Kwa namna hii ya uanasiasa tuko hatarini

Ngekewa

JF-Expert Member
Jul 8, 2008
7,705
1,288
Tambwe unatulepeka wapi?


Kulwa Karedia



TANGU mwanzoni mwa miaka ya 1992 baada ya kuingia mvumo wa vyama vingi nchini, tumekuwa tukishuhudia wimbi la wanasiasa wachanga kuingia katika siasa kila kukicha na kwa mtindo wa kipekee.
Wengi wao tumeona wamekuwa na mafanikio mazuri katika kutetea matatizo ya Watanzania, lakini wengine wamekuwa mabingwa wa kutoa lugha chafu ambazo zimeshindwa kuwajenga wao na taifa na badala yake zimekuwa hatarishi.
Nimeanza na maneno haya kwa makusudi kwa nia moja tu ya ‘kumtendea haki’ Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Propaganda wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tambwe Hizza kutokana na kauli yake ya isiyo ya kiiungwana aliyotoa mkoani Mbeya wiki iliyopita.
Kauli ya mwanasiasa huyo ambaye alikuwa bingwa wa kutoa lugha za kejeli ambayo hata gazetini siwezi kuaandika dhidi ya CCM wakati huo akiwa na Chama Cha Wananchi (CUF) leo hii tena anataka kuwagombanisha Watanzania baada ya kusahau mauji ya Zanzibar karibu miaka minane iliyopita.
Alikuwa bingwa wa kutoa kejeli na kumbukumbu zetu zinaonyesha katika moja ya mikutano yake ambayo aliwahi kuhutubia kwenye viwanja vya Mwembeyanga, Tandika, Dar es Salaam, Hizza alitamka maneno haya “Sitarudi CCM labda mama yangu awe amekufa”.
Kauli hii ilikuwa nzito ambayo tuliamini wazi kwamba Hizza hatarudia makosa, lakini leo hii amelamba matapishi yake mwenywe baada ya kujiunga na CCM. Baada ya kusota akiwa na CUF na kuona mambo magumu aliamua kukimbilia CCM, kiongozi huyo anaonekana tena kutaka kuibua hisia mbaya ambazo zinaweza kupelekea machafuko ndani ya taifa letu tulivu.
Nasema hivyo kwa sababu wiki iliyopita akihutubia moja ya mikutano ya kampeni za CCM katika uchaguzi mdogo huko Mbeya Vijijini, alitamka maneno yanayoonekana wazi kwamba yasipodhibitiwa yanaweza kuhatarisha usalama wa taifa.
Alisema yeye ndiye aliyehamasisha kundi la vijana wa CUF mwaka 2001 kuandamana kisiwani Zanzibar, mara baada ya uchaguzi mkuu na kusabisha vijana 27 kupoteza maisha kwa kupigwa risasi na Polisi.
Tunakumbuka baada ya mauji hayo ambayo yalilitia doa la umwagaji wa damu taifa, huku aliyekuwa Amiri Jeshi Mkuu, Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, akiwapandisha vyeo askari kadhaa kwa kazi nzuri waliyoifanya baada vurugu hizo.
Hizza alitoa kauli hii kwa nyakati tofauti katika vijiji vya Igalukwa, Mlowo na Owowo Kata ya Isuto, katika kampeni za kumnadi mgombe wa CCM, Mchungaji Luckson Mwanjali.
Kwa mtu yeyote mwenye akili timamu, lazima ajiulize kauli hii imetolewa ikiwa imelenga nini wakati huu ambao tukio hilo lilitokea mwezi kama huu. Kibaya zaidi Hizza bila uoga anasema yeye na viongozi wengine wa CUF walishiriki kuwatia jazba na hamasa vijana hali iliyosababisha wauwe na Polisi. Hii ni kauli ya kijinga ambayo Watanzania wanapaswa kuipuza na kuona kiongozi anasumbuliwa na ‘njaa’ kali ambayo ilimkimbiza CUF.
Huyu ni kiongozi wa aina gani katika taifa huru kama hili? Au ndiyo wanasiasa wanaota kama uyoga mchana na usiku bila kujali maslahi ya taifa? Anasema ujinga wa vijana wale kujitokeza kwenye maandamano hayo bila utaratibu ndiyo chanzo cha kufanya wauwawe. Kauli ya Hizza inaonyeshwa kwamba inaungwa mkono viongozi wa ngazi za juu wa CCM ambao hadi leo hii hatujasikia wanamkemea hadharani au kukanusha kauli hii.
Tunasema kama CCM itaendelea kukumbatia aina ya viongozi kama Hizza, ipo siku ambayo damu itamwagika kwa watu wachache ambao wanaojipendekeza kwenye majukwaa ya kisiasa bila kujali maslahi ya taifa. Hata Watanzania wenzangu watakubalina na mimi kwamba ndani ya CCM imegeuka kuwa shimo la takataka kwa kuchota wanasiasa kutoka kambi ya upinzani kisha kuwapatia vyeo.
Hili halina ubishi, kwani baada ya Hizza kujiunga na CCM kapewa cheo alichonacho hivi sasa, tena kibaya tunaambiwa kitengo cha propaganda ambacho kimekusudia kuwadanganya Watanzania kila kukicha. Tunasikitishwa na kauli hii ambayo bado inagusa hisia za Watanzania hasa waliowapoteza ndugu zao katika mapambano haya yaliyozua gumzo kubwa ndani na nje ya nchi yetu.
Watu walipoteza watoto wao, kaka, wajomba, dada na hata shangazi zao na pengo hilo halijazibika hadi sasa, inakuwaje tunakuwa na viongozi ambao hata uhakika wa elimu yao unatutia shaka kutaka kutuvuruga.
Hapa namnukuu, “Tuliwatia jazba vijana wa CUF kwa takwimu za serikali vijana 27 walipoteza maisha najutia hali hii, nawasihi vijana msidanganywe na wanasiasa wanaotumia ili wapate maslahi yao binafsi”.
Kwa mtu mwenye akili timamu kauli hii haiingi akilini hata siku moja, kiongozi makini hawezi kutonesha kidonda kiasi hiki akitambua wazi athari zake mbele ya jamii.
Ndiyo maana nasema Hizza kauwa? Na kama hakuuwa kwanini anatoa lugha za uchochezi.
Tunasema kauli ya kiongozi mmoja tu kwenye jamii inaweza kutuletea maafa ya kivita kama yaliyotokea Rwanda mwaka 1994 ambako watu karibu 800,000 walipoteza maisha katika vita ya kimbari.
Tunamini wale Wahutu na Watutsi hawakupigana baada ya upuuzi tunaamini kuna watu waliosababisha haya, hasa baada ya rais wao Juvenal Habiryama kuuwawa wakati ndege yake ikikaribia kutua kwenye uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kigali.
Lakini kibaya zaidi napenda kuhoji utendaji kazi wa Jeshi la Polisi nchini juu ya kauli za kijinga kama hizi, kukaa kimya bila ya kuchukuwa hatua zozote. Tunamini suala hili lilikuwa limetosha ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Robert Manumba, kumkamata na kumhoji Hizza juu ya kauli hii.
Kwa jeshi makini hapa ndiyo tulipaswa kuona “mpiga debe” huyu anahojiwa haraka na kukanusha maneno hayo kama alivyoyatamka ili kufuta picha mbaya ambayo inaweza kujitokeza mbele ya jamii.
Tunaamini utendaji kazi wa DCI Manumba na vijana wake ni makini na unaotia matumaini baada ya kupoteza mwelekeo katika miaka kadhaa iliyopita, hivyo tunataka kuona wanachukuwa hatua dhidi ya Hizza. DCI jiulize, nani asiyetambua maumivu yaliyowapata wenzetu mwaka 2001 jamani…tenda haki kwa kila mmoja ili mchango wake mbele ya jamii utambulike.
Kutokamatwa kwa Hizza kuonyesha wazi kwamba yeyote aliyoko ndani ya CCM kukamatwa kwake kunahitaji kibali maalum kutoka kwa vigogo kama tulivyozoea. Hatutaki kuona kila kukicha wanaokamatwa ni wakwapuaji wa simu, cheni wakabaji mitaani lakini watoa kauli za uchochozi wanaendelea kutamba kwenye majukwaa ya kisiasa.
Umefika wakati sasa wa CCM kujisafisha haraka kwa kutoa tamko zito juu ya Hizza ili kurejesha imani kwa wale waliofiwa na hata wananchama wake ambao tunaamini wapo waliochukizwa na kauli hii.
Tunapenda kusema kwamba vyama vya siasa vinapaswa kuwa makini na wanasiasa ambao wanaokena kuwa ‘sumu’ mbele ya jamii baadala ya kukurupuka na kuwapa vyeo ambavyo hatuoni manufaa yoyote katika vita ya kupunguza umasikini.
Namalizia kwa kusema, Tambwe Hizza umetumwa na nani katika hili? Hatutaki utuletee machafuko yasiyokuwa na msingi wowote katika taifa lenye utulivu, amani na mshikamano.
 
Back
Top Bottom