Unanikumbusha mbali sana mkuu.
Hiyo picha ya kwanza ni miaka ya 1960. Enzi hizo fasheni yetu ilikuwa suruali za kubana sana kama za vijana wa leo - hiyo aliovaa huhu bwana. Elvis Presley alikuwa ndio habari ya mjini na twist ndio dansi lenyewe. George Mukabi, Edward Masengo, Mwenda Jean Bosco, Frank na dadazake, Salim Abdallah ndio walikuwa wakali wa muziki wa dansi Afrika Mashariki.
Sasa kuhusu hizi suruali za kubana hawa vijana wa siku hizi wana bahati sana. Siku hizo waziri mkuu alikuwa mzee Kawawa. Alitoa amri kuwa tusivae tena hizi suruali za kubana na yeyote ataekutwa amevaa kipimo kilikuwa kupitisha chupa ya soda. Kama chupa haikuweza kuporomoka kutoka kiunoni mpaka chini miguuni hiyo suruali ilitiwa mkasi. Lakini sasa mabebi ndio walikuwa wanatufukuzilia sisi wenye suruali hizo - Ee bwana we, patashika gani hiyo mitaani.
Sasa ikaja miaka ya 70. Hapo tukiwa vyuoni tulitilia hizi bell-bottom (picha ya pili). Staili hiyo nayo ilivuma kipindi kirefu huku tukivaa viatu vya gorofa. Watu wengi waliteguka miguu kwa viatu hivi vikiitwa raizoni (raised-on shoes).
Ushauri: Fasheni ikipitwa na muda usiitupe. Iweke na mjukuu wako anaweza kuja kuitumia kama fasheni mpya kwao.
Asante kwa kunipa fursa ya time-travel back to the past.