HADITHI: DIMBWI LA HUBA

HADITHI: DIMBWI LA HUBA

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,638
Image may contain: one or more people, people standing, text, outdoor and water


HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 01
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....
...
Walitembea wakiwa wameangalia chini lakini ghafla
kila mmoja alinyanyua macho kuangalia mbele na moja
kwa moja yalitua kwenye uso wa mwenzake. Wote
waliteremsha macho chini na kuendelea na safari yao
iliyokuwa ikiwakutanisha katika njia moja.
Baada ya hatua mbili, kila mmoja hakukubaliana na alichokiona, wote
wakanyanyua tena macho kupata uhakika wa kile walichokiona. Kila mmoja
aliponyanyua uso wake, walijikuta wakitazamana tena na kuwafanya
watabasamu bila kusema kitu. Kwa vile walikuwa wamekaribiana,
walipishana bila kusemeshana, kila mmoja akatazama chini.
Baada ya kupishana, kila mmoja bado macho yake yalikuwa na hamu ya
kuona zaidi uzuri wa mwenzake. Walitembea hatua zaidi ya sita, mmoja
akaamua kugeuka kumwangalia mwenzake kwa kumuibia, wakati mmoja
anageuka na mwingine naye aliona sehemu ile inafaa kugeuka kumuangalia
mwenzake. Ikawa kama mwanzo, wakakutanisha tena macho yao, safari hii
kila mmoja alisimama na kumtazama mwenzake kwa muda kisha kila mtu
alitikisa kichwa na kugeuka kuendelea na safari yake.
Msichana Zulfa roho ilimuuma kutosikia hata sauti ya kijana mzuri
aliyeugusa moyo wake kwa ghafla, hakuwahi kupenda katika maisha yake,
siku zote moyo wake haukuwahi kuguswa kama siku ile lakini hakupata hata
nafasi ya kusikia sauti yake zaidi ya tabasamu lililousambaratisha moyo wake
na kutamani kumuona tena hata kusikia sauti yake. Lakini kwa bahati mbaya
kwake ilikuwa siku ya kwanza kumuona na hakuwa na uhakika wa kumuona
tena kutokana na muda mwingi kuwa shuleni kwenye ulinzi mkali.
Kilichokuwa kikimuudhi ni tabia ya wanaume wengi kumsumbua
kimapenzi, kwa kuwa moyoni hakuwakubali, alijisikia karaha sana. Lakini
aliyempenda hata salamu yake hakuisikia zaidi ya tabasamu.
Sued naye moyoni mwake alijilaumu kushindwa kumsalimia binti mrembo

kama yule aliyekutana naye, tena mwenye tabasamu mwanana lenye kumtuliza
simba mwenye njaa. Aliamini haikuwa bahati yake, kama ingekuwa hivyo basi
angemsalimia hata kusikia sauti yake. Aliamua kuachana naye na kuendelea na
mambo yake.
***
Sued baada ya mizunguko yake, aliingia katika ‘Internet Cafe’ kuperuzi
mitandao mbalimbali. Baada ya kulipia, alikaa kwenye kompyuta aliyoelekezwa
Akafungua tovuti aliyokuwa anaitaka, akili na mawazo yake vikazama kwenye
mtandao. Siti ya pili aliingia msichana mmoja aliyekuja kuperuzi kwenye
mtandao.
Wakati akiperuzi, kuna kitu kilimtatiza, ikabidi aombe msaada siti ya pili
alipokuwa amekaa Sued aliyekuwa amezama kwenye tovuti.
“Samahani kaka naomba msaada wa...” yule msichana alishindwa kumalizia
sentensi yake baada ya kumuona mtu ambaye hakutegemea kumuona tena.
Wakati huo Sued alikuwa amenyanyua uso wake ili amsikilize yule msichana ana
shida gani, naye akajikuta akishtuka na kushika mdomo.
“Haa!”
“Basi,” yule msichana alisema kwa aibu huku akirudi kwenye kiti chake lakini
Sued hakukubali suala hilo lipite, akanyanyuka hadi kwenye kompyuta ya yule
msichana na kumsemesha:
“Unasemaje mrembo?”
“Aah! Basi.”
“Basi nini mrembo?”
“Basi tu,” Zulfa alijibu akiwa ametazama chini kwa aibu za kikekike.
“Sikiliza mrembo, nina imani leo ni siku yetu ya kwanza kuonana na ajabu
tumeonana zaidi ya mara moja. Mara ya kwanza hatukuzungumza lakini safari
hii nimeweza kuisikia sauti yako ambayo haina tofauti na umbile mantashau
ulilobarikiwa na mwenyezi Mungu. Basi tusiipoteze nafasi hii angalau tujuane
kwa majina ili siku nyingine tukikutana tusiwe na ugeni tena.”
“Naitwa Zulfa Kipepeo.”
“Kipepeo wa Kayenzo?”
“Ndiyo.”
“Mmh! Kumbe mtoto wa mkubwa?”
“Lakini ana haki ya kupendwa na wanaume wazuri kama wewe.”
“Mi naitwa Sued.”
“Jina zuri sana,” Zulfa alisema huku akimwemwesa midomo.
“Halishindi lako,” Sued alijibu mapigo.
“Langu nimelizoea naliona la kawaida lakini lako jipya akilini na moyoni
mwangu. Hakika ni jina zuri, hongera kuwa na jina zuri kama ulivyo mwenyewe.”
“Asante, lakini sikushindi wewe.”
“Kwa mwanamke kuwa mzuri ni jambo la kawaida ila wanaume ni nadra
sana.”
“Asante.”
“Na hapa mjini umefuata nini?”
“Nasoma Shule ya Sekondari ya Wasichana Bwira.”
“Na huku mjini?”
“Siku za Jumamosi huwa tunapewa ruhusa ya kuja mjini mara mojamoja.”
“Nafikiri itakuwa nafasi yetu ya kuonana kila ukija mjini, una simu?”
“Ninayo lakini tukiwa shuleni haturuhusiwi kutumia mpaka tutakaporudi
nyumbani.”
“Shuleni unatakiwa kurudi saa ngapi?”
“Ulikuwa unasemaje?”
“Tungetafuta sehemu tukakaa tuzungumze kidogo.”
“Japo tupo chini ya uangalizi mkali lakini mimi kukutana na wewe ni bahati
kama nyota ya jaha hivyo siwezi kuipoteza.”
Walikubaliana kuondoka pale na kwenda kwenye bustani iliyokuwa karibu
na Ziwa Victoria kupunga upepo. Kila mmoja alikuwa na furaha moyoni kwa
kukipata kile alichokiamini amekipoteza.
Wakawa wanapunga upepo huku Zulfa akiwa amemlalia Sued mapajani
utafikiri wapenzi wa muda mrefu kwa jinsi walivyokuwa.
“Sued yaani Mungu wa ajabu sana,” Zulfa alivunja ukimya.
“Kwa nini mpenzi?”
“Nilijua sitakuona tena, si unajua tukiingia shule hatutoki hasa mimi mvivu
sana kuja mjini.”
“Nina imani leo Mungu alitukutanisha kwa sababu zake.”
“Halafu baby, wiki ijayo nakwenda nyumbani likizo, nina imani utanimisi sana
kwa mwezi mzima, ila kwa vile uhusiano wetu umeanza rasmi baada ya mwezi
kwisha nikirudi kila Jumamosi tutakuwa pamoja.”
“Basi nakuomba ukapajue nyumbani ili ukija uje moja kwa moja.”
“Hakuna tatizo lakini nikitoka kwenu narudi shule moja kwa moja.”
“Mwisho kurudi shule saa ngapi?”
“Saa kumi na mbili jioni.”
“Basi nina imani tuna muda wa kuzungumza mpaka jioni.”
Walikubaliana na kwenda nyumbani kwa akina Sued Mabati, walipofika
walizungumza hadi saa kumi na mbili kisha Sued akamsindikiza mpenzi wake
huyo, mtoto wa tajiri mkubwa jijini. Kabla ya kuachana, Zulfa alimueleza Sued:
“Sued mpenzi, sijawahi kupenda, wewe ndiye mwanaume wangu wa kwanza
kukupenda hata kuutambua mwili wangu, ukinitenda sitakuwa na maisha,” Zulfa alisema kwa sauti ya kubembeleza lakini yenye msisitizo.
“Zulfa nakuahidi mbele ya mwanga huu wa jioni kuwa sitakutenda, macho
yangu yamekuwa kama kipofu aliyebahatika kufumbua macho mara moja na
kukuona wewe peke yako. Nakuahidi sitampenda mwanamke yeyote chini ya
jua zaidi yako.”
“Nashukuru mpenzi wangu baki salama Mungu akipenda tutaonana.”
“Nakutakia safari njema.”
Waliagana kila mmoja akiwa na donda la mapenzi kwa kuona mwezi mmoja ni
sawa na miaka mia moja.
Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 02
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
“Nashukuru mpenzi wangu baki salama Mungu akipenda tutaonana.”
“Nakutakia safari njema.”
Waliagana kila mmoja akiwa na donda la mapenzi kwa kuona mwezi mmoja ni
sawa na miaka mia moja.
SASA ENDELEA...

BAA DA YA MWEZI MMOJA

Baada ya mwezi mmoja kukatika, Sued alitarajia kumuona mpenzi wake Zulfa
lakini haikuwa hivyo. Kila jumamosi ilipofika, aliamini atamuona bila mafanikio.
Alijaribu kuvumilia akiamini labda atamuona lakini haikuwa hivyo, mwezi wa pili
ulikatika bila kumuona mpenzi wake.
Uvumilivu ulimshinda, akaamua kwenda kuulizia shuleni kwao japo ilikuwa
hairuhusiwi mtu baki kwenda kuonana na mwanafunzi zaidi ya mlezi au mzazi.
Sued alifunga safari hadi Shule ya Wasichana ya Bwira, alipofika alisimama
mbali kidogo na shule, akaanza kupanga jinsi ya kuingia shuleni hapo kutokana
na kukutana na tangazo kubwa kabla ya kuingia shule likiorodhesha sheria za
shule ikiwemo ya watu wanaotakiwa kuwatembelea wanafunzi pale shuleni.
Aliamini ingekuwa vigumu kwake kuweza kuingia shuleni ili aweze kuonana
na mpenzi wake Zulfa. Njia nyepesi ilikuwa kusimama pale kama atamuona
mwanafunzi yeyote akitoka nje ya shule amuulizie. Muda nao ulizidi kukatika,
ilipotimu saa nane aliamini kabisa hawezi kuonana naye, akaamua kujitoa
mhanga ili aweze kupata taarifa za Zulfa.
Alisogea hadi kwenye geti la shule, mlinzi alipomuona anasogea alimuuliza:
“Nikusaidie nini kijana?”
“Nimekuja kumuona binamu yangu.”
“Nani?”
“Zulfa.”
“Umesoma bango hilo hapo?”
“Ndiyo.”
“Sasa wewe ni nani yake?”
“Binamu yake.”
“Binamu yake, wewe ni mlezi?”
”Hapana.”
“Sasa umekuja kivipi wakati si mlezi wala mzazi?”
“Nimekuja kuulizia kama amerudi kuna vitu nilimtuma kwa anko.”
“Anko wako nani?”
“Mzee Kipepeo, baba Zulfa.”
“Ulimtuma nini?”
“Sasa mbona maswali yote unamaliza wewe, nikionana yaye nitamueleza
yeye.”
Mara gari la mkuu wa shule lilisimama mbele ya geti la shule, ilibidi mlinzi
aachane kwa muda na Sued ili akafungue geti. Baada ya geti kufunguliwa
mkuu wa shule hakuingiza gari ndani, akamuuliza mlinzi:
“Kijana huyu anafanya nini hapa?”
“Sijui anashinda na binamu yake.”
“Binamu yake nani?”
“Anasema Zulfa.”
“Zulfa! Hapa tulikuwa na Zulfa mmoja, Zulfa Kipepeo.”
“Ndiye huyohuyo.”
“Alikuwa anasemaje hebu mwambie aje hapa.”
“Wee kijana hebu njoo,” mlinzi alimwita Sued kwa sauti ya juu.
Sued alisogea kwenye gari na kumuamkia mkuu wa shule kwa unyenyekevu.
“Shikamoo mzee.”
“Marahaba kijana, una shida gani?” mkuu wa shule alimuuliza akiwa
amemkazia macho.
“Nimekuja kumuona binamu yangu.”
“Nani?”
“Zulfa Kipepeo.”
“Mzee Kipepeo ni nani yako?”
“Mjomba.”
“Sasa hapa ulikuja kufanya nini?”
“Wakati Zulfa anataka kwenda likizo alikuja nyumbani kuniaga, kuna vitu
nilimtuma kwa mjomba lakini nashangaa mwezi wa pili unakatika bila majibu
yoyote ndiyo maana nimekuja ili anieleze mjomba kampa ujumbe gani.”
“Wewe unakaa wapi?”
“Mabati.”
“Sasa kwa nini hukwenda kwake moja kwa moja umekuja huku?”
“Mjomba alitukataza tusiende kwake, mara nyingi nikiwa na shida
humtumia Zulfa.”
“Kwa hiyo huna taarifa yoyote ya Zulfa?”
“Ndiyo.”
“Ni kweli Zulfa miezi miwili iliyopita alikwenda likizo kama wanafunzi
wengine, lakini baada ya muda wa kurudi shuleni kufika Zulfa hakuonekana.
Tulisubiri wiki mbili ndipo tulipouliza kwao na kuelezwa kuwa Zulfa hatarudi
tena shule.”
“Ha! Kwa nini?” Sued alishtuka.
“Zulfa anatakiwa aende kusoma nje ya nchi, kila kitu kilikuwa tayari na
kilichokuwa kinasubiriwa ni siku ya kuondoka.”
“Ina maana hajaondoka?”
“Kutokana na maelezo niliyopewa na mama yake ataondoka mwisho wa
mwezi.”
“Asante mkuu,” Sued alisema huku akigeuka na kuondoka bila kuongeza kitu.
“Kijana...kijana.”
Mkuu wa shule alimwita Sued ambaye alionekana kuchanganywa na taarifa ile
lakini hakugeuka, aliendelea kutembea mpaka alipovuka geti la shule. Baada ya
kutoka eneo la shule, Sued alikwenda kukaa chini ya mti mmoja kisha akaanza
kuangua kilio kwa sauti ya chini kutokana na taarifa zilizoupasua moyo wake za
Zulfa kupelekwa nje ya nchi kusoma, mtu aliyeahidiana naye kuwa wapenzi wa
kufa na kuzikana.
Kila aliyepita pale alimuuliza Sued ana tatizo gani, baada ya kuona maswali
yamezidi alipanda gari na kurudi nyumbani, macho yake yakiwa yamemvimba
kwa ajili ya kulia. Alipofika kwao aliingia chumbani kwake moja kwa moja,
kutokana na kuendelea kuumia aliendelea kulia chumbani kwake.
Mama yake baada ya kumkosa mchana wakati wa chakula, baada ya kumuona
amerudi alimfuata kutaka kujua alikuwa wapi. Alipoingia chumbani alishtuka
hali aliyomkuta nayo mwanaye.
“Sued mwanangu mbona hivi! Unaumwa?”
“Hapana.”
“Sasa mbona upo hivyo?”
“Basi tu mama natamani kufa.”
“Kufa?”
“Ndiyo mama.”
“Kwa nini?”
“Nina imani bila Zulfa siwezi kuishi?”
“Zulfa ndiye nani?”
“Mwanamke niliyemchagua kuwa mke wangu.”
“Sasa huyu Zulfa kafanya nini?”
“Nimeambiwa anataka kwenda nje kusoma.”
“Sasa tatizo nini?”
“Sicho tulichokipanga, mzee wake ana roho mbaya aliona kumuoa mwanaye
ningefaidi.”
“Huyo Zulfa anakaa wapi?”
“Kayenzo.”
“Kayenzo, mtoto wa nani?”
“Kipepeo.”
“Yule tajiri wa Kayenzo?”
“Ndiyo mama.”
“Mwanangu mbona unataka mazito, kwanza baba yako akisikia unafikiri
kutakuwa na usalama? Unataka kumchokoza baba yako? Kwanza mapenzi
umeyaanza lini mpaka kufikia hatua ya kupanga na ndoa wakati huna kazi wala
chumba.”
“Ningejua nitamuweka wapi na anakula nini.”
“Mwanangu achana na wazo hilo, muda ukifika utampata msichana mwingine
mzuri kuliko Zulfa.”

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 03
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
“Mwanangu mbona unataka mazito, kwanza baba yako akisikia unafikiri
kutakuwa na usalama? Unataka kumchokoza baba yako? Kwanza mapenzi
umeyaanza lini mpaka kufikia hatua ya kupanga na ndoa wakati huna kazi wala
chumba.”
“Ningejua nitamuweka wapi na anakula nini.”
“Mwanangu achana na wazo hilo, muda ukifika utampata msichana mwingine
mzuri kuliko Zulfa.”
SASA ENDELEA...

“Mama hakuna mwanamke mwingine atakayempiku Zulfa, mama sikuwahi
kupenda na sitapenda tena zaidi ya Zulfa.”
“Basi ndiyo hivyo amekwenda kusoma na akirudi atatafuta msomi mwenzake
wewe wa kidato cha nne umeula wa chuya.”
“Mama wee fanya utani, mimi bila ya Zulfa siwezi kuishi.”
“Umekula?”
“Kuna faida gani ya kula wakati sina furaha.”
“Mwanangu kula, kila kitu niachie mimi.”
“Utafanya nini?”
“Mimi najua, kula kwanza.”
Sued alikubali kula huku akisubiri kujua mama yake anataka kufanya nini ili
kuweza kumpata Zulfa.
***
Upande wa pili, Zulfa wiki mbili kabla ya kurudi shuleni moyo wake ulikuwa
na shauku ya kumuona mpenzi wake Sued, kiumbe aliyeuteka moyo wake.
Wiki mbili kwake ilikuwa kama miaka ishirini, akiwa amekaa chumbani kwake
akicheza gemu kwenye laptop yake, mama yake alikwenda chumbani kwake
akiwa na uso wa furaha.
“Hodi mwanangu.”
“Karibu mama,” Zulfa aliacha kucheza gemu na kumtazama mama yake,
akakutana na uso uliojaa furaha.
“Mama mbona unaonekana una furaha?”
“Ni kweli mwanangu nina habari njema kwako.”
“Habari gani mama?”
“Ile nafasi aliyokuwa akiitafuta baba yako imepatikana.”
“Nafasi! Nafasi gani?”
“Ya kwenda kusoma nje.”
“Nje wapi?”
“Ina maana huna taarifa kuwa kuna nafasi ya kwenda Sweden?”
“Ndiyo najua.”
“Basi mwanangu baada ya miezi miwili na nusu unatakiwa uondoke kwenda
kuanza masomo.”
“Nitakwendaje wakati sijamaliza shule?” Zulfa alishangazwa na taarifa zile za
ghafla.
“Hiyo siyo sababu, elimu yako haihitaji kumaliza shule unaweza kujiunga tu.”
“Lakini mimi sikupanga kwenda sasa hivi.”
“Hiyo siyo juu yako, wewe ni mtoto tu unatakiwa kukubaliana na
kinachoamriwa na wazazi wako.”
“Sawa, lakini mimi naona hakuna umuhimu wa kwenda kusoma nje kwani
elimu ya sasa nchini imekuwa sana.”
“Acha ujinga huoni watoto wa vigogo wote wanasoma nje?”
“Mbona Wazungu wanakuja kusoma chuo kikuu huku?”
“Zulfa sitaki kuulizwa maswali ya kitoto, mi nilifikiri ungefurahi kusikia
umepata nafasi adimu ya kwenda kusoma nje! Nafasi yenyewe baba yako
kapoteza fedha nyingi ili kuhakikisha unaipata hasa baada ya kuonesha una
uwezo wa kielimu kuliko ndugu zako wote. Tena mimi mama yako ndiye
niliyekuwa nikimsumbua kila siku, hata sehemu aliyokata tamaa nilimpa moyo
na hatimaye imepatikana.”
“Lakini mama mimi sasa hivi siendi popote mpaka nimalize elimu yangu si
bado miezi sita tu?”
“Hiyo miezi sita ya kwako, lakini yetu unatakiwa uondoke haraka ili kuwahi
mwanzo wa masomo mapema.”
“Mama mi siendi.”
“Nini?” mama Zulfa alishtushwa na kauli ya mwanaye.
“Nasema siendi mpaka nimalize shule.”
“Zulfa unatania au unasema kweli?”
“Nasema kweli mama, siendi popote mpaka nimalize shule.”
“Zulfa hebu acha utani mama.”
“Mama nasema kweli wala sitanii, siendi popote mpaka nimalize shule, kama
mlijua hivyo hakukuwa na haja ya mimi kusoma mwaka huu.”
“Hayo unayosema utakuja kumueleza baba yako?”
“Nitamueleza tu mama.”
Mama Zulfa alitoka chumbani kwa binti yake huku akiwa amepoteza furaha
yake na kumshangaa mwanaye kugoma kwenda kusoma nje ya nchi na kutaka
kuendelea na elimu ambayo siku zote ilionekana ya kubabaisha japo kuna shule
za kulipia zilikuwa zikijitahidi kidogo.
Aliamini kinachomsumbua mwanaye ni hali ya mazoea, kuzoea mazingira ya
shule na mashoga zake. Lakini aliamini kama angemuelewesha faida ya kwenda
kusoma nje bila kutumia nguvu wala kulifikisha suala hilo kwa baba yake
angemuelewa.
Chumbani, Zulfa baada ya kutoka mama yake alijikuta akipoteza furaha ya
muda mfupi aliyokuwa nayo ya kuomba muda uende haraka ili aende kuonana
na mpenzi wake Sued. Taarifa ya mama yake iliivuruga furaha yake yote kwa
kumlazimisha kwenda kusoma nje.
Moyoni aliichukia safari ile ya kwenda kusoma nje, kitu alichokitaka mbele
yake ni penzi la Sued na si kingine kwa wakati ule. Aliapa kupigana kwa
nguvu zote ili amalize kipindi kile ndipo ajue atafanya nini.
Jioni mama yake kabla ya kufikisha ujumbe wa Zulfa kwa baba yake,
alimfuata tena chumbani kwake na kumbembeleza:
“Mwanangu Zulfa bado una msimamo wako?”
“Mama mimi siendi popote bila kumaliza muda wangu uliobakia.”
“Sikiliza mwanangu, hebu funguka mawazo. Safari hii ina faida kubwa sana
maishani mwako.”
“Sijakataa, ila mpaka nimalizie muhula wa mwisho. Nimejiandaa kwa ajili
ya kumaliza shule na mawazo yangu yote nimeyaelekeza huko na si nje ya
nchi.”
“Mwanangu hebu nielewe, hii ni nafasi adimu tena nimemlazimisha sana
baba yako, unafikiri atanielewaje?”
“Mwambie miezi sita siyo mingi avumilie nitakwenda.”
“Na masomo nayo yakusubiri?”
“Mlitakiwa mnieleze mapema, nimejifua kuhakikisha mtihani wa mwisho
napata ‘division one’, tena ya alama za juu.”
“Hiyo haina umuhimu kama elimu tuliyokutafutia.”
“Elimu ya hapa kwangu ina muhimu mkubwa, kuna watu tulipinga nani
atamzidi mwenzake, itaonekana nimewakimbia.”
“Hata wakisema, ukirudi utakuwa upo juu kuliko wao.”
“Sawa, lakini mimi siendi.”
“Kwa hiyo upo tayari nimwambie baba yako?”
“Nipo tayari.”
“Haya tusilaumiane.”
“Nitamwambia ukweli.”
Mama Zulfa aliona ushawishi wake umegonga mwamba kutokana na akili za kitoto za mwanaye. Aliamua kwenda kumwambia baba yake huenda akimkemea atabadili msimamo wake.

Itaendelea kesho
 
SEHEMU: 04
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

Mama Zulfa aliona ushawishi wake umegonga mwamba kutokana na akili
za kitoto za mwanaye. Aliamua kwenda kumwambia baba yake huenda
akimkemea atabadili msimamo wake.
Baba Zulfa aliamini ule ni utani wa mwanaye, alijua anamtania mama yake
hivyo hakuwa na wasiwasi na taarifa ile.
Majira ya saa nne usiku baada ya shughuli zote za kutwa, kula na kuoga,
mzee Kipepeo alimtuma msichana wa kazi kumfuata Zulfa aliyekuwa
chumbani amejilaza huku amefura kwa hasira kutokana na taarifa
alizoletewa na mama yake za kwenda kusoma nje ya nchi.
Zulfa alikuja mbele ya wazazi wake waliokuwa wamekaa sebuleni
wakiangalia vipindi vya usiku kwenye runinga. Alipofika, bila kusema kitu
alikaa kochi la karibu na wazazi wake. Mzee Kipepeo aliyaondoa macho
kwenye runinga na kumgeukia mwanaye aliyeonesha hayupo katika hali yake ya
kawaida.
“Zulfa mama,” alimwita kwa sauti ya chini yenye kusikika.
“Abee,” aliitikia kwa sauti ya chini bila kuwaangalia wazazi wake.
“Eti mama kuna nini?”
Zulfa hakujibu kitu, alitazama chini tu kitu kilichomfanya baba yake kumgeukia
mkewe na kumuuliza:
“Mke wangu ni hilihili tu au kuna lingine?”
“Ni hilo tu mume wangu kama kuna lingine aseme mwenyewe.”
“Eti mama hutaki kwenda kusoma nje?”
“Sijakataa ila mpaka nimalize muda wangu uliobakia.”
“Mwanangu elimu ya maana ni nje ya nchi hivyo nafasi hii ni ya dhahabu
mwanangu.”
“Baba nielewe, mimi nipo tayari kwenda kusoma nje lakini nina imani miezi
minne iliyobakia si mingi kwa nini nisimalizie nijue nimevuna nini?”
“Hayo hayana umuhimu tena, kama umepata nafasi hii ambayo tumegombea
watu wengi, tulikuwa watu zaidi ya mia moja, nafasi zilikuwa tano tu, tena watu
maarufu lakini uwezo wangu na nguvu yangu kubwa serikalini tumepata moja
kati ya nafasi hizo chache.”
“Wazazi wangu sijakataa, nimekubali ila baada ya kufanya mtihani wangu wa
mwisho.”
“Sikiliza, kuondoka kwako si ombi bali amri, umebakiwa na miezi miwili, shule
hutarudi tena zaidi ya kujiandaa na safari yako.”
“Kama amri mi siendi.”
“Nini?” baba yake aliuliza kwa sauti ya ukali.
“Nasema siendi popote,” Zulfa alijibu kwa kiburi.
“Kama huendi na hapa uondoke,” baba yake alimtisha.
“Sawa nitaondoka,” Zulfa alizidi kumjeuria baba yake.
“Wewe Zulfa jeuri ya kumjibu hivyo baba yako umeitoa wapi?” mama aliingilia
kati.
“Sijaitoa popote, kwa nini hamtaki kunisikiliza na mimi? Hata kama ni mtoto
nina haki ya kusikilizwa.”
“Sasa nasema hivi shule utakwenda kwa nguvu au kwa hiyari,” baba alitoa
amri.
“Kama mtanilazimisha nitakunywa sumu.”
“Kunywa tu.”
“Sawa, nitakunywa mfurahi.”
“Unajua wewe mtoto unataka kunichezea,” mzee Kipepeo alisema huku
akinyanyuka na kumfuata Zulfa aliyekuwa bado amekaa kwenye kochi. Alipofika
alimshika mkono na kumnyanyua, akamuuliza kwa hasira:
“Wee kinyago unasemaje?”
“Kama nilivyosema siendi mpaka nifanye mtihani wa mwisho,” Zulfa alijibu
kwa kujiamini.
“Etiii,” mzee Kipepeo alimsukuma kidogo mwanaye na kumpelekea kofi zito
lililomrusha nyuma na kujigonga ukutani, akateremka chini ya zulia.
“Pumbavu, wewe ni nani unayeweza kubishana na mimi?” mzee Kipepeo
alisema kwa hasira.
Lilikuwa ni kofi zito lililompata barabara Zulfa, akajigonga ukutani na kuanguka
chini akiwa amepoteza fahamu.
“Mume wangu umefanya nini?” mama Zulfa alishtuka baada ya kushtushwa
na muanguko wa mwanaye.
“Mpumbavu huyu, hawezi kunikosea heshima. Nimepoteza kiasi gani cha
fedha kwa ajili yake?”
“Lakini mume wangu hukutakiwa kuchukua uamuzi mzito kama huu, ona
mtoto ulivyomfanya.”
Mama Zulfa alisema huku akimtazama mwanaye aliyekuwa amepoteza
fahamu huku damu zikimtoka mdomoni na puani.
“Umeua mume wangu,” mama Zulfa alisema huku akilia.
“Nini?” Mzee Kipepeo alishtuka.
“Umemuua mtoto.”
“Nooo, hapana!”
Mzee Kipepeo alimbeba Zulfa na kutoka naye nje hadi kwenye gari na safari
ya kuelekea hospitali ikaanza mara moja, mkewe akiwa ametoka na nguo ya
kulalia, khanga aliyojifunga ilimdondoka bila mwenyewe kujua, hakukumbuka
hata kuvaa viatu.
****
Wakati nyumbani kwa mzee Kipepeo yakiendelea hayo, mjini Sued naye
alikuwa ameuwasha moto. Usiku baba yake baada ya kurudi alielezwa na
mkewe matatizo ya mwanaye. Baada ya kumsikiliza mkewe alitumwa mtu
kwenda kumwita. Sued aliyekuwa amevimba macho kwa kulia, alifika mbele ya
baba yake.
“Vipi wewe?”
Sued hakujibu kitu, alitazama chini baba yake alimuuliza tena.
“Una tatizo gani?”
“Sina,” alijibu kwa sauti ya chini.
“Eti na wewe umekua siku hizi?”
Sued hakujibu kitu, aliinama tu. Kitendo kile kilimuudhi sana baba yake,
akamsogelea na kumtikisa huku akimuuliza:
“Unalia nini?”
Sued bado hakujibu kitu, alihofia kumwambia baba yake yaliyo moyoni
mwake.
“Baba Sued si nimekueleza vituko vya mwanao?”
“Eti una mpenzi?”
Swali lilikuwa zito kwa Sued na kujikuta kwa mara nyingine akikosa jibu,
kitendo kile kilimuudhi baba yake. Kwa hasira alisema kwa sauti ya juu:
“Unasikia wewe ngedere, upuuzi wako sitaki kuusikia tena, haya toka mbele
yangu.”
Sued alirudi chumbani kwake huku akishukuru kutopigwa na baba yake
ambaye alikuwa mkali kama pilipili. Moyoni alijiapiza kuwa atamtafuta popote
mpenzi wake kabla hajaondoka. Japo alikuwa hajawahi kufika Kayenzo lakini
aliapa kuhakikisha anafika hata kuingia katika jumba la mzee Kipepeo ili tu
amuone mpenzi wake Zulfa.
Zulfa baada ya kufikishwa hospitali, alipatiwa huduma ya haraka na kuonesha
alipata mshtuko kichwani baada ya kujigonga ukutani. Alipewa mapumziko ya
siku moja kabla ya siku ya pili kuruhusiwa kurudi nyumbani huku msimamo
wake ukiwa uleule wa kuendelea kusoma na kufanya mtihani ndipo aende Ulaya
kusoma.
Wazazi wake hawakujua mtoto wao hakuwa na hamu ya kusoma kama
alivyosema zaidi ya kukutana na mpenzi wake Sued. Moyoni aliamini kabisa
alichokuwa akikikosa katika maisha yake kilikuwa ni kumpata mtu sahihi
atakayeupokea moyo wake kwa mikono miwili.
Sued alikuwa mwanaume wa kwanza kumteka kiakili, kimoyo na kimwili,
hakuwaza kumkosa kwa ghafla kiasi kile. Aliamini kama atakubali kwenda Ulaya
kusoma tena bila kumuaga lazima atamuona si mkweli na kutafuta mpenzi
mwingine.
Siku zote aliamini mapenzi ya kweli si fedha bali upendo wa dhati toka moyoni
mwa mtu, hata kama angekwenda kusoma nje na kurudi na madigrii mangapi
kama hakuonesha upendo wa dhati kwa Sued hawezi kumkubali na matokeo
yake kuangukia kwa wanaume wasio na mapenzi ya kweli.
Pamoja na umri wake wa miaka 19, alikuwa na ufahamu mkubwa katika
mapenzi. Aliogopa kumpa mtu asiye sahihi moyo wake na mwisho kuambulia
mateso mazito. Katika maisha yake, alipanga kumpa mtu dhamana ya moyo
wake ambaye atakuwa sahihi.
Cha ajabu, kwa nguvu za aina yake alijikuta akimkabidhi moyo wake Sued,
mvulana ambaye kwa muda mfupi moyo wake ulimuamini kwa asilimia kubwa
na kumuona ndiye chaguo sahihi kwake.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 05
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
Pamoja na umri wake wa miaka 19, alikuwa na ufahamu mkubwa katika
mapenzi. Aliogopa kumpa mtu asiye sahihi moyo wake na mwisho kuambulia
mateso mazito. Katika maisha yake, alipanga kumpa mtu dhamana ya moyo
wake ambaye atakuwa sahihi.
SASA ENDELEA...

Cha ajabu, kwa nguvu za aina yake alijikuta akimkabidhi moyo wake Sued,
mvulana ambaye kwa muda mfupi moyo wake ulimuamini kwa asilimia kubwa
na kumuona ndiye chaguo sahihi kwake.
Kwa kipindi kifupi, alijikuta akitamani kuwa naye kiasi cha kutotamani tena
kuendelea na masomo zaidi baada ya mtihani wake wa kidato cha sita. Alijiona
tayari anafaa kujiamulia maisha yake, hasa katika mapenzi kwa vile alikuwa
tayari anajua zuri na baya pia kuwa na utashi wa kujiamulia kitu akipendacho.
Moyoni alipanga kupigana kwa nguvu zote kuhakikisha haendi nje kusoma
japo aliamini wazazi wake walikuwa na nguvu kubwa. Kwa muda uliokuwa
umebaki, alipanga kutoroka na kwenda mjini kumfuata Sued ambaye angejua
wafanye nini kwa kuamini angeondoka na kiasi kikubwa cha fedha ambacho
kingewawezesha kuishi sehemu yoyote chini.
Pamoja na kujua hasira za baba yake huku mama yake akijitahidi
kumbembeleza kubadili msimamo wake, lakini hakuwa tayari kumkubalia
mama yake ili wajue kweli amepania kumaliza mtihani wake wa kidato cha sita
uliokuwa umebakia miezi minne kufanyika.
***
Wazazi wake walizidi kumbembeleza aende shule kwa hiyari yake kuliko
kulazimishwa lakini bado Zulfa alishikilia msimamo wake. Baba yake alimueleza
atake asitake lazima atakwenda kusoma. Akaendelea kuwatishia wazazi wake
kuwa kama watamlazimisha basi atajiua. Tishio lile lilimtisha sana mama yake na
kutaka ushauri kwa mumewe kuliko kutumia nguvu nyingi.
“Sasa mume wangu tutafanya nini maana mtoto pamoja na vitisho vyote
bado msimamo wake upo palepale na sasa bado wiki mbili wakati kila kitu kipo
tayari kwa safari, itakuwaje?”
“Mke wangu ni utoto tu unamsumbua, akifika huko atatulia mwenyewe,
kwani wewe ulikuwa na wazo gani?”
“Wasiwasi wangu ni kumpoteza mtoto wetu, si unajua ndilo jicho letu.”
“Ni kweli lakini lazima wazazi tuoneshe msimamo ili mtoto asituendeshe.”
“Utakuwa umesababisha wewe.”
“Kwa nini mke wangu?”
“Ulimlea kama mtoto wa jicho kiasi cha kunikataza hata mimi mama yake
nisimfokee.”
“Lakini mke wangu kumtafutia shule nje kuna ubaya gani?”
“Hakuna ubaya lakini ndiyo hivyo na yeye alikuwa amepanga yake sasa
tutafanyaje?”
“Ile ni tisha toto tu, atatulia mwenyewe.”
Wakiwa katikati ya mazungumzo, Zulfa alitokea na mabegi yake, kitu
kilichowashangaza wazazi wake.
“Wee mtoto unakwenda wapi?” mama aliuliza.
“Shule,” aliwajibu kwa mkato.
“Kufanya nini?” baba mtu aliuliza.
“Kusoma.”
“Wee mtoto una wazimu, hebu rudisha mabegi yako ndani bado wiki mbili
uondoke.”
“Kwenda wapi?” Zulfa alijibu kwa kiburi, kitu kilichowashangaza wazazi wake
na kujiuliza jeuri ile kaitoa wapi.
“Mwanangu Zulfa una nini mama?” mama yake alimuuliza huku akimfuata
alipokuwa amesimama.
“Mama kwa nini hamtaki kunielewa?”
“Kukuelewa kivipi?”
“Nataka kurudi shule nikafanye mtihani japo nina imani nimepoteza vitu
vingi lakini kwa muda uliobakia lazima nitapata chochote, bado dhamira
yangu ya kupata ‘division one’ tena ya juu ipo palepale.”
“Tunajua lakini chonde mwanangu hebu badili msimamo wako kwani elimu
ya nje ni nzuri hata kukuwezesha kupata kazi nzuri popote katika dunia hii.”
“Ni kweli lakini kwanza nimalizie elimu niliyoisotea kwa miaka kumi na tatu,
nawashangaa nyie kwani bado miezi mitatu tu nimalize lakini hamtaki.”
“Sikiliza mwanangu, sisi wazazi wako hatuwezi kukupeleka sehemu
mbaya, tumepoteza fedha nyingi kuipata nafasi hiyo. Nakuomba mwanangu
kipenzi badili uamuzi wako ili uende kusoma,” mzee Kipepeo alimbembeleza
mwanaye.
“Si mnanilazimisha, basi mtapeleka mzoga wangu kwenda kusoma.”
Zulfa alisema huku akielekea chumbani kwake, kauli ile iliwafanya wazazi
wake kugeukiana na kutazamana, kila mmoja akitafuta jibu kwa mwenzake.
“Itakuwaje?” mama Zulfa alimuuliza mumewe.
“Yaani naushangaa ujasiri wa mwanao, sijui ameutoa wapi? Lakini utapoa
tu, bado utoto unamsumbua kwa vile hajui faida ya kile anachokifuata huko
nje.”
“Mume wangu unafanya utani mtoto yupo serious.”
“Sasa unataka tukubaliane na matakwa yake, mtoto siku zote ni kupata amri
ya wazazi wake.”
“Lakini kauli yake ya kupeleka mzoga wake umeichukuliaje?”
“Ni vitisho tu, kwenda nje ndiyo ajiue?”
Zulfa pamoja na vitisho vyote bado wazazi wake hasa baba yake msimamo
wake ulikuwa uleule wa yeye kwenda kusoma nje ya nchi. Aliamini akitumia
kiburi huenda akakosa kila kitu, akaamua kurudi matawi ya chini ili wazazi
wake waamini amekubali kwenda kusoma na yeye kupata nafasi ya kutoroka
kumfuata Sued mjini.
Alitoka chumbani na kuwafuata wazazi wake waliokuwa wamekaa sebuleni
wakiwa hawajui wafanye nini baada ya msimamo mkali wa mtoto wao,
kitu kilichowachanganya sana. Kama isingekuwa amelipa fedha nyingi basi
wangekubaliana na matakwa yake.
Wazazi wake walipomuona akisogea mbele yao bila mabegi, walinyamaza
na kumtazama mtoto wao anataka kusema nini. Zulfa alipofika mbele ya
wazazi wake alipiga magoti, kitu kilichowashangaza na kujiuliza kwa nini
anafanya vile.
“Baba,” alianza kumwita baba yake.
“Naam mwanangu,” baba yake aliitikia kwa shauku ya kutaka kujua mtoto
wake anataka kusema nini.
“Mama,” alimwita pia mama yake.
“Abee mwanangu.”
“Wazazi wangu naomba mnisamehe sana kwa yote niliyoyafanya kwa
kuwakosea heshima kwa kukataa mlichonitafutia. Naomba radhi sana wazazi
wangu kwa kuwakosea kwa kiasi kikubwa.”
“Tumekusamehe mtoto wetu, pia nilifurahi sana kusikia kauli yako na
kugundua kosa lako hakika umekuwa mwenzetu,” Mzee Kipepeo alisema akiwa
amejaa tabasamu pana.
“Hata mimi mwanangu sijawahi kupata furaha ya ajabu kama leo yaani
nimefarijika sana kama siku niliyojifungua na kukuleta duniani, asante
sana mwanangu kwa kutambua thamani yetu kwako,” mama Zulfa alisema
akimkumbatia mwanaye huku machozi yakimtoka.
“Wazazi wangu najua kiasi gani nimewavunjia heshima, najua kiasi gani
uamuzi wangu ulivyowachanganya. Kuanzia sasa hivi wazazi wangu nimekubali
kwenda kusoma nje ya nchi.”
“Asante mwanangu kwa kukubaliana nami,” mzee Kipepeo alimkumbatia
mwanaye aliyeanza kumnyima raha.
“Basi wazazi wangu naomba nikapumzike.”
“Hakuna tatizo mama kapumzike.”
Zulfa alirudi chumbani kwake akiwa na furaha baada ya mpango wake kwenda
kama alivyotaka kwa kuwapumbaza akili wazazi wake ili wiki mbili zilizobaki
aweze kujipanga na kutoroka.
Baada ya kuondoka, wazazi wake walikuwa na furaha sana, mzee Kipepeo
akamwambia mkewe:
“Unaona eeh! Tungelegeza angetupanda kichwani.”
“Siamini yaani mwanangu leo kanifurahisha sana.”
“Wacha nifike mjini mara moja, Zulfa leo alinichanganya sana.”
Mzee Kipepeo alitoka nje kwa ajili ya kwenda mjini na kumwacha mkewe
akiwahimiza wafanyakazi waandae chakula cha mchana.
***
Sued baada ya uzalendo kumshinda aliamua kwenda Kayenzo kumtafuta Zulfa
kabla ya muda wake wa kusafiri. Alipanda malori hadi njia panda ya kuelekea
Kayenzo, haukupita muda mrefu ilipita ‘pick up’ inayoelekea Kayenzo aliomba
lifti na kukubaliwa.
Alifika katika Mji wa Kayenzo majira ya saa tano asubuhi, mji ule alikuwa
mgeni hivyo hakujua mzee Kipepeo anakaa sehemu gani. Alimuuliza kijana
mmoja aliyekuwa akiuza karanga.
“Samahani, eti mzee Kipepeo anakaa sehemu gani?”
“Fuata hii barabara kuelekea ziwani, ukifika tu utakuta jumba la kifahari ndipo
hapo kwa mzee Kipepeo.”
“Asante.”
“Tena mzee Kipepeo huyo anapita.”
Sued alimtazama yule mzee aliyekuwa kwenye gari la kifahari, kisha
alimshukuru yule kijana. Alifuata barabara ya kuelekea ziwani kwa mwendo wa
dakika kama saba na kujikuta akitokea kwenye jumba kubwa lililokuwa na uzio
mkubwa.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 06
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
Sued alimtazama yule mzee aliyekuwa kwenye gari la kifahari, kisha
alimshukuru yule kijana. Alifuata barabara ya kuelekea ziwani kwa mwendo wa
dakika kama saba na kujikuta akitokea kwenye jumba kubwa lililokuwa na uzio
mkubwa.
SASA ENDELEA....

Alisimama na kujiuliza atafanyaje ili kuwasiliana na mpenzi wake, alijitahidi
kuuzunguka ule uzio labda atamuona Zulfa au hata mfanyakazi wa pale ili
amuagize. Kwa mbali alimuona mfanyakazi akikatia majani alimwita kwa
kumfanyia:
“Psiiiii.”
Yule jamaa aliacha kukata majani na kusogea kwa Sued.
“Vipi?”
“Safi, pole na kazi.”
“Asante, nikusaidie nini?”
“Zulfa yupo?”
“Zulfa! Wewe nani unayemuuliza Zulfa?”
“Ni rafiki yake, naomba uniitie.”
“Mmh! Wewe ndiyo uwe rafiki na Zulfa?” yule mtunza nyumba alishtuka.
“Ndiyo, naomba uniitie.”
“Siwezi, unataka nifukuzwe kazi kwa ajili yako, unamjua Zulfa au unamsikia?”
“Huwezi kufuzwa.”
“Ndugu yangu, wavulana wengi wamekuwa wasumbufu sana kiasi cha
kumfanya mzee ampeleke shule za kukaa hukohuko.”
“Najua hunijui lakini Zulfa akisikia nilikuja na wewe umekataa kuonana naye
naamini utaikosa kazi na kama utanikutanisha naye nina imani utaongezewa
mshahara.”
“Wewe umetoka wapi?”
“Mjini, najua ana siku chache za kuwepo kabla ya kwenda kusoma nje ya
nchi.”
“Pamoja na hayo lakini siwezi kukuitia wacha anifukuze kazi kwa kutokuitia
muhuni kama wewe.”
“Naomba nikutume kitu kimoja wala usimwite atoke nje, nenda tu
kamwambie Sued toka mjini yupo nje.”
“Halafu?”
“Wewe utaona.”
“Bwana wewe king’ang’anizi, ngoja nikamwambie.”
Yule jamaa hakwenda ndani, alizunguka kwenye chumba cha Zulfa na
kumgongea dirishani, Zulfa aliyekuwa amejipumzisha baada ya kuwachachafya
wazazi wake, alijinyanyua na kusogea dirishani, akafungua na kukutana na
Mabula, mtunza nyumba.
“Mabula vipi?”
“Eti kuna jamaa mmoja anasema sijui nikutajie jina lake.”
“Ili iweje? Mabula nimeshakukataza mara ngapi kuniita kutokana na upuuzi
wa wanaume, au nimweleze baba akufukuze kazi?” Zulfa alikuwa mkali.
“Nimemueleza na kusema eti kama akiondoka bila kuonana na wewe, ukijua
basi mimi lazima unifukuze kazi.”
“Mabula usinichekeshe, nikufukuze kazi kwa ajili ya kutoonana na mtu?”
“Amesema na kama ukikutana naye basi lazima uniongeze mshahara.”
“Mabula nawe kwa utani, huyo mtu ni nani?”
“Anaitwa Su..su..sudiii.”
“Acha utani anaitwa nani?”
“Sudi.”
“Anatoka wapi?”
“Mjini.”
“Wewe! Sued au Sudi?”
“Inawezekana ni Sued.”
“Mungu wangu! Mabula unasema kweli au unatania?”
“Kweli yupo nje ya uzio.”
“Mwambie nakuja mpeleke maeneo ya ziwani nakuja huko sasa hivi,” Zulfa
alijikuta katika furaha ambayo hakuitegemea muda ule.
“Dada mbona umefurahi ndiye shemeji nini?”
“Mabula bwana mpeleke kwanza nakuja kama ni yeye nitakupa zawadi
kubwa sana.”
Mabula alirudi mpaka kwa Sued na kumpeleka maeneo ya ziwani kumsubiri
Zulfa huku akimshangaa.
“Aisee rafiki wewe kiboko yaani Zulfa hajawahi kuwa na rafiki wa kiume, sote
huwa tunamwita Bikira Maria.”
“Hata mimi ni rafiki wa kawaida tu.”
Zulfa ndani alipagawa na kuwa kama kuku anayetaka kutaga kwa furaha,
hakutaka kutokea mlangoni kuepuka kuulizwa, akatokea dirishani ili kwenda
kumuona laazizi wake, Sued.
Alikuta Mabula tayari amemfikisha ufukweni Sued na kukaa mchangani
wakiangalia ziwani, mitumbwi ya wavuvi ikipita kwa mbali kidogo huku
mandhari yake ikivutia machoni. Zulfa alitokea nyuma yao bila wao kumuona
na kwenda kumziba macho Sued kwa viganja vyake.
“Mmh!” Sued aliguna.
Zulfa aliondoa mikono machoni na kumkumbatia Seud kwa nyuma na kufanya
wote walale chini.
“Siamini...siamini,” Zulfa alisema akiwa amemshikilia Sued mabegani huku
amemtazama usoni.
“Kwa nini?”
“Yaani wee acha tu, ungekuja kusikia Zulfa ameshafariki.”
“Kwa sababu gani tena mpenzi wangu?”
“Ni historia ndefu, samahani Mabula naomba usogee pembeni utupishe
tuzungumze,” Zulfa alimueleza mtunza shamba wao.
“Dada mi si nikaendelee na kazi?”
“Hapana Mabula, kakae pale unisubiri, ukirudi nyumbani baba akikuuliza
utasemaje?”
“Baba amekwenda mjini.”
“Whaooo! Basi kaa hapohapo mpaka tumalize mazungumzo yetu.”
“Hakuna tatizo dada.”
Mabula alisogea pembeni huku akishangaa kumuona Zulfa akionesha
mapenzi mazito kwa mwanaume, kitu ambacho hakuwahi kukiona katika siku
zote alizokaa pale akiwa mfanyakazi wa kazi za nje. Siku zote aliamini kabisa
Zulfa hayajui mapenzi kutokana na kuwazodoa wavulana wote waliomfuata
kupitia kwake na mwisho kutishiwa kufukuzwa kazi. Lakini siku ile aligundua
kumbe Zulfa naye anapenda kama watu wengine na mapenzi yalivuka mipaka
na kuwa kichaa cha mapenzi.
Wakati Mabula akiwaza hayo, Zulfa bado hakuamini kama angeweza kuonana
na Sued siku kama ile, mtu ambaye alikuwa ameanza kumkatia tamaa na kutaka
kutoroka kumfuata mjini.
“Unajua siamini!” Zulfa bado alionesha kumshangaa Sued.
“Kwa nini Baby?”
“Nimeamini Sued unanipenda, sikuamini kama ungefunga safari kuja mpaka
huku kunifuata.”
“Wee acha tu huwezi kuamini uzalendo ulinishinda nikaja shule kuuliza.”
“Wewee! Pale shule hawaruhusu mtu yeyote kuingia tofauti na mzazi au
mlezi, tena anayefahamika kwa maandishi.”
“Basi mimi nilifika kukuulizia.”
“Naona uliishia getini, walikujibu nini?”
“Nilitengeneza uongo wa ajabu.”
“Wewee! Ikawaje?”
“Nilikutana na mkuu wa shule.”
“Muongo! Yupoje?”
“Mzee mmoja amefuga sharubu.”
“Mmh! Labda ulimuona nje.”
“Alinikuta getini nikiulizia kwa mlinzi, alinishangaa kuwepo pale, ndipo
niliposogea kwenye gari lake na kukuulizia.”
“Jamani Sued, ulimuulizia vipi ikiwa familia yangu yote anaijua?”
Sued alimueleza alivyomuulizia na majibu aliyojibiwa shule.
“Baada ya kuelezwa unasafiri bado wiki mbili, nilichanganyikiwa siku ile kwa
kweli nilishindwa kula.”
“Mmh! Pole sana mpenzi wangu, hata mimi nilichanganyikiwa kufikia hatua
ya kukorofishana na wazazi wangu.”
“Kwa sababu gani?”
Zulfa alimuelezea yote yaliyotokea wiki mbili kabla ya kurudi shule na yote
yaliyoendelea mpaka asubuhi ya siku ile.
“Kwa hiyo ulikuwa unasemaje?” Sued baada ya kumsikiliza Zulfa alimuuliza.
“Wazo langu lilikuwa kutoroka na kukufuata mjini tuishi pamoja.”
“Mmh! Tutaishi vipi ikiwa wazazi wangu hawawezi kukubali nikae na
mwanamke?”
“Sasa tutafanyaje, lazima nitoroke katika siku hizi mbili.”
“Mmh! Huu mtihani.”

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 07
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....
ILIPOISHIA:
Zulfa alimuelezea yote yaliyotokea wiki mbili kabla ya kurudi shule na yote
yaliyoendelea mpaka asubuhi ya siku ile.
“Kwa hiyo ulikuwa unasemaje?” Sued baada ya kumsikiliza Zulfa alimuuliza.
“Wazo langu lilikuwa kutoroka na kukufuata mjini tuishi pamoja.”
“Mmh! Tutaishi vipi ikiwa wazazi wangu hawawezi kukubali nikae na
mwanamke?”
“Sasa tutafanyaje, lazima nitoroke katika siku hizi mbili.”
“Mmh! Huu mtihani.”
SASA ENDELEA...

“Sued acha kuniangusha nakutegemea wewe, mimi nitachukua ndani kiasi
kikubwa cha fedha na kwenda kuishi popote bila matatizo.”
“Tukitafutwa?”
“Kuna sehemu zingine hata magazeti hayafiki, tukienda huko tutakaa muda
mrefu na dawa uwahi kunipa mimba tutakuwa tumefuta safari ya kwenda nje
kusoma kwa vile nitakuwa najiandaa kujifungua.”
“Zulfa naweza kufia gerezani.”
“Nakuapia kama tutafanikiwa kutoroka na kubeba ujauzito nikijifungua
salama narudi nyumbani.”
“Wazo siyo baya, nami nimepata wazo, tukatafute nguo za kuvaa pia ndevu
za bandia ili watu wasikufahamu kama mwanamke ili tuweze kuishi kwa muda
mrefu.”
“Wazo lako zuri, lakini mbona umbile langu la kike nitawezaje kuishi kama
mwanaume?”
“Sikiliza Zuu, kifuani kwako matiti ni madogo hivyo hata ukivaa kanzu hakuna
wa kukujua kama wewe ni mwanamke.”
“Mmh! Sawa, basi katafute vitu vyote hivyo kisha uje tuondoke au mimi
nikufuate mjini?”
“Hapana, tutaondokea hapahapa, wakati unazungumza hayo nilipata wazo.”
“Wazo gani?”
“Upande wa pili wa ziwa hili kuna nini?”
“Kuna vijijini, nasikia wavuvi wa samaki ndiyo wanaoishi huko.”
“Basi huko ndipo pazuri.”
“Bebiii sijazoea maisha ya kijijini, kwa nini tusiende mkoa wowote na kupanga
kwenye hoteli yoyote na kuishi ndani bila kutoka?”
“Tukienda mjini kama tutatafutwa ni rahisi kupatikana, lakini baba yako
mawazo yake yote yataelekea mjini kwa kukutangaza katika vyombo vya habari.
Hapo lazima tutakamatwa kwa muda mfupi pengine kabla hata huo muda wa
kwenda shule haujaisha.”
“Lakini kweli, lazima nikiondoka baba atahamishia mawazo yake mjini na
kutufanya tuishi bila wasiwasi.”
“Sasa tutafanyaje, mi sina fedha.”
“Usiwe na wasi, nikiingia ndani nitamtuma Mabula akuletee.”
“Tunatakiwa tuondoke lini?”
“Kesho, tusipoteze muda, ondoka sasa hivi ukafanye manunuzi ya vitu hivyo.
Kesho njoo majira ya mchana na kwenda kufanya mipango na watu wenye
mitumbwi ya injini mkubaliane kiasi gani cha kutuvusha ng’ambo ya pili. Usiku
nitatoa vitu vyangu vya muhimu vya kutumia huko tuendako na kuvificha
sehemu ili nikitoka mtu asijue chochote.”
“Hakuna tatizo.”
“Basi ngoja nikachukue fedha ili uwahi mjini,” Zulfa alinyanyuka alipokuwa
amekaa na kumgeukia Mabula aliyekuwa mbali kidogo.
“Mabula njoo,” Mabula alisogea kusikiliza alichoitiwa:
“Naam.”
“Kuna mzigo nitakupa umletee huyu.”
“Hakuna tatizo.”
“Mpenzi kama hivyo basi, bai,” Zulfa alimbusu Sued mbele ya Mabula kisha
alimshika mkono Mabula na kurudi naye ndani. Kabla hajafika mbali aligeuka na
kumueleza:
“Kasimame pembeni ya uzio ili akupe akiwa ndani.”
Sued alifuata maelekezo na kwenda kusimama pembeni ya uzio, baada ya
muda Mabula alitoka na bahasha na kumpatia Sued aliyeipokea na kuondoka
zake kurudi mjini. Alipata lifti mpaka mjini na kwenda moja kwa moja chumbani
kwake baada ya kufika kwao.
Alipoingia chumbani alijifungia na kuzihesaba fedha alizopewa za maandalizi.
Zilikuwa milioni moja taslimu. Alishtuka kuziona fedha nyingi kiasi kile, alichukua
robo ya fedha zile na kwenda mjini kununua vitu muhimu kwa ajili ya safari yao.
Alinunua ndevu na nywele za bandia zake na za mpenzi wake, kanzu za kutosha,
makatambuga na vitu muhimu vya huko waendako.
Baada ya kupata vitu, alivificha kwa rafiki yake ili kesho aondokee huko bila
kutiliwa mashaka na wazazi wake. Upande wa pili, Zulfa alikuwa na furaha isiyo
kifani baada ya kufanikiwa kumuona mpenzi wake na kupanga mpango wa
kutoroka kabla ya muda wa kupelekwa shule haujafika. Aliomba Mungu siku ya
pili ifike haraka ili aweze kutoroka na mpenzi wake.
Alikusanya vitu vyao vya muhimu ambavyo angevitumia akiwa mafichoni na
kuchukua kiasi kikubwa cha fedha chumbani kwa wazazi wake ambao walikuwa
wamekwenda mjini.
Baada ya kufungasha mzigo wa kutosha, usiku aliuficha sehemu ya nje ili
aweze kuondoka nao bila mtu kujua.
Baada ya kufanikisha kila kitu, alikuwa mtu wa furaha muda wote, kitu
kilichowatia faraja wazazi wake na kuamini kweli Zulfa amekubali kwenda
kusoma nje ya nchi.
***
Siku ya pili, baada ya muda kukatika bila kuwepo na dalili za kuonekana Sued, Zulfa alikuwa mwingi wa wasiwasi, muda wote alitoka nje kuangaliakama Sued amefika lakini mpaka saa nane mchana inafika hakukuwa na dalili zozote za kufika. Alijiuliza atakuwa amepatwa na nini ikiwa alimuahidi mpaka saa sita mchana angekuwa amefika. Akatoka mpaka nje na kumfuata Mabula kumuulizia.
“Mabula umemuona Sued?”
“Sued! Ndiye nani?” Mabula alishtuka.
“Si yule kaka wa jana.”
“Nani, shemeji?”
“Ndiyo.”
“Mmh! Sijamuona.”
“Utani huo, niambie ukweli Mabula hujamuona kweli?”
“Zulfa siwezi kukudanganya, kwani vipi?”
“Alisema atakuja nashangaa mpaka sasa hivi sijamuona.”
“Kama alisema atakuja unatakiwa kumsubiri,” Mabula alimpa moyo Zulfa
aliyeonekana kupagawa.
“Muda unakwenda, unafikiri tutaondoka saa ngapi?” Zulfa alijisahau na
kutaka kumwaga mtama mbele ya kuku.
“Kwani mnataka kwenda wapi?”
“Mmh! Aah! Tupo tu,” Zulfa alijigundua kuwa ameropoka mbele ya Mabula
siri yake na Sued ambayo hakutaka mtu yeyote aijue zaidi yao wawili.
“Lakini nadhani atakuwa njiani, vuta subira.”
“Nitavuta subira mpaka saa ngapi wakati muda unakwenda? Huoni kama siku
ya leo inaweza kukatika hivihivi, unafikiri akija usiku tutaondokaje?”
“Kwenda wapi?”
“Ooh! Unajua leo nachanganya mambo, Mabula hebu nenda ziwani
ukamuangalie kama utamuona.”
“Sawa dada.”
“Mi nitakuwa ndani.”
“Hakuna tatizo.”
Mabula alielekea ziwani na Zulfa alirudi ndani, nyumba ikiwa chungu na
kuona kama mpango utakwenda ndivyo sivyo. Alijitahidi kuficha hofu yake
kwa kutengeneza tabasamu mbele ya wazazi wake lakini akiingia chumbani
moyo ulimuuma kama katafuna vitu vichungu. Ingekuwa usiku angelia sana
lakini mchana aliogopa wazazi wake kuiona hali ile na kuihoji.
Zulfa alianza kukata tamaa ya kutoroka siku ile na kuamini huenda kuanzia
siku ya kesho yake angekuwa katika ulinzi mkali kwa vile angekuwa katika
maandalizi ya mwisho kabla ya kuondoka siku tatu zijazo.
Alipanga kama Sued hataonekana siku ile, atasubiri mpaka siku ya pili lakini nayo ikipita basi atajiua usiku wa kuamkia siku ya safari.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 08
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
Zulfa alianza kukata tamaa ya kutoroka siku ile na kuamini huenda kuanzia
siku ya kesho yake angekuwa katika ulinzi mkali kwa vile angekuwa katika
maandalizi ya mwisho kabla ya kuondoka siku tatu zijazo.
Alipanga kama Sued hataonekana siku ile, atasubiri mpaka siku ya pili lakini
nayo ikipita basi atajiua usiku wa kuamkia siku ya safari.
SASA ENDELEA...
***
Wakati yeye akiteseka, kumbe Sued alikuwa amefika mapema na kwenda
ziwani kufanya mpango wa usafiri. Alimtafuta mvuvi mmoja na kumuulizia
safari kwenda kisiwa cha ng’ambo ya ziwa.
“Sijawahi kumpeleka mtu upande wa pili, mara nyingi hufika kule kufuata
samaki kama huku wakipungua,” nahodha wa mtumbwi alimwambia Sued.
“Ina maana kule kuna samaki sana?”
“Hujawahi kufika?”
“Nilifika muda mrefu sana.”
“Kule hakukauki samaki, mpaka kufika kule inachukua saa tatu.”
“Hakuna tatizo, sasa nitakulipa kiasi gani?”
“Utakachoona kinafaa.”
“Kwani ukifuata samaki huwa unalipwa kiasi gani?”
“Elfu arobaini.”
“Basi mimi nitakulipa mara mbili.”
“Hakuna tatizo sasa unakwenda huko saa ngapi? Tuwahi mapema ili na
mimi niwahi kurudi kabla ya kiza hakijaingia.”
“Naomba uweke mtumbwi wako tayari, tukifika tunaondoka.”
Baada ya kukubaliana, alirudi nyumbani kwao na Zulfa ili kumueleza
kinachoendelea. Njiani alikutana na Mabula aliyekuwa akielekea ziwani,
alipomuona alishtuka.
“Ha! Rafiki?”
“Vipi Mabula?”
“Si safi sana.”
“Si safi kuna nini?’
“Zulfa anakutafuta, yaani hana raha.”
“Basi nenda kamwambie nimefika.”
“Yaani atafurahi huyoo,” Mabula alisema huku uso wake ukitawaliwa na
tabasamu pana na kugeuka kupeleka taarifa.
***
Sauti ya kugongwa dirisha ilimshtua Zulfa na kumfanya akurupuke hadi
dirishani na kufungua dirisha haraka, akashangaa kumuona Mabula amerudi
mapema.
“Mabula vipi?”
“Furahi sasa.”
“Nifurahi nini Mabula?”
“Shemu amekuja.”
“Wewee!”
“Kweli nimekuta naye anatoka ziwani na begi lake mgongoni.”
“Asante Mabula, ni habari njema sana kwangu, yupo wapi?”
“Yupo nje ya uzio.”
“Mwambie nakuja.”
Mabula alirudi kwa Sued kumueleza kuwa Zulfa anakuja.
“Vipi, yupo wapi?”
“Anakuja.”
“Naweza kuingia ndani?”
“Ingia tu.”
Sued alivuka uzio na kuingia kwenye bustani ya mle ndani, baada ya muda
Zulfa alifika akiwa na tabasamu pana.
“Waoo my darling.”
“Waoo my sweet.”
Walikumbatiana na Sued kuchukua nafasi ile kumnong’oneza Zulfa.
“Mpenzi hatuna muda wa kupoteza, kila kitu kipo tayari.”
“Mabula naomba utupishe kidogo, naomba kwa muda huu uwe upande wa
nyuma ya nyumba mpaka nitakapokuita.”
“Hakuna tatizo,” Mabula aliondoka na kuwaacha.
Baada ya kuondoka, Sued alimueleza hatua aliyofikia kwa wakati ule.
“Sasa nitaondokaje, si kila mtu atanijua ni mimi?”
“Kuna vitu nimekuja navyo, vua hizo nguo vaa hizi.”
Kwa haraka, Zulfa alivaa kanzu ya kiume ya hagali (vazi la mwanaume la
kichwani la kitambaa cheupe kinachoshikizwa na mshipi na kigwe).
Alimbandika ndevu nyingi na kumvisha miwani, miguuni alimvisha
makatambuga. Kwa muda mfupi, Zulfa alibadilika na kuwa kama mwanaume.
Baada ya zoezi lile kukamilika, walichukua mizigo yao na kuelekea ziwani
ambako walikuta mtumbwi upo tayari.
Walipanda na safari ya kuelekea kijiji cha ng’ambo ilianza bila mtu yeyote
kujua Zulfa mtoto wa tajiri Kipepeo ndiye aliyekuwemo kwenye mtumbwi, hata
dereva wa mtumbwi ule hakumjua.
***
Baada ya mwendo wa saa moja, safari ya kwenye maji ilianza kumpa shida
sana Zulfa, kila alipoyatazama maji alijikuta akiona kizunguzungu na kutaka
kutapika, muda wote akawa amejiziba mdomo kwa kutumia mkono wake ili
asitapike.
“Vipi?” Sued alimuuliza kwa kunong’ona.
“Nasikia kizunguzungu na kichefuchefu,” Zulfa alisema kwa shida.
“Vimilia tutafika,” Sued alimpa moyo mpenzi wake.
“Vipi?” nahodha wa mtumbwi aliuliza.
“Anasikia kizunguzungu na kichefuchefu.”
“Usiangalie maji.”
Safari iliendelea huku Zulfa akifumba macho lakini kizunguzungu kiliendelea.
“Sued nasikia kizunguzungu.”
Zulfa alisema kwa sauti yake ya kike iliyomshtua yule nahodha wa boti na
kumshangaa mwanaume mwenye ndevu ana sauti ya kike.
“Mkumbatie ili kumtoa woga.”
Sued alimkumbatia Zulfa ambaye kidogo woga wa safari ulipungua, safari
ilichukua saa tatu. Walifanikiwa kufika Kijiji cha Some majira ya saa kumi na
mbili na nusu. Walipofika, walimlipa fedha yake na yeye kugeuza akiwaacha mtu
na mpenzi wake akijua ni wanaume wawili kwenye Pwani ya Some.
Baada ya kuteremka kwenye boti, alisogea pembeni kupanga waelekee wapi
kwani eneo walilokwenda likuwa geni kwao.
“Sued tutaelekea wapi?” Zulfa aliuliza.
“Tutaelekea kwenye makazi ya watu na kutafuta chumba cha kupanga ili
tujipange, nina imani baada ya muda mfupi tutajenga utaratibu wa kuishi.”
“Sued bado nasikia kichefuchefu,” Zulfa hakumalizia, alianza kutapika
mfululizo.
Zulfa alitapika sana mpaka nguvu zikamuishia, Sued akamsogeza ziwani na
kummwagia maji kisha alimwacha apumzike kwa kulala kwenye mchanga. Muda
nao ulikuwa unakatika, giza nalo lilianza kuimeza nuru ya mchana.
Hali ile ilimtisha Sued na kujiuliza usiku ukiingia itakuwaje kuhusu kupata pa
kulala. Alimuamsha Zulfa aliyekuwa amelala kwenye mchanga usingizi mzito ili
waondoke.
“Zulfa... Zulfa,” alimwamsha kwa kumtikisa.
“Abee.”
“Amka giza limeingia, hatujui mji huu uko vipi.”
“Sued sina nguvu kabisa, niache nipumzike kidogo.”
“Giza linaingia na hatujui mji huu usalama wake upo vipi.”
“Sijui kama nitaweza kutembea,” Zulfa alisema huku akijinyanyua alipokuwa
amelala na kukaa kitako.
Sued alimshika mkono na kumnyanyua ili kujaribu kutembea lakini bado
miguu ilikuwa haina nguvu.
“Sued niache nipumzike.”
“Zulfa tutakaa huku ziwani mpaka saa ngapi? Kibaya si wenyeji, hatujui
mazingira ya mji huu huenda kuna wanyama wakali.”
“Sasa nitatembeaje miguu yote haina nguvu, nilivyotapika unafikiri ni kitu
kidogo, mbavu zote zinaniuma nilijua nakufa.”
“Pole mpenzi ni mchafuko wa ziwa wala si ugonjwa.”
“Sasa nitafanyaje maana hata kutembea siwezi, ingekuwa hiyari yangu
ningelala hapa mpaka asubuhi.”
“Sawa lakini bado hatujui mazingira ya huku na usalama wake pia baridi ya
usiku hasa sehemu za ufukwe ni kali.”
“Basi niache nilale kidogo nina imani nitapata nguvu.”
“Sina jinsi lakini ingekuwa uwezo wangu ningetafuta njia yoyote tuondoke
huku.”
“Basi nibebe.”
“Itabidi iwe hivyo kwani sasa hivi giza limetanda, tuwahi kabla halijawa
kubwa.”
Ilibidi Sued ambebe Zulfa mgongoni huku amemshikia mabegi. Kwa vile
sehemu waliyokuwa wanakwenda ilikuwa ipo kilimani, alitembea kwa shida
kutokana na mtu aliyembeba kuwa mzito kutokana na kujiachia pia uzito wa
mabegi.
Japo alikuwa ameelemewa lakini alijitahidi kuhakikisha anaondoka eneo la
ziwani, mpaka anakaribia eneo wa watu alikuwa amechoka sana na kuamua
kumtua chini mpenzi wake.
“Zulfa nimechoka sana mpenzi wangu.”
“Pumzika mpenzi hata mimi nakuonea huruma.”
Kwa vile waliamini sehemu waliyokuwa ilikuwa salama, walipumzika
kwa muda. Sued alikumbuka kwenye begi kuna juisi na biskuti pamoja na
maji, akatoa na kula. Baada ya kula, Zulfa alijikuta akipata nguvu kidogo
na kukubaliana kuingia kijijini usiku ule uliokuwa kimya, ikionesha wenyeji
wameshalala.
“Sasa tunakwenda wapi?” Zulfa alimuuliza Sued.
“Tugonge nyumba yoyote ili tupate hifadhi kwa ajili ya leo tu, kesho tutajua
tufanye nini?”

Itaendelea Jumatatu
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 09
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....
...ILIPOISHIA:
Sued na mpenzi wake waliingia ndani, mzee alijua wote ni wanaume ila
mmoja ana sauti ndogo ya kike. Walielekezwa kulala katika chumba ambacho
kilionekana kina vumbi nyingi kwenye gunia. Walitandika blanketi na kulala.
“Wanangu vumilieni vumbi kutokana na chumba hicho kutotumika kwa
kipindi kirefu. Japo hewa ilikuwa nzito iliyomsumbua sana Zulfa walivumilia,
kutokana na uchovu walilala mpaka siku ya pili.
SASA ENDELEA...
***
Jioni ya siku ile, mzee Kipepeo na mkewe baada ya chakula cha usiku
walishangaa kutomuona Zulfa kwa muda mrefu, kitu kilichomshtua mzee
Kipepeo.
“Mama Zulfa, mwanao sijamuona muda mrefu, yupo wapi?”
“Mmh! Hata mimi, lazima atakuwa chumbani kwake akicheza gemu.”
“Si unajua kesho ndiyo maandalizi ya mwisho?”
“Najua, vitu vya kumnunulia naona vimekamilika kwa asilimia mia.”
“Na kuhusu sherehe ya kumuaga.”
“Maandalizi yamekwenda vizuri, ukumbi upo tayari, waliochukua tenda ya
vyakula nao wamesema kila kitu kimekwenda vizuri.”
“Nimefurahi kusikia hivyo.”
“Unajua sikuamini Zulfa alipokubali kwenda shule bila shinikizo, kwa kweli
kama mzazi nilifarijika sana.”
“Angekwenda tu, si unajua alikuwa anatikisa kibiriti.”
“Na yote kwa ajili yako, unajua Zulfa anakusikiliza sana wewe kuliko mimi?”
“Hakuna, kila mtu anamsikiliza.”
“Lakini wewe zaidi.”
Wakiwa katikati ya mazungumzo msichana wa kazi alipita, mama Zulfa
akamuita na kumtuma:
“Pili hebu kamwite Zulfa chumbani kwake.”
“Sawa mama.”
Pili alikwenda hadi chumbani kwa Zulfa na kugonga mlango kwa muda lakini
ndani palikuwa kimya. Alirudia tena kugonga huku akimwita kwa jina.
“Da’ Zuu unaitwa na mama,” alisema mfanyakazi huyo lakini hakukuwa na
jibu.
Aliufungua mlango na kuchungulia ndani akidhani labda amelala, chumbani
hakukuwa na mtu. Baada ya kumkosa, alirudi sebuleni walipokuwa wamekaa
wazazi wa Zulfa na kuwaeleza kuwa hakumuona.
“Umemtazama msalani au bafuni?”
“Hapana.”
“Rudi ukamtafute.”
Alirudi hadi chumbani kwa Zulfa na kumtafuta msalani na bafuni, huko pia
hakumuona, akarudisha majibu.
“Sijamuona.”
“Sasa atakuwa wapi?” mzee Kipepeo aliuliza.
“Kwa kweli sijui.”
“Mama Zulfa mtoto atakuwa wapi? Au alikuaga anatoka kachelewa kurudi?”
“Walaa, mume wangu toka tutoke si tumerudi pamoja?”
“Sasa atakuwa wapi?”
“Hata mimi nashangaa.”
“Hebu kamuangalieni nje huenda amekwenda dukani.”
“Ameanza lini kwenda dukani? Kwani kina Pili wana kazi gani?”
“Pengine amefuata kitu ambacho hataki mtu mwingine akijue.”
“Sasa ndiyo atoke usiku?”
“Hebu Pili kamfuateni dukani.”
Pili na wenzake walimfuata Zulfa dukani, walizunguka maduka yote bila
kumuona na kurudisha majibu kuwa hawajamuona. Majibu yale yaliwashtua
sana wazazi wa Zulfa.
“Mume wangu kuna kitu, haiwezekani Zulfa mpaka muda huu hajaonekana.”
Ilibidi wafanye msako mkubwa kila kona ya nyumba na eneo lililowazunguka.
Baada ya kumkosa, taarifa zilipelekwa polisi na kuanza msako mkali
kumtafuta Zulfa. Mpaka kunakucha alikuwa hajaonekana. Wazazi wa Zulfa
walichanganyikiwa sana na kujikuta wakifikiria labda amejiua.
“Mume wangu inawezekana kabisa Zulfa amejiua kutimiza lengo lake kama
tutamlazimisha kwenda shule.”
“Wazo gani hilo mke wangu, mbona alibadilika na mwenyewe kukiri
amekubali kwenda kusoma nje?”
“Sasa atakuwa wapi?”
“Tuiachie serikali ifanye upepelezi wake.”
“Mume wangu, moyo wangu mzito sana, wasiwasi wangu Zulfa ameyakatisha
maisha yake.”
“Acha kuwaza ujinga, ajiue kwa ajili ya kwenda kusoma?”
“Mume wangu yaani moyo wangu mzito kuna kitu kizito kimemtokea
mwanangu.”
Kila muda waliulizia taarifa kwa watu waliokuwa wakimtafuta Zulfa. Jibu
lilikuwa lilelile kuwa haonekani. Kutoonekana kwa Zulfa kuliacha simanzi nzito
kwa wazazi wake. Kila mfanyakazi wa ndani aliyeulizwa alisema alimuona
mchana tu.
Wazazi wa Zulfa walikesha kufuatilia taarifa za Zulfa yupo wapi, mpaka siku ya
pili inaingia hakukuwa na taarifa yoyote kuhusu kuonekana kwa Zulfa akiwa hai
au amekufa.
Siku ya pili walipeleka taarifa katika vyombo vya habari za kumtafuta Zulfa,
kila chombo cha habari kilimtangaza Zulfa, kuanzia kwenye magazeti na runinga
picha zake zilionekana. Redio zilimtangaza kwa wajihi wake ili mtu akimuona
atoe taarifa polisi.

KATIKA KIJIJI CHA SOME
Siku ya pili, Sued alikuwa wa kwanza kuamka lakini Zulfa alikuwa bado ana
uchovu hivyo aliendelea kulala. Sued siku ya pili baada ya kuamshwa na mzee
Katumba aliamka akiwa ametapakaa vumbi mwili mzima.
“Vipi kijana umeamkaje?”
“Namshukuru Mungu nimeamka salama, shikamoo.”
“Marahaba, vipi mwenzako hajaamka?”
“Bado.”
“Angeamka niwapeleke kwa mjumbe.”
“Mzee wangu kwa vile upo peke yako kwa nini tusikae hapa tuwe kama
wanao na kukusaidia kazi?”
“Sawa, lakini siwezi kukaa na ninyi bila kujua mnatoka katika familia ya nani ili
mkipata matatizo niweze kujua nitaanzia wapi?”
“Mzee wangu, kama tulivyokueleza tumeuza kila kitu chetu na kuondoka
kuja kutafuta maisha baada ya wazazi wetu kufariki. Unaonaje tulichonacho
tukitumie na wewe kama mzazi wetu.”
“Mmh! Sawa,” mzee Katumba alishusha pumzi nzito.
“Baba nina imani hata mazingira ya hapa tutayabadilisha kutoka nyumba ya
nyasi na kuwa ya udongo na bati.”
“Sawa kijana wangu nimekuelewa.”
Walikubaliana na mzee Katumba waishi pale kama sehemu ya familia
yake, Zulfa aliamka baada ya kulala vya kutosha. Mzee Katumba baada ya
kuwaelekeza baadhi ya vitu vya muhimu kutumia pale alielekea ziwani kuchuuza
samaki. Siku ile Sued na Zulfa waliitumia kwa ajili ya kufanya usafi wa chumba
watakachokuwa wanakaa.
Sued alikusanya matofali na kutengeneza kitanda kwa kujaza mchanga kisha
kutandika blanketi juu. Walitengeneza chai na viazi vya kuchemsha, wakafungua
kinywa. Baada ya kupata kifungua kinywa, wapenzi hao wawili walijilaza kwenye
mkeka na kupunga upepo.
“Sued unafikiri nitaishi katika hali hii mpaka lini?” Zulfa alimuuliza Sued.
“Kwa muda mfupi, mpaka tukimzoea tutamueleza ukweli.”
“Unajua kuishi katika maisha ya kuigiza naweza kujisahau na kumfanya
afahamu mapema kuwa mimi ni msichana, unafikiri atasema nini?”
“Tutajua, we mwenyewe umeona maisha yake ni ya kubahatisha, tukiyabadili
na kumpunguzia ugumu wa maisha lazima atatuelewa na tutaishi kwa uhuru
mkubwa.”
“Nitafurahi kuishi kwa uhuru huo.”
“Lakini kwa sasa nataka tuishi hivihivi, mwache aendelee kujua sisi wote ni
wanaume.”
“Nitajitahidi japo najiona kama nipo kifungoni, nitakuwa naomba usiku uingie
haraka ili niwe huru.”
“Lakini unaonaje maisha yetu mapya?” Sued alimuuliza Zulfa.
“Mmh! Najisikia raha moyoni mwangu, Sued nakuahidi mchana wa jua kuwa
nitakupenda kuliko kitu chochote kilicho chini ya jua. Wewe ndiye mwenye
chakula cha moyo wangu, wewe ndiye pumzi zangu, maudhi yako ni kuyachezea
maisha yangu.
“Sued nimekubali kukosana na wazazi wangu kwa ajili yako, najua hasira
zao kwangu ni kubwa kwa kupoteza fedha zao nyingi kwa ajili ya kunipeleka
nje kusoma. Nakuomba uwahi kunipa mimba kabla hatujakamatwa kwa vile
naamini hatutaweza kuishi katika maisha haya milele, lazima kuna siku nitatoka
kwenye jumba la kobe nami niishi kama wanawake wengine.”
“Ni kweli mpenzi wangu, nami nakuahidi kuwa mtumishi wako, wewe ndiye
mfalme wa maisha yangu, nimekuwa kipofu niliyefumbua macho na kukuona
wewe peke yako mbele yangu na baada ya hapo macho yangu yalifunga.
Nilipokufungia moyoni mwangu, ufunguo niliumeza, sikuweza kuutupa baharini
kwa kuhofia unaweza kumezwa na samaki chewa kisha kuletwa tena duniani
na kuweza kuufungua moyo wangu lakini amini hakuna kitu kitakachokutoa
moyoni mwangu.
“Penzi lako limenipa ujasiri wa kuweza kupambana na simba mkali na kuweza
kumuua kwa mkono wangu. Umekuwa kielelezo sahihi cha nini maana ya
mapenzi na kupenda na nini maana ya penzi la dhati. Nimekuwa mwanafunzi
wako mzuri niliyejifunza mengi juu yako kuhusu upendo, nami naapa mbele ya
Muumba mbingu na nchi kuwa nitakupenda mpaka pumzi zangu za mwisho,”
Sued alijiapiza kwa Zulfa.
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 10
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
“Penzi lako limenipa ujasiri wa kuweza kupambana na simba mkali na kuweza
kumuua kwa mkono wangu. Umekuwa kielelezo sahihi cha nini maana ya
mapenzi na kupenda na nini maana ya penzi la dhati. Nimekuwa mwanafunzi
wako mzuri niliyejifunza mengi juu yako kuhusu upendo, nami naapa mbele ya
Muumba mbingu na nchi kuwa nitakupenda mpaka pumzi zangu za mwisho,”
Sued alijiapiza kwa Zulfa.
SASA ENDELEA...

“Asante mpenzi wangu, naamini yote niliyofanya yamekuwa sahihi,
umenifanya nisijutie nilichokifanya cha kupingana na wazazi wangu.”
“Zulfa wakili wa maumivu ya moyo wako ni wewe mwenyewe na wala si mzazi wako.”
“Nami nimeutetea moyo wangu kwako bila wewe kuonekana, nilipanga siku ya kesho ndiyo iwe siku yangu ya mwisho ya kuvuta pumzi.”
Siku ile walishinda nyumbani mpaka aliporudi mzee Katumba akiwa na samaki wake aliobakiza kwa ajili ya kitoweo. Siku zote alipokuwa peke yake alikuwa akirudi na samaki wake mmoja aliyemtumia kwa siku tatu na unga wake kilo moja aliokula siku nne. Walipomuona, walikwenda kumpokea mzigo aliokuwa nao wa samaki na unga.
“Pole na kazi mzee wetu,” Sued alimpa pole.
“Aah! Wee acha tu kila kukicha hali ni hiihii, hakuna muda wa kupumzika, siku
ukipumzika ujue unalala na njaa au utaua mtaji.”
“Nina imani huu ni wakati wako wa kupumzika, Mungu ametuleta ili tukulee.”
“Nitashukuru maana kuna siku huwa nafanya biashara huku naumwa.”
“Kuanzia kesho nitakwenda na wewe kuangalia biashara ili niifanye mimi.”
“Hakuna tatizo.”
Sued na Zulfa walitengeneza mboga ya jioni na kuandaa chakula cha usiku. Baada ya chakula cha usiku, walikuwa na kikao cha kifamilia.
“Ndiyo vijana wangu, hebu kwanza nifahamisheni majina yenu maana sijui la
mtu yeyote.”
“Mi naitwa Salum na mdogo wangu anaitwa Fadhil.”
“Vizuri, mi naitwa mzee Katumba, nina muda wa miaka kumi kijijini hapa.”
“He! Mzee ulitokea wapi?”
“Ukeke.”
“He! Toka Ukeke mpaka huku ulifikaje?” Sued alishtuka.
“Miaka kumi iliyopita tulikuwa tukivusha magendo, wakati tukifuatiliwa
na polisi kwa bahati mbaya kalua letu liligonga mwamba na kupasuka, katika
kujiokoa baadhi ya watu tuliokuwemo tuliogelea na kujikuta tumetokea kwenye pembe ya Pwani ya Some. Huwezi kuamini hatukuweza kuondoka hapa baada ya kukosa usafiri kwa zaidi ya miaka miwili.
Mwanzo usafiri ulifika mara moja kwa miezi sita, na usafiri wenyewe ulikuwa kwa ajili ya wavuvi waliokuwa wakifuata samaki. Siku zilivyozidi kukatika watu wakahamia na kuwa kijiji kamili, miaka ilivyokuwa ikienda mbele ndivyo kisiwa hiki kilivyozidi kuwa maarufu kwa uvuvi wa samaki.
“Huwezi kuamini kwa miaka yote hatukujua kumbe baada ya msitu mkubwa huko mbele kuna miji ya watu waliokuwa wanaishi kama kawaida, pia kuna barabara ya kukurudisha mjini japo unazunguka sana mpaka kufika mjini.
“Mji wetu ulizidi kuongezeka umaarufu, ukaanza kujengeka kwa kasi kwa
wavuvi wengi kuhamia huku na kujenga.
“Sasa hivi sehemu hii imekuwa maarufu kwa uvuvi, watu kutoka mjini huja
kununua samaki ambao hupatikana kwa bei rahisi. Basi mpaka leo tunaendelea na maisha tukiwa sisi ndiyo wenyeji.”
“Mzee katika muda wote huo hukuwahi kuwa na mwanamke?”
“Mmh!” mzee Katumba swali lile lilimfanya ashushe pumzi ndefu kisha akasema:
“Najua mtanishangaa kwa hali niliyoionesha baada ya kuniuliza swali hilo ambalo kwa upande wangu limekuwa kama kulichubua kovu la moyoni mwangu,” baada ya kusema vile, mzee Katumba alifuta machozi yaliyowafanya Sued na Zulfa kushtuka.
“Vijana wangu msinishangae kwa hali niliyokuwa nayo, naweza kuwaeleza ili nanyi mfunguke akili kwa vile mnakuwa na ipo siku yanaweza kuwakuta kama yangu hivyo muwe makini na kiumbe anayeitwa mwanamke.”
“Kwa nini baba?” aliuliza Sued.
“Miaka saba na nusu iliyopita, kwa vile nilikuwa mzoefu wa ziwa nilijiingiza katika uvuvi ambao ulinipatia kipato kikubwa kwa haraka kutokana na uzoefu wangu wa ziwa.
“Kwa muda mfupi niliweza kutengeneza fedha nyingi na kuweza kumiliki mitumbwi zaidi ya minne. Kutokana na kuwa na fedha nyingi nilihamia mjini na kununua jumba la kifahari sehemu za Goma na nyumba nyingine Igo na Mabati. Pia nilinunua na magari matatu.
“Kutokana na ulimbukeni nilijikuta nikiingia kwenye starehe, nilikuwa nikibadili wanawake, jina langu lilikuwa maarufu sana pale mjini Goma.
“Ulimbukeni ule ulisababisha nikawa natoa kuliko kuingiza baada ya kupata msichana mzuri ambaye alinimaliza akili. Nilimpa kila alichotaka hata ambacho hakikuwa ndani ya uwezo wangu. Biashara zangu zikaanza
kuyumba, nikaanza kuuza baadhi ya magari yangu na fedha zote ziliteketea kwenye starehe ya yule binti mrembo .
“Kwa vile nilikuwa katika fungu la kukosa nilimaliza magari yote,
nikauza nyumba zangu mbili na kusahau jumba nililokuwa nakaa nilikuwa nimelimilikisha kwa yule mwanamke, tena kwa maandishi.
“Baada ya kuuza nyumba zile, niliuza na boti zangu zote, hali yangu ya maisha ikaanza kuyumba ndipo nilipotaka kuuza lile jumba ambalo ndilo lililoniingiza katika matatizo makubwa baada ya kutaka kuliuza kwa nguvu.
“Yule mwanamke alipotaka kunizuia kuiuza nyumba yangu nilimpiga kipigo kizito kilichosababisha apate kilema cha maisha. Baada ya kukamatwa nilihukumiwa kifungo cha miaka sita gerezani, baada ya kutoka nilikuta mji umebadilika. Nilijikuta mgeni wa kila kitu, sikuwa na mbele wala nyuma.
“Kwa aibu ya kukaa mjini niliamua kurudi kijijini kwangu Some kumalizia muda wa kuendelea kuishi duniani. Baada ya kufika huku kwa vile nilikuwa nafahamika, nilipata kieneo hiki na kujenga nyumba yangu hii. Tokea hapo sikuwa na jipya, sikujua nianzie wapi. Baada ya kusoma hali ya hapa nilianza kazi ya kupara samaki, baada ya kupata mtaji kidogo nikaingia kwenye
kuchuuza samaki.
“Japo roho ilikuwa ikiniuma lakini sikutakiwa kumlaumu mtu kwa vile mimi mwenyewe maisha niliyachezea nayo yakanitupa. Basi vijana wangu napenda kuwaasa kwa vile mmeamua kutafuta maisha nina hakika kwa juhudi zenu hamtachelewa kupata mafanikio, hivyo basi nawaombeni mheshimu matumizi ya fedha. Kinachotoka kiwe kidogo kuliko kinachoingia, ni makosa kutumia zaidi ya kinachoingia.
“Pia jiepusheni na kuendekeza wanawake, ni viumbe wanaokula kama mamba, wanameza bila kutafuna. Naweza nisiwalaumu lakini kwa upande mwingine lazima niwalaumu kwa vile chanzo cha matatizo ni wao. Kama ningepata mwanamke mwenye uchungu na maisha angeniongoza sasa hivi nisingekuwa na taabu kama hizi.”
“Kwa hiyo mzee una muda gani toka utoke kifungoni?”
“Mwaka sasa.”
“Na hiyo nyumba yako ulipotoka hukuifuatilia?”
“Wala hata kuitazama kwani niliamini kosa nililifanya mwenyewe, yule mwanamke alikuwa na haki japo alinihadaa na kuuza nyumba zangu lakini niliyompa aliisimamia huoni kama yule hakuwa mtu mzuri.”
“Pole sana mzee.”
“Asante.”
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda sana waliingia kulala kuitafuta siku ya pili, kila usiku ulipoingia ilikuwa faraja kwa Zulfa ambaye alirejea kwenye uhalisia wake wa kike kwa kuwa na mpenzi wake. Siku zote Sued alimueleza mpenzi wake wawe makini ili asishike ujauzito mapema ili waweze kujipanga.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 11
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda sana waliingia kulala kuitafuta siku ya pili, kila usiku ulipoingia ilikuwa faraja kwa Zulfa ambaye alirejea kwenye
uhalisia wake wa kike kwa kuwa na mpenzi wake. Siku zote Sued alimueleza mpenzi wake wawe makini ili asishike ujauzito mapema ili waweze kujipanga.
SASA ENDELEA...
MJINI KAYEZO
Hali ilizidi kuwa tete katika nyumba ya mzee Kipepeo juu ya kutoweka
ghafla kwa Zulfa, walijaribu kwenda kuuliza shuleni. Jibu lilikuwa
hajaonekana. Mkuu wa shule aliwabana marafiki wa karibu wa Zulfa akidhani
wana taarifa yoyote ya Zulfa. Lakini hakukuwa na jibu la kujua yupo wapi zaidi
ya wao kujua angekuwa yupo safarini nje ya nchi.
Kwa mama Zulfa hali ilikuwa mbaya baada ya presha kupanda na kushuka
kila alipomfikiria mwanaye aliyetoweka ghafla. Vyombo vya usalama vilifanya
msako kila kona. Akili zao walielekeza mjini wakiamini maisha aliyokuwa
akiishi Zulfa asingeweza kwenda kijijini.
Mwanzo walikuwa na wasiwasi wa kuumwa lakini kila kona hakukuwa na
taarifa zozote za kifo au kuokotwa mwili wa msichana.
“Mume wangu mtoto atakuwa amekwenda wapi?” mama Zulfa alimuuliza
mumewe, mkono ukiwa shavuni kwa huzuni.
“Nitajuaje mke wangu, hata mimi nimechanganyikiwa.”
“ Nani kamteka mwanangu?”
“Kwa kweli sijui lolote sasa. Sijui ndiyo katoroka?”
“Kama katoroka atakuwa amekwenda wapi?”
“Nitajuaje, inawezekana ametimiza dhamira yake.”
“Lakini si alisema atajiua?”
“Mke wangu tusiombe hayo.”
“Sasa mbona haonekani?”
“Mimi nitafanyaje mke wangu? Kumbuka nimepoteza fedha nyingi kwa ajili
yake.”
“Mume wangu fedha na mtoto kipi bora?”
“Mtoto, lakini kumbuka nimepoteza fedha nyingi kwa ajili yake.”
“Kwani polisi wanasemaje?”
“Bado wanaendelea kufanya uchunguzi.”
“Mpaka lini?”
“Siwezi kuwapangia.”
“Kuna faida gani kuwa na polisi kama mwanangu anapotea wanashindwa
kumpata?”
“Mke wangu hawajui ametorokea au yupo wapi, lazima wafanye upelelezi,
nina imani kama yupo hai atapatikana.”
Mtunza shamba Mabula alikuwa kwenye wakati mgumu huku akijiuliza
Zulfa atakuwa amekwenda wapi. Kuna kipindi alitamani kuwaeleza jinsi
alivyokutana na Sued lakini aliamini angefia gerezani kwa kuonekana aliujua
mpango ule mapema lakini hakusema, naye aliamua kufa kiofisa na tai
shingoni.
Wiki ilikatika bila taarifa zozote za kuonekana wala kupatikana tetesi za
mahali alipo Zulfa. Hali ile iliikumba hata nyumba ya mzee Juma, baba yake
Sued. Nayo ilikuwa katika wakati mgumu kutokana na kutoweka ghafla kwa
mtoto wao.
“Baba Sued mtoto atakuwa wapi?” mama Sued alimuuliza mumewe.
“Swali gani hilo mke wangu? Mi nitajuaje? Wote tumekuwa tukimtafuta
bila mafanikio kwa wiki sasa.”
“Mume wangu, wiki inakatika sasa na hatujafanya mchakato wowote wa
kumtafuta. Kila nikikueleza tutoe taarifa polisi unasema atarudi, sasa yupo
wapi?”
“Mke wangu, Sued ameondoka mara ngapi kwenda kucheza mpira na
kurudi bila kuaga, lakini hili la sasa limenitisha.”
“Mmh! Nimekumbuka si unakumbuka siku ile alipokuwa akilia kwa ajili ya
mwanamke?”
“Nakumbuka, sasa huyo mwanamke ndiye anamfanya akimbie nyumbani,
huo uwezo wa kumtunza ameutoa wapi?”
“Mume wangu unajua sasa hivi kuna taarifa gani zinazotikisa mji?”
“Za kupotea kwa binti wa mzee Kipepeo.”
“Unajua binti huyo ndiye mpenzi wa mwanao?”
“Usiniambie!” kauli ile ilimshtua baba Sued.
“Ukweli ndiyo huo, msichana aliyemrusha akili mwanao ni mtoto wa mzee
Kipepeo.”
“Kipepeo huyuhuyu tajiri wa Kayenzo?”
“Huyohuyo.”
“Utani huo! Hawalingani hadhi hata kidogo kama mbingu na ardhi kwanza
kamuona wapi?”
“Hayo sijui ila kwa maelezo ya mwanao walikubaliana waoane baada ya
yule binti kumaliza darasa la kumi na nne.”
“Sasa hicho kichekesho, Sued hana kazi wala chumba, kula kulala yake
anategemea wazazi, hiyo fedha ya kuolea na kumtunza angeitoa wapi?”
“Ungetoa wewe baba yake,” mama yake alitania.
”Mwanao kila siku namwambia ajishughulishe, mipira na yeye, yeye na
mipira leo hii anataka kuoa huyo mwanamke angemlisha hewa?”
“Mume wangu twende mbele turudi nyuma, kutoweka kwa Sued na Zulfa
binti wa Kipepeo ni kitendawili ambacho huenda tunaofahamu ni mimi na
wewe.”
“Kitendawili gani?”
“ Nina wasiwasi mwanao kamtorosha mtoto wa watu.”
“Sasa akikamatwa si atafungwa? Halafu bado siamini kama Sued anaweza
kumtorosha huyu binti wa tajiri kama Kipepeo. Ni kitu kisichowezekana hata
kidogo, atampeleka wapi?”
“Sasa unataka kuniambia Sued amekwenda wapi?”
“Hilo ndilo linatakiwa kufanyiwa kazi, tena mke wangu usiropoke kuhusu
mwanao kuwa na uhusiano na mtoto wa Kipepeo, tutajiingiza kwenye
matatizo ya kujitakia bure.”
“Sasa tufanyeje?”
“Tukaripoti polisi ili tuweke tahadhari.”
“Tufanye hivyo lakini amini usiamini kupotea kwa Sued kunaambatana na
Zulfa, lazima kutakuwa na kitu,” bado mama Sued aliamini alipo Zulfa ndipo
alipo Sued.
Wakati wanajiandaa kwenda kutoa taarifa polisi, katika taarifa ya habari
iliyokuwa ikiendelea redioni, tajiri mzee Kipepeo alikuwa ametangaza
zawadi ya milioni tano kwa mtu atakayepeleka taarifa ya kuonekana kwa
Zulfa akiwa hai au amekufa.
“Umesikia mke wangu, sasa jipendekeze sijui Zulfa alikuwa mpenzi wa
mwanangu utaozea gerezani,” baba Sued alimuonya mkewe.
“Mume wangu siwezi kumueleza mtu yeyote taarifa hizi.”
Walifika polisi na kutoa taarifa za kutoweka kwa mtoto wao, baada ya
kuwasilikiza mkuu wa kituo aliwauliza:
“Ana muda gani hajaonekana nyumbani?”
“Mmh! Wiki sasa?”
“Ana tabia ya kuondoka nyumbani bila taarifa?”
“Hapana.”
“Mbona mmechelewa kutoa taarifa?”
“Tuliamini yupo huenda tunapishana naye mimi nikienda kazini yeye
anakuwepo.”
“Wewe baba mnapishana sawa, hata wewe mama?”
“Mi’ nilikuwa sipo nimerudi jana na kuuliza nikaelezwa hajaonekana ana
wiki nzima.”
“Mmekwenda hospitalini kuulizia?”
“Hatujaenda.”
“Sasa nendeni hospitali zote kuulizia mgonjwa wenu, kama mtamkosa
nendeni polisi kuulizia huenda yupo mahabusu kwa makosa na mwisho
kabisa mkimkosa nendeni mochwari, nina imani katika sehemu hizo
nilizowaelekeza lazima moja mtamkuta.”
“Sawa tumekuelewa.”
Baada ya kutoa taarifa waliondoka huku mama Sued akiamini kabisa alipo
Zulfa ndipo alipo Sued.
“Mume wangu niamini alipo Zulfa mtoto wa Kipepeo ndipo alipo
mwanangu Sued.”
“Kwa hiyo tusiende sehemu hizo?”
“Twende tu kama ushahidi lakini mwisho utakubaliana na mimi.”
Walianza safari ya kuzungukia hospitali zote na vituo vya polisi bila
mafanikio, mwisho walimalizia mochwari, vilevile hakukuwa na sura wala
kivuli cha Sued.
***
Zawadi kubwa ya kwa mtu yeyote atakayewezesha kupatikana kwa
Zulfa akiwa hai au amekufa iliongezwa na kufikia milioni kumi, hali
iliyowapagawisha watu wengi. Kila mmoja aliwaza kuuaga umaskini kupitia
kumpata mtoto wa tajiri.
Kila mmoja alinunua gazeti na kukata kipande cha sura ya Zulfa na
kutembea nacho ili akikutana naye aweze kumtambua kwa urahisi. Biashara
ya magazeti ilipata soko kwa kila mmoja kuitafuta milioni kumi.
Polisi nao walihaha kumtafuta Zulfa kutokana na dau nono la milioni mia
moja kama watafanikiwa kumrejesha Zulfa akiwa hai au milioni hamsini
akiwa amekufa. Mkuu wa polisi, Khatim Naheka alisambaza picha za Zulfa
kila kona ya nchi na nchi jirani.
Picha zikabandikwa barabarani, kila mmoja alikuwa na kazi ya kumtafuta
kwa matumaini ya kupata donge nono. Kila kona ambayo mkuu huyo wa
polisi alipeleka picha, aliahidiwa msaada mkubwa wa kumtafuta kwa hali na
mali.
Mkuu wa Polisi akiwa na vijana wake, walihangaika wiki nzima, hawakulala
kwa ajili ya kumtafuta Zulfa kila kona bila mafanikio.
“Kwanza poleni,” mkuu wa polisi aliwapa pole vijana wake walioonekana
kuchoka.
“Asante mkuu,” waliitika kwa pamoja.
“Inaonekana shughuli imekuwa pevu tofauti na tulivyodhania.”
“Ni kweli hata mimi nilijua ya kitoto,” mmoja wa vijana wake alichangia.
“Mnafikiri anaweza kuwa ameuawa?” aliuliza swali akiwa amewakazia
macho.
“Sidhani,” mmoja hakukubaliana na wazo la bosi wake.
“Sasa atakuwa wapi?”
“Huenda ametekwa ili mtekaji apewe kiasi kikubwa cha fedha kutokana
na utajiri wa mzee Kipepeo,” mmoja alichangia.
“Lakini mzee Kipepeo alisema aligoma kwenda kusoma na kutishia kujiua,
hamuoni kama ametekeleza alichokisema?”
“Kuna maelezo alisema kuwa alibadili msimamo wake na kuwa tayari
kwenda kusoma sasa tushike lipi?”
“Sasa kipi kimemfanya atoweke muda mfupi kabla ya kwenda kusoma?”
“Labda ametoroshwa na mwanaume?” mwingine alitoa wazo.
“Si rahisi,” mwingine alipinga.
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?” mkuu aliuliza.
“Nataka tuingie vijijini huenda wamemuua na kumtupa.”
“Sasa kijijini atakuwa anafanya nini hasa tukizingatia mtoto wa tajiri
maisha yake yalikuwa ya kudekezwa na kusoma shule za gharama kama
mlivyosikia alikuwa anapelekwa nje ya nchi kusoma!”
“Nielewe aishi vipi ili iweje, nasema huenda ameuawa?” mkuu alikuwa
mkali kidogo.
“Samahani mkuu,” aliomba radhi.
“Sikilizeni, sheria za kipelelezi zinaelekeza ufike sehemu yoyote
wanayoishi watu ili tukikosa sehemu zote tujipange kwa mpango mwingine.
Hamtaki fedha aliyotuahidi?”
“Nani asiyetaka, tena mimi nikipata nanunua nyumba,” mmoja alichangia.
“Sasa jiandaeni kuzunguka vijiji vyote vya mkoa huu ili tujue tumekwama
wapi,” mkuu alitoa amri.
“Sawa bosi.”
Walikubaliana kuanza msako kijiji kwa kijiji mpaka wajue mwisho wa
kupotea kwa Zulfa, mtoto wa tajiri Kipepeo.

ITAENDELEA KESHO
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 12
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
“Nielewe aishi vipi ili iweje, nasema huenda ameuawa?” mkuu alikuwa mkali kidogo.
“Samahani mkuu,” aliomba radhi.
“Sikilizeni, sheria za kipelelezi zinaelekeza ufike sehemu yoyote
wanayoishi watu ili tukikosa sehemu zote tujipange kwa mpango mwingine.
Hamtaki fedha aliyotuahidi?”
“Nani asiyetaka, tena mimi nikipata nanunua nyumba,” mmoja alichangia.
“Sasa jiandaeni kuzunguka vijiji vyote vya mkoa huu ili tujue tumekwama
wapi,” mkuu alitoa amri.
“Sawa bosi.”
Walikubaliana kuanza msako kijiji kwa kijiji mpaka wajue mwisho wa
kupotea kwa Zulfa, mtoto wa tajiri Kipepeo.
SASA ENDELEA...

KIJIJINI SOME
Siku zilizidi kukatika huku mzee Katumba akiamini kabisa ana vijana wawili wa kiume, Salum na Fadhil. Muda wote Zulfa alivaa kanzu na kizibao, juu alivaa higal na ndevu zake za kubandika ambazo zilimfanya mtu aamini
ni mwanaume mwenye uso wa kike.
Sued naye alianza kazi ya kuchuuza samaki na kuuza, kwa muda mfupi alijulikana kutokana na uuzaji wake samaki kwa bei ndogo, kitu kilichofanya kila mtu kijijini ampende. Baada ya kuzoeleka pwani, alinunua boti mbili ambazo zilifanya kazi ya uvuvi. Kwa muda mfupi walinyanyua banda la mzee Katumba na kujenga nyumba ya matofali na mabati.
Katumba alijikuta akianza kurudisha afya yake kutokana na kula vizuri na kulala pazuri, hata kazi zake hazikuwa za nguvu, zaidi ya kusimamia shughuli za uvuvi. Zulfa aliyefahamika kwa jina la Fadhil, siku zote alishinda nyumbani na kazi
yake kubwa ilikuwa kupika. Siku moja mzee Katumba alikuwa akiumwa na kubakia nyumbani. Akiwa amekaa kwenye kiti cha uvivu alishikwa na hamu ya kuku, alimwita Zulfa aliyekuwa akiosha vyombo vya chai.
“Fadhil mwanangu.”
“Naam baba,” Zulfa aliitikia kwa sauti nzito kidogo.
“Mwanangu nina hamu ya kuku leo.”
“Hakuna tatizo baba.”
“Basi nenda bandani ukakamate kuku umchinje nitakusaidia kumbanika.”
“Sawa baba ngoja nimalizie kuosha vyombo.”
“Fadhil.”
“Naam baba.”
“Kwa nini huendi kujishughulisha na kazi ngumu?”
“Muda bado ukifika nitafanya tu baba ondoa shaka, si unaona
tumegawana, ninyi ziwani mimi nyumbani mkirudi mnakuta kila kitu tayari.”
“Wewe mtoto wa kiume ukijilegeza siku za usoni maisha yatakuwa
magumu sana.”
“Wasiwasi wako tu baba, wala usiwe na shaka na mimi,” Zulfa akiwa na wasiwasi alijitahidi kumjibu.
“Basi mchinje huyo kuku ili aliwe na chakula cha mchana.”
Ule ulikuwa mtihani mkubwa sana kwa Zulfa, katika maisha yake hakuwahi kuchinja kuku, pia alikuwa akimuogopa sana kiumbe huyo. Alijiuliza atafanyaje ili kuweza kumchinja kuku wakati amekubali mwenyewe? Aliomba kwa Mungu Sued awahi kurudi ili amchinje.
Zulfa alijizungusha labda Sued atatokea lakini muda ulizidi kukatika bila
kuonekana na ilikuwa vigumu kurudi muda ule, mara nyingi alikuwa akitoka
alfajiri anarudi saa nane mchana baada ya kumaliza biashara zake za samaki.
“Fadhil huyo kuku utamchinja saa ngapi?” mzee Katumba aliuliza baada ya
muda kukatika bila kuonesha dalili za kumchinja.
“Nitamchinja baba,” Zulfa alijibu huku akijitahidi kuvuta muda zaidi.
“We mbona umelegea sana tofauti na kaka yako?”
“Baba namchinja sasa hivi.”
“Kama hutaki si useme, mtoto wa kiume umelegea kama mtoto wa kike,” mzee Katumba alizungumza kwa sauti ya ukali.
Kauli ile ilimuumiza sana Zulfa na kuona anaonewa, heri ingejulikana moja yeye ni mwanamke ili aishi kwa amani kuliko masimango ya kila siku kuwa analegea wakati ni maumbile yake. Ili asiharibu mpango wao, alikwenda kwenye banda la kuku huku mapigo ya moyo yakimwenda mbio kwa kuhofia kuparuliwa na kuku.
Alifungua mlango wa banda na kumkamata kuku huku akijipa moyo, baada ya kumshika alichukua kisu na kuzunguka naye nyuma ya nyumba
ili amchinje bila mzee Katumba kumuona. Alimfanya kama wanaume wanavyofanya wakati wa kuchinja kuku. Kwa vile hakuwa mzoefu alimchinja katikati ya shingo kwa kutumia nguvu nyingi sana. Baada ya kumchinja alitenga maji na kumnyonyoa kisha aliandaa mboga ya mchana.
Sued alirudi na kukuta chakula kimeandaliwa, baada ya kutenga kwenye mkeka mzee Katumba alimsifia Zulfa kwa mapishi yake.
“Hakika mwanangu pote unaniudhi lakini kwenye mapishi unaniacha hoi,
hongera mwanangu unajua kupika.”
“Asante baba.”
“Baba Zulfa anajua kupika sana hata nyumbani tulikuwa tukimtegemea,”
Sued alitia chumvi na kujikuta akijisahau na kumwita Zulfa jina lake halisi.
“Wee Salumu yaani kupika mdogo wako unamwita Zulfa?” mzee Katumba alifikiri amemtania kwa vile anapenda kupika.
“Hapana baba ulimi hauna mfupa, Fadhil anajua kupika.”
“Nawe Fadhil gangamala ona kaka yako anakuita majina mabaya kwa sababu ya kulegea kwako,” mzee Katumba alimtahadharisha Zulfa.
“Atangangamala tu baba.”
Baada ya chakula, wakati Zulfa akitoa vyombo na kuingiza ndani, alipotaka kutoka alishtuka kuona mjumbe wa nyumba kumi akiwa ameongozana na askari wanne. Alijikuta akirudi ndani haraka huku mapigo ya moyo wakimwenda mbio.
Aliwasikia wakibisha hodi, alisogea kwenye upenyo na kuchungulia nje. Mzee Katumba na Sued waligeuka kuwatazama ambapo waliwaona askari pamoja na mjumbe wa nyumba kumi. Mzee Katumba alinyanyuka na kuwakaribisha.
“Karibuni.”
“Asante.”
“Mzee Katumba ugeni wako huu.”
“Karibuni sana.”
“Jamani huyu ndiye mtu wangu katika nyumba zangu kumi anaitwa
Katumba.”
“Tunashukuru kumfahamu.”
“Mzee mwenzangu hawa ni wageni toka mjini wamekuja kufanya msako
wa binti wa mzee Kipepeo, tajiri wa Kayenzo aliyetoweka ghafla mjini.”
Kauli ile iliwafanya Sued na Zulfa kila mtu moyo wake kupasuka paah! Wakaona wamekwisha. Sued alijizuia kuficha hofu yake lakini presha ya Zulfa ilikuwa kubwa na kumfanya ashindwe kusimama, akajikuta akijitupa kitandani.
Nje mjumbe aliendelea kutoa maelezo: “Mzee mwenzangu wamekuwa wakizunguka kila pembe ya nchi na nchi za jirani bila mafanikio. Wamekuja hapa kufanya upekuzi na kutaka kujua historia ya wageni walioingia mjini muda si mrefu. Japo najua kwako huna kijana wa kike lakini nimewaleta kuwaondoa hofu ili wakiondoka wajue kijiji hiki wanayemtafuta hayupo.”
“Karibuni, nina vijana wawili wa kiume, huyu mkubwa anaitwa Salum na mdogo wake Fadhil. Zaidi ya hawa sijapata mgeni mwingine.”
“Kwa hiyo una vijana wawili tu?”
“Ndiyo.”
“Huyu Fadhil yupo wapi?”
“Aliingia ndani, Sued hebu kamwite mdogo wako.”
Sued aliingia ndani huku akijiuliza Zulfa atakuwa kwenye hali gani kama amesikia akitafutwa. Alipoingia ndani alimkuta akihema kwa kasi. Alimtikisa na kumwita,
“Zulfa...Zulfa.”
“Ni..ni..ache kwanza.”
Sued alisimama kwa muda akijiuliza wakati huo sauti ilitoka nje na kuuliza:
“Salum mwaka mzima hata kutoka nje mdogo wako kalegea?”
“Baba Fadhil kichwa kinamuuma analia.”
“Mdogo wako pengine ugonjwa si mkubwa anapenda kudeka kama mtoto wa kike.”
“Achana naye,” kauli ya mkuu wa msafara ilisema huku akimgeukia mzee Katumba.
“Wala hujawahi kusikia bahari za msichana mgeni kijijini?”
“Mmh! Sijasikia, nina imani mjumbe angekuwa wa kwanza kusikia ambaye anafahamu taarifa za watu wa nyumba zote.”
“Mzee mwenzangu kijiji kikubwa na nyumba zangu ni kumi, kama ukisikia toa taarifa kuna zawadi kubwa imetolewa kama kuna mtu atamuona huyo msichana basi atapata milioni kumi taslimu.”
“Utani huo.”
“Kweli mzee wangu, kama atamuona tujulishe mara moja.”
“Hakuna tatizo wazee wangu ninaweza kuwa mmoja wa watu wanaokula bata uzeeni.”
“Basi acha tupite,” askari aliyeonekana ana cheo cha V tatu na mwenge ambaye ndiye aliyekuwa kiongozi wa msafara ule alisema:
“Karibuni tena.”
Waliondoka kuelekea sehemu nyingine na kumfanya Sued aliyekuwa amesimama mlangoni kurudi ndani huku mapigo ya moyo yakiwa bado juu. Sued alimfuata Zulfa na kumkuta bado amejilaza na kuhema kwa kasi mikono ikiwa kifuani.
“Zulfa...Zulfa,” alimwita kwa sauti ya chini.
“Niache kwanza naomba unipepee.”
Sued alichukua kipande cha boksi na kuanza kumpepea Zulfa aliyekuwa akivuja jasho kwa hofu. Baada ya kutulia, aliomba maji ya kunywa na kutulia kidogo kisha alisema pumzi zikiwa bado juu.

Itaendelea Jumatatu
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 13
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
“Zulfa...Zulfa,” alimwita kwa sauti ya chini.
“Niache kwanza naomba unipepee.”
Sued alichukua kipande cha boksi na kuanza kumpepea Zulfa aliyekuwa
akivuja jasho kwa hofu. Baada ya kutulia, aliomba maji ya kunywa na
kutulia kidogo kisha alisema pumzi zikiwa bado juu.
SASA ENDELEA...

“Pole mpenzi.”
“Asante.”
“Vipi?”
“Ha..ha..pana nilishtuka sana yaani hata sijui wangenigundua
ingekuwaje?”
“Mmh! Wee acha hata mimi nilichanganyikiwa, afadhali ulikuwa ndani
bila hivyo tungeumbuka. Na ubishi wako ungetuponza.”
“Ubishi ipi?”
“Kama ningekubaliana na wewe kumweleza ukweli mzee Katumba na
wewe kuishi kama mwanamke leo tulikuwa tumeumbuka.”
“Mmh! Wee acha tu.”
“Pole mpenzi tumeweza kulivuka hili nina imani tutaishi kwa usalama
zaidi.”
“Pamoja na hayo lakini nimekuwa katika kipindi kigumu sana nikiwa
nyumbani.”
“Kipindi gani tena mpenzi wangu?”
“Mi mwanamke nitawezaje kazi za kiume?”
“Kazi zipi?”
“Kila siku nalaumiwa na baba kuhusu kulegea kwangu, najitahidi lakini
bado nitabakia mwanamke.”
“Nitajitahidi kumueleza una matatizo, hutakiwi kufanya kazi ngumu.”
“Kingine leo niliambiwa nichinje kuku.”
“Ehe, ikawaje?”
“Nimejizungusha labda utatokea lakini wapi.”
“Kwa hiyo akamchinja mwenyewe?”
“Amchinje wapi, nimemchija mimi.”
“Muongo!”
“Kweli kuku huyu nimemchinja mimi.”
“Zulfa hebu acha uongo, wewe si uliniambia unamuogopa kuku hata
kumshika? Ulianzaje mpaka kumchinja?”
“Wee acha, aliponieleza nimchinje nilichanganyikiwa mtoto wa kike,
nimezuga labda utatokea wapi.”
“Ukafanyaje?”
“Ilibidi nimshike huku haja ndogo ikinitoka kwa mbali na kumchinja, leo
nimewalisha kibudu.”
“Haki ya nani?”
“Kama huamini kamuulize baba.”
“Ngoja nikamuulize,” Sued alisema huku akitoka ndani na kumuuliza mzee
Katumba.
“Eti baba kuku wa leo kamchinja nani?”
“Fadhil.”
“Muongo baba.”
“Kweli, lakini kwa mbinde.”
“Nashangaa anaogopa sana kuku.”
Baada ya kuhakikishiwa kuwa Zulfa kachinja kuku alirudi ndani.
“Umeamini?”
“Ndiyo.”
“Basi mpenzi siku zinavyozidi kwenda nitapewa majukumu makubwa na
kuzidi kusimangwa kuwa nimelegea kama mtoto wa kike, sasa jamani mi si
mwanamke jamani?”
“Basi mpenzi nitajitahidi kuwa karibu na wewe.”
***
Siku zilizidi kukatika, ikawa usiku ukifika, Sued na Zulfa wanageuka na kuwa wapenzi, siku zote mzee Katumba aliamini kabisa Zulfa ni mwanaume lakini aliyelegea na sauti yake kutokuwa kavu kama mwanaume mwingine.
Sued akiwa katika kazi zake za samaki, alipata kipande cha gazeti
kinachoonesha picha ya Zulfa akitafutwa na kutolewa zawadi kwa mtu atakayemuona ya shilingi milioni kumi na tano na gari huku zawadi ikizidi kuongezwa kila kukicha.
Alilichukua lile gazeti na kumpelekea mpenzi wake, baada ya kulisoma alisema:
“Mmh! Kazi ipo sijui siku akiniona atanifanya nini?”
“Mmh! Sijui.”
“Lakini naapa sirudi nyumbani, nitazeekea hukuhuku.”
Zulfa aliridhika na maisha yale japo alitamani kuishi maisha ya uhuru zaidi kama mwanamke kuliko kuishi maisha ya maigizo yaliyokuwa yakimpa shida. Kwake usiku ulikuwa ni sherehe kwani alikuwa akirudi kwenye asili yake ya kike na kulala na mpenzi wake kwa raha zao.
Mara kwa mara walikuwa wakifanya mapenzi bila mpangilio na kujikuta Zulfa akishika ujauzito. Dalili zilianza kwa Zulfa kushindwa kuziona siku zake kwa miezi mitatu mfululizo huku akianza kuchagua baadhi ya vyakula.
Siku moja wakiwa chumbani usiku, Zulfa alimueleza Sued mabadiliko yake.
“Sued siielewi hali yangu.”
“Kivipi?”
“Mwezi wa tatu sasa sijaziona siku zangu.”
“Wewee, acha utani!”
“Kweli mpenzi.”
“Unataka kuniambia una mimba?”
“Nina wasiwasi huo maana hata vyakula sasa hivi nachagua.”
“Mmh! Shughuli ipo.”
“Sasa tutafanyaje?”
“Hakuna cha kufanya tumueleze ukweli baba ili ajue wewe si mwanaume
bali mwanamke.”
“Mmh! Atatuelewa?”
“Atatuelewa si unajua tumeishi naye kama mzazi wetu hawezi kutugeuka.”
“Sued, yaani aache milioni kumi na tano na gari kwa ajili yetu?”
“Sidhani kama atatugeuka, kumbuka tumemtoa wapi na leo hii amesahau shida zake wakati alikuwa ameshajikatia tamaa ya maisha.”
“Hapana usimwambie.”
“Kwa hiyo?”
“Tukae kimya, tutajua baadaye.”
Walikubaliana kutomwambia kitu mzee Katumba.
Siku zilizidi kukatika huku ujauzito wa Zulfa ukizidi kukua, pia hata
maumbile nayo yalibadilika kwa kunawiri huku mwili ukiongezeka uzito.
Homa na maumivu ya kichwa ya mara kwa mara vilimsumbua, muda wingi alishinda amelala.
Hali ile ilimfanya Sued ajitahidi kuificha ili mzee Katumba asigundue kwa kufanya majukumu yote ya nyumbani na kumuachia mzee Katumba kuendelea na shughuli za mwaloni.
Hali ya Zulfa ilimshtua mzee Katumba na kuhoji:
“Vipi mbona kila siku Fadhil analala tu kama anaumwa si tumpeleke hospitali?”
“Anatumia dawa ila sasa anaendelea vizuri,” Sued alijibu.
“Mmemlea vibaya sana mdogo wako, ugonjwa kidogo tu analala hapa tupo wanaume watupu anatakiwa kugangamala.”
“Hapana baba kweli Fadhil anaumwa,” Sued alimtetea mpenzi wake.
“Basi akizidiwa utanijulisha.”
“Nina imani hali yake itakuwa nzuri muda si mrefu.”
“Ajabu mdogo wako pamoja na kuumwa lakini ananenepa.”
Sued hakumjibu kitu alicheka tu na kuagana na mzee Katumba aliyekuwa
akiwahi kwenye shughuli zao za samaki, akamuacha Sued aliyebaki kwa ajili ya kumhudumia Zulfa ambaye hakulala vizuri usiku wa kuamkia siku ile.
Baada ya kuondoka, Sued alirudi ndani alipokuwa amelala Zulfa.
“Vipi mpenzi?”
“Mmh! Mwili hauna nguvu kabisa pia kichefuchefu kinakuwa kikali, hali
inavyoendelea huko mbele nina wasiwasi wa kujulikana.”
“Vumilia tu mpenzi.”
“Nitavumilia mpaka lini, hivi siku tukishinda nyumbani wawili na baba
unafikiri itakuwaje?”
“Nitajitahidi kuwa pamoja na wewe, hata nikitoka nitawahi kurudi, pia hali hii itaisha tu kwa vile ujauzito kwanza husumbua lakini baada ya muda huwa kawaida.”
“Itakuwa kawaida vipi na tumbo linakuwa tena kwa kasi, unafikiri tumbo
hili tutamwambia nini baba?”
“Tutamwambia kitambi.”
“Mpenzi, kumbuka baba ni mtu mzima anayejua kuliko sisi kwa hiyo
hatuwezi kumfanya mtoto bila kujua nini kinaendelea.”
“Sasa tufanyeje?”
“Nakuomba tuondoke hapa.”
“Zulfa twende wapi?”
“Sijajua lakini mimi huyu mzee simuamini hata kidogo.”
“Usiseme hivyo Zulfa, kumbuka tuna muda mrefu tupo na huyu mzee, sasa hivi ni kama mzazi wetu wa damu, lazima tumwambie ili uweze kuishi kwa amani na katika hali yako ya kike.”
“Sued usiombe kumueleza taarifa zetu mzee Katumba unakumbuka siku ile walipokuja polisi kunitafuta?”
“Nakumbuka.”
“Alisemaje?”
“Mmh! Nakumbuka alisema ule ndiyo utajiri anaomba usiku na mchana ili awe mmoja wa watu watakaomuona Zulfa.”
“Sasa leo hii tumwambie kuwa mimi ndiye ninayetafutwa kutakuwa na usalama kweli?”
“Sasa tutafanya nini?”
“Tutoroke.”
“Twende wapi?”
“Sijajua lakini tufanye mpango tutoroke kwa siri.”
“Zulfa mpenzi hali yako hairuhusu twende sehemu isiyo salama.”
“Mmh! Sasa sijui tufanye nini tumbo ndilo linazidi kukua miezi sita kama mwaka mzima.”
“Mpenzi nakuhakikishia mzee Katumba hawezi kutugeuka.”
“Mmh! Nakuomba suala la kumwambia mpaka tukose ufumbuzi kabisa, lakini kwa sasa tukomae tutapata tu ufumbuzi.”
Walikubalia kuvuta muda wa kumueleza mzee Katumba kuhusu hali ya Zulfa.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 14
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500....

ILIPOISHIA:
“Zulfa mpenzi hali yako hairuhusu twende sehemu isiyo salama.”
“Mmh! Sasa sijui tufanye nini tumbo ndilo linazidi kukua miezi sita kama mwaka mzima.”
“Mpenzi nakuhakikishia mzee Katumba hawezi kutugeuka.”
“Mmh! Nakuomba suala la kumwambia mpaka tukose ufumbuzi kabisa, lakini kwa sasa tukomae tutapata tu ufumbuzi.”
Walikubalia kuvuta muda wa kumueleza mzee Katumba kuhusu hali ya Zulfa.
SASA ENDELEA...

Mzee Katumba alijikuta akiingiwa na wasiwasi na hali ya Fadhil ‘Zulfa’, kila alivyomuangalia alikuwa na kila dalili za mwanamke mjamzito lakini kilichomshangaza ni ndevu na jina lake. Hakutaka kufanya haraka aliendelea kufanya upalelezi wa kina na kugundua Fadhil si mwanaume kama alivyompokea bali mwanamke.
Alijawa na mawazo mengi juu ya hali ile na kujiuliza kwa nini
wamemdanganya kuwa Fadhil ni mwanaume kumbe ni wanamke. Hali ya mimba nayo aliingundua baada ya kuliona tumbo la Zulfa ambalo lilikuwa mimba isiyo na siri na wala si kitambi kama alivyoelezwa.
Alijikuta akiingiwa na wasiwasi juu ya siri ile na kuwaza huenda ndiyo yule msichana anayetafutwa na baba yake mjini mzee Kipepeo. Wazo la kwenda serikali ya kata kuwaeleza wasiwasi wake kwa yule kijana aliye naye na kuja kukamatwa na kuonekana siye atakuwa amejiharibia kila kitu na kusababisha wale vijana kumkimbia na kuondoka na mali zao.
Aliamua kukaa kimya ili auone mwisho wake kwa kuamini ule tayari ni moto uliofunikwa na shuka lazima moshi ungeonekana tu. Kila kukicha tumbo la Zulfa lilizidi kukuwa na hali yake ilizidi kuwa mbaya, kichwa kikawa kinamuuma, kichefuchefu nacho kilimsumbua sana kiasi cha kumfanya muda wote awe amelala tu, kazi zote alifanya Sued.
Mzee Katumba naye alitaka kujua hali ya Fadhil kuwa ya kitandani kila kukicha.
“Salum mdogo wako ana tatizo gani?”
“Mwili tu unakosa nguvu ila hajambo.”
“Naomba tumpeleke hospitali kwani hali kwa sasa inanitisha kila kukicha Fadhil amekuwa mtu wa kulala tu kazi zote za pwani zimenielemea mimi. Kama ugonjwa wake mkubwa tumpeleke mjini kwa matibabu mazuri. Nina imani fedha tunayo.”
“Nimekuelewa mzee wangu, jibu nitakupa kesho ngoja tuwasiliane na mwenzangu.”
“Sawa, lakini sitaki wiki hii ipite lazima Salum apelekwe kwenye tiba ya uhakika.”
“Sawa mzee wangu.”
Mzee Katumba aliondoka na kwenda mwaloni kwenye shughuli zao
za samaki. Baada ya kuondoka Sued alimfuata Zulfa ndani na kumueleza wasiwasi wa mzee Katumba juu ya hali yake.
“Zulfa hali ni mbaya.”
“Kwa nini tena mpenzi?” Zulfa alishtuka.
“Mzee kaja juu anataka kuhakikisha unatibiwa.”
“Mmh! Sasa itakuwaje?”
“Kwa nini tusimwambie ukweli?”
“Hapana usimwambie, tutoroke.”
“Twende wapi, ona hali yako ilivyo hata miguu imevimba.”
“Nina wasiwasi sana kumwambia ukweli anaweza kutugeuka mpenzi wangu.”
“Hawezi mpenzi... hawezi ameshakuwa sehemu yetu.”
“Sued milioni kumi na tano na gari kwa ajili ya ubinadamu?”
“Siamini kama anaweza kutugeuka, tumemfanyia mangapi leo atugeuke?”
“Mmh! Sawa basi mwambie lakini hata simuamini hata kidogo.” Zulfa bado hakumuamini kabisa mzee Katumba. Walikubaliana kumweleza ukweli mzee Katumba kuhusiana na hali ya
Zulfa kuwa si mwanaume bali mwanamke pia kuhusu hali yake ya ujauzito uliokuwa na miezi saba.
***
Usiku baada ya chakula, Sued alimwita mzee Katumba chumbani kwao ili wamueleze ukweli. Zulfa alikuwa amekaa kitandani kajifunga shuka na kujiegemeza ukutani. Sued alikaa kitandani na mzee Katumba alikaa kwenye kigoda.
“Naam wanangu mnasemaje, nina imani kuna jambo mnataka kuniambia?” mzee Katumba alivunja ukimya.
“Ndiyo mzee wetu.”
“Haya zungumzeni wanangu.”
“Samahani mzee wetu,” Sued alianza kusema.
“Bila samahani.”
“Nina imani wewe ndiye mzazi wetu kwa sasa.”
“Ni kweli kabisa.”
“Kwanza tunashukuru kwa kutupokea na kuishi kama sehemu ya familia
yako.”
“Nashukuru kwa kulitambua hilo.”
“Mzee najua kuna vitu vimekupa wakati mgumu kwa mwenzangu na
kukupa maswali magumu yasiyo na majibu.”
“Kuhusu nini?”
“Nina imani mwenzangu ukimuangalia ana dosari nyingi za kuwa
mwanaume ambazo hukuzingundua.”
“Ni kweli,” mzee Katumba alikubali ili kumpa kichwa Sued kuwa alikuwa na akili kuliko yeye.
“Mzee kuna kitu tulikuficha muda mrefu lakini leo hatuna budi kukueleza ukweli.”
“Kitu gani hicho?”
“Mwenzangu si mwanaume kama tulivyokutambulisha mwanzo.”
“Ni nani?”
“Mwanamke.”
“Kumbe, kwa nini mlinificha?”
“Kutokana kutokuamini mapema kukueleza siri hii.”
“Sasa kama mngenieleza kulikuwa na tatizo gani?”
“Mzee hii ilikuwa siri nzito sana ambayo hatukutaka mtu yeyote aijue kwa vile umeishakuwa mzazi wetu hatuna budi kukueleza ukweli.”
“Ukweli gani?”
Sued hakuwa na budi kumueleza kisa kizima kutoka mwanzo wa uhusiano mpaka walipofika kwake kwa mara ya kwanza. Taarifa zile zilikuwa kama bomu moyoni mwa mzee Katumba kwa kuamini kile ni kifungo, kwamba kama mzee Kipepeo akigundua mwanaye anayemtafuta yupo kwake lazima atakasirika sana.
Pili aliwaza utajiri kwa kuamini akiwazunguka basi angeuaga umaskini na kurudia enzi zake pia kama watakamatwa Sued na mwenzake angeendelea kulimiki mali yote peke yake.
Alitulia kwa muda huku jasho likimtoka, kitu kilichomshtua Sued.
“Mzee vipi?”
“Mmh! Jamani kwa nini hakunieleza mapema, hamuoni kama
mnanitafutia balaa?”
“Hapana mzee wetu kila kitu kitakwenda kwa siri.”
“Vijana hakuna jambo la siri, lazima mtanirudisha tena gerezani, na uzee
huu si nitafia gerezani?”
“Baba mbona tumeishi muda wote kwa siri hii nzito bila mtu kujua?”
“Mmh! Hapana.”
“Kwa hiyo?”
“Heri muondoke mwende popote lakini si kwangu.”
“Mzee kumbuka tumekutoa wapi na leo upo wapi, kama kutafutwa kwa mwenzangu wameishakata tamaa.”
“Mmh! Ipo kazi.”
“Chondechonde mzee wetu.”
“Basi nimewaeleweni, lakini najua mmenitafutia tatizo.”
“Hapana baba tusitiri kwa hili,” Sued alimpigia magoti.
“Sawa wanangu lakini nimeshtuka sana.”
“Tunajua, tuliogopa kukueleza mapema.”
“Sawa basi nimewaelewa, je, suala la kujifungua litakuwaje?”
“Tutamleta mkunga hapahapa ambaye hajui lolote kuhusiana na taarifa yetu.”
“Mmh! Sawa, basi tuweni makini msije niponza.”
“Tutakuwa makini mzee wetu.”
Waliagana na mzee Katumba aliyerudi chumbani kwake kwenda kulala na kuwaacha na mjadala mzito.
“Bebi umemuelewa baba?” Zulfa aliyekuwa kimya muda wote wakati wa mazungumzo ya mzee Katumba na Sued alimuuliza mpenzi wake.
“Kumuelewa kivipi mpenzi?” Sued hakuelewa swali la Zulfa.
“Unajua mimi simwelewielewi kabisa baba.”
“Sijakuelewa, humuelewi kivipi?”
“Naona amekubali shingo upande.”
“Kwa hiyo?”
“Nina wasiwasi anaweza kutugeuka.”
“Sidhani.”
“Mpenzi acha kumuamini mtu kirahisi namna hiyo, huyu mzee si
mzazi wetu wa kutuzaa anaweza kutugeuka kwa ajili ya fedha,” Zulfa alimtahadharisha Sued juu ya mzee Katumba.
“Zulfa acha kujitia presha, kushtuka kwake ilikuwa lazima kwa vile kitu
tulichomueleza hakukitegemea, hata kama ungekuwa wewe ungeshtuka.”
“Ni kweli ningeshtuka lakini kwenye suala la fedha usimuamini hata mzazi wako.”
“Una maana gani?”
“Baba yangu kuna siku aligombana na mama kwa ajili ya fedha iliyopotea ndani katika mazingira ya utatanishi, kitendo kile kilinishtua sana, baadaye nilimuuliza baba iweje amshtumu mama kuwa amemuibia wakati siku zote anasimamia mali zake?
“Baba alinijibu kuwa usimuamini mtu yeyote kwa suala la fedha, hata awe mzazi wako kwa vile kuna watu wametoa familia zao kafara kwa ajili ya utajiri. Hata mwanafunzi wa Masihi alimgeuka kiongozi wake kwa ajili ya fedha.”
“Kwa hiyo unamaanisha nini?”
“Kwa zawadi ya milioni kumi na tano na gari lazima baba atatugeuka.”
“Sasa tutafanyaje na wewe upo kwenye hali hiyo?”
“Mpenzi samahani, ngoja nifike msalani, haja ndogo nimeizuia kwa kipindi kirefu naweza kupasuka kibofu,” Zulfa alisema huku akiteremka kitandani.
“Wahi mpenzi.”
Zulfa alitoka nje peke yake na kumuacha Sued amejilaza kitandani, kutokana na woga Zulfa hakuingia ndani ya bafu, alichuchumaa pembeni ya choo na kujisaidia haja ndogo. Baada ya kumaliza kujisaidia, wakati anataka kunyanyuka alimuona mzee Katumba akitoka nyumbani kwake. Alitulia pale
chini kwa vile hakupenda amuone.
Mzee Katumba kutokana na kiza, hakuweza kumuona Zulfa aliyekuwa amechuchumaa pembeni ya choo. Kwa vile Zulfa alikuwa ameishalizoea giza alimuona vizuri mzee Katumba akinyata hadi kwenye dirishani lao na kusikiliza kwa muda kisha alitoka kwa kunyata kurudi mlangoni kwake.
Aliufunga mlango wake kisha aliondoka kuelekea njia ya nyuma ya nyumba. Hali ile ilimshtua sana Zulfa na kujiuliza mzee Katumba kufanya vile ana maana gani? Baada ya hali kutulia alinyanyuka na kurudi ndani, mlangoni alikutana na Sued aliyekuwa akimfuata nje baada ya kumuona amechelewa.
“Vipi?” Zulfa alimuuliza Sued.
“Safi, mbona umechelewa?”
“Mmh! Hata sijui.”
”Hujui nini mpenzi wangu?” kauli ile ilimshtua Sued.
“Hata simuelewi baba.”
“Kafanya nini?”
Zulfa ilibidi amueleze Sued aliyoyaona nje, kitu kilichomshtua mpenzi wake.
“Zulfa hebu acha utani!”
“Si utani mpenzi wangu, kuchelewa kwangu nilikuwa bado
nimechuchumaa chini nilipokuwa najisaidia na kuyaona yote.”
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Hata sijui.”
“Sasa kusikiliza dirishani kwetu alikuwa akimaanisha nini?” Sued alizidi kuchanganyikiwa.

ITAENDELEA KESHO
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 15
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500...

ILIPOISHIA:
Zulfa ilibidi amueleze Sued aliyoyaona nje, kitu kilichomshtua mpenzi
wake.
“Zulfa hebu acha utani!”
“Si utani mpenzi wangu, kuchelewa kwangu nilikuwa bado
nimechuchumaa chini nilipokuwa najisaidia na kuyaona yote.”
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Hata sijui.”
“Sasa kusikiliza dirishani kwetu alikuwa akimaanisha nini?” Sued alizidi
kuchanganyikiwa.
SASA ENDELEA...

“Hata sielewi, baada ya kusikiliza kwa muda alifunga mlango wake na
kupitia njia ya nyuma ya nyumba.”
“Usiku huu atakuwa amekwenda wapi?”
“Sued kubaliana na kauli yangu.”
“Ipi?”
“Baba mzee Katumba fedha imemtoa imani.”
“Kwa hiyo atakuwa amekwenda wapi usiku huu?”
“Huenda kaenda kwa Kasabi.”
“Kufanya nini?”
“Kuchukua boti ili aende kwa baba kutoa taarifa.”
“Zulfa una uhakika gani mpenzi wangu?”
“Sued inawezekana mwenzangu huijui fedha vizuri, fedha ni shetani
anayeweza kuwasambaratisha hata wapendao, mtu akamgeuka rafiki yake
kipenzi.”
“Hebu tusubiri kidogo.”
“Tusubiri nini?”
“Kuona amekwenda wapi.”
“Sued leo silali hapa.”
“Sasa tutalala wapi?”
“Popote lakini nje ya mji huu.”
“Sikiliza mpenzi, ili kupata ukweli niache niende kwa Kasabi ili tupate ukweli
huenda ana safari nyingine.”
“Wee nenda lakini leo ikipita salama nitaondoka peke yangu na kukuacha
hapa kwa vile unaona umefika,” Zulfa alitokwa na imani kabisa na mzee
Katumba.
“Usitumie hasira mpenzi, hebu subiri kidogo.”
“Unataka kufanya nini?”
“Nakwenda kwa Kasabi.”
Sued alisema huku akivaa fulana na kutoka kuifuata njia aliyopita mzee
Katumba, alikwenda kwa tahadhari kubwa ili asikutane naye njiani na
kuonekana kama alikuwa akimfuatilia. Japo usiku ulikuwa wa kiza lakini Sued
alitembea macho yake yakiangalia mbele zaidi.
Kila alipomuona mtu akija mbele alijificha na mtu akipita alimuangalia kama
ni mzee Katumba. Alipomgundua siyo yeye aliendelea na safari yake mpaka
kwenye nyumba aliyokuwa akikaa dereva wao wa boti na kutembea kwa
tahadhari kubwa.
Alipokaribia kwa Kasabi aliisikia sauti kama ya mzee Katumba, sauti ile
ilimfanya mapigo yake ya moyo yaende kwa kasi. Alisogea hadi karibu na
chumba cha Kasabi na kuzunguka nyuma ya nyumba sehemu ya dirishani
kusikia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea ndani.
“Basi tuwahi kabla hakujapambazuka.”
“Kwa nini tusiondoke kesho alfajiri?”
“Kasabi utaniudhi, hili linatakiwa kufanyika usiku huu na alfajiri inatakiwa
niwe nimekwisharudi hapa.”
“Sawa mzee wangu, lakini mi si mzoefu sana na safari za usiku.”
“Niachie mimi, nitaendesha kwenda na kurudi kwani kazi ya kutembea
majini usiku ndiyo maisha niliyokulia.”
“Sawa mzee wangu.”
Baada ya muda alisikia mlango ukifungwa na kusikia sauti za nyayo
zikitembea. Sued alishindwa kuelewa mzee Katumba usiku ile anakwenda
wapi, alitamani kumuuliza lakini aliona kama ataharibu kila kitu.
Aliwaacha wao waelekee njia ya ziwani na yeye kurudi nyumbani kumpa
taarifa mpenzi wake alichokikuta kwa Kasabi.
***
Mzee Katumba na Kasabi waliwasili Kayenzo saa sita usiku, baada ya kuipaki
boti yao walielekea nyumbani kwa mzee Kipepeo. Kwa vile hapakuwa mbali
walitumia muda wa dakika tano kufika kwa mzee Kipepeo. Walipofika getini walisimamishwa na askari aliyekuwa akilinda.
“Mna shida gani?”
“Tuna shida na mzee.”
“Mzee gani?”
“Kipepeo.”
“Sasa hivi amelala njooni kesho.”
“Shida yetu ni kumuona leo na si kesho,” alijibu mzee Katumba aliyekuwa
amesimama mbele ya geti.
“Hairuhusiwi kuamshwa akiwa amelala.”
“Sisi si wenyeji wa hapa, nimeingia usiku huu na tunatakiwa usiku huu
turudi tulipotoka.”
“Mmetokea wapi?”
“Some.”
“Some ng’ambo ya ziwa kule kwenye samaki wengi?”
“Ndiyo, tuna shida na mzee lazima tuonane naye kutuchelewesha
kunaweza kukuweka matatani.”
“Mna shida gani?’
“Si ya kumwambia mtu mwingine ila yeye mwenyewe.”
“Hebu subirini,” mlinzi alisema huku akichukua mkonga wa simu na
kubofya namba kadhaa kisha akapiga. Baada ya kuita kwa muda ilipokelewa
ndani.
“Haloo Manoni una shida gani?”
“Mzee kuna wageni hapa wana shida na wewe.”
“Manoni nilikueleza vipi kuhusu wageni wa usiku, waambie waje kesho.”
“Mzee wametoka ng’ambo wamefika muda huu wanataka wakuone ili
waondoke usiku huu.”
“Wana shida gani?”
“Wamekataa kuniambia wamesema wanataka kukueleza mwenyewe.”
“Wanawake au wanaume?”
”Wanaume wawili, mmoja mtu mzima na mwingine kijana.”
“Hebu mpe simu nizungumze naye siwezi kutoka nje muda huu.”
“Sawa mzee.”
Mlinzi alifungua geti na kumweleza mzee Katumba aingie ndani ili
azungumze na mzee Kipepeo kwenye simu.
“Mzee zungumza na bosi kwenye simu.”
“Sawa,” mzee Katumba alisema huku akipokea simu.
“Haloo.”
“Haloo, ndiyo una shida gani usiku huu?”
“Nafikiri tungeonana tungezungumza vizuri kuliko kwenye simu.”
“Muda huu si wa kuonana, hata hivyo nimefanya uungwana kuzungumza
na wewe, sema tu tatizo lako kwenye simu.”
“Sawa mzee wangu, nilikuwa nimekuletea taarifa za binti yako.”
“Binti yangu?” mzee Kipepeo alishtuka.
“Ndiyo.”
“Nani?”
“Zulfa.”
“Zulfa?” alizidi kustushwa na taarifa ile.
“Ndiyo?”
“Umemuona?”
”Ndiyo.”
“Yupo hai?”
“Ndiyo.”
“Muongo!”
“Kweli kabisa mzee wangu.”
“Nakuja.”
Mzee Kipepeo taarifa zile zilimshtua sana na kujikuta akipagawa, kitu
kilichomshtua mkewe aliyeshtuka usingizini.
“Mume wangu vipi?”
“Zulfa.”
“Zulfa! Kafanya nini?”
“Ameonekana.”
“Wapi?” mkewe aliuliza huku akikaa kitako macho yamemtoka pima.
“Kuna mtu yupo nje ameleta taarifa zake.”
“Mume wangu usiwe unaota, taarifa gani za usiku wa manane?”
“Mke wangu kuna watu wapo nje wametoka Some.”
“Some! Usiku huu wamekujaje?”
“Si ndiyo tukawaulize.”
“Wasiwe wanataka fedha ya bure kwa kutunga uongo kuwa Zulfa
kaonekana, walikuwa wapi siku zote?”
“Mke wangu siwezi kutoa hata senti tano bila kumuona kwanza
mwanangu.”
Walitoka sebuleni na kuwasha taa kisha waliwaruhusu wageni kuingia
ndani, wakaingia na kwenda kukaa sebuleni.
“Karibuni,” Alisema mzee Kipepeo huku akijifunga vizuri msuli.
“Asante,” walijibu kwa pamoja.
“Ndiyo karibuni sana.”
“Tumekaribia mzee wangu, mi naitwa Katumba ni mwenyeji wa Some na
huyu ni dereva wetu wa boti anaitwa Kasabi.“
“Ndiyo, umesema una taarifa za binti yangu?”
”Ndiyo.”
“Umemuona wapi?”
“Kwanza kabla ya yote kama nitafanikisha kumpata nitapata hiyo zawadi?”
Katumba aliulizia kwanza zawadi.
“Nilitangaza mwenyewe sikulazimishwa na mtu, nikimpata binti yangu
akiwa hai au amekufa nitatoa nilichokiahidi.”
Basi mzee Katumba alianza kuelezea historia ya Sued na Zulfa toka siku
ya kwanza kufikia kwake, yeye akijua wote wale ni wanaume kwa majina ya
Salum na Fadhil. Akaeleza alivyokaa nao kama watoto wake, muda ukikatika
bila kujua kama Fadhil ni mwanamke mwenye jina la Zulfa anayetafutwa kwa
udi na uvumba mjini na mzazi wake.
Japokuwa tabia za Zulfa zilimchanganya kuonekana kama za kike, lakini
kwa vile alikuwa na ndevu alishindwa kumtambua. Ila tabia zake kila kukicha
zilikuwa zikimchefua kwa kuonekana kudeka sana na kulegea pia kutofanya
kazi ngumu.
Mabadiliko ya Fadhil yalimshtua baada ya siku moja kuliona tumbo la
kike, alishtuka na kutojua kwa nini walimficha kuwa ni mwanamke. Aliamua
kusubiri mpaka muda wa kujifungua ili aujue ukweli.
Ndipo siku ile majira ya saa tatu usiku baada chakula cha usiku walipomwita
chumbani kwao na kumweleza ukweli kuwa Fadhil si jina lake bali anaitwa
Zulfa Kipepeo na ni mtoto wa tajiri huyo anayetafutwa na wazazi wake. Mzee
Katumba aliendelea kuelezea kuwa alishtuka sana na kuwaomba waondoke
kwa vile aliogopa kufungwa kama ingejulikana wapo pale.
Lakini walimbembeleza waendelee kukaa palepale mpaka atakapojifungua.
Alisema aliwakubalia mdomoni lakini moyoni alipanga kupeleka taarifa zile
kwa mzee Kipepeo kabla hakujapambazuka.
“Unayosema ni kweli?” mama Zulfa aliuliza akiwa haamini.
“Ndiyo.”
“Zulfa mwanangu?”
“Ndiyo mama.”
“Ana ujauzito?”
“Tena wa miezi saba.”
“Mungu wangu, mtoto huyu.”
“Yaani hata mimi nashangaa maisha ya hapa yalivyo mazuri aliyoyakimbia
na kuja kuishi kijijini pasipo na umeme.”
“Mume wangu unasemaje?” mama Zulfa alimuuliza mumewe aliyekuwa
ameshikilia tama akiwa haamini alichoambiwa.
“Kwa vile ameleta taarifa usiku, kesho tutakwenda na polisi kumkamata
huyo kijana na kumrudisha Zulfa nyumbani.”
“Hapana mume wangu mguu wako mguu wao, namtaka mwanangu kabla
hakujapambazuka.”
“Tutafanyaje?”
“Wachukue wafanyakazi wako na polisi wawili muwafuate usiku huu,
tumia boti kubwa, namtaka mwanangu... namtaka mwanangu,” mama Zulfa
alichanganyikiwa kusikia mwanaye yupo hai.
Mzee Kipepeo alitoka hadi kituo cha polisi ambako aliwakuta polisi
wamepitiwa na usingizi. Baada ya kugonga meza walishtuka na kushangaa
kumuona mzee Kipepeo usiku ule.
“Vipi mzee mbona saa hizi?” askari aliuliza huku akifikicha macho.
“Si salama, mkuu yupo?”
“Kuna nini tena mzee?”
“Naomba kwanza nimuone mkuu wenu.”
“Yupo ofisini kwake.”
Mzee Kipepeo alivuka kaunta na kuelekea kwenye ofisi ya mkuu wa kituo,
aligonga mlango na kumfanya mkuu aliyekuwa amesinzia kushtuka na kusema
kwa sauti ya juu:
“Nani?”
“Mimi mkuu,” mzee Kipepeo alisema huku akiingia, alipomuona alishtuka:
“Ha! Mzee mbona usiku?”
“Binti yangu kaonekana.”
“Kaonekana?” mkuu alishtuka na kumfanya akae sawa kitini.
“Ndiyo.”
“Wapi?”
“Some.”
“Si ng’ambo ya ziwa?”
“Ndiyo.”
“Kwa hiyo unasemaje mzee wangu?”
“Nahitaji askari wa kuondoka nao usiku huu kwenda kumchukua mwanangu
na kumtia hatiani mtu aliyemtorosha.”
“Unataka askari wangapi mzee wangu?”
“Kwani leo kituoni wapo wangapi?”
“Sita.”
“Wanne watanitosha.”
Mkuu wa kituo alitoka ofisini kwake na kuwakuta vijana wake wamekaa
wakisubiri kujua kilichompeleka pale mzee Kipepeo usiku ule.
“John, Kisese, Makumi na J4 chukueni silaha na ongozaneni na mzee.”
Askari waliochaguliwa na mkuu wa kituo walichukua silaha na kuongozana
na mzee Kipepeo. Mzee Kipepeo alirudi hadi nyumbani na kuwaamsha
wafanyakazi wake wote na kuwachukua kumi na tano kuongeza idadi ya watu
wanaomfuata Zulfa.
Alitumia boti yake aliyokuwa akiitumia katika shughuli zake na kubeba
watu wote wale. Mama Zulfa kutokana na uchungu wa mwanaye naye alitaka
kuingia kwenye boti akamsake mwanaye lakini mumewe alimkataza kwa vile
yeye hakuwa na umuhimu kwenye safari ile.
Baada ya watu wote kuingia kwenye boti, safari ya kurudi Some ilianza.
Boti iliondoka Kayenzo saa nane za usiku na ilibeba watu ishirini na mbili.
Mzee Katumba kila boti ilivyokuwa ikizidi kwenda ndivyo alivyoona anauaga
umasikini kwa vile alijua watawakamata kama kuku kwenye banda kwa vile
hawakujua nini kinaendelea.
Safari ilichukua saa tatu, waliingia Some saa kumi na moja alfajiri, mzee
Katumba aliongoza kundi la watu ishirini kuelekea kwake. Wakiwa njiani
askari mmoja alitoa wazo.
“Jamani tunaonekana kama tunakwenda kwenye sherehe, hili ni tukio zito
mzee tukikaribia kwako tujulishe ili tufanye kazi ya kijeshi.”
“Sawa vijana wangu, tumekaribia.”
“Nyumba yenyewe ipo wapi?”
“Ile mbele inayoonekana bati.”
“Mzee kumbe unajiweza kuwa na bati kijijini!” askari mmoja alitania.
“Hivyohivyo tunaganga njaa.”
“Samahani naomba tutangulie ili tuiweke nyumba chini ya ulinzi,” alisema
askari aliyekuwa ameshikilia bunduki.
“Mi nafikiri hakuna haja ya kutumia silaha kwa vile kundi hili hawezi
kukimbia,” mzee Katumba alitoa wazo.
“Lazima tuiweke chini ya ulinzi kwa silaha, hatujui mtuhumiwa amejiandaa
vipi au ana silaha gani?”
“Hana silaha yoyote.”
“Huwezi kutufundisha kazi mzee, wewe umeshatuonesha nyumba kazi
nyingine tuachie sisi,” askari mmoja alimkata kauli mzee Katumba.
“Jamani msitumie nguvu, hakikisheni mwanangu anakuwa salama,” mzee
Kipepeo aliyekuwa kimya muda wote aliwatahadharisha polisi.
“Hakuna tatizo mzee, kazi tutaifanya vizuri sana.”
Askari walitangulia kwenye nyumba kwa kufuata maelekezo ya sehemu
gani wapo Zulfa na mpenzi wake Sued. Baada ya kufika na kuzunguka
nyumba wanayoishi wapenzi wawili, waliwaita na vijana wa mzee Kipepeo
ambao nao waliizingira nyumba ile.
Baada ya kuhakikisha kila kitu kipo vizuri askari mmoja aliuvaa mlango wa
nyumba ya akina Sued ambao ulisalimu amri na wote watatu waliingia ndani
kama wanakwenda kumkamata gaidi, silaha zikiwa mikononi. Kwa vile ndani
palikuwa na giza, mmoja alikuwa na tochi kubwa mkononi.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 16
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500...

ILIPOISHIA:
Baada ya kuhakikisha kila kitu kipo vizuri askari mmoja aliuvaa mlango wa nyumba ya akina Sued ambao ulisalimu amri na wote watatu waliingia ndani kama wanakwenda kumkamata gaidi, silaha zikiwa mikononi. Kwa vile ndani palikuwa na giza, mmoja alikuwa na tochi kubwa mkononi.
SASA ENDELEA...

Waliingia chumbani na kushangazwa na hali iliyokuwemo ndani ya chumba hicho, hakukuwa na mtu yeyote. Walijaribu kuangalia chini ya kitanda lakini hawakukuta kitu chochote.
“Mzee hakuna kitu ndani!” askari alipaza sauti.
“Nini?” mzee Katumba alishtuka.
“Humu ndani hakuna mtu.”
“Acha utani kijana angalia vizuri wamo ndani wamelala,” mzee Katumba alisema huku akiingia ndani.
“Mzee watu waliolala humu ndani wapo wapi?”
“Mmh! Watakuwa wapi sasa?”
“Hebu waangalieni msalani?”
Mtu mmoja aliingia msalani ambako hakukuwa na mtu, alitoka na kusema:
“Hata huku hakuna mtu.”
“Sasa watakuwa wapi?” mzee Katumba alichanganyikiwa kuwakosa watu aliowaacha wamelala.
“Mzee huyo mwanangu yupo wapi?” aliuliza mzee Kipepeo ambaye naye
alishtuka mambo kwenda tofauti.
“Mzee wangu hata mimi nachanganyikiwa nimewaacha wamelala, hata tukiwauliza majirani watasema ukweli. Eti Kasabi mpaka usiku Salum alikuwa wapi?”
“Niliagana naye hapa baada ya kufuata fedha ya mafuta ya boti.”
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Lakini toka mwanzo sielewi umenifuata na sasa tumekuja na polisi kwani kuna nini?” Kasabi aliuliza.
“Salum kumbe alimtorosha binti wa watu na kuja naye huku.”
“Binti gani?”
“Fadhil.”
“Sasa mzee kweli umechanganyikiwa, Fadhil si mvulana, ubinti umetoka wapi?”
“Walitudanganya lakini Fadhil jina lake ni Zulfa na si mvulana ni msichana
yule.”
“Makubwa! Mmh!” Kasabi naye alichanganyikiwa kusikia Fadhil hakuwa
mwanaume ila msichana.
“Na zile ndevu?”
“Alibandika tu aonekane mwanaume.”
“Jamani, sasa walifanya vile ili iweje?”
“Hata mimi walinieleza usiku wa jana ukweli na ule unene wa Fadhil kumbe
ni ujauzito.”
“Sasa jamani hamkutuleta mje mjadiliane, mngejadiliana kabla ya kuja,”
mzee Kipepeo aliingilia kati baada ya kuona mjadala unakuwa mrefu.
“Mzee wangu yaani nashangaa sana, kwangu ni kama njozi za mchana, kilichotokea nimewaacha wamelala,” mzee Katumba alijitetea.
“Mzee si kuna siku tulikuja hapa ukasema una vijana wawili wa kiume?”
askari mmoja alimkumbuka mzee Katumba na siku waliyofanya oparesheni ya kumsaka Zulfa kijijini Some.
“Ndiyo kijana wangu, kumbe yule mwingine si mvulana ni msichana
alibandika ndevu za bandia. Na yule kijana mliyekuwa mkimuuliza ndiye aliyemtorosha binti wa mzee.”
“Mzee kweli huyo kijana tulimuona ila mwenzake hatukumuona hasa baada ya kuelezwa ni mvulana.”
“Sasa atakuwa wapi?”
“Hata sijui lakini hatakuwa mbali, tuanzishe msako wa nyumba kwa nyumba,” askari alitoa wazo.
Kwa vile kulikuwa kumepambazuka, alitaarifiwa mwenyekiti wa kitongoji kile taarifa za kuwa kijana wa pili wa mzee Katumba hakuwa mwanaume bali mwanamke na ndiye aliyekuwa akitafutwa. Baada ya taratibu zote, msako ulianza kijijini kizima nyumba kwa nyumba.
Msako ulianza nyumba kwa nyumba lakini hawakuonekana, walikubaliana kuwatafuta nje ya kijiji kwa kuamini hata kama wametoroka hawatakuwa mbali lazima watawapata. Waliongezewa nguvu na vijana wa Some kuhakikisha wanawatia mikononi. Waliingia mashambani kuwasaka kwa kutawanyika kila kona.
***
Sued baada ya kurudi kutoka kwa Kasabi alikomfuatilia mzee Katumba, aliingia ndani na kumkuta Zulfa akiwa amekaa kitandani akimsubiri kwa hamu akitaka kujua ya huko alikokwenda amekutana na kitu gani. Alipomuona anaingia tu alimuuliza:
“Ehe! Za huko?”
“Mmh!” Sued aliguna.
“Mbona unaguna?”
“Yaani hata sielewi, baba kamchukua Kasabi eti waende Some usiku huu.”
“Umeamini sasa?”
“Bado sijajua anakwenda kufanya nini.”
“Sued jamani unanisikitisha, kama kusoma hujui hata picha huoni?”
“Ina maana kaenda kutoa taarifa kwa baba yako?”
“Unafikiri anakwenda wapi na kwa nini asiende siku zote aende leo baada ya kumueleza kuwa sisi ni kina nani!”
“Kwa hiyo?” Sued alichanganyikiwa.
“Hakuna cha kwa hiyo, tuondoke hapa la sivyo tutakutwa. Unafikiri baba akipata taarifa itakuwaje? Siku haitapita lazima atakuja usiku huu. Lazima utakamatwa wewe na kufungwa hata bila kufikishwa mahakamani kwa vile baba yangu ni mtu mkubwa pia ana hela. Nami sipo tayari kukupoteza, nataka nijifungue ikiwezekana ukiwa unanishuhudia kwa macho yako pia umbebe mtoto wetu.”
“Sasa tufanyeje maana hapa nilipo nimechanganyikiwa,” Sued aliomba msaada kwa Zulfa.
“Sued mpenzi wangu, hapa tunatakiwa tuondoke usiku huu tukaishi popote ili kuhakikisha hatutengani.”
“Unafikiri kama wakija kututafuta tutakimbilia wapi?”
“Tukajifiche mlimani nina imani wakija kututafuta na kufanikiwa kujificha wakiondoka tutaishi hukohuko mpaka nijifungue kisha tutarudi nyumbani, nina imani wazazi wangu hawatanilazimisha tena kwenda kusoma zaidi ya kunioza kwako ili niwe mkeo wa halali tena kwenye maisha ya uhuru.”
“Mmh! Sidhani kama baba yako atakubali, lazima atanifunga tu,” Sued alisema kwa sauti ya woga.
“Hawezi labda atufunge wote, Sued nimejitoa kwako kwa hali na mali,
nitakupigania muda wote wa pumzi zangu.”
“Najua, lakini najua hasira za baba yako ni kubwa sana kwangu.”
“Tukipata watoto zitayeyuka kama donge la mafuta kwenye kikaango cha
moto.”
“Mmh! Siamini.”
“Sued tufunge vitu vya muhimu tuondoke, majadiliano hayana nafasi kwa
muda huu.”
Walifunga vitu vya muhimu na kuamua kuondoka usiku uleule, walifunga mlango vizuri na kutoka eneo la nyumbani kwao bila kujua wanakwenda wapi.
Walivuka maeneo ya watu na kuanza kuingia kwenye mashamba, giza nalo lilitishia usalama wao kwa kuhofia kukutana na wanyama wakali wanaotembea usiku.
Zulfa ujauzito wake ulisababisha avimbe miguu, hali iliyomfanya atembee taratibu kwa kusikilizia maumivu. Lakini alivumilia huku akiuma meno ili kuhakikisha wanaondoka eneo la kijiji na kwenda kwenye mlima uliokuwa mbali kidogo na eneo wanaloishi. Mlima ule ulikuwa na miti mingi iliyofanya uwe unatisha sana.
Zulfa alikuwa msichana mwoga sana, hata mende alimuogopa lakini katika mapenzi alikuwa jasiri kuliko Sued, alikuwa tayari hata kupambana na simba kuliko kumpoteza mpenzi wake.
Walitembea kimyakimya ili wasizungumze lolote, wanakijiji wasiwasikie huku wakiwa wameshikana mikono. Baada ya mwendo wa saa tatu, walivuka eneo la tambarare lililokuwa na mashamba na mapori na kuanza kupanda mlima.
Kutokana na giza la usiku ule ulitakiwa ujasiri mkubwa ambao ndiyo aliokuwa nao Zulfa. Walipanda hadi juu kwa kuvutana huku Zulfa akionekana kuchoka sana.
Walipofika sehemu ambayo waliiona inafaa, waliamua kupumzika ili asubuhi watafute sehemu nzuri ya kukaa kwa kipindi kile.
Walitafuta sehemu isiyokuwa na mawe na kujilaza kutokana na uchovu wa kutembea zaidi ya saa nne. Zulfa ndiye aliyekuwa amechoka sana na kuhema kwa shida kutokana na hali yake ya ujauzito.
Sued alimwagia maji kichwani mpenzi wake ambayo yalipunguza presha kisha alimfunika blanketi na usingizi ulimpitia. Wa kwanza kuamka alikuwa Sued, macho yake yalipoangalia chini ya mlima kwa mbali aliona watu wengi wakielekea kwenye mlima waliokuwa.
Alishtuka sana, alipoangalia vizuri alimuona mzee Katumba akiwa miongoni
mwa watu wale, askari na mmoja wa wafanyakazi wa mzee Kipepeo, baba wa
mpenzi wake. Alimshtua Zulfa aliyekuwa kwenye usingizi mzito.
“Zulfa...Zulfa.”
“Nini mpenzi?”
“Amka.”
“Niache kidogo mwili umechacha unaniuma kila kona.”
“Amka mpenzi tunakamatwa.”
“Na nani?”
“Hebu amka uangalie chini ya mlima kwa mbali uone kundi la watu wanakuja
upande wetu.”
“Mungu wangu wako wapi?” Zulfa alisema huku akikurupuka alipokuwa
amelala na kutazama chini ya mlima. Alishtuka kuona kundi la watu wakisogea kwenye mlima ule, baada ya kutuliza macho baadhi ya watu aliwafahamu.
“Ha! Yule si baba mzee Katumba?”
“Ndiye.”
“Na..na..yule si Masanja na John.. Mohamed..na..na aah,” Zulfa
alichanganyikiwa na kushindwa afanye nini kwa vile watu walikuwa wamekaribia
kwenye mlima ule.
“Sued mpenzi wangu unaona sasa?”
“Sasa mimi kosa langu nini?”
“Nilikueleza tusimweleze yule mzee matokeo yake ni haya.”
“Bebi tulishayazungumza, tujipange jinsi wa kujiokoa ili tusishikwe na si
kulaumiana.”
“Sasa tutafanyaje maana hapa akili yote imepoteza uwezo wa kufikiri.”
“Tunatakiwa tutafute eneo tujifiche na si kitu kingine.”
“Mmh! Tufanye hivyo mara moja la sivyo tutakamatwa wanazidi kuja.”
“Na hii mizigo yetu?”
“Hata sijui tufanye nini, Sued we mwanaume tumia akili yako bwana.”
“Ooh! Nimepata wazo.”
“Wazo gani?”
“Kwa vile hatuna njia yoyote ya kujiokoa na watu wenyewe wamekaribia, lazima tufiche mizigo yetu ili nasi tujifiche.”
“Sued mawazo gani hayo! Yaani tuifiche mizigo wapi na sisi tujifiche wapi tusionekane, kwa nini tusitorokee upande wa pili tuwakimbie?”
“Zulfa mpenzi unafikiri tukikimbia tutafika wapi bila kukamatwa?”
“Mpaka wafike tutakuwa tumefika mbali.”
“Zulfa hali yako huitazami, unatembea kama kinyonga unafikiri tutafika wapi
bila kukamatwa?”
“Nitajitahidi mpenzi wangu,” Zulfa alisema huku akiuma meno kujinyoosha
kiuno.
“Sikiliza, mizigo hii tunaificha na sisi tunajificha wakitukamata potelea mbali.”
“Tutajificha wapi mpenzi wangu bila kuonekana?”
“Hebu subiri.”
Sued alisema huku akiondoka eneo lile na kuelekea mbele kidogo kwenye mti mmoja mkubwa ulioota juu ya mwamba mmoja ambao kwa chini kulikuwa na kisima cha maji yaliyokuwa yakitokea kwenye pango lililotokea ndani ya mwamba ule.
Aliuangalia mti ule mkubwa, labda wanaweza kupanda juu na kujificha.
Zulfa alibakia akiwatazama watu ambao walikuwa mbali kidogo wakiukaribia
ule mlima. Wasiwasi ulimjaa na kutamani dunia iwameze ili usionekane kwani aliamini kama watakamatwa, lazima mpenzi wake atafungwa na baba yake ambaye alijua ana hasira sana kwa kumtoroka.
Sued naye aliendelea kuuangalia ule mti ambao chini yake kulikuwa na chanzo cha maji yaliyokuwa yakielekea bondeni kwa kutengeneza mito na mifereji na kutumika na wanakijiji wa Some. Alipouangalia ule mti aliona kama angekuwa peke yake angeweza kuukwea na kujificha lakini hali ya mwenzake ya ujauzito asingeweza kuupanda mtu ule mkubwa.
Akiwa anajiuliza afanye nini sauti za watu zilizidi kuukaribia mlima zilisikika na kuzidi kumchanganya Zulfa aliyemfuata Sued aliyekuwa bado akiangalia jinsi ya kujificha.
“Sued wamefika!”
“Muongo!”
“Kweli wamefika, wamekaribia.”
Sued alitoka eneo lile na kurudi sehemu waliyokuwa mwanzo wakiwatazama watu kwa chini ya mlima na kushangaa kuwaona bado wako mbali japo ndiyo walianza kuupanda mlima.
“Sasa tutafanya nini?” Zulfa aliyekuwa akitetemeka alimuuliza mpenzi wake aliyekuwa ametuliza mawazo akiwatazama watu wakianza kuupanda mlima.
“Sued mbona hunijibu au umeridhika tukamatwe?”
“Subiri,” Sued alisema huku akienda kwenye mti mmoja mkubwa
na kuvunja tawi na kurudi nalo kisha alianza kuchimba sehemu yenye udongo.
“Sued unataka kufanya nini?” Zulfa hakuelewa mpenzi wake anataka
kufanya nini.
“Zulfa punguza presha pupa yako inaweza kuharibu kila kitu,” Sued
alimuonya mpenzi wake.
“Sawa mpenzi wangu lakini wanakaribia.”
“Nimekwambia hebu tulia basi.”
“Sawa mpenzi wangu,” Zilfa alikubali huku akijikunyata kwa hofu kwa kuamini wamekamatwa.

Itaendelea Jumatatu
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 17
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500...

ILIPOISHIA:
“Sued unataka kufanya nini?” Zulfa hakuelewa mpenzi wake anataka kufanya nini.
“Zulfa punguza presha pupa yako inaweza kuharibu kila kitu,” Sued alimuonya mpenzi wake.
“Sawa mpenzi wangu lakini wanakaribia.”
“Nimekwambia hebu tulia basi.”
“Sawa mpenzi wangu,” Zilfa alikubali huku akijikunyata kwa hofu kwa
kuamini wamekamatwa.
SASA ENDELEA...

“Lakini Sued umeyataka yote,” Zulfa alishindwa kutulia aliendelea
kumlaumu mpenzi wake.
“Bebii hebu tulia kwanza.”
“Sawa.”
Sued baada ya kuchimba shimo fupi aliingiza mizigo yao na kuifukia kisha alichukua michanga mikavu na kuiweka juu ya sehemu waliyoificha mizigo yao na kumweleza mpenzi wake:
“Nifuate.”
“Wapi tunakwenda?”
“Zulfa acha ubishi hebu twende,” Sued alikuwa mkali.
“Sawa mpenzi wangu,” Zulfa alikubali.
Waliongozana hadi kwenye mti ule mkubwa ambao kwa chini yake
kulikuwa na maji yaliyokuwa yakitokea kwa ndani kwenye pango ambalo
ndani kulikuwa na kiza kizito.
“Sued huku wapi tena?”
“Hatuna sehemu nyingine ya kujificha lazima tuingie kwenye maji haya kwani kiza chake cha ndani nina imani hawawezi kutuona.”
“Hapana panatisha sana huko, siwezi kuingia, jifiche mwenyewe mi
nitajua pa kujificha,” sehemu aliyoambiwa aingie ilivyokuwa ilimtisha sana, akakataa.
“Zulfa unanipenda?” Sued alimuuliza mpenzi wake aliyeonekana hayupo tayari kuingia, wakati huo sauti za watu zilizidi kusogea kuonesha hawapo mbali.
“Ndiyo mpenzi wangu nakupenda kuliko chochote kilicho chini ya jua.”
“Kama unanipenda naomba tufe wote.”
“Mmh! kweli nguvu ya mapenzi ni kubwa sana, sina jinsi mpenzi wangu nipo tayari kwa lolote nitaingia hata nikifa nitakufa katika kulipigania penzi langu,” Zulfa alikuwa tayari kuingia kwenye pango lenye maji na kiza kizito.
Wakati huo sauti za watu zilikuwa zikisogea na kuwafanya wazidi
kuchanganyikiwa. Zulfa aliona kama wanachelewa alimsukumia Sued
kisimani bila kujua kina chake na yeye kujirusha ndani ya maji.
Sued baada ya kuangukia ndani ya kisima kilichokuwa kimejaa maji.
Kwa vile alikuwa hajui kina chake alijikuta akizama mpaka chini bila kupata kuzuizi chochote na kumfanya atapetape kutaka kujiokoa kutokana na kina kuwa kirefu kwenda chini.
Bahati nzuri katika kutapatapa alibahatika kushika mizizi ya mti ule
mkubwa iliyokuwa ikitoka juu iliyoingia majini na kuwa kama kamba.
Aliishikilia kwa nguvu na kuanza kujinyanyua juu kutafuta hewa, kwa kudra ya Mungu aliweza kukanyaga jiwe lililokuwa pembeni ya kisima kile, hivyo kumsaidia kupanda juu na kutulia. Alivuta hewa kwani sehemu aliyoibukia ilikuwa chini ya mwamba wa pango lile na sehemu yenyewe ilikuwa na giza na kuweza kuuona mwanga kwa mbele yake.
Zulfa naye alifika chini na kuanza kutapatapa kujiokoa na kifo cha maji. Sued ambaye alikuwa tayari kavuta pumzi ya kutosha alizama ndani ya maji na kumtafuta mpenzi wake ambaye aliamini anaweza kufa maji kwa vile hakuwa na ujuzi wa maji tofauti na yeye aliyekuwa mtundu wa kuogelea kwenye ziwa na kwenye mito.
Sued alikwenda mpaka chini ambako alikutana na Zulfa akitapatapa kutaka kuokoa maisha yake, alimshika na kupanda naye juu kwa msaada wa mizizi ya mti na kumsimamisha juu ya jiwe ambalo lilimuwezesha kutoa kichwa nje na kuweza kuvuta hewa ambayo aliipoteza kwa muda alipokuwa chini ya maji.
Sued alimshikilia mpenzi wake aliyekuwa akihema kwa kasi ili asirudi tena kwenye maji. Taratibu pumzi za Zulfa zilianza kukaa vizuri na kuweza kushikilia mizizi ya mti mwenyewe huku akisimama juu ya jiwe.
Wakiwa wametulia wamefichwa chini ya mwamba wa pango lile ambalo juu yake kulikuwa na mti mkubwa ulioingiza mizizi yake ndani ya maji, waliwaona watu wakifanya msako kila kona ya mlima kuwatafuta.
Sued aliyasikia mapigo na pumzi za mpenzi wake kutokana na hofu, baada ya kuwaona watu wawili wakisogea kwenye kisima kile. Baada ya kufika karibu na kisima aliyasikia mazungumzo yao ya kuyasifia yale maji.
“Aisee maji safi kweli haya,” Zulfa alimtambua aliyekuwa akisema alikuwa ni mmoja wa wafanyakazi katika nyumba ya baba yake.
“Haya ndiyo tunategemea kunywa na kumwagia mashamba, wananchi tunaokaa mbali na ziwa,” kijana mmoja mwenyeji wa Some alimjibu.
Baada ya muda waliongezeka wengine ambao walifika kunywa maji na wengine kunawa jasho la kuhangaika kuwatafuta watu bila mafanikio. Waliwasikia wakiulizana:
“Sasa watakuwa wamekwenda wapi?”
“Mzee Katumba anasema wakati anaondoka walikuwa wamelala
anashangaa kutowakuta.”
“Mimi nina wazo,” mmoja alisema.
“Wazo gani?”
“Mi naona kuja huku tunajisumbua tu.”
“Kwa nini?”
“Kama mzee Katumba aliweza kwenda mjini usiku ule, wale
wanashindwa vipi kwenda mjini? Hivi kweli mlima na pori hili linavyotisha,
mchana tu mtu hawezi kuja peke yake ndiyo waje usiku wawili huku?”
“Mmh! Kweli inawezekana unachokisema ni kweli.”
“Kama wangekuwa wapo huku tungewaona hata kama wangekuwa
wamevuka mlima wasingefika mbali.”
Wakati wakijadiliana kumbe ndani ya lile pango walilokuwa amejificha Sued na Zulfa kulikuwa na nyoka mkubwa aliyekuwa akiishi mle. Wakiwa wametulia wamekumbatiana, yule nyoka alitoka sehemu yake kwenda nje
kuota jua. Wa kwanza kumwona alikuwa Zulfa ambaye alipiga kelele ya
woga.
“Mamaa! Nyoka tunakufa,” kelele zile zilimfanya Sued kugeuka na
kushtuka kumuona nyoka mkubwa akielekea upande wao.
Sued kwa haraka alimziba mdomo na kumkumbatia kwa nguvu mpenzi wake huku akimnong’oneza wafumbe macho. Zulfa akiwa anatetemeka na mapigo ya moyo kwenda mbio, alimshikilia kwa nguvu Sued huku akifumba macho asione kinachoendelea kwa yule nyoka, kama atawameza wote wawili au vipi. Japo uwezo wa kuwameza hakuwa nao.
Waliokuwa wamekaa karibu na kile kisima waliisikia sauti ya mwanamke ya mshtuko na kuwafanya washtuke. Wakiwa bado hawaelewi sauti ile inatoka wapi, mmoja aliuliza:
“Jamani mmesikia sauti ya mwanamke?”
“Mi nimesikia,” mmoja aliunga mkono.
“Hata mimi,” na mwingine alisema amesikia.
“Inaweza kuwa inatoka wapi?”
“Mmh! Hata sijui, mlima wote tumemaliza kutafuta bila mafanikio, labda
kisimani tu.”
“Sasa wakae kisimani wamekuwa chura au nyoka?” mmoja alihoji.
Sued na Zulfa waliendelea kukumbatiana huku wakimuomba Mungu wasimezwe na nyoka ambaye walijua lazima angewafanya kitu chochote kibaya cha kuwadhuru. Waliendelea kumuomba Mungu huku wakiwasikia wale watu wakiijadili sauti ya mwanamke ya woga inatoka wapi.
“Jamani sauti hiyo itakuwa inatoka wapi?”
“Mmh! Kama sikosei imetoka kisimani,” mmoja alijibu.
“Kisimani?” mwingine alishtuka.
“Mmh! Inawezekana ni ya jini, mlima huu mkubwa,” mmoja alichangia.
“Inawezekana kweli ni sauti ya jini, milima kama hii huwa haikosi vitu vya
kutisha. Kuna taarifa mlima huu kuna nyoka mkubwa sana, lakini hajawahi
kumdhuru mtu yeyote. Waliokuja kwenye mlima huu wapo waliobahatika
kumuona akiota jua.
Wapo wanaosema ni mzimu na wengine jini linalolinda mlima na kisima
hiki.”
“Basi inawezekana hata hiyo sauti ni yake.”
“Basi mlima huu haufai.”
“Jamani vipi mbona mmekaa?” Sauti toka mbali iliwauliza wale vijana
ambao walikuwa wakiijadili sauti waliyoisikia bila kumuona mtu.
“Jamani tumechoka, hakuna dalili zozote wa kuonekana watu hao.”
“Kwa hiyo?”
“Naona turudi tu, tukubali wametuzidi akili.”
“Na kweli, kama walikaa na mzee Katumba zaidi ya mwaka na nusu bila
kujua anakaa na watu wa aina gani itakuwa sisi?”
“Wale kama majasusi wana uwezo wa kujibadili kulingana na mazingira.”
“Kulingana na maelezo ya mzee Katumba yule msichana mimba yake ni kubwa sana, hivyo lazima ataonekana tu.”
Baada ya kutafuta kwa zaidi ya saa tatu bila mafanikio, waliamua
kuondoka kwenye ule mlima. Sued na Zulfa waliwasikia watu wale
wakisema wanaondoka na baada ya muda hali eneo lile ilikuwa kimya.
Wa kwanza kufumbua macho alikuwa Sued ambaye alipepesa macho kuangalia wapo katika hali gani. Alimwita mpenzi wake kwa sauti ya kunong’ona kwa kuweka mdomo karibu na sikio.
“Zulfa.”
“Mmh!”
“Upo sawa?”
“Nipo sawa sijui wewe?”
“Mi nipo sawa.”
“Nasikia kimya wameondoka?” Zulfa aliuliza kwa sauti ya uchovu wa maji.
“Inawezekana nimesikia wakisema wakiondoka.”
“Na yule nyoka?”
“Zulfa usimtaje tumuombe Mungu tutoke salama.”
“Yaani hapa naona maisha yetu ni Mungu tu.”
“Ndiye tunatakiwa kumuomba bila hivyo tutakufa tunajiona.”
“Basi tutoke haraka hapa nguvu zimeniishia naweza kuangukia kwenye maji na kufa.”
“Sasa fanya hivi wacha nitangulie juu kisha nikuvute, naamini kwa hali yako huwezi kufika juu peke yako.”
“Fanya haraka hali ni mbaya.”
Sued alitembea kutumia mizizi huku akikanyaga kwenye mawe ya
pembeni mpaka nje. Baada ya kuiona ile njia ni nyepesi kutoka mle tofauti na alivyofikiria, alirudi ndani ya kisima na kukaa nyuma ya mpenzi wake kisha wakawa wanatoka kwa kufuata maelekezo yake.
Walifanikiwa kutoka nje ya maji Zulfa akiwa hoi kizunguzungu kilikuwa kikubwa alijilaza chini akiwa hajitambui. Sued alijitahidi kumtoa eneo lile, kwa vile hakujua yule nyoka mkubwa baada kutoka ndani ya pango alielekea wapi.
Alimsaidia kutembea taratibu huku akimshikilia kwenye bega. Baada ya mwendo mfupi Zulfa alishtuka baada ya kuona kitu cha kutisha. Bila kutoa sauti alimuonesha mpenzi wake kwa kidole. Sued aligeuza shingo na kushangaa kumuona yule nyoka waliyemuona pangoni akiwa amejilaza kwenye jiwe kubwa akiota jua.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 18
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500...
.ILIPOISHIA:
Alimsaidia kutembea taratibu huku akimshikilia kwenye bega. Baada
ya mwendo mfupi Zulfa alishtuka baada ya kuona kitu cha kutisha. Bila
kutoa sauti alimuonesha mpenzi wake kwa kidole. Sued aligeuza shingo
na kushangaa kumuona yule nyoka waliyemuona pangoni akiwa amejilaza
kwenye jiwe kubwa akiota jua.
SASA ENDELEA...
Hawakusema kitu walibadili njia ili kurudi sehemu waliyoficha mizigo
yao. Walitembea huku Zulfa akitetemeka kwa hofu na kumshikilia mpenzi
wake kwa nguvu ili asiwe mbali naye. Walipofika sehemu waliyoficha vitu
vyao, Zulfa alikuwa na wasiwasi wa kumezwa na yule nyoka mkubwa.
“Sued tuondoke, huku hapatufai.”
“Kwa nini?”
“Sued unauliza jibu, ina maana yule nyoka hukumwona?” Zulfa alionesha
kumshangaa mpenzi wake.
“Nina imani yule nyoka hana madhara kwetu.”
“Sued! Tokea lini nyoka akakosa madhara?”
“Yule si nyoka wa kawaida kama wengine.”
“Ni nyoka wa aina gani?”
“Yule ni mlinzi wa mlima, misitu na maji.”
“We umejuaje?”
“Ina maana hukusikia wale watu waliokuwa wakitutafuta walivyokuwa
wakizungumza?”
“Nilikuwa na moja pale? Akili yangu ilihama nikabakia mwili, kilichoendelea sikujua, nilijua tunakufa kifo kibaya cha kumezwa na nyoka.”
“Wale watu wamesema huyu nyoka hana madhara kwa mtu asiyekuwa
na mawazo mabaya kama kukata miti, kuchoma moto au kuharibu vyanzo
vya maji. Lazima humtokea na kumtisha lakini huwa hafanyi lolote baya.”
“Mmh! Inawezekana, kwani siamini kama alitupita bila kutufanya lolote,
au hakutuona?”
“Asituone vipi, tulikuwa mbele yake. Kutuacha salama nimekubaliana
na wale watu waliosema huyu ni jini au mzimu wa mlima huu.”
“Kwa hiyo?”
“Tusiondoke kwenye mlima huu kwani naamini ni sehemu salama sana
kwetu kuweza kujificha kwa muda wa kusubiri wewe kujifungua.”
“Mmh! Sawa lakini bado nina wasiwasi na yule nyoka.”
“Mpenzi wangu kama kutudhuru angetudhuru ndani ya maji.”
“Sawa, basi nifanyie mpango wa chochote kitu hapa nina njaa balaa,”
Zulfa alilalamika njaa.
Sued baada ya kufukua mizigo yao walitoa viazi vya kuchemsha na
samaki wa kukaanga walioondokana nao kwao na kumpa mpenzi wake.
Alibeba chupa na kufuata maji kisimani.
“Sued angalia mpenzi wangu usijemezwa na nyoka,” Zulfa
alimtahadharisha mpenzi wake.
“Ondoa shaka.”
Sued alielekea kisimani kuchota maji, alipofika kisimani wakati
amechuchumaa anachota maji alisikia miti kama inavunjika. Alipogeuka
alimuona yule nyoka mkubwa kwa mbali akielekea pale kisimani. Pamoja
na kufahamu hawezi kumfanya kitu chochote.
Hakujiamini alijikuta akitaharuki na kujiuliza asimame palepale au
akimbie, lakini miguu ilikuwa mizito. Nyoka alizidi kumsogelea na
kumfanya avujwe na jasho la hofu mwili mzima kama kamwagiwa maji.
***
Baada ya mizunguko ya kutwa nzima bila mafanikio watu wote walirudi
Some kujiuliza wale watu wamekwenda wapi.
“Mzee ni kweli au unatuchezea akili?” mzee Kipepeo aliuliza akiwa
amechanganyikiwa na kujiuliza atamwambia nini mkewe kama akirudi bila
ya Zulfa.
“Ningekuwa nasema uongo hata mwenyekiti wangu angekanusha.”
“Inawezekana walikuwepo lakini si mwanangu.”
“Mzee wangu, ni jana usiku wamenieleza ukweli kuwa yule niliyekuwa
najua ni mvulana lakini legelege ni msichana. Na kwa mdomo wao
wamenieleza kuwa yule msichana ni mtoto wa mzee Kipepeo.”
“Sasa wapo wapi?”
“Ndiyo nashangaa.”
“Inawezekana mzee alipotaka kuwafukuza na kuonesha hayupo tayari
kuwaunga mkono waliingiwa na wasiwasi na kutoroka,” alichangia askari
mmoja.
“Kama ni hivyo, kwa nini uliwakatalia kisha kabla ya kujua kama
wamekubaliana na wewe ukachukua jukumu la kuja kututaarifu?” mzee
Kipepeo aliyekuwa amekosa raha aliuliza.
“Tena mzee ulitakiwa kutoa taarifa kwa kiongozi wako wa kijiji ili
wawekwe chini ya ulinzi kisha ndiyo uje kutoe taarifa,” askari mwingine
alichangia.
“Mwanangu mawazo hayo sikuwa nayo! Sikuwaza kama watanifanyia
kitu kama hiki.”
“Sasa hatuna jinsi lazima turudi ila nawaombeni mtu yeyote au watu
wowote watakaobahatika kumuona binti yangu akiwa hai au amekufa
nitawapa kila mmoja milioni ishirini.”
“Milioni ishirini!” walishtuka vijana wa Kijiji cha Some.
“Ndiyo, kuanzia sasa nakuombeni hakuna kulala mpaka apatikane.”
“Hakuna tatizo kazi hiyo tutaifanya.”
Mzee Kipepeo na watu wake ilibidi wakubali matokeo na kurudi
Kayenzo kufanya shughuli zingine huku moyoni akijiuliza atamwambia
nini mkewe, ambaye taarifa za kuonekana mwanaye kidogo zimtie uchizi.
Baada ya kufika Kayenzo, mzee Kipepeo alionekana mtu mwenye uso
wa simanzi, hata mkewe aliliona hilo lakini kwanza alitaka kujua taarifa
ya mwanaye.
“Mume wangu mtoto yupo wapi?”
“Mke wangu hi habari ndefu.”
“Habari ndefu gani mume wangu, Zulfa yupo wapi?”
“Ametoroka.”
“Ametoroka?”
“Ndiyo mke wangu, imeonekana yule mzee aliwakaripia kabla ya
kukubaliana kukaa pale. Inaonesha nao waliingia wasiwasi wakatoroka
usiku uleule.”
“Walijuaje kama amekuja kwetu?”
“Hapo ndipo penye utata.”
“Inawezekana siyo wenyewe.”
“Basi tungewakuta.”
“Mmh! Watakuwa wamekwenda wapi? Some ni kijiji kidogo sana ina
maana mmeshindwa kuwaona?”
“Mke wangu toka tuondoke jana mpaka muda huu sijapumzika wala
sijatia kitu tumboni kwa ajili ya kumtafuta mwanao.”
“Ooh! Pole sana mume wangu, sasa watakuwa wamekwenda wapi usiku
huo?”
“Wasiwasi wa watu huenda nao wamekuja mjini.”
“Basi tumuombe Mungu tuweze kuwaona.”
“Nakuapia mke wangu siku nikimshika huyo mwanaharamu aliyeniharibia
mwanangu na kunitia hasara na kunisumbua, nitamfanya kitu kibaya,
nitamtafuna mbichi,” mzee Kipepeo alisema kwa hasira mpaka machozi
yakamtoka.
“Mume wangu tumuombe Mungu amlinde mwenetu, nina imani
ataonekana tu. Kwa vile sasa ni mjamzito na ujauzito wake ni mkubwa basi
tuhakikishe tunatoa taarifa ili msako ufanyike kila kona ya nchi.”
“Tena ngoja,” mzee Kipepeo alisema huku akichukua simu yake.
“Unataka kufanya nini?” mkewe alimuuliza.
“Nataka kumpigia mkuu wa jeshi la polisi ili asambaze taarifa, nina imani
hawapo mbali pia kuhakikisha kwenye hospitali zote kunakuwa na ulinzi wa
kutosha ili kupata taarifa za Zulfa.”
“Kwa nini usingeoga na kula kwanza mume wangu?”
“Mke wangu hata hamu ya kula ninayo, yaani Zulfa kajua kututenda.”
“Ni kweli, lakini ulitakiwa kupata hata maziwa kulipasha tumbo moto
kwanza.”
“Hapana mke wangu niwie radhi niache nifanye hili kwanza, nina imani
hawatakuwa mbali.”
“Kwani huyo kijana aliyemtorosha mwenetu anakaa wapi?”
“Kwa kweli sijui, kwa vile ni mjamzito hiyo itaturahisishia kuwagundua
wapo wapi.”
“Haya mume wangu, ngoja nikuandalie maziwa.”
Mama Zulfa alikwenda jikoni kumchukulia maziwa mumewe ambaye
aliwasiliana na mkuu wa polisi aliyemhakikishia kumpa ushirikiano
mkubwa, kuhakikisha mwanaye anapatikana akiwa hai.
***
Sued alikuwa amechanganyikiwa baada ya kumshuhudia nyoka akielekea
upande alipokuwa akichota maji huku nguvu zikimuishia. Alijikuta akitulia
kama sanamu kusubiri majaliwa yake. Taratibu yule nyoka alisogea karibu
yake huku akiutoa ulimi wake, macho yake meusi yaking’aa kichwa
chake kilikuwa tofauti na nyoka wengine katikati ya kichwa alikuwa
kama kavishwa taji la kimalkia, pia rangi yake ilikuwa nzuri sana yenye
kubadilikabadilika na kufanya apendeze sana kumtazama.
Pamoja na sifa za nyoka huyo, kila alivyokuwa akisogea ndivyo Sued
jasho la woga lilivyokuwa likimtoka. Alizibana pumzi zake huku mapigo
ya moyo yakipungua kuonesha wakati wowote yanaweza kusimama.
Alipomkaribia alifumba macho asione anavyomezwa na nyoka yule.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 19
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500...

ILIPOISHIA:
Sued alibidi amweleze ukweli mpenzi wake aliyokutana nayo. Kauli ile
ilimshtua sana Zulfa.
“Mpenzi wangu naomba tuondoke sehemu hii si salama.”
“Mpenzi hapa hatuondoki.”
“Hapana tuondoke, huoni tunajitafutia balaa la kuliwa na nyoka?”
“Kitendo cha leo basi ndicho kilichonipa ujasiri wa kuendelea kuishi
kwenye mlima huu.”
“Kivipi wakati umejikojolea?”
“Ni kweli nimejikojolea kwa hofu, lakini ile imenidhihirishia yule nyoka
hamdhuru mtu.”
“Kwa hiyo?”
“Tutaishi bila hofu yoyote kwa kuwa nimeamini nyoka huyu hana madhara
kwa mwanadamu.”
“Mmh! Pole mpenzi wangu.”
“Asante.”
SASA ENDELEA...
***
Jioni ilipoingia walitengeneza sehemu ya kulala ambayo ilikuwa salama. Wakiwa wamejilaza juu ya majani yaliyotandikwa kitenge, Sued alimuuliza Zulfa.
“Mpenzi utajifungulia wapi?”
“Hukuhuku.”
“Zulfa!” Sued alishtuka.
“Unashtuka nini?”
“Utajifunguaje bila vifaa vya kujifungulia?”
“Kila kitu ninacho,” Zulfa alimtoa hofu mpenzi wake.
“Unacho! Ulichukua saa ngapi na lini?”
“Toka nilipopata wazo la kutoroka, nilifanya manunuzi ya vifaa vyote vya
kujifungulia kwa kuamini maisha yetu kabla ya kujifungua yasingekuwa kwa
yule mzee.”
“Kwa nini ulifikiria hivyo?”
“Huwezi kuamini yule mzee sikumuamini hata kidogo, hasa baada ya
kuisikia historia yake iliyojaa tamaa. Nataka kueleza kitu kama angejua mimi
mwanamke asingesita kunitaka kimapenzi.”
“Mmh! Sasa vifaa hivyo ulivipata wapi?”
“Mjini.”
“Mjini?” Sued alishtuka sana kusikilia yale.
“Ndiyo.”
“Mjini umeenda lini?”
“Nilimtuma mtu.”
“Ulimtumaje?”
“Nilimwandikia mtu vitu muhimu vinavyotakiwa kuwepo mwanamke
anapojifungua na kumpa fedha kwenda kununua.”
“Sawa ulimpa, ulimwambiaje?”
“Nilimweleza kuna dada mmoja mjamzito anataka kujifungua.”
“Mmh! Ulimpa nani?”
“Kasabi.”
“Kasabi?”
“Ndiyo, alipokuwa akipeleka samaki wa oda mjini.”
“Mmh! Kweli ulijiandaa, sawa vifaa tunavyo utajifunguaje bila muuguzi?”
bado Sued alikuwa njia panda.”
“Sued suala la kujifungua nitakuelekeza jinsi ya kunihudumia ili
nijifungue salama.”
“Mmh! Nitaweza?”
“Utaweza, si kazi sana, tena nitakufundisha kuanzia kesho usije niua na
mwanangu.”
“Sawa mpenzi.”
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda, walimbatiana na kuitafuta siku ya
pili.
***
Siku ya pili walipoamka walitengeneza sehemu yao ya kuishi, ambayo waliitengeneza maalumu kwa kuishi sehemu ile ikiwa pamoja na kuziba
juu kwa ajili ya mvua na jua. Waliyaanza maisha rasmi katika mlima ule, kweli mapenzi upofu, uziwi ububu kumjaza mtu ujasiri penye matatizo. Kutokana mapenzi mazito kwa Sued, Zulfa alifurahia maisha yale ya shida ya kuishi kwa kujificha kama magaidi.
***
Baada ya wiki chakula walichokuja nacho kiliisha. Sued usiku aliteremka
mpaka mjini na kununua vitu vya muhimu, kwenye maduka na magenge
ambayo aliamini hawamuelewi na kurudi navyo mlimani kuendelea
maisha yao huku siku za kujifungua Zulfa zikisogea.
Siku moja akiwa amefuata bidhaa kijijini Some, alipokaribia kwenye duka analo nunulia bidhaa, kwa vile alikuwa akitokea kizani alisikia watu wakizungumza ambao hawakumuona akija. Alisimama kuwasikiliza.
“Jamani, sasa wiki ya pili inakatika bila kumuona, labda umefananisha?”
“Ni yeye kabisa anaye tafutwa.”
“Mmh! Sasa mbona haonekani wiki ya pili inakatika?”
“Inawezekana vitu alivyonunua havijaisha ila nina uhakika wakati
wowote atakuja. Vumilieni tu,” alisikia sauti ya muuza duka.
Maneno yale yalishtua sana Sued na kujua mambo yameharibika,
kumbe kwenda pale muuza duka alimtambua na kutoa taarifa kwa polisi
jamii kumvizia ili kumkamata. Taratibu aligeuza na kurudi alipotoka kwa
mwendo wa haraka. Alipotoka eneo la makazi ya watu akatimua mbio.
Alifika kwa mpenzi wake akihema bila alichokifuata. Zulfa alipomuona
alishtuka na kumuuliza:
“Kulikoni mpenzi wangu? Umerudi unahema bila kitu ulichokifuata?”
“Mpenzi wee acha tu, leo nilikuwa nakamatwa bila kujua.”
“Kukamatwa?”
“Ndiyo, kumbe wamenishtukia.”
“Mungu wangu! Umewakimbiaje?”
Alimuelezea hali aliyokutana nayo alipokaribia dukani.
“Wewee!” Zulfa alishtuka.
“Yaani ni Mungu tu, lakini wangenikamata kijinga sana.”
“Mmh! Sasa tutafanyaje?”
“Hata sijui, au tumfuate Kasabi ili awe anatukusanyia vitu ambayo
vitatutosha zaidi ya wiki mbili vikiisha awe anatuletea tena.”
“Sued unataka kufanya nini?’
“Kasabi namwamini sana.”
“Sued acha ujinga, huu si muda wa kumuamini mtu, hata baba yangu
simwamini kwa vile ana mapungufu.”
“Unafikiri tutaishije mpenzi wangu, kumbuka vyakula vyote vya muhimu
vimeisha.”
“Sued lazima tuwe wabunifu, siamini kama tutakufa na njaa, tuumize
akili, wewe mwanaume gangamala.”
“Mmh! Nitajitahidi.”
“Bahati nzuri mlima wote umezungukwa na mashamba na miti ya
matunda, tukiutumia vizuri usiku, nina imani maisha yatakwenda vizuri.”
“Nashukuru mpenzi kwa moyo na mipango yako mizuri, yote nitayafanyia
kazi.”
“Hatuna njia lazima tukubali kuyabadili maisha yetu, ikiwezekana tuishi
kama watu wa kale tule matunda, viazi, mihogo na mboga za majani na
maisha yatakwenda,” Zulfa alimpa mikakati mpenzi wake.
“Lakini nakuonea huruma mpenzi wangu.”
“Huruma! Ya nini mpenzi wangu?”
“Kukulisha vitu ambavyo hujazoea pia maisha ya mateso.”
“Mpenzi chakula changu kikubwa ambacho sikitaki kukikosa na nikikosa
naamini naweza kufa ni kimoja tu.”
“He! Chakula gani?”
“Upendo wako wa dhati, nimeamini upendo ndani ya moyo ni tiba ni
furaha na chakula kisichochosha kukila kila wakati. Sued unaweza kuona
nateseka kwa vile nimeacha vitu vingi vya kifahari, maisha mazuri kwa
wazazi wangu na kuja huku.
“Huwezi kuamini maisha ninayoishi pembeni yako kwangu naamini ni
zaidi ya peponi. Hata kama nitaikosa pepo ya Mungu nina imani nitakuwa
nilifika kabla ya wengine.”
“Zulfa, najua unanipenda na kushindwa kuziona taabu na shida zote.”
“Hata wewe Sued unanipenda, ndiyo maana tupo wote hapa.”
“Ni kweli, lakini naamini nimekunyima vitu vingi, nimekunyima malezi ya wazazi wako, elimu uliyotaka kuipata, maisha mazuri ya kuwa karibu na wazazi wako. Ona leo nakulaza sehemu kama hii, hatuna tofauti na wanyama!”
“Sued Mungu alipoiumba nafsi aliipa siri kubwa sana, ndiyo maana huwezi kuiongoza nafsi ya mtu mwingine bali yeye mwenyewe. Siku zote wa pembeni huwa mshauri lakini mwenye uamuzi wa mwisho ni wewe mwenyewe, uongo?”
“Kweli.”
“Basi moyo wa mtu unapopenda kitu na kukipata basi huwa
amekamilisha kila kitu kizuri na raha zote.”
“Kwa nini?”
“Mapenzi yana shule?”
“Hapana.”
“Yana profesa?”
“Hapana.”
“Kati ya maskini na tajiri nani anafurahia mapenzi?”
“Tajiri.”
“Sued upo mbali sana kiufahamu, samahani kwa kukueleza hilo.”
“Bila samahani mpenzi wangu.”
“Penzi halina gharama zaidi ya kujitoa wewe mwenyewe, kuna wangapi
wana fedha lakini wanateswa na mapenzi? Mapenzi ni kama nguvu ya
umeme, hasi na chanya zikutane ili kutengeneza nguvu moja.
“Haya ndiyo mapenzi halisi, mapenzi matamu yenye kumsahaulisha mtu
umaskini wake na kumfanya tajiri hata kama hana kitu. Sued nakupenda
zaidi ya kupenda, wewe ni kila kitu kwangu, sijutii kuwa huku, sijutii kuwa
na wewe, naupongeza moyo wangu kulipata chaguo lake sahihi.
“Wengi wamecheza pata potea wameangukia katika mapenzi ya uongo
na matokeo yake kuteseka na kufikia hatua ya kuchanganyikiwa na wengine kukatisha maisha yao sababu ya mapenzi. Sued niahidi hutaniacha
milele.”
“Zulfa mpenzi wangu nimeamini penzi linashinda pesa, linashinda kila
kiuzungukacho moyo. Siamini na sitaamini kama leo upo pembeni yangu
mtoto wa tajiri uliyekimbia maisha mazuri kwenu.”
“Sued ukisema hivyo unakosea, kwani hata wewe una wazazi wako, nawe umeikimbia familia yako kwa ajili yangu, sote tunatakiwa kuwa chini ya wazazi haijalishi upo katika maisha ya aina gani.”
“Sawa nimekuelewa mpenzi wangu, naomba nikuahidi kwa usiku huu
wa nyota na Mungu ni shahidi wetu. Zulfa mimi na wewe mpaka mmoja
atakapoitwa na Mungu na kama anatusikia basi tufe pamoja.”
“Asante mpenzi wangu, umezidi kunidhihirishia pepo ya dunia ndiyo
7ninayoishi kwa sasa, nakupenda sana mpenzi wangu.”
“Nami nakupenda sana.”
Walikumbatiana katika mapenzi mazito, kwa vile usiku ulikuwa mkubwa
usingizi haukuchelewa kuwachukua.

Itaendelea kesho
 
HADITHI: DIMBWI LA HUBA
SEHEMU: 20
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500...

ILIPOISHIA:
“Sawa nimekuelewa mpenzi wangu, naomba nikuahidi kwa usiku huu wa nyota na Mungu ni shahidi wetu. Zulfa mimi na wewe mpaka mmoja atakapoitwa na Mungu na kama anatusikia basi tufe pamoja.”
“Asante mpenzi wangu, umezidi kunidhihirishia pepo ya dunia ndiyo ninayoishi kwa sasa, nakupenda sana mpenzi wangu.”
“Nami nakupenda sana.”
Walikumbatiana katika mapenzi mazito, kwa vile usiku ulikuwa mkubwa usingizi haukuchelewa kuwachukua.
SASA ENDELEA...

***
Sued baada ya kuponea kwenye tundu la sindano kukamatwa, ilibidi abadili utafutaji wa chakula. Hakutaka tena kwenda mjini kununua mahitaji muhimu kwa kuhofia kukamatwa baada ya kugundua alikuwa akitafutwa na kiza ndicho kilichomuokoa.
Alianza kuwinda wanyama wadogo na ndege kwa ajili ya kitoweo na usiku kwenda kwenye mashamba kuchimba viazi na mihogo, walivyotumia kwa ajili ya chakula cha kila siku.
Muda wote waliokaa kule mlimani hakuwahi kufika mtu yeyote, aliamini hofu ya yule nyoka mkubwa ndiyo iliyowasaidia kuishi kule kwa watu kuogopa kufika.
Maisha yaliendelea huku muda wa kujifungua Zulfa ukikaribia. Siku zote Zulfa alimpa semina mpenzi wake namna ya kumsaidia atakapopata uchungu ili aweze kumsaidia kujifungua salama. Sued alijitahidi kushika mafunzo yale ili kuhakikisha hafanyi makosa kwa vile angeweza kumpoteza mtoto wao kipenzi.
Kama kawaida majira ya jioni baada ya jua kupungua ukali, Sued aliingia kuwinda kitoweo baada ya Zulfa kutamani sana nyama yoyote ya ndege au mnyama kati ya sungura au pimbi.
Sued alichukua manati yake na rungu lake alilolipa jina la Inkosikazi ambalo lilikuwa halifanyi makosa katika kumsulubu mnyama. Alianza kuuzunguka mlima kama kawaida yake kwa taratibu huku macho yake yakiangalia chini na juu, kama atapata ndege na wanyama wadogo.
Alijikuta akizunguka sehemu kubwa ya mlima bila kuona kitu chochote, njiwa wengi walikuwa wakisimama miti ya mbali, hata aliporusha mawe hakuwapata aliambulia patupu.
Akiwa amekata tamaa na kuamini siku ile mpenzi wake ataula wa chuya, alishtushwa na majani kucheza kwa mbele. Alituliza macho kwenye mlio ule. Mara alimuona sungura akitokeza huku akitazama kulia na kushoto kuangalia usalama wake.
Yule sungura hakuweza kumuona Sued aliyekuwa amejificha nyuma
ya mti. Baada ya kuridhika na usalama wake aliendelea kula majani laini yaliyokuwa sehemu ile. Kwa vile hakuwa na wasiwasi na eneo lile alikula majani kwa uhuru mkubwa.
Sued alibadili njia ili atokee nyuma yule sungura na kuweza kumpa
pigo moja la nguvu pigo lililonyooka kama la Msolopagazi. Alitembea kwa tahadhari kubwa ili kuhakikisha hamshtui. Alifanikiwa kufika nyuma ya kichaka ambacho mbele yake kulikuwa na bonde la kuelekea chini ya mlima.
Baada ya kufika nyuma ya kichaka alimchungulia sungura kwa chati ili amshtukize kwa pigo la kichwa, kila alivyokuwa akijiandaa kumrukia bado alipata shida kutokana na sungura kumpa mgongo.
Wazo la haraka lilikuwa ampige rungu la kwenye uti wa mgongo ili
amvunje na kumkamata. Wakati akiwaza yale kumbe pembeni yake kulikuwa
na nyoka mkubwa aliyekuwa naye akimwania yule sungura. Baada ya hesabu za nyoka kutimia alijirusha ili kumkamata yule sungura na wakati huo Sued naye alikuwa amejirusha ili kushusha pigo la nguvu kwa sungura.
Alishtuka kumwona nyoka mkubwa akikurupuka kwenye kichaka kuja upande wake. Ili kuokoa maisha yake alijirusha zaidi kumkwepa na kumfanya aangukie kwenye miti bondeni.
Pamoja na miti kumchana ilimsaidia asiangukie mawe, lakini mti mmoja ulimchoma kwenye mguu, chini ya goti na kukatikia ndani. Kutokana na kujipigiza kwenye matawi ya miti alijikuta akipoteza fahamu kabla hajafika chini ya mlima.
***
Zulfa alijikuta akiingiwa na wasiwasi baada ya mpenzi wake kuchelewa kurudi. Haikuwa kawaida yake kuchelewa vile. Mpaka kiza kinaingia hakuonekana. Alijiuliza Sued atakuwa amekwenda wapi, wasiwasi wake mwingine alifikiri labda amekamatwa na wanakijiji waliokuwa wakimtafuta.
Alijalibu kuvuta muda labda atarudi lakini muda ulikatika huku giza likizidi kuimeza nuru ya mchana. Hali ile ilizidi kumtia mashaka, alitamani kwenda kumtafuta mpenzi wake.
Alinyanyuka kwa kujilazimisha, tumbo lilikuwa kubwa sana na miguu nayo
ilikuwa imevimba, sana hata kutembea kwake ilikuwa shida, kazi zote za muhimu alizifanya Sued na kumfanya Zulfa muda mwingi awe amepumzika tu huku mwili ukifutuka kutokana na mimba kumkubali.
Kweli penzi la dhati ni chakula cha nafsi, humfanya mtu ajione
hajapungukiwa na kitu hata kama ni maskini wa kutupa. Zulfa pamoja na maisha ya shida bado alinenepeana kwa vile alipata upendo wa dhati toka kwa Sued ambaye kwake alikuwa ndiyo chakula na tiba ya moyo wake.
Aliyanyuka kwa kujilazimisha na kujaribu kutembea huku ameuma meno. Alitembea kidogo lakini alishindwa kwenda mbele kizunguzungu kilikuwa kikali na kumfanya akae alipokuwa amefika.
Zulfa alianza kulia akijua mpenzi wake yupo matatizoni na kuamini kama ameshikwa na kukaa kimya kuwa yeye yupo kule basi angekufa na mimba yake, kwa vile hakukuwa na mtu wa kumsaidia wala sauti yake isingefika mbali ili kupata msaada.
Alilia mpaka sauti ikamkauka na macho kumvimba akimlilia mpenzi wake ambaye hakujua yupo katika hali gani. Wasiwasi mwingine uliomfanya alie sana alihofia pengine amekutana na yule nyoka na kummeza. Siku zote hakumuamini kwa vile alielezwa nyoka hana rafiki.
Aliendelea kumlilia mpenzi wake mpaka akapandwa na presha na
kupoteza fahamu.
***
Manyunyu ya mvua yalimzindua Sued aliyekuwa amepoteza fahamu, alinyanyuka alipokuwa amelala na kukaa kitako. Kiza kilikuwa kimetanda eneo lile, akajikuta akijiuliza pale amefikaje.
Mwili ulikuwa ukimuuma kila kona na kusikia uchungu ukizidi kila
manyunyu yalipogusa mwili wake, kuonesha amepata majeraha mwili mzima, alipondondoka toka juu ya mlima.
Alikumbuka alikutana na nini mara ya mwisho, woga ulimtawala baada ya kukumbuka alichokutana nacho. Aliamini kabisa pale alipo si sehemu salama alitakiwa kuondoka haraka. Alipojinyanyua ili aondoke alihisi maumivu makali sana kwenye mguu wa kushoto. Alipojipapasa aligundua kuna kipande kidogo cha mti kimekatikia ndani.
Aliamini pale hapakuwa sehemu ya kufanya utaratibu wa kukitoa kipande cha mti. Pia alimfikiria mpenzi wake muda ule angekuwa katika hali gani baada ya kumkosa muda mrefu.
Kila alipojaribu kukanyaga chini maumivu yalikuwa makali sana. Aliuma meno kutaka kulazimisha kutembea lakini mguu ulikataa. Alikata tawi la mti na kumsaidia kutembelea mguu mmoja, alianza kupanda mlima kurudi kwa mpenzi wake.
Alitembea kwa shida huku mwili ukimuuma kama kidonda. Alifanikiwa kufika juu ya mlima kwa shida na kwenda sehemu wanayokaa, lakini hakumwona mpenzi wake.
Alijaribu kumwita kwa sauti lakini hakukuwa na jibu, alisogea kwa mbele kumtafuta huku akijiuliza Zulfa atakuwa amekwenda wapi hasa ukizingatia hali yake ilivyokuwa. Wasiwasi wake aliwaza huenda mpenzi wake amejaribu kumtafuta na kutereza mlimani na kuanguka chini kama yeye alivyoanguka.
Aliogopa kufikia tumbo na kumsababishia madhara makubwa ambayo yangemfanya apoteza maisha na kiumbe kilichomo tumboni.
Alipotembea huku macho yake yakiwa yamezoea kiza, aliona kitu kimelala chini alikisogelea na kukuta ni mpenzi wake akiwa hajitambui. Alipomfikia na kumpima alikuwa anahema kwa mbali, pia alikuwa amelalia ubavu kitu kilichompa matumaini kuwa hakulalia tumbo.
Alichukua maji na kummwagia kichwani, baada ya muda Zulfa alirudiwa na fahamu na kuita.
“Sued.”
“Naam.”
“Umerudi mpenzi wangu?”
“Ndiyo.”
“Ooh! Asante Mungu kama usingerudi ningekuwa nani mimi katika dunia
hii?”
“Vipi mbona umelala hapa?”
“Nilikuwa nataka nikutafute mpenzi wangu lakini kizunguzungu kilikuwa kikali kilichonifanya nishindwe kutembea na kukaa chini lakini presha ilikuwa kubwa iliyonifanya nipoteze fahamu.”
“Pole sana mpenzi wangu.”
“Asante, Sued ulikuwa wapi mpenzi wangu?”
“Twende kwanza kwetu nitakueleza kila kitu.”
Baada ya Zulfa kunyanyuka ili waelekee wanapoishi, alishtuka kumwona mpenzi wake akitembea kwa msaada wa fimbo kwa kuchechemea.
“He! Sued nini tena?”
“Ni kisa kirefu, twende kwanza kwetu.”
Pamoja na hali yake Zulfa alijikuta akimsaidia mpenzi wake kutembea
huku akilia kitu ambacho Sued hakukipenda.
“Sasa unalia nini?”
“Unafikiri hii hali ni nzuri?”
“Nimeshatokea, la muhimu kujitibu ili tujue tutaishi vipi.”
Walipofika, Zulfa alichemsha maji ya moto kwa ajili ya kumkanda Sued aliyekuwa hatamaniki kwa damu iliyokuwa imemtapakaa kwa majeraha madogo yaliyokuwa yametoa damu nyingi.
Baada ya kuwasha moto, Zulfa alichukua kijinga cha moto ili amuangalie mpenzi wake. Hali aliyomuona nao na kipande cha mti kilichokuwa ndani ya mguu, ilimfanya aangue kilio upya, ikabidi Sued amkemee.
“Unalia nini?”
“Wewe hii hali unaipenda?”
“Hata kama siipendi imeshatokea, machozi si tiba. Cha kufanya nisaidie kunikanda na kunimulikia nikitoe kipande cha mti.”
“Mungu wangu ukitoe bila ganzi?”
“Zulfa hebu acha utoto, ganzi huku tutaitoa wapi?”
“Sued nimekumbuka, tulifundishwa kutengeneza ganzi pasipo na ganzi.”
“Utafanyaje?”
“Tuifunge damu isitembee chini ili sehemu ya jeraha ife ganzi.”
“Hayo ndiyo mawazo kuliko kulia.”
“Sawa mpenzi, nitajitahidi japokuwa moyo unaniuma sana.”
“Haya ndiyo maisha tuliyoamua kuishi kwa hiyo tuwe tayari kupambana na
changamoto kama hizi.”
“Sawa mpenzi wangu, kwani ilikuwaje?”
“Ngoja kwanza tumalize zoezi hili.”
“Sawa mpenzi wangu.”
Zoezi la kutoa kipande cha mti lilianza mara moja kwa kufunga mguu na kamba chini ya paja kwa nguvu na kuifanya damu iishie juu ya goti, baada ya muda mguu ulianza kupoteza mawasiliano kwenda chini.
Sued alichukua kisu na kuanza kukitoa kipande cha mti, pamoja na kuufunga mguu bado maumivu aliyasikia japo si sana na kufanikiwa kukitoa, kisha alichukua kijinga cha moto na kuunguza sehemu yenye jeraha ili kuua wadudu wa magonjwa ya kuambukiza.
Mpaka anakitoa kipande cha mti haja ndogo ilimtoka bila kujijua. Zulfa hakutazama, alifumba macho muda wote mpaka alipoambiwa tayari. Baada ya kukandwa mwili mzima alijilaza, kwa vile walikuwa wamejiandaa, alimeza vidonge vya kupunguza maumivu.
Zulfa hakuweza kujua sababu ya mpenzi wake kuwa katika hali ile, kutokana na mpenzi wake kutaka kupumzika kutokana na maumivu ya mwili.

Kupitia page hii Hadithi hii unakatishiwa hapa kwa vile kitabu chake kipo mtaani kama imekuvutia tafuta kitabu chake kwa Tshs 3500 tu. Nawatakia usomaji mwema.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom