Hadithi: Giza Lenye Faraja

Hadithi: Giza Lenye Faraja

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,638
Image may contain: text that says 'Nyemo Chilongani Darkness Of Comfort (Giza lenye Faraja)'
 
HADITHI: DARKNESS OF COMFORT (GIZA LENYE FARAJA)
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI
SIMU: 0718069269/0758860093

YUNNAN, China.

Lilikuwa ni moja ya matukio ya kuhuzunisha, vilio vilitawala kila kona, idadi kubwa ya watu walikuwa wamepoteza maisha na wengi kujeruhiwa,
Wachina hawakuamini kile kilichokuwa kimetokea, japokuwa matetemeko ya ardhi yalikuwa yamezoeleka nchini China, ila la siku hiyo lilikuwa kiboko.
Jimbo la Yunnan lilikuwa limetetemeshwa, majengo mengi yakaanguka huku barabara zikiharibiwa vibaya, mabomba ya maji yaliyokuwa yamechimbiwa ardhini yakafukuliwa na kuanza kumwaga maji hovyo.
Madereva waliokuwa barabarani, wakashindwa kuyakontro magari yao na kujikuta wakipata ajali, majengo yaliyokuwa yamewekwa vioo, vyote vikavunjika na hata majengo mengine kudondoka.
Tetemeko hilo la ardhi ambalo lilidumu kwa zaidi ya dakika moja lilileta maafa makubwa jimboni hapo.
Miongoni mwa nyumba zilizokuwa zimepata maafa makubwa kutokana na tetemeko hilo la ardhi lilikuwepo jengo la umma lililojengwa na serikali ya China kwa ajili ya kuwasaidia watu wasiokuwa na kazi yoyote ile, jengo la ghorofa kumi lililokaliwa na watu zaidi ya elfu moja.
Hakukuwa na tofali lolote lililosimama, jengo zima lilikuwa limedondoka chini. Hakukuwa na mtu aliyeweza kumpa pole mwenzake kwani asilimia sitini ya watu, majengo yao yalikuwa yamedondoshwa na tetemeko hilo kubwa kuwahi kutokea nchini China.
Kila mtu alionekana kuwa bize mahali hapo, utoaji wa vifusi ulikuwa ukiendelea huku kwa wale waliokuwa na makoleo au vyombo vyovyote vile walikuwa wakiendelea kufukua kwa ajili ya kuzitoa maiti na watu waliojeruhiwa vibaya.
“来帮我们” (njooni mnisaidie) alisikika jamaa mmoja huku akijitahidi kutoa vifusi vya jengo hilo.
Watu waliokuwa pembeni wakaanza kusogea kule alipokuwa jamaa yule, vifusi vikubwa vya matofali vilikuwa chini huku vikiwa vimeifukia miili ya watu waliokufa na wale waliokuwa majeruhi, wakaanza kuitoa miili hiyo hata kabla magari ya serikali hayajafika.
Miili ilijawa vumbi, matofali makubwa na mazito yalikuwa yamewafunika. Miili mingine haikuweza kutolewa kwani vifusi vilivyokuwa vimewafunika vilikuwa vikubwa na vizito. Kwa miili waliyoweza kuitoa, waliitoa lakini ile ambayo kwao ilionekana kuwa vigumu kuitoa, wakaachana nayo na kusubiri magari ya serikali.
Kila mmoja kwa wakati huo alikuwa bize kumsaidia mwenzake, wale wasiokuwa na nguvu, walikaa pembeni huku wakiangalia kazi iliyokuwa ikiendelea kwa wenzao. Baada ya dakika chache, magari makubwa ya serikali yakafika mahali hapo na kuanza kutoa vifusi vile.
Picha ambayo ilionekana mahali hapo ilimtisha kila mtu, watu wengi walikuwa wamekufa kwa kudondokewa vibaya na vifusi vile, wapo waliokuwa wamepasuka vichwa na damu kuwatoka nyingi huku wengi wakiwa wamevunjwavunjwa viungo vyao.
“我找我的朋友” (namtafuta rafiki yangu) alisikika msichana mmoja wa kichina.
Kwa kumwangalia tu, naye alikuwa mmoja wa waathirika wa tetemeko lile, mwili wake ulikuwa umejaa vumbi huku ikiwa ni vigumu kumtambua kwa kumwangalia mara moja.
Naye alikuwa amesogea hapo na kutaka kumuona rafiki wake ambaye hakuwa akijulikana na watu waliokuwa bize wakiondoa vifusi.
“舒押嗯,这边走” (Shu Yan, sogea huku) alisema mwanamke mmoja na kumvuta msichana yule ambaye alikuwa na miaka kumi na sita.
Muda wote msichana huyo alikuwa akilia, kila mwili uliokuwa ukitolewa mahali hapo alikuwa akiusogelea na kuanza kuuangalia ili apate kujua kama alikuwa ndiye huyo rafiki yake au la.
Miili iliendelea kutolewa lakini hakumuona mtu aliyemhitaji hali iliyomuongezea kilio zaidi.
Kutokana na maafa makubwa yaliyotokea siku hiyo kutokana na tetemeko kubwa lililokuwa limetokea, jioni ya siku hiyo taarifa rasmi ikatolewa na kuonyesha kwamba zaidi ya watu elfu sitini walikuwa wamefariki dunia, ilikuwa ni idadi kubwa zaidi ya tetemeko lililotokea mwaka 1822.
Shu Yan, msichana masikini asiyekuwa na ndugu, msichana aliyekuwa akiishi ndani ya jengo lililokuwa limedondoka, alijikalia chini pembeni huku akilia, kila alipokuwa akiyaona majengo mengine yaliyokuwa yamedondoka kutokana na tetemeko lile la ardhi, alibaki akilia tu.
“李察,你在哪里?” (Richard, upo wapi?) aliuliza Shu Yan huku akijifuta machozi yake.
Swali lake hilo halikupatiwa jibu, alibaki akilia tu, machozi yaliendelea kububujika mashavuni mwake huku akiyafuta kwa kutumia nguo yake chafu aliyokuwa ameivaa.
Usiku mzima Shu Yan hakulala, alikuwa akilia tu huku akihitaji kumuona rafiki yake huyo. Mara ya mwisho kabisa kuonana naye, alikumbuka kwamba alikwenda chooni mara baada ya kumuacha Richard akiwa koridoni na watoto wengine, kipindi hicho ndicho ambacho tetemeko hilo la ardhi likatokea na hakujua kama rafiki yake huyo alikufa au la.
Urafiki wake na Richard ulikuwa ni wa karibu mno. Wote walikuwa watoto masikini waliokutana ndani ya jengo hilo, walisaidiana kwa kila kitu na hata walipokuwa wakitoka kwenda kuomba mitaani, bado waliambatana pamoja.
Watu waliwashangaa mitaani, halikuwa jambo la kawaida kumuona msichana wa kichina akiambatana na mtu mweusi. Kwa Shu Yan, hakutaka kujali, kwake, urafiki huo ulikuwa ni zaidi ya kila kitu maishani mwake, hakuangalia rangi, urefu au ufupi, kitu pekee alichokuwa akikiangalia, moyo wake ulisemaje.
“Ninataka kukuona Richard, umeniacha peke yangu, ninahitaji kukuona, upo wapi Richard wangu,” alisema Shu Yan lakini maneno yake yalikuwa si kitu, ni kama machozi ya samaki, kila alipolia, yalichukuliwa na maji.
Serikali ya China ikatoa msaada mkubwa kwa ajili ya watu walioathiriwa na tetemeko lile la ardhi. Wakatenga sehemu maalumu ambayo ikafanywa kama kambi ya muda kwa ajili ya watu hao.
Shu Yan hakuonekana kuwa na furaha, bado shauku yake ilikuwa ni kumuona rafiki yake aliyekuwa akimpenda kwa mapenzi yote, Richard ambaye alipotea na hakujua kama alikuwa hai au alikuwa mfu.
Usiku mzima mawazo yake yalikuwa kwa Richard tu. Hakulala, usiku mzima alikuwa akimfikiria rafiki yake huyo. Machozi yalikuwa yakimbubujika kwani moyo wake ulimuuma mno.
Mpaka asubuhi inafika bado alikuwandani ya kambi ya watu walioathiriwa na tetemeko lile, bado hakujua mahali alipokuwa Richard. Siku hiyo hakutaka kubaki hivyohivyo tu, alichokifanya ni kuanza kumtafuta katika kambi hiyo.
Alitumia muda wa dakika zaidi ya arobaini na tano, hakufanikiwa kumuona na hata alipoulizia, hakukuwa na mtu aliyekumbuka kama alimuona baada ya tetemeko lile.
“最后一次见他,他就在走廊” (Mara ya mwisho kumuona alikuwa koridoni) alisema jamaa mmoja, mkono wake ulikuwa umevunjika na alifungwa POP.
“他在哪里?” (Yupo wapi?) aliuliza Shu Yan.
“我不知道” (Sifahamu) alijibu jamaa yule.
Shu Yan alihisi kuchanganyikiwa, hakuamini kwamba mpaka muda huo hakuwa amemuona rafiki yake aliyekuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati ambaye aliamini kwamba mpaka jengo lile linaanguka usiku, Richard alikuwa ndani ya jengo hilo palepale koridoni.
Siku hiyo hakutaka kukaa kambini, alichokifanya ni kuondoka na kuelekea katika Hospitali ya HKM (Hospital of Kunming Medical) iliyokuwa katikati ya Jimbo la Yunaan.
Alipofika huko, akamuulizia mtu huyo, majina yalipoletwa mikononi mwake na kutazama kama kulikuwa na jina la Richard, hakuweza kuliona.
Hapo ndipo alipochanganyikiwa zaidi, hakujua mahali alipokuwa rafiki yake huyo, moyo wake ukawa kwenye majonzi makubwa. Kila alipokuwa akijifikiria mahali ambapo Richard angeweza kuwepo, hakupata jibu.
Moyo wake ukagubikwa na majonzi mazito, hakujua ni kitu gani alichotakiwa kufanya mahali hapo. Kilio chake kikaongezeka, machozi yakaendelea kumbubujika mashavuni mwake.
Hakuwa na wazazi, mtu pekee ambaye aliamini kwamba angempa faraja ya moyo alikuwa mtu mmoja tu, huyu aliitwa Richard ambaye mpaka katika kipindi hicho hakujua mahali alipokuwa.
“Nitamtafuta tu, siwezi kumuacha, ninampenda Richard, ni ndugu yangu, rafiki wangu pia, siwezi kumuacha, ni lazima nimuone tena, na hata nisipomuona, nataka kuiona maiti yake tu niridhike” alisema Shu Yan huku akijifuta machozi yake.
Kumpoteza Richard lilikuwa pigo kubwa maishani mwake.

Je Shu Yan ataweza kumpata Richard akiwa hai au maiti?
Je Richard amekufa au yupo hai?
Je huyu Richard ni nani?
Tukutane kesho saa nane mchana mahali hapa.
 
SEHEMU YA 02


Watu walikuwa wamekusanyika nyumbani kwa bwana Walusanga Ndaki kwa ajili ya kusherehekea siku yake ya kuzaliwa ya kufikisha miaka arobaini na mbili. Kelele za shangwe zilikuwa zikisikika nyumbani hapo, watu walikula na kunywa mpaka kusaza.
Bwana Walusanga alikuwa Mtanzania aliyekuwa akiishi nchini China ndani ya jiji la Chuxiong. Alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa matajiri ambao walimiliki kiasi kikubwa cha fedha katika akaunti yake.
Japokuwa kulikuwa na ugumu kujenga nyumba nchini China hasa kwa wageni, kwa bwana Walusanga wala hakupata tatizo lolote lile, alifanikiwa kujenga nyumba zake mbili za kifahari ambazo zilikuwa karibu na Bahari ya Sicbuan.
Alikuwa mwanaume wa Kitanzania lakini kutokana na biashara zake kuwa nyingi, akahamia nchini China ambapo maisha yake yaliendelea kuwa huko huku akiwa na mke wake aitwaye Diana na mtoto wake wa kiume aliyeitwa Richard.
Fedha zilikuwa zikiongezeka kila siku, hakukoma kufanya biashara na Wachina, mara nyingi alikuwa akifungua biashara zake na kuwaajiri Wachina na kuwalipa vizuri tu.
Jina lake likawa kubwa, watu wengi waliokuwa wakiishi katika Jimbo la Kunming ndani ya Jiji la Chuxiong walimfahamu kutokana na ukaribu wake, mapenzi yake kwa watu wa China na hata ajira alizokuwa akizitoa tofauti na wachina matajiri ambao wengi wao hawakutaka kutoa ajira.
“Ningependa kumshukuru mke wangu kwa kunifanya niwe hivi nilivyo, ninampenda sana,” alisema mzee Walusanga, watu wote wakaanza kupiga makofi ya shangwe.
“Mke wangu, hebu sogea hapa kwanza,” alisema bwana Walusanga, mke wake akaanza kusogea pale alipokuwa amesimama, akaupitisha mkono wake begani kwa mkewe.
“Huyu ndiye kila kitu kwangu, ninafanya mambo mengi kwa ajili yake, toka nilipokuwa masikini mpaka katika utajiri huu, bado nilikuwa naye, ninampenda na kumthamini. Kama ningeulizwa ni nani ninayetakiwa kumshukuru katika maisha yangu, ukiachilia Mungu, ningemshukuru huyu mrembo,” alisema bwana Walusanga huku akiachia tabasamu pana.
Makofi yakaongezeka mahali hapo, kila mmoja alionekana kuwa na furaha isiyo kifani. Mara baada ya kumsifia sana mke wake, akamuita mtoto wake aliyekuwa na miaka kumi na saba, Richard na kuanza kumsifia mbele ya wageni wale.
“Huyu naye hayupo nyuma, ni kijana mcheshi sana, ana akili nyingi na pia anafahamu mengi sana, ninapenda kuchukua nafasi hii kumwambia kwamba ninampenda sana, baada ya kifo changu, yeye ndiye atakuwa mrithi wa kila kitu,” alisema bwana Walusanga, kama kawaida watu wakaanza kupiga makofi.
Siku hiyo ilikuwa ni shangwe tu. Muda wa muziki ulipofika, ukafunguliwa na watu kujumuika pamoja.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, kila siku akaunti zake ziliingizwa fedha kutokana na biashara mbalimbali alizokuwa akizifanya nchini hapo, jina lake likawa kubwa, alikuwa akipendwa kila kona.
Kama ilivyo kwa matajiri wengine kuwa na maadui, basi hata kwake ilitokea pia. Matajiri wengi hasa Wachina hawakuwa wakimpenda kwa sababu alizifanya biashara zao kuwa ngumu kufanyika jambo lililowapelekea kuandaa fitina.
Kitu cha kwanza wakaanza kuwatumia viongozi wa serikalini kwa ajili ya kuchunguza mwenendo wake mzima wa biashara zake.
Wakaanza kumchunguza kuhusu ulipaji wake wa kodi, kila kitu kilikuwa poa, hakuwa na tatizo lolote. Walipoona hapo wameshindwa, wakaanza kuchunguza bidhaa zake, kwa kila kitu kilichokuwa kimefanyika, bwana Walusanga alikuwa makini kupita kawaida.
Walipoona wameshindwa, mikakati mipya ikaanza kupangwa kwamba walitakiwa kumuua na kuchukua fedha zake zote zilizokuwa benki. Mpango mzima ukasimamiwa na tajiri mkubwa ambaye alikuwa kwenye ushindani naye, huyu aliitwa Tai Peng.
Pamoja kwamba alikuwa na fedha nyingi lakini kitendo cha kukaa nyuma ya bwana Walusanga kilimuuma, hakumpenda hata kidogo, alimchukia kupita kawaida.
“Ni lazima auawe,” ilisikika sauti ya bwana Tai Peng simuni.
Mkakati mzito ukapangwa, ilikuwa ni lazima bwana Walusanga auawe hata kama alikuwa na ulinzi kiasi gani. Mchakato wa kwanza kabisa kufanyika ilikuwa ni kumuwekea sumu katika kahawa yake ofisini.
Wakacheza mchezo na sekretari kwa ajili ya kukamilisha mpango wao huo, cha kushangaza, sekretari hakufanikiwa kwani hata kahawa hakuwa akinywa, yaani alionekana kama alijua kilichokuwa kikiendelea.
Hawakuishi hapo, walichokifanya ni kumuandalia ajali ya gari, mpango kabambe ukaandaliwa na ulitakiwa kufanyika ndani ya siku chache. Kweli ajali ikatokea, kitu cha kushangaza, hakuwepo ndani ya gari hilo zaidi ya dereva wake na wakati alipokuwa akipanda, walimuona.
Kila kitu walichokuwa wakikifanya, ikashindikana, hapo ndipo walipoamua kumuua kwa kumpa taarifa, kwamba ajiandae kufa, labda kuishi kwa presha kwa kuogopa kufa kungemfanya kuweweseka na hatimae kumuua.
****
“Mke wangu!” aliita bwana Walusanga, alikuwa akitetwa na jasho.
“Kuna nini mume wangu? Mbona upo hivyo?” aliuliza bi Diana.
“Nimepokea ujumbe simuni mwangu.”
“Unasemaje?”
“Umeandikwa kwa kichina, sijajua umeandikwa nini.”
“Sasa umeuelewa? Kwa nini uogope?”
“Nahisi ni wa kitisho, sijawahi kutumiwa meseji ya kichina.”
“Usihofu mume wangu. Inawezekana ukawa ni ujumbe wa kawaida au kuna mtu kakosea namba,” alisema bi Diana.
“Inawezekana kweli?”
“Ndiyo. Lala kwa amani bwana, ukiwa na wasiwasi, utatutia wasiwasi na sisi pia,” alisema bi Diana.
“Ila sina amani.”
“Kwa nini?”
“Huu ujumbe, kila nikiuangalia, nakosa amani,” alisema bwana Walusanga.
“Achana nao, hebu tulale mpenzi,” alisema bi Diana.
Japokuwa alikubaliana na mkewe lakini bado alikuwa na wasiwasi tele, kila alipokuwa akifikiria kuhusu ujumbe ule moyo wake uliendelea kukosa amani. Alijua fika kwamba halikuwa jambo rahisi kwa mtu kukosea meseji kwake, tena mbaya zaidi ujumbe ulikuwa umekuja kwa kichina.
Alichokifanya mara baada ya kuamka ni kumtafuta wakili wake, msichana aliyeonekana kuwa mrembo, mwenye asili ya kizungu, huyu aliitwa Stacie Alexander ambaye alikuwa na uwezo mkubwa wa kuifahamu lugha ya Kichina.
“We are coming to kill you,” (tunakuja kukua) alisema Stacie alipokuwa akiisoma meseji ile.
Hapo ndipo bwana Walusanga akapata uhakika kwamba hofu yake juu ya meseji ile ilikuwa sahihi kabisa, kulikuwa na watu ambao walijipanga kwa ajili ya kumuua.
Hakutaka kujiuliza sababu, alijua kwamba kutokana na utajiri mkubwa aliokuwa nao ndiyo uliowafanya watu kumtafuta na kutaka kumuua, hivyo, akaandaa ulinzi mkubwa.
Kila alipokuwa akienda, ulinzi wake ulikuwa mkubwa zaidi ya kipindi cha nyuma. Alitembea na watu watatu, wote walikuwa na bastola viunoni huku yeye mwenyewe akiwa amevalia vazi kwa ndani lenye uwezo wa kuzuia risasi.
Ulinzi huo haukusaidia kitu, baada ya siku mbili, alijikuta akiwa katikati ya watu waliovaa vinyago huku walinzi wake wote wakiwa wamepigwa risasi.
Bwana Walusanga alikuwa akitetemeka kwa hofu, hakuwa akijua watu hao walihitaji nini mpaka waliamua kumtafuta kwa kiasi hicho. Kitu cha kwanza kabisa, akapakizwa ndani ya gari lenye vioo visivyoonyesha ndani na kupelekwa sehemu ambayo ilikuwa karibu na ule Ukuta wa China.
Akalazwa sehemu iliyokuwa na nyasi nyingi zilizoloana na kisha kuelekezewa mdomo wa bunduki. Alizidi kutetemeka kwa hofu, hakujua watu hao walikuwa wakina nani na walitaka nini kutoka kwake.
Baada ya dakika chache, bwana Tai Peng akatokea mahali hapo. Kwanza akashangaa, alimwangalia mzee huyo kwa macho yenye maswali mengi lakini mwisho wa siku akapewa jibu kwamba alitakiwa kufa mahali hapo kama asingefanya kitu kimoja tu, kuwakabidhi utajiri mkubwa aliokuwa nao.
“Haiwezekani, fedha na mali zangu ni kwa ajili ya mke wangu na mtoto wangu,” alisema mzee Walusanga.
“Unasemaje?”
“Siwezi kutoa kila kitu nilichokuwa nacho.”
Kilichofuata ni kupiga ngumi mfululizo. Japokuwa alisikia maumivu makali lakini msimamo wake ulikuwa uleule, mali na fedha zake zilikuwa ni kwa ajili ya familia yake tu.
“Tufanye nini?”
“Ninaitaka familia yake hapa,” alisema Tai Peng.
Hilo wala halikuwa tatizo, vijana wakaondoka mahali hapo, maagizo waliyokuwa wamepewa ni kwamba ndani ya dakika thelathini wawe wamekwishafika hapo huku wakiwa na familia hiyo.
Hiyo wala haikuwa kazi kubwa, kwa kutumia uwezo wao mkubwa, dakika arobaini baadae walikuwa mahali hapo huku wakiwa wameongozana na mke wake, bi Diana.
Alipomuona mumewe tu, akaanza kulia, hakuamini kama mwanaume mtanashati alikuwa vile kama alivyokuwa. Moyoni aliumia, akaanza kulia mfululizo, akamfuata mume wake na kupiga magoti.
Shati lake lilikuwa limetapakaa damu na uso umevimba, mateso makubwa aliyoyapokea kutoka kwa watu hao yalimpa wakati mgumu mno. Hakuweza kuongea vizuri, kila alipokuwa akimwangalia mke wake, alitamani kuongea lakini sauti haukutoka.
“Mtoto wake yupo wapi?” aliuliza Tai Peng.”
“Hatujafanikiwa kumuona.”
“Acheni utani. Nendeni mkamlete mahali hapa, nataka asikie uchungu juu ya kile kitakachokwenda kutokea kwa familia yake,” alisema mzee Tai Peng.
“Sawa mkuu,” waliitikia vijana wale na kuanza kwenda huko, mikononi walikuwa na bunduki zao, walijiandaa kwa kila kitu, ilikuwa piga ua, lazima Richard aletwe mahali hapo. Hawakujua kwamba kila kitu kilichokuwa kikitokea, bwana Walusanga alikifahamu, hivyo alijipanga vilivyo kwa ajili ya kuzilinda mali na fedha za familia yake.

Je nini kitaendelea?
Je Richard ataweza kupatikana?
Nini kitatokea akipatikana?
Je bwana Walusanga na mkewe, bi Diana watauawa?
Itaendelea.
 
SEHEMU YA 03


Diana alikuwa ndani ya nyumba na mtoto wake, uso wake ulionyesha wasiwasi mwingi, halikuwa jambo la kawaida kwa mumewe kumpigia simu na kutokupokea, na kama kuna siku kitu kama hicho kilitokea, basi alikuwa akimtaarifu kwa njia ya meseji kwamba alikuwa kwenye kikao au sehemu yoyote ile.
Siku hiyo ilikuwa ni ya tofauti sana, alikuwa mtu mwenye mawazo, kila kitu kilichokuwa kikiendelea kilimtia wasiwasi mno. Maswali hayakuisha kichwani mwake, hakujua mumewe alikuwa wapi, kitendo cha simu yake kuita mpaka kukata, kilimtoa amani kabisa.
Ingawa ilikuwa ni usiku sana lakini hakupata hata lepe la usingizi, kila alipojigeuza huku na kule, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria mume wake tu. Alipoona kwamba ameshindwa kabisa kulala, akatoka nje ya chumba chake na kuelekea sebuleni, huko, bado aliendelea kuwa na mawazo lukuki.
“Jamani, naomba unipigie simu mume wangu uupoze moyo wangu,” alisema Diana huku akiiangalia simu yake.
Hakukuwa na kitu kilichobadilika, bado hali iliendelea kuwa vilevile. Ilipofika saa nane usiku, mara akasikia minong’ono ya watu nje ya nyumba yake, akashikwa na wasiwasi lakini hata kabla hajachukua uamuzi wowote ule, akafungua pazia na kuchungulia nje. Hakuona mtu.
Moyo wake haukuwa na amani hata kidogo, tayari akahisi kwamba kulikuwa na kitu kilichotaka kutokea, alichokifanya ni kuelekea chumbani kwa mtoto wake, Richard, alikuwa amelala fofofo.
Akamsogelea kitandani pale na kukaa karibu yake. Mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda mno.
Baada ya dakika ishirini, akasikia mlio wa risasi, akashtuka, Richard aliyekuwa amelala, akaamka na kushangaa kumuona mama yake akiwa pembeni yake.
“Kuna nini mama?” aliuliza Richard.
“Sijui kuna nini, amka,” alisema bi Diana.
“Baba yupo wapi?”
“Hajarudi.”
“Hajarudi?”
“Ndiyo. Njoo huku,” alisema bi Diana na kumvuta mtoto wake mpaka chooni.
Chooni kulionekana kuwa pa kawaida sana lakini kulikuwa kumetengezwa shimo kwa siri ambalo juu yake lilifunikwa na bati gumu. Halikuwa jambo jepesi kugundua kwamba ndani ya choo hicho kulikuwa na shimo, hata Richard mwenyewe, siku hiyo alikiona kitu hicho kuwa kigeni.
“Mama, kuna nini?” aliuliza Richard wakati mama yake akilitoa bati hilo gumu lililoendana na sakafu.
“Ingia humu.”
“Mama. Niambie kwanza kuna nini.”
“Ingia tu.”
Richard hakuwa na jinsi, kwa sababu aliambiwa aingie, akaingia, akashuka ngazi mpaka chini na mama yake kubaki juu huku akiwa amelirudishia bati lile.
Hapo, kidogo moyo wake ukapata ahueni, kitendo cha kuona kwamba mtoto wake alikuwa sehemu salama kikamuondolea asilimia kadhaa za hofu moyoni mwake.
Wala hazikupita dakika nyingi, mlango ukafunguliwa watu wanne waliokuwa na bunduki kuingia ndani huku wakiongozana na mmoja wa walinzi, bi Diana akajua fika kwamba kidole cha mlinzi ndicho kilichotumika kuufungua mlango huo uliokuwa ukifungwa kwa mashine maalumu mpaka mtu uweke alama ya kidole.
“Hebu twende huku,” alisema jamaa mmoja, sura yake ilikuwa imefichwa na kinyago.
Bi Diana alikuwa akitetemeka kwa hofu, kijasho chembamba kikaanza kumtoka, kila alipokuwa akiwaangalia watu wale, hawakuonekana kuwa na huruma. Wakamchukua na kuanza kuondoka naye mahali hapo.
Nje, walinzi wote waliokuwa wakilinda mahali hapo walikuwa chini, damu zilikuwa zikiwatoka, walikuwa wamekufa baada ya kupigwa risasi za kichwa na kifua, kwa jinsi picha ilivyokuwa ikionekana mahali pale, bi Diana alibaki akilia tu.
Njiani, bi Diana alikuwa akiomba msamaha tu lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyemuelewa. Gari liliendeshwa kwa mwendo wa kasi mpaka katika sehemu ambayo ilikuwa na kipori fulani na kisha kuteremshwa.
Bado alikuwa na wasiwasi mwingi. Aliposhikwa mkono na kupelekwa kule alipotakiwa kwenda, akamuona mume wake akiwa chini, damu zilikuwa zikimtoka, akashindwa kuvumilia, akaanza kumsogelea, alipomfikia, akamkumbatia na kuanza kulia naye.
“Mume wangu, mume wangu, kuna nini?” aliuliza bi Diana huku akianza kububujikwa na machozi.
Bwana Walusanga hakuweza kuongea, alibaki akigunaguna tu kwa maumivu makali. Uso wake ulikuwa umevimba, damu ziliendelea kumtoka, alitia huruma mahali pale alipokuwa.
Huku wakiwa wamekumbatiana, wakasikia maagizo yakitolewa kwamba hata mtoto wao, Richard alikuwa akihitajika mahali hapo kwa ajili ya kufanya kazi ambayo ilikuwa imebakia.
Wakashtuka, wakabaki wakilia tu huku wakiwa wamekumbatiana, hawakuamini kama mwisho wa kila kitu ungekuwa namna hiyo. Wakati mwingine walikuwa wakijuta kuwa nchini China, ni heri wangekuwa nchini Tanzania, hata kama wangeuawa, basi wangeuawa ndani ya nchi yao.
“Tumuombe Mungu wasimpate Richard,” alisema bi Diana huku akiwa hana uhakika kama Richard hatoweza kupatikana.
****
Wanaume watatu wakarudi ndani ya nyumba hiyo, ilikuwa ni saa tisa usiku na hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akifahamu kile kilichokuwa kimeendelea ndani ya nyumba hiyo. Walichokifanya ni kuzama ndani na kisha kuanza upekuzi wao.
Walianza na vyumbani, kote huko, Richard hakupatikana, hawakuishia hapo, walikwenda jikoni na kufungua makabati yote lakini hakukuwa na mtu yeyote zaidi ya wafanyakazi wa ndani waliokuwa wamewafunga kamba.
“Richard yupo wapi?” aliuliza jamaa mmoja huku akionekana kuwa na hasira.
“Hatujui yupo wapi,” alijibu mfanyakazi mmoja.
“Mnamfichaeee, nitawapiga risasi.”
“Kweli tena hatujui.”
Wanaume wale hawakutaka kuishia hapo, walichokifanya ni kuendelea kumtafuta Richard ndani ya nyumba hiyo. Walimtafuta mpaka inafika saa kumi na moja alfajiri lakini hawakuweza kumpata, walichokifanya ni kuondoka zao. Hawakujua kama Richard alikuwa katika shimo lililokuwa bafuni.
****
Richard alikuwa akitetemeka kupita kawaida, bado aliendelea kushangaa kwa sababu gani mama yake alikuwa amemuingiza ndani ya shimo lile huku baba yake akiwa hajarudi nyumbani hapo japokuwa ilikuwa usiku mzito.
Alibaki shimoni mule huku kichwa chake kikijaza maswali mengi yasiyokuwa na majibu. Baada ya dakika kadhaa, akasikia sauti za watu, mama yake akaanza kulia, tayari akajua kwamba kulikuwa na hatari, hivyo akasogea karibu zaidi ili aweze kusikia vizuri.
Mara kwa mara mlango wa chumbani ulikuwa ukifunguliwa na kufungwa huku sauti za watu wale zikiendelea kusikika, alichokifanya ni kuondoka mahali hapo.
Huku machozi yakimbubujika mashavuni mwake, Richard akaanza kupiga hatua ndani ya bomba lile, kulikuwa na giza totoro lakini hakuonekana kujali, hakujua bomba lile lilipoishia, kitu alichokuwa akikitaka ni kujiona akiwa amefika sehemu salama tu.
Maji machafu yalikuwa yakipita kuelekea mbele kabisa huku sauti za panya zikisikika katika shimo hilo. Mwili wake ulikuwa ukitetemeka lakini hakuwa radhi kurudi nyuma kwani tayari alijua kwamba hali ya amani haikuwa salama nyumbani.
Baada ya dakika kadhaa, akaanza kusikia sauti ya mawimbi, hapo akajua kwamba tayari alikuwa amefika baharini. Akaongeza kasi yake ya kutembea, akatokea katika bahari ya Sicbuan. Hapo ndipo safari yake ndefu maishani mwake ilipoanza, akaanza kukimbia pembezoni mwa bahari, alipoelekea, hakupafahamu, ila alijua kwamba alikuwa baharini, machozi yaliendelea kumtoka lakini hakusimama, alikuwa akiyaokoa maisha yake.
***
Vijana wakarudi kwa bosi wao, japokuwa walikuwa wameagizwa kurudi mahali hapo pamoja na mtoto, hawakuwa naye. Bwana Tai Peng alionekana kukasirika, hakuamini pale alipoambiwa kwamba mtoto Richard hakuwa amepatikana.
Huyo ndiye alikuwa mtu muhimu sana, aliamini kwamba endapo angemuua bwana Walusanga na mke wake, bi Diana bado isingekuwa imejitosheleza kwa sababu kulikuwa na mtu mwingine aliyebaki.
“Mmemkosa vipi?” aliuliza bwana Tai Peng huku akionekana kukasirika.
“Hatujui mkuu.”
“Mlitafuta vyumba vyote?”
“Ndiyo. Lakini tukamkosa.”
“Aagghh! Watatuambia ukweli tu,” alisema bwana Tai Peng.
Bwana Tai Peng akayarudisha macho yake kwa bi Diana, alikuwa akilia huku akiwa amemkumbatia mume wake kipenzi aliyekuwa hajiwezi. Bwana Tai Peng akamchukua bi Diana na kumsimamisha, akaanza kumwangalia usoni, akachukua bunduki yake na kumuelekezea bwana Walusanga.
“Una dakika moja tu ya kutuambia mtoto wako yupo wapi,” alisema bwana Tai Peng huku akiwa amemuelekezea bunduki bwana Walusanga.
Bi Diana hakusema kitu, alikuwa akilia tu. Alimpenda sana mtoto wake, hakutaka kuona akiuawa na wakati alikuwepo. Japokuwa mumewe alikuwa ameelekezewa bunduki na njia mojawapo ya kumuokoa ilikuwa ni kusema ukweli mahali mtoto Richard alipokuwa lakini hakutaka kuwa muwazi.
“Una sekunde thelathini za kutuambia mahali alipokuwa mtoto,” alisema bwana Tai Peng huku akiikoki bunduki yake.
Bi Diana alikuwa akilia tu. Ingawa alikuwa akimpenda sana mtoto wake lakini pia alimpenda mno mume wake. Hakutaka kuona akiuawa, kila alipotaka kusema ukweli mahali mtoto wake alipokuwa, alinyamaza.
“Paaaaaaa,” ulisikika mlio wa risasi, bwana Walusanga alikuwa akipiga kelele huku risasi ile ikiwa imepenya mguuni mwake na kuutoboa mfupa.
Maumivu aliyoyasikia bi Diana moyoni mwake yalikuwa ni zaidi ya maumivu ya mguu aliyoyasikia bwana Walusanga. Uso wake ukabadilika, akashikwa na hasira, akatamani kumrukia bwana Tai Peng, amkabe na kumuua.
“Una sekunde kumi nyingine, tuambie mtoto alipo,” alisema bwana Tai Peng huku akiwa ameielekezea bunduki katika mguu mwingine wa mzee Walusanga.
“Usiwaambie, kama kuniua waache waniue, usiwaambie,” alisema bwana Walusanga kwa maumivu mkali.
Kama alivyoambiwa na mume wake ndivyo alivyofanya, hakutaka kueleza ukweli mahali alipokuwa mtoto wake. Bwana Walusanga aliendelea kumiminiwa risasi mahali pale, ilipotoka miguu, ikahamia mikono na mwisho kummalizia risasi ya kichwa lakini bado bi Diana hakuthubutu kuzungumza ukweli japokuwa alitamani kufanya hivyo.
“Bado na wewe. Tuambie mtoto wako yupo wapi.” Alisema bwna Tai Peng huku akiwa amemunyooshea bi Diana bunduki ile.
“Una sekunde thelathini tu,” aliongezea bwana Tai Peng.

Je nini kitaendelea?
Je bi Lydia atasema mahali alipo Richard?
Itaendelea.
 
SEHEMU YA 04


Ulikuwa ni usiku sana lakini Richard hakutaka kusimama, alikuwa akiendelea kusonga mbele pembezoni mwa bahari ile. Upepo mkali bado uliendelea kuvuma huku kukiwa na giza totoro.
Hakukuwa na mtu yeyote ufukweni hivyo hakuweza kusimama, aliendelea kwenda mbele zaidi na baada ya dakika kadhaa, kwa mbali akawaona watu waliokuwa wamewasha moto huku wakiwa pembeni wakiota moto ule.
Wakati akiendelea kupiga hatua kuwafuata watu wale, mawazo yake yakaanza kurudi nyuma katika kipindi ambacho mama yake alimwambia aingie ndani ya shimo nay eye kubaki juu. Kichwa chake kilikuwa na maswali yasiyokuwa na majibu, kwa nini alimuingiza shimoni na watu wale waliofika mahali pale walikuwa wakina nani, kila alipojiuliza, alikosa jibu.
Alipowafikia watu wale, wote wakashtuka, haikuwa kawaida kumuona mtu ufukweni hapo tena usiku kama huo, walichokifanya ni kumuita na kuanza kumuuliza maswali machache.
“Unatoka wapi?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Nimetoka kule,” alijibu Richard huku akiinyoonyeshea kidole nyia aliyotokea.
“Umefikaje hapa?”
“Nilikuwa nakimbia.”
“Unakimbia nini?”
Richard hakujibu swali hilo, akaanza kumkumbuka mama yake na machozi kuanza kumbubujika mashavuni mwake. Watu wale wakabaki wakimshangaa, wakamwambia wamsogelee zaidi na hapo ndipo Richard akaanza kuwahadithia.
“Nililetwa huku na mjomba wangu, aliniambia kwamba kulikuwa na sherehe ya watoto huku ufukweni, tulipofika kule, kuna watu wakanifuata na kunichukua, walinipeleka kule kwenye majani kwa lengo la kuniua,” alisema Richard, kila alichokuwa akikizungumza, kilikuwa ni uongo.
“Ikawaje?”
“Nikafanikiwa kuwatoroka.”
“Wapo wapi? Bado wapo kule?”
“Sijajua.”
“Hebu twende tukawaangalie,” alisema mwanaume mmoja, akasimama, akachukua bunduki iliyokuwa pembeni yake.
Kama alivyofanya, na wenzake wakafanya vilevile, nao wakasimama na kuchukua bunduki zao na kumtaka Richard awapeleke kule aliposema kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wakitaka kumuua.
Richard akabaki akitetemeka, hakujua kama wale watu aliokuwa akiwaambia hivyo walikuwa wanajeshi, alichokifanya, akajitoa hofu na kuanza kuondoka nao kuelekea huko, walipofika, hakukuwa na mtu.
“Watakuwa wametoroka tu. Mjomba wako yupo wapi?” alisema mwanaume mmoja na kuuliza.
“Sijui, sijajua kama wamemuua au vipi,” alisema Richard.
Kitu alichokihitaji mahali hapo ni msaada tu, akawaambia watu hao na wao kumuongoza mpaka nje kabisa huku wakisema kwamba ule ufukwe ulikuwa ni wa kijeshi na hivyo hakukutakiwa kuonekana mtu yeyote ambaye hakuwa mwanajeshi.
Alipofikishwa barabarani, Richard akaondoka huku akipita pembezoni mwa barabara. ALitembea kwa muda wa dakika arobaini na tano, kwa mbali, mbele yake akauona moto ukiwa umewashwa, akaanza kuusogelea, alipofika eneo lile, kulikuwa na watoto wengi waliokuwa wamelala huku mapipa yakiwa yamesimamishwa, hayo ndiyo yaliyokuwa yamewashwa moto.
Alipofika eneo hilo, Richard akanyata na kwenda sehemu kulipokuwa na maboksi na kisha kukaa hapo.
Machozi hayakukoma machoni mwake, bado yaliendelea kumbubujika mfululizo, kila wakati alikuwa mtu wa majonzi tu, kumbukumbu za kile kilichokuwa kimetokea bado kilimuumiza kwa kuona kwamba ni lazima kulikuwa na kitu kibaya kwani hakikuwa kitu cha kawaida kwa mama yake kumwambia aingie shimoni.
“Kuna kitu, ila ni nini na kwa nini hata baba hakurudi nyumbani?” alijiuliza Richard.
Hicho kilikuwa kitu kingine ambacho kiliuumiza moyo wake. Siku zote baba yake alikuwa akiwahi kurudi nyumbani lakini siku hiyo ilikuwa tofauti kabisa, baba yake alikuwa amechelewa kurudi tofauti na siku nyingine.
Siku hiyo kila kitu kilionekana kuwa tofauti kabisa kwake. Matukio yote yaliyokuwa yametokea yaliacha maswali mengi yasiyokuwa na majibu kichwani mwake.
Mtoto wa kitajiri, usikuwa wa leo alikuwa katika kundi la watoto wa mitaani, shida ambazo alikuwa akizisikia, leo alikuwa akijionea mwenyewe. Alimuomba Mungu amuepushe na vitu vibaya vyote ambavyo vingeweza kutokea maishani mwake na mwisho wa siku amruhusu kukutana tena na wazazi wake, kila alichokuwa akikiomba, kilionekana kuwa kama muujiza kutokea.
Usiku huo alikaa hapo na hakutaka kuondoka. Mawazo yake bado yalikuwa yakiwafikiria wazazi wake tu. Asubuhi ya siku inayofuata ilipofika, kila mtoto wa mtaani aliyekuwa akimwangalia Richard alibaki akimshangaa.
Hakuonekana kuwa kama wao, hakuonekana kuwa na maisha magumu kama waliyokuwa wakiishi. Hakukuwa na mtu aliyemsogelea, kila mmoja alikuwa akimuogopa.
Mtu pekee ambaye alipata ujasiri wa kumsogelea alikuwa msichana ambaye alijitambulisha kwa jina la Shu Yan. Alipomuona Richard amekaa kiunyonge, akapiga hatua na kumfuata, alipomfikia, akaanza kuzungumza naye.
Richard hakuonekana kuwa kwenye hali ya kawaida, alikuwa mkimya na mwenye huzuni tele, kwa Shu Yan ilikuwa ngumu sana lakini mwisho wa siku, Richard akaufumbua mdomo wake.
“Ninaitwa Richard,” alijibu Richard.
Wakaanza kuzungumza kwa kirefu, muda wote, Shu Yan alionekana kujifikiria kitu, maswali kibao yalikuwa yakimiminika kichwani mwake juu ya kijana huyo. Hakuonekana kuwa kama watoto wengine, alikuwa tofauti kabisa.
Hiyo ndiyo ikawa siku ya kwanza kwa Richard kuanza maisha yake mitaani. Baada ya siku mbili, akaziona taarifa kwenye magazeti kwamba baba na mama yake walikuwa wameuawa na miili yao kutupwa ufukweni.
Ilikuwa taarifa mbaya kwake, alijitahidi kuyazuia machozi yasimtoke lakini mwisho wa siku akashindwa, akajikuta akianza kububujikwa na machozi huku moyo wake ukiwa kwenye maumivu makali.
“Mbona unalia?” aliuliza Shu Yan.
“Hakuna kitu. Ninasikitika sana kujiona nikiteseka mtaani, hivi ni lini na sisi tutakuwa na fedha?” aliuliza Richard huku akijitahidi kuuficha ukweli.
“Usijali, tuendelee kuomba tu. Ila naomba tubadili sehemu,” alisema Shu Yan.
“Tubadili sehemu! Kivipi?”
“Twende mji mwingine kabisa.”
“Mji gani?”
“Tuondoke hapa tuelekee Chuxiong na tuelekee Yunnan, nadhani huko tutafanikiwa zaidi kwani hapa kuna watoto yatima wengi,” alisema Shu Yan.
“Tutafikaje huko?”
“Tuombe kwa wiki hii, baada ya hapo, tutapata nauli na kuelekea huko,” alisema Shu Yan.
“Sawa.”
Walikuwa ni marafiki wawili waliokuwa wamezoeana sana, kila sehemu mmoja alipokuwa na mwenzake alikuwa mahali hapo. Walilala pamoja huku wakiomba pamoja mitaani.
Ukaribu wao ukawashangaza watu wengi, halikuwa jambo rahisi kumkuta Mchina akiwa karibu na mtu mwenye ngozi nyeusi kama walivyokuwa wawili hao. Ukaribu wao ukaanzisha maswali mengi lakini hawakuonekana kujali.
Japokuwa baadhi ya maeneo kulikuwa na ubaguzi mkubwa wa rangi lakini hiyo haikufanya wawili hao kuachana, kila walipokuwa waliendelea kuwa pamoja.
“Hivi wazazi wako wapo wapi?” aliuliza Richard.
“Mpaka sasa hivi sijajua, nilipata taarifa kwamba nilitupwa mtaani, niliokotwa na kupelekwa katika kituo cha watoto yatima, baadae nikatoroka,” alijibu Shu Yan.
“Kwa nini ulitoroka?”
“Nilitaka kuwa huru, nilitamani kuwa na fedha zangu, hicho ndicho kilichonifanya nitoroke,” alijibu Shu Yan.
Siku hiyo waliendelea kuulizana maswali mpaka ilipofika saa sita usiku, wakalala katika maboksi kama kawaida yao.
“Usiku mwema.”
“Nawe pia.”
Usiku huo hukuwa wa kawaida, ilipofika saa nane, minong’ono ya watu fulani ikaanza kusikika mahali hapo. Richard akayafumbua macho yake, wanaume wanne walikuwa wamesimama mbele yake huku wakiulizana maswali.
Mapigo ya moyo wa Richard ukaanza kudunda kwa nguvu, ghafla, wakamvamia na kumnyanyua juujuu, Richard akaanza kupiga kelele. Watu wale hawakujali, waliendelea kumbeba na kuanza kuelekea naye sehemu ambayo walipaki gari, walikuwa ni vijana kutoka kwa bwana Tai Peng, walikuwa wametumwa kumchukua Richard na kisha kumuua kama wazazi wake.
****
“Paaaaa…..” mlio wa risasi ukasikika mahali hapo, bi Diana akaanguka chini na kufariki dunia.
Bwana Tai Peng akaichukua bunduki yake na kuanza kuifutafuta, hilo ndilo lilikuwa lengo lake, kitu alichokuwa akikitaka ni kuwaua watu hao na mwisho wa siku kujichukulia fedha zake.
Mtu pekee ambaye alikuwa akikisumbua kichwa chake kwa wakati huo alikuwa Richard tu. Alichokifanya ni kuwaagiza vijana wake ili waende kumtafuta mtoto huyo, popote ambapo wangemkuta ilikuwa ni lazima wamuue nay eye kupelekewa mwili tu.
“Popote mtakapompata, muueni na mniletee mwili wake tu,” alisema bwana Shu Yan kwa hasira.
Vijana hao wakaondoka na kuelekea mitaani, huko, walikuwa na kazi moja ya kumtafuta Richard tu. Halikuwa jambo jepesi kwao, walijitahidi kuzunguka kila kona lakini hawakuweza kumpata.
“Tufanye nini?” jamaa mmoja alimuuliza mwenzake.
“Sijiu. Ila tuendelee kumtafuta. Ni lazima tumpate na lazima tumuue,” alisema kijana mwingine.
Hawakukata tamaa, waliendelea kumtafuta zaidi. Kadri walivyozidi kuzunguka huku na kule wakimtafuta na kumkosa na ndipo hasirza zao zilizidi kuongezeka zaidi. Kwa kuwa Richard alikuwa mtoto mweusi, hapo ndipo walipoanza kuulizia.
Hakukuwa na mtu aliyekuwa akimfahamu, kwa kila mtu aliyeulizwa, alisema kwamba hakuwa akimfahamu mtoto huyo. Baada ya kusumbuka kwa wiki nzima ndipo walipokuja kusikia tetesi kwamba kulikuwa na mtoto mweusi ambaye naye alijiunga na kundi la watoto wa mitaani ambao kazi yao kubwa ilikuwa ni kuombaoba tu.
“Twendeni huko,” alisema jamaa mmoja, wakachukua gari na kuanza kuelekea huko.
Walipofika, wakalipaki gari lao kwa mbali, wakaweza kumuona Richard akiwa na msichana mmoja wa Kichina huku wakipiga stori tu. Kutokana na wingi mkubwa wa watu, hawakutaaka kumfuata, bali walisubiri mpaka giza litakapoingia na ndipo wamfuate.
Baada ya masaa mawili, giza likaanza kuingia, bado hawakuona kama huo ulikuwa muda sahihi wa kumfuata mtoto huyo, ilipofika usiku wa manane, wakaandaa bunduki zao na kuanza kumfuata huku wakionekana kuwa makini sana.
Walipomfikia, wakamvamia, wakambeba juujuu na kuanza kuondoka naye kuelekea ndani ya gari. Hakukuwa na mtu aliyejua, ila kelele za Richard ndizo zilizowafanya watu wengine kushtuka kutoka usingizini, walipoangalia, mtoto huyo alikuwa amebebwa juujuu na watu waliokuwa wamevalia suti, walikuwa wakilifuata gari lao.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 05


Watu wale walikuwa wakiendelea kulifuata gari lao huku wakiwa wamembeba Richard, kitu walichokuwa wakikitaka mahali hapo ni kumpeleka sehemu mtoto huyo na kisha kumuua, hayo ndiyo yalikuwa maagizo waliyopewa na mzee Tai Peng.
Bado Richard alikuwa akipiga kelele za kuomba msamaha huku akiwataka watu wale wamuonee huruma na kumuachia lakini hakukuwa na mtu aliyeelewa, walichokuwa wakikitaka mahali hapo ni kutekeleza maagizo waliyokuwa wamepewa, hivyo tu.
Huku wakiendelea kupiga hatua kulifuata gari lao, ghafla wakaanza kusikia kelele za watu, wale watoto wa mitaani waliokuwa mahali hapo, wakageuka kuona ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, wakashtukia wakianza kupigwa mawe mfululizo.
Hawakurusha mawe peke yake, bali kila kitu kilichoonekana kuwa ni silaha, walikitumia kuwarushia watu hao. Kadiri kelele zilivyoendelea kusikika na ndivyo ambavyo watoto hao wa mitaani pamoja na wahuni kadhaa walivyoendelea kuwasogelea huku wakiendelea kuwarushia mawe na silaha nyingine.
Walipoona kwamba kadiri walivyokuwa wakipiga hatua na ndivyo watu wale walioonekana kuwa na hasira walivyozidi kusogea, kwa kuyaokoa maisha yao, wakamuachia Richard na kuanza kukimbia.
Hiyo haikuwa sababu, japokuwa walikuwa wamemuachia mtoto huyo lakini bado walikimbizwa huku wakirushiwa mawe yao. Mpaka wanalifikia gari lao, kila mmoja alikuwa hoi, wengine walikuwa wamejeruhiwa vibaya, gari likawashwa na kuondolewa mahali hapo.
“Wale ni wakina nani?” aliuliza Shu Yan huku akimuinua Richard.
“Sijui ni wakina nani.”
“Walikuwa wakitaka nini kutoka kwako?”
“Sijui Shu Yan.”
Kuanzia usiku wa siku hiyo Richard akaanza kuishi kwa wasiwasi mwingi, hakuwa mtu wa kujiachia kiholelaholela tu, kila kitu kilichokuwa kimetokea kilimtia hofu kubwa moyoni mwake.
Mpango wa kuomba mitaani kwa ajili ya kutafuta fedha za kuelekea katika Jimbo ya Yunnan haukuwepo tena kwa upande wake, Shu Yan ndiye aliyekuwa akitafuta nauli hiyo.
Baada ya wiki moja, fedha zilizokuwa zikihitajika zikapatikana na hivyo kuamua kuhama katika Jimbo hilo na kuelekea Yunnan.
Hawakuwa na ndugu yeyote yule, walikuwa wawili tu na waliahidiana kusaidia akatika kila kitu. Ndani ya treni, hawakuwa na fedha, zote walizitumia katika nauli ya kuwasafirisha kutoka Chuxiong mpaka huko Yunnan.
Japokuwa walikuwa na njaa lakini hawakuwa na cha kufanya, walikuwa wakivumilia tu mpaka pale walipoingia ndani ya jimbo hilo huku tayari wakiwa wametumia masaa manne.
Maisha mapya yakaanza huko. Shinda iliwatafuta mno na hawakuwa na kitu kingine zaidi ya kuendelea kuomba mitaani. Mtoto wa bilionea ambaye aliogelea fedha, leo hii alikuwa mtoto wa mitaani aliyeishi kwa kuombaomba tu.
Wazazi wake walikuwa wameuawa na hivyo kubaki peke yake tu. Kwa nchini China, hakuwa na ndugu yeyote, watu wengi aliokuwa akiwafahamu na ambao alijua fika kwamba walikuwa ndugu zake walikuwa nchini Tanzania tu.
Wakati mwingine alitamani kurudi katika nchi hiyo ili hata kama itatokea atakufa basi afe akiwa ndani ya nchi hiyo. Hilo halikuwa jambo jepesi kutokea, umasikini aliokuwa nao ulikuwa ni wa kupitiliza.
Mwezi mzima walikuwa ndani ya jiji hilo, alikuwa amekwishazoeana sana na Shu Yan kiasi kwamba kila alipokuwa akimwangalia, alimuona kuwa ndugu yake wa damu, tofauti ilikuwa rangi tu.
“Nataka nipambane mpaka niwe na fedha kama baba yangu,” alisema Richard.
“Kumbe baba yako alikuwa na fedha?”
“Ndiyo. Alikuwa na fedha sana, tena bilionea,” alisema Richard huku akiwa amejiinamia chini.
“Sasa kwa nini hakukuachia hizo fedha?”
“Sijui kwa nini, inaniuma sana, mimi siyo mtu wa kuzurura mitaani na kuomba msaada Shu Yan. Nilizaliwa katika familia yenye fedha sana,” alisema Richard.
“Pole sana.”
“Asante. Hivi umekwishawahi kumsikia mzee fulani anaitwa Walusanga Ndaki?” aliuliza Richard.
“Ndiyo. Ni mzee tajiri sana, alikuwa akitusaidia sana watoto wa mitaani. Alifariki mwezi uliopita, amefanya nini?” alisema Shu Yan na kuuliza swali.
“Ndiye baba yangu.”
“Baba yako?”
“Ndiyo.”
“Acha utani. Mzee Walusanga ni baba yako?”
“Ndiyo.”
“Sasa imekuwaje mpaka upo hapo mtoto wa bilionea?” aliuliza Shu Yan huku akionekana kupigwa na mshangao.
Hapo ndipo ambapo Richard akaanza kusimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea katika maisha yake ya nyuma kabla wazazi wake hawajafariki. Kila alipokuwa akihadithia, Shu Yan alikuwa makini akimsikiliza tu.
Alisimulia zaidi mpaka siku ya mwisho kumuona mama yake huku baba yake akiwa hajarudi nyumbani kwao.
“Pole sana.”
Maisha ya Yunnan hayakuwa mepesi kama walivyotegemea, yalikuwa ni maisha magumu yaliyowafanya kulala siku nyingi na njaa kuliko kula. Hawakukata tamaa, bado walikuwa pamoja huku maisha ya kuombaomba mitaani ikiendelea kama kawaida yao.
Hawakuwa na pa kulala, kila siku walilala mitaani ila baada ya kukutana na binti aitwaye Lucy Liu, akawaambia kwamba hawakutakiwa kuteseka kwa kukosa pa kulala bali kulikuwa na jumba moja kubwa la ghorofa ambalo lilitengwa kwa ajili ya kuishi kwa watu wasiokuwa na nyumba.
Hawakutaka kuuliza, wakataka kupelekwa katika jumba hilo, Lucy akawapeleka na walipofika, wakaanza kupanda juu. Ndani, kulikuwa na idadi kubwa ya watoto, wengi wao walikuwa wakilala koridoni tu.
Hayo ndiyo yakawa makazi yao mapya, kila siku walipokuwa wakitoka katika mizunguko yao, walirudi mahali hapo na kulala katika korido kwa kubanana na watoto wengine.
“Ni lazima baba yako atakuwa ameacha fedha, inakupasa kujua hizo fedha zipo wapi,” alisema Shu Yan.
“Nitajuaje?”
“Sijui, ila ni lazima ujue,” alijibu Shu Yan.
Hayo ndiyo yalikuwa maneno aliyokuwa akiyazungumza Shu Yan kila siku. Alijua fika kwamba Richard alikuwa mtoto wa bilionea na hivyo hakutakiwa kuishi maisha aliyokuwa akiishi katika kipindi hicho.
Kila alipokuwa akimwangalia Richard, aliuona utajiri wa wazi machoni mwake, kijana huyo hakutakiwa kuwa hivyo kwa kuwa alitoka katika moja ya familia ya kitajiri sana.
Baada ya mwezi mmoja kumalizika, usiku wa siku moja, walipokuwa wakijiandaa kulala koridoni, Shu Yan akamvuta Richard pembeni na kuanza kuongea naye, maneno mengi aliyoyaongea siku hiyo ni kwamba ilikuwa ni lazima wamtafute wakili wa baba yake kwa kuamini kwamba mtu huyo angekuwa akifahamu mengi kuhusiana na fedha hizo.
Hilo halikuwa na tatizo, kwa kuwa alikuwa akimfahamu wakili wa baba yake, akaahidi kumtafuta ili amwambie ukweli juu ya utajiri wa baba yake.
“Tukimpata huyo, basi tutakuwa tumetoka kwenye umasikini,” alisema Shu Yan.
“Kweli?”
“Ndiyo. Cha msingi tuanze kumtafuta kesho.”
“Hakuna tatizo.”
“Sawa. Ngoja niende chooni. Nikirudi tutaongea mengi mahali pa kuanzia kesho kabla ya kulala,” alisema Shu Yan.
“Sawa. Nakusubiria,” alisema Richard.
Shu Yan akainuka na kuelekea chooni huku akimuacha Richard akiwa na baadhi ya watoto wengine wa mitaani koridoni pale.
Isiku wa siku hiyo katika kipindi ambacho Shu Yan alikuwa chooni na Richard kuwa koridoni ndiyo ulikuwa usiku ambao tetemeko la ardhi likatokea na jumba hilo kuangushwa huku baadhi ya watu wakifariki dunia na mamia kujeruhiwa vibaya.
Mpaka ilipofika kesho asubuhi, bado Shu Yan hakujua Richard alikuwa wapi. Japokuwa alijitahidi sana kumtafuta lakini mahali alipokuwa kulionekana kuwa mtihani mkubwa na mgumu kupafahamu.
“Upo wapi Richard, njoo tena kwangu, hata kama umekufa, nitataka kuuona mwili wako,” alijisema Shu Yan, naye alikuwa miongoni mwa watu walionusurika katika tetemeko hilo la ardhi.

Je nini kitaendelea?
Je Richard amekufa?
 
SEHEMU YA 06


ILIPOISHIA

Tetemeko la ardhi linatokea katika Jimbo la Yunnan nchini China, watu wengi wanapoteza maisha na wengine kujeruhiwa baada ya majengo makubwa kuanguka. Katika tetemeko hilo, msichana wa Kichina Shu Yan anampoteza rafiki yake kipenzi mweusi, huyu anaitwa Richard.
Alijaribu kufuatilia kila sehemu kuona kwamba inawezekana akawa majeruhi, akamkosa, akajaribu kuziangalia maiti zote, napo hakuwepo, anabaki na sintofahamu.
Upande wa pili, kabla ya tukio hilo, baba yake Richard, mzee Walusanga alikuwa tajiri mkubwa nchini China, alimiliki majumba ya kifahari na biashara nyingi ambazo zilimpatia fedha kila siku.
Huku maisha yakiendelea, anatokea tajiri mwingine wa Kichina, huyu anaitwa Tai Peng. Kitu anachokitaka ni kuchukua utajiri wa mzee Walusanga, anachokifanya, anamuua yeye na mke wake, bi Diana na kisha kuanza kumtafuta Richard kwa ajili ya kumuua kwani bila kufanya hivyo aliona kwamba kungeweza kutokea tatizo lolote na hata huo utajiri wa mzee Walusanga asiupate.
Amewatuma vijana wake kumtafuta mtoto huyo ambaye hana baba wala mama lakini ameachia utajiri mkubwa, wanapofika mitaani, wanafanikiwa kumpata. Huku wakimchukua na kuanza kuondoka naye, watoto wa mitaani na wahuni wanawapiga mawe, wanamuachia na kukimbia.
Shu Yan ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa Richard, anamshauri walihame jimbo la Chixong na kwenda Yunnan, wanakwenda huko huku lengo lao likiwa ni kutafuta maisha kwa kuombaomba mitaani.
Je nini kitaendelea?
Je bwana Tai Peng ataweza kumpata Richard?

SONGA NAYO....

Bwana Tai Peng alionekana kuwa na hasira, hakuamini kile kilichokuwa kikizungumzwa na vijana wake kwamba walifanikiwa kumkamata Richard lakini bahati mbaya watoto yatima na wahuni wengine wa mitaani walikuwa wakiwarushia mawe na vitu vingine vilivyowapelekea kumuacha mtaani na wao kuondoka.
Kila alipokuwa akiwaangalia watu wale, aliyauma meno yake kwa hasira, akajikuta akianza kujipapasa kiunoni, akaichukua bunduki yake na kuwamiminia risasi vijana wake.
Macho yake yalibadilika, mwili wake ulikuwa ukitetemeka kwa hasira, hakuamini kwamba mchakato wake mzima wa kumtafuta Richard na kumuua ulikuwa umeshindikana kwa mara ya pili.
Huyo ndiye alikuwa mtu pekee aliyebaki katika dunia hii na ambaye alikuwa na uhitaji wa kutumia uwezo wake wote, nguvu zake zote kuhakikisha kwamba mtoto huyo anauawa na mambo mengine kuendelea.
Huku akiwa anamfikiria Richard, kulikuwa na kitu kingine kilichokuwa kikikiumiza kichwa chake, hiki kilikuwa ni jinsi ya kuupata utajiri mkubwa aliokuwa akiumiliki marehemu mzee Walusanga.
Alihakikisha kwamba anatumia kila njia ili kujua ni kwa namna gani angeweza kupata kiasi hicho cha fedha kilichokuwa katika akaunti zake zote, kitu pekee ambacho alikiona kufaa sana kwa wakati huo ni kumuita kijana aliyekuwa mkali wa kompyuta, ambaye aliwahi kuweka historia ya kuiibia serikali ya China kiasi kikubwa cha fedha kwa kutumia kompyuta, huyu aliitwa Pin Pong.
“Siwezi kufanya kazi hiyo, nipo serikalini, wizi wa namna hiyo ni hatari kwangu,” alisema Pong mara baada ya kuitwa na bwana Tai Peng.
“Usijali. Mtu mwenye akaunti hiyo amekwishakufa, hakuna mtu yeyote anayefuatilia, ukifanikisha, nakupa dola milioni mbili,” alisema mzee Tai Peng, alionekana kuwa na uchu wa kuzitaka fedha hizo.
“Ila serikali itajua.”
“Itajuaje? Itaanza vipi kujua?”
“Kwa hiyo unasema mwenye akaunti kafariki?”
“Ndiyo.”
“Na ndugu zake?”
“Nao wamefariki.”
“Mmmh!”
“Ndiyo hivyo. Ninahitaji unisaidie kufanya hivyo.”
“Sawa. Hakuna tatizo. Kitu cha kwanza kabisa unachotakiwa kukifanya ni kuniandalia kiasi changu cha fedha kama malipo na kisha nitakufanyia hiyo kazi yako, sawa?” alisema Pong na kuuliza.
“Hakuna tatizo.”
Kuhusu fedha, wala halikuwa tatizo kwa bwana Tai Peng, kwa wakati huo, kitu pekee alichokuwa akikitaka ni kupata fedha kutoka katika akaunti ya mzee Walusanga.
Hakufikiria ni kwa jinsi gani angemuacha Richard katika maisha ya kimasikini, hakujali kama Richard angeishi vipi, kitu ambacho alikuwa akikijali kwa wakati huo na ambacho kwake kilionekana kuwa muhimu ni maisha yake na ya familia yake tu.
Siku iliyofuata, asubuhi na mapema Pong alikuwa mahali hapo na alikuja na vitu vyote ambavyo alitakiwa kuvitumia siku hiyo, cha kwanza kabisa kilikuwa laptop yake.
Ujio wake ndani ya nyumba hiyo ulikuwa siri kubwa, hakutaka mtu yeyote afahamu kitu chochote kile, kwa sababu alikuwa amekwishakatazwa na serikali ya China kufanya wizi wa mtandaoni na hivyo kumpa ajira yenye malipo makubwa, hakutakiwa kujihusisha na wizi huo, kwa hiyo hata kuingia ndani ya nyumba hiyo bado ilikuwa siri kubwa.
“Ninaanza kazi, japokuwa imepita kipindi kirefu, acha niingie mzigoni,” alisema Pong na kisha kuanza kazi.
Japokuwa alikuwa akitumia kompyuta yake ndani ya sebule hiyo huku akiwa amezungukwa na watu zaidi ya saba, mbele yao kulikuwa na televisheni kubwa yenye inchi zaidi ya sitini ambayo ilikuwa imeunganishwa na kompyuta ile huku ikichukua kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika kompyuta ile.
Bwana Tai Peng alikuwa mwenye furaha tele, kila alipokuwa amesimama mahali pale, alitamani kushangilia kwa furaha kwani ndani ya muda mfupi alikuwa akienda kuwa zaidi ya milionea.
Imani yake kubwa ilikuwa kwa Pong aliyekuwa mtaalamu wa masuala ya kompyuta ambaye alisoma mpaka kichwa kikamuuma, aliyajua masomo yote, kuanzia network, programming na mengineyo.
Kazi haikuwa ndogo, kila wakati alikuwa akikuna kichwa chake kuashiria kwamba kile alichokuwa akikifanya hakikuwa kidogo bali kilihitaji utulivu wa hali ya juu. Kitu alichokifanya ni kuingia katika Benki ya Chinesse na kisha kuingiza namba za akaunti ya mzee Walusanga.
Hapo, kompyuta ikaanza kusubiri, akaunti yake ikaja na kuanza kuingiza codes za benki hiyo, hapo napo akaanza kusubiri. Kijasho chembemba kikaanza kumtoka, moyoni mwake alikuwa akimuomba Mungu amfanikishe katika kile alichokuwa akikifanya.
Kwa bwana Tai Peng, muda wote alikuwa na presha, bado alikuwa haamini kama dakika chache zijazo, akaunti yake ingeingiza zaidi ya dola bilioni arobaini. Mwili wake ulikuwa ukitetemeka kwa furaha, kama ilivyokuwa kwa Pong, hata naye kijasho kilikuwa kikimtoka.
“Huleeeeee, nishaningia kwenye akaunti yake, ngoja isome kuna kiasi gani nikutumie,” alisema Pong kwa furaha huku mikono yake ikiwa juu, data zikaanza kujikusanya, wote walitaka kujua kulikuwa na kiasi gani ili fedha ziamishwe, yaani kwa kizungu tungesema ‘Money Transfer’

Je nini kitaendelea?
Je mtaalamu Pong ataweza kuzihamisha fedha hizo?
Je Richard atapona?
 
SEHEMU YA 07


ILIPOISHIA

Tetemeko la ardhi linatokea katika Jimbo la Yunnan nchini China, watu wengi wanapoteza maisha na wengine kujeruhiwa baada ya majengo makubwa kuanguka. Katika tetemeko hilo, msichana wa Kichina Shu Yan anampoteza rafiki yake kipenzi mweusi, huyu anaitwa Richard.
Alijaribu kufuatilia kila sehemu kuona kwamba inawezekana akawa majeruhi, akamkosa, akajaribu kuziangalia maiti zote, napo hakuwepo, anabaki na sintofahamu.
Upande wa pili, kabla ya tukio hilo, baba yake Richard, mzee Walusanga alikuwa tajiri mkubwa nchini China, alimiliki majumba ya kifahari na biashara nyingi ambazo zilimpatia fedha kila siku.
Huku maisha yakiendelea, anatokea tajiri mwingine wa Kichina, huyu anaitwa Tai Peng. Kitu anachokitaka ni kuchukua utajiri wa mzee Walusanga, anachokifanya, anamuua yeye na mke wake, bi Diana na kisha kuanza kumtafuta Richard kwa ajili ya kumuua kwani bila kufanya hivyo aliona kwamba kungeweza kutokea tatizo lolote na hata huo utajiri wa mzee Walusanga asiupate.
Amewatuma vijana wake kumtafuta mtoto huyo ambaye hana baba wala mama lakini ameachia utajiri mkubwa, wanapofika mitaani, wanafanikiwa kumpata. Huku wakimchukua na kuanza kuondoka naye, watoto wa mitaani na wahuni wanawapiga mawe, wanamuachia na kukimbia.
Shu Yan ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa Richard, anamshauri walihame jimbo la Chixong na kwenda Yunnan, wanakwenda huko huku lengo lao likiwa ni kutafuta maisha kwa kuombaomba mitaani.
Je nini kitaendelea?
Je bwana Tai Peng ataweza kumpata Richard?

SONGA NAYO....

Watoa vifusi walikuwa wakiendelea na kazi yao ya kutoa vifusi kama kawaida, miili ya watu waliokufa iliendelea kutolewa huku kukionekana kutokuwa na majeruhi wengine waliokuwa wamebakia.
Hali ilitisha mno, hakukuwa na mtu aliyevumilia, wengi walihuzunika lakini kuna wengine ambao walikuwa wakilia tu, mioyo yao iliumia kupita kawaida.
Wakati wanaendelea kutoa vifusi hivyo, ghafla, watu fulani ambao walikuja na gari la serikali mahali hapo wakaonekana kushtuka, mbali na miili ambayo walikuwa wakiendelea kuitoa katika vifusi hivyo, kulikuwa na mwili wa mtu mmoja, kwa kumwangalia alionekana kama mtu aliyekata roho lakini kwa mbali, mikono yake ilikuwa ikichezacheza.
Walichokifanya watu wale ni kupiga kelele za kuwaita wenzao, walipokuja, wakasaidiana kukitoa kifusi hicho, mtoto aliyekuwa na miaka kumi na saba, akatolewa huku akiwa anahema kwa mbali sana kwani hata waliposikiliza mapigo yake ya moyo, yalikuwa yakidunda kwa mbali mno.
“他死了” (anakufa) alisema mtu mmoja, mmoja wa waokoaji wa watu wale waliokuwa wakitoa vifusi.
“讓他走” (tumpelekeni hospitali) alisema jamaa mwingine.
Hakukuwa na muda wa kupoteza, siku hiyo, hawakuwa wametoa majeruhi hata mmoja, kila waliyekuwa wakimtoa, alikuwa amekwishakufa. Toka siku iliyopita ambapo tetemeko kubwa la ardhi lilikuwa limetokea, ni watu wachache ndiyo waliokuwa wamenusurika kufa, ila wengi walikuwa wamepoteza maisha.
Wakamchukua Richard na kuondoka naye kuelekea hospitali, bado mapigo yake ya moyo yaliendelea kuwa chini mno, kila aliyekuwa akimwangalia mtoto huyo, ilionekana dhahiri kwamba muda wowote ule ungeweza kukata roho.
Mara baada ya kumfikisha katika hospitali ya Jiji la Yunnan, machela ikaletwa, akapakizwa na kuanza kupelekwa katika chumba maalumu kwa ajili ya kuanza tiba.
Alikuwa kijana mweusi, walimkuta katika kifusi cha nyumba ya serikali iliyoanguka, nyumba ambayo ilikuwa ikikaliwa na watu masikini ndani ya jiji hilo.
Kitu cha kwanza kabisa, ili kuyarudisha mapigo yake ya moyo, wakamuwekea dripu yenye dawa maalumu ya kuyarudisha mapigo yake ya moyo katika hali ya kawaida. Katika kila kitu kilichokuwa kikifanyika, Richard alikuwa kimya, hakujua kitu gani kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
****
“Hakuna fedha,” ilisikia sauti ya Pong, kila mmoja akashtuka.
“Unasemaje?” aliuliza bwana Tai Peng huku akisogea karibu zaidi, alitaka kuhakikisha kile alichokuwa ameambiwa.
Alionekana kuchanganyikiwa, maneno aliyosema Pong kwamba ndani ya akaunti ya mzee Walusanga hakukuwa na fedha yoyote ile ilimchanganya. Alipomsogelea Pong, akaanza kuangalia vizuri kwenye kompyuta kwani alihisi kwamba hata kwenye ile televisheni hakuwa akiona vizuri.
Kile alichokuwa amekizungumza Pong ndicho kilichokuwa kimetokea, akaunti ya mzee Walusanga haikuwa na fedha hata dola moja. Zilikwenda wapi? Au zilihamishwa, hakukuwa na mtu mwingine? Hakuna aliyejua.
“Unanitania,” alisema bwana Tai Peng, alionekana kuchanganyikiwa.
“Hakuna kitu, nahisi zilihamishwa,” alisema Pong.
“Unaweza kuangalia ‘bank statement’ ya akaunti tujue zilihamishwa kwenda akaunti gani?” aliuliza bwana Tai Peng, kichwa chake kilichanganyikiwa kabisa.
“Hakuna tatizo.”
Kama ilivyokuwa kawaida, yake, Pong akaanza kazi yake ya kuangalia ni akaunti gani fedha hizo zilikuwa zimehamishiwa.
Kazi haikuwa nyepesi hata mara moja, bado vidole vyake vilikuwa vikiendelea kubonyeza vitufe vya kompyuta yake ya mapajani (laptop). Hata yeye mwenyewe alionekana kuchanganyikiwa, kuingia ndani ya akaunti ile na kukuta hakukuwa na fedha yoyote na wakati aliambiwa kwamba mtu huyo alikuwa bilionea, kulimchanganya.
“Umepata nini?” aliuliza bwana Tai Peng.
“Fedha zake hazikuamishwa ila zilitolewa,” alijibu Pong.
“Nani alizitoa?”
“Sijajua, hilo ndiyo la kufuatilia huko benki,” alisema Pong.
Bwana Tai Peng hakutaka kubaki kimya alichokifanya ni kuwatuma vijana wake waelekee Benki ya Chinesse na kuuliza ni nani alikuwa amezitoa fedha hizo kutoka katika akaunti hiyo.
Baada ya dakika kadhaa, vijana hao walikuwa katika benki hiyo ambapo wakaomba kuonana na meneja kwa kuwaambia kwamba walikuwa vijana kutoka kwa bwana Tai Peng.
Kitu alichokifanya meneja yule ni kupiga simu kwa bwana Tai Peng ambaye akathibitisha kwa wale walikuwa vijana wake na hivyo kuwaruhusu kuingia ndani. Swali aliloulizwa ni moja tu, ni nani aliyekuwa amekuja kuchukua fedha za mzee Walusanga Ndaki.
“Alikuja yeye mwenyewe kama wiki mbili zilizopita,” alijibu meneja.
“Alikuwa peke yake?”
“Kifamilia, alikuja peke yake, ila mbali na hapo, alikuja na mwanasheria wake,” alisema meneja.
“Kwa hiyo walizichukua hizo fedha?”
“Ndiyo. Ila walipoelekea baada ya hapo, hatujui, labda atafutwe mwanasheria wake,” alisema meneja.
“Mwanasheria wake ni nani?”
“Pei Pei Young,” alijibu meneja.
“Huyu mwanasheria maarufu ninayemfahamu?”
“Ndiye huyohuyo.”
“Sawa. Hakuna tatizo. Mpaka nyumbani kwake tunapafahamu. Asante sana,” alisema kijana mmoja na kisha kutoka ndani ya ofisi ya meneja huyo.
***
Taarifa zilipomfikia bwana Tai Peng, moja kwa moja akawatuma vijana wake wengine kwa mwanasheria wa mzee Walusanga, Pei Pei Young aliyekuwa akiishi katika Mtaa wa Wun-Wen uliokuwa pembezoni mwa jiji la Chixiong.
Vijana wale wakajipanga vilivyo, wakachukua bunduki zao na kuanza safari ya kuelekea Wun-Wen. Walipofika huko, hawakutaka kupoteza muda, wakaelekea katika sehemu iliyokuwa na nyumba kubwa na ya kifahari ya mwanasheria huyo.
Walipofika, kwa sababu ilikuwa usiku, kitu cha kwanza kabisa, wakawazimisha walinzi na kuanza kuusogelea mlango wa kuingia ndani huku wakiwa wamekwishaambiwa kwamba mwanasheria huyo na familia yake walikuwa ndani ya nyumba hiyo. Mlango haukuwa na kitasa bali kulikuwa na kimashine kidogo kilichokuwa na vitufe kadhaa kama kalkuleta ambacho hutumika kuingiza namba za siri na mlango kufunguka.
Hapo, wakaonekana kuwa kwenye hali ngumu, hawakuzifahamu namba za kuufungulia mlango huo wa chuma ambao pia haukuwa rahisi kupigwa na kung’oka, walichokifanya ni kuzunguka upande wa pili mpaka kwenye dirisha moja dogo la choo, hapo ndipo walipotaka kupatumia kuingilia ndani.
Wakaanza kubebana na kuvivunja vioo vya madirisha hayo na kupenya ndani. Tofauti na hali ya kawaida, nyumba nzima ilikuwa kimya kitu kilichoonyesha kwamba inawezekana walinzi walikuwa wamewadanganya kwamba mwanasheria Pei Pei alikuwepo ndani ya nyumba hiyo na familia yake, wakawarudia walinzi.
“Mmetudanganya!” alisema jamaa mmoja.
“Wapo ndani. Hakuna mtu aliyetoka,” alisema mlinzi mmoja.
“Mnatutania sasa,” alisema jamaa mmoja, usoni alikuwa amevaa kinyago kama wenzake.
“Kweli tena.”
Hakukuwa na kingine cha kuuliza, alichokifanya ni kuchukua bunduki yake na kummiminia mlinzi mmoja, damu zikaruka na kubaki kimya mahali hapo. Akageukiwa mlinzi mwingine.
“Tuambie ukweli, Pei Pei yupo wapi?”
“Sijui, alikuwa ndani,” alisema mlinzi yule huku akitetemeka kwa hofu, tayari kifo kilikuwa mlangoni.
“Unatutania.”
“Kweli, alikuwa ndani,” alisema mlinzi yule.
Hawakutaka kushughulika naye sana, walichokifanya ni kurudi tena ndani ya nyumba ile na kuanza kumtafuta. Walikwenda kwenye kila chumba na kila sehemu huku wakihakikisha kwamba hakukuwa na handaki.
“Mmemuona?” aliuliza jamaa mmoja.
“Hapana. Ila tuna wasiwasi.”
“Wasiwasi wa nini?”
“Tumesikia minong’ono ndani ya chumba kimoja ambacho kimefungwa, bila shaka wapo huko. Twendeni,” alisema jamaa mmoja na kuanza kuelekea katika sehemu iliyokuwa chumba kile.
Walipoufikia mlango, wakakishika kitasa na kuanza kuufungua, mlango ulikuwa mgumu kufunguka, hawakutaka kukata tamaa, waliendelea kuufungua mlango ule na walipoona kwamba unakuwa mgumu kufunguka, wakaanza kuumiminia risasi mfululizo, sauti za watu waliokuwa ndani ya chumba kile zikaanza kusikika.
“Wapo ndani,” alisema jamaa mmoja na kuendelea kuumiminia risasi mlango ule, wala haukuchukua muda, ukafunguka na kuingia ndani. Mwanasheria, Pei Pei alikuwa amepiga magoti chini huku akilia kama mtoto, mbali na yeye, pembeni mwake kulikuwa na familia yake ambao wote walikuwa wakilia.
“Umetusumbua sana mpumbavu wewe,” alisema jamaa mmoja na kumshika Pei Pei na kuanza kutoka naye nje. Alikuwa akimburuza tu bila kujali kitu chochote kile. Pei Pei akakiona kifo mbele yake.
Ingawa alijua fika mahali fedha zilipokuwa, usiku wa siku hiyo alijiahidi kwamba asingeweza kutoa siri, fedha zile aliambiwa kwamba ni za Richard, alikuwa tayari kuuawa lakini si kuusema ukweli.

Je nini kitaendelea?
Je mwanasheria Pei Pei na familia
 
SEHEMU YA 08


TULIPOTOKA

Mara baada ya kujikusanyia fedha nyingi na kuwa mtu mweusi wa kwanza kuwa tajiri nchini China, mzee Walusanga Ndaki anajikuta akiingia katika matatizo na tajiri wa China aitaye Tai Peng.
Wivu na tamaa ya kutaka kumiliki fedha za mzee Walusanga ndiyo unaompelekea tajiri huyo wa China kumuua mzee Walusanga na mkewe, bi Diana kwa ajili ya kujichukulia fedha hizo.
Huku kila kitu kikiwa kimekamilika, anakuja kugundua kwamba mtoto wa mzee huyo, Richard hakufa hivyo anaagiza vijana wake wamtafute kwani bila kumpata ingekuwa kazi bure kwa kuona kwamba inawezekana fedha hizo alizokuwa akitaka kuzichukua zikachukuliwa na mtoto huyo.
Huku akiwa amewatuma vijana wake kumtafuta na kumuua Richard, anaamua kumuita mtaalamu wa kompyuta kwa ajili ya kuzihamisha fedha za mzee Walusanga na kuziweka katika akaunti yake, cha kushangaza, mtaalamu huyo anapoingia katika akaunti ya mzee Walusanga, hawakuti fedha zozote zile.
Haishii hapo, anawatuma vijana wake waende benki kuangalia ni nani alikwenda kuchukua fedha hizo, ripoti anayopewa ni kwamba mzee Walusanga alikwenda na mwanasheria wake, Pei Pei na kuzichukua fedha hivyo, anachoamuru, Pei Pei atafutwe na kueleza ukweli ambapo vijana hao wanakwenda nyumbani kwa mwanasheria huyo, wanamchukua yeye na familia yake na kuwapeleka chumbani huku wakiwaburuza, kitu wanachokitaka ni kuambiwa mahali fedha zilipo.
Upande wa pili, msichana Shu Yan ambaye ni rafiki mkubwa Richard, haelewi mahali alipokuwa rafiki yake huyo. Mara ya mwisho kuonana naye ilikuwa ni siku ile ambayo tetemeko la ardhi lilitokea katika Jiji la Yuannan. Baada ya hapo, ametembea sehemu nyingi kumtafuta rafiki yake huyo lakini hakufanikiwa kumpata. Kinachomjia kichwani ni kuona kwamba rafiki yake huyo alikuwa amekufa.

SONGA NAYO..

Richard alikuja kupata fahamu baada ya masaa matano kupita. Aliposhtuka tu kutoka katika usingizi huo, macho yake yakaanza kuangalia huku na kule, alikuwa ndani ya ukumbi mkubwa ambapo kulikuwa na vitanda vingi, kote huko kulikuwa na watu waliokuwa wamelala.
Kitu kingine ambacho alikiona mahali hapo ilikuwa ni dripu ya maji aliyokuwa amewekewa huku mdomo na pua yake vikiwa vimefunikwa na chombo maalumu cha kumsaidia kupata hewa safi kitandani hapo.
Japokuwa alijiuliza sana juu ya mahali alipokuwa lakini mwisho wa siku alikuwa na jibu moja tu kwamba mahali alipokuwepo palikuwa ni hospitali na kitu pekee alichokukuwa akikikumbuka ni kwamba mara ya mwisho kabisa alikuwa ndani ya jengo moja la ghorofa walilokuwa wakilitumia kwa kulala usiku, baadae, tetemeko la ardhi likatokea na jengo lile kuanza kuanguka, baada ya hapo, hakujua kile kilichokuwa kimeendelea zaidi ya kujikuta ndani ya chumba hicho.
Mwili wake ulikuwa umefungwa bandeji kitu kilichoonyesha kwamba alikuwa na majeraha makubwa mwilini. Akajitahidi kuinuka kitandani pale lakini akashindwa kufanya hivyo zaidi ya kusikia mwili ukimuuma tu.
Kumbukumbu zake zikaendelea kujirudisha kama mkanda wa filamu, akaanza kumkumbuka rafiki yake kipenzi, Shu Yan ambaye mpaka katika kipindi hicho hakujua alikuwa mahali gani, alitamani kuwauliza madaktari au manesi juu ya rafiki yake huyo, lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyetokea mahali hapo zaidi ya wale wagonjwa wenzake ambao wote walionekana kuwa kwenye hali mbaya.
Wala hazikupita dakika nyingi, nesi mmoja akaingia ndani ya chumba hicho, kwa haraka, akaichomoa ile mashine ya oksijeni iliyokuwa imepachikwa puani na mdomoni mwake na kumuita nesi yule.
“Hautakiwi kuitoa hii,” alisema nesi yule huku akianza kuirudishia mashine ile.
“Subiri kwanza. Hapa ni wapi?”
“Hospitali.”
“Hospitali gani?”
“Shwai Phei.”
“Nani alinileta hapa?” aliuliza Richard.
“Subiri kwanza. Weka hiyo mashine, nitakujibu maswali yako baadae,” alisema nesi yule na kuirudisha mashine ile kwa Richard.
Kichwa chake kilikuwa kwenye mawazo mengi juu ya rafiki yake, Shu Yan, hakujua kama alikuwa hai au naye alikuwa amekufa baada ya tetemeko lile la ardhi ambalo lilisababisha nyumba ile waliyokuwa wakiishi kuanguka.
Aliendelea kukaa hospitalini hapo zaidi, kadiri muda ulivyokuwa ukizidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo majeruhi wengi wa tetemeko lile walivyokuwa wakiletwa. Japokuwa alijiona kuwa na majeraha makubwa lakini kuna kipindi kingine alimshukuru Mungu kwani watu waliokuwa wakiletwa walikuwa zaidi yake.
Hakuwa na ndugu wala rafiki, aliendelea kukaa ndani ya hospitali ile huku hata chakula alichokuwa akila ni kile kilichokuwa kikiletwa maalumu kwa wagonjwa ambao hawakuwa na ndugu wala marafiki ambao walikuja kuwaona.
Hiyo ilikuwa siku ya kwanza, alitegemea kuona Shu Yan akija mahali hapo kama alikuwa hai lakini hakuweza kufika, siku ya pili ilipoingia na kuona kimya, hapo ndipo alipogundua kwamba inawezekana rafiki yake huyo alikuwa amekufa katika tetemeko lile.
“Shu Yan upo wapi? Kama upo hai njoo nikuone na kama ulifariki, naomba nijue sehemu uliyozikwa,” alisema Richard huku machozi yakianza kumbubujika mashavuni mwake.
Ilipofika siku ya tatu, nesi yule ambaye mara kwa mara alikuwa akija kumuona akaingia ndani ya chumba hicho, aliwaacha wagonjwa wote na kwa mwendo wa harakaharaka akaanza kusogea kule alipolazwa Richard.
Mkononi alikuwa na picha ya kijana huyo, uso wake ulikuwa ukionyesha furaha kubwa kitu kilichomshangaza sana Richard kwani siku hiyo alionekana kuwa tofauti na siku nyingine.
Alipomfikia, tabasamu pana likaongezeka usoni mwake, bado Richard alikuwa akishangaa, hakuwa akielewa ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea moyoni mwa nesi yule.
“Kuna nini?” aliuliza Richard huku akionekana kuwa na maswali mengi yasiyo na majibu.
“Huyu ni nani?” aliuliza nesi yule, alikuwa akimuonyeshea picha yake.
“Mmmh! Ni mimi. Umeipata wapi picha yangu?” aliuliza Richard huku akionekana kushtuka.
“Ndugu zako wanakuja kukuona, ilikuwa imebandikwa sehemu zote hapa mjini” alisema nesi yule.
“Ndugu zangu! Ndugu gani? Sina ndugu hapa China, wazazi wangu walifariki,” alisema Ricard.
“Mmmh! Inawezekana vipi? Mbona wao wanakufahamu vilivyo. Bado unaonekana haujakaa sawa, tulia kwanza,” alisema nesi yule.
“Kweli nesi, sina ndugu.”
Nesi hakuonekana kushtuka, bado uso wake ulikuwa wenye furaha kubwa, kitu alichokuwa akitaka ni kuwaona ndugu wa Richard wakifika mahali hapo kwani kwa maelezo yaliyoendana na ile picha yalisema kwamba walikuwa wakimtafuta Richard aliyepotea baada ya tetemeko la ardhi kutokea na kwa mtu yeyote ambaye angefanikisha kupatikana kwake, angepewa dola elfu kumi.
“Nisubiri, nadhani watakuwa wamekwishafika,” alisema nesi yule na kuondoka mahali hapo kwa mwendo wa kasi.
Richard akabaki akijiuliza maswali mfululizo, hakuelewa kile kilichokuwa kinaendelea, kuambiwa kwamba ndugu zake walikuwa wakimtafuta tena kwa kubandika picha zake barabarani kilimshtua.
Hofu ikamshika moyoni mwake, akaanza kuhisi kwamba ndugu hao ambao walizisambaza picha zake, hawakuwa ndugu kama walivyojitambulisha bali walikuwa ni walewale vijana ambao mwezi uliopita walikuwa wamemkamata na kutaka kumuingiza ndani ya gari.
“Hapana, sina ndugu hapa China, wazazi wangu walikwishakufa kitambo,” alisema Richard huku akikisumbua kichwa chake juu ya kitu gani alitakiwa kukifanya mahali hapo kwani tayari aliona kwamba kama angesema akutane na hao watu waliojitambulisha kama ndugu zake, ni lazima angeuawa tu.
Mara mlango ukaanza kufunguliwa! Mapigo yake ya moyo yakawa juu.
****
Mwanasheria Pei Pei na familia yake wakawekwa sakafuni, japokuwa mke wake na watoto wake wawili walikuwa wakilia lakini watu wale hawakutaka kujali. Mikono yao ilikuwa imeshika bunduki, walionekana kuwa na roho mbaya kiasi kwamba wangeweza kuwaua muda huohuo endapo wasingepewa ushirikiano waliokuwa wakiutaka.
Pei Pei alijua kila kitu kilichokuwa kikitokea, alijua fika kwamba watu hao walikuwa wametumwa na wabaya kwa ajili ya zile fedha ambazo alikuwa amezitoa benki na kuzificha kwa ajili ya mtoto wa bilionea Walusanga.
“Tuambie kitu kimoja tu. Fedha zipo wapi?” alisema jamaa mmoja, kwa sauti aliyoitoa, hakuonekana kuwa na masihala hata kidogo.
“Fedha zipi?” aliuliza Pei Pei.
“Paaaaa…” kilisikika kibao kizto kutoka kwa jamaa mmoja, akaanguka chini.
“Tuambie fedha zipo wapi?”
“Fedha zipi?” aliuliza tena, jamaa akakoki bunduki yake.
“Una sekunde thelathini za kutuambia mahali fedha zilipo,” jamaa yule alisema huku akiikoki bunduki yake na kumnyooshea mtoto wake mmoja.
Huo ulikuwa mtihani mgumu kwa Pei Pei, hakujua ni kitu gani alichotakiwa kukifanya. Fedha ambazo alizitoa benki na mzee Walusanga alikuwa amezificha sehemu kwa kuwa katika kipindi ambacho mzee huyo alikuwa akitishiwa, alijua kwamba angeweza kuuawa na hivyo fedha zake kuchukuliwa.
Alikabidhiwa na kuambiwa kwamba ilikuwa ni lazima afanye juu chini kama Richard hatokufa, basi fedha hizo akabidhiwe yeye na kama ikitokea amekufa basi fedha hizo zipelekwe kwa watoto yatima na watu wenye matatizo mbalimbali barani Afrika hasa katika nchi ya Tanzania.
Kitendo cha kulazimishwa aseme mahali fedha zilipo lilikuwa suala gumu kwake lakini pia alipoona kwamba mtoto wake amenyooshewa bunduki tayari kwa kuuawa, huo ukawa mtihani mwingine mkubwa.
Kuna sauti mbili moyoni mwake zikaanza kushindana, kuna moja ilimwambia kwamba ni lazima aseme mahali fedha zilipokuwa ili kuiokoa familia yake lakini kuna sauti nyingine ilimwambia hakutakiwa kufanya hivyo kwani fedha zile hazikuwa za watu wale, fedha zilikuwa za Richard ambaye mpaka katika kipindi hicho hakujua yupo wapi.
“Sijajua mnazungumzia fedha zipi,” alisema Pei Pei huku akianza kulia.
“Paaaaa….” Mlio wa risasi ukasikika mahali hapo, mtoto wake mmoja akaanguka chini, damu zilikuwa zikimtoka kifuani na kuanza kuhangaika pale chini, mara akatulia tuli.
Yalikuwa ni zaidi ya maumivu moyoni mwake, machozi yaliyokuwa yakimbubujika yakaongezeka zaidi, mke wake, akaushika mwili wa mtoto wake na kuupakata huku akianza kulia kwa uchungu.
Ilikuwa ni moja ya picha yenye kuhuzunisha sana, damu zilizokuwa zimetapaa mahali hapo zilionyesha ni kwa jinsi gani watu wale walivyokuwa na roho mbaya. Hasira kali ikamkaba, akatamani kuwarukia vijana wale na kuanza kupambana nao kama mwanaume ila kila alipokuwa akiziangalia bunduki zile, akaamua kutulia.
“Mbona mnaniuliza familia yangu, naomba msifanye hivyo, nitawapa kiasi chochote cha fedha,” alisema Pei Pei huku akiomba kwa kuikutaniha mikono yake na huku akiwa amepiga magoti.
“Hatutaki fedha zako, tunataka fedha zile mlizozitoa benki,” alisema jamaa yule.
“Fedha zipi? Benki ipi? Sijui chochote kile,” alisema Pei Pei huku akilia kama mtoto, japokuwa alikuwa akidanganya, kama watu wale wangekuwa na huruma, wangeyaamini maneno yake.
“Una sekunde thelathini za kutuambia mahali fedha zilipo,” alisema jamaa yule huku akiikoki bunduki yake na kumnyooshea mtoto mmoja wa Pei Pei.
“Una sekunde kumi tu….una sekunde tisa…una sekunde nane…una sekunde saba….” alisema jamaa yule huku akiendelea kuzihesabu sekunde zilizobakia.

Je nini kitaendelea?
Je Pei Pei atakubali kutaja mahali fedha zilipo?
Je Richard ataweza kuuawa hospitalini hapo?
Tukutane kesho.
 
SEHEMU YA 09


TULIPOTOKA...

Mambo yameharibika! Tetemeko kubwa la ardhi linatokea nchini China katika Jimbo la Yunaan, watu wengi wanakufa na wengine kujeruhiwa. Miongoni mwa watu waliojeruhiwa viabaya, yupo mtoto wa bilionea mkubwa aliyeuawa na bilionea wa Kichina, Tai Peng.
Baada ya kuchukuliwa majeruhi, Richard anapelekwa hospitalini ambapo baada ya muda nesi anaingia na kumwambia kwamba kuna ndugu zake wamefika mahali hapo kuja kumuona. Anashtuka kwa kuona kwamba hana ndugu, je hao walikuwa wakina nani?

Upande wa pili, wakili Pei Pei ambaye alichukua fedha benki na bilionea, mzee Walusanga anachukuliwa yeye na familia yake na watu wasiojulikana na kupelekwa sebuleni, hapo, wanataka kujua kitu kimoja tu, mahali pesa hizo zilipokuwa.
Pei Pei hataki kusema kitu, yupo radhi kufa lakini si kuongea ukweli. Huku akiwa amegoma kabisa, mtoto wake wa kwanza anapigwa risasi, anaambiwa aseme fedha zilipo, anagoma, hivyo mtoto wake wa pili kuelekezewa bunduki. Ili kumuokoa mtoto wake, anatakiwa kusema ukweli mahali fedha zilipo.

SONGA NAYO…

Wakili Pei Pei alibaki akitetemeka, machozi yalikuwa yakimbubujika huku moyo wake ukidunda kupita kawaida. Wakati huo, watu hao walikuwa mahali hapo kwa kutaka kujua kitu kimoja tu, sehemu ambapo alikuwa amezihifadhi fedha alizozitoa benki na mzee Walusanga.
Sauti ya yule mtu ikiwa inahesabu ilisikika vilivyo masikioni mwake, tayari mtoto wake mmoja alikuwa amepigwa risasi na sasa hivi walitaka kumpiga risasi mtoto wake mwingine endao tu asingeweza kusema ukweli juu ya mahali fedha zilipokuwa.
Moyo wake haukutaka kabisa kuitaja sehemu hiyo, alibaki kimya huku akiendelea kutetemeka, moyoni alikuwa akimuomba Mungu amuepushie mbali tukio hilo la mauaji lakini kwa wakati huo, aliyasikia maombi yake yakigonga ukuta na kumrudia, hayakusikika kwa Mungu hata chembe.
“Paaaaa….” Ilisikika sauti ya risasi, akayainua macho yake na kumwangalia mtoto wake, alitaka kufahamu kama alipigwa risasi au la. Alichokiona hakuamini, mtoto wake wa pili naye alikuwa chini huku damu zikimtoka kifuani, alikuwa amepigwa risasi moja katika sehemu ambayo wala hakukuwa na nafasi ya kupona tena.
“Noooooo!!!!” alisema Pei Pei kwa hasira.
Alionekana kama mtu aliyechanganyikiwa, kile alichokuwa amekiona kilikuwa ni kitu kilichomuuma mno. Alibaki akilia tu, ghafla akajikuta akisimama na kumvama yule mtu aliyekuwa na bunduki kwa lengo la kutaka kupambana naye.
Kwa wakati huo hakutaka kuogopa, hakujali kama watu wale walikuwa na bunduki au la, kitu pekee alichokuwa akitaka kukifanya ni kupambana na watu hao tu. Japokuwa alikuwa na nguvu za ajabu ambazo hakujua zilitoka wapi lakini alishindwa kupambana nao, akajikuta akipigwa na kitako cha bunduki na kudondoka chini.
“Tunahitaji kujua mahali fedha zilipo,”alisema jamaa yule huku akiikoki bunduki yake, kwa wakati huu, alitaka kumuua mke wake pia.
Huo ukawa mtihani mgumu kwa Pei Pei, hakujua ni kitu gani alitakiwa kukifanya. Tayari aliwapoteza watoto wake wawili ndani ya dakika tano tu, hiyo ikaonekana kutokutosha, pia watu hao walitaka kumuua na mke wake aliyekuwa akimpenda.
Ni kweli alijua mahali fedha zilipokuwa, alijua kila kitu lakini moyo wake haukuwa radhi kuzungumza kitu chochote kile. Yeye mwenyewe alijishangaa, moyo wake ulikuwa tayari kuipoteza familia yake lakini hakuwa radhi kusema mahali fedha zile zilipokuwa.
“Nisamehe mke wangu,” alisema Pei Pei huku akilia, alimwambia mkewe wa uchungu mkubwa moyoni mwake.
Jamaa yule hakunyamaza, aliendelea kuhesabu zaidi, alianzia kumi kushuka chini. Katika kila namba aliyokuwa akiitaja, Pei Pei hakusema kitu, alikuwa kimya huku akiendelea kulia kama mtoto. Ilipofika moja tu, mlio wa risasi ukasikika mahali pale na mke wake kudondoka chini na damu kuanza kumtoka.
Ilikuwa moja ya picha mbaya ambazo aliwahi kuziona katika maisha yake, hakuamini kwamba ndani ya kipindi kifupi angeweza kuipoteza familia yake kwa ajili ya kuzilinda fedha alizopewa ambazo hata hazikuwa zake, upendo wake mkubwa kwa usiku wa siku hiyo ukamponza na kujikuta katika maumivu makali.
Roho ya Pei Pei ilionekana kuwa ya kishujaa, watu wale hawakuamini kama mtu alikuwa tayari kuiona familia yake ikiuawa lakini si kusema mahali fedha zilipokuwa. Alichokifanya jamaa yule mara baada ya kuona Pei Pei hakusema kitu, akachukua bunduki yake, akaikoki na kumuelekezea Pei Pei.
“Zamu yako imefika. Tuambie mahali fedha zilipo,” alisema jamaa yule.
“Nipo tayari kuteswa, nipo tayari kuuawa kama ilivyouawa familia yangu, ila sitokuwa tayari kusema mahali fedha zilipo. Kama mnataka kuniua, sawa, niueni nikaungane na familia yangu huko ilipo,” alisema Pei Pei kijasiri mpaka kuwafanya watu wale kushangaa.
“Kumi…tisa…nane….saba….” alihesabu jamaa yule lakini bado Pei Pei hakutaka kuufungua mdomo wake kutaja mahali fedha zilipokuwa, alikuwa tayari kuuawa mahali hapo.
“Nyie niueni tu,” alisema Pei Pei.
Familia yake yote ilikuwa imeuawa, hakuona kama kulikuwa na sababu ya kuendelea kuishi tena, angeishi vipi na wakati familia yake nzima ilikuwa imepigwa risasi, kwake, hayo yalikuwa ni zaidi ya maumivu, hakukuwa na kitu kilichomuuma duniani kama kuona familia yake ikiuawa, tena mbele ya macho yake.
Jamaa yule alipomaliza kuhesabu, akabonyeza kitufe cha bunduki, bahati nzuri kwa Pei Pei na bahati mbaya kwa mpigaji yule wa risasi, haikutoka risasi yoyote ile, risasi zote zilikuwa zimekwisha.
“Nini tena? Muue tusepe zetu,” alisema jamaa mmoja.
“Hakuna kitu.”
“Unasemaje?”
“Risasi zimekwisha.”
“Hapana. Haiwezekani.”
Alichokifanya jamaa yule ni kuifungua risasi yake, hakukuwa na risasi yoyote ile, yaani pamoja na kujiandaa kuja ndani ya nyumba hiyo, hawakuwa wamebeba risasi nyingi kitu kilichoonekana kuwa kama uzembe mkubwa.
“Yaani ni lazima afe hata iweje,” alisema jamaa yule.
“Kwa hiyo tumuue vipi?”
“Tumechome moto ndani ya nyumba hii.”
“Mmmh!”
“Haina jinsi, tufanye hivyo,” alisema jamaa yule.
Huo ndiyo mpango waliokuwa wameafikia kwamba ilikuwa ni lazima Pei Pei achomwe moto ndani ya nyumba yake. Walichokifanya ni kumfunga kamba mikono yake na kisha kuelekea nje ambapo wakachukua dumu la mafuta ya petroli lililokuwa garini na kuanza kuimwagia nyumba ile kuanzia ndani mpaka nje.
“Piga kiberiti,” alisema jamaa mmoja na mwingine kukiwasha kiberiti, kilichofuata, ni mlipuko kubwa na nyumba ile kuanza kuteketezwa kwa moto.
****
Bado Richard alikuwa akitetemeka kitandani pale, nesi aliyeondoka ambaye alisema kwamba kulikuwa na ndugu zake waliokuja kumuona alimtisha, kijasho chembamba kiliendelea kumtoka, huku akiwa kwenye hali hiyo, mara mlango ukafunguliwa.
Mtu aliyeingia, alikuwa nesi mwingine, alipomuona tu akiwa amefumbua macho yake, tabasamu kubwa likautawala uso wake, akaanza kumsogelea na kuanza kuyapima mapigo yake ya moyo.
“Moyo wako unakwenda kasi sana, kuna nini?” aliuliza nesi yule.
“Nataka kuondoka kurudi nyumbani, tena sasa hivi,” alisema Richard huku akionekana kumaanisha kile alichokuwa akikiongea.
“Uondoke kurudi nyumbani! Hapana, subiri kwanza bado haujawa sawa,” alisema nesi yule huku akiiweka mashine ile ya kusikilizia mapigo ya moyo shingoni mwake.
Richard hakutaka kuongea kitu chochote, ili asifikiriwe vibaya, akajifanya kuwa mpole. Nesi yule alipomaliza kazi zake ndani ya chumba hicho kikubwa, akaondoka zake.
Richard hakutaka kuendelea kubaki ndani ya chumba hicho, alichokifanya ni kuchomoa sindano zote za dripu alizokuwa amechomwa na kisha kutoka itandani pale. Kitu pekee kilichokuja kichwani mwake wakati huo ni kuondoka kuelekea mitaani na kwenda kumtafuta rafiki yake, Shu Yan.
Hatua zake kuufuata mlango wa nyuma zilikuwa ni za harakaharaka, hakutaka kutembea taratibu kwa kuhisi kwamba watu wale waliojitambulisha kama ndugu zao wangefika na kumchukua kitu ambacho hakutaka kitokee.
Huku akiwa ameukaribia ule mlango wa nyuma, mlango wa mbele ukafunguliwa, alipogeuka nyuma na kuangalia, nesi yule aliingia na wanaume watatu, kwa jinsi walivyoonekana, walionekana kuwa watu hatari.
“Yupo wapi?” aliuliza jamaa mmoja kwa sauti kubwa, hakujali kama sehemu waliyokuwepo ilikuwa ni hospitalini na wagonjwa walikuwa wengi.
“Alikuwa hapa,” alijibu nesi yule huku akikishika kitanda alichokuwa amelazwa Richard.
“Yupo wapi?” alirudia swali lile, wakati huu akaitoa bunduki yake, nesi akashtuka zaidi.
“Alikuwa hapa,” alijibu nesi yule huku akitetemeka.
Wakiwa bado wanaangalia huku na kule, kwa mbali wakamuona Richard, walimfahamu vilivyo, alikuwa kijana mwenye ngozi nyeusi, walipomuona tu, hapohapo wakaanza kumfuata, alichokifanya Richard ni kuufungua mlango ule wa nyuma na kisha kuanza kukimbia, watu wale wakaanza kumkimbiza, wagonjwa na nesi, wote wakapigwa na butwaa.
Tayari hatari ilikuwa mbele yake, alikuwa akikimbia kwa kasi huku akifungua mlango huu na kuufunga, aliufungua huu na kuufunga. Japokuwa alikuwa akijisikia uchovu mwilini mwake lakini hakutaka kujali, aliendelea kupiga hatua kwa kasi, alipofika nje, akaongeza mwendo na kukimbia zaidi.
“Simamaaaaaa,” ilisikika sauti ya mlinzi mmoja wa getini, alikuwa ameshika bunduki, alionekana kuwa na wasiwasi na Richard.
Wakati anasema hayo, walinzi wenzake wawili nao wakatokea, kama alivyokuwa amefanya mwenzao, nao wakachukua bunduki zao na kumnyooshea Richard ambaye alibaki akitetemeka.
“Wanakuja kuniua,” alisema Richard huku akitetemeka.
“Nani anakuja kukuua?” aliuliza mlinzi mmoja.
Hata kabla Richard hakujibu swali hilo, mlango ule ukafunguliwa na wanaume watatu waliokuwa na bunduki wakatokea. Kwanza kitedo cha kumuona Richard amesimama mbele yao kama hatua thelathini kiliwashangaza, kitu pekee kilichowashtua, kilikuwa ni uwepo wa walinzi waliokuwa wameshika bunduki na kumnyooshea Richard.
Ghafla, wakaona bunduki za walinzi wale zikianza kuwaelekezea wao, walichokifanya, ni kuanza kurushiana risasi mahali hapo. Ilikuwa ni lazima kufanya hivyo, kumpata Richard halikuwa jambo jepesi, walihitajika kumwaga damu kwanza.
“Paaaaa….paaaaa….paaaaa” milio ya risasi ikaanza kusikika mahali hapo. Eneo la hospitalini likaonekana kuwa uwanja wa vita, kwa jinsi hali ilivyoonekana, ilikuwa ni sawa na filamu za kina Anord na Rambo.

Je nini kitaendelea?
Je Richard atakamatwa?
Na je wakili Pei Pei atauawa kama familia yake?
Je fedha zipo wapi?
Je Richard atazipata fedha hizo?
Itaendelea.
 
SEHEMU YA 10


Nyumba ilikuwa ikiteketea, majirani waliokuwa wamelala ndani ya nyumba zao wakaamka na kuanza kutoka nje, kile alichokiona hawakuweza kuamini, nyumba kubwa na ya kifahari ilikuwa ikiteketezwa kwa moto.
Kitu cha kwanza kilichokuja katika vichwa vyao ni kuhusu wakili Pei Pei na familia yake. Kadiri walivyokuwa wakijiuliza ni kitu gani walitakiwa kukifanya na ndivyo ambavyo moto ule uliendelea kuongezeka zaidi kitu kilichowapelekea kuwapigia simu kitengo cha zimamoto ambao walifika mahali hapo ndani ya dakika chache.
“Mmmh! Kitu gani kilitokea?” aliuliza jamaa mmoja huku watu wa zimamoto wakiendelea kuuzima moto ule.
“Hata mimi sifahamu. Nahisi kuna tatizo,” alisema jamaa mwingine.
Hakukuwa na mtu aliyefahamu kilichokuwa kimetokea, walinzi wa mlangoni wa nyumba hiyo hawakuwa wakionekana, kila walipokuwa wakijaribu kuwatafuta, bado hawakuwapata.
Mara baada ya moto kuzimika, hawakutaka kuingia ndani kwani bado kulikuwa na joto kali. Walisubiri kwa takribani dakika ishirini na ndipo baadhi ya polisi waliofika mahali hapo na watu wa zimamoto wakaingia.
“Hii si shoti ya umeme kama nilivyofikiri, nadhani kuna mtu ameichoma moto nyumba hii,” alisema polisi mmoja.
“Hata mimi nahisi hivyohivyo, harufu kali ya ptroli inaeleza kila kitu. Sasa ni nani amefanya hivi?” aliuliza polisi mmoja kwa sauti ya chini huku akiwa ameshika tochi iliyokuwa ikimulika huku na kule.
“Sijajua. Hebu kwanza tuwatafute wahusika wa nyumba hii,” alisema polisi yule wa kwanza.
Walichokifanya ni kuingia ndani ya kila chumba kwa ajili ya kuwatafuta wenyeji wa nyumba ile yaani wakili Pei Pei na familia yake. Hakukuwa na kitu kilichokuwa kimesalia, kila kitu kiliteketezwa na moto ule mkubwa.
Walizunguka katika kila chumba, hawakufanikiwa kumuona mtu yeyote yule ila waliporudi sebuleni kwa mara ya pili, wakafanikiwa kuiona miili ya watu watatu ikiwa sakafuni, miwili ilikuwa ni ya watoto na mmoja ukiwa ni wa mtu mzima, tena alikuwa mwanamke.
“Mungu wangu!” alisema polisi mmoja, kile alichokuwa akikiona mbele yake haikuweza kuaminika.
Miili ilikuwa imeunguzwa vibaya na moto ule, halikuwa jambo jepesi kugundua watu wale walikuwa ni wakina nani kwa kuwaangalia mara moja tu. Bado ilikuwa ikitoa moshi huku ikiwa imekauka mno.
Kilichofanyika ni kuitoa miili ile ndani ya nyumba ile kwa kutumia mifuko mikubwa ya nailoni na kuipeleka nje. Kila mtu aliyeiona, alishika kichwa chake kwa masikitiko makubwa, hawakuamini kile walichokuwa wakikiona.
Wala haukuchukua muda mrefu, mkuu wa polisi wa Jimbo la Yunaan akafika mahali hapo, yeye mwenyewe alionekana kuchanganyikiwa mara baada ya kuiona nyumba ya wakili mkubwa nchini China ikiwa imeteketezwa kwa moto.
Alichokifanya ni kuwafuata baadhi ya majirani waliokuwa pembeni, lengo lake kubwa lilikuwa ni kuwauliza maswali kadhaa.
“Nini kilitokea?” aliuliza mkuu wa polisi, Li Yeng.
“Nadhani kuna mtu amehusika katika mauaji haya,” alijibu jirani mmoja.
“Kwa nini unahisi hivyo?”
“Nilianza kusikia milio ya risasi, ilikuwa mitatu, nilishtuka lakini kabla sijafanya lolote ndani ya nyumba yangu, nikaiona nyumba hii ikiteketea kwa moto,” alisema jamaa huyo.
“Una muda gani hujawahi kumuona Pei Pei?”
“Kama wiki moja hivi.”
“Unahisi yeye ndiye aliyeua?”
“Sijui. Kwani yeye hajafa?” aliuliza jamaa yule.
“Asante kwa ushirikiano wako.”
Miili yote iliyokuwa imetolewa ndani ya nyumba hiyo, mwili wa wakili Pei Pei haukuwepo kitu kilichozua maswali mengi kwamba alikuwepo sehemu gani. Maelezo kutoka kwa baadhi ya majirani yakachukuliwa na kupelekwa katika Kituo cha Polisi cha Yunaan.
Kila mtu aliyeyasoma maelezo hayo aligundua kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilitokea kabla ya nyumba hiyo kuchomwa moto, na mtu wa kwanza ambaye alishukiwa katika madai hayo alikuwa mmiliki wa nyumba hiyo, bwana Pei Pei.
Kama nyumba ilikuwa imepigwa shoti ya umeme, kwa nini kulikuwa na harufu ya mafuta ya petroli? Na kama nyumba ilikuwa imeteketea kwa bahati mbaya, kwa nini dakika chache kabla ya nyumba kuteketea kwa moto kulisikika milio ya risasi?
Mbali na maswali hayo, kulikuwa na swali ambalo lilimtatiza kila mmoja. Kama wakili Pei Pei hakuwa akihusika na mauaji ya familia yake, mbona ndani ya nyumba hakuwepo na wakati gari lake lilikuwepo? Kila swali walilokuwa wakijiuliza, jibu lililokuja ni kwamba Pei Pei ndiye alikuwa muuaji wa familia hiyo.
****
Kamba zilikuwa zimekaza mikono yake, kila alipokuwa akijaribu kujifungua, alishindwakabisa kuzifungua. Watu wale waliokuwa wameiteketeza familia yake wakatoka nje na kisha kuwasha moto nyumba ile.
Wakili Pei Pei alijitahidi kujifungua kamba zile ili aweze kukimbia lakini alishindwa kufanya hivyo kwani zilikuwa zimefungwa vilivyo. Moto ukaingia ndani na kuanza kuteketezwa, ulipomkaribia, akawa hana jinsi, akatulia na kuanza kusali sala zake za mwisho tayari kabisa kwa kuteketezwa kwa moto huo.
Mbele ya macho yake, akaiona miili ya watoto wake na mkewe ikianza kuteketezwa kwa moto ule. Moyo wake ulimuuma lakini hakuwa na jinsi, kila kitu kilichokuwa kikitokea alijiona kama yupo ndotoni ambapo baada ya muda mfupi angeshtuka kutoka usingizini na kujikuta akiwa kitandani.
Hiyo haikuwa ndoto, kila kitu kilichokuwa kikitokea, kilikuwa ni maisha halisi, miili ya familia yake ikaendelea kuteketezwa na moto ule na kuhamia kwake, akaanza kuteketezwa na yeye pia.
Alipiga kelele kwa maumivu makali huku akijaribu kuomba msaada lakini sauti yake haikuweza kutoka kabisa. Mwili wake ukaendelea kuunguzwa kwa moto ule.
“Nisaidieniiiiiiii…..” alipiga kelele Pei Pei lakini bado moto ule uliendelea kumuunguza.
Hakutaka tena kuendelea kuomba msaada tu, aliona kwamba kwa hatua aliyokuwa amefikia sasa alitakiwa kupambana kwa nguvu zake kuhakikisha kwamba anajiokoa kutoka katika moto ule na si kuendelea kuteketea.
Kitu cha kwanza, huku akiendelea kuteketea, akazipeleka kamba zile katika moto mkali, kamba zikaanza kuteketea na mwisho wa siku kukatika. Asilimia sitini ya mwili wake ulikuwa umeteketezwa kwa moto, miguu yake, tumbo na sehemu za usoni zote hizo zilikuwa zimeunguzwa vibaya.
Pei Pei hakutaka kukaa hapo, huku akiwa kwenye maumivu makali akaanza kukimbilia jikoni ambapo hakukuwa na moto kabisa na kisha kujimwagia maji kwa kuamini kwamba angeweza kuyapunguza maumivu makali ya moto ule, alipomalizia, akaufungua mlango na kutokomea zake.
Kwa jinsi alivyokuwa ameunguzwa na moto ule, ilikuwa ni vigumu kugundua kwamba mtu huyo alikuwa wakili Pei Pei, nusu ya sura yake iliunguzwa vibaya huku miguu yake na tumbo lake vikiwa vimeteketezwa vibaya mno.
****
Kwa sababu ilikuwa usiku sana, hakukuwa na mtu aliyeweza kumgundua, hakuwa na msaada mahali hapo, japokuwa alikuwa akitembea kwa maumivu makali lakini alijitahidi kupiga hatua na kuelekea barabarani.
Alipoifikia, akaanza kutembea pembezoni mwa barabara huku akiwa kwenye aumivu makali. Ilikuwa ni usiku sana na alitamani gari lipite ili aombe lifti lakini kwa bahati mbaya kwa upande wake, hakukuwa na gari yoyote ile iliyopita.
Safari yake hiyo ilichukua zaidi ya dakika arobaini na ndipo akafika katika nyumba moja kubwa na ya kifahari, hapo palikuwa ni nyumbani kwa rafiki wake wa siku nyingi, mzee Alexander, mwanaume Mzungu kutoka nchini Marekani, alikuwa wakili kama alivyokuwa.
“Wewe nani?” aliuliza bwana Alexander, alishindwa kumtambua Pei Pei mara moja kwa kumwangalia.
“Pei Pei.”
“Hapana. Eeeeh! Nini kimetokea tena?” aliuliza Alexander huku akionekana kushangaa.
“Nisaidie kwanza, nimepata tatizo,” alisema Pei Pei huku akiingia ndani.
Kwa sababu ilikuwa ni usiku sana, akamuamsha mkewe, bi Amanda ambaye alifika hapo na kuanza kumwangalia Pei Pei. Kwa jinsi alivyoonekana, ilikuwa ngumu mno kumgundua, mwili wake ulikuwa umeungua kwa kiasi kikubwa sana, hatua ya kwanza kabisa kufanyika ilikuwa ni kumpatia huduma ya kwanza kwa kumpaka asali na dawa nyingine ambazo zilionekana kufaa kwa vidonda alivyokuwa navyo.
Muda wote, Pei Pei alikuwa akilia kwa maumivu, kadiri alivyokuwa akipakwa asali na ndivyo ambavyo alilia kama mtoto mdogo. Ngozi yake ya nje ilikuwa imebanduka kwa kiasi kikubwa, aliposhikwa hapa, alilia, aliposhikwa pale, alilia, yaani kila aliposhikwa, alilia kwa maumivu makali.

Je nini kitaendelea?
Je Pei Pei ataweza kupona?
Je Pei Pei ataweza kukamatwa?
Nini kitatokea kwa Richard?
Tuonane kesho mahali hapa.
 
Bado risasi ziliendelea kusikika katika eneo zima la hospitali, watu walikuwa wakikimbia huku na kule kuyaokoa maisha yao. Katika kipindi chote hicho, Richard alikuwa amelala chini kifudifudi huku mikono yake ikiwa kichwani.
Wala hazikupita dakika nyingi polisi wakatokea mahali hapo na kuanza kushirikiana na walinzi wale kuwashambulia watekaji wale kutoka kwa bwana Tai Peng. Mapambano hayo ya kurushiana risasi yalidumu kwa zaidi ya dakika ishirini, vijana wale wakaonekana kuzidiwa hasa mara baada ya risasi walizokuwa nazo kuisha. Hiyo ikaonekana kuwa hatari kwao, kuisha kwa risasi zile kulimaanisha kwamba wangeweza kukamatwa na hivyo kufikishwa mbele ya sheria na kushtakiwa kwa kile kilichokuwa kimetokea hospitalini hapo.
“Tujisalimishe,” alishauri kijana mmoja.
“Hapana. Hapa ni kukimbia tu,” alisema mwingine.
Hilo lilionekana kuwa wazo zuri, walichokifanya ni kuanza kukimbia. Japokuwa polisi wale waliendelea kuwarushia risasi lakini hakukuwa na mtu yeyote iliyompata.
Richard hakutaka kubaki mahali hapo, bado maisha yake yalionekana kuwa kwenye hali ya hatari, alichokifanya, tena huku akiwa mwenye hofu nyingi ni kuinuka na kuanza kukimbia.
Akaingia mtaani, hakutaka kusimama, bado aliendelea kukimbia kwa lengo la kuyaokoa maisha yake. Hakujua mahali alipokuwa akielekea, hakuwa na sehemu yoyote ile, kitu alichokuwa akikitaka ni kuondoka tu.
Maisha yake yalikuwa na misukosuko mingi, hakujua ni nani alikuwa nyuma ya kila mpango wa kumuua. Hakujua sababu wala hakujua kama watu hao waliokuwa wakitaka kumuua ndiyo waliowaua wazazi wake.
Alikimbia mpaka Gou Nux, hii ilikuwa sehemu pekee iliyokuwa ikitumiwa na vijana wengi Jijini Yunaan kwa kucheza michezo ya kamari. Alipofika hapo, hakutaka kuwafuata vijana waliokuwa wamejikusanya sehemu tofautitofauti kwa kutengeneza makundi, alisogea pembeni kabisa na kutulia juu ya mbao na kuanza kufikiria misukosuko kadhaa aliyokutana nayo.
Aliiona dunia ikiwa imemuelemea, hakuwa na tumaini lolote lile mahali hapo, kila alipokuwa akikaa na kufukiria njia alizokuwa akizipitia, moyo ulimuuma na alibubujika machozi mashavuni mwake.
“Mungu nisaidie, peke yangu sitoweza, na kama unaona ni jambo jema kuwafuata wazazi wangu, naomba ulifanikishe hilo haraka,” alisema Richard huku akionekana kukata tamaa kabisa.
Hapo ndipo mawazo juu ya msichana aliyekuwa naye karibu ambaye alikuwa rafiki yake mkubwa, Shu Yan yakamjia kichwani mwake, alijiona kupata nguvu mpya ya kutaka kuondoka na kwenda kumtafuta msichana huyo ambaye mpaka katika kipindi hicho hakujua kama alikuwa hai au naye alikufa katika jengo lile lililodondoka.
Safari yake ikaanza, alikuwa akielekea kule kulipokuwa na jengo lile walilolitumia kwa ajili ya kusogezea siku zao, alijua kwamba lilikuwa limeanguka lakini lengo la kwenda huko, alitaka kuona kama angeweza kusikia kuhusu mwili wa msichana huyo.
Alipofika, ni vifusi tu ndiyo vilikuwa vimekusanywa sehemu mbalimbali, alijaribu kuangalia huku na kule kwa kutegemea kwamba angeweza kumuona Shu Yan, hakuweza kufanikiwa.
“Shu Yan upo wapi? Au na wewe ulikufa kama wengine?” alijiuliza Richard bila kupata jibu.
Alichokifanya ni kuulizia kuhusu sehemu walipokuwa wamepelekwa majeruhi na miili ya watu waliokufa katika tetemeko hilo walipopelekwa, hilo wala halikuwa tatizo, akaambiwa mahali majeruhi na miili ilipopelekwa na kuanza kwenda huko.
Kichwa chake kilikuwa na mawazo mengi, sala ya kimoyomoyo ilikuwa ikiendelea moyoni mwake, hakutaka kusikia kwamba Shu Yan alikufa katika jengo lile lililodondoka na hata kama ilitokea na yeye kujeruhiwa, alimuomba Mungu asiwe amepatwa na majeraha makubwa yatakayomfanya kushindwa kufanya chochote kile.
“Nimekuja kumuona rafiki yangu,” alisema Richard mara baada ya kufika katika zahanati ndogo ya muda iliyojengwa kwa maturubai kwa ajili ya watu walioathirika na tetemeko hilo.
“Anaitwa nani?”
“Shu Yan.”
“Ana miaka mingapi?”
“Kumi na sita.”
“Anaishi wapi?”
“Alikuwa akiishi katika jengo la serikali.”
“Sawa. Nisubiri hapahapa.”
Nesi Yule akaondoka, Richard akabaki benchini na kumsubiria. Idadi ya watu bado ilikuwa kubwa mahali hapo, wapo watu waliokuwa wameumia vibaya mpaka bandeji walizokuwa wamefungwa kuwa na madoa ya damu. Kila alipokuwa akiwaangalia, alimshukuru Mungu kwa kumlinda.
“Nimerudi,” alisema nesi baada ya kumrudia Richard.
“Vipi?”
“Sijamuona mtu huyo.”
“Hapana. Umeangalia vizuri?”
“Ndiyo. Una uhakika ni majeruhi?”
“Hapana. Sina uhakika sana. Lakini nilihisi ameletwa mahali hapa,” alisema Richard.
“Nenda kajaribu kuangalia katika hospitali ya jiji, inaelekea alifariki na mwili wake kupelekwa huko,” alisema nesi yule.
Richard hakutaka kuendelea kukaa mahali hapo, alichokifanya ni kuondoka huku akionekana kuwa na mawazo lukuki. Wala hakuchukua muda mrefu, akafika katika hospitali hiyo ambapo aliulizia kwamba anamtafuta ndugu yake na kupelekwa katika chumba kilichokuwa na maiti za watu waliofariki katika tetemeko lile.
Huku akiwa na hofu, akaanza kuangalia ndani ya chumba hicho kwa kutumia msaada wa mhusika wa chumba kile. Alifunguliwa droo moja baada ya nyingine lakini mpaka wanafika mwisho, hakuweza kuiona maiti ya Shu Yan, akachanganyikiwa zaidi.
“Yupo wapi? Yaani kotekote hayupo, atakuwa wapi sasa?” alijiuliza Richard bila kupata jibu.
****
Pei Pei hakutaka kutoka ndani ya nyumba ya wakili mwenzake wa Kizungu, Alexander, aliendelea kubaki ndani ya nyumba hiyo huku matibabu yakiendelea kila siku. Mwili wake uliharibiwa kwa kiasi kikubwa, madawa makali aliyokuwa akiyatumia ndiyo ambayo kwa kiasi kikubwa yakaanza kuleta nafuu mwilini mwake.
Daktari ambaye alikuwa mtaalamu wa kutibu majeraha ya ngozi hasa inapokuwa imeunguzwa kwa moto, kila siku alikuwa akifika ndani ya nyumba hiyo na kumtibia Pei Pei ambaye kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo hali yake ilizidi kutengemaa.
Bado mawazo yake juu ya familia yake hayakumuisha, kila siku moyo wake ulikuwa ukimuuma mno kila alipokumbuka familia yake ambayo iliuawa ndani ya nyumba yake tena mbele ya macho yake.
Moyo wake ukajawa na maumivu makali, akajiahidi kisasi kwa kila mtu ambaye alihusika katika uteketezaji wa familia yake aliyokuwa akiipenda kwa moyo wa dhati. Kila alipokuwa akikaa, hakusita kuyazungumzia maumivu makubwa aliyoyapata mara baada ya kuiona familia hiyo ikiuawa.
“Ninataka kuondoka, bado kuna kazi ya kufanya,” alisema Pei Pei.
“Hapana. Subiri kwanza, bado haujawa vizuri,” alisema Alexander.
“Najua, lakini kuna mtu nahitaji kumuona kabla hawajamuua.”
“Mtu gani?”
“Mtoto wa mteja wangu, anaitwa Richard.”
“Yupo wapi?”
“Sijajua. Kama nilivyotaka kuuawa mimi na hata huyo pia anatakiwa auawe. Ninahofia kwamba wanaweza kumpata na kumuua. Naomba niondoke niingie mitaani kumtafuta,” alisema Pei Pei.
“Haiwezekani. Bado haujapona.”
“Alex, ninashukuru kwa kila kitu, naomba uniruhusu niondoke. Bado nina safari ndefu mno, naomba uniruhusu tu, bila kufanya hivi atauawa kabla sijampa kile ambacho baba yake ametaka nimpe,” alisema Pei Pei, wakati mwingine alikuwa akiugulia maumivu, bado mwili wake ulikuwa na maumivu na majeraha kadhaa ya kuunguzwa kwa moto.
“Hilo ni jambo lisilowezekana, hata kama umeomba lakini hapana, hauwezi kutoka humu mpaka upone kabisa,” alisema Alexander.
Huo ndiyo uamuzi uliokuwa umefikiwa, lilikuwa jambo gumu kwa Alexander kumruhusu Pei Pei kwenda mitaani kumtafuta mtu aliyekuwa akitaka kumtafuta na wakati hali yake kiafya haikuwa nzuri.
Alijitahidi kumlinda na kumjali kwa kumletea dokta ndani ya nyumba hiyo. Alipewa dawa nyingi ambazo zilimfanya kutengemaa na kuanza kurudi katika hali yake ya kawaida.
Mwezi mmoja ulipotimia huku akiendelea kuwa ndani ya nyumba hiyo, Pei Pei hakutaka kukubali, kila alipokuwa akilala, aliona maono kwamba Richard alikuwa akitafutwa na watu kwa ajili ya kuuawa, kwake, alijiona kuwa mkombozi pekee wa motto huyo.
“Ni lazima nitoroke, siwezi kukaa ndani ya nyumba hii, ni lazima nimtafute Richard nimpe fedha zake,” alisema Pei Pei, siku hiyo alidhamiria kutoroka ndani ya nyumba hiyo.

Je nini kitaendelea?
Tukutane kesho mahali hapa.
Hadithi hii hutolewa kuanzia jumatatu mpaka ijumaa, weekend hupumzika.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom