Tukudzi
Member
- Jun 22, 2019
- 40
- 17
NA PAULINE ONGAJI
MARADHI ya Covid -19 bila shaka yameuka jinamizi sio tu nchini, bali ulimwenguni kote. Lakini pia ugonjwa huu umekuwa funzo kwetu kama Wakenya kuhusu mambo mengi. Hasa umetukumbusha kuhusu uwezo wetu wa kuzalisha bidhaa kama nchi. Pindi baada ya virusi vinavyosababisha maradhi haya kuthibitishwa kuingia nchini, sekta mbali mbali ambazo zilikuwa zimeangamia, ghafla zilifufuka. Kwa sasa uwezo wa Kenya wa kuunda barakoa za kujikinga kutokana na maambukizi ya virusi hivi, umepiku matarajio ya wengi.
Pili, Taasisi ya Kitaifa ya Utafiti wa Kimatibabu KEMRI ilitangaza kuanza rasmi kuunda vifaa vya kupima virusi hivyo, na hivyo kurahisisha shughuli za kupata matokeo upesi. Hayo kando, wanafunzi 16 wa Chuo Kikuu cha Kenyatta waliunda mtambo unaosaidia wagonjwa wa maradhi haya, kupumua. Uvumbuzi huu unanuiwa kuimarisha uwezo wa vyumba vya wagonjwa mahututi, kushughulikia wagonjwa wa maradhi haya.
Sio hayo tu. Sasa viwanda kadha wa kadha vinajikakamua usiku na mchana kuunda dawa za kuua virusi. Ni vigumu kuamini tunazungumzia taifa ambalo ukitembea katika baadhi ya maduka yake ya jumla, utapata vichokoa meno vilivyoagizwa kutoka China. Ukweli ni kwamba uwezo wa uvumbuzi ambao Kenya imeafikia katika kipindi hiki kifupi, umeshinda hatua ambazo taifa hili limepiga kwa miaka mingi. Lakini ukiangalia vyema, tangu jadi Wakenya wamekuwa wakijikakamua kuunda bidhaa zao halisi.
Kwa mfano, unapotembelea masoko ya Uhuru au Kariobangi jijini Nairobi, utapata taswira kamili ya jinsi mafundi wetu wanavyojitahidi kushona nguo za kila aina. Kumbuka, wanafanya hivi huku wakiendelea kupata ushindani mkali kutoka kwa soko la mitumba, vile vile mavazi yanayoagizwa kutoka China na Uturuki, miongoni mwa mataifa mengine. Nakumbuka wakati mmoja katika pilkapilka zangu za uanahabari, nilikutana na bwana mmoja aliyevumbua jiko la kutumia mawe fulani badala la makaa.
Lakini licha ya uvumbuzi huu wa kipekee, alinieleza jinsi harakati zake za kutaka usaidizi wa kuboresha mtambo huu, zilivyolemazwa na urasimu katika afisi husika za Serikali. Bila shaka, suala la ubora wa bidhaa zetu pia linapaswa kuangaziwa, lakini ukweli kama Waswahili wanavyosema, penye nia pana njia, na awali, nia hii haikuwa imeshika kasi.
Kwa nini tusiwaunge mkono mafundi, wazalishaji na wabunifu wetu ili waendelee kuunda bidhaa zao, na katika harakati hizo kuimarisha ubora? Hata mataifa yanayotamba kiuchumi ulimwenguni hayakuanza kwa kuunda bidhaa za ubora wa hali ya juu. Wakati mmoja wavumbuzi kutoka mataifa haya waliunda bidhaa duni, na ni kupitia makosa waliyofanya, vile vile utafiti, ndipo wameendelea kuboresha uwezo wa viwanda vyao kuunda bidhaa za hali ya juu tunazong'ang'ana kununua kwa sasa.