Chama Cha Mapinduzi (CCM)
Kwa ufupi
Ni siku chache baada ya kushindwa kura ya maoni akidai haki haikutendeka, kuhujumiwa
Kigogo mmoja wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kahama, mkoa wa Shinyanga, ambaye pia alikuwa akiwania kuteuliwa na chama hicho kugombea ubunge wa Jimbo wa Ushetu na kushindwa katika kura ya maoni, ameamua kuacha kukitumikia chama hicho na kuhamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Kigogo huyo amekiahama chama hicho pamoja na wanachama wengine 50 wa CCM siku chache baada ya kuangushwa katika kura ya maoni za ubunge, akidai haki haikutendeka wakati wa kampeni na upigaji kura hiyo.
Akizungumza na NIPASHE mjini hapa mwishoni mwa wiki, Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Kahama, Juma Protasi, alisema wanachama wa CCM zaidi ya 50 wamejiunga na chama chao akiwamo Bukakiye ambaye alikuwa mweka hazina wa chama hicho tawala wilaya ya Kahama.
Alisema kati ya waliojiunga na Chadema, 12 ni mabalozi wa CCM Kahama mjini na mwenyekiti wa chama hicho tawi la Majengo.
Protasi alisema Chadema kwa sasa kinaendelea kuimarisha ngome zake kwa ajili ya kuandaa mazingira ya ushindi katika majimbo yote matatu wilayani humo ya Ushetu, Kahama Mjini na Msalala.
CHANZO: NIPASHE