Shamuhuna anapaswa kuwajibika kwa migogoro ya ZFA?
MCHEZO wa soka visiwani hapa, katika siku za hivi karibuni unazidi kukatisha tamaa kutokana na chuki, mifarakano, majungu na fitina ambazo zinaelekea kuupeleka mchezo huo kaburini na kubaki kuwa historia miongoni mwa wapenda soka wa Zanzibar.
Hizo ni kauli za wadau wa soka, wakiwemo viongozi wa juu wa chombo kinachosimamia mchezo huo visiwani hapa (ZFA), baada ya wawakilishi wawili wa Zanzibar katika mashindano ya kimataifa kujikuta wakiianza vibaya michuano hiyo, huku malumbano yakizidi kushamiri kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar (BTMZ) na chama chenye jukumu la kusimamia mchezo wa soka Zanzibar.
Mwanzoni mwa mwezi huu, mashabiki wa soka walielekeza macho na masikio yao katika viwanja vya Amaan na Gombani kushuhudia vipigo kwa timu zao mbili za Miembeni na Chipukizi na kuondoa matumaini ya soka la zamani kurejea Zanzibar.
Wakati hayo yakitokea, viongozi wa Miembeni nao chupuchupu kutwangana makonde na wenzao wa ZFA Taifa, katika kikao kilichoitishwa kujadili gharama za mjumbe wa Chama cha Soka Taifa atakayeambatana na Miembeni nchini Afrika Kusini, kwa ajili ya pambano la marudiano dhidi ya Mamelodi Sundown.
Mzozo huo uliibuka kati ya Naibu Mkurugenzi wa Miembeni, Abubakar Bobea na Makamu wa Rais wa ZFA, Alhajj Haji Ameir baada ya Miembeni kuendelea kutetea msimamo wake wa kutomgharamia mjumbe wa chama hicho, katika safari hiyo ya bondeni.
Kama mnataka tumlipie nauli mjumbe wenu, bora aende Mzee Zam Ali (Katibu Mkuu ZFA), ambaye ana matatizo ya presha na huko tutamsaidia kupata matibabu, badala ya Maulid Hamad Maulid (Msemaji wa ZFA)
. mnataka mambo, wakati hamna uwezo, kama hamna pesa bora mjiuzulu, alisema Bobea.
Uongozi wa Miembeni, uliitwa na ZFA Taifa makao makuu ya chama hicho yaliyopo katika Uwanja vya Amaan, kueleza sababu za kukataa kumgharamia mjumbe wake, kwenda Afrika Kusini, kitendo ambacho ZFA inadai kuwa ni kinyume na taratibu za mashirikisho ya soka ya kimataifa ya CAF na FIFA.
Uongozi wa Miembeni, hivi karibuni uliwashtua wapenda soka kwa madai ya kutokuwa na uwezo wa kumgharamia mjumbe huyo, licha ya kutangaza kuwa itaondoka na ujumbe wa watu 31 kwenda Afrika Kusini, akiwemo Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Wilaya ya Mjini, Nassor Salum Aljazeera, ambaye ni hasimu mkubwa wa ZFA taifa.
Aljazeera katika siku za hivi karibuni, aliushangaza umma pamoja na Rais wa ZFA, Ali Ferej Tamim, kutokana na kujivika kofia isiyomwenea ya kuiwakilisha Miembeni katika kikao cha majadiliano kilichofanyika kabla ya mechi ya Miembeni na Mamelodi Sundown.
Mgawanyiko wa vyombo vyenye dhamana ya michezo, umesababisha viongozi wa ZFA taifa kutoaminiwa katika masuala ya fedha, kutokana na Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar (BTMZ), kwa kushirikiana na wizara husika, kutoa fedha moja kwa moja kwa klabu bila kupitia ZFA taifa, jambo linalolalamikiwa na viongozi wa chama hicho.
Hivi karibuni Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, kupitia BTMZ ilizipa Miembeni na Chipukizi, sh milioni 20 kwa ajili ya maandalizi ya michezo yao ya awali, kitendo ambacho kiliwashangaza viongozi wengi wa ZFA Taifa.
Ni kweli Aljazeera alihudhuria kikao kile, mimi nilishangaa kumwona, lakini baadaye nilipouliza niliambiwa kuwa anaiwakilisha Miembeni na yeye ni mmoja kati ya watu wanaotoa mchango mkubwa ndani ya klabu hiyo, alisema Ali Ferej Tamim.
Kamati tendaji ya ZFA Taifa, ilimteua Msemaji wake, Maulid Hamad Maulid, kuongozana na timu hiyo nchini Afrika Kusini, ambako kiutaratibu hutakiwa kuandika ripoti ya mchezo, jambo ambalo litawagharimu Miembeni endapo wataondoka bila ya kiongozi yeyote kutoka chama cha kitaifa.
Habari kutoka ndani ya ZFA, zinasema chama hicho kimewasiliana na Chama cha Soka Afrika Kusini na kueleza kuwa hakijatuma mjumbe yeyote katika msafara wa timu hiyo, baada ya Miembeni kumkataa mjumbe aliyeteuliwa na kamati tendaji kuongozana na msafara huo.
Taarifa zilizopatikana zinaeleza kwamba, huduma wanazozitumia ZFA taifa hivi sasa zinajadiliwa kwa karibu, ikiwemo ofisi wanazotumia, samani na mishahara ya wafanyakazi wasiopungua 10, kutokana na viongozi wa ZFA kushindwa kumuomba radhi Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma Shamuhuna kama walivyoahidi katika siku za hivi karibuni.
Chimbuko la mgawanyiko baina ya vyombo vyenye dhamana na michezo, imetokana na makovu ya uchaguzi mkuu wa chama hicho kutokana na kuanguka kwa baadhi ya wagombea waliokuwa wakiungwa mkono na serikali na hivyo kupoteza imani kwa baadhi ya viongozi waliopo madarakani.
Source: TZ Daima