Kuharunika, kugehazika, kuyudaika, kusimonika na kuyezebelika

Kuharunika, kugehazika, kuyudaika, kusimonika na kuyezebelika

Rosh Hashannah

JF-Expert Member
Joined
Sep 13, 2017
Posts
3,415
Reaction score
2,043
(sehemu I)

Ni vitu gani hivi? Hivi si vitu bali virusi vya ajabu vinavyoupelekesha Ukristo katika karne hii na mwongo huu. Usihangaike nitakueleza nawe utavitambua kwa wepesi wa macho ya nyama. Wala hakutahitajika darubini kali kuvibaini. Punde tu utavielewa kikamilifu kabisa. Kama unavyo mwenyewe utatambua dalili ulizonazo, matatizo yatabaki mawili tu, dawa ya kujiponyea na kinga ya kuwakingia waamini wanaochipukia. Zaidi ya hayo, virusi hivyo vitabainika vyema kwa vile unawafahamu sana wahusika wa Kibiblia: Haruni, Gehazi, Yuda Iskariote, Simoni mcheza mazingaombwe na malkia Yezebeli. Kwa mada hii napenda kukusomesheni na kukutafakarisheni Kut 32:1-35, 2Fal 5:1-27, Lk 22:1-6, Mdo 8:9-25 na 1Fal 21:1-29 mtawalia.

Kut 32:1-35 ni kisa cha uasi wa Israeli kwa ndama wa dhahabu. 2Fal 5:1-27 ni kisa cha Naamani na zawadi zake nono. Luka 22:1-6 ni kisa cha usaliti wa Yuda Iskariote. Mdo 8:9-25 ni kisa cha Simoni mcheza mazingaombwe. 1Fal 21:1-29 ni kisa cha malkia Yezebeli kumuua Nabothi kwa ajili ya shamba lake dogo la mizabibu.
Nivumilie. Makosa waliyotenda watu hao ndio nitakayoyaongelea kama virusi vinavyoupelekesha Ukristo leo. Si jambo la bure mifano ya kushangaza kuripotiwa kwenye Biblia. Kila kitu ndani ya Biblia kimekusudiwa kisomwe kwa nia maalum. Mungu wetu si chizi eti afanye kitu kisicho na lengo takatifu. Makosa ya watu wa kale yaliandikwa yawe masomo kwetu kusudi tusitumbukie katika makosa ya aina hiyo hiyo (1Kor 10:8). Kumbe, tufumbuane macho ili tusiangamie kiholela. Kama tumepatwa na virusi hivyo, tujisahihishe haraka. Nawaombeni sana katika mambo ya dhambi tuitangulize alahaula. Basi, twende hatua kwa hatua.

Kuharunika
Katika simulizi la ndama wa dhababu, mhusika mkuu ni Haruni aliyeshikilia ukubwa pale Musa alipokwenda kuonana na Mungu mlimani. Jambo hili limeelezwa vizuri katika Kut 32:1-35. Tunasimuliwa, Waisraeli walipoona Musa anakawia kurudi walimshawishi Haruni awatengenezee Mungu wa kumwabudu. Pasipo kupima mambo na kusali, Haruni akakubali kichwa kichwa tu. Akaitisha vikuku vya akina mama akaviyeyusha na kuwatengenezea watu ndama wa dhahabu na kuwaruhusu waiserebukie na kuiabudu kama Mungu wao. Mkasa huu wa mtu mkubwa kufanyizwa kosa kutokana na kuelekezwa na anaowaongoza ndiyo kirusi ninachokiita kuharunika.

Haruni alipaswa kuangalia akili ya kuambiwa angechanganya na yake, yaani alipaswa apime vizuri alichopendekezewa na anaowaongoza. Yeye hakufanya hivyo, badala ya kuongoza aliongozwa. Kama kiongozi wa kiroho alipaswa kumuuliza Mungu afanye nini hapo kwa sababu alitanzika. Ilimpasa asali kusudi awajibu na kuwaelekeza watu inavyotakiwa. Kinyume chake, hakufikiri kwa kujitegemea, hakumuuliza Mungu wala hakusali akakurupuka kufuata matakwa ya watu waliompa pendekezo la nini afanye. Narudia. Kutokupima mambo hivyo na kukubali kufanya alichopendekezewa tu ndiko ninakokuita kuharunika. Haruni aliharunika.
Musa aliporudi kutoka mlimani na kumkuta Haruni ameharibu mambo alishangaa mno. Kweli aliyakuta mambo yameharibika kwa watu kumwacha Mungu wa kweli na kuserebukia na kuiabudu ndama wa dhahabu alimuuliza Haruni swali gumu: “Watu hawa wamekufanya nini hata ukaleta dhambi kuu hii juu yao?” Kwa maneno mengine swali hili lilikuwa, “Kaka Haruni watu hawa wamefauluje kukudanganya wewe kiongozi mzima hata wewe kufanya walivyotaka wao badala ya wewe kusali na kujipatia jawabu zuri la kiroho hata kuwasaidia kubaki na imani ya kweli? Wamekulisha nini au wamekupa nini hata ukasahau nafasi yako ya uongozi?
Kifupi, kwa swali hilo Haruni hakuwa na jibu lenye mashiko bali alijikanyagakanyaga tu. Jibu lake lilionesha utoto wake mwenyewe. Alisema, “Hasira ya bwana wangu isiwake: wewe unawajua watu hawa, ya kuwa wamejielekeza kwa mabaya. Maana waliniambia, ‘Katufanyie miungu, itakayokwenda mbele yetu kwa maana mtu huyo Musa, aliyetutoa katika nchi ya Misri, hatujui yaliyompata.’ Nikawaambia, ‘Mtu yeyote aliye na dhahabu na aivunje,’ basi wakanipa, nami nikaitupa ndani ya moto, akatoka ndama huyu.” Kwa jibu hili, Haruni hakusema lolote isipokuwa kujisema kwamba alikuwa mpumbavu mkubwa. Alizungukazunguka tu akiona aibu kukiri ujinga wake mwenyewe.

Tusemeje sasa? Tuseme ifuatavyo: Leo hii WAKLERI KADHAA wameharunika. Walei wanasema hivi nao wanafanya tu. Akili ya kuambiwa hawachanganyi na yao. Ndipo wanachukua vikuku vya wanawake, ndiyo pesa, na kutengeneza ndama wa dhahabu wanaoabudiwa na watu siku hizi.
Walei wamewaambia, “Tuna laana tufanyieni ibada za kuvunja miti ya ukoo na kutuondolea laana,” wakleri wamekubali wanafanya kama walivyoambiwa. Wameharunika na kusahau kabisa kwamba habari za kulaaniwa kwa watu si mafundisho ya Kanisa Katoliki.
Walei wamewaambia, “Tuna maradhi mengi tufanyieni makongamano ya maombezi na uponyaji, tupone kwa njia za mkato na fasta,” wakleri wamekubali wanafanya kama walivyoambiwa. Wameharunika na kusahau kabisa kwamba uponyaji haufanyiki kwa matamasha. Yesu, Bwana wetu, hakufanya hivyo na wala sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa haiendi kwa namna hiyo. Wamesahau kwamba kufanya miujiza kwa matamasha si mafundisho ya Kanisa Katoliki isipokuwa uongo wa makanisa “private” wanayopiga pesa za wajinga ndio walio kwa kuwafanyia miujiza ya kisanii.

Wamesahau wamisionari walipotukuta na maradhi walikazana kujenga zahanati, vituo vya afya na hospitali, kinyume chao, wakleri Waafrika wanakazana kufanya makongamano ya uponyaji kwa maombezi. Kifupi, Kanisa letu limeshuka chini. Inasikitisha, yaani Kanisa Katoliki pamoja na zahanati, vituo vya afya, hospitali na wataalamu wake linakopi ujinga wa makanisa yasiyo hata na kisanduku cha dawa za huduma ya kwanza (first aid kit).

Walei wamewaambia, “Tuna matatizo ya ufukara tufanyieni ibada za kutupatia mafanikio kwa njia nyepesi ya kukemea umaskini na kuamuru kwa maneno watu tupate ajira, magari, nyumba na kadhalika kwa kusali tu,” wakleri wamekubali wanafanya kama walivyoambiwa. Wameharunika na kusahau kabisa kwamba “injili ya mafanikio pasipo kufanya kazi” si mafundisho ya Kanisa Katoliki. Wameharunika hata kukubali akili nyepesi ya Kinjikitile ya kutatua tatizo gumu kwa maneno matupu. Kinjikitile aliwaaminisha watu kwamba risasi zingegeuka maji kwa kuzitamkia tu, “MAJI, MAJI, MAJI, MAJI!”

Maskini! Wamesahau wamisionari walipotukuta na ufukara wa kunuka walikazana kutufundisha kilimo na ufugaji, kinyume chao, wakleri Waafrika wanakazana kufanya makongamano ya kuondoa umaskini wa watu kwa maombezi na makemeo ya “UMASKINI ONDOKA!” “UMASKINI ONDOKA!” “ROHO YA UMASKINI ACHILIA!” “ROHO YA UMASKINI ACHILIA!” Kifupi, Kanisa letu limeshuka chini. Tunajilisha ujinga na akili ya Kinjikitile. Inasikitisha, yaani Kanisa Katoliki pamoja na shule, vyuo na wataalamu wake linakopi ujinga wa makanisa ya “private.”
Walei wamewaambia, “Tuna matatizo ya ajira, ujane, kutopata watoto, kutoolewa na kadhalika tufanyieni ibada kali matatizo hayo yayeyuke kwa miujiza,” wakleri wamekubali wanafanya kama walivyoambiwa. Wameharunika na kusahau kabisa kwamba miujiza kumbakumba haikuamriwa na Yesu na hayo wanayong’ang’ania walei yafanywe si mafundisho ya Kanisa Katoliki.

Walei wamewaambia, “Kuna walozi na wachawi angani, hewani na katika mitaa yetu tuzindikieni anga na turuhusuni tuwe tunasali usiku wa manane tuzuie ndege za wachawi zisiruke,” wakleri wamekubali wanafanya kama walivyoambiwa. Wameharunika na kusahau kabisa kwamba miujiza kumbakumba haikuamriwa na Yesu na hayo wanayong’ang’ania walei yafanywe si mafundisho ya Kanisa Katoliki.

Katika yote, kinachosikitisha zaidi katika kuharunika ni kwamba hakuna “Musa” wa kuwashtusha walioharunika. Hakuna “anayemusika.” Hakuna mwenye uwezo wa kuwauliza walioharunika, “Watu hawa wamewafanya nini hata mkaleta dhambi kuu hii juu yao?” Kwa maneno mengine hakuna anayewauliza, “Enyi akina Haruni watu hawa wamefauluje kuwadanganyeni ninyi viongozi wazima hata ninyi kufanya walivyotaka wao badala ya ninyi kusali na kujipatia majawabu mazuri ya kiroho hata kuwasaidia kubaki katika imani ya kweli ya Kanisa Katoliki? Wamekulisheni nini au wamekupeni nini hata mkasahau nafasi zenu za uongozi?

Masomo ya miaka saba Seminarini, na wengine kupewa fursa ya kupata masomo ya juu katika vyuo vikuu bora, yalikusudiwa wakleri wasiharunike. Lakini loh, wanavyoharunika inatufanya watu tusione maana ya kuwa na Seminari Kuu wala maana ya mkleri kupelekwa ng’ambo kwa masomo ya juu. Lakini balaa, baba lao, ni kule kushindwa kwa baadhi yao kufundisha wenyewe hata kuwakaribisha viongozi wa “makanisa ya private” wawafundishie kondoo wao! Ha! Haiingii akilini! Hata kufundisha kunabinafsishwa!

Nimalizie kwa mfano bayana zaidi. Kuharunika ndiko kunakofanya Karismatiki wasikemewe na yeyote hata kama wanafanyiza mambo kinyume kabisa na maagizo ya Yesu Kristo, Bwana wetu (rej. Mt 6:5-8) na kinyume kabisa na Maandiko Mtakatifu (rej. 1Kor 14:26-40). Hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba wakleri wanashindwa kujua kwamba kwa vitendo vyao Karismatiki ni wapinga Kristo na wapinga Maandiko Matakatifu kwa viwango vipi. Kushindwa huko ndiko kunakowafanya siyo tu wasiwakemee bali hata wao wenyewe wawemo ndani. Lakini “poa”, nitalijadili jambo hili katika makala rasmi, makala itakayokwenda kwa kichwa cha “MAKONGOMANO YA AIBU NA MAKONGAMANO YA HAIBA.” Humo nitaeleza jinsi sisi viongozi tulioharunika tunavyoachilia au kushadidia “makongamano ya kulofazana” huku tunamsingizia Roho Mtakatifu kuyadhamini.

Ndipo sisi tunapiga kelele, kutoana mapepo na eti kufunguliana kutoka kwenye laana na uchawi wakati wenzetu Ulaya, Marekani na Asia wanafanya makongamano haiba, makongamano ya kiuchumi kupanga mikakati mikubwa ya kibiashara na kiuchumi. Nadhani katika mwezi huu wa Juni tumeshasikia habari ya makongamano ya kiuchumi ya Shagri-La, ya St. Petersburg, ya Qatar na kadhalika. Sasa linganisha makongamano hayo na yetu ya kulofazana katika majimbo, dekania au parokia na kadhalika yanayofanyika katika miezi ya Mei, Juni na Julai kila mwaka. Makongomano yetu na yao ni tofauti kama ya kati ya kaniki na kanga au kati ya usiku na mchana. Katika makongamano yetu, eti akina baba na wake zao na watoto wao na wajukuu zao, makleri na watawa na walei wao wanakusanyika kumlilia Mungu awajalie ajira, awaondolee ujane, awapatie wachumba, awaondolee umaskini, awafungue kwenye vifungo vya nuksi, “awatoe mapepo”, “awatoe majini”, awaondolee madeni na kadhalika. Ha! Aibu! Yaani hatufanyi mikakati ya pamoja ya kutumia akili na rasilimali zetu! Kwa namna hii hatuendi mbele bali tunapiga mbio kurudi nyuma. Matokeo yake Waafrika hatutaamka kamwe (ng’o) na kwa namna hiyo tutakae mkao wa kutawaliwa na kuombaomba milele.

Kugehazika
Nabii Elisha alikuwa na kijana wake aliyekuwa akimsaidia kazi. Baada ya Naamani kuponywa ukoma wake, Naamani alitaka kumzawadia nabii Elisha pesa vipande elfu tatu na mavazi mawili ya sikukuu. Elisha alikataa akisema aliyemponya ukoma ni Mungu na si yeye nabii. Alibaini vitu vile vingelingana na malipo ya huduma aliyoitoa. Kinyume chake, kijana Gehazi aliona kukataa vitu vile vizuri ulikuwa ujinga wa hali ya juu. Moyoni mwake aliona nabii angelipokea vitu vile kama malipo ya kufanikisha muujiza. Basi, akanuia yeye kuvichukua vitu vile alivyokataa nabii.
Basi, Gehazi alimtoroka Elisha, akamfukuzia Naamani njiani na kumdanganya kwamba nabii Elisha alighairi na hivyo alikuwa anavitaka vitu vile kwa vile huko nyuma amefikiwa na manabii wenzake wawili. Naamani akatoa vipande elfu sita na mavazi yale ya sikukuu wakati ilikuwa uongo mtupu. Gehazi akajipatia mali kwa ulaghai. Kutamani na kujipatia mali katika huduma za Mungu ndiko ninakokuita kugehazika. Gehazi alitaka huduma ya kinabii ilipiwe na siyo kutolewa bure. Kisa hiki kimesimuliwa vizuri katika 2Fal 5:1-27.
Tusemeje sasa? Tuseme ifuatavyo:
Siku hizi wakleri wengi wanatoa huduma za kiroho wakidai namna ya malipo. Wamegehazika. Wakitoa sakramenti ya Ubatizo, lazima aliyehudumiwa atoe asante. Wakitoa sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa, lazima aliyehudumiwa atoe asante. Wakitoa sakramenti ya Ndoa, lazima waliohudumiwa watoe asante. Wakiadhimisha misa, lazima waliohudumiwa watoe asante. Kifupi, hakuna tena kufanana na Elisha, yaani kutoa huduma bure kama alivyopendekeza Yesu (Mt 10:8). Kanuni inayojengeka sasa ni “Sakramenti au huduma ya kiroho kwa mshiko.” Inakuwa kana kwamba tunaishi falsafa ya “Hapendwi mtu, ila pochi.”
Nimepata habari ya ziada ya kusikitisha, eti kwamba mapadre na maaskofu wengine wakitembelea parokia au taasisi fulani, lazima “washikwe mkono” kwa bahasha nono. Jambo hili linawakera sana waamini. Kwa nini? Kwa sababu limeongeza michango katika Kanisa Katoliki. Lakini hapo hapo pamefungulia mlango uovu mwingine. Karismatiki wameona fursa ya kujipenyeza na mafundisho yao ya kizushi. Wamepatiwa uwezekano wa “kununua njia” ya kuingilia mahali na kupandikiza uovu wao. Ni hivi, kwa kuwa Maaskofu na mapadre wanapenda sasa wakitoa huduma “washikwe mkono kwa bahasha nono”, huwa wanaandaa bahasha hizo nono na kuwakabidhi na hivyo kuwafunga macho na midomo waweze kujieneza jimboni au parokiani pasipo kusahihishwa wala kukemewa na mtu yeyote. Alahaula, ni kanuni ile ile ya “Penye udhia penyeza rupia.” Kumbe, ni kugehazika kunakosababisha viongozi wanunulike na vinywa vyao vifumbike. Asalaleh!

Kuyudaika
Hapa tuwaache akina Yuda kedekede waliosimuliwa katika Biblia Takatifu, tumchukue Yuda mmoja tu, Yuda Iskariote. Kwa kituko alichokifanya ninajenga msamiati wa kuyudaika. Kisa hiki kimesimuliwa vizuri katika Lk 22:1-6. Yuda Iskariote aliishi na Yesu kinafiki tu. Yeye alikuwa anawinda kutengeneza pesa tu. Mkoba aliopewa autunze kama mhasibu akawa anadokoa vilivyokuwa vikitiwa ndani yake. Kila jambo alililotazama alilitazama kwa macho ya kutengeneza pesa ajinufaishe yeye. Ndiyo kisa Yesu alipokuwa anapakwa mafuta ya gharama kubwa, akatafsiri kama hasara kwani yangeuzwa kungelipatikana pesa nyingi za kuwasaidia maskini. Lakini mwinjili anasema hilo alilisema kiunafiki tu, wala hakuwa anawawazia maskini kwa dhati isipokuwa kinyume chake alikuwa akitamani mafuta yangeuzwa zikapatikana pesa nyingi ambazo zingeliingizwa kwenye mfuko yeye akapata nafasi ya kuiba pakubwa (Yn 13:4-8).
Kutokana na uchu wa kipato binafsi, mwishoni mwa mambo, Yuda Iskariote aliona hata akimuuza Yesu mwenyewe atapata kitu ndipo akamuuza kweli. Ndugu zanguni, huko kuishi kanisani na kutenda kazi kwa kuwinda pesa ili mtu ajinufaishe, unafiki na uroho unaomfikisha pahala pa mtu kumwona Yesu kama bidhaa ya kuuzwa ndiyo ninayoiita kuyudaika.
Tusemeje sasa? Tuseme ifuatavyo: Siku hizi, si wakleri haba walioyudaika. Wanaweza kuwekwa katika nafasi kubwa au pengine hata ndogo ambapo watakuwa wanafanya kazi wakipiga hesabu za jinsi ya kujipatia kitu tu. Mali wanazokadhiwa wanaweza kudokoa na jambo lenye kuuzika wanaweza kuuza. Aghalabu, wanakuwa na jicho la kunyemelea fursa za kutengeneza pesa katika hayo hayo wanayosema wanayatumikia bure. Jambo hili linawafanya walioyudaika wawe katika fikra endelevu za kutafuta jinsi gani ya kumuuza Yesu au Ukristo na wao kujitajirisha binafsi. Ndipo hapo wanapoishia “kuibiadhisha” au “kubiasharisha” injili kwa uongo na ulaghai mwingi.
Hata hoja ya kuipokea karismatiki mahali husema kwamba kiongozi mhusika ameyudaika maana utasikia, “karismatiki wanafaa kwa sababu wanapokuwapo wanaongeza utoaji wa sadaka na zaka”. Ebo! kuyudaika huko! Tangu lini Yesu alisema, “Nendeni dunia kote kwa kipaumbele cha kuchangisha watu sadaka na zaka?” Kumbe, ndugu zanguni, kuyudaika ndiko kunakoibusha kashfa nyingi katika ofisi kubwa kubwa kanisani ikiwa pamoja na benki ya Kanisa huko Vatikano.
Mzee wenu Pd. Titus Amigu
 
(sehemu II)

Kusimonika
Simoni, mcheza mazingaombwe, alitamani kupata karama ya Roho Mtakatifu kwa kuinunua kutoka kwa mitume. Alitaka kuwa na uwezo na mamlaka juu ya watu kwa kigezo cha kuwa na karama ya pekee. Mtume Petro hakuingia katika kishawishi cha kumuuzia Simoni karama. Badala yake alikataa kuuza karama. Huko kutaka kupata uwezo au karama ya Roho Mtakatifu kwa kununua au “kuzungumza” na mwenye uwezo wa kumpatia fulani kipawa cha Roho Mtakatifu ndiko ninakoita kusimonika. Kisa hiki kimesimuliwa vizuri katika Mdo 8:9-25.
Tusemeje sasa? Tuseme ifuatavyo: Kanisani mwetu wapo watu wanaotamani kupata karama mbalimbali za Roho Mtakatifu. Hao wanawazungukia zungukia wakubwa wanunue. Ndipo hapo viongozi wasipokataa kishawishi hicho wanaweza kuwapatia watu hao wanachotaka kwa “proposal”, kwa upendeleo, a.k.a kwa undugu, “ndugunization.”
Hii maana yake ni kwamba badala ya kumwacha Roho Mtakatifu awagawie karama anaowataka mwenyewe, wanadamu wanamwongoza Roho Mtakatifu awagawie watu karama, hasa ya uongozi, kwa wale wanaowataka wao. Hapa ndipo panapoingia kuteuana au kuchaguana kwa ukanda, ukabila, utaifa na kadhalika. Lakini ni hapo hapo watu wanapochafuana, kusengenyana, kukashifiana, kuchongeana na kadhalika ili fulani akose na badala yake apate fulani wanaomtaka wao. Kusimonika ndiyo mzizi wa ukabila, upendeleo, majungu, kashfa na kuchafuana mintarafu vyeo na mamlaka kanisani. Ndivyo inavyofikia Roho Mtakatifu kufadhaishwa. Lakini ni aibu na dhambi kubwa kumfadhaisha Roho Mtakatifu katika ugawaji wa karama zake kwa wale awapendao.
Hayo tisa, kumi ni kwamba kutoka kusimonika zinazaliwa dhambi za aina yake tatu. Mosi, baadhi wanaoona mambo yamekaa ovyo ovyo kanisani, wanajisemea mioyoni mwao, “Isiwe taabu!” wanajiundia makanisa yao na kujipa wenyewe vyeo wanavyotaka: unabii, utume, uchungaji, uaskofu na kadhalika. Uamuzi huu ndio unaozalisha makanisa kila kukicha na hali kadhalika viongozi wa kujitangaza wenyewe. Kwa nini wanafanya hivyo kirahisi? Ni kwa sababu “Kufa kwa mdomo, mate kutawanyika.”
Pili, wengine ndiyo hivyo wanakamatana na wakubwa wanaoweza kuuza karama na hivyo kusaidiwa kuingia bwawani mara maji yanapotibuka mahali hivyo kuponywa kwa kuwapitia wengine. Kwa mfano wa muujiza wa kutumbukia bwawani Bethesda (Yn 5:1-7), parokia, taasisi au majimbo yanapokuwa wazi na kuhitajika kuwapata watu wa kuongoza sehemu hizo, maji huwa yametibuka na mwenye mtu wa kumsaidia kutumbukia bwawani hutumbukizwa mara wakati yule asiye na wa kumsaidia kutumbukia hubaki pembeni akipitwa na watu miaka nenda rudi hadi anafia hapo hapo pembeni mwa bwawa.
Tatu, wengine hujaribu “kumboost” Roho Mtakatifu kwa kwenda kutafuta dawa au hirizi kwa waganga wa kienyeji kusudi wateuliwe au wachaguliwe kwenye vyeo vya kidini, yaani sawa kabisa na wanavyofanya baadhi ya wanasiasa hapa kwetu Afrika.

Kuyezebelika
Mwishowe tutafakari kuyezebelika. Yezebeli alikuwa malkia wa nguvu wa Israeli, mke wa mfalme machachari kabisa aliyeitwa Ahabu. Yezebeli alipenda mali. Alipenda pia kujipura kama mwanamke yeyote anavyopenda. Lakini pamoja na hayo alipenda sana kuambiwa mambo mazuri hata kwa kudanganywa. Masikio yake yalikuwa na njaa na kiu isiyoisha ya kuambiwa maneno ya kupendeza na kusuuza moyo na mwili. Yaani hakuona ajizi kuvikwa kilemba cha ukoka. Kwa kukidhi hitaji hili la kuambiwa mambo mazuri mazuri, aliwaajiri manabii 400 ambao alikuwa akiwalipa mshahara kwa kumtabiria alivyotaka. Ni manabii hao aliowachinja Eliya pale mlimani Karmeli baada ya kuwashinda katika shindano la kuchomesha sadaka za kuteketezwa pasipo kuwasha moto wa kawaida (1 Fal 18:20-40).
Kuishi kwa mtindo huo wa malkia Yezebeli ndiko ninakoita kuyezebelika. Aidha katika kupenda kwake sana utajiri alimfanyia mumewe mpango wa kumuua Nabothi wachukue shamba lake la mizabibu. Mfalme Ahabu alifanyiwa mpango huo nao wakafaulu kulipata shamba la Nabothi, dhambi ambayo Mungu aliiona na kuwaadhibu Ahabu na mkewe, Yezebeli. Kisa hiki kimesimuliwa vizuri katika 1Fal 21:1-29.
Tusemeje sasa? Tuseme ifuatavyo: Hapa Afrika, siku hizi walei wetu wengi na kwa namna ya pekee akina mama wengine wanayezebelika. Kuna msako mkali wa mali, hata wale walio matajiri tayari. Watu wetu wengi, siku hizi wanataka kuambiwa maneno mazuri tu na wako tayari kuwatunza na kuwapa mapesa watu wanaowatimizia matamanio ya namna hiyo. Kwa namna hii wanajichagulia watu wa kuwahubiria yale wanayopenda kuyasikia tu (2Tim 4:3-5). Hawawataki kabisa watu wanaohubiri habari za mateso. Hawataki kusikia chochote juu ya fumbo la mateso hata kama kwenye Biblia imesemwa wazi kwamba tutapata uzima wa milele kwa kupitia mateso mengi (Mt 10:18, Lk 23:31, Mdo 14:22 na kadhalika). Wanaowaambia wakiwa wajane watawapatia waume wenye mali zao, wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao.
Wanaowaambia wakiwa maskini watawapatia mali, magari, nyumba na utajiri kwa miujiza wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao. Wanaowaambia wakiwa wagonjwa watawapatia afya na uponyaji kwa njia ya mkato kwa maombezi, kulialia, kufunga na kukesha wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao. Wanaowaambia wakiwa na matatizo yoyote watapata suluhu wakinunua keki, leso, chupi, maji, fagio za upako na kadhalika, wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao. Wanaowaambia wakiwa na tatizo la umaskini watawapatia utajiri kwa kuwajambia usoni wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao. Wanaowaambia wakiwa na matatizo watawapatia suluhu kwa kunywa maji walioga wao wachungaji, wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao.
Wanaowaambia wakiwa hawajaolewa watawapata wachumba kwa upepo wa kisulisuli wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao.
Wanaowaambia wakiwa na matatizo ya “kukataliwa” wataondolewa roho hiyo mbaya kwa kunyonywa matiti, wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao.
Wanaowaambia wakitaka kwenda mbinguni wanunue tiketi za kuendea huko kwa pesa tasilimu wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao. Wanaowaambia wakiwa na tatizo la umaskini watapata baraka kwa kuvaa chupi zenye upako wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao.
Wanaowaambia wakiwa na majumbani kwao watapata baraka wakikomboa ardhi zao kwa baraka ya udongo wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao.
Wanaowaambia wakiwa na matatizo ya mikosi watapata baraka wakikomboa nyayo zao wanawafurahia na kuwatumikia kwa pesa na michango yao. Ha! Kuyezebelika kunawapeleka watu kwenye vitendo vya mataahira. Kama mnanipata uzuri, kuyezebelika ndiko kunakowafanya wenye imani henamu wawe machangudoa wa imani, wakitoka katika kanisa hili hadi lingine.

Wanakanisa Tumegawana Dhambi
Kuharunika, kugehazika, kuyudaika, kusimonika ni hasa dhambi za viongozi wa Kanisa wakati kuyezebelika ni hasa dhambi ya walei. Kwa tofauti hii, si kwamba wakleri ndiyo pekee watakaoliangamiza Kanisa Katoliki bali walei vile vile. Mchango wao una uzito vile vile kwani virusi hivi vimezusha mzunguko mshenzi. Kuharunika kunazaa kugehazika, kugehazika kunazaa kuyudaika, kuyudaika kunazaa kusimonika na yote hayo yanazaa kuyezebelika na halafu kuyezebelika kunazaa kuharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika. Ni kweli wanakanisa tumegawana dhambi lakini mapato yake ya jumla ni uharibifu wa imani mtambuka.
Naweka kesi hii mezani. Mtu unajiuliza hivi kiongozi anafikia kuikubaki Karismatiki katika eneo lake na kishapo kulialia inapomharibia mambo? Jibu lake aliharunika, akagehazika, kuyudaika na kusimonika na wale walimfikisha hapo wameyezebelika. Lakini hii ndiyo ajabu ya kukaribisha ugonjwa halafu baadaye kulialia kwa sababu ya maumivu yake. Ni ajabu ya kukaribisha ugonjwa na kisha baadaye kuanza kutafuta dawa ya kutibia. Kosa hili lilifanyika kwa mara ya kwanza mwaka 1975 ambapo Baba Mtakatifu Paulo VI aliharunika. Tulijiruhusu tuchezee wembe, na sasa unapotukata eti tunaulizana kwa nini ni mkali hivyo! Ebo! Hapa hata mimi nachelea kuujibu “ushangazi” huu.
Mzee wenu Pd. Titus Amigu
 
(sehemu III)

Makleri WAKISHAharunika, Kugehazika, Kuyudaika na Kusimonika
Makleri wakishaharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wanakuwa mapooza. Mtu aliyepooza huwa hana nguvu. Huweza hata kukosa nguvu ya kichwani na mwilini. Hivyo huweza kushindwa kufikiri, kuona, kusema seuze kutenda. Kifupi, waliopooza hawezi kufanya lolote. Unaweza kuchukua vitu vya mtu aliyepooza asiweze kusema chochote maana hana nguvu ya kukukabili wewe unayevichukua. Aliyepooza anaweza kuona simu yake inachukuliwa asiweze kuzuia wala kwa kupiga kelele wala kwa kumfukuza mwizi. Aliyepooza anaweza kuona pesa yake ikichukuliwa na kibaka asiwe kuzuia wala kwa kupiga kelele wala kwa kumfukuza kibaka. Aliyepooza anaweza kuona mkewe au mumewe akichukuliwa asiweze kuzuia wala kwa kupiga kelele wala kwa kumfukuza mgoni wake na kadhalika.
Ndiyo kisa makleri wakishagueka mapooza hawawezi kupinga chochote wala kwa maneno wala kwa vitendo. Wameshakosa nguvu. Mkasa huu ukishatokea, Kanisa zima linaingizwa hatarini kupoteza mustakabali na hadhi yake. Aidha, walei huingia katika hatari kubwa mno ya kupotea mbugani. Ni ukweli ule ule aliosema Yesu kwamba apigwapo mchungaji, kondoo hutawanyika kwa vile hukosa mtu wa kuwaongoza. Yesu Kristo alisema watu wasipayukepayuke wanaposali (Mt 6:5-8). Kinyume chake, watu watapayuka payuka mbele ya makleri wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Yesu Kristo wanayesema wanamfuata aidha kujiita “Alter Christus.” Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia alichosema Kristo maana wao ni Kristo wengine na mtu aliye Kristo hawezi kumpinga Kristo Yesu.

Mfano mwingine. Yesu Kristo alisema watu wasiwaige wanaopayukapayuka (Mt 6:5-8). Kinyume chake, watu watawaiga lakini wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Yesu Kristo wanayesema wanamfuata aidha kujiita “Alter Christus.” Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia alichosema Kristo maana wao ni Kristo wengine na mtu aliye Kristo hawezi kumpinga Kristo Yesu.

Mfano mwingine tena. Maandiko Matakatifu yanasema ikiondokea watu kunena kwa lugha wanene wawili au watatu, si zaidi, tena mbele ya mfasiri vinginevyo wapagani watasema ni wendawazimu (1Kor 14:26-28). Kinyume chake, watu watanena hata mambo yasiyoeleweka lakini wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Biblia wanayosema wanaisoma na kuifundisha. Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia kinachosema Maandiko Matakatifu maana wao ndio walimu waliosomea kufundisha Biblia walipokuwa Seminari Kuu.

Mfano mwingine bado. Maandiko Matakatifu yanasema ikiondokea watu kutabiri watabiri wawili au watatu tena mbele ya mpambanuaji vinginevyo wapagani watasema Mungu wao ni Mungu wa machafuko (1Kor 14:28-33). Kinyume chake, watu watatabiri wengi hata kwa kujituma wenyewe lakini wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Biblia wanayosema wanaisoma na kuifundisha. Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia kinachosema Maandiko Matakatifu maana wao ndio walimu waliosomea kufundisha Biblia walipokuwa Seminari Kuu.
Makleri walioharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika katika kupooza kwao hata watu wafanye mambo yenye kupingana na Yesu Kristo huku wakimsingizia Roho Mtakatifu, ingawa katika Biblia yao imeandikwa Roho Mtakatifu hatapingana na Yesu (Yn 14:12-15), hawatafanya lolote. Watu watakuwa wanamhubiri “roho mtakafujo”, lakini wao wataona sawa tu. Watu watahubiri habari za kuokoka ingawa Yesu alisema “ATAKAYEvumilia mpaka mwisho ndiye ATAKAYEokoka” (Mk 13:13), wao wataona sawa tu. Wala hawataona shida yoyote kwamba watu wanaoingia katika itikadi ya kuokoka, yaani kuyakisha WAMEokoka, wameasi Ukatoliki kwa vile haiwezekani mtu akaikubali sera ya Ulokole, kwa kusemewa sala ya toba, akabaki bado Mkatoliki aliyebatizwa kwa sakramenti ya Ubatizo.
Aidha, watu watakapokuwa wanatafuta miujiza wala hawatakumbuka hata kidogo kwamba Yesu aliwaita watafuta miujiza watu wa uzao wa zinaa (Mt 12:38-42). Yaani katika neno hilo watu wataunda hata kamati za huduma za miujiza, wasiseme kitu chochote bali wataona sawa tu na pengine wenyewe kujiingiza katika harakati hizo hizo za kulazimisha miujiza hata kwa usanii na utapeli pasipo haya ya uso. Wanaweza hata wao wenye kujiingiza katika shughuli za kuwadanganya wagonjwa na wenye dhiki: vilema, viziwi, bubu, vipofu na kadhalika. Hii hasara kweli kweli.
Hadi hapa nadhani mmenipata uzuri wasomaji wangu. Makleri walioharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wanaweza kuvunjiwa mambo yao mbele ya macho yao hata hadi altareni pao wasiseme wala wasifanye lolote kwa vile wamekuwa mapooza. Ndiyo hivyo tena, paka akitoka panya hutawala hadi vitandani!
Namalizia. Mfano mkubwa mintarafu madhara ya kuharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika kwa mustakabli wa Kanisa zima ni jinsi malezi ya mapadre yalivyoparaganyishwa huko Ulaya na Marekani hadi kuwa yanawazaa makleri dhaifu, yaani wasio na hofu ya Mungu na dhaifu wa kulinda na kutunza mafundisho ya Kanisa Katoliki pamwe na kusababisha kuanguka kwa miito mitakatifu. Tayari huko wapo makleri wanaoona ushoga, utoaji mimba na kadhalika kama mizaha tu.
Wakubwa wa huko walipofikia mahali pa kukubali kuwalea waseminari kama raia wengineo kwa masomo ya vyuo vikuu tu, yaani pasipo kuwazamisha kwenye imani Katoliki, ndipo mwanguko ulipoanza. Sasa hivi kwao upadre umekuwa moja ya kazi tu, tena kazi isiyopendeza ukilinganisha na zingine.
Nasikitika kusema eti sasa mtindo huo wa kuwasomesha waseminari wakuu unaingizwa huku Afrika pia, eti kwamba Seminari kuu zigeuzwe taasisi za elimu ya juu tu, kwa maana hiyo seminarini wasomeshwe watu wowote wale pamoja na waseminari wakuu huku mitaala yao ikipitishwa na vyombo vinavyosimamia vyuo vya elimu ya juu vyote katika kila nchi husika. Kwa bahati mbaya, eti kwa sababu ya ufukara tumeshindwa na bado tunashindwa kukataa mabadiliko haya. Eti tunakubali mayai yote aatamie kanga, mwishoni kati ya ndege watakaototolewa tuwapate kuku tunaowahitaji!
Hapa nachelea kucheka kwani kwa kadiri yangu, huko ndiko kuamua kuvunja mayai ya mwisho ya Kanisa Katoliki. Hivi hapo adui hajatuingiza mkenge? Amerika ya Kusini, Afrika na Asia yalikuwa mabara ya mwisho yaliyokuwa yakitunza mayai ya mwisho ya Kanisa Katoliki. Kumbe, sasa hayo yakishavunjwa nayo, ashakumu si matusi, Kanisa Katoliki litalewa kama lililokunywa GM (Gongo Mavi). Lakini ukitaka kuielewa vizuri GM, nenda Musoma wakakueleze vyema aina hiyo ya gongo inavyopatikana.
Mapato mabaya ya kilele kabisa ni kwamba katika “sintofahamu” ya kanisani, makleri wengi kujiweka kando na kuwa “watazamaji wa picha linaloendelea” huku wakiwaachia wachezaji kiwanjani, ndio wakubwa waamke na kutatua mambo waliyokuwa wanatakiwa wayatatue kwa ushirikiano. Ndiyo “sintofahamu” hiyo. Lakini mkasa ndio huo tena, wakati huo huo wakubwa wenyewe wanaweza nao wasiwe wasomaji wa nyakati bali wenye kuangalia mambo mengine tu, labda yenye kuleta pesa kanisani tu.
Ndiyo maana watu wa Kanisa katika nyakati nyeti kabisa wanaweza kuacha kuangalia mambo ya imani, wakakutanika kwa gharama kubwa kuongelea mambo yenye washughulikiaji wengi wengine. Kwa mfano, kuacha kuzungumzia moto unaowaka wa kuvurugika kwa Ukatoliki, wao wanaweza kuitisha mikutano mikubwa kuongelea uharibifu wa mazingira, shida inayozungumziwa na NGO’s tele kabisa duniani. Kifupi, maana yake yale yenye watu wa kuyashughulikia sana eti ndiyo hayo hayo wanayojitutumua kuyashughulikia wakati yao halisi yakiungua au kuoza. Lakini hapa tukumbushane: Mashaka ya Yesu ni kama atakaporudi ataikuta imani duniani au la, na si vinginevyo hasa (Lk 18:8).

Walei WAKISHAyezebelika
Walei wakishayezebelika wanageuka “machangudoa wa imani.” Watu wakishageuka machangudoa wanakosa uwezo wa kumjua mtu hatari na vitu hatari. Kwa kisa hicho wanaweza kumfuata yeyote anayewavuta kwa mluzi mzuri. Atakuja Kibwetere akidai anaijua tarehe ya mwisho wa dunia, watakwenda naye. Atakuja Mwamposa watakwenda naye na kadhalika. Wakiuziwa keki za upako, watanunua. Ashakum si matusi, wakiuziwa “chupi za upako”, watanunua. Wakiambiwa wanunue fagio za upako, watanunua.
Wakiambiwa walete udongo wa majumbani kwao ukombolewe, wataleta. Wakiambia walete nyayo zao zikombolewe, wataleta. Wakiambiwa walete matiti yao yanyonywe na “askofu” yaondolowe “roho ya kukataliwa”, wataleta. Ashakum si matusi, wakiambiwa walale chini “wajambiwe” na nabii wapate utajiri kwa ushuzi huo, watalala. Wakiambiwa watege vichwa wapate teke la upako, watatega. Wakiambiwa wanunue tiketi za kuingilia mbinguni, watanunua. Wakiambiwa ili wapone utasa na ugumba wafanye mapenzi hadharani kusudi watu wawaombee Roho Mtakatifu, watafanya. Wakiambiwa wanapokuja kanisani wasivae chupi kusudi Roho Mtakatifu awaingie vizuri, hawatavaa na kadhalika.
Kifupi, tuseme, tabia zote zinazokutikana kwa changudoa wa kimwili changudoa wa kiimani huwa nazo. Hukosa haya ya uso. Huweza kusema hata mambo ya kuaibisha asione vibaya. Ashakum si matusi! Changudoa haoni aibu. Anaweza kujisifu kutembea na mume wa mtu. Anaweza kutamba mbele ya watu pasipo aibu akisema, “Acha weee, fulani ana fedha bwana, si bahili yule anatoa, anajali sana yule kuliko wanaume wengine bwana niliopata kutembea nao!” “Anahonga sana yule!” “Ana maneno mazuri sana yule!” Maneno kama haya ni maneno ya mtu kujiabisha mwenyewe, lakini changudoa hawezi kuona shida kuyatamka mbele ya watu tena waliotegemea ajiheshimu au aone haya.
Ndivyo ilivyo sasa kati yetu. Siku hizi walei wetu walioyezebelika hawaoni haya kumsifu mchungaji fulani eti anafundisha vizuri hata kama mafundisho yale si ya Kanisa lake. Hawaoni haya kutamba wanakwenda kwenye makanisa mbalimbali huko na huko kwa sababu hawashibi katika Kanisa Katoliki. Ebo! Mbona hii ni kauli ya aibu kusemwa na mtu mzima, yaani mtu aliyebatizwa pamoja na kupewa Kipaimara. Ni aibu. Kweli mtu mzima, nyumbani mwake mkikosekana chakula anahamia kwa jirani? Mumeo akiwa si fasaha wa kusema unahamia kwa bwana mpya? Mkeo akiwa hawezi kupika chakula vizuri ndiyo unamtaliki na kumwoa mwingine? Babayo akiwa fukara, unamtafuta baba mpya? Mamayo akipata ajali na kukatika miguu, unamtafuta mama mpya? Utu uzima siyo kubakia pako na kutafuta suluhisho? Kama ni ukosefu wa chakula, kusaidiana na kutafuta chakula ili mshibe nyumbani mwenu wenyewe. Kama ni shida ya kipato, kusaidiana na kutafuta kipato kusudi mwe na chenu nyumbani mwenu wenyewe na kadhalika.
Ni upaka kubadili nyumba kadiri vyakula vinavyonukia kwa jirani. Kwa upaka, paka aliyezaliwa Dodoma anaweza kufia Mbeya akihama nyumba hii kwenda ile kila mwaka. Haijuzu kwa Mkatoliki kufanana na paka.
Wakristo kujitangaza kwamba wanakwenda huko na huko kuhemea shibe ni jambo la aibu sana kiimani. Iliwapasa waone haya mbele ya watu. Kwa nini? Kwa sababu ni jambo linaloonesha
utoto wao wenyewe. Hapo Kipaimara kilikuwa na maana gani kwao? Kati ya Wamakonde tabia ya mtoto wa fulani kwenda kula kwa jirani ni tabia ya aibu mno. Tabia hiyo huitwa “KUDANGALOKA.”
“Kudangaloka” ni tabia ya aibu mno. Ni aibu mara mbili, mosi, kwa mtoto mwenyewe, kwa nini anahemea majumbani mwa watu wakati ana wazazi na kwao. Ina maana hawezi kuvumilia hali ngumu ya maisha? Pili, ni aibu kwa wazazi, kwa babaye na mamaye, kwamba wanashindwa kumudu kupata chakula kwa ajili ya watoto wao. Lakini katika yote ni aibu zaidi ya mtoto kwa ukufi wa uvumilivu, maana ilimpasa avumilie pamoja na wazazi wake hata akisaidiana nao watafute cha kwao.

Aliyeonja Nyama ya Watu
Nimesema mengi, aheri nimalize. Namalizia kwa kauli moja. Ni hivi, watu wanasema mtu aliyeonja nyama ya mtu haachi. Kama sasa hivi tumeingia sana kumtumikia bwana mpya, pesa, ugonjwa utaendelea tu na hata kuwa sugu kabisa. “Pesa” amekuwa bwana wetu wa pili ijapokuwa Yesu alitukanya akisema hatuwezi kutumikia mabwana wawili, Mungu na pesa, maana ima tutampenda huyu na kumchukia yule au tutampenda yule na kumchukia huyu (Mt 6:24).
Nakufikirisha. Unadhani sasa tunapokamuana pesa kwa michango na harambee mbalimbali tutaacha lini kufanya hivyo? Unadhani tukikamiilisha kujenga makanisa na kumbi za mikutano tutaacha kukamuana michango na harambee? Thubutu yake! Aliyeonja nyama ya mtu haachi! Tukishamaliza kujenga majengo tunayokazania kuyajenga, tutabuni mambo mengine na hivyo kuendelea kukamuana. Tutakuwa tumechovya asali hatutakubali kuchovya mara moja. Tutakuwa tumejijengea mazoea ya harambee na michango na “mazoea yana tabu.”
Sioni kitu cha kutuachisha Waafrika usakaji wetu mali na miujiza. Sioni kitu kitakachosimamisha kuharunika, kugehazika, kuyudaika, kusimonika na kuyezebelika. Kama ni kuacha labda tutuacha siku ya kiyama tu, jambo litakalotuwia balaa kubwa kwa maana tutaadhibiwa kwa kutupwa motoni. Lakini ikitokea hivyo hakutakuwa na ajabu yoyote kwa sababu “Kenge hasikii mpaka atoke damu masikioni.”
Mzee wenu Pd. Titus Amigu
 
Basi huko ulipo copy hii mada ungeipangilia vizuri katika aya na vituo ndio u-paste hapa JF.
 
Mwamba padre. Usijisikie vibaya. Hubirini maisha ya watu na siyo mda wote mtu anaingia kanisani then anatoka na michango kibao
 
Tumsifu Yesu Kristu
(sehemu III)

Makleri WAKISHAharunika, Kugehazika, Kuyudaika na Kusimonika
Makleri wakishaharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wanakuwa mapooza. Mtu aliyepooza huwa hana nguvu. Huweza hata kukosa nguvu ya kichwani na mwilini. Hivyo huweza kushindwa kufikiri, kuona, kusema seuze kutenda. Kifupi, waliopooza hawezi kufanya lolote. Unaweza kuchukua vitu vya mtu aliyepooza asiweze kusema chochote maana hana nguvu ya kukukabili wewe unayevichukua. Aliyepooza anaweza kuona simu yake inachukuliwa asiweze kuzuia wala kwa kupiga kelele wala kwa kumfukuza mwizi. Aliyepooza anaweza kuona pesa yake ikichukuliwa na kibaka asiwe kuzuia wala kwa kupiga kelele wala kwa kumfukuza kibaka. Aliyepooza anaweza kuona mkewe au mumewe akichukuliwa asiweze kuzuia wala kwa kupiga kelele wala kwa kumfukuza mgoni wake na kadhalika.
Ndiyo kisa makleri wakishagueka mapooza hawawezi kupinga chochote wala kwa maneno wala kwa vitendo. Wameshakosa nguvu. Mkasa huu ukishatokea, Kanisa zima linaingizwa hatarini kupoteza mustakabali na hadhi yake. Aidha, walei huingia katika hatari kubwa mno ya kupotea mbugani. Ni ukweli ule ule aliosema Yesu kwamba apigwapo mchungaji, kondoo hutawanyika kwa vile hukosa mtu wa kuwaongoza. Yesu Kristo alisema watu wasipayukepayuke wanaposali (Mt 6:5-8). Kinyume chake, watu watapayuka payuka mbele ya makleri wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Yesu Kristo wanayesema wanamfuata aidha kujiita “Alter Christus.” Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia alichosema Kristo maana wao ni Kristo wengine na mtu aliye Kristo hawezi kumpinga Kristo Yesu.

Mfano mwingine. Yesu Kristo alisema watu wasiwaige wanaopayukapayuka (Mt 6:5-8). Kinyume chake, watu watawaiga lakini wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Yesu Kristo wanayesema wanamfuata aidha kujiita “Alter Christus.” Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia alichosema Kristo maana wao ni Kristo wengine na mtu aliye Kristo hawezi kumpinga Kristo Yesu.

Mfano mwingine tena. Maandiko Matakatifu yanasema ikiondokea watu kunena kwa lugha wanene wawili au watatu, si zaidi, tena mbele ya mfasiri vinginevyo wapagani watasema ni wendawazimu (1Kor 14:26-28). Kinyume chake, watu watanena hata mambo yasiyoeleweka lakini wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Biblia wanayosema wanaisoma na kuifundisha. Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia kinachosema Maandiko Matakatifu maana wao ndio walimu waliosomea kufundisha Biblia walipokuwa Seminari Kuu.

Mfano mwingine bado. Maandiko Matakatifu yanasema ikiondokea watu kutabiri watabiri wawili au watatu tena mbele ya mpambanuaji vinginevyo wapagani watasema Mungu wao ni Mungu wa machafuko (1Kor 14:28-33). Kinyume chake, watu watatabiri wengi hata kwa kujituma wenyewe lakini wao kwa vile wamepooza hawawezi kusema wala kupinga chochote maana hawawezi kuona kitendo hicho kinavyosigana na mafundisho ya Biblia wanayosema wanaisoma na kuifundisha. Laiti wasingeharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wangesimamia kinachosema Maandiko Matakatifu maana wao ndio walimu waliosomea kufundisha Biblia walipokuwa Seminari Kuu.
Makleri walioharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika katika kupooza kwao hata watu wafanye mambo yenye kupingana na Yesu Kristo huku wakimsingizia Roho Mtakatifu, ingawa katika Biblia yao imeandikwa Roho Mtakatifu hatapingana na Yesu (Yn 14:12-15), hawatafanya lolote. Watu watakuwa wanamhubiri “roho mtakafujo”, lakini wao wataona sawa tu. Watu watahubiri habari za kuokoka ingawa Yesu alisema “ATAKAYEvumilia mpaka mwisho ndiye ATAKAYEokoka” (Mk 13:13), wao wataona sawa tu. Wala hawataona shida yoyote kwamba watu wanaoingia katika itikadi ya kuokoka, yaani kuyakisha WAMEokoka, wameasi Ukatoliki kwa vile haiwezekani mtu akaikubali sera ya Ulokole, kwa kusemewa sala ya toba, akabaki bado Mkatoliki aliyebatizwa kwa sakramenti ya Ubatizo.
Aidha, watu watakapokuwa wanatafuta miujiza wala hawatakumbuka hata kidogo kwamba Yesu aliwaita watafuta miujiza watu wa uzao wa zinaa (Mt 12:38-42). Yaani katika neno hilo watu wataunda hata kamati za huduma za miujiza, wasiseme kitu chochote bali wataona sawa tu na pengine wenyewe kujiingiza katika harakati hizo hizo za kulazimisha miujiza hata kwa usanii na utapeli pasipo haya ya uso. Wanaweza hata wao wenye kujiingiza katika shughuli za kuwadanganya wagonjwa na wenye dhiki: vilema, viziwi, bubu, vipofu na kadhalika. Hii hasara kweli kweli.
Hadi hapa nadhani mmenipata uzuri wasomaji wangu. Makleri walioharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika wanaweza kuvunjiwa mambo yao mbele ya macho yao hata hadi altareni pao wasiseme wala wasifanye lolote kwa vile wamekuwa mapooza. Ndiyo hivyo tena, paka akitoka panya hutawala hadi vitandani!
Namalizia. Mfano mkubwa mintarafu madhara ya kuharunika, kugehazika, kuyudaika na kusimonika kwa mustakabli wa Kanisa zima ni jinsi malezi ya mapadre yalivyoparaganyishwa huko Ulaya na Marekani hadi kuwa yanawazaa makleri dhaifu, yaani wasio na hofu ya Mungu na dhaifu wa kulinda na kutunza mafundisho ya Kanisa Katoliki pamwe na kusababisha kuanguka kwa miito mitakatifu. Tayari huko wapo makleri wanaoona ushoga, utoaji mimba na kadhalika kama mizaha tu.
Wakubwa wa huko walipofikia mahali pa kukubali kuwalea waseminari kama raia wengineo kwa masomo ya vyuo vikuu tu, yaani pasipo kuwazamisha kwenye imani Katoliki, ndipo mwanguko ulipoanza. Sasa hivi kwao upadre umekuwa moja ya kazi tu, tena kazi isiyopendeza ukilinganisha na zingine.
Nasikitika kusema eti sasa mtindo huo wa kuwasomesha waseminari wakuu unaingizwa huku Afrika pia, eti kwamba Seminari kuu zigeuzwe taasisi za elimu ya juu tu, kwa maana hiyo seminarini wasomeshwe watu wowote wale pamoja na waseminari wakuu huku mitaala yao ikipitishwa na vyombo vinavyosimamia vyuo vya elimu ya juu vyote katika kila nchi husika. Kwa bahati mbaya, eti kwa sababu ya ufukara tumeshindwa na bado tunashindwa kukataa mabadiliko haya. Eti tunakubali mayai yote aatamie kanga, mwishoni kati ya ndege watakaototolewa tuwapate kuku tunaowahitaji!
Hapa nachelea kucheka kwani kwa kadiri yangu, huko ndiko kuamua kuvunja mayai ya mwisho ya Kanisa Katoliki. Hivi hapo adui hajatuingiza mkenge? Amerika ya Kusini, Afrika na Asia yalikuwa mabara ya mwisho yaliyokuwa yakitunza mayai ya mwisho ya Kanisa Katoliki. Kumbe, sasa hayo yakishavunjwa nayo, ashakumu si matusi, Kanisa Katoliki litalewa kama lililokunywa GM (Gongo Mavi). Lakini ukitaka kuielewa vizuri GM, nenda Musoma wakakueleze vyema aina hiyo ya gongo inavyopatikana.
Mapato mabaya ya kilele kabisa ni kwamba katika “sintofahamu” ya kanisani, makleri wengi kujiweka kando na kuwa “watazamaji wa picha linaloendelea” huku wakiwaachia wachezaji kiwanjani, ndio wakubwa waamke na kutatua mambo waliyokuwa wanatakiwa wayatatue kwa ushirikiano. Ndiyo “sintofahamu” hiyo. Lakini mkasa ndio huo tena, wakati huo huo wakubwa wenyewe wanaweza nao wasiwe wasomaji wa nyakati bali wenye kuangalia mambo mengine tu, labda yenye kuleta pesa kanisani tu.
Ndiyo maana watu wa Kanisa katika nyakati nyeti kabisa wanaweza kuacha kuangalia mambo ya imani, wakakutanika kwa gharama kubwa kuongelea mambo yenye washughulikiaji wengi wengine. Kwa mfano, kuacha kuzungumzia moto unaowaka wa kuvurugika kwa Ukatoliki, wao wanaweza kuitisha mikutano mikubwa kuongelea uharibifu wa mazingira, shida inayozungumziwa na NGO’s tele kabisa duniani. Kifupi, maana yake yale yenye watu wa kuyashughulikia sana eti ndiyo hayo hayo wanayojitutumua kuyashughulikia wakati yao halisi yakiungua au kuoza. Lakini hapa tukumbushane: Mashaka ya Yesu ni kama atakaporudi ataikuta imani duniani au la, na si vinginevyo hasa (Lk 18:8).

Walei WAKISHAyezebelika
Walei wakishayezebelika wanageuka “machangudoa wa imani.” Watu wakishageuka machangudoa wanakosa uwezo wa kumjua mtu hatari na vitu hatari. Kwa kisa hicho wanaweza kumfuata yeyote anayewavuta kwa mluzi mzuri. Atakuja Kibwetere akidai anaijua tarehe ya mwisho wa dunia, watakwenda naye. Atakuja Mwamposa watakwenda naye na kadhalika. Wakiuziwa keki za upako, watanunua. Ashakum si matusi, wakiuziwa “chupi za upako”, watanunua. Wakiambiwa wanunue fagio za upako, watanunua.
Wakiambiwa walete udongo wa majumbani kwao ukombolewe, wataleta. Wakiambia walete nyayo zao zikombolewe, wataleta. Wakiambiwa walete matiti yao yanyonywe na “askofu” yaondolowe “roho ya kukataliwa”, wataleta. Ashakum si matusi, wakiambiwa walale chini “wajambiwe” na nabii wapate utajiri kwa ushuzi huo, watalala. Wakiambiwa watege vichwa wapate teke la upako, watatega. Wakiambiwa wanunue tiketi za kuingilia mbinguni, watanunua. Wakiambiwa ili wapone utasa na ugumba wafanye mapenzi hadharani kusudi watu wawaombee Roho Mtakatifu, watafanya. Wakiambiwa wanapokuja kanisani wasivae chupi kusudi Roho Mtakatifu awaingie vizuri, hawatavaa na kadhalika.
Kifupi, tuseme, tabia zote zinazokutikana kwa changudoa wa kimwili changudoa wa kiimani huwa nazo. Hukosa haya ya uso. Huweza kusema hata mambo ya kuaibisha asione vibaya. Ashakum si matusi! Changudoa haoni aibu. Anaweza kujisifu kutembea na mume wa mtu. Anaweza kutamba mbele ya watu pasipo aibu akisema, “Acha weee, fulani ana fedha bwana, si bahili yule anatoa, anajali sana yule kuliko wanaume wengine bwana niliopata kutembea nao!” “Anahonga sana yule!” “Ana maneno mazuri sana yule!” Maneno kama haya ni maneno ya mtu kujiabisha mwenyewe, lakini changudoa hawezi kuona shida kuyatamka mbele ya watu tena waliotegemea ajiheshimu au aone haya.
Ndivyo ilivyo sasa kati yetu. Siku hizi walei wetu walioyezebelika hawaoni haya kumsifu mchungaji fulani eti anafundisha vizuri hata kama mafundisho yale si ya Kanisa lake. Hawaoni haya kutamba wanakwenda kwenye makanisa mbalimbali huko na huko kwa sababu hawashibi katika Kanisa Katoliki. Ebo! Mbona hii ni kauli ya aibu kusemwa na mtu mzima, yaani mtu aliyebatizwa pamoja na kupewa Kipaimara. Ni aibu. Kweli mtu mzima, nyumbani mwake mkikosekana chakula anahamia kwa jirani? Mumeo akiwa si fasaha wa kusema unahamia kwa bwana mpya? Mkeo akiwa hawezi kupika chakula vizuri ndiyo unamtaliki na kumwoa mwingine? Babayo akiwa fukara, unamtafuta baba mpya? Mamayo akipata ajali na kukatika miguu, unamtafuta mama mpya? Utu uzima siyo kubakia pako na kutafuta suluhisho? Kama ni ukosefu wa chakula, kusaidiana na kutafuta chakula ili mshibe nyumbani mwenu wenyewe. Kama ni shida ya kipato, kusaidiana na kutafuta kipato kusudi mwe na chenu nyumbani mwenu wenyewe na kadhalika.
Ni upaka kubadili nyumba kadiri vyakula vinavyonukia kwa jirani. Kwa upaka, paka aliyezaliwa Dodoma anaweza kufia Mbeya akihama nyumba hii kwenda ile kila mwaka. Haijuzu kwa Mkatoliki kufanana na paka.
Wakristo kujitangaza kwamba wanakwenda huko na huko kuhemea shibe ni jambo la aibu sana kiimani. Iliwapasa waone haya mbele ya watu. Kwa nini? Kwa sababu ni jambo linaloonesha
utoto wao wenyewe. Hapo Kipaimara kilikuwa na maana gani kwao? Kati ya Wamakonde tabia ya mtoto wa fulani kwenda kula kwa jirani ni tabia ya aibu mno. Tabia hiyo huitwa “KUDANGALOKA.”
“Kudangaloka” ni tabia ya aibu mno. Ni aibu mara mbili, mosi, kwa mtoto mwenyewe, kwa nini anahemea majumbani mwa watu wakati ana wazazi na kwao. Ina maana hawezi kuvumilia hali ngumu ya maisha? Pili, ni aibu kwa wazazi, kwa babaye na mamaye, kwamba wanashindwa kumudu kupata chakula kwa ajili ya watoto wao. Lakini katika yote ni aibu zaidi ya mtoto kwa ukufi wa uvumilivu, maana ilimpasa avumilie pamoja na wazazi wake hata akisaidiana nao watafute cha kwao.

Aliyeonja Nyama ya Watu
Nimesema mengi, aheri nimalize. Namalizia kwa kauli moja. Ni hivi, watu wanasema mtu aliyeonja nyama ya mtu haachi. Kama sasa hivi tumeingia sana kumtumikia bwana mpya, pesa, ugonjwa utaendelea tu na hata kuwa sugu kabisa. “Pesa” amekuwa bwana wetu wa pili ijapokuwa Yesu alitukanya akisema hatuwezi kutumikia mabwana wawili, Mungu na pesa, maana ima tutampenda huyu na kumchukia yule au tutampenda yule na kumchukia huyu (Mt 6:24).
Nakufikirisha. Unadhani sasa tunapokamuana pesa kwa michango na harambee mbalimbali tutaacha lini kufanya hivyo? Unadhani tukikamiilisha kujenga makanisa na kumbi za mikutano tutaacha kukamuana michango na harambee? Thubutu yake! Aliyeonja nyama ya mtu haachi! Tukishamaliza kujenga majengo tunayokazania kuyajenga, tutabuni mambo mengine na hivyo kuendelea kukamuana. Tutakuwa tumechovya asali hatutakubali kuchovya mara moja. Tutakuwa tumejijengea mazoea ya harambee na michango na “mazoea yana tabu.”
Sioni kitu cha kutuachisha Waafrika usakaji wetu mali na miujiza. Sioni kitu kitakachosimamisha kuharunika, kugehazika, kuyudaika, kusimonika na kuyezebelika. Kama ni kuacha labda tutuacha siku ya kiyama tu, jambo litakalotuwia balaa kubwa kwa maana tutaadhibiwa kwa kutupwa motoni. Lakini ikitokea hivyo hakutakuwa na ajabu yoyote kwa sababu “Kenge hasikii mpaka atoke damu masikioni.”
Mzee wenu Pd. Titus Amigu
 
Nimejitahidi kusoma aisee bonge moja la idea mkuu. Yani its a nice message Mungu ambariki aliyetunga. Mwenye macho na asome..usiposoma na wewe unataka kusimonika
 
Back
Top Bottom