Sildenafil Citrate
JF-Expert Member
- Jan 29, 2021
- 573
- 2,553
Akiwa katika Mkutano wa hadhara uliofanyika Kibamba, leo Julai 7, 2023, Mgombea urais wa CHADEMA (2020) Tundu Lissu amedai katika historia ya Tanzania kama nchi, hakuna Rais amewahi kusaini mkataba wa ajabu alioutafsiri kuwa tukio la kijinga kuwahi kutokea kama Rais Samia.
“Rais wetu amefanya kitu cha kijinga hakuna aliyewahi kufanya kitu cha aina hii. Hakuna Rais wa nchi hii, sio Nyerere, so Mwinyi, sio Mkapa, sio Kikwete na sio Magufuli aliyewahi kujiingiza kijinga namna hii” amesema.
Lissu ambaye kila baada ya kutoa ufafanuzi mdogo aliuliza watu mara kwa mara kuwa “Nauliza, huyu mama kapewa nini?” alibainisha pia kuwa hata hao wote wanaomtetea nao wamepewa nini? Amesema anafahamu kuwa Prof. Kitila Mkumbo amezawadiwa uwaziri baada ya kuusifia Mkataba huo, hawa wengine wamepewa nini?
Aidha, Makamu Mwenyekiti huyo wa CHADEMA amesema tangu aanze kufuatilia mikataba ya nchi hii enzi za Mkapa hajawahi kukukutana na mkataba mbovu wa aina hii unaoizidi hata ile ya madini ambayo walau huonesha ukomo wake.
Baadhi ya changamoto hizo ni kuipa DP World mamlaka makubwa, kutokuwa na ukomo na vipengele rahisi vya kuuvunja pamoja na kutokutaja manufaa mahusus ambayo Tanzania itayapata kwenye mkataba huo.
“Tumeliwaaa”, ni sehemu ya maneno yaliyotawala sana pia kwenye mkutano huo ambayo Tundu Lissu aliyatamka.
Amewaomba Watanzania wote kutosuburi kamati kuu ya CHADEMA ikae na kutoa msimamo, bali wote kwa umoja wao watoke hadharani kuukataa.
“Tuseme wote kwa pamoja, mama umetukosea sana, futa huo Mkataba. Peleka Azimio Bungeni, Bunge lifute huo Mkataba kwa sababu hauna manufaa yoyote kwa nchi yetu. Kama wewe umehongwa au kuahidiwa kitu na hao waarabu wako utajuana nao mwenyewe, sisi hatutaki” alisema
Amebainisha kuwa kuukataa mkataba huu sio udini wala ubaguzi, bali ni kukataa kuchezewa sababu kwa mkataba huu Rais Samia anatuchezea watanzania.
Ameshangaa kuona bado mabango ya “nani kama mama” yapo barabarani, kwanini watu wanaendelea kumchekea?
Kupambana na mkataba huu inahitajika shughuli kwelikweli kwa sababu wana fedha, wana polisi na wana mbinu chafu lakini watanzania wakiungana kwa mamilioni hawataweza kuwazuia.
Katika hatua nyingine, Lissu ameonya kuwa huenda mkataba huu hautaondolewa wala kupelekwa Bungeni kubadilishwa. Njia pekee itakayobaki ni kumuondoa Rais Samia mwaka 2025 kwenye uchaguzi mkuu kupitia sanduku la kura, uwe mwaka wake wa mwisho kukanyaga Ikulu ya nchi hii.
Pia, hili litaenda sambamba na kudai katiba mpya, na inawezekana mambo haya yote yakafanikiwa.