nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Imeandikwa na Halima Mlacha; Tarehe: 10th January 2012 @ 14:35
SERIKALI imekanusha tetesi kwamba ina mpango wa kutoimarisha ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Hata hivyo imesisitiza kuwa haitopelekeshwa kwa kuwa imejiwekea utaratibu kwa kuzingatia maslahi ya Watanzania.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Stergomena Tax alisema hayo jana wakati alipozungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam kuhusu mustakabali mzima wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Alisema kumekuwepo na upotoshaji wa makusudi au kutoelewa msimamo wa Tanzania kuhusu uharakishwaji wa Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki, itifaki mbalimbali ikiwamo ya sarafu moja na ya ulinzi na usalama.
"Serikali imekuwa ikilaumiwa kuwa inachelewesha kwa makusudi hatua mbalimbali za utengamano, lawama hizi hazina msingi kwani nchi yetu inaamini kuwa jumuiya ina faida nyingi na ndio maana mwaka 1999 ilisaini mkataba wa kujiunga nayo," alisema Tax.
Alisema Serikali inatambua kuwa jumuiya ni ya watu na hata kwenye mkataba wa kujiunga na jumuiya unasema wazi kuwa kuwepo na maridhiano ya makubaliano ya wote.
"Kama sisi tunavyoheshimu mtazamo wa wengine na wengine nao waheshimu mtazamo wetu."
Alisema katika kipengele hicho hakuna eneo linasema mtazamo au mawazo ya wengi ndio sahihi na ndio maana katika suala la ardhi Tanzania ilisimama kidete hali ambayo baadaye
hata nchi nyingine za umoja huo zilikubali na kuona umuhimu wake.
Alisema katika itifaki ya ushirikiano wa siasa, sarafu moja na ulinzi na usalama, Serikali haiwezi
kuharakishwa na kutoa uamuzi wake bali inatumia utaratibu iliyojiwekea ili kuimarisha zaidi mtengamano huo na si kukurupuka.
"Mkisikia Tanzania imekataa kitu jiulizeni sababu na mpime kama sababu hizo zinajenga taswira ya Tanzania au kubomoa na iwapo maslahi ya Watanzania yamezingatiwa…naombeni vyombo vya habari muwe makini na masuala haya kwani ni muhimu sana kwa Watanzania," alisema.