Kupima moyo bure hosp ya aga khan dsm

MIUNDOMBINU

JF-Expert Member
Apr 14, 2010
465
96
by.:Fredy Azzah

MAMIA ya wananchi jana walimiminika katika Hospitali ya Aga Khan Dar es Salaam (AKHD), kupima magonjwa ya moyo na kuelimishwa juu ya athari na namna ya kujikinga na ugonjwa huo.

Mapema mwezi huu, Mwenyekiti wa madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo Kanda ya Mashariki, Dk Mustaafa Bapumia, alitangaza kampeni ya siku mbili ya kupima na kutoa elimu juu ya magonjwa ya moyo ambayo ilianza jana kwenye hospitali hiyo.

Tangu saa 2:00 asubuhi hadi 6:00 mchana jana hiyo zaidi ya watu 300 walikuwa wamefika hospitalini hapo kupimwa matatizo ya moyo.

Jana hiyo Bapumia ambaye pia ni Mganga Mkuu wa magonjwa hayo katika hospitali ya Aga Khan Dar es Salaam , aliliambia Mwananchi kuwa wengi wa watu waliojitokeza ni wale ambao tayari wanajijua kuwa wana matatizo hayo tofauti na matarajio yao ya kupata wananchi wasiojua afya zao.

“Watu wengi tuliowapokea leo ni wale ambao tayari wanajitambua kuwa wana matatizo ya moyo, wengine walikuwa wakitibiwa Amana na katika hospitali nyingine hapa jijini na mikoani,” alisema Bapumia na kuongeza:

“Tumewapokea wote na kuamua kuwafanyia vipimo vya ECG, (kipimo cha kuangalia mapigo ya moyo, matundu katika moyo na matatizo mengineyo), pia kuna watoto wadogo tumewaona, na wagonjwa wengine wameletwa hapa wanatumia baiskeli za wagonjwa, tunaendelea kuwahudumia wote kwa wakati,”.

Bapuma alisema timu ya madaktari na wauguzi 23 ikiongozwa na yeye mwenyewe itatoa huduma hizo za vipimo na elimu kwa wagonjwa wote waliofika katika hosptali hiyo kwa muda uliopangwa.

Kwa mujibu wa Bapumia, matatizo ya moyo yanawakabili zaidi ya asilimia 50 ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 60.

“Tatizo la shinikizo la damu (BP) linawasumbua watu wengi, lakini tunaangalia sana ukimwi na malaria, watu wengi wanasumbuliwa na ugonjwa huu, lakini hawajijui na wakija kugundua tatizo linakuwa tayari limekuwa sungu,” alisema mganga huyo.

Baada ya kampeni hiyo kufanyika jana, awamu ya pili itakuwa Mei 8 mwaka huu hospitalini hapo kuanzia saa 2:30 asubuhi mpaka saa 8:00 mchana.

Alisema pamoja na wagonjwa wa moyo wengi kuwa na ugonjwa huo kwa kurithi , lakini watu wanaotumia sigari na pombe kwa wingi wako hatarini zaidi kupata matatizo hayo.

Alisisitiza kuwa, lengo lao ni kuwaona wale wananchi ambao hawajajitambua afya zao na kuwa wale ambao tayari wanazijua afya zao, waendelee na madaktari wao.

Naye Dk Wilfred Kaizirege ambaye ni daktari katika hospitali hiyo aliitaka jamii kuwa na mazoeya ya kupima afya zao mara kwa mara ili kuepuka garama kubwa za kutibu matatizo ya moyo.

SOURCE:WWW.MWANAINCHI.CO.TZ
 
Back
Top Bottom