hasa ukichukulia kwamba karata hii imepewa kipaumbele mara baada ya kugundua kwamba karata yao ya Ufisadi imebuma. Karata hii walitaka kuitumia wana CCM ndani ya chama chao wakati Kikwete akiwania kuwa Mgombea Urais kwa kumtuhumu Kikwete kuwa mgonjwa na ikashindikana hivyo ni ajabu sana kuona kwamba CCM chini ya uongozi wa Kikwete bado inataka kuitumia karata ileile iliyoshindwa!!!
Kwa kutumia karata hii, CCM imemtuhumu Lowassa kuwa ni mgonjwa na kumtungia magonjwa mbalimbali. Vilevile mgombea wa CCM amekuwa akija na komedi mbalimbali kama kuruka kutoka kwenye gari, kupiga push ups, kutumia ishara ya mabadiliko ya UKAWA kwa kuzungusha mikono yake mara nyingi kwa mbele (Kwa maana ya UKAWA, unapozungusha mikono yako kwa mbele una maana unakubali kwamba Lowassa ni mabadiliko na unapozungusha kwa nyuma unakubali kwamba mabadiliko ni Lowassa!!!), n.k.
Lakini juhudi zote hizi za kumfanya Lowassa aonekane mgonjwa na hivyo hafai kuwa Rais zimegonga mwamba kwani zimeongeza hasira tu kwa wananchi hasa baada ya CCM kushindwa kutetea hoja yao ya kumtuhumu Lowassa na ufisadi kwa kumburuta mahakamani kama yeye mwenyewe alivyowaambia. Matokeo yake Magufuli na wapambe wake wanaonekana kituko wanapojaribu kujionyesha kwamba wao wana afya nzuri zaidi ya Lowassa kwani wananchi hawaangalii nguvu ya mwili bali akili ya kichwani ya mtu wanapofanya maamuzi ya kumteua mtu kwenye ofisi nyeti kama ya Rais kwani Ikulu sio mahali pa kwenda kubeba zege au kupigana ngumi. Hivyo karata hii nayo imeshindwa.
Karata ya matusi tena ya nguoni wanayomtukana Lowassa nayo imesaidia tu kuongeza hasira za wananchi na kuwadharau CCM kama genge la wahuni na hivyo kuwafanya hata wazee ambao kawaida huwa wanaiunga mkono CCM kuichukia baada ya kugundua kwamba kuiunga mkono CCM ni kuwaunga mkono wahuni wanaoongozwa na kinara wao Mgombea Urais Magufuli ambao hawana hay ahata kidogo kutukana matusi makubwa makubwa mbele ya watoto wao tena kwenye vioo vya jamii kupitia televisions, radio, n.k.
Karata ya mwisho ya Ukanda kwa kuwatuhumu CHADEMA kwamba ni watu wa Kaskazini hatimaye imegonga mwamba vibaya mno kule Mwanza wakati Wasukuma walivyojitokeza kwa wingi kwa mafuriko yaliyovunja rekodi ya mafuriko ya uchaguzi mkoani mwanza pale wenyeji wa Mwanza walipojitokeza kwenye mkutano wa UKAWA uliohitimishwa na Lowassa. Mwanza ni eneo ambalo kuna Wasukuma wengi ambao ndio kabila la Magufuli lakini Wasukuma wameonyesha kwamba hawaangalii ukabila katika kuamua mstakabali wa maisha yao na vizazi vijavyo bali wanaangali sera na uwezo wa mgombea katika kuwaletea maendeleo.
CCM wameshindwa kuelewa kwamba karata ya Ukanda kwa CHADEMA sasa hivi haina nguvu tena kwani CHADEMA haigombei uchaguzi huu kama CHADEMA bali kama UKAWA hivyo kuwaunganisha watanzania wa dini na makabila yote wanaotaka katiba mpya bila kujali makabila yao au dini zao. Vilevile wameshindwa kuelewa kwamba athari za umasikini walizoziacha kwenye jamii kwa wizi wao wa mali ya umma kumewaathiri Watanzania mno kiasi kwamba ajenda yao kuu ni mabadiliko nje ya mfumo uliowafanya wawe maskini kiasi hiki na sio ukabila wala udini.
Hivyo karata zote wanazotumia dhidi ya Lowassa zimegonga ukuta na zinazidisha tu hasira ya wanachi dhidi ya CCM na kuongeza umaarufu wa Lowassa ndio maana idadi ya mashabiki wa Lowassa inazidi kuongezeka kadri siku ya kupiga kura inavyokaribia. Hii inathibitisha usemi kwamba siku ya kifo cha nyani basi miti yote huteleza.
Hivyo CCM wajiandae kuwa chama cha upinzani bungeni kwani wimbi la Watanzania kuhitaji mabadiliko nje ya CCM ni kubwa mno ambalo hawawezi kulizuia hata kama wakiamua kumwaga damu za Watanzania ili wabakie madarakani kwa mtutu wa bunduki.