nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,860
- 5,803
- Wednesday, July 20, 2011, 6:40
- Habari kuu, Mtanzania
*Wabunge wa CCM wachachamaa, wataka ang'olewe
*Shelukindo aeleza alivyopelekewa bahasha
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
KATIBU Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo anadaiwa kuwakashfu wabunge kwa kuwafananisha na wasanii wa maigizo wa kikundi cha The Original Comedy.
Jairo anadaiwa kutoa maneno hayo juzi nje ya ukumbi wa Bunge muda mfupi baada ya Bunge kuahirishwa na wabunge wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kwenda katika kikao chao kabla ya mjadala wa bajeti kuahirishwa juzi jioni.
Chanzo chetu cha habari kilichokuwa ndani ya kikao hicho cha wabunge wa CCM kiliiambia MTANZANIA juzi kuwa madai ya kashfa hiyo yaliwekwa wazi na Mbunge wa Mafia, Abdulkarim Shaha alipokuwa akichangia mada katika kikao hicho.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Jairo alitoa lugha hiyo iliyoonekana kuwaudhi wabunge wa CCM baada ya kukutana na Shaha nje ya ukumbi wa Bunge.
"Tulipokuwa katika kikao chetu hali ilikuwa mbaya kwa sababu wabunge walikuwa wakitoa madukuduku yao kuhusu hali ilivyokuwa juu ya hiyo bajeti iliyokwamishwa.
"Wakati tunajadili, Shaha alisimama na kueleza jinsi Serikali inavyotakiwa kufanya kukabiliana na huu mgawo wa umeme ambako alipendekeza inunuliwe mitambo haraka iwezekanavyo na Jairo achukuliwe hatua za haraka kwa kuondolewa katika nafasi yake.
"Pamoja na maelezo mengi aliyosema, alituambia kuwa wakati wabunge tumetoka nje ya ukumbi wa Bunge baada ya Bunge kuahirishwa, alikutana na Jairo, wakazungumza kisha akamwambia sisi wabunge ni kama ‘comedy' hatumfanyi kitu hata tukifanyaje.
"Aliposema hivyo, wabunge wakalipuka kwa hasira wakasema lazima huyu ang'oke kwa sababu anaonekana kuwa na kiburi kwa kuwa anateuliwa na Rais.
"Kauli hiyo ya Shaha ikaungwa mkono na Mbunge wa Shinyanya Mjini, Stephen Masele ambaye alipigilia msumari na kusema alichosema Shaha ni kweli kwa kuwa hata yeye alimsikia.
"Inaonekana kauli hiyo ya Shaha ilimshangaza Waziri Mkuu Mizengo Pinda ambaye ndiye alikuwa Mwenyekiti wa kikao kwani aliuliza, ni kweli amesema hivyo?, ‘Shaha akasema ni kweli, ‘I swear' (naapa) aliniambia," kilisema chanzo chetu.
Chanzo hicho kilisema baada ya Shaha kuzungumza, Waziri Mkuu alichukua nafasi yake na kuendelea kueleza ugumu wa upatikanaji wa umeme na wakati huo huo
Mbunge wa Mwibara, Alphaxard Lugola, alikuwa akinyoosha mkono kwa muda mrefu bila kupewa nafasi ya kuzungumza.
"Mimi nilikuwa namuona Lugola amenyoosha mkono, lakini hakuruhusiwa kuzungumza, alipoona hoja yake itakufa kwa kuwa Waziri Mkuu alikuwa ameshaanza kuhitimisha, akaamua kusimama kwa nguvu bila kuruhusiwa na kumkatisha Pinda huku akisema kuwa ana mawazo tofauti na wenzake waliokuwa wamekwisha kuchangia.
"Aliporuhusiwa kuzungumza akapigiwa makofi na kuanza kumtaka Waziri Mkuu asilichukulie rahisi rahisi hili suala la umeme kwa sababu ndilo lililowahi kuvunja Baraza la Mawaziri na kuwa chanzo cha Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa, kuondoka madarakani.
‘Vilevile alieleza jinsi alivyokuwa hakuridhishwa na kauli ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Stephen Wassira, ambaye muda mfupi uliopita alikuwa amesema Serikali imekubali kuondoa bungeni hoja ya mjadala wa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa sababu imesikia kilio cha wabunge.
"Lugora alisema kauli hiyo ya Wassira inakwenda kinyume na kauli ambayo imekuwa ikitolewa na Serikali, kwamba Serikali ni sikivu hivyo akahoji ni kwa nini kilio cha wananchi kuhusu mgawo wa umeme hakijasikilizwa badala yake kinasikilizwa kilio cha wabunge.
"Kwa hiyo, akasisitiza Jairo aondolewe katika nafasi yake na pia Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), William Mhando, naye ang'olewe kwa sababu naye ni chanzo cha kukosekana kwa umeme nchini. Hata hivyo Waziri Mkuu alisema suala la Mhando inahitaji uchunguzi kuona jinsi TANESCO inavyohusika katika mgao huo.
"Yeye Lugora alikuwa na hoja moja kwamba, bila Jairo na wenzake kuondoka wizarani hapo, umeme hautapatikana kwa sababu kukosekana kwa umeme kunamfaidisha yeye kwa njia anazojua na pia akatoa mfano wa nchi ya Kongo (Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo – DRC) akisema migogoro ya mara kwa mara nchini humo inawanufaisha baadhi ya watu," kilisema chanzo hicho.
Kuhusu Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo, ambaye ndiye aliyesoma bungeni barua iliyodaiwa kuandikwa na Jairo kwenda katika idara za wizara yake ili zichangwe mabilioni ya fedha kwa ajili ya kufanikisha bajeti hiyo, chanzo chetu kilisema mbunge huyo aliweka wazi kila kitu.
‘Alisema kuwa usiku wa kuamkia Jumatatu alifuatwa na watu wanne wakiwa na bahasha kwa ajili ya kumtuliza.
"Huyo mama alichamaa akatuambia uamuzi wake wa kusoma barua ile ya Jairo bungeni ulikuwa wa nia nzuri, akasema usiku wa leo (juzi) watu wanne walimfuata wakiwa na bahasha, akasema walikuwa wametumwa na -–(akamtaja Jairo) ila alikataa kupokea bahasha hiyo.
"Alisema pamoja na kukataa bahasha hiyo, aliomba ushauri kwa wabunge wenzake kuhusu hiyo bahasha, wakamwambia usikubali kuichukua nenda kaisome tu hiyo barua maana wamezoea.
"Kwa hiyo, ndiyo maana mmeona wakati mama huyo anachangia alianza kwa kusema kuwa kuna watu walikuwa wamemuomba asichangie lakini yeye akakomaa na kusema liwalo naliwe, akamwaga mboga," kilisema chanzo chetu.
Hata hivyo, chanzo hicho kilisema baadhi ya makubaliano yaliyokuwa yamefikiwa katika kikao chao hayakufuatwa kwani wakati Pinda analiambia Bunge kuwa serikali imeondoa bungeni bajeti ya wizara hakutakiwa kutaja hoja hiyo itawasilishwa tena bungeni baada ya muda gani.
"Tulikuwa tumekubaliana kwamba Waziri Mkuu atakaposimama kueleza nia ya kuahirisha hoja hiyo, asitaje muda kamili wa kuirudisha tena bungeni, lakini kwa bahati mbaya Spika (Anne Makinda) ambaye hakuhudhuria kikao chetu, akabadilisha upepo baada ya kusoma kanuni na kutaka Bunge lielezwe hoja hiyo itakuwa tayari baada ya muda gani.
"Kwa hiyo, mpango wetu ulibadilika kwa sababu hoja yetu ilikuwa kwamba tunaweza kuliambia Bunge kwamba, hoja itakuwa tayari baada ya muda fulani kisha Serikali ikakwama,.
‘Lakini kwa kuwa Waziri Mkuu alibanwa hakukuwa na njia nyingine ya kukwepa badala yake akasema bajeti hiyo itakuwa tayari baada ya wiki tatu," kilisema chanzo hicho.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, baadhi ya wabunge wa CCM waliochangia mada hiyo katika kikao chao ni Mbunge wa Mbozi Mashariki, Godfrey Zambi, Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka, Mbunge wa Bumbuli, Januari Makamba na Mbunge wa Singida Magharibi, Mohamed Misanga.
Wengine ni Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu na Mbunge wa Viti Maalum, Margareth Sitta ambaye alishangaa Serikali kushindwa kununua mitambo wakati ina uwezo wa kununua ndege.
Wakati hali ikiwa hivyo, taarifa zinasema iwapo Jairo hataondolewa madarakani hadi kufikia siku ya bajeti hiyo kuwasilishwa tena bungeni, wabunge hao wanapanga kuikwamisha tena ili liwe fundisho kwa serikali.
Juzi, Waziri Mkuu Pinda aliondoa hoja bungeni ya mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha wa 2011/2012 kwa kile alichosema kuwa ni kutokana na idadi kubwa ya wabunge waliochangia kuonyesha kutoridhishwa na hali ya upatikanaji wa umeme nchini.
Kutokana na mabadiliko hayo, Bunge jana lilitoa ratiba mpya iliyoonyesha kuwa bajeti hiyo sasa itawasilishwa tena bungeni Agosti 13 mwaka huu.