Hoja za Katiba mpya, Dowans zisiminywe

mzambia

JF-Expert Member
Dec 31, 2010
885
60
BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaanza vikao vyake kesho kutwa mjini Dodoma, ambapo wabunge watafanya shughuli mbalimbali ikiwamo kujadili hotuba ya rais aliyoitoa Novemba mwaka jana wakati akilizindua Bunge baada ya uchaguzi wa Oktoba 30.

Wakati wabunge wakikusanyika kesho kutwa katika viwanja hivyo, wabunge wawili kutoka vyama vya upinzani wameonyesha nia ya kupeleka hoja binafsi ya kutaka Bunge litoe mwongozo juu ya mchakato utakaowezesha kupatikana kwa Katiba mpya.

Hoja nyingine ni ile ya kulitaka Bunge lijadili kushindwa kwa serikali katika mahakama ya kimataifa inayojishughulisha na utatuzi wa migogoro ya kibiashara dhidi ya Kampuni ya Dowans ambayo inapaswa kulipwa sh bilioni 94 na TANESCO.

Kimsingi hoja hizi mbili zina masilahi makubwa kwa taifa, kwa kuwa kwa muda mrefu Tanzania imekuwa ikikabiliwa na matatizo mbalimbali yanayotokana na upungufu uliomo ndani ya Katiba ambayo pamoja na nchi kuingia katika mfumo wa vyama vingi bado kuna vipengele ni kandamizi.

Sekta ya umeme nayo kwa muda mrefu imekuwa ikienda kwa mwendo wa kusuasua kwa sababu ya kutokuwapo kwa mikakati madhubuti ya kutatua matatizo yanayojitokeza, hivyo kuifanya nchi kutokuwa na umeme wa uhakika.

Tunaamini kuwa wabunge watatumia fursa hii ya kukutana kwao kuweka mbele masilahi ya taifa kwa kuruhusu na ikiwezekana kujadili kwa ufasaha hoja hizi badala ya kufuata itikadi za chama.

Tunasema hivyo kwa kuwa tayari kumeanza kusisika minong’ono kuwa baadhi ya wabunge hasa wa chama tawala ambao wapo wengi wamekuwa wakifanya mizengwe ili hoja hizo zisipate nafasi kwa hofu ya kukiweka mahali pabaya chama chao.

Hatuamini kama wabunge makini wanaweza kufanya hujuma ya aina hiyo kwa hoja zenye masilahi kwa taifa, hasa katika kutatua matatizo ya muda mrefu yanayolikumba taifa hili.

Tunawaomba wabunge waweke mbele masilahi ya wananchi ambao kadiri siku zinavyokwenda ndivyo wanavyozidi kuwa maskini kutokana na mgawanyo mbovu wa rasilimali za taifa.

Sote tunajua umuhimu wa sekta ya umeme kwa taifa kiuchumi, hivyo hakuna sababu kwa wabunge kufanya masihara katika mambo muhimu yanayogusa moja kwa masilahi ya wananchi.

Kadiri tunavyofanya mzaha katika sakata hili ndivyo tunavyozidisha ugumu wa maisha kwa wananchi. Tunaamini kuwa wabunge watatumia fursa hii kujadili hoja zenye lengo la kuitoa nchi yetu hapa tulipo na wala si kujadili zaidi siasa na porojo zenye kumuumiza mwananchi.

SOSI: TZ DAIMA
 
Back
Top Bottom