Kweli Ndugai, Watanzania tunadekeza uvivu mno

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
KATUNI(615).jpg

Maoni ya katuni


Katika ukurasa wa kwanza wa gazeti hili leo kuna habari kuhusu posho za wabunge, lakini ndani yake Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, akielezea kwa hisia kali tabia ya uvivu ya watu wa taifa hili.

Katika habari hiyo ambayo ni sehemu ya mahojiano yake na kipindi cha Dakika 45 cha ITV, Ndugai pamoja na mambo mengine alisema kuwa uvivu, visingizio na kuwa na maneno mengi badala ya kuchapa kazi kwa muda sasa imekuwa sehemu ya maisha ya watu wetu.
Alisema wazi, hakuna taifa lolote duniani ambalo linaweza kupiga hatua za maendeleo kama watu wake hawafanyi kazi.
Uzembe, uvivu na tabia ya kupendelea kupiga domo mwaka baada ya mwaka inasababisha watu wetu kwa maefu kushindwa

kupata ajira, kwa sababu waajiri wengi hupendelea wenye uwezo wa kuchapa kazi na kutimiza malengo. Huu ni udhaifu ambao kama taifa tunapaswa kuungalia na kuutafutia tiba.

Tunakubaliana na Ndugai kwa kiwango kikubwa kwamba kweli ndani ya taifa hili wapo watu wengi ambao wanadhani kuwa uvivu ni jambo la kuendeleza, mara nyingi wakalia maneno, majungu na kushindwa kuchapa kazi, matokeo yake wanakaribisha umasikini si kwao binafsi tu bali hata kwa taifa kwa ujumla.

Katika miaka ya hivi karibuni nguvu kazi kubwa ya taifa hili ikijumuisha vijana zaidi imeamua kuwa wazururaji mijini na hata vijijini; vijana wengi hawafanyi kazi. Uzalishaji mali kwao si kitu cha kuwahangaisha.
Ni dhahiri dunia nzima sasa inakabiliwa na changamoto kubwa za kiuchumi, hali ya maisha imezidi kuwa ngumu si kwa nchi za ulimwengu wa tatu kama Tanzania tu, bali hata zile zilizoendelea na ambazo zilidhaniwa kuwa ziko salama.

Changamoto hizi za kiuchumi zinaweza tu kukabiliwa kwa njia ya kufanya kazi kwa bidii zaidi, kujituma zaidi na kwa kweli kila mmoja kutoka jasho ili ale. Hakuna vya bure tena katika dunia ya leo.

Uchapakazi wa sasa ni wa kiushindani, tija ni lazima iongezeke lakini pia ubora wa kile kinachozalishwa au huduma inayotolewa. Ni kwa kutoka jasho kwa wingi zaidi kunaweza tu kumhakikisha kila mmoja usalama wa mahitaji yake.

Ni bahati mbaya kwamba katika miaka ya sasa vijana wengi, ambao ni nguvu kubwa inayotegemewa, wamejiruhusu kuishi maisha ya ombaomba, kile wanachojishughulisha nacho hakika hakiwawezeshi kukidhi mahitaji yao muhumu na kujiwekea akiba japo kidogo, mtindo huu wa maisha unazidisha mzunguko wa umasikini siku baada ya siku.

Kimsingi taifa letu halina uhaba wa rasilimali, ardhi ni ya kumwaga tena yenye rutuba ya kutosha, pamoja na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi bado tuna maji mengi yanayoruhusu kilimo cha umwagiliaji. Vyote hivi kwa vijana wengi ni kama havipo, maisha yanayoonekana yanawezekana kwao ni kukumbilia mijini kuzurura na hata wanaobakia vijijini hawataki kujishughulisha, kutwa wako vijiweni.

Hakika hatuwezi kusonga mbele kama tabia kama hizi zitaendekezwa na kuachwa kuwa sehemu ya mfumo wa maisha ya watu wetu. Kuna kila sababu ya kuleta mabadiliko, haya ni lazima yaanze na fikra, kwamba si kweli maisha mazuri yanaweza kupatikana

mijini tu; kwamba kazi pekee ambazo vijana wanamudu ni kuendesha uchuuzi wa peremende, soksi mkononi, na bidhaa nyingine ambazo haziwezi kuwasaidia kumudu mahitaji yao muhimu, achilia mbali kuweka akiba.
Ndugai amesema wazi, hakutafuna maneno, kwa bahati mbaya si mara ya kwanza kauli kama hizi zinatolewa na viongozi wa aina ya Ndugai, kinachokosekana sasa ni utayari wa taifa kuchukua hatua chungu ili kuhakikisha kila mtu anatoka jasho ili ale.

Ni kweli nchi hii ni ya kidemokrasia, ni kweli pia kila mtu ana uhuru wa kwenda kokote atakako alimradi havunji sheria, lakini kuendelea kuendeleza uhuru na demokrasia ambayo hajengi wajibu kwa kila raia ni kujidanganya kwamba kuna siku tutafanikiwa kutokomeza umasikini katika taifa hili.

Ni rai yetu kwamba mwaka huu uwe wa mabadiliko, kwa mtu mmoja mmoja kujitambua, lakini zaidi sana serikali kukaza kamba kwa kuhakikisha kwamba taratibu za kisheria na kinanuni zinazingatiwa kwa kila mtu kufanya kazi inayoeleweka. Tukichukua

mwelekeo huo, hakika nguvu kazi inayozurura mchana kutwa itakuwa na manufaa kwa taifa hili na hivyo kusaidia kuvuka ngazi moja ya umasikini kwenda kwenye hali njema zaidi. Tubadilike sasa.

CHANZO: NIPASHE
 

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom